Ijumaa, 11 Agosti 2023

Chapa za Yesu !


Wagalatia 6:17-18 “Tangu sasa mtu asinitaabishe; kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu. Ndugu zangu, neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu. Amina.”



Utangulizi:

Wagalatia 6:17-18 “Tangu sasa mtu asinitaabishe; kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu. Ndugu zangu, neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu. Amina.”

Leo tutachukua muda kutafakari kwa kina maneno ya mkuu wa wajenzi mwenye hekima yaani  Paulo mtume alipokuwa anamalizia waraka wake kwa Wagalatia, Paulo hapa alikuwa akiwaaga Wagalatia na kuwaonya kuwa wakae katika kweli, Ambayo kwaajili ya hiyo yeye aliitesekea huku akiamini kuwa watayashika Mafundisho yakeTangu sasa mtu asinitaabishe kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesuhuenda haya yalikuwa ni maneno yake ya mwisho na yenye kuonyesha msimamo wake imara kuhusiana na uhusiano wake na Kristo, endapo Wagalatia hawatajali habari ya injili na njia ile aliyokuwa amewahubiri, Msimamo anaouweka Paulo hapa unafanana sana na ule Uliowekwa na Yoshua kwa wana wa Israel  katika hutuba yake ya mwisho kwamba wachague ni nani watakayemtumikia lakini yeye na nyumba yake wameamua kumtumikia Bwana. Ona:-

Yoshua 24:14-15 “Basi sasa mcheni Bwana, mkamtumikie kwa unyofu wa moyo na kwa kweli; na kuiweka mbali miungu ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, na huko Misri; mkamtumikie yeye Bwana. Nanyi kama mkiona ni vibaya kumtumikia Bwana, chagueni hivi leo mtakayemtumikia; kwamba ni miungu ile ambayo baba zenu waliitumikia ng'ambo ya Mto, au kwamba ni miungu ya wale Waamori ambao mnakaa katika nchi yao; lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana.”  

Ni katika mazingira kama hayo Paulo mtume alikuwa akiwaonya Wagalatia kuifuata injili iliyo sahihi na mafundisho yaliyo sahihi ambayo yeye aliwaelekeza, Lakini mwanzoni alionyesha masikitiko yake vilevile kuwa wako watu waliowafundisha makanisa ya Galatia kushika sheria kadhaa ikiwemo kutahiriwa jambo ambalo halikuwa na ulazima katika wokovu wa mwanadamu lakini Wagalatia wengi waligeuka na kusahau mafundisho sahihi na badala yake wakawa wakirejea kwenye mafundisho manyonge yenye upungufu:-

Wagalatia 4:9-11. “Bali sasa mkiisha kumjua Mungu, au zaidi kujulikana na Mungu, kwa nini kuyarejea tena mafundisho ya kwanza yaliyo manyonge, yenye upungufu, ambayo mnataka kuyatumikia tena? Mnashika siku, na miezi, na nyakati, na miaka. Nawachelea, isiwe labda nimejitaabisha bure kwa ajili yenu.

Paulo alionya wazi kuwa wale wanaohubiri injili inayounga mkono maswala ya sheria kama tohara wanafanya hivyo kwa kuogopa mateso, Kwani kila mtu anayeihubiri kweli ya injili kama ilivyo Wayahudi walikuwa wakimuudhi na wakali sana na waliendesha msako mkali wa mateso ambayo Paulo mtume yalimkuta mara kadhaa

 

Wagalatia 6:11-14 “Tazameni ni kwa herufi gani kubwa nimewaandikia kwa mkono wangu mimi mwenyewe! Wote watakao kuonekana ni wazuri kwa mambo ya mwili, ndio wanaowashurutisha kutahiriwa; makusudi wasiudhiwe kwa ajili ya msalaba wa Kristo, hilo tu. Kwa maana hata wao wenyewe waliotahiriwa hawaishiki sheria; bali wanataka ninyi mtahiriwe, wapate kuona fahari katika miili yenu. Lakini mimi, hasha, nisione fahari juu ya kitu cho chote ila msalaba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambao kwa huo ulimwengu umesulibishwa kwangu, na mimi kwa ulimwengu.”

 

Ni kwaajili ya hayo Paulo mtume anaonyesha kuwa amekwisha kuiweka kweli wazi na amekwisha kuwaandikia Wagalatia na amekwisha kuwapa injili ya kweli na kuwaonya na ni wao ndio wenye maamuzi ya kuamua kuifuata njia sahihi na mafundisho sahihi ya Kristo au la  na yeye kuonyesha msimamo wake kuwa yeye anaendelea kuubeba msalaba na kuwa yuko tayari kuteseka kwaajili ya Kristo na hatachuja kwa namna yoyote kiwango cha injili anayoihubiri  na kuwa yeye yuko tayari na amekwishateseka na ataendelea kuteseka kwaajili  ya injili ya Kristo,  Yeye anawapenda sana Wagalatia  na ni watoto wake aliowazaa mwenyewe kiroho, lakini anashangazwa wanapoigeukia injili nyingine! Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-

*      Maana ya neno chapa.

*      Kuchukua chapa za Yesu Kristo.

Maana ya neno chapa

Wagalatia 6:17-18 “Tangu sasa mtu asinitaabishe; kwa maana ninachukua mwilini mwangu chapa zake Yesu. Ndugu zangu, neema ya Bwana wetu Yesu Kristo na iwe pamoja na roho zenu. Amina.”

Neno Chapa linalotumika katika maandiko hapo katika Biblia ya kiyunani linatumika neno STIGMA ambalo asili ya neno hilo ni STIZO ambalo kwa kiingereza linafafanuliwa kama - incised Mark au a punched Mark for recognition of ownership yaani ni alama isiyofutika au chanjo inayowekwa katika mwili wa mnyama au mtumwa kwaajili ya kutambua kuwa ni mali ya mtu Fulani, chapa hii pia hutumika kuelezea alama za huduma ya askari yaani SCAR OF SERVICE yaani majeraha ya askari aliyeshiriki vita za aina mbalimbali.

Nyakati za Biblia wakati wa zama za agano jipya lilipokuwa likiandikwa  watu waliokuwa na alama au chapa au makovu walikuwa ni watu wa aina tatu, Watumwa, Askari na Watawa hawa walikuwa na alama au makovu yaliyotokana na shughuli zao, Askari hususani waliokuwa na uzoefu wa vita mbalimbali walijulikana pia kwa kuwa na makovu ya aina mbalimbali katika miili yao, Watumwa nao walikuwa na alama za moto ambapo mmiliki wa mtumwa angeweka chombo maalumu katika moto na kumuweka alama mtumwa wake kuonyesha kuwa mtumwa huyo anamilikiwa na Bwana wake na kuwa hana uwezo wa kumilikiwa na mtu mwingine, lakini na watawa Devotee watu walioamua kujitoa kwa ajili ya Mungu walikuwa pia na alama za kuonyesha kuwa wao ni mali ya Mungu,kwa maisha yao ya kujikana mtindo wao wa maisha na mavazi, ni Katika wazo kama hili Paulo mtume anaonyesha wazi kuwa mwili wake umejaa majeraha kama askari aliyejeruhiwa katika vita za aina mbalimbali, lakini vilevile yeye kama mtumwa wa Yesu Kristo anaendelea kuchomwa na kuwekwa alama hizo kama mtumwa asiyelipwa au mtumwa asiye na faida, akiwa na alama nyingi za mateso kwaajili ya Yesu Kristo,  alama hizi ni changamoto mbalimbali na upinzani wa aina mbalimbali aliokutana nao kwaajili ya injili, aidha mtindo wake wa maisha na mwenendo na tabia zake zinaendelea kukua na kuwa kama za Kristo akidhihirisha ya kuwa yeye ni mtu aliyejiotoa kwa Yesu Ona:-

2Wakorintho 11:21-27 “Nanena kwa jinsi ya kujidhili kana kwamba sisi tulikuwa dhaifu. Walakini, akiwa mtu anao ujasiri kwa lo lote, (nanena kipuuzi), mimi nami ninao ujasiri. Wao ni Waebrania? Na mimi pia. Wao ni Waisraeli? Na mimi pia. Wao ni uzao wa Ibrahimu? Na mimi pia. Wao ni wahudumu wa Kristo? (Nanena kiwazimu), mimi ni zaidi; katika taabu kuzidi sana; katika vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi. Kwa Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi; kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; katika kusafiri mara nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang'anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi.”

 

Paulo sasa amekuwa mtu mzima kama ungeweza kumuona hungeweza kufurahia sura yake iliyoharibiwa na iliyojaa makovu, mikono inayotetemeka kwa vipigo, majeraha ya kuumizwa katika vipigo vya aina mbalimbali, kule Filipi alipigwa na kutiwa gerezani, huko Listra alipigwa mawe mpaka akapoteza fahamu, huko Melita alivunjikiwa na jahazi  haya yote yalimfanya mtume huyu aliyekuwa mrefu mwembamba na mwenye macho ya bluu na matege miguuni, na nywele zilizokuwa zimejisokota kuwa na sura ya Yesu aliyesulubiwa, Paulo hakuwa anatafuta umaarufu, wala hakuwa mnenaji hodari kama wanafalsafa wa kiyunani, alidharaulika na kukataliwa, Hakuna mtu katika nyakati za kanisa la kwanza aliyekuwa anatafuta kuwa maarufu, kila mmoja alikuwa akiihubiri injili na kuifanya kazi ya Mungu kwa moyo na wengi waliumizwa vibaya walitiwa magerezani  walikuwa kama askari waliopigana vita nyingi wakiwa na makovu ya mwilini na moyoni,  Kimsingi Mtume amekwisha kuiweka kweli hadharani, ni wajibu wao sasa wagalatia kuyashika aliyowafundisha lakini yeye anachukua alama za Kristo, yeye anabaki na msimamo mkali wa kumfuata Yesu kama alivyo hana mpango wa kurejea nyuma bali kushikamana na hatua zake Kristo, akikubali kuteseka kwaajili ya Kristo lakini vilevile kukua kiimani na kuendelea kukua kitabia na kiuadilifu kufika kwenye ubora wa tabia na mwenendo kama aliokuwa nao Kristo!;-

Kuchukua chapa za Yesu Kristo.

Kimsingi kama tulivyoona hapo awali kwamba waliokuwa na alama hizo walikuwa ni Watumwa, Askari na watawa, Watumwa waliwekwa alama ya utumwa na Bwana wao kuonyesha kuwa wanamilikiwa alama hizo zilipatikana kwa chuma kupashwa moto na kisha wakachomwa na kubaki na alama hiyo kudhihirisha kuwa wao ni watumwa wa mtu fulani milele na hawawezi kuepuka, Askari nao walikuwa na alama za mkuu wa majeshi yao ili wasiweze kabisa kujitoa kutoka kwa kamanda wao, lakini vilevile alama za makovu zilizodhihirisha kuwa walishiriki vita nyingi na wanauzoefu wa vita na waliojitoa kuishi maisha ya utawa walijitoa kwa Mungu waliwekwa alama hizo  na kuhani, wakionyesha kwa maisha yao na mwendo wao kuwa wao wamejitoa kuishi kwaajili ya Mungu, alama hizo kwa kuwa ziliwekwa kwa moto ziliacha majeraha au makovu katika miili yao, Kimsingi alama ya utumwa pia ilikuwa ni alama ya aibu na sio ya heshima,  Paulo anautumia mfano huo kujitangaza kuwa yeye ni Mtumwa wa Yesu Kristo asiye na faida  ni kama hawezi kumtoroka Kristo yeye ni mfungwa kwake, na zaidi ya yote yuko tayari kuishi kwaajili ya Kristo akifuata nyayo zake na tabia zake na mwendo wake:-  

Filemoni 1:1 “Paulo, MFUNGWA wa Kristo Yesu, na Timotheo aliye ndugu yetu, kwa Filemoni mpendwa wetu, mtenda kazi pamoja nasi, na kwa Afia, ndugu yetu, na kwa Arkipo askari mwenzetu, na kwa kanisa lililo katika nyumba yako. Neema na iwe kwenu, na amani, zitokazo kwa Mungu, Baba yetu, na kwa Bwana Yesu Kristo.

2Timotheo 4:7 “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;”

Unaweza kuona Paulo anajitaja kama Mtumwa maana yake ni Mfungwa na zaidi ya yote Mpiganani nimevipiga vita vilivyo vizuri (Askari) anakubali kuaibishwa kwaajili ya Kristo mbele ya macho ya watu wa dunia hii, alama anazozizungumza Paulo ilikuwa ni Utumwa wa Yesu Kristo, Askari mwema kama mpiganaji na kama mtu aliyejitoa kwaajili ya Kristo akikubali kuaibishwa na sio kutafuta heshima, Lakini zaidi ya yote kuonyesha tabia na mwenendo wa ukomavu wa kuishi kama Kristo mwenyewe na hataki kutaabishwa katika hilo!

Tuwapo hapa duniani Yesu alisema tunayo dhiki, na ziko changamoto za aina mbalimbali, kazi yetu kubwa ni kuihubiri kweli na kuhakikisha tunawaambia watu kile ambacho Mungu ametuagiza, lakini lazima ufikie wakati tuwe na maamuzi yetu yakuwa hata watu waseme nini kuhusu maisha yetu au maisha yako jambo kubwa la msingi ni kuchukua chapa za Yesu, kila mwanadamu anaweza kukosea, kila mwanadamu anaweza kufanya uzembe, kila mwanadamua anaweza kufanya makosa na wako watu ambao wanabaki na makosa na uzembe na tabia zetu za zamani kuendelea kuzitumia kama mfano wa kutuchafua na kujaribu kututaabisha nataka nikuambie:-

-          Kama wako wanaosengenya wasengenye sana lakini watangazie kuwa tangu sasa mtu asinitaabishe nachukua chapa za Yesu

-          Kama kuna wanaoshutumu na kulaumu walaumu sana lakini waelewe jana sio leo ziko chapa za Yesu, tunaweza tusibebe chapa za Kristo katika miili yetu lakini tunawezxa kuzibeba katika mioyo yetu, tumekuwa makomandoo, tu meumizwa sana, tumekataliwa sana, tumesengenywa sana, tumezomewa sana, tumeaibishwa sana, tumeshutumiwa sana, tumeonekana kutokufaa sana tumechakazwa sana, tumedhulumiwa sana, tumesingiziwa sana, lakini haijalishi kama tumebaki na Kristo na njia ya mateso tulioipitia inakomaza mishipa yetu na kutufanya tuwe kama Kristo basi ni Dhahiri dunia inatakiwa itambue kuwa tunachukua chapa zake Kristo!

-          Kama kuna waliopata somo kupitia makosa yetu na tabia zetu za wakati wa ujinga na wabaki nazona wazitumie kama somo, na wazitumie kama shuhuda  lakini sisi tunachukua chapa za Yesu, chapa za Kristo ni ukomavu unaoonyesha kuwa tuna uzoefu wa vita, tunasonga mbele na tunaendelea kuishi maisha ya utauwa, Mungu huwakomaza watu wake kupitia changamoto mbalimbali jambo kubwa la maana ni kubaki na Kristo na kudumu katika Imani bila kujali kuwa ni aina gani ya mapito tunapitia! 

-          Iwe inili yetu inakubalika au iwe haikubaliki, maadamu tumehubiri kweli mtu asitutaabishe tunachukua chapa za Yesu, hatudaiwi mikono tumenawa na mavumbi tu mekun’guta, sasa tunalenga kuwa kama Yesu

-          Wakati mwingine injili inapohubiriwa sio lazima watu waikubali hata Yesu alifanya miujiza mingi Kapernaumu, Bethasaida na Korazin lakini hawakumuamini hivyo sisi sio wa kwanza  tunachukua chapa za Kristo, tunaishi na kuigiza tabia na mwenyedno wa Kristo na hiki ndicho tulichoitiwa

-          Tangu sasa mtu asinitaabishe maana nachukua chapa za Yesu, aidha ionekane nimebarikiwa au ionekana kama nimelaaniwa haijalishi wa Muhimu ni Kristo, mwenedo wake, tabia zake na uwezo wake mkubwa wa kuvumilia mateso alipokuwa duniani ni chapa tosha ambazo mkristio anapaswa kuzichukua

-          Kama ni mateso, Yesu na mitume waliyapitia, kusemwa vibaya, kushutumiwa kusingiziwa na kadhalika hiyo haiwezi kusababisha tusimfuate Yesu, au tusiendelee kuwa na tabia na mwenendo kama ule wa Kristo ni lazima tuitangazie jamii ya kuwa tunachukua chapa za Yesu kwa midomo yetu na kwa matendo yetu na kwa muitikio katika maswala magumu na changamoto ngumu tunazozipitia

-          Lazima majamii ifahamu kuwa maneno yao, matusi yao, masingizio yao, mashutumu yao, uzushi wao na uongo wao hauwezi kuzuia kitu chochote wala kumshawishi Mungu kufuta jina langu na la wale walio kama mimi wasichukue kwenye kitabu cha uzima wala tusiache kuchukua chapa za Yesu

-          Wanaotarajia kuwa watatupunguza makali, watashusha kasi yetu, na kutufanya kuwa somo la lawama ni lazima wajue kuwa sisi tumekusudia kuchukua chapa za Yesu, Tangu sasa mtu asinitaabishe nachukua chapa za Yesu!

-          Wewe kama unaona ujanja kuifuata dunia, kuiba, na kujinufaisha kwa masengenyo na dhuluma na wizi na uasherati na zinaa na uadui na ugomvi na uchawi, chuki, wivu, hasira, uzushi, uuaji, ulevi, uwongofitina na majungu, hongera zako hizo ni chapa za Shetani, sisi tutwaonyesha chapa za Kristo, kwamba tuna uwezo wa kuwa na furaha katika mazingira yoyote, kuwa na Amani, kuvumilia na kuonyesha utu wema, na uaminifu, na kiasi chapa za Yesu katika mazingira yoyote yale hakuna kitu chochote duniania nitaweza kutufanya tusimfuate Yesu

-          Kwanini ? kwa sababu Hakuna kitu kinaweza kututenga na Upendo wa Kristo!  HAKUNA !

Warumi 8:35-39 “Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Rev. Innocent Mkombozi Samuel Jumaa Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!

Hakuna maoni: