Matendo 2:46-47 “Na siku zote kwa moyo
mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakimega mkate nyumba kwa nyumba, na kushiriki
chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe, wakimsifu Mungu, na kuwapendeza
watu wote. Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa.”
Utangulizi
Ni muhimu kufahamu kuwa nyakati
za kanisa la kwanza licha ya kuwa walikuwa wakikutana hekaluni kuabudu lakini
pia walikuwa na tabia ya kukutana na kuabudu nyumba kwa nyumba, jambo hili
lilichangia kwa kiasi kikubwa washirika kuwa na uwezo wa kutambuana kushirikiana
na kutiana moyo lakini pia makanisa ya nyumbani yalichochea kwa kiasi kikubwa
ukuaji wa kanisa mama, Ukiacha hilo pia wahudumu wenye huduma ya kichungaji,
watenda kazi, Wanafunzi na wenye hekima wanapata nafasi ya kutumia vipawa vyao,
na kujifunza kivitendo, malezi ya kanisa na kutengeneza njia rahisi ya kufungua
matawi ya kanisa katika sehemu zingine za mji wetu, tunaweza kuhitimisha kwa
kusema kuwa huduma ya makanisa ya nyumbani ni mpango wa Mungu wa ukuaji wa
kiroho, kihuduma na kiidadi, lakini ni moyo wa kutengeneza umoja na ushirikiano
wa karibu kwa huduma ya kichungaji.
Warumi 16:3-4. “Nisalimieni Priska na
Akila, watenda kazi pamoja nami katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata
kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu,
ila na makanisa ya Mataifa yote pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika
nyumba yao.”
Ukiichunguza Biblia utaweza kuona
kuwa nyakati za karne ya kwanza wakati kanisa linaanza watenda kazi walikuwa na
makanisa nyumbani, kwa hiyo huduma katika makanisa ya nyumbani halikuwa swala
geni au lisilo la kibiblia, na huduma hizi za makanisa ya nyumbani zimeonyesha
mafanikio makubwa sana katika maeneo mengi duniani ikiwemo Afrika na Asia na sehemu nyingine duniani, lakini pia makanisa
ya nyumbani yameonyesha mafanikio makubwa katika maeneo ambayo injili inapigwa
marufuku, leo basi tutachukua muda kujifunza somo hili Huduma katika makanisa
ya nyumbani kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-
- Maana ya makanisa ya nyumbani
- Huduma katika makanisa ya nyumbani
- Faida ya huduma katika makanisa ya
nyumbani
Maana ya makanisa ya nyumbani
Makanisa ya nyumbani au kanisa la
nyumbani ni mkusanyiko mdogo wa washirika wa Kanisa la mahali pamoja au katika
mji mmoja ambao wanakusanyika katika mitaa yao, katika nyumba mojawapo ya
mtenda kazi au mtu aliyejitoa kutoa nyumba yake kwa ajili ya ibada, kwa kusudi la kukusanyika pamoja kwa
ibada katika siku mojawapo ya juma inayokubalika kwaajili ya kufanya ibada za
pamoja, kuomba pamoja, kujifunza neno la Mungu, kuumega mkate na kushirikiana
na kujuana hali kwa ukaribu na kwa pamoja, makanisa ya nyumbani yanaweza
kukutana katika sebule ya mshirika mmojawapo na yakiwa na uwezo wa kuwa na
wanachama kuanzia 6-10 au 10-30 kulingana
na uwezo wa sebule au mahali pa kuabudia wanakokutana washirika hao,
Makanisa ya nyumbani sio mbadala wa kanisa mama hata kidogo lakini ni vikundi
vidogo vidogo vinavyoundwa na watu kwa kusudi la kulifanya kanisa mama
kuendelea kuwa na nguvu na kukua katika upendo na ushirika, makanisa haya
yanasaidia sana kuleta umoja wa kweli Maandiko yanaonyesha kuwa kulikuwa na
makanisa ya namna hii nyakati za mitume:-
Kanisa katika nyumba ya Prisila na Akila – Warumi 16:3-4 “Nisalimieni Priska na Akila, watenda kazi pamoja nami
katika Kristo Yesu; waliokuwa tayari hata kukatwa kichwa kwa ajili ya maisha
yangu; ambao ninawashukuru, wala si mimi tu, ila na makanisa ya Mataifa yote
pia; nisalimieni na kanisa lililomo katika nyumba yao.”
1Wakorintho 16:19-20 “Makanisa ya Asia
wawasalimu. Akila na Priska wawasalimu sana katika Bwana, pamoja na kanisa
lililoko ndani ya nyumba yao. Ndugu wote wawasalimu. Salimianeni kwa busu
takatifu.”
Nimfa pia anatajwa kuwa alikuwa na kanisa la Nyumbani huko Kolosai –
Wakolosai 4:14-15 “Luka, yule tabibu mpendwa, na
Dema, wanawasalimu.Wasalimuni ndugu walioko Laodikia, na Nimfa, na kanisa
lililo katika nyumba yake.”
Pia rafiki wa Paulo Mtume aitwaye Philemoni – Philemoni 1:1-3. “Paulo, mfungwa wa Kristo Yesu, na Timotheo aliye ndugu
yetu, kwa Filemoni mpendwa wetu, mtenda kazi pamoja nasi, na kwa Afia, ndugu
yetu, na kwa Arkipo askari mwenzetu, na kwa kanisa lililo katika nyumba yako.
Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu, Baba yetu, na kwa Bwana Yesu
Kristo”
Huduma katika makanisa ya nyumbani
Huduma katika makanisa ya
nyumbani zinaendeshwa na watendakazi, wanafunzi pamoja na wenye hekima ambao
wamepitia mafunzo mbalimbali katika kanisa letu, hawa sasa wanawajibika
kuyahudumia makanisa hayo katika makazi karibu na mitaani kwao wanakokaa
washirika, Neno la Mungu linaonyesha kuwa huduma za kiroho, maombezi, kuongoza
watu katika wokovu, na kuwajenga watu zinaweza kufanyika pia katika nyumba za
watu kwa taratibu maalumu, Yesu alithamini pia shughuli za kuwahudumia watu
nyumba kwa nyumba ukiacha kuwa alikuwa akihitajika na umati mkubwa wa watu.
Marko 1:29-34 “Na mara walipotoka katika
sinagogi, walifika nyumbani kwa Simoni na Andrea, pamoja na Yakobo na Yohana.
Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara
wakamwambia habari zake. Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa
ikamwacha, akawatumikia. Hata kulipokuwa jioni, na jua limekwisha kuchwa,
walikuwa wakimletea wote waliokuwa hawawezi, na wenye pepo. Na mji wote ulikuwa
umekusanyika mlangoni.Akaponya wengi waliokuwa na maradhi mbalimbali, akatoa
pepo wengi, wala hakuwaacha pepo kunena, kwa sababu walimjua.”
Luka 19:5-9 “Na Yesu, alipofika mahali
pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa
kushinda nyumbani mwako. Akafanya haraka, akashuka, akamkaribisha kwa furaha.
Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu
mwenye dhambi. Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali
yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia
mara nne. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu
naye ni mwana wa Ibrahimu.”
Luka 10:38-42 “Ikawa katika kuenenda kwao
aliingia katika kijiji kimoja; mwanamke mmoja jina lake Martha akamkaribisha
nyumbani kwake.Naye alikuwa na umbu lake aitwaye Mariamu, aliyeketi miguuni
pake Yesu, akasikiliza maneno yake. Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa
utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu
alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. Bwana akajibu
akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi;
lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema,
ambalo hataondolewa.”
Tunajifunza hapo kutoka kwa
Mwalimu mkuu Yesu Kristo kwamba nyumbani ni mahali ambapo huduma zote zinaweza
kufanyika bila shaka yoyote uwepo wa Mungu unakuwepo popote walipo wawili au
watatu ambao wamekusanyika kwa jina lake
Mathayo 18:18-20 “Amin, nawaambieni, yo
yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote
mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. Tena nawaambia, ya
kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba,
watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu
wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”
Hata hivyo ni muhimu kufahamu
kuwa huduma ya makanisa ya nyumbani ni sehemu ndogo tu ya ushirika mkuu na kwa
sababu hiyo kuhudhuria katika hekalu kuu hakuwezi kupoteza maana sawa tu na
kuhudhuria katika masinagogi hakukuwahi kuondoa maana ya kwenda Hekaluni, wala
kuacha kuhudhuria ibada za muhimu katika kanisa letu, tunajifunza pia kuwa
Paulo alihudumu katika kanisa kuu na makanisa ya nyumbani huku akitembelea
nyumba kwa nyumba na kuwahudumia hii ilileta mafanikio na ufanisi mkubwa
nyakati za kanisa la kwanza:-
Matendo 20:17-21 “Toka Mileto Paulo akatuma
watu kwenda Efeso, akawaita wazee wa kanisa.Walipofika kwake, akawaambia, Ninyi
wenyewe mnajua tangu siku ya kwanza nilipokanyaga hapa Asia, jinsi nilivyokuwa
kwenu wakati wote, nikimtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote, na kwa machozi, na
majaribu yaliyonipata kwa hila za Wayahudi; ya kuwa sikujiepusha katika
kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa bali naliwafundisha waziwazi, na
nyumba kwa nyumba, nikiwashuhudia Wayahudi na Wayunani wamtubie Mungu, na kumwamini
Bwana wetu Yesu Kristo.”
Kwa hiyo tunaweza kufundisha,
kuomba, kuabudu, kuuliza maswali, kutambuana na kuhubiri injili, na watu wakaokoka, na kujenga
umoja wenye nguvu huku tukifahamiana sana kuliko katika kanisa kubwa na mpango
huu ni mahususi sana endapo kanisa mama linalenga kuwa kanisa kubwa lenye
kusanyiko kubwa la watu maelfu kwa maelfu
Faida ya huduma katika makanisa ya nyumbani
Kanisa la nyumbani lina faida
kubwa sana endapo kanisa mama lina malengo ya kuwa kanisa kubwa lenye nwaamini
maelfu kwa maelfu yaani Mega Church,
Kanisa linapokuwa kubwa bila kuwa na makanisa ya nyumbani kunakuwa na ugumu wa
kutambuana, kuangalia changamoto wanazokutana nazo waamini wetu, kukosa msaada
wa karibu anapokuwa mtaani ambako hajui kama kuna wenzake wa karibu wanaishi
huko, lakini pia kama mtu ana vipawa na karama ambazo kwa hizo Mungu yu amtumia
ni vigumu kutambulika na kutumika bila mfumo wa makanisa ya nyumbani kwa hiyo
kuna umuhimu mkubwa sana kwa kanisa letu kuwa na mfumo huu wa makanisa ya
nyumbani, pamoja na faida lukuki zinazoweza kutolewa na kanisa la nyumbani hapa
tunaweza kuona faida kadhaa :-
- Makanisa ya nyumbani husaidia kukua
kiroho – Kanisa la nyumbani linaleta utulivu na nafasi ambayo kila
mmoja hutambulika lakini sio hivyo tu mtu anaweza kupata nafasi ya kuuliza
maswali, kueleza changamoto anazokuta
anazo na kupata mtenda kazi wa karibu na eneo lake ambaye anaweza
kumsaidia katika kujifunza na kukua kiroho kwa hiyo kanisa la nyumbani ni
njia bora zaidi ya kuangaliana sisi kwa sisi katika mazingira yote
Waebrania 10:24-25 “tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo
na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya
wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile
kuwa inakaribia”
- Makanisa ya nyumbani yanatoa huduma ya
ushirika wa kweli – hakuna mahali ambapo watu watafahamiana kwa
ukaribu kama katika ushirika wa makanisa ya nyumbani, watabebeana mizigo
kama makanisa ya nyumbani, watashirikiana katika shida na furaha kama
kanisa la nyumbani kwa ujumla ule upendo wa kweli katika Kristo tunaweza
kuonyeshana kwa uhalisia katika
makanisa ya nyumbani, wakati kanisa kubwa linainua hisia zetu ni kanisa la
nyumbani ndilo linaloleta mapinduzi makubwa ya kiroho, na kiushirika.
Matendo 2:41-42 “Nao waliolipokea neno lake wakabatizwa; na siku ile
wakaongezeka watu wapata elfu tatu. Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume,
na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali.”
- Makanisa ya nyumbani yanahusika kwa
ukaribu na huduma ya kichungaji – kama mshirika anapitia changamoto za
aina mbalimbali mchungaji kiongozi hawezi kujua bila taarifa za wale walio
karibu naye ikiwa ni pamoja na kiongozi wa kanisa la nyumbani ambaye ni
mtenda kazi pamoja na Mchungaji wetu, Kanisa la nyumbani ni rahisi
kumtambua kila mtu, ni rahisi kutambua mtu anayepitia changamoto ni rahisi
kumuombea mtu ni rahisi kujua mtu anaye lega lega katika Imani na ni
sehemu ambayo hakuna mtu anasahaulika wala kupotea na ni rahisi kufuatiliwa na kurejezwa katika Imani
Wagalatia 6:1-2 “Ndugu zangu, mtu akighafilika katika kosa lo lote, ninyi
mlio wa Roho mrejezeni upya mtu kama huyo kwa roho ya upole, ukijiangalia nafsi
yako usije ukajaribiwa wewe mwenyewe. Mchukuliane mizigo na kuitimiza hivyo
sheria ya Kristo.”
- Makanisa ya nyumbani ni nyenzo ya
uinjilisti rahisi – Ni vigumu wakati mwingine kumualika mtu katika
kanisa mama na akakubali hasa kama hajawahi kuingia katika makanisa ya
watu wanaohubiri wokovu, lakini ni rahisi mtu kualikika katika makanisa ya
nyumbani anajisikia salama maana ni sebule ya mtu na ni kwa watu
anaowajua, ni rahisi kualika majirani, na wakafika hawaogopi kuliko
inavyokuwa katika majengo ya makanisa makubwa na kwa njia hiyo ni rahisi kumuhubiri injili na pia kutoa
mwaliko wa kuja katika kanisa kubwa huduma za kiroho zaidi.
Matendo 5:42 “Na
kila siku, ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri
habari njema za Yesu kwamba ni Kristo.”
- Makanisa ya nyumbani ni nyenzo ya
kulea viongozi – wakati mwingine kutokana na programu ambazo
zinaendelea katika kanisa kubwa kuna uwezekano wa kushindwa kuwapa watu
wengine madhabahu, au kupatikana kwa uhaba, lakini makanisa ya nyumbani
kwa sababu ni kundi dogo linaweza kumshirikisha kila mtu na zaidi ya yote
viongozi wetu waliopata nafasi ya kupitia shule mbalimbali ya za kihuduma wanapata nafasi ya kuhudumu na
kuombea watu na kuchunga kanisa dogo na kulikuza jambo ambalo linaweza
kuwarahisishia uanzishaji wa makanisa wanapokuwa wameitwa katika wito
maalumu, Ni katika kanisa la nyumbani viongozi hujifunza kivitendo, karama
zinagunduliwa, wachungaji wajao wanabainika, walimu wazuri wanabainika,
wainjilisti wazuri wanabainika na watendakazi wapya wanabainika
2Timotheo 2:1-2 “Basi wewe, mwanangu, uwe hodari katika neema iliyo katika
Kristo Yesu. Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo
uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”
- Makanisa ya nyumbani ni nyenzo ya kupanuka
kwa kanisa – Kanisa hutawanyika kwa haraka kutokana na kuweko kwa
makanisa ya nyumbani kama eneo la kanisa kubwa liko mbali sana na sehemu fulani
ni kupitia makanisa ya nyumbani tunaweza kuanzisha tawi lingine bila
kuhitaji gharama kubwa za kukodisha jengo, aidha makanisa ya nyumbani
hayawezi kuzuiliwa na mateso au upinzani, katika nchi nyingi ambazo injili
inapingwa makanisa ya nyumbani imekuwa ni njia ya siri ya kulifanya kanisa
kuendelea mbele. Makanisa ya nyumbani yametumiwa na watumishi wengi wa
Mungu katika huduma zao na kusababisha ukuaji na upoanukaji mkubwa wa
kanisa mama hivyo makanisa haya ni nyenzo ya ukuaji wa Kanisa kubwa
kiroho, kiidadi, kijiografia na kadhalika
Matendo 6:5-7 “Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote;
wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, na Filipo, na
Prokoro, na Nikanori, na Timoni, na Parmena, na Nikolao mwongofu wa Antiokia;
ambao wakawaweka mbele ya mitume, na walipokwisha kuomba wakaweka mikono yao
juu yao. Neno la Mungu likaenea; na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika
Yerusalemu; jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile Imani.”
Matendo 8:1-4 “Siku ile kukatukia adha kuu ya kanisa lililokuwa katika
Yerusalemu; wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao
mitume. Watu watauwa wakamzika Stefano, wakamfanyia maombolezo makuu. Sauli
akaliharibu kanisa, akiingia kila nyumba, na kuwaburuta wanaume na wanawake na
kuwatupa gerezani. Lakini wale waliotawanyika wakaenda huko na huko
wakilihubiri neno.”
-
Kanisa la
The Church of Pentecost huko Ghana – ni moja ya kanisa kubwa sana miongoni
mwa madhehebu ya kipentekoste wana mfumo wa makanisa ya nyumbani “cell system” zaidi ya maelfu na kutokana na watendakazi kuyasimamia
makanisa hayo kwa uaminifu kanisa limeweza kuwa na washirika karibu milioni
tatu na likatumia makanisa ya nyumbani kuzalisha makanisa 99 katika nchi
nyingine na sehemu mbalimbali za Afrika magharibi
-
Kanisa la
The works and Mission Baptiost Church – Ni moja ya makanisa makubwa sana
nchini Ivory Coast kanisa hili linaongozwa na Askofu Dion Robert kanisa lake lina mfumi wa makanisa ya nyumbani ambayo yamesababisha mfumuko mkubwa wa ukuaji
wa kanisa kanisa lina cell Groups
makanisa ya nyumbani 18,000,. 14,000 ya watu wazima na 4,000 ya watoto kupitia mfumo huo
kanisa la Bishop Dion sasa lina washirika 150,000
katika ibada moja wakutanano kuabudu
-
Christian
Rivival Church – Ni kanisa kubwa na linalokua kwa kasi lililoko Afrika ya
kusinikanisa hili mlina mfumo wa makanisa ya nyumbani yanayounganisha watu na majirani, kanisa hili lina maelfu ya
makanisa ya nyumbani na linaongezeka kwa kasi
-
Lighthouse
Chapel International – Ni kanisa kubwa linaoongezeka kwa kazi lina
wanafunzi wanaohusika kusimamia makanisa ya nyumbani likitumia mfumo ule ule
uliokuwa unatumiwa na mitume nyakati za kanisa la kwanza
-
Living
Faith Church Woldwide (Winners Chapel, Nigeria) – ni Kanisa lenye watu
50,000 wanaoabudu mahali pamoja pale kwenye makao makuu yao wao wanatumia mfumo
wa makanisa ya nyumbani yanayosimamiwa na watenda kazi, kanisa hili kwa sasa
lina waamini zaidi ya milioni sita duniani
-
Deeper
life Bible church Nigeria - lina
waamini wapoatao 65,000 wanaoabudu
katika ibada moja, lakini siri mojawapo ya mafanikio yao ni mfumo wa makanisa
ya nyumbani yenye viongozi mahiri na walimaanisha
-
Full
Gospel Bible Fellowship - Ni moja ya
Kanisa la kipekee la kipentekoste lililoanzishwa nchini Tanzania na Askofu Mkuu
Zakaria Kakobe, ukiacha makanisa
haya kuenea nchi nzima kanisa kuu lililoko Sam Nunjoma pale Mwenge Dar es
Salaam linaundwa na makanisa ya nyumbani zaidi ya 600 yaliyoenea kila mahali
katika mji wa Dar es Salaam, viongozi wa makanisa ya nyumbani wana mafundisho
maalumu ambayo huyatoa kwa pamoja kila mahali katika mtaa husika na viongzi hao
wenye utii wa hali ya juu hutoa taarifa ya kazi wanayoifanya kwa viongozi wao
na kwa mchungaji kiongozi, Makanisa hayo ya meunda umoja imara na kulifanya kanisa
kuu kuwa imara, aidha zinapofungishwa ndoa kwa wingi makanisa hayo
hujishughulisha au kuhusika kwa kiwango Fulani katika usimamizi wa wanandoa hao
kuanzia safari zao za uchumba na
kadhalika, makanisa haya pia huusika na matukio ya misiba mazishi na mengineyo
Kama tunataka makanisa yetu yakue
na kuwa na washirika wengi sana basi ni nashauri tujiandae na mfumo huu maalumu
utakaosaidia kufikisha huduma kwa ufasaha katika jamii, na kulifanya kanisa
kuwa nyenzo rahisi na inayoweza kuwafikia watu kwa njia nyepesi, tusikusanye
sadaka yoyote katika makanisa ya nyumbani, hii itasaidia kuwaondolea kongwa
washirika lakini pia itakuokoa na majaribu ya kifedha kama kiongozi wa makanisa
ya nyumbani kutokuwa na muda wa kutoa hesabu ya mapato na matumizi, makanisa ya
nyumbani yaanzishwe kwa kusudi la kufikisha huduma karibu na watu na sio
kwaajili ya kukusanya mapato, washirika wote wa makanisa ya nyumbani watatoa
sadaka zao katika kanisa kuu lililoko katika mji husika, makanisa ya nyumbani msisitizo
wake ni wa kifamilia kuifanya familia ya Kikristo kuishi pamoja na kushirikiana
na kubebeana mizigo, makanisa ya nyumbani pia ni makanisa ya Mungu, kusudi kuu
ni kuabudu na kujifunza neno la Mungu na
kutiana moyo, Ni muhimu makanisa haya yakaendeshwa kwa kanuni za kimaandiko na
yakatambua viongozi wao na kuwaheshimu, Makanisa ya nyumbani ni kielelezo na
nuru katika mitaa yetu kuendelea kumuhubiri Kristo kivitendo na kuuishi kwa upendo
kama Mungu alivyotuamuru
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni