Mathayo 18:18-20 “Amin, nawaambieni, yo
yote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yo yote
mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbinguni.Tena nawaambia, ya
kwamba wawili wenu watakapopatana duniani katika jambo lo lote watakaloliomba,
watafanyiwa na Baba yangu aliye mbinguni. Kwa kuwa walipo wawili watatu
wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”
Utangulizi:
Tumejifunza huduma ya makanisa ya
nyumbani na tumeona faida zake kwamba Mungu anaheshimu makusanyiko yetu
yanayojenga umoja upendo na ushirikiano, Lakini sasa hatuna budi kwenda ndani
zaidi na kujifunza kivitendo sasa namna ya kustawisha Kanisa la nyumbani, sasa
tunaweza je kuanza Kanisa la nyumbani
1. Ni lazima kumuomba Mungu – Kila kitu
katika ulimwengu wa roho kinaweza kupata ufunguzi endapo kitaanza na maombi,
Nyakati za kanisa la kwanza Paulo mtume na wengineo watenda kazi pamoja naye
waliweza kuifanya kazi kubwa ya Mungu ambayo kimsingi ilianzia katika maombi,
kila kitu cha kiroho ni matokeo ya maombi kwa hivyo tunapotaka kuanzisha kanisa
la nyumbani ni lazima tumuombe Mungu na Mungu atatoa muongozo na kutupa neema
na mpenyo wa jinsi ya kunzisha makanisa hayo.
Matendo 13:1-3 “Na huko Antiokia katika kanisa lililokuwako palikuwa na
manabii na waalimu, nao ni Barnaba, na Simeoni aitwaye Nigeri, na Lukio
Mkirene, na Manaeni aliyekuwa ndugu wa kunyonya wa mfalme Herode, na Sauli.
Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana ibada na kufunga, Roho Mtakatifu
akasema, Nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha
kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao, wakawaacha waende zao.”
Mathayo 9:36-38 “Na alipowaona makutano, aliwahurumia, kwa sababu walikuwa
wamechoka na kutawanyika kama kondoo wasio na mchungaji. Ndipo alipowaambia
wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni
Bwana wa mavuno, apeleke watenda kazi katika mavuno yake.”
2. Kufanya
utafiti wa mitaa na kubainisha vigezo – ili tuweze kuufikia mji kimkakati
na kihuduma hatuna budi kufanya utafiti, wa kina kuhusu mitaa ambayo tunalenga
kufungua kanisa la nyumbani na kubainisha vigezo vitakavyotusaidia kuweka
makanisa ya nyumbani, katika maandiko tunaona kwamba Israel walipotaka kuirithi
nchi ya kanaani walituma wapelelezi kuangalia nchi, kwa hiyo ni muhimu kufanya
survey (ulinganifu na utafiti) wa kujua wapi tunaweka nini na nani anaweza
kufika eneo Fulani na kanisa linaweza kuwa wapi, kwa mfano kama eneo husika ni
wanajeshi, au askari ni nani anaweza kutuwakilisha katika eneo hilo, ama kuna
chuo kikuu ni nani anaweza kutuwakilisha katika eneo hilo au ni uzunguni,
uswahilini na kadhalika ni muhimu kujua ni watu gani tunawafikia ili tuweze
kukidhi vigezo vyao, kwa mfano kama eneo ni la wasomi wa vyuo vikuu na likawako
kanisa la nyumbani huko, mtendakazi atakayepelekwa kusimamia atakuwa ni yule
anayeendana na vigezo vya eneo husika, Kanisa lazima tufanye mambo kwa kutumia
busara na akili, tujue idadi ya watu
hasa washirika wetu na ile jamii ya wale tunaotaka kuwafikia ni wa aina
gani !
Hesabu 13:17-20 “Musa akawapeleka ili waipeleleze nchi ya Kanaani,
akawaambia, Pandeni sasa katika Negebu mkapande milimani, mkaitazame nchi ni ya
namna gani; na watu wanaokaa ndani yake, kwamba ni hodari au dhaifu, kwamba ni
wachache au wengi;na nchi wanayoikaa kwamba ni njema au mbaya; kwamba wanakaa
katika matuo au katika ngome;”
Yoshua 2:1-2 “Yoshua, mwana wa Nuni, akawatuma watu wawili kutoka
Shitimu kwa siri, ili kupeleleza, akawaambia, Enendeni mkaitazame nchi hii, na
Yeriko. Wakaenda wakafika nyumbani kwa kahaba mmoja jina lake aliitwa Rahabu,
wakalala huko. Mfalme wa Yeriko akaambiwa, kusema, Tazama, watu wawili wa wana
wa Israeli wameingia humu leo usiku, ili kuipeleleza nchi.”
Yoshua 7:2-3 “Kisha Yoshua akatuma watu kutoka Yeriko mpaka mji wa Ai,
ulio karibu na Bethaveni, upande wa mashariki wa Betheli, akawaambia, akisema,
Pandeni juu mkaipeleleze nchi, basi wakapanda juu wakaupeleleza Ai. Wakarejea
kwa Yoshua wakamwambia, Wasiende watu wote, ila waende watu kama elfu mbili,
tatu, wakaupige Ai; usiwataabishe watu wote kwa kuwaendesha huko; maana watu
hao ni wachache tu.”
3. Tutambue nyumba na mwenyeji wetu – Kanisa
la nyumbani linaitwa la nyumbani kwa sababu linafanyia ibada zake katika sebule
za watu, kila mtu anaustaarabu wake na anaipenda sebule yake, kwa hiyo
kukaribisha watu katika sebule yako ili kufanyike ibada ni kujitoa katika hali
ya juu sana sio swala jepesi, lakini jambo hili Mungu analiheshimu na
kusababisha Baraka, utoaji wa nyumba au mahali kwaajili ya kuabudia linapaswa
kuwa jambo la hiyari na sio la kulazimishwa, mtu anayejitoa nyumba yake sio
lazima iwe nzuri au kamili bali anaitoa kwaajili ya Bwana mtu huyu Mungu
atamheshimu sana na kumbariki mno, Mungu aliibariki nyumba ya Oded-Edom kwa sababu alikubali Sanduku
la Agano la Bwana Mungu wa Israel likae nyumbani mwake, Mtu anayekubali nyumba
yake iwe sehemu ya kufanyia ibada hana tofauti na Obedi- Edom
Luka 10:5-7 “Na nyumba yo yote mtakayoingia, semeni kwanza, Amani
iwemo nyumbani humu; na akiwamo mwana wa amani, amani yenu itamkalia; la,
hayumo, amani yenu itarudi kwenu. Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na
kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame
kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii.”
2Samuel 6:10-12. “Basi Daudi hakutaka kulileta sanduku la Bwana kwake mjini
mwa Daudi; ila Daudi akalihamisha nyumbani kwa Obed-edomu, Mgiti. Sanduku la
Bwana akalitia katika nyumba ya Obed-edomu, Mgiti, muda wa miezi mitatu; naye
Bwana akambarikia Obed-edomu, na nyumba yake yote. Kisha mfalme Daudi akaambiwa
ya kwamba, Bwana ameibarikia nyumba ya Obed-edomu, na vitu vyote alivyo navyo
kwa ajili ya sanduku la Mungu. Daudi akaenda, akalileta sanduku la Mungu, toka
nyumba ya Obed-edomu mpaka mji wa Daudi, kwa shangwe.”
4. Weka viongozi waliopitia shule ya huduma – Baada
ya kuwa tumepata haya yote tunaweka viongozi wetu ambao wamejifunza kutoka kwetu
wana mafundisho yetu yaliyo sahihi, walio waaminifu kwetu, wanaotii uongozi,
wanaojua kuhudumia watu wenye Imani yetu, viongozi hao ni viongozi watumisi na
sio wachungaji wenye mamlaka kamili ya kichungaji
Matendo 14:21-23 “Hata walipokwisha kuihubiri Injili katika mji ule, na
kupata wanafunzi wengi, wakarejea mpaka Listra na Ikonio na Antiokia, wakifanya
imara roho za wanafunzi na kuwaonya wakae katika ile Imani, na ya kwamba
imetupasa kuingia katika ufalme wa Mungu kwa njia ya dhiki nyingi.Na
walipokwisha kuwachagulia wazee katika kila kanisa, na kuomba pamoja na
kufunga, wakawaweka katika mikono ya Bwana waliyemwamini.”
Mfumo wa ibada katika makanisa ya nyumbani haupaswi kuzidi saa moja
- Utafungua
kwa maombi.
- Itafanyika
ibada ya kusifu na kuabudu kwa ufupi.
- litahubiriwa
neno la Mungu la kibiblia na sio maoni ya mtu (sawa na mafundishio katika
kanisa letu) tunakuwa na mafundisho maalumu na tutayagawa kwa walimu wa
makanisa ya nyumbani na watafundisha kwa kadiri watakavyokuwa wanapangiwa
na kiongozi husika.
- Ushirika,
maswali, maombi na maombezi, na taarifa za ufuatiliaji.
- Kufunga
kwa maombi.
Hakuna kanisa la nyumbani
linalotakiwa kujiendesha kinyume na utaratibu uliowekwa na kanisa mama ambalo
ndilo lenye mamlaka ya mwisho.
Kama kanisa la nyumbani litakapokuwa
kubwa taarifa itatolewa na litalazimika kugawanywa na kuwa na kiongozi mwingine
aliyepitia shule ya huduma
Kiongozi wa kanisa la nyumbani
jihadhari na mafundisho potofu. Jilinde na uasi au kulikata kundi, jihadhari
kuligeuza kanisa kuwa klabu ya maswala ya kijamii na michango ya upatu kila
kitu kifanyike kwakufuata utaratibu usafi na ushuhuda mwema wa Kirsto
Kanisa la nyumbani sio mfumo au
wazo jipya ni mpango wa Mungu wa kibiblia tangu zamani za mitume na kwa kufanya
hivi waliupindua ulimwengu
Kama ilivyo kwa watenda kazi
kiongozi wa kanisa la nyumbani atawajibika kutoa taarifa katika mfumo
utakaowekwa na kanisa kuu.
1Wakorintho 14:40 “Lakini mambo yote na
yatendeke kwa uzuri na kwa utaratibu.”
Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni