Alhamisi, 24 Agosti 2023

Usiwape wanawake nguvu zako!


MIthali 31:1-3 “Maneno ya mfalme Lemueli; mausia aliyofundishwa na mama yake. Ni nini, mwanangu? Tena ni nini, mwana wa tumbo langu? Tena, ni nini mwana wa nadhiri zangu? Usiwape wanawake nguvu zako; Wala moyo wako usiwape wale wawaharibuo wafalme.”


Utangulizi:

Kitabu cha Mithali ni kitabu kinachotufunza maswala ya muhimu katika maisha na maadili na maonyo ya kila siku pamoja na kutupa hekima jinsi na namna inavyotupasa kuenenda, Moja ya maswala ya msingi tunayojifuza leo ni pamoja na wosia aliopewa Mfalme Lemuel kutoka kwa mama yake ambayo alimfunza ili kutusaidia sisi tuliofikiwa na miisho ya zamani hizi.

Mithali 31:2-3 “Ni nini, mwanangu? Tena ni nini, mwana wa tumbo langu? Tena, ni nini mwana wa nadhiri zangu? Usiwape wanawake nguvu zako; Wala moyo wako usiwape wale wawaharibuo wafalme

Mama anaonekana kusisitiza sana kuonyesha namna anavyohitaji  umakini wa jambo ambalo anataka kulileta kwa mwanae ambalo pia analileta kwetu, ambalo kimsingi ingawa lilikuwepo katika siku za zamani sana na leo linaendelea kushika kasi kwa namna mbalimbali, tutajifunza somo hili USIWAPE WANAWAKE NGUVU ZAKO kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:- 

Ø  Maonyo kutoka kwa mama.

Ø  Usiwape wanawake nguvu zako

Ø  Mambo yawapasayo wanaume kufanya! 

Maonyo kutoka kwa mama.

Ni muhimu kufahamu kuwa katika mtazamo wa kale wa mashariki ya kati jukumu kubwa la malezi na makuzi mazima ya mtoto awe wa kiume au wa kike na hata misingi ya imani yake ilisadikiwa kuwa ilitoka kwa mama, Kama mtoto angeonyesha hekima na ubora baba yake angejivunia sana na kama mtoto akionyesha tabia mbaya waliangalia sana kuwa mama yake alikuwa ni mtu wa namna gani ona Mithali 10:1 “Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye; Bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.” Kwa msingi huo utaweza kuona hata nyakati za utawala wa wafalme wale waliokuwa waovu au waliofanya mema mama zao walitajwa na ubini wao kuonyesha kuwa chanzo cha tatizo au mafanikio ya mfalme husika imechangiwa na  aina ya  mama aliyekuwa naye ona kwa mfano

2Nyakati 29:1-2 “Hezekia alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala katika Yerusalemu miaka ishirini na kenda; na jina la mamaye aliitwa Abiya binti Zekaria. Akafanya yaliyo ya adili machoni pa Bwana, sawasawa na yote aliyoyafanya Daudi babaye.”  

Unaona kama mfalme alifanya vizuri maana yake kulikuwa na mama mzuri mwenye tabia nzuri mwenye busara na hekima na mcha Mungu anayetoka katika familia iliyofunzwa vizuri, kadhalika pia wamama walitajwa kulingana na aina ya mfalme kama mfalme huyo alikuwa mwovu utaweza kuona na aina ya mama anatajwa na anakotokea ona kwa mfano

1Wafalme 15:1-3 “Mwaka wa kumi na nane wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, Abiya alianza kutawala juu ya Yuda. Miaka mitatu akatawala huko Yerusalemu; na jina la mamaye aliitwa Maaka, binti Absalomu. Akaziendea dhambi zote za babaye, alizozifanya kabla yake; wala moyo wake haukuwa mkamilifu na Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi babaye.”

Ni kwaajili ya mambo kama haya Mungu aliwaelekeza Israel kuhakikisha kuwa wanaoza watoto wao kwa watu sahihi wenye tabia njema ili mioyo yao isikenguke kutoka kwa Bwana ona

Kumbukumbu 7:1-4 “Bwana, Mungu wako, atakapokutia katika nchi uendayo kuimiliki, atakapoyang'oa mataifa mengi watoke mbele yako, Mhiti, na Mgirgashi, na Mwamori, na Mkanaani, na Mperizi, na Mhivi, na Myebusi, mataifa saba makubwa yenye nguvu kukupita wewe; wakati Bwana, Mungu wako, atakapowatoa mbele yako, nawe utawapiga; wakati huo ndipo uwaondoe kabisa; usifanye agano nao, wala kuwahurumia; wala usioane nao; binti yako usimpe mwanawe mume, wala usimtwalie mwanao mume binti yake. Kwa kuwa atamkengeusha mwanao mume asinifuate, ili wapate kuabudu miungu mingine; ndipo itakapowaka hasira ya Bwana juu yenu, naye atakuangamiza upesi.”

Kwa msingi huo kwa mujibu wa maandiko Mwanamke ana nafasi kubwa sana ya kuambukiza maswala ya kiimani na uadilifu kwa watoto kuliko tunavyoweza kufikiri ukweli huu unathibitishwa pia katika maisha ya Timotheo ambaye baba yake alikuwa myunani na mama yake myahudi na bibi yake alikuwa myahudi pia na imani ilitembea kwa wanawake hao mpaka kwa kijana wao Timotheo ona kile Paulo mtume anakithibitisha hapa

2Timotheo 1:5 “nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo.”

Unaona Paulo mtume mkuu wa wajenzi pia alikuwa na imani kuwa imani njema iliyokuwa kwa bibi yake Timotheo, ilikaa wazi pia ndani ya mama yake Eunike na alikuwa na imani kuwa Timotheo ameirithi, ni ukweli ulio wazi kuwa uadilifu, imani,  tabia na mwenendo wetu unaathiriwa kwa kiwango kikubwa na wazazi wetu wa kike kifupi imani inakaa kwa mwanamke.

Ni katika hali kama hiyo Mfalme Lemuel anakumbuka sana mausia aliyopewa na mama yake, yalikuwa ni maelekezo Muhimu sana ambayo mama yake aliyazungumza kwa msisitizo akimtaka kijana wake ayashike ili aweze kufanikiwa katika maisha yake na katika ufalme wake, Mama yake alikuwa anajua mioyo ya wanawake wa ulimwengu huu na alikuwa na ujuzi kuwa watu wengi sana hususani wanaume wamepotezewa Muda, na kupotezewa heshima zao na kuharibikiwa katika uchumi na mafanikio yao kupitia wanawake, ona tena maonyo hayo muhimu

MIthali 31:1-3 “Maneno ya mfalme Lemueli; mausia aliyofundishwa na mama yake. Ni nini, mwanangu? Tena ni nini, mwana wa tumbo langu? Tena, ni nini mwana wa nadhiri zangu? Usiwape wanawake nguvu zako; Wala moyo wako usiwape wale wawaharibuo wafalme.”

Usiwape wanawake nguvu zako!

Katika maelekezo hayo muhimu ambayo Lamuel alipewa na Mama yake na ameshirikisha jamii hapa ili wote tuweze kujifunza ni hatari kuhusu wanawake! USIWAPE WANAWAKE NGUVU ZAKO  hili ni moja ya maonyo ya msingi sana ambayo tunataka kujifunza na sisi leo, kila kijana wa kiume anapaswa kulitilia hilo maanani, jambo hili la kuwapa wanawake nguvu zako pia linaendana na linalofuata WAWAHARIBUO WAFALME, kuwapa wanawake nguvu zako na kuwapa wanawake moyo wako kunaleta anguko la mfalme! Kunaangusha, kuonaondoa heshima, kunaharibu mwelekeo wa maisha kunasambaratisha ustawi wa kiuchumi wa mtu, Nafsi yako ikitekwa na uzuri wa wanawake hatima ya kijana wa kiume inakuja kuwa yenye majuto makubwa baadaye jambo hili limeonywa mara kadhaa katika maandiko ona

Mithali 5:1-10 “Mwanangu, sikiliza hekima yangu; Tega sikio lako, mzisikie akili zangu; Upate kuilinda busara, Na midomo yako iyahifadhi maarifa. Maana midomo ya malaya hudondoza asali, Na kinywa chake ni laini kuliko mafuta; Lakini mwisho wake ni mchungu kuliko pakanga; Ni mkali kama upanga wa makali kuwili. Miguu yake inatelemkia mauti; Hatua zake zinashikamana na kuzimu; Hata asiweze kuiona njia sawa ya uzima; Njia zake ni za kutanga-tanga wala hana habari. Basi, wanangu, nisikilizeni sasa, Wala msiache maneno ya kinywa changu. Itenge njia yako mbali naye, Wala usiukaribie mlango wa nyumba yake. Usije ukawapa wengine heshima yako, Na wakorofi miaka yako; Wageni wasije wakashiba nguvu zako; Kazi zako zikawa ndani ya nyumba ya mgeni;”

Unaweza kuona maonyo ya Mfalme Sulemani yanaenda sambamba na Maonyo ya mama yake Lemuel wote wanaonya Hasara zinazoweza kupatikana kwa Mwanaume kujihusisha na wanawake hususani katika maswala mazima ya kufanya ngono, kufanya zinaa au umalaya au kuwanda wanda katika maisha yetu na uzuri wa wanawake au kutaka kuwaonja wanawake wa aina zote wanaojitokeza katika maisha yetu jambo hili lina madhara kadhaa ambao wenye hekima wameyaainisha hapo, usiwape wanawake nguvu zako!

Nini maana ya KUWAPA WANAWAKE NGUVU ZAKO neno nguvu linalotumika hapo katika kiebrania ni CHAYIL ambalo kimsingi linazungumzia UWEZO, yaani uwezo wako wote kama vile Jeshi au kila kitu ulicho nacho ambacho kinakujenga wewe kuwa wewe, Mfano, HESHIMA, FEDHA, MALI, WATOTO, KAZI, AU NJIA ZAKO ZOTE ZA UCHUMI, MAISHA YAKO, AU MUDA, Kwa hiyo neno CHAYIL ni mjumuisho wa maswala kadhaa muhimu kama kazi, heshima, cheo, muda nguvu na uwekezaji wako wote.  Kwa mujibu wa wenye hekima hapo ni kuwa unapojitoa katika maisha ya kuwapenda wanawake na umalaya  utafutilia mbali kila ambacho umesumbuka kukijenga kwa miaka kadhaa ya maisha yako neno WAHARIBUO  katika Kiebrania ni DEREK  ambalo maana yake ni kufutuilia mbali,  wanaume wengi hutumia nguvu zao na  na muda wao kujijenga kitaaluma, kiuchumi, kiroho na kadhalika lakini moja ya changamoto kubwa sana kibinadamu inayowapata wanaume ni kuwa wanapokuwa na mafanikio makubwa na kuwa maarufu na kuwa na nguvu kubwa kiuchumi, na hata kimwili na kujipatia umaarufu basi adui mkubwa sana wa mafanikio yao au anguko lao kubwa sana linalowakabili ni WANAWAKE, kila mwanamke anavutiwa sana na mwanaume aliyejijenga, Mwenye fedha, mwenye six Park, aliye ha umaarufu, mwenye uchumi mzuri, mwenye tabia nzuri, mwenye nyumba, gari na mafanikio mbalimbali katika maisha, Mama wa Lemuel alikuwa na ufahamu huo na akamuonya mwanaye kuwa asitoe moyo wake kwa hawa wanaoangusha wafalme sikiliza; wafalme hapa sio lazima wawe watu walioko kwenye mamlaka za kiserikali au rais na kadhalika Ufalme hapa unazungumzia kufikia kiwango Fulani cha utukufu ni kiwango Fulani cha mafanikio, kilele Fulani cha mafanikio na heshima unapokifikia hicho wewe ni mfalme na unaweza kuharibikiwa kama moyo wako hautajali kujilinda na wanawake, na kumbuka vilevile Mama wa Lamuel Hakusema Mwanamke bali amesema wanawake maana yake ile hali ya kupenda kumiliki au kutembea na wanawake wengi baada ya mafanikio, kitabu hicho hicho kumbuka kuwa kina imani kuwa mtu muadilifu anaweza kutafuta mke mmoja tu na akatulia naye Mithali 31:10 “Mke mwema, ni nani awezaye kumwona? Maana kima chake chapita kima cha marijani.” Kwa hiyo tatizo sio mke tatizo ni wanawake hawa wanaleta uharibifu na neno la Mungu linathibitisha hayo kama tutakavyoona mbeleni:-

-          Kiuchumi – Maandiko yanatufundisha kuwa tangu siku za zamani limekuwa ni jambo la kawaida kuwa kunapokuwa na mahusiano ya kimapenzi kati ya mwanamke na Mwanaume fedha au mali huusika katika kuwapa wanawake, wanaume wameumbiwa kutoa na wanawake wamaumbiwa kupokea, hivyo linaweza kuwa jambo la kawaida wanawake kutaka malipo katika mahusiano,

 

Mwanzo 38:14-18Basi akavua nguo za ujane wake, akajivika utaji, akajifunika uso, akakaa mlangoni pa Enaimu, karibu na njia ya kuendea Timna. Maana aliona ya kwamba Shela amekuwa mtu mzima, wala hakuozwa awe mkewe. Yuda alipomwona alimdhania kuwa ni kahaba, maana amejifunika uso.  Akamgeukia kando ya njia, akasema, Niruhusu niingie kwako. Maana hakujua ya kuwa ni mkwewe. Akamwuliza, Utanipa nini, ukiingia kwangu? Akasema, Nitakuletea mwana-mbuzi wa kundini. Naye akamwuliza, Je! Utanipa rehani hata utakapomleta? Akasema, Nikupe rehani gani? Akamjibu, Pete yako ya muhuri, na kamba yake, na fimbo yako iliyo mkononi mwako. Basi akampa, akaingia kwake, naye akapata mimba.”

 

Ni kifungu cha zamani sana japo kinaweza kuwa na mafunzo mengine mengi tofauti lakini moja ya kitu tunajifunza hapo ni kuwa tangu zamani wanawake walipenda kupokea kitu kutoka kwa wanaume na wanaume walihonga, mwanamke aliuliza utanipa nini ukiingia kwangu? Na mwanaume alisema nitakupa mwanambuzi, katika nyakati za leo wanawawake wameharibika zaidi, hali ya kutaka kuhongwa imepanuka katika kiwango ambacho leo kinaitwa kuchunwa, wanaume wamepewa majina ya mabuzi na wanawake ni wachunaji, kuna utapeli mwingi na mkao mkubwa wa wanawake kuhitaji fedha kama malipo ya ngono, lakini sio kwa malipo ya ngono tu ila watawekeza mioyo yao katika kuwaelemea wanaume kwa sababu mbalimbali mojawapo ikiwa ni ugumu wa maisha lakini vilevile na kwa moyo wa ubinafsi hata kama hawauzi mapenzi au kufanya biashara ya mapenzi, lakini vyovyote vile hali hii inachangia katika kudhooficha uchumi wa mwanaume, wanawake wa leo ambao wengi wao wana mikopo wanayotakiwa kurejesha mawazo yao makubwa yamekuwa katika fedha zaidi kuliko kwenye penzi lenyewe kuwaendekeza Malaya kutakueletea anguko la kiuchumi, na kufilisi uwezo wako, katika maeneo mbalimbali likiwemo hili la uchumi.

 

-          Nguvu – Huu ni uwezo wa kimwili na Kiroho, kisaikolojia wanawake wanavutiwa sana na Mwanaume mwenye nguvu, hili sio jambo la ajabu kiasili, kwani hata wanyama katika ulimwengu wao majike huwa hayavutiwi na mwanaume mnyonge, kama mwanaume atakuwa hana nguvu anapoteza heshima kwa mwanamke, lakini hata hivyo kujihusisha katika ngono kulikokithiri kwa wanawake wa aina mbalimbali pia hupelekea kupoteza nguvu za kimiwli, na kiroho na nguvu za uzazi au hata nguvu za kiume 

 

Zaburi 127:3-5 “Tazama, wana ndio urithi wa Bwana, Uzao wa tumbo ni thawabu. Kama mishale mkononi mwa shujaa, Ndivyo walivyo wana wa ujanani. Heri mtu yule Aliyelijaza podo Lake hivyo. Naam, hawataona aibu Wanaposema na adui langoni

 

Maandiko yanazungumzia umuhimu wa watoto, Nguvu ya familia yoyote ni watoto wake tabia ya kujaribu kujifurahisha na kila mwanamke inaweza kuathiri uzao wako au unaweza kupoteza mbegu zako na watoto wako wakawa wa mtu mwingine, wako watu wengi leo wamezaa hovyo hovyo  na wamezaa mpaka na wake za watu na ni ngumu kwenda kudai watoto katika familia isiyokuwa yako, watoto wanajenga jamii ni thawabu kutoka kwa Mungu lazima wazaliwe katika utaratibu na mpangilio maalumu ili uzao wako usipotee kama mishale mkononi mwa shujaa ndivyo walivyo watoto wa ujanani, Heri mtu yule aliyelijaza podo lake, yaani heri mtu mwenye mishale mingi, kuwa na watoto wengi lilikuwa moja ya jambo lenye heshima kubwa sana nyakati za Biblia. Lakini sio watoto waliotawanyika ni watoto wanaolelewa katika boma moja (Podo) ni chombo maalumu cha kuhifadhia mishale ambayo unaweza kuitumia wakati wa mapambano, shujaa hawezi kutumia mshale ambao hauko kwenye podo lake!, Uzaaji wa watoto hovyo hovyo pia unaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa katika kuharibu uchumi na uadilifu wa kitabia unaoukusudia uwe kwa watoto wako!

 

Aidha pia nguvu zako za kiume zinaweza kuharibiwa kupitia tabia ya kulala hovyo na wanawake, asili ya nguvu zako za kiuchumi, kimwili na kiroho pia inaweza kuharibiwa kama hutakuwa na tahadhari na wanawake hasa unapokuwa na mahusiano ya kingono na wao.

 

Waamuzi 16:13-18 “Delila akamwambia Samsoni, Hata sasa umenidhihaki, umeniambia maneno ya uongo; niambie sasa, waweza kufungwa kwa kitu gani? Akamwambia, Ukivifuma hivi vishungi saba vya nywele za kichwa changu katika mtande wa nguo. Basi akazifunga kwa msumari, akamwambia Samsoni, Wafilisti wanakujia. Naye akaamka usingizini, akaung'oa ule msumari, na ule mtande. Mwanamke akamwambia, Wawezaje kusema, Nakupenda; na moyo wako haupo pamoja nami? Umenidhihaki mara hizi tatu, wala hukuniambia asili ya nguvu zako nyingi. Ikawa, kwa vile alivyomsumbua kwa maneno yake kila siku, na kumwudhi, roho yake ikadhikika hata kufa. Ndipo alipomwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akamwambia, Wembe haukupita juu ya kichwa changu kamwe; maana mimi nimekuwa Mnadhiri wa Mungu, tangu tumboni mwa mama yangu; nikinyolewa, ndipo nguvu zangu zitanitoka, nami nitakuwa dhaifu, nitakuwa kama wanadamu wenzangu. Delila alipoona ya kuwa amemwambia yote yaliyokuwa moyoni mwake, akatuma mtu akawaita wakuu wa Wafilisti, akisema, Njoni huku mara hii tu, maana ameniambia yote aliyo nayo moyoni mwake. Ndipo wakuu wa Wafilisti wakamwendea wakachukua ile fedha mikononi mwao.”

 

-          Heshima – Daudi alikuwa ni Mfalme aliyeheshimika sana mbele za Mungu na wanadamu kwa ujumla ndiye mtu anayetajwa katika maandiko kuwa aliupendeza moyo wa Mungu, jambo hili lilimpa heshima kubwa sana lakini aliposhiriki ngono na mke wa Mtu alipoteza mamlaka yake na heshima, jambo hili lilimletea aibu kubwa sana ona

 

 2Samuel 11:4 “Basi Daudi akapeleka wajumbe, akamtwaa; naye akaingia kwake; naye akalala naye; (maana yule mwanamke amekwisha kutakasika unajisi wake); kisha akarudi nyumbani kwake.

 

Unaona kitendo hiki hata Nathan nabii alimweleza wazi kuwa kwa jambo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru ona

 

2Samuel 12:14 “Lakini, kwa kuwa kwa tendo hili umewapa adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atakayezaliwa kwako hakika yake atakufa.”  

 

Nguvu na heshima aliyokuwa anapewa Daudi iliingia shidani kupitia zinaa alijivunjia heshima japo alitubu na aliendelea kuuelekeza moyo wake kwa Mungu, Lakini aliitia daosari karatasimyake ya kuwa mfalme muadilifu

 

Mwanaye Sulemani vilevile anajieleza mwenyewe kuwa wanawake ndio sababu ya anguko lake kubwa na anaeleza wazi kuwa anguko lake lilisababishwa na upenzi wake mkubwa kwa wanawake na kutokusikiliza mausia ya mama yake Lemuel anayejitaja hapa ni mwandishi wa kitabu hiki Jina Lemuel kwa Kiibrania maana yake ni “ALIYEJITOA KWA MUNGU” au “KWAAJILI YA MUNGU FOR GOD OR DEVOTED TO GOD  jina hilo halijulikani katika orodha nya wafalme wa Yuda na Israel ni huenda ni jina ambalo Sulemani aliitwa na mama yake Bathsheba au ni jina analoamua kulitumia katika utunzi wa stori hii au shairi hili kwa ni ni  anatumia jina hili nadhani anatumia jina la fumbo kwa kusudi tu la kutuletea somo husika katika Israel, kwa msingi huo mwandihi wa Mithali hizi ni Suleimani na hapa anaonyesha hekima yake aliyiojifunza kutoka kwa mama yake mwenye hekima na uadilifu kwa hiyo  hakujawahi kuwa na historia ya kuwepo mfalme aliyeitwa Lemuel, na hivyo tunaamini Lemuel ni Suleimani nanamamam yake ni Bathsheba. Sasa Pamoja na heshima kubwa sana aliyokuwa nayo na hekima aliyopewa na Mungu Sulemani aliharibikiwa kwa kutokufuata maonyo  na mafundisho ya mama yake na hapa anataka kutumia uzoefu alioupata kutufunza sis nasi tusiharibikiwe!.

 

1Wafalme 4:4-6. “Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake. Kwa kuwa Sulemani akamfuata Ashtorethi, mungu mke wa Wasidoni na Milkomu, chukizo la Waamoni. Sulemani akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, wala hakumfuata Bwana kwa utimilifu, kama Daudi baba yake.”

 

Anguko hili la Sulemani la kufikia hatua ya kuabudu miungi mingine ndilo kwa namna Fulani limechangiwa na moyo wake wa kuwapenda wanawake wengi ona

 

1Wafalme 4:1-3 “Mfalme Sulemani akawapenda wanawake wengi wageni, pamoja na binti yake Farao, wanawake wa Wamoabi, na wa Waamoni, na wa Waedomi, na wa Wasidoni, na wa Wahiti, na wa mataifa Bwana aliyowaambia wana wa Israeli, Msiingie kwao, wala wasiingie kwenu; kwa kuwa hakika wataigeuza mioyo yenu kuifuata miungu yao. Sulemani akaambatana nao kwa kuwapenda. Akawa na wake mia saba binti za kifalme, na masuria mia tatu; nao wakeze wakamgeuza moyo.”

 

Akiwa katika hali hii ya majuto baadaye ndio anatuasa kama Lemuel akionya kuwa tusikilize hekima sio lazima sana Mwalimu awe mama Lakini katika mafunzo ya Hekima wakati wowote chanzo cha mafunzo kinaitwa mama, kama mtu alikuwa na hekima kubwa sana na mali nyingi na muda na mafanikio mengi sana akapata hata anguko la kuabudu miungu ni sawa na kupoteza muda wake na kuharibikiwa katika kila kitu, Suleimani alikuwa na akili moyoni mwake hangeweza kuzungumza habari za baba yake na mama yake Bathsheba kama sisi tunavyoweza kuzungumza lakini akilini alikuwa na ujuzi kujihusu kuhusu na kupitia uzoefu alioupata ni uwazi kuwa Sheria ya Mungu pia ilikuwa imewaonya wafalme kutokujitwalia wake wengi Kumbukumbu 17: 17 “Wala asijizidishie wake, ili moyo wake usikengeuke; wala asifanye fedha zake na dhahabu kuwa nyingi mno.” Lakini yeye hakusikiliza wala kujali jambo lililopelekea kuleta madhara makubwa katika maisha yake!

 

-          Nguvu za kiroho – Kupenda wanawake licha ya kuharibu nguvu za uchumi, heshima na mali pia wanawake wanaharibu hali ya Msimamo wa kiroho, Kupenda wanawake husababisha kuwapenda wao zaidi kuliko kumpenda Mungu, Ni swala lililowazi kuwa Baba Yetu Adamu angeweza kutokukubaliana na Mwanamke katika kula lile tunda na angeweza kutoa ripoti kwa Mungu kwa kile kilichotokea na pia kuwa na toba au kuomba msamaha kwa tukio lile hii inawezekana ya kuwa ilichangiwa kwa kiwango kikubwa na upendo wake kwa mkewe na Mungu akimsomea hukumu anaanza kwa kusema Kwakuwa umeisikiliza sauti ya mkeo …. Ona

 

Mwanzo 3:17-19 “Akamwambia Adamu, Kwa kuwa umeisikiliza sauti ya mke wako, ukala matunda ya mti ambao nalikuagiza, nikisema, Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako; michongoma na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni; kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.”

 

Muda usingeweza kutosha kurejea hali ya Mwamuzi maarufu Samsoni, na Mfalme maarufu Daudi na mtu mwenye hekima Sulemani, hasa Sulemani tunaona kuwa aligeuzwa moyo kuabudu Miungu mingine, hapa tunajifunza kuwa ukiacha shetani na ushawishi mwingine wa Dunia wanawake wana nafasi kubwa sana ya kugeuza mwelekeo wa Moyo wa Mwanaume,

 

Mambo yawapasayo wanaume kufanya!

 

Luka 10:27. “Akajibu akasema, Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote; na jirani yako kama nafsi yako.”

 

Ni muhimu kufahamu kuwa wanaume wanawajibika katika kila hali itakayotokea katika maisha yao, wanaume wanatakiwa kutumia nguvu zao, akili zao, fedha zao na hisia zao zote ambazo Mungu amewapa kuhakikisha kuwa wanalinda usalama wao na baraka ambazo Mungu amezikusudia kwao, Kama wanaume wanampenda Mungu basi nivema akili zao, na moyo wao na roho zao zikaelekezwa kwa Mungu na kulitiii neno lake.

 

Moja ya adhabu iliyotangazwa na Mungu katika bustani ya Edeni kama mgogoro kati ya mwanamke na mwanaume ni pamoja na ugomvi dhidi ya nguvu, yaaani mamlaka na utawala ona Mwanzo 3:16 “Akamwambia mwanamke, Hakika nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.”

 

Kimsingi sehemu muhimu ambayo nataka kila mtu msomaji wangu na wasikilizaji wangu waweze kunielewa ni eneo ambalo maandiko yanasema TAMAA YAKO ITAKUWA KWA MUME NAYE ATAKUTAWALA, katika maandiko ya kiibrania neno NENO tamaa linatajwa kama neno TESHUQAH Katika kiibrania kwa kiingereza ni STRETCHING OUT AFTER  ambalo maana yake ni kujaribu kujitutumua dhidi ya  na Mungu anapotangaza mgogoro huu anaoshesha na matokeo ni kutawaliwa neno naye ATAKUTAWALA – linasomeka kama MASHAL ambalo hapa linatumika kama kuzidiwa, kutawaliwa, au kuwa na nguvu juu yako, kwa tafasiri nzuri maana yake ni kuwa wanawake watakuwa na tamaa ya kutaka kuwatawala wanaume lakini hatimaye watatawaliwa unaweza kuona

 

Kwa hiyo kinachotokea ni kuwa mwanaume anapojitoa katika mapenzi, kwa haraka sana Mwanamke atajinyoosha kwenye utawala, atatawala hisia zako, mwili wako, tama yako, uchumi wako, roho yako na kuiteka nafsi yako na usipoweza kujinasua katika hilo maana yake UMEWAPA WANAWAKE NGUVU ZAKO  na uwezo wako wa kutawala mambo mengine unakuwa umeishia hapo, akiweka msingi wa maongozi katika kanisa Paulo mtume katika nafsi yake analiweka hili wazi kuwa kama kiongozi hawezi kuitawala nyumba yake hataweza kufaa kuwa mtawala katika kanisa ona 1Timotheo 3:4-5 “mwenye kuisimamia nyumba yake vema, ajuaye kutiisha watoto katika ustahivu; (yaani, mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje Kanisa la Mungu?)

 

Kwa msingi huo ili mwanaume ajikwamue ni lazima ajui kujitawala na kutawala na akiweza hicho hatawekwa chini ya uweza wa kitu chochote,aidha kabla ya kujiingiza katika mahusiano mwanaume anatakiwa kupiga hesabu kama mtu aendaye vitani ajue kuwa anajiingiza katika gharama kubwa sana Luka 14:31 “Au kuna mfalme gani, akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana na yule anayekuja juu yake na watu elfu ishirini?

 

Kila mwanaume ana nguvu ya kutubu na kufanya mabadiliko katika maisha yake, kama mapenzi yanachukua nafasi kubwa sana katika kazi zetu, na kutupa kupuuzia maswala ya msingi kama Familia na ibada kwa Mungu wetu tunazo nguvu za kutengeneza mambio ya nyumba zetu na kuwa watulivu, wote tunauwezo wa kushinda, wanaume wote kwa namna moja ama nyingine tuna udhaifu wote ukiacha Yesu Kristo, lakini iko nguvu katika maamuzi ambazo tunaweza kufanya, tunaweza kutubu, neno toba katiika kiyunani ni Mtanoia ambalo maana yake ni kugeuka kuna nguvu ya kufanya maamuzi ya kugeuka na kuacha njia zetu mbaya na tukajikuta tunafanikiwa badala ya kuzitumia nguvu zetu na kupotea tunaweza kuzitumia nguvu zetu katika kumtii Mungu  

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!     



Hakuna maoni: