Jumamosi, 9 Machi 2024

Basi, wanaume, Changamkeni!


Matendo 27:14-25 “Baada ya muda mchache ukavuma upepo wa nguvu wa namna ya tufani, uitwao Eurakilo, merikebu iliposhikwa, na kutoweza kushindana na upepo, tukaiacha tukachukuliwa. Na tukipita upesi karibu na kisiwa kidogo kiitwacho Kauda tukadiriki kuikweza mashua; lakini kwa shida. Walipokwisha kuikweza wakatumia misaada, wakaikaza merikebu kwa kupitisha kamba chini yake, nao wakiogopa wasije wakakwama katika fungu liitwalo Sirti, wakatua matanga wakachukuliwa vivi hivi. Na kwa maana tulikuwa tukipigwa sana na ile tufani, siku ya pili yake wakaanza kuitupa shehena baharini. Siku ya tatu wakatupa vyombo vya merikebu kwa mikono yao wenyewe. Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka. Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao, akasema, Wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na kutokung'oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi mmoja miongoni mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami, akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. Basi, wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa.”





Utangulizi:

Wanaume ni moja ya rasilimali muhimu sana duniani kama vile ilivyo kwa wanawake, Wanaume wana mchango mkubwa sana katika jamii, kupitia uwepo wao, kazi zao, ubunifu wao, uongozi wao na katika mahusiano ya kijamii, wana mchango mkubwa sana katika familia,  Wanaume wana Mchango mkubwa katika jamii na viwandani na katika siasa na hivyo kuwa na mchango mkubwa sana wa maendeleo endelevu duniani, lakini zaidi ya yote wana umuhimu mkubwa sana katika kanisa la Mungu!, Mungu aliwatumia wanaume kama makuhani nyakati za Agano la kale, lakini katika kanisa wana mchango mkubwa sana, wana uwezo wa kuongoza, kufundisha, kuendeleza mwili wa Kristo na maendeleo mazima ya kiroho, kwa hiyo Kanisa haliwezi kabisa kuwapuuzia wanaume, Nyakati za Kanisa la kwanza Mitume waliwapa wanaume kipaumbele kikubwa sana kuna wakati hata kuongoza ibada Paulo mtume alitamani sana wanaume waifanye kazi hiyo, Katika juma hili ambalo watu wanawazungumzia wanawake mi nimechagua kujizungumzia, ili pamoja na mambo mengine tusisisitize mambo tukawaacha nyuma wanaume!

1Timotheo 2:5-8 “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu; ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote, utakaoshuhudiwa kwa majira yake. Nami kwa ajili ya huo naliwekwa niwe mhubiri na mtume, (nasema kweli, sisemi uongo), mwalimu wa Mataifa katika imani na kweli. Basi, nataka wanaume wasalishe kila mahali, huku wakiinua mikono iliyotakata pasipo hasira wala majadiliano.”

Paulo hamaanishi kuwa wanawake hawapaswi kuomba, Lakini yeye anawataka wanaume kuwa mstari wa mbele katika maombi kila mahali, wawe ndii viongozi wakubwa wa ibada nyumbani na hata makanisani,  wao ni kichwa cha familia, ni viongozi wa familia na hivyo ni viongozi wa jamii, Nyakati za leo kumekuwako na wimbi kubwa sana la wanawake kuwa na muitikio mkubwa wa kufika katika ibada na kumtafuta Mungu hata kuliko wanaume, kwa hiyo wanawake wengi wanafunguliwa na kufanikiwa, wanaponywa mioyo yao na kuwa mbali na misongo ya mawazo, wanapata unafuu, wananawiri kuliko wanaume, hii ni kwa sababu wanaume wako mstari wa mbele kupambana na dhuruma za maisha huku wakiwaachia wanawake kuutafuta uso wa Mungu, jambo linalopelekea wanaume kushambuliwa zaidi kuliko wanawake na hata kuwafanya wazimie mioyo, Leo Bwana anataka kuwakumbusha wanaume kuwa mstari wa mbele na kuchangamkia kuutafuta uso wa Mungu na uwepo wa Mungu ikiwezekana kuwazidi wanawake, wanaume wengi wamekuwa wakiishi kwa kutegemea maombi ya wake zao  na hata kufikiri kuwa ni wajibu wa wake zao kuwaombea lakini neno la Mungu linawataka wanaume kuchangamka na kurejea katika nafasi yao na kusimama na bwana na kwa kufanya hivi Kanisa litakuwa na nguvu kubwa sana na taifa letu litakuwa na maendeleo makubwa sana endapo wanaume wataamka na kuchangamka Basi wanaume Changamkeni! Tunajifunza somo hili wanaume changamkeni kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Nafasi ya Mwanaume katika moyo wa Mungu

·         Nguvu ya Mwanaume mwenye kumcha Mungu

·         Basi wanaume Changamkeni!


Nafasi ya Mwanaume katika moyo wa Mungu

Ni muhimu kufahamu kuwa Maandiko matakatifu yamewapa wanaume nafasi kubwa sana na kipaumbele cha hali ya juu katika kuonyesha kuwa wako katika moyo wa Mungu, wanaume ni wazo la Mungu, Mungu alipokusudia kuumba ulimwengu katika wazo lake kamili alikusudia kumuumba mwanaume, hivyo mwanaume ni kiongozi, ni chaguo la kwanza la Mungu bila kupuuzia wanawake lakini wanaume ni wazo la msingi,

Mwanzo 2:7-17 “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai. BWANA Mungu akapanda bustani upande wa mashariki wa Edeni, akamweka ndani yake huyo mtu aliyemfanya. BWANA Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa; na mti wa uzima katikati ya bustani, na mti wa ujuzi wa mema na mabaya. Ukatoka mto katika Edeni wa kuitilia bustani maji, na kutokea hapo ukagawanyika kuwa vichwa vinne. Jina la wa kwanza ni Pishoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Havila, ambako kuna dhahabu; na dhahabu ya nchi ile ni njema; huko kuna bedola, na vito shoham. Na jina la mto wa pili ni Gihoni; ndio unaozunguka nchi yote ya Kushi. Na jina la mto wa tatu ni Hidekeli; ndio unaopita mbele ya Ashuru. Na mto wa nne ni Frati. BWANA Mungu akamtwaa huyo mtu, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza. BWANA Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula,walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.”

Mungu alimpa Mwanaume nafasi ya Kwanza kabla ya kuumbwa kwa mwanamke, maandiko yako wazi kuwa wanaume walikuwa ni watii, kwa Mungu, walishika maagizo ya Mungu na hawakutenda dhambi, mpaka alipokuja mwanamke ndipo ilipotokea makosa, na Paulo mtume anaweka wazi kuwa mwanamume ndiye wakwanza kuumbwa kwa msingi huo wanaume ndio wakwanza kumjua Mungu na hawakuwahi kudanganywa! Mpaka alipokuja mwanamke na kuwa wala Mwanaume hakudanganywa! Ona

1Timotheo 2:13-14 “Kwa maana Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza, na Hawa baadaye.Wala Adamu hakudanganywa, ila mwanamke alidanganywa kabisa akaingia katika hali ya kukosa.”

Kwa msingi huo utaweza kuona kuwa wanaume wanapewa kipaumbele kikubwa zaidi katika kujenga mahusiano na Mungu kama viongozi wa dunia, ni jambo la kusikitisha kuona wanaume wanaachwa, ama wanapuuzuia hali ya kumcha Mungu, huku nafasi hizo zikienda kwa wanawake, kitendo cha wanaume kupuzia maswala ya Mungu, hakuna tofauti kabisa na wayahudi kumpuuzia Kristo, Maandiko yanaonyesha kuwa kama Israel ingemtii Kristo yaani wayahudi kungekuwa na baraka kubwa sana duniani, hali kadhalika kama kila mwanaume akisimama katika nafasi yake tutakuwa na dunia ya tofauti sana, muda usingeliweza kutosha kuonyesha jinsi wanaume wa kwanza katika maandiko walivyokuwa mstari wa mbele katika kujenga uhusiano na Mungu kuliko wanaume wa leo, Nuhu, Ibrahimu, Isaka, Yakobo, Ayubu, Daudi, Sulemani, na wanaume wengi kadhaa wa kadhaa walisimama na Mungu na kudumisha uhusiano na yeye, Mpaka Mungu akaitwa Mungu wa Ibrahimu na Isaka na Yakobo, Je unadhani Mungu hakuwa Mungu wa Sara, na Rebeka na Raheli? Mungu hana upendeleo alikuwa ni Mungu wao lakini waume zao ndio waliokuwa mstari wa mbele, katika kujenga madhabahu, kutafuta uso wa Mungu na kupata miongozo mbalimbali na Mungu aliwatumia na kuwa Baraka kubwa kwa dunia, leo hii wanaume wakisimama, na kuielekeza mioyo yao kwa Mungu, Nakuhakikishia Dunia itakuwa ya tofauti na ndio maana Roho wa Bwana leo anasema Basi wanaume changamkeni! Wanaume ndio waliokuwa wamepewa kipaumbele kikubwa sana katika ukuhani na baadaye katika maongozi ya Kanisa, Mungu anawaamini wanaume lakini wanaume wanapozubaa Mungu hashindwi kuwatumiwa wanawake na akiwatumia wanawake haitawapa heshima wanaume yaani itakuwa aibu kwetu wanaume kama tutazubaa na kumwachia Mungu nafasi ya kumtumia mwanamke! ona

Waamuzi 4:4-9 “Basi Debora, nabii mke, mkewe Lapidothi, ndiye aliyekuwa mwamuzi wa Israeli wakati ule. Naye alikaa chini ya mtende wa Debora, kati ya Rama na Betheli, katika nchi ya vilima vilima ya Efraimu; wana wa Israeli wakakwea kwake, awaamue. Huyo akatuma mtu akamwita Baraka wa Abinoamu toka Kedesh-Naftali, akamwambia, Je! Bwana, Mungu wa Israeli, hakutoa amri, akisema, Enenda, ukawavute kwako, huko katika mlima wa Tabori, watu elfu kumi wa wana wa Naftali, na wa wana wa Zabuloni? Nami nitakuvutia Sisera, amiri wa jeshi lake Yabini, hata mto wa Kishoni, pamoja na magari yake, na wingi wa watu wake; nami nitamtia mkononi mwako. Baraka akamwambia, Kama utakwenda pamoja nami ndipo nitakwenda; bali kama huendi pamoja nami, mimi siendi. Basi akasema, Hakika nitakwenda pamoja nawe, lakini safari utakayoiendea haitakupatia heshima wewe; maana Bwana atamwuza Sisera katika mkono wa mwanamke. Debora akainuka, akaenda pamoja na Baraka mpaka Kedeshi.”

Tito 1:5-9 “Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji kama vile nilivyokuamuru; ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii. Maana imempasa askofu awe mtu asiyeshitakiwa neno ,kwa kuwa ni wakili wa MUNGU;asiwe mtu wa kujipendeza nafsi yake,asiwe mwepesi wa hasira,asiwe mlevi wala mgomvi,asiwe mpenda mapato ya aibu. bali awe mkaribishaji, mpenda wema, mwenye kiasi, mwenye haki, mtakatifu, mwenye kudhibiti nafsi yake; akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.”

Unaona yaani tukinena kiwazimu ni kuwa ilikuwa ni mapenzi kamili kabisa Mungu kuwatumia wanaume lakini kama wanaume hawachangamki na wanazubaa, Mungu kwa shingo upande atawatumiwa wanawake, Debora alikuwa ni nabii mwamuzi, na alipewa ujumbe na Mungu kuwa Baraka anapaswa kwenda kumpiga Sisera kwani Bwana amemtia mikononi mwake, Lakini Baraka alikuwa amezubaa na akasema mimi siwezi kwenda bila wewe Debora, Debora alimueleza wazi kuwa kama nitekwenda nawe basi ujue ya kuwa Mungu atamtia Sisera komandoo katika mikono ya Mwanamke nawe hutaheshimika yaani itakuwa ni aibu kwako, Leo hii wanaume wengi wamepoteza mwelekeo, wameshindwa kusimama katika zamu zao na kuacha maswala ya Imani katika mikono ya kina mama ili hali Mungu alikuwa anawategemea wawe viongozi, wa kiroho, kijamii na hata kiuchumi, Bwana ampe neema kila Mwanaume kuchangamka na kumrudia Mungu katika jina la Yesu Kristo ameen!

Wanaume katika Nyumba wanapewa nafasi sawa na Nafasi ya Bwana Yesu Efeso 5:22-28 “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili. Lakini kama vile Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo. Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa. Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe.”

Unaona Nafasi ya Yesu Kristo katika familia imewekwa kwa mwanaume, Mwanaume ni mwokozi katika familia, ni kiongozi wa kiroho na ibada hivo ndivyo maandiko yanavyotaka na kuelekeza ndio protokali (Itifaki) ya kiroho na kama ikiwa tofauti Mungu hawezi kuuunga mkono uasi katika familia kwa maana ya kuwa kama mwanamke atachukua nafasi ya kichwa ni wazi kuwa familia hiyo haitakuwa ikiungwa mkono na Mungu, lakini je si lazima mwanaume asimame katika zamu yake duty ? lazima mwanaume ashike hatamu, awe mstari wa mbele, Mungu amekufanya kuwa kuhani wa Familia, mwokozi wa familia, mtunga shetia na mweka utaratibu wa familia sasa endapo hutasimama katika nafasi yako nakuhakikishia hautuwezi kufurahia uwepo wa Mungu majumbani mwetu!

Nguvu ya Mwanaume mwenye kumcha Mungu.

Kwa kuwa wanaume wana nafasi kubwa sana katika moyo wa Mungu, Ni muhimu kufahamu kuwa kama wao wakitoa kipaumbele katika maswala ya Mungu wanakuwa na nguvu kubwa sana katika jamii na familia na kusababisha maendeleo makubwa sana katika taifa,  Maandiko yanaonyesha wazi kuwa Mwanaume akimcha Mungu kunakuwa na mafanikio makubwa sana na uzao wake unabarikiwa ona

Zaburi 112:1-4 “Haleluya. Heri mtu yule amchaye Bwana, Apendezwaye sana na maagizo yake. Wazao wake watakuwa hodari duniani; Kizazi cha wenye adili kitabarikiwa., Nyumbani mwake mna utajiri na mali, Na haki yake yakaa milele. Nuru huwazukia wenye adili gizani; Ana fadhili na huruma na haki.”

Neno Heri mtu yule amchaye Bwana – katika Biblia ya kiingereza linatumika Neno Blessed is the man who fears the Lord, Neno hilo Man kwa kiibrania linatumika neno IYSH kimatamshi eesh ambalo tafasiri yake ni male Person kwa hiyo hapo anazungumzwa mwanamume, Heri Mwanaume yule amchaye Bwana, na andiko liko wazi kuwa mwanaume akimcha Bwana uzao wake unakuwa hodari duniani, kizazi chake kinabarikiwa, na zaidi ya yote atakuwa na utajiri na mali, sasa mwanaume anatafuta nini? Unatafuta nini tena kumcha Bwana ndio deal kumcha bwana kunakufanya mwanaume uwe na mafanikio, siri hii kama wanaume wangeijua leo, wangehudhuria ibada kuliko wanawake, wanagekuwa mstari wa mbele kwenye maombi na ibada, na utoaji usingekuwa ishu uchumi usingekuwa ishu kwa sababu maandiko yanaonyesha kungekuwa na mafanikio makubwa sana Basi wanaume changamkeni! 

Basi wanaume Changamkeni!

Kutokana na wanaume kuwa na nafasi kubwa sana katika moyo wa Mungu, na kutokana na ukweli kuwa wanaume wakiwa mstari wa mbele katika kumcha Mungu kunakuwa na Baraka kubwa sana, wanaume wamekuwa wahanga wakubwa sana wa mashambulizi ya Shetani katika maisha yao, wanaume ndio wanaoonewa zaidi na shetani,  wanateswa sana na kutokana na ugumu wao wanaumia na kufa kimya kimya, wanaume hata kibaiolojia wanazaliwa wachache, mbegu ya uzazi wa kiume hufa mapema kuliko mbegu ya uzazi wa kike, lakini hata maisha ya wanaume yamekuwa ya taabu sana  na wako nyuma wakipambana na kutafuta riziki huku wakikosa Baraka za kiroho, wanaume wamekuwa kama Esau na wanawake wamekuwa kama Yakobo katika habari ya Baraka za Mungu

Katika mstari wetu wa Msingi, tunaowaona wanaume wakiwa katika chombo ambacho kilikumbwa na dhoruba  na maandiko yanaeleza kuwa walipigwa katika chombo kile mpaka wakakata tamaa ya kuishi, chombo hiki kilikuwa kimejaa wanaume, kilikuwa kina wanaume wacha Mungu akiwepo Paulo Mtume, na Luka mwandishi wa habari hii, na wengineo, pia kulikuwa na Manahodha wa meli, walikuwepo askari, na kulikuwa na wafungwa wote walikuwa wanaume, na shehena za wafanya biashara bila shaka nao walikuwa ni  wanaume, na katika wafungwa kulikuwa na wafungwa waliofungwa kwa sababu ya uhalifu na wengine kwaajili ya injili,  kimsingi chombo hiki kinaonyesha wanaume wakiwa katika safari yao na dunia yao wakiwa wanapigwa na dhuruba, chombo hiki chenye dhoruba hakionyeshi dalili ya kuweko kwa wanawake, labda wao walikuwa majumbani salama lakini wanaume hawa ni wahangaikaji kwaajili ya maswala mbalimbali ya maisha na haya yamepelekea wakawemo katika chombo hiki wakikumbana na upepo wa hatari, mawimbi na dhuruba, giza na kupoteza matumaini ya kuishi!

Matendo 27:6-10 “Na huko yule akida akakuta merikebu ya Iskanderia, tayari kusafiri kwenda Italia, akatupandisha humo. Tukasafiri polepole kwa muda wa siku nyingi, tukafika mpaka Nido kwa shida; na kwa sababu upepo ulikuwa ukituzuia tukapita chini ya Krete, tukaikabili Salmone. Tukaipita kwa shida, pwani kwa pwani, tukafika mahali paitwapo Bandari Nzuri. Karibu na hapo pana mji uitwao Lasea. Na wakati mwingi ulipokwisha kupita, na safari ikiwa ina hatari sasa, kwa sababu siku za kufunga zilikuwa zimekwisha kupita, Paulo akawaonya, akawaambia, Wanaume, naona kwamba safari hii itakuwa na madhara na hasara nyingi, si ya shehena na merikebu tu, ila na ya maisha yetu pia.”

Paulo akawaambia WANAUME naona kwamba safari hii itakuwa na madhara na hasara nyingi, si ya shehena na merikebu tu ila na maisha yetu pia, ilikuwa ni safari ya wanaume iliyojawa na taabu na masumbufu ya kila namna, na wanaume hawa wako hatarini, hatarini kupata hasara, hatarini kukumbwa na dhuruba, hatarini kupoteza mali na hatarini kupoteza kila kitu, hii ilikuwa ni safari ya kawaida ya kimisionari kwa Paulo mtume, ya kiserikali kwa askari, ya kiserikali kwa wafungwa na ya kibiashara kwa wafanya biashara lakini wote wako hatarini na wote wanakabiliwa na kupoteza maisha  hali ilikuwa ngumu, njaa iliwapiga, baridi iliwapiga, kila mmoja alinyamaza kimya na ukweli hata kina Luka na wengineo wote walikata tamaa, hakuna mtu alikula kitu kwa siku 14 wala aliyeongea kitu!

Matendo 27:15-20 “merikebu iliposhikwa, na kutoweza kushindana na upepo, tukaiacha tukachukuliwa. Na tukipita upesi karibu na kisiwa kidogo kiitwacho Kauda tukadiriki kuikweza mashua; lakini kwa shida. Walipokwisha kuikweza wakatumia misaada, wakaikaza merikebu kwa kupitisha kamba chini yake, nao wakiogopa wasije wakakwama katika fungu liitwalo Sirti, wakatua matanga wakachukuliwa vivi hivi. Na kwa maana tulikuwa tukipigwa sana na ile tufani, siku ya pili yake wakaanza kuitupa shehena baharini. Siku ya tatu wakatupa vyombo vya merikebu kwa mikono yao wenyewe. Jua wala nyota hazikuonekana kwa muda wa siku nyingi, na tufani kuu ikatushika, basi tukakata tamaa ya kuokoka.”

Wanaume hawa walikata tamaa, walikuwa katika hali mbaya, chombo kimewapiga, upepo umewabishia hawajui kuogelea wengine, wamepoteza mwelekeo dhuruba inawapeleka kule wanakotaka wamepoteza mwelekeo wamekata tamaa ya kuokoka, mizigo imepotea, meli imewavunjikia, kama ni ndoto za kibiashara na kupata faida zimetupiliwa mbali, kila kitu kimepoteza umuhimu, hutarajii tena kufika Rumi, wala kuiona familia yako tena, kazi haina maana, ndoto zimekufa umezingirwa na dhoruba hii ndio hali ya wanaume hawaoni hata chembe ya matumaini ni giza na nuru haiko tena, matumaini yamekwenda manahodha wamepoteza tumaini, watu wameshusha nanga, na wanasubiri kifo tu, na katika mkusubiria kifo hata akida alikuwa anawaza kuwaua wafungwa

Ni Katika mazingira kama hayo Ndipo Mungu akasema na Paulo mtume kuwakumbusha wanaume kwamba wanapaswa kuchangamka, uhai wao uko mikononi mwa Mungu aliyeziumba mbingu na nchi na bahari Ni Mungu yule asiyebadilika, wakati ukutikiswa na mazingira ya aina yoyote katikati ya giza nene na lenye kukatyisha tamaa na kupoteza tumaini yeye yuko, Ni Mungu siyeshindwa anaweza asizuie dhuruba lakini hawezi kukuacha uharibiwe!

Matendo 27:21-25 “Na walipokuwa wamekaa wakati mwingi bila kula chakula, Paulo akasimama katikati yao, akasema, Wanaume, iliwapasa kunisikiliza mimi na kutokung'oa nanga huko Krete, na kupata madhara haya na hasara hii. Sasa nawapeni shauri, iweni na moyo mkuu, kwa maana hapana hata nafsi mmoja miongoni mwenu atakayepotea, ila merikebu tu. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami, akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe.Basi, wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa.”

Yalikuwa ni maneno ya kutia moyo sana kutoka kwa mtumishi wa Mungu Paulo katika wakati ule na hata leo Bado Mungu anazungumza na wanaume hawako baharini kama hawa, lakini wako kwenye mashua zao zenye dhouruba mbalimbali na bahari zao zenye majanga mbalimbali, wengine wakiwa manahodha wa vyombo vyao  na wanachokiona ni giza tu,  wanaume wamepoteza matumaini lakini leo uko ujumbe kwaajili ya wanaume Bwana amenituma nikuambie leo, Haijalishi unapitia hali gani, haijalishi umepoteza nini, umepoteza mizigo, umepoteza kazi, umepata hasara kwenye biashara yako, uko gerezani, ni mfungwa, ni askari, ni mtumishi wa Mungu, umetia nganga, huelewi hali itakuwaje ni majanga kwenye ndoa yako,  umepoteza mwelekeo katika maisha, umelowa, unasubiri kufa? Umepigika kisawasawa, huoni hata nyota ya matumaini, giza limekuzunguka pande zote, unasubiria kifo kikukute hapo hapo ulipo? Changamka, nasema changamka nasema Basi wanaume changamkeni. Basi wanaume changamkeni,  Basi wanaume changamkeni, Mungu yule ambaye mimi ni wake naye ndiye nimuabuduye amesema msiogope, Ni Mungu aliye karibu ni Mungu ambaye amenihakikishia kuwa utafika, amenihakikishaia kuwa mko salama mkononi mwangu, Mungu huyu ni mwaminifu haijalishi unapita katika hali gani lakini yeye anasema changamkeni,  Changamka kwa sababu unayoyahangaikia utayapata ukimpata Mungu kwanza, Mungu anataka makanisa yajae wanaume, waombaji wawe wanaume, lunch hour service (ibada za mchana maeneo ya karibu na kazini yajae wanaume Mungu anataka kukubariki, usikubali Heshima yako ikaenda kwa mwanamke changamka leo changamka kokote uliko huu ni ujumbe maalumu kwaajili yako Bwana amekuona nasema changamka wanaume changamkeni tusiogope dhuruba za aina yeyote kwani Mungu wetu habadiliki ahadi zake ni ndio na kweli, neno lake limahakikishwa Bwana amekekukusudia mema  naam na naamini ndivyo itakavyokuwa

Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”

Wanaume changamkeni Bwana amenituma kuwakumbusha kusimama katika nafasi yenu, mko katika moyo wake mgeukieni yeye yuko tayari kuwabariki, yuko tayari kutoa msaada tele katika maisha yenu  na taabu zenu, hamtaogopa dhuruba mkiwa na yeye Basi wanaume changamkeni, nasema basi wanaume changamkeni, nasema basi wanaume changamkeni haleluyaaaaaaaa!

Na. Rev Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!




Hakuna maoni: