Jumanne, 11 Aprili 2023

Baba Mikononi mwako Naiweka Roho yangu!


Luka 23:44-46 “Hapo ilikuwa yapata saa sita, kukawa giza juu ya nchi yote hata saa kenda, jua limepungua nuru yake; pazia la hekalu likapasuka katikati. Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu.”

Utangulizi:

Tunaendelea kujifunza kuhusu maneno ya Yesu aliyoyasema pale msalabani, ambayo yana maana pana sana kama utapata nafasi ya kujifundisha moja baada ya jingine, Leo nataka kuzungumzia kuhusu maneno ya mwisho miongoni mwa maneno saba aliyoyazungumza Yesu pale msalabani ambalo ni BABA MIKONONI MWAKO NAIWEKA ROHO YANGU!, Maneno haya ni sehemu ya maombi aliyokuwa akiyaomba Bwana Yesu Pale msalabani kwa kutumia Zaburi, yeye alipaza sauti kubwa sana na kuyasema maneno haya na kisha akakata roho, watu wengi sana huyaogopa maneno haya wakidhani ya kuwa ukiyasema basi utakuwa unajitakia kifo, au unaweza ukayasema inapofika saa yako ya mwisho, lakini maneno haya yana maana tofauti kabisa na namna ambavyo wengi wetu tumefikiri kwa siku nyingi, hata hivyo kabla ya kuyafanyia uchambuzi na upembuzi yakinifu ni vema kwanza tukajikumbusha tena maneno mengine katika maneno yote saba aliyoyasema Bwana Yesu Pale msalabani, maneno hayo ni pamoja na :-

·         Baba uwasamehe kwa maana hawajui walitendalo Luka 23:34

·         Amin nakuambia leo hii utakuwa pamoja nani peponi Luka 23:43

·         Mama tazama mwanao, mwana tazama mama yako Yohana 19:26-27

·         Mungu wangu Mungu wangu mbona umeniacha Mathayo 27:46

·         Nina kiu Yohana 19:28

·         Imekwisha Yohana 19:30

·         Baba mikononi mwako naiweka roho yangu Luka 23:46

Baba mikononi mwako naiweka roho yangu

Kama tulivyoona ya kwamba maneno haya BABA MIKONONI MWAKO NAIWEKA ROHO YANGU Yalizungumzwa na Bwana Yesu kama maneno ya mwisho pale msalabani na kisha Yesu akakata roho na matukio mengi ya kushangaza yakajitokeza wakati mwana wa Mungu akikata roho, Maandiko haya ya msingi yanatuambia hivi tuone tena:-

 Luka 23:46 “Yesu akalia kwa sauti kuu, akasema, Ee Baba, mikononi mwako naiweka roho yangu

kimsingi maneno haya yana asili ya Lugha ya kiibrania na yanatoka moja kwa moja katika Zaburi ya 31:5 thelathini na moja, mstari wa tano, Na hivyo kimsingi Mwandishi au waandishi wa agano jipya waliruka maneno muhimu kutoka katika zaburi hii ambayo yana maana pana sana nay a muhimu  linapokuja swala la kufufuka kwa Yesu na sikukuu ya Pasaka, labda waandishi walikuwa na dhana kama yetu ya kufikiri kuwa Yesu alikuwa amevuta pumzi yake ya mwisho ya uhai na kuamua kufa kwa kukabidhi roho yake kwa baba yake, basi. Lakini maneno haya yanasomeka namna hii katika Zaburi yenyewe ya asili ambayo Yesu alikuwa akiinukuu kama maombi pale msalabani  ona -

Zaburi ya 31:5 “Mikononi mwako naiweka roho yangu; Umenikomboa, Ee Bwana, Mungu wa kweli.”

Aidha ili ieleweke vema pia zaburi hii katika kiingereza inasiomeka namna hii hasa kwa tafasiri ya Biblia ya kiingereza ya ESV yaani “English Standard Version” yanasomeka hivi Psalm 31:5 “Into your hand I commit my spirit; you have redeemed me, O LORD, Faithful God”, Kwa msingi huo pale msalabani Yesu alikuwa anasali kwa kunukuu Zaburi ya 31:5 akiwa katika hali ya mateso makali mno wakati akiwa katika hali yake ya mwilini duniani akiteseka maneno aliyoyasema Yesu kwa tafasiri ya ESV yalitakiwa kusomeka hivi MIKONONI MWAKO NAIWEKA ROHO YANGU,UMENIKOMBOA EE BWANA, MUNGU MWAMINIFU, Kwa hiyo utakubaliana nami kuwa kuna maneno ya msingi yalirukwa au yalipoteza maana wakati wa kufanya tafasiri katika lugha mbalimbali, nataka sasa nikuchukue taratibu ili iweze kujua kwa uwazi maneno haya na maana yake namna yalivyo na nguvu kuliko tunavyoweza kufikiri utanielewa tu, kwanza tuangalia neno NAIWEKA kwa undani kisha tuunganishe na maneno yaliyorukwa katika Luka 23:46 na kuyaona kwa uhalisia wake katika Zaburi 31:5

Usemi huo unakubaliana wazi kabisa na Lugha za kiibrania na kiyunani ambapo neno NAIWEKA ROHO YANGU kwa kiingereza “I COMMIT” katika lugha ya Kiibrania linatumika neno “AFKID” na kiyunani neno “DIAPRATO”, Neno la kiibrania AFKID kwa kiingereza linasomeka kama “I DEPOSIT” ambalo Kiswahili chake ni kuweka amana au kuacha kitu cha thamani kubwa mfano fedha kwa mtu au taasisi unayoiamini kwa kusudi la kuja kuchukua kitu hicho baadaye, mfano ni kama vile tunavyoweka fedha zetu bank na kisha tunakuwa na haki au uhakika wa kuzichukua wakati wowote unaona!, na neno la kiyunani “DIAPRATO” kwa kiingereza “ENTRUST” ambalo maana yake kukabidhi jukumu Fulani muhimu kwa mtu unayemuamini kuwa atalifanya, atalinda na kukuwakuilisha salama, Hatakuangusha. Kama Neema ya Mungu itakuwa imefunuliwa kwako sasa utakuwa umefahamu kuwa  Yesu aliposema BABA MIKONONI MWAKO NAIWEKA ROHO YANGU, kama alinukuu Zaburi 31:5 Basi Yesu alikuwa akisema maneno haya “BABA MIKONONI MWAKO NAIWEKA AMANA ROHO YANGU, UMENIKOMBOA EE BWANA, MUNGU MWAMINIFU.

Hii maana yake ni nini maana yake Yesu alipaza Sauti yake kwa imani pasipo shaka akatamka kwa uhakika kuwa anaiweka Roho yake amana kwa Mungu mwaminifu na ambaye anaweza kumrejeshea na sio anaweza kukaa nayo jumla jumla, Yesu aliamini katika uweza wa baba yake ya kuwa anauweza wa kuirejesha Roho yake tena na sio hivyo tu yeye mwenyewe anauwezo wa kuichukua atakapokua anaitaka kama wewe unavyoweza kuchukua fedha zako kutoka katika bank wakati unapotaka, Hii maana yeke ni kuwa Yesu kristo aliutoa uhai wake yeye mwenyewe  na hakuna mtu anayeweza kumuondolea uhai, lakini licha ya kuutoa mwenyewe yeye pia anauwezo wa kuutwaa tena uhai wake au roho yake, Aidha tunajifunza kuwa maneno yale yalikuwa na maana ya kuiweka roho yake kwa muda tu, na kisha ataichukua tena, kwa hiyo kukata roho kwa Yesu kulikuwa ni kwa muda na kuwa angafufuka tena !

Yohana 10:17-18 “Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.”

Kwa msingi huo Yesu alimaanisha kuwa hakuna anayeweza kuuondoa uhai wake hapa inajumuisha kila kitu mbinguni na duniani hakuna anayeweza kuiondoa uhai wake, kifo cha Msalabani ilikuwa ni hiyari yake mwenyewe kwaajili ya kuwakomboa wanadamu na ndio maana anapendwa na baba  kwa sababu hakuna aliyemshurutisha, Yesu anayo mamlaka ya kuyatoa maisha yake na anayo mamlaka ya kuyachukua tena, hivyo ni kwa hiyari yake mwenyewe kwa kawaida yeye humuheshimu baba yake, na hafanyi neno Bila kuagizwa na baba hasa alipokuwa Duniani neno linasema:-

Yohana 5;19  Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda; kwa maana yote ayatendayo yeye, ndiyo ayatendayo Mwana vile vile.”

Yesu anazungumza hii katika hali ya ubinadamu wake hali ya kumtegemea baba yake akiwa duniani, hali ya kujinyenyekeza, lakini neno lake baba mikononi mwako naiweka roho yangu linatufungulia akili kujua uweza na mamlaka kubwa aliyonayo Yesu Kristo, lakini linatuthibitishia kuwa alikuwa na uhakika wa kufufuka!

Yesu hakufa kama afavyo mchuuzi, ulikuwa ni mpango wake kamili wa kumuokoa mwanadamu, mpango ambao baba wa mbinguni alifurahishwa nao, kwa mamlaka hii, tunaweza kukabidhi chochote kwake, na anauwezo wa kuturejeshea, kama kuna vitu tulipokonywa au kuumizwa au kuibiwa au kudhulumiwa vyovyote iwavyo tunaye Yesu mwenye uwezo wa kuturejeshea maradufu yeye anauwezo wa kufisha na kuuhisha, anajeruhi na anaponya, nani yeye mwenye uwezo wa kuokoa hivyo kama kuna kitu kimepotea katika maisha yetu iwe amani, furaha na kadhalika Huyu Yesu anauwezo mkubwa ana mamlaka kubwa yeye ni Mungu na anajitambulisha kuwa hakuuawa isipokuwa ilikuwa kwa hiyari yake ni sadaka aliyojitoa yeye anauwezo wa kuutoa uhai wake na kuuchukua tena na anaweza kufanya hivyo na lolote kwa yeyote akimtumainia yeye, Maandiko yanasema!  

Kumbukumbu 32:39 “Fahamu sasa ya kuwa Mimi, naam, Mimi ndiye, Wala hapana Mungu mwingine ila Mimi; Naua Mimi, nahuisha Mimi, Nimejeruhi, tena naponya; Wala hapana awezaye kuokoa katika mkono wangu,”

Hakuna jambo la Msingi kama kukabidhi maisha yetu, mali zetu, ndoa zetu, kazi zetu, watoto wetu, waume zetu, wake zetu, mashamba yetu, magari yetu, afya zetu, na lolote lila katika mikono salama ya baba wa mbinguni ambaye tunajua anaweza kulinda kile tunachiomkabidhi, hakikisha kuwa katika maisha yako unamkabidhi Mungu mwaminifu maisha yako kwa sababu yeye anauwezo wa kutunza, kulinda na kukurejeshea kila kinachopotea ni kwa Mungu pekee ndipo tunapokuwa na uhakika wa kurejezewa kila kilichopotea endapo kweli katika maisha yetu tulimkabidhi yeye, watu wengi wamekabidhi maisha yao na mali zao kwa watu mabaradhuli na wakapoteza Yesu anatukumbusha kuwa ukijikabidhi kwa Mungu mwaminifu hakuna cha kupoteza ! ni muhimu wakati huu wa msimu wa Pasaka kukabidhi maisha yetu kwa Mungu mwaminifu yeye atayarejesha tena yatakapopotea kwa sababu yoyote ile, tukiamini kazi aliyoifanye Yesu Msalabani hakika yeye naye atatufufua siku ya mwisho

Yohana 6:53-54 “Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho.”

Na Rev Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!



Hakuna maoni: