Jumapili, 20 Agosti 2023

Kuuwa simba bila kitu cho chote mkononi!


Waamuzi 14:5-6 “Ndipo Samsoni na baba yake na mama yake wakatelemkia Timna, wakafika mashamba ya mizabibu huko Timna; na tazama, mwana-simba akamngurumia. Roho ya Bwana ikamjilia kwa nguvu, naye akampasua kana kwamba anampasua mwana-mbuzi, wala hakuwa na kitu cho chote mkononi mwake; lakini hakuwaambia baba yake na mama yake aliyoyafanya.”


 

Utangulizi:

Mungu wetu tunayemwamini na kumuabudu ni Mungu mwenye nguvu sana, uwezo wake na mamlaka yake haiwezi kulinganishwa na kitu chochote ni Mungu mwenye nguvu ni Mungu mwenye uwezo mkubwa mno na ndio maana tunamtegemea kwa kila jambo.

Isaya 9:6-7 “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, Tumepewa mtoto mwanamume; Na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; Naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, MUNGU MWENYE NGUVU, Baba wa milele, Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani Hayatakuwa na mwisho kamwe, Katika kiti cha enzi cha Daudi na ufalme wake; Kuuthibitisha na kuutegemeza Kwa hukumu na kwa haki, Tangu sasa na hata milele. Wivu wa Bwana wa majeshi ndio utakaotenda hayo.”

Maandiko yanatufundisha hivyo na kutuelezea hivyo kuwa Mungu wetu ni mwenye nguvu, kwa msingi huo kila mwanadamu anapaswa kumwamini Mungu na kumtegemea akijua wazi kuwa hakuna jambo lolole linaloshindikana kwa Mungu, Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna jambo linamuudhi Mungu kama kutokumuamini au kama hatuamini nguvu zake maana yake ni kuwa tumemuwekea mpaka (limitations) Jambo hilo ni Uasi, ni jambo la kuhuzunisha la kusikitisha na ni kama tumerudi nyuma na kumwacha au kutokukumbuka matendo yake.

Zaburi 78:40-42 “Walimwasi jangwani mara ngapi? Na kumhuzunisha nyikani! Wakarudi nyuma wakamjaribu Mungu; Wakampa mpaka Mtakatifu wa Israeli.Hawakuukumbuka mkono wake, Wala siku ile alipowakomboa na mtesi.”

Watakatifu waliotutangulia waliamini katika nguvu za Mungu, na kumtegemea katika maswala mbali mbali ya maisha na wakafanikiwa sana, Lakini wale ambao hawakumuamini walimsikitisha sana na hakupendezwa nao wala kuwafurahia, Mungu hafurahii mtu mwenye kusita sita lakini anamfurahia mtu anayemuamini.

Waebrania 10:38 “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye”.      

Mungu anataka tumuamini, anataka tuamini uwezo wake na anataka tumuamini Nguvu zake na anataka tuzitafute nguvu zake na kuutafuta uso wake kila siku, tutendapo hayo utaweza kuona tutakuwa na furaha na amani na Mungu wetu atatutendea mambo makubwa katika njia nyepesi sana 1Nyakati 16:11 “Mtakeni Bwana na nguvu zake; Utafuteni uso wake siku zote.Tukifanya hivyo uweza ule wa Mungu na utendaji na mamlaka na nguvu za Mungu zitadhihirika ndani yetu katika namna nyepesi sana kuliko tunavyofikiri.

Leo tutachukua Muda kuangalia kwa kina tukio la Samsoni kumuua simba kwa mikono yake bila kutumia chombo chochote na maana yake kubwa ambayo Mungu amekusudia kutufundisha katika siku ya leo! Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Mungu hutumia njia mbalimbali katika kutatua changamoto za wanadamu.

·         Maana ya kuua simba bila kitu chochote mkononi.

·         Kuuwa Simba bila kitu chochote mkononi.

Mungu hutumia njia mbalimbali katika kutatua changamoto za wanadamu.

Wote tutakubaliana kwamba Mungu hutumia njia mbalimbali katika kutatua changamoto za wanadamu kwa kadiri apendavyo Roho Yeye Yule, na maandiko yametupa mwongozo, kwa mfano wana wa Israel walipokuwa wanatoka Misri kuelekea katika inchi ya ahadi inchi ya Kanaani Fimbo ya Musa ilitumika sana kama ishara ya mamlaka yake na Mungu aliitumia fimbo ya Musa kufanya Miujiza, mfano walipokuwa wamekutana na kikwazo katika kuivuka bahari ya Shamu, bado tunaona Mungu alimuelekeza Musa kutumia fimbo na ikawa ufumbuzi wa changamoto mbalimbali.

Kutoka 14:15-16 “BWANA akamwambia Musa, Mbona unanililia mimi? Waambie wana wa Israeli waendelee mbele. Nawe inua fimbo yako, ukanyoshe mkono wako juu ya bahari, na kuigawanya; nao wana wa Israeli watapita kati ya bahari katika nchi kavu.”             

Unaona hapa kwa maelekezo ya Mungu wana wa Israel walivuka kikwazo cha bahari ya shamu Musa akipewa maelekezo ya kuitumia fimbo, nasisitiza tena kwa maelekezo Nawe inua fimbo yako unaona! Mungu ndiye aliyemuelekeza Musa kutumia fimbo iliyokuwa mkononi mwake kufanya ishara na miujiza, na ni katika hali kama hiyo wana wa Israel walipokuwa wanapaswa kuvuka ng’ambo ya Mto Yodrani  Mungu alitoa maelekezo mengine kwa kiongozi aliyekuwepo Yoshua Mungu alitoa maelekezo mengine namna watakavyouvuka mto wa Yordani ona.

Yoshua 3:5-8 “Yoshua akawaambia watu, Jitakaseni; maana kesho Bwana atatenda mambo ya ajabu kati yenu. Kisha Yoshua akawaambia makuhani, akasema, Liinueni sanduku la agano, mkavuke mbele ya hao watu. Wakaliinua sanduku la agano, wakatangulia mbele ya watu. Bwana akamwambia Yoshua, Hivi leo nitaanza kukutukuza mbele ya Israeli wote, wapate kujua ya kuwa mimi nitakuwa pamoja na wewe, kama nilivyokuwa pamoja na Musa. Nawe uwaamuru hao makuhani walichukuao sanduku la agano, ukawaambie, Mtakapofika ukingo wa maji ya Yordani, simameni katika Yordani. Basi Yoshua akawaambia wana wa Israeli, Njoni huku, mkayasikie maneno ya Bwana, Mungu wenu. Yoshua akasema, Kwa jambo hili mtajua ya kuwa Mungu aliye hai yu kati yenu, na ya kuwa hatakosa kuwatoa mbele yenu Mkanaani, na Mhiti, na Mhivi, na Mperizi, na Mgirgashi, na Mwamori, na Myebusi. Tazama, sanduku la agano la Bwana wa dunia yote linavuka mbele yenu na kuingia Yordani. Basi sasa twaeni watu kumi na wawili katika kabila za Israeli, kila kabila mtu mmoja. Itakuwa, wakati nyayo za makuhani walichukuao sanduku la Bwana, Bwana wa dunia yote, zitakaposimama katika maji ya Yordani, hayo maji ya Yordani yatatindika, maji yale yashukayo kutoka juu; nayo yatasimama kama chuguu.”       

Unaona kwa mara nyingine tena katika matukio yenye kufanana kuvuka bahari ya shamu na kuvuka mto wa Yordan Mungu akiwa ni yule yule lakini wakati wanatoa maelekezo ya kuvuka mto wa Yordani alitoa maelekezo mengine ni katika mtindo huo huo wakati wa waamuzi Mungu aliweza kutoa ushindi kwa waamuzi hao kwa nyenzo mbalimbali ambazo Mungu aliweka mkono wake na kuwapa ushindi mfano:-

1.       Mungu alimtumia Mwamuzi Shamghari kuwapa Israel ushindi kwa kutumia konzo la ng’ombe Waamuzi 3:31Tena baada yake huyo alikuwapo Shamgari mwana wa Anathi, aliyepiga katika Wafilisti watu mia sita kwa konzo la ng'ombe; yeye naye aliwaokoa Israeli.” (Konzo la Ngombe ni mti mgumu unaotumika kuunga gari au kokoteni unaosukumwa na Ngombe)

 

2.       Mungu alimtumia Yael Mwanamke kuleta ushindi kwa wana wa Israel dhidi ya Sisera kwa kutumia nyundo na kigingi  Waamuzi 4:17-21 “Lakini Sisera akakimbia kwa miguu, akaifikilia hema ya Yaeli mkewe Heberi, Mkeni; kwa maana palikuwa na amani kati ya Yabini, mfalme wa Hazori, na nyumba ya Heberi, Mkeni. Yaeli akatoka kwenda kumlaki Sisera, akamwambia, Karibu Bwana wangu, karibu kwangu; usiogope. Akakaribia kwake hemani, naye akamfunika kwa bushuti.  Akamwambia, Tafadhali nipe maji kidogo ninywe; maana nina kiu. Akafungua chupa ya maziwa, akampa kunywa, akamfunika. Naye akamwambia, Simama mlangoni pa hema; kisha itakuwa mtu awaye yote akija na kukuuliza, akisema, Je! Yupo mtu hapa, basi, mjibu, La, hapana. Ndipo Yaeli, mkewe Heberi, akatwaa kigingi cha hema, akashika nyundo mkononi mwake, akamwendea polepole, akamtia kile kigingi katika kipaji chake, nacho kikapenya, hata kuingia mchangani; kwa maana usingizi mzito ulikuwa umemshika; basi akazimia, akafa.”

 

3.       Muda usingeweza kutosha kuona namna Mungu alivyotumia watu mbalimbali na nyenzo mbalimbali kutenda miujiza na kuwaletea ushindi watu wake lakini hatimaye tunamuona Samsoni naye baada ya kujiliwa na Roho wa Mungu akiua Simba bila kitu chochote Mkononi ona

 

Waamuzi 14:5-6 “Ndipo Samsoni na baba yake na mama yake wakatelemkia Timna, wakafika mashamba ya mizabibu huko Timna; na tazama, mwana-simba akamngurumia. Roho ya Bwana ikamjilia kwa nguvu, naye akampasua kana kwamba anampasua mwana-mbuzi, wala hakuwa na kitu cho chote mkononi mwake; lakini hakuwaambia baba yake na mama yake aliyoyafanya.”

Maana ya kuua simba bila kitu chochote mkononi.

Tunajifunza nini katika mifano hiyo hapo juu namna na jinsi Mungu alivyotumia njia mbalimbali katika kuiwasaidia watu wake kupata ufumbuzi na changamoto zilizokuwa zikiwakabili, nikiwa nimetulia zangu natafakari tu kuhusu Mungu ghafla ujumbe huu ulinijia nilimsikia Roho Mtakatifu mwenyewe akiniambia neno HILI KUUA SIMBA BILA KITU CHOCHOTE MKONONI  na mawazoni ilikuja moja kwa moja picha ya Samsoni akikabiliana na mwana simba na kumuua Biblia inasema akampasua mwana simba, nikawaza na kufikiri kwa haraka kuna jambo gani Roho Mtakatifu anataka kuniambia, Mungu kweli alifanya kazi na watu mbalimbali lakini pia na waamuzi mbalimbali kutatua changamoto za wanadamu kwa kutumia vifaa mbalimbali, lakini mwamuzi maarufu zaidi Samsoni katika tukio la kuua simba alitumia mikono tu bila ya kuwa na kitu chochote Mkononi.

Leo hii kumekuwepo na idadi kubwa sana ya matumizi ya vifaa vya kiroho, watu wanaponywa na kuamini katika uponyaji na usuluhishi wa changamoto zao kupitia vifaa vya kiroho, chumvi, mafuta, maji ya Baraka, udongo, vitambaa, sabuni na kadhalika kila mmoja akidai ni muongozo aliopewa na Roho Mtakatifu, hatuwezi kuingilia maelekezo yao na wala hatuwezi kukataa kuwa vinafanya kazi kwa jina la Yesu, vinafanya Lakini tusisahau pia kuwa Mungu ametuagiza kutumia mikono yetu kwaajili ya uponyaji na kwa kutumia jina la Yesu ona kwa mfano:-

Marko 16:17-18 “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa; wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya.”

Maandiko yanatufundisha kuwa tunaweza kukemea pepo na changamoto nyingine na zikaondoka kwa kutumia jina la Yesu tu, na tunaweza kuweka mikono yetu juu ya wagonjwa nao wakapata afya pia tunaweza kutumia vinywa vyetu na tukamuomba Mungu naye akafanya bila haja ya kutumia vifaa vya kiroho, matumizi ya vifaa vya kiroho yanaonyesha udhaifu mkubwa sana wa kiimani katika nyakati tulizonazo, watu wanahitaji sana kuona vitu vinavyoonekana na vitu ambavyo wanaweza kugusa ndipo waweze kuamini Mungu wetu ni mwenye nguvu kubwa sana aliiumba ulimwengu kwa neno tu na kila kitu kikawa kama kilivyokuwa kuua simba bila kitu chochote mkononi ni ishara ya kuwa yako mambo Mungu anaweza kuyafanya bila kuhitaji kutumia vifaa vya kiroho, Roho Mtakatifu anataka kulikumbusha kanisa kurudi katika utukufu wake na kuondoka katika udhaifu kutumia vifaa vya kiroho ni kwa watoto wachanga kiimani ni ishara ya kuwa kanisa limepoteza mamlaka, kanisa limesahau msingi wa matumizi ya Jina la Yesu jina lanye uwezo wa kufanya lolote hata bila msaada wa kitu chochote cha kuonekana  ufike wakati sasa kanisa tubatilishe mambo yote ya kitoto,

1Wakorintho 13:11 “Nilipokuwa mtoto mchanga, nalisema kama mtoto mchanga, nalifahamu kama mtoto mchanga, nalifikiri kama mtoto mchanga; tokea hapo nilipokuwa mtu mzima, nimeyabatilisha mambo ya kitoto.”

 

Kuua Simba bila kitu chochote mkononi

Kama nilivyogusia hapo juu ni kuwa kuua simba bila kitu chochote mkononi kunamaanisha uwezo wa kukabiliana na changamoto zozote kutoka kwa ibilisi kwa kutumia jina la Yesu hata bila kutumia vifaa vya kiroho, Maandiko kinabii yanamtafasiri Shetani kama simba aungurumaye akitafuta mtu aweze kummeza ona 1Petro 5:8 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.”

Shetani pamoja na changamoto zote zinazotokana na yeye ni simba aungurumaye kanisa likirejea katika mamlaka yake na nguvu zake litakuwa na uwezo wake na nguvu zake za awali watakuwa na ufahamu kuwa iko mamlaka kubwa ya kutamka jina la Yesu na likaleta matokeo makubwa jina lenyewe tu peke yake hata bila ya kifaa chochote cha kiroho sio kila wakati tutatumia tu vifaa vya kiroho sio kila wakati Mungu atatoa maelekezo yale yale lakini kukaa katika uwepo wa Mungu kunatusaidia kuwa na mamlaka ya kutosha kutamka neno na ikawa

-          1Wafalme 17:1 “Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu, Kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu.”

 

-          2Wafalme 4:16 “.Akasema, Panapo wakati huu mwakani, utamkumbatia mwana. Akasema, La! Bwana wangu, wewe mtu wa Mungu, usiniambie mimi mjakazi wako uongo. Yule mwanamke akachukua mimba, akazaa mtoto mume wakati uo huo mwakani, kama Elisha alivyomwambia.”

 

-          2Wafalme 7:1 “Elisha akasema, Lisikieni neno la Bwana; Bwana asema hivi, Kesho panapo saa hii, kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, langoni pa Samaria.”       

 

-          Matendo 3:6-9 “Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu. Akaondoka upesi akasimama, akaanza kwenda; akaingia ndani ya hekalu pamoja nao, akienda, akiruka-ruka, na kumsifu Mungu. Watu wote wakamwona akienda, akimsifu Mungu.”

 

-          Matendo 13:8-12. “Lakini Elima, yule mchawi (maana ndiyo tafsiri ya jina lake), akashindana nao, akitaka kumtia yule liwali moyo wa kuiacha ile imani. Lakini Sauli, ambaye ndiye Paulo, akijaa Roho Mtakatifu, akamkazia macho, akasema, Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za Bwana zilizonyoka? Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda. Mara kiwi kikamwangukia na giza, akazunguka-zunguka na kumtafuta mtu wa kumshika mkono na kumwongoza. Ndipo yule liwali, alipoyaona yaliyotendeka, akaamini, akiyastaajabia mafundisho ya Bwana.”

 

-          Mathayo 8:5-10 “Hata alipoingia Kapernaumu, akida mmoja alimjia, akamsihi, akisema, Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani, mgonjwa wa kupooza, anaumwa sana. Yesu akamwambia, Nitakuja, nimponye. Yule akida akamjibu, akasema, Bwana, mimi sistahili wewe uingie chini ya dari yangu; lakini sema neno tu, na mtumishi wangu atapona. Kwa maana mimi nami ni mtu niliyewekwa chini ya mamlaka, mwenye askari chini yangu; nikimwambia huyu, Nenda, huenda; na huyu, Njoo, huja; na mtumwa wangu, Fanya hivi, hufanya. Yesu aliposikia hayo, alistaajabu, akawaambia wale waliomfuata, Amin, nawaambieni, Sijaona imani kubwa namna hii, kwa ye yote katika Israeli.”

 

-          Marko 11:23-24 “Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng'oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.”

 

-          Matendo 3:6-7 “Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu.”     

Hitimisho.

Maandiko yote hapo juu ni ushahidi ulio wazi ya kuwa kama tukisimama imara katika maombi tutaweza kua simba bila kitu chochote mkononi yaani hatutahitaji sabuni, wala chumvi wala maji ya Baraka wala udongo wa upako tutatamka tu kwa Imani na kwa mamlaka ya jina la Yesu na yale yaliyokusudiwa na Mungu kupitia watumishi wake yatatimia, kuuwa simba bila kitu chochote mkononi ni shara ya ushujaa wa ngazi ya juu sana, kama ilivyo katika jamii ya kimasai,  Neno la Mungu limetaja watu watatu tu  ambao walikuwa na uwezo wa kuua simba bila kutumia silaha ama kitu Mkononi

Samsoni - Waamuzi 14:5-6 “Ndipo Samsoni na baba yake na mama yake wakatelemkia Timna, wakafika mashamba ya mizabibu huko Timna; na tazama, mwana-simba akamngurumia. Roho ya Bwana ikamjilia kwa nguvu, naye akampasua kana kwamba anampasua mwana-mbuzi, wala hakuwa na kitu cho chote mkononi mwake; lakini hakuwaambia baba yake na mama yake aliyoyafanya.”

Daudi1Samuel 17:34-36 “Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi, mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua. Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai.”          

Benaya - 2Samuel 23:20-21. “Tena Benaya, mwana wa Yehoyada, mtu hodari wa Kabseeli aliyekuwa amefanya mambo makuu; aliwaua simba wakali wawili wa Moabu, pia akashuka akamwua simba katikati ya shimo wakati wa theruji. huyo naye akamwua Mmisri, mtu mrefu; naye huyo Mmisri alikuwa na mkuki mkononi; lakini yeye alimshukia na gongo, akamnyakulia Mmisri mkuki mkononi mwake, akamwua kwa mkuki wake mwenyewe.”            

Biblia inaonyesha mashujaa wakubwa watu hodari waliowahi kuua simba ambao ni Samsoni, Daudi na Benaya na benaya ndiye anaonekana kuongoza katika kufanya mauaji ya simba wengi zaidi, kufikia ngazi hii ya juu zaidi ya ushujaa ndilo jambo ambalo Mungu analitazamia, kwa kila mmoja wetu, ifikie wakati hata kama tutasahau kifaa fulani cha kiroho lakini tuwe na uweza na mamlaka ya kiungu na uwezo wa kutumia Jina la Yesu na mamlaka katika jina hilo         kusababisha mambo makubwa ya uponyaji na miujiza na utatuzi wa changamoto mbalimbali wakati mwingine bila haja ya kutumia kifaa chochote cha kiroho, hii ndio ngazi ya juu kabisa ya kimamlaka ambayo tunapaswa watu wa Mungu kuitafuta na kuitumia.

Matendo 4:12 – “Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”

Wafilipi 2:9-1 1 – “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Matendo 2:21 – “Na itakuwa kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa.”

Warumi 10;13 – “Kwa kuwa, Kila atakayeliitia Jina la Bwana ataokoka.”

Kanisa ni muhimu kwetu kukumbuika na kujiimarisha kiimani katika matumizi ya jina la Yesu na kusababisha mamlaka ya kiungu kutokea na kutenda kazi na kupunguza dhana ya matumizi ya vifaa vya kiroho, matumizi ya jina la yesu katika utatuzi wa changamoto mbalimbali bila kutumia vifaa vya kiroho ndio kuuwa simba bila kitu chochote Mkononi.

Na. Rev. Innocent Mkombozi Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Hakuna maoni: