Jumatatu, 24 Julai 2017

Bwana asipoulinda mji,Yeye aulindaye akesha bure.!

Mstari wa msingi: Zaburi 127:1-2 “Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji Yeye aulindaye akesha bure. Kazi yenu ni bure, mnaoamka mapema, Na kukawia kwenda kulala, Na kula chakula cha taabu; Yeye humpa mpenzi wake usingizi”

Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kila mwanadamu anatamani kufanikiwa katika maeneo mbalimbali ya Maisha, Hakuna mwanadamu asiyetamani kuwa na familia nzuri, nchi nzuri,mji mzuri, ulinzi na usalama au kuepushwa kutoka katika mauaji na uasi wa namna mbalimbali, mafanikio kazini, Mafanikio katika biashara,mafanikio katika masomo,amani katika ndoa, afya njema, Ushindi katika vita au dhidi ya adui zako,Mafanikio katika ibada na kadhalika, Ni kwaajili ya hayo wanadamu wanaweza kuhangaika huko na huko na kuweka juhudi zao zote, Maarifa yao yote na akili zao zote, katika kuhakikisha kuwa wanayafanikisha hayo.

Katika kifungu hiki cha maandiko ya Zaburi, ambayo inasadikiwa kuwa ni iliandikwa na Sulemani tunapata kiini kikuu kwamba JUHUDI ZA MWANADAMU PEKEE BILA UWEPO WA MUNGU NI BURE, Katika kifungu hiki mwandishi hapingi kabisa hali ya kuwa na bidii, lakini anazungumzia bidii bila Mungu anataka tumshirikishe Mungu au kumuweka Mungu katika nafasi ya kwanza kuliko maswala mengine tunayoyapa kipaumbele!

 "Bwana asipoijenga nyumba Waijengao wafanya kazi bure"

Familia.

Biblia inaonyesha kuwa tunamuhitaji Mungu katika Familia zetu na katika ujenzi wa nyumba zetu, bidii ya aina yoyote ya kujenga familia au nyumba bila uwepo wa Mungu au kufanya kazi kwa bidii huku ukiwa umemtupa Mungu nje au huku Mungu akiwa ameondoa mkono wake ni bidii ya bure.
Yesu Kristo katika mafundisho yake ameunga mkono swala la kumuweka Mungu au yeye mbele zaidi hata ya familia zetu, Yeye anataka nini hasa anataka tumuweke yeye mbele kwanza hata katika familia zetu, na katika mioyo yetu na akili zetu na hata nguvu zetu, angalia katika Mathayo 10:37, 22:37,

Mathayo 10:37 “Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili” Mathayo 22:37 “Akamwambia, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.” Biblia inataka kutufundisha kuwa ustawi wa familia zetu unamuhitaji Mungu na kwamba kila mtu anayehitaji familia bora ni lazima amuweke Mungu mbele.

Ulinzi.

Mwanadamu anapofanikiwa sana au nchi au taifa linapoteza kujiamini, na kwa sababu hiyo uhitaji wa Ulinzi na usalama hujitokeza, Hapo ndipo unapokuta majumba yakizungushiwa kuta kubwa sana na mageti na milango ya chuma na kampuni za ulinzi, Makusudi makubwa ya kutafuta ulinzi ni pamoja na kutunza zile Baraka ambazo Mungu ametupa, Hata hivyo kanuni ambayo sulemani anatufundisha hapa ni kuwa si vibaya kuwa na ulinzi lakini ni lazima tusimame katika msingi nwa maandiko kuwa Mlinzi wetu wa kweli ni Mungu tu Zaburi 121:1-8 “Nitayainua macho yangu niitazame milima, Msaada wangu utatoka wapi? Msaada wangu u katika Bwana, Aliyezifanya mbingu na nchi. Asiuache mguu wako usogezwe; Asisinzie akulindaye; Naam, hatasinzia wala hatalala usingizi, Yeye aliye mlinzi wa Israeli. Bwana ndiye mlinzi wako; Bwana ni uvuli mkono wako wa kuume. Jua halitakupiga mchana, Wala mwezi wakati wa usiku. Bwana atakulinda na mabaya yote, Atakulinda nafsi yako. Bwana atakulinda utokapo na uingiapo, Tangu sasa na hata milele.”

Katika kazi zetu.

Nimapenzi ya Mungu kila mtu afanye kazi, na kila mtu asome kwa bidii, kufanya kazi ni kuishi kwa hekima, lakini vilevile kufanya kazi kutasaidia kupata mahitaji yetu kwaajili ya familia zetu, 1Thesalonike 4:11-12, “Tena mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza; ili mwenende kwa adabu mbele yao walio nje, wala msiwe na haja ya kitu cho chote.”Lakini pamoja na kufanya kazi zetu kwa bidii kwa kusudi la kujipatia mahitaji yetu nay a familia zetu ili tusiombeombe tusiwe na haja ya kitu chochote Biblia inasisitiza umuhimu wa kumuweka Mungu mbele katika kila tulifanyalo, Mafanikio ya kweli yanamuhitaji Mungu kwanza Biblia inaonyesha kuwa unaweza kujikusanyia kwa bidii zako zote kisha Mungu akampa mwingine Muhubiri 2:26, Yesu anashauri kwamba afhadhali kuutafuta ufalme wa Mungu kwanza Mathayo 6:33

Vita

Mara zote kunapotokea vita watu hutamani kupata ushindi katika vita hiyo, na ni kwa sababu hiyo kila taifa hujitahidi kuwa na jeshi lililo hodari na lenye uzoefu wa vita , lakini vile vile kununua silaha kali sana na kujiandaa kwa mapambano Biblia inaonyesha kuwa maandalizi ya vita hayakuhakikishii ushindi ni Mungu pekee anayeweza kuleta ushindi Mithali 21:31, “Farasi huwekwa tayari kwa siku ya vita, lakini Bwana ndiye aletaye wokovu” Zana za kivita hazikuhakikishii ushindi, ushindi wa kweli unaletwa na Mungu mwenyewe kwa wale wanaozingojea fadhili zake, Mataifa mengi makubwa katika historia ya dunia yalianguka kwa asababu ya kiburi na kutokumtegemea Mungu Zaburi 33:16-21 “Hapana mfalme aokokaye kwa wingi wa uwezo, Wala shujaa haokoki kwa wingi wa nguvu. Farasi hafai kitu kwa wokovu, Wala hamponyi mtu kwa wingi wa nguvu zake. Tazama, jicho la Bwana li kwao wamchao, Wazingojeao fadhili zake. Yeye huwaponya nafsi zao na mauti, Na kuwahuisha wakati wa njaa. Nafsi zetu zinamngoja Bwana; Yeye ndiye msaada wetu na ngao yetu. Maana mioyo yetu itamfurahia, Kwa kuwa tumelitumainia jina lake takatifu”

Akili.
Mithali 3:5-6 Watu wengi sana wamefikiri kuwa kuwa na akili ndio suluhisho la kila kitu, lakini akili na ujuzi visipotumika kwahekima na kwa kumtegenmea Mungu kamwe haviwezi kutuletea ufanisi tunaoukusudia Mithali 3:5-7 Biblia inasema “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako.Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu”

Hitimisho:

Ni muhimu kukumbuka kuwa katika kila tulifanyalo hatuna budi kumshirikisha Mungu, chochote tunataka kukifanya ni Muhimu Mungu akawekwa mbele, Ujuzi wetu na utaalamu wetu na bidii yetu, na akili zetu lazima zikubali kuangalia Yesu anasema nini vinginevyo tunaweza kuvua samaki usiku kucha bila kupata kitu Luka 5:4-6. “Hata alipokwisha kunena, alimwambia Simoni, Tweka mpaka kilindini, mkashushe nyavu zenu mvue samaki. Simoni akajibu akamwambia, Bwana mkubwa, tumefanya kazi ya kuchosha usiku kucha, tusipate kitu; lakini kwa neno lako nitazishusha nyavu. Basi, walipofanya hivyo walipata samaki wengi mno, nyavu zao zikaanza kukatika;”

“Unaweza kuamka Mapema na kukawia kwenda kulala na kula kwa kujinyima sana Lakini Mungu akiwa Kipenzi chako utalala Usingizi mtamu tu” Mathayo 6:33 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. ”

Mungu akubariki kwa kuchagua kumtanguliza yeye katikakila Jambo!

Na Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!

Maoni 9 :

Unknown alisema ...

nimeipenda barikiwa pastor

Unknown alisema ...

Hakika MUNGU ni mkuu katika wakuu wote.na yeye u wa kutumainiwa.Yatupasa kumuumba muda wote na kumtumikia pia.

Kelvin vulla alisema ...

Hakika Mungu ni pendo na anatupenda wote licha ya madhaifu yetu. Tumtegemee yeye siku zote za maisha yetu

Bila jina alisema ...

Mafundisho mazuri Sana mungu awajaze na hekima maarifa na ufahamu muweze kusaidia wale ambao hawajafika kiwango cha juu wafike katika jina la yesu

Bila jina alisema ...

Ubarikiwe Mtumishi

Bila jina alisema ...

kuna namna nilikuwa nimekata tamaa na kuona kama vile bidii zangu ni bure. ndipo asubuhi moja Roho akanikumbusha juu ya Neno hili kutoka Zaburi. upon searching it on google nikakutana na blog hii na neno hili. nikakumbushwa jambo muhimu sana. juhudi zangu nilikuwa naona kama kukamata upepo kwa sababu nilikuwa nimemuweka Mungu kando na kutegemea juhudi zangu tu. asante Rev Kamote! Mungu akubariki sana!! Hakika ni Mungu tu anayeweza kufanikisha mipango yangu na juhudi zangu.

Bila jina alisema ...

Mungu awe mtangulizi wa kila jambo ninalotenda,anipa amani,ateta na adui zangu,Mungu akuzidishie mnenaji wa hili neno

Bila jina alisema ...

Nimebarikiwa sana na chapisho hili

Bila jina alisema ...

Amina.Mungu akubariki.