Mathayo 12:42 “Malkia wa kusini atasimama
siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa;
kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya
Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”
Utangulizi:
Moja ya wanawake maarufu katika Biblia
ni pamoja na Malkia wa kusini (Malkia wa
Sheba) Mwanamke huyu mashuhuri mwenye mikogo isiyokuwa ya kawaida amewahi
kusifiwa na Yesu Kristo kama moja ya mwanadamu mwenye maamuzi thabiti ya
kutafuta hekima kwa gharama yoyote ile bila kujali umbali, Mwanamke huyu
alikataa ujinga na kuona kuliko kubaki na ujinga ni vema akasafiri kwenda mbali
kwa gharama kubwa kwenda kuitafuta Hekima, Aliandaa maswali yake magumu na
akasafiri mpaka Yerusalem makao makuu ya mji wa Israel kwaajili ya kusikia na
kupokea Hekima kutoka kwa mfalme Suleimani, Hekima ambayo Suleimani alipewa na
Mungu.
1Wafalme 10:1-13 “Na malkia wa Sheba
aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa
maswali ya fumbo. Akaingia Yerusalemu na wafuasi wengi sana, na ngamia
wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia
Sulemani, akazungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. Naye Sulemani
akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme
asimwambie. Naye malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani, na nyumba
aliyokuwa ameijenga, na chakula cha mezani pake, na watumishi wake walivyokaa,
na kusimamia kwao wangoje wake, na mavazi yao, na wanyweshaji wake, na daraja
yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana, roho yake ilizimia. Akamwambia mfalme,
Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za
hekima yako. Lakini mimi sikuzisadiki habari hizo, hata nilipokuja na kuona kwa
macho yangu; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na
kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri watumishi hawa
wako, wasimamao mbele yako siku zote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe
Bwana, Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha
Israeli; kwa kuwa Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa
mfalme, ufanye hukumu na haki. Basi akampa mfalme talanta za dhahabu mia na
ishirini, na manukato mengi, mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena
wingi wa manukato, kama hayo malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani. Tena
merikebu za Hiramu, zilizochukua dhahabu kutoka Ofiri, zikaleta kutoka Ofiri
miti ya msandali mingi sana, na vito vya thamani. Mfalme akafanya kwa mia hiyo
ya msandali nguzo za nyumba ya Bwana, na za nyumba ya mfalme, na vinubi na
vinanda vya hao waimbaji; wala haikuja miti ya msandali kama hiyo, wala
haikuonekana, hata leo. Naye mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake
yote, kila alilotaka, zaidi ya hayo aliyopewa na Sulemani kwa ukarimu wake wa
kifalme. Basi, akarudi akaenda zake katika nchi yake, yeye na watumishi wake.”
Leo basi tutachukua muda
kujifunza kwa habari ya mwanamke huyu mashuhuri katika Biblia ili tuweze
kujifunza na kufuata mfano wake wa kutafiti na kutafuta kujua habari za Yesu
Kristo ambaye ni mkuu kuliko Suleimani kwa gharama yoyote, Ikiwa yeye alitoka
pande za mwisho za dunia kwaajili ya kutafuta Hekima kwa Suleimani sisi kama
watu wa Mungu tunajikumbusha kuitafuta hekima ya Yesu Kristo, tutajifunza somo
hili Malkia wa Sheba atasimama na watu wa kizazi hiki kwa kuzingatia vipengele
vitatu vifuatavyo:-
·
Ufahamu
kuhusu malkia wa Sheba.
·
Kujifunza
kutoka kwa malkia wa Sheba.
·
Malkia wa
sheba atasimama na watu wa kizazi hiki.
Ufahamu kuhusu malkia wa Sheba.
Malkia wa Sheba ni moja ya
wanawake maarufu sana katika Biblia, mwanamke huyu alitawala katika eneo la
Pembe ya Afrika hususani Ethiopia na sehemu za Asia ya kusini yaani uarabuni au
Arabuni ya kusini, wakazi wa eneo lake waliitwa Sheba au Saba, eneo la utawala
wake ulikuwa ni sehemu ya Uarabuni ya kusini na pembe ya Afrika ikijumuisha
mataifa ya Yemen, Eritrea, Sudani, na Ethiopia, Malkia huyu ni maarufu kwa jina
la “Bilqis” katika lugha ya kiarabu
akiwa maarufu sana huko Yemen kwa jina hilo, na pia akijulikana kwa jina la “Makeda” katika nchi ya Ethiopia, hata
hivyo Malikia huyu hakutajwa kwa jina lake katika Neno la Mungu yaani Biblia,
lakini anatajwa tu kama Malikia wa kusini au Sheba au “Malkat Saba” kwa kiebrania na kwa kirumi “Basilissa Saba” katika Biblia ya Septuagint. Habari zake na kuvuma kwake katika historia amekuwa
maarufu zaidi katika Taifa la Ethiopia zaidi kuliko Yemen ambao kila mmoja
anadai ndiko alikotokea Malkia huyu, hata hivyo tafiti zinaonyesha kuwa waseba
au washeba waliishi eneo lote la uarabuni na pembe ya Afrika kwa hiyo huenda
utawala wake ulikuwa ni eneo lote la pembe ya Afrika na maeneo ya Arabuni ya
kusini, Yemen na Oman yaani arabuni ya kusini ya leo. Lakini anatajwa zaidi
katika eneo la Ethiopia ambako watoto wake walitawala badala yake, historia za
kale za Kiethiopia ziitwazo Kebra Negast zinaonyesha kuwa
alitembelea Yerusalem na alizaa mtoto na Mfalme Suleimani na mtoto huyu aliitwa
Meneleki I ambaye alikuwa baba wa
wafalme wote wa Ethiopia wenye nasaba na mfalme Suleimani huko Ethiopia mpaka
Mfalme maarufu zaidi Haile Selassie.
Malkia wa Sheba Anajitokeza katika
maandiko akisafiri kwa ngamia, akiwa na zawadi ya viungo mbalimbali, dhahabu na
mawe ya thamani akisafiri kwa safari ya msafara wa kifahari mpaka kwa Suleimani
kwaajili ya kujifunza na kuuliza maswali magumu ya maisha kutoka kwake, vyovyote
ilivyo Malkia huyu ana jambo muhimu la kutufunza ambalo ni kubwa kuitafuta
Hekima pamoja na mambo mengine.
1Wafalme 10:1-10 “Na malkia wa Sheba
aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa
maswali ya fumbo. Akaingia Yerusalemu na wafuasi wengi sana, na ngamia
wachukuao manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia
Sulemani, akazungumza naye mambo yote aliyokuwa nayo moyoni. Naye Sulemani
akamfumbulia maswali yake yote; wala hakukuwa na neno alilofichiwa mfalme
asimwambie. Naye malkia wa Sheba alipoona hekima yote ya Sulemani, na nyumba
aliyokuwa ameijenga, na chakula cha mezani pake, na watumishi wake walivyokaa,
na kusimamia kwao wangoje wake, na mavazi yao, na wanyweshaji wake, na daraja
yake ya kupandia mpaka nyumba ya Bwana, roho yake ilizimia. Akamwambia mfalme,
Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za
hekima yako. Lakini mimi sikuzisadiki habari hizo, hata nilipokuja na kuona kwa
macho yangu; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na
kufanikiwa kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri watumishi hawa
wako, wasimamao mbele yako siku zote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana,
Mungu wako, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli;
kwa kuwa Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme,
ufanye hukumu na haki. Basi akampa mfalme talanta za dhahabu mia na ishirini,
na manukato mengi, mengi sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena wingi wa
manukato, kama hayo malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani.”
Maandiko yanamtaja mwanamke huyu kwa
sifa kubwa tano muhimu sana:-
1.
Alikuwa
Mtafiti, mwenye kupenda kujifunza na mwenye busara.
Malikia huyu
anasifiwa katika maandiko kama mwanamke ambaye licha ya kuwa kiongozi katika
taifa lake yeye aliposikia habari za Hekima ya mfalme Suleimani, akapanga
kusafiri kutoka nchi ya mbali, Yesu anaita pande za mwisho wa Dunia kwaajili ya
kujifunza kutoka kwa Mfalme huyu mwenye hekima na tunaelezwa kuwa alikuwa
amejipanga kwani alikuja na maswali magumu sana kwa Mfalme Suleimani ambayo
alijibiwa yote na roho yake ikazimia. Napenda
sana tafasiri ya kiingereza ya NIV inaeleza hivi “She came to Jerusalem to test him with hard questions” yaani
malikia huyu alikuja Yerusalem kumjaribu (Suleimani) kwa Maswali magumu sana na
maswali yake yote yalijibiwa.
2Nyakati 9:1-9 “Na
malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani, alikuja ili amjaribu Sulemani
kwa maswali ya fumbo huko Yerusalemu, mwenye wafuasi wengi, na ngamia wachukuao
manukato, na dhahabu nyingi sana, na vito vya thamani; alipomfikilia Sulemani,
akamwambia mambo yote aliyokuwa nayo moyoni mwake. Naye Sulemani akamfumbulia
maswali yake yote; wala halikuwako neno alilofichiwa Sulemani, asimwambie. Naye
malkia wa Sheba alipoona hekima ya Sulemani, na nyumba aliyoijenga, na vyakula
vya mezani mwake, na kikao cha watumishi wake, na usimamizi wao wangoje wake,
na mavazi yao; na wanyweshaji wake, na mavazi yao; na daraja yake ya kupandia
mpaka nyumba ya Bwana; roho yake ilizimia. Akamwambia mfalme, Ndizo kweli
habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima yako.
Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na kuona kwa macho yangu;
wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe umezidi kuliko habari
nilizozisikia. Heri watu wako, na heri hawa watumishi wako, wasimamao mbele
yako sikuzote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako,
aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa mfalme wake
Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli, kuwathibitisha
milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu na haki. Basi
akampa mfalme talanta mia na ishirini za dhahabu, na manukato mengi mengi sana,
na vito vya thamani; wala haukuja wingi wa manukato, kama hayo aliyopewa mfalme
Sulemani na malkia wa Sheba.”
2.
Alikuwa mkarimu mtoaji:
Maandiko
yamenukuu zawadi alizokuja nazo Malkia wa Sheba kwa Mfalme Suleimani kuwa ni zawadi za kipekee na
nyingi sana kiasi kwamba neno la Mungu linasema kuwa wala hakujawahi kuja tena
wingi wa manukato sawa na yale ambayo malkia wa Sheba aliwahi kumletea Suleimani,
utoaji huu unatufunza ya kuwa Malkia huyu alikuwa na moyo wa utoaji alikuwa na
moyo wa ukarimu, hakutaka kumtembelea mtumishi wa Mungu, huku akiwa mikono
Mitupu, alitambua ya kuwa kutokana na umaarufu aliokuwa nao Suleimani na
utajiri wake hangehitaji kitu lakini Moyo wa malikia unaonekana tena katika
eneo hili, wote tunajua kuwa Mungu ambaye ni mfalme wetu ana kila kitu na
hahitaji lolote kutoka kwetu lakini Moyo wetu wa ukarimu kwake unaweza
kupelekea yeye aturidhie, na kuipokea sadaka yetu kama alivyofanya Habili.
Suleimani aliipokea zawadi na kumpa zawadi mara dufu kuliko zake
1Wafalme 10:13 “Basi
akampa mfalme talanta za dhahabu mia na ishirini, na manukato mengi, mengi
sana, na vito vya thamani; wala haukuja tena wingi wa manukato, kama hayo
malkia wa Sheba aliyompa mfalme Sulemani. Tena merikebu za Hiramu, zilizochukua
dhahabu kutoka Ofiri, zikaleta kutoka Ofiri miti ya msandali mingi sana, na
vito vya thamani. Mfalme akafanya kwa mia hiyo ya msandali nguzo za nyumba ya
Bwana, na za nyumba ya mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala
haikuja miti ya msandali kama hiyo, wala haikuonekana, hata leo. Naye mfalme
Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila alilotaka, zaidi ya hayo
aliyopewa na Sulemani kwa ukarimu wake wa kifalme. Basi, akarudi akaenda zake
katika nchi yake, yeye na watumishi wake.”
3.
Alikuwa
mwenye bidii kuitafuta hekima.
Malikia huyu
anasifiwa na Yesu Kristo kuwa alitoka pande za mwisho za dunia yaani katika
ncha ya bara la Afrika kutoka mbali sana Ethiopia na kuja kuitafiti Hekima ya Suleimani,
Yesu anasema Malikia huyu atasimama siku ya hukumu na watu wa kizazi hiki
kuwahukumu kwa uzembe, kukosa bidii, moyo wa kujifunza wakati wao wamejaaliwa
sana Hekima iliyokubwa kuliko ya Sulemaini, yaani mafundisho ya Yesu Kristo!
Mathayo 12:42 “Malkia
wa kusini atasimama siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye
atawahukumu kuwa wamekosa; kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za
dunia ili asikie hekima ya Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”
Maandiko
yanatuasa kuitafuta hekima kwa gharama yoyote ile, kutokana na hekima kuwa na
thamani kuliko madini yoyote Malikia huyu aliigundua siri hiyo na kujitajidi
sana kuitafuta Hekima, alikuwa na bidii katika kutaka kufahamu na kujifunza
tofauti sana na watu wa kizazi hiki, kama yeye alisafiri kwenda mbali sana
kutafuta maarifa akiwa na maswali yake magumu je watu wa kizazi hiki unaweza
kuwaandalia kila kitu lakini wakawa wavivu wa kusoma tu! Nyakati za leo hekima
inapatikana karibu sana, Elimu na ujuzi na maarifa yako katika kiganja cha kila
mtu leo, lakini watu hawana hamu wala kiu na shauku ya kujipa muda wa kusoma na
kujifunza n ahata kufanya utafiti wa neno la Mungu tu, na unapoandaa mada na
ikawa ndefu kwaajili ya kuweka mafafanuzi zaidi kizazi hiki hakitaki,
kinafurahia kuperuzi, habari za udaku, koneksheni, siasa, michezo na burudani
lakini kiu ya hekima ya kiungu na kuutafuta uso wa Mungu imekuwa ni ndogo sana,
malikia anatufundisha kuyatafuta maarifa.
Mithali 4:5-7 “Jipatie
hekima, jipatie ufahamu; usiusahau; Wala usiyakatae maneno ya kinywa changu.
Usimwache, naye atakuhifadhi; Umpende, naye atakulinda. Bora hekima, basi
jipatie hekima; Naam, kwa mapato yako yote jipatie ufahamu.”
4.
Alikuwa
mcha Mungu.
Katika lugha
yake kumhusu Suleimani malikia huyu anaonyesha ya kuwa alikuwa na ujuzi kuhusu
Mungu na alikuwa mcha Mungu, Yeye hakuwa tu amevutiwa na Suleimani pekee bali
alikuwa amesikia habari za Mungu wa Suleimani, maandiko yanaonyesha kuwa ni
kwaajili ya jina la Bwana alikuja na sio hivyo tu bali pia alimtukuza Mungu wa
Suleimani kutokana na umaminifu wake kwake na kwa watu wake Israel. Na alitambua kuwa Mungu anawapenda Wayahudi.
1Wafalme 10:1 “Na
malkia wa SHEBA ALIPOSIKIA HABARI ZA SULEMANI JUU YA JINA LA BWANA, alikuja ili
amjaribu kwa maswali ya fumbo.”
2Nyakati 9:5-8 “Akamwambia
mfalme, Ndizo kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako
na za hekima yako. Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na
kuona kwa macho yangu; wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe
umezidi kuliko habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri hawa watumishi
wako, wasimamao mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako. NA AHIMIDIWE BWANA,
MUNGU WAKO, aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa
mfalme wake Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli,
kuwathibitisha milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu
na haki.”
5.
Alitambua
kuwa Mungu anawapenda Israel.
Malikia huyu
alipoona kuwa Mungu amewapa watu wake Israel kiongozi mzuri, mwenye hekima ya
kupita kawaida alielewa wazi kuwa hukumu na haki zitafanyika vizuri, maamuzi
mazuri ya kumpendeza Mungu yatafanyika kwa manufaa ya taifa la Israel, alielewa
wazi kuwa Mungu anawapenda Israel, Mungu akilipenda taifa lolote lile
atalisimamishia kiongozi mzuri, Mcha Mungu na mwenye kuchukia rushwa na mwenye kupenda
haki na asiye na upendeleo ambaye ataamua mambo kwa haki, Lakini Mungu akitaka
kuwahukumu ataachilia kiongozi mbaya awatawale, siri ya mafanikio ya taifa
lolote lile kuinuka ni pamoja na taifa hilo kuwa taifa la haki.
Mithali 14:34 “Haki
huinua taifa; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote.” Mithali 29:2 “Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi; Bali mwovu
atawalapo, watu huugua.”
Uwepo wa
kiongozi kama Suleimani mwenye akili nyingi na hekima nyingi kulimfanya malikia
wa Sheba kutafasiri kuwa Mungu anawapenda watu wake Israel, Kama Malikia wa Sheba
angepata nafasi ya kumuona Bwana Yesu akiwa duniani angelisema Mungu ameupenda
ulimwengu, kwa kuwa Yesu ni mkuu kuliko Suleimani. Na maamuzi yake na utawala wake ni wa haki
Kujifunza kutoka kwa malkia wa Sheba
Umuhimu wa kufanya utafiti – Malikia wa Sheba hakukubali kusikia tu
kuhusu Suleimani bali yeye mwenyewe alitaka kuthibitisha na kujipatia ukweli wa
Mambo na kuona kama ndivyo ulivyo, wakristo tunajifunza hapa umuhimu wa kufanya
utafiti, unaposikia jambo, au mafundisho ya injili hata kama yanatolewa na
muhubiri mkubwa kiasi gani ni lazima kufanya utafiti na kujiridhisha ili uone
kama mambo ndivyo yalivyo, Utafiti unasaidia kujua mzizi wa jambo lolote iwe ni
tukio, fundisho, majungu, masingizio na kadhalika na kutusaidia kupata suluhu
ya mambo, Utafiti wa kina unatusaidia kujithibitishia mambo, kupata ushahidi,
kujifunza, kupata taarifa, kudhibiti matukio na kadhalika, utafiti unasaidia
kujenga usalama wa taifa, Malikia alikuwa na taarifa za kila kinachoendelea
ulimwenguni, na sasa alitaka kujionea ukweli wa mambo na kujithibitishia kama
hakuna chumvi katika hilo na kupata kweli iliyonyooka
1Wafalme 10:6-7 “Akamwambia mfalme, Ndizo
kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima
yako. LAKINI MIMI SIKUZISADIKI HABARI HIZO, HATA NILIPOKUJA NA KUONA KWA MACHO
YANGU; tena, tazama, sikuambiwa nusu; wewe umezidi kwa hekima na kufanikiwa
kuliko habari nilizozisikia.”
Kwa bahati mbaya sana wakristo wa
nyakati za leo hawana muda wa kufanya utafiti kuhusu neno la Mungu na mambo
mengine na kujithibitiashia kama neno hilo ndivyo lilivyo na kwa sababu hiyo
watu wengi leo ni rahisi kudanganyika, kumekuwa na mafundisho mengi potofu
katika nyakati za leo, au mafundisho ambayo hayako sawa na kweli za neno la
Mungu aidha kwa sababu ya watu wenye hila au kwa sababu ya kutafasiriwa vibaya
kwa neno la Mungu bila nia ovu, hata hivyo jambo la kusikitisha ni kuwa watu
wengi wa kizazi hiki wamekosa uungwana kwani hawayachunguzi mambo ili kupata
uhakika wake Malikia anatufundisha kuwa ni lazima tufanye uchunguzi na utafiti,
tusikimbilie haraka hara kuamini kila tunachofundishwa na kuitikia amina lakini
tufanye utafiti, tujithibitishie wenyewe, na ikiwezekana kujionea wenyewe!
Matendo 17:10-11 “Mara hao ndugu
wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia
katika sinagogi la Wayahudi. Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa
Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo,
wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”
Je wewe huwa unafanya utafiti wa
mambo na kujiridhisha kama ndivyo yalivyo? Ukifanya hivyo utakuwa na busara
kama Malikia wa Sheba na watu wa Beroya, Yesu alipoagiza wakristo wawe
wanafunzi hakutaka tuwe tu watu waamini bali alitaka tuwe shule tujifunze, tuwe
na maswali yetu na tutafute namna ya kujibizana, tufanye utafiti na
kujithibitishia mambo.Kila kitu duniani kinahitaji utafiti lakini Neno la Mungu
linahitaji utafiti zaidi kwa ubora wake na viwango vyake
Uthubutu wa kufanya mambo makubwa – Malikia wa Sheba alithubutu
kusafiri safari ndefu sana kwaajili ya kutafuta maarifa na Elimu, Lakini pia
kwaajili ya jina la Mungu na kwaajili ya kuitafuta kweli, Neno uthubutu katika
kiyunani ni “Afthentikόtita” kwa kiingereza “Authenticity” maana yake ni kanuni ya kujithibitishia,
kujihakikishia, kutaka kujionea, kutaka kuweka mambo sawasawa, Mtu anayetafuta
hekima na maarifa anataka kuweka mambo sawa, Malikia alithubutu, tunaagizwa
katika maandiko kuitafuta sana na kuishika sana Elimu, hekima na maarifa na
kuwa na bidii hata kuthubutu kufanya lolote tukitafuta mambo makubwa kwaajili
ya Mungu. Malkia alisafiri kutoka mbali sana huu ni uthubutu, wa kufanya mambo
makubwa kwaajili ya utukufu wa Mungu na ndio uthubutu uliosifiwa na Bwana Yesu
Je wewe unathubutu?
Mathayo 12:42 “Malkia wa kusini atasimama
siku ya hukumu pamoja na watu wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa wamekosa;
kwa sababu yeye alikuja kutoka pande za mwisho za dunia ili asikie hekima ya
Sulemani, na hapa yupo aliye mkuu kuliko Sulemani.”
Alikuwa mkarimu – Maandiko yanatufundisha kuwa wakarimu, kanuni
mojawapo ya mafanikio ya kibiblia ni kutoa au kuwapa watu vitu, na tunapofanya
hivyo Mungu hutubariki zaidi, hakuna kanuni ya kumpangia mtu katika utoaji
msingi wa agano jipya unawataka watu kutoa kwa ukarimu, au kwa kadiri ya neema
waliyojaliwa na Bwana, kwa hiyari na kwa moyo mkunjufu, utoaji na ukarimu ni
sehemu muhimu sana ya kuonyesha ubora wa mtu! Upendo wake na kujitoa kwake.
Matendo 20:34-35 “Ninyi wenyewe mnajua ya
kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja
nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa
kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema
mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”
Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa;
kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu
watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho
mtakachopimiwa.”
Ni ukweli ulio wazi kuwa kanuni
hii ya mafundisho ya Bwana Yesu ilifanya kazi kwa Malikia wa Kushi, kwani ni
ukweli usiopingika kuwa wakati anajitoa na zawadi nyingi sana kwa mfalme
Suleimani, Mfalme alimpa yeye zawadi zilizo nyingi zaidi kuliko alizotoa yeye,
na kututhibitishia ukweli wa lile neno apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu
2Nyakati 9:9-12 “Basi akampa mfalme talanta
mia na ishirini za dhahabu, na manukato mengi mengi sana, na vito vya thamani;
wala haukuja wingi wa manukato, kama hayo aliyopewa mfalme Sulemani na malkia
wa Sheba. Tena watumishi wa Hiramu, pamoja na watumishi wa Sulemani, walioleta
dhahabu kutoka Ofiri, wakaleta miti ya msandali, na vito vya thamani. Mfalme
akayafanya kwa miti hiyo ya msandali madari ya nyumba ya Bwana, na nyumba ya
mfalme, na vinubi na vinanda vya hao waimbaji; wala haijatokea kama hiyo katika
nchi ya Yuda. Mfalme Sulemani akampa malkia wa Sheba haja yake yote, kila
alilotaka, zaidi ya vile alivyomletea mfalme. Basi akarudi, akaenda zake katika
nchi yake, yeye na watumishi wake.”
2Wakorintho 9:6-7 “Lakini nasema neno hili,
Apandaye haba atavuna haba; apandaye kwa ukarimu atavuna kwa ukarimu. Kila mtu
na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima;
maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.”
Alimwabudu Mungu wa Israel – Malikia wa Sheba alimuabudu Mungu wa
Israel, yeye alitambua wazi kuwa Mungu amempa Suleimani ile hekima kwaajili ya
utukufu wake na kwaajili ya upendo kwa watu wake hivyo baada ya kujithibitishia
ukweli wa Mambo alimuabudu Mungu wa Israel na kumhimidi. Hakuna jambo muhimu na
kubwa sana duniani kuliko yote kama kumuabudu Mungu.
2Nyakati 9:5-8 “Akamwambia mfalme, Ndizo
kweli habari zile nilizozisikia katika nchi yangu za mambo yako na za hekima
yako. Lakini mimi sikuyasadiki maneno yao, hata nilipokuja na kuona kwa macho
yangu; wala, tazama, ukuu wa hekima yako sikuambiwa nusu; wewe umezidi kuliko
habari nilizozisikia. Heri watu wako, na heri hawa watumishi wako, wasimamao
mbele yako sikuzote, wakisikia hekima yako. Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako,
aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti chake cha enzi, kuwa mfalme wake
Bwana, Mungu wako; kwa kuwa Mungu wako amewapenda Israeli, kuwathibitisha
milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme juu yao, ufanye hukumu na haki.”
Malkia wa Sheba atasimama na watu wa kizazi hiki.
Luka 11:31 “Malkia wa Kusini ataondoka siku ya hukumu pamoja na watu
wa kizazi hiki, naye atawahukumu kuwa na hatia; kwa sababu yeye alikuja kutoka
ncha za dunia aisikie hekima ya Sulemani; na hapa pana mkubwa kuliko Sulemani.”
Yesu alimsifia na kumtaja malikia
wa Sheba ya kuwa atasimama siku ya hukumu na watu wa kizazi hiki na kuwapa
hatia kwa sababu yeye alitoka mbali kwaajili ya hekima ya Suleimani ili hali
sisi tunaye Yesu na mafundisho yake ambaye ni mkuu kuliko Suleimani, Sifa kubwa
sana aliyo nayo malikia huyu ni moyo wake wa kuitafuta hekima bila kujali kuwa
ataipatia wapi lakini alilazimika kusafiri safari ndefu sana ilhali yeye ni
mwanamke lakini hakujali kama kuitafuta hekima hiyo kungemgharimu mambo
mangapi.
Wako watu
wanasikia ujumbe wa Yesu Kristo ambao unahubiriwa kila iitwapo leo, wanaona na
kusikia mafundisho kuhusu maswala mbalimbali ya kweli za injili lakini
wanapuuzia na hawajali, Malikia aliona kuwa habari za Mungu kupitia Suleimani
zilikuwa ni za Muhimu kuliko mali, aliamua kuiacha inchi yake kwa Muda kwa
sababu ya kujifunza, aligundua kuwa Mungu ndiye chanzo cha Hekima yote kwani
alielewa kuwa hata Hekima aliyokuwa nayo Suleimani inatoka kwa Mungu alikubali
kuwa Mungu anawapenda wayahudi, alimtukuza Mungu na kumuabudu.
1Wafalme 10:9 “Na ahimidiwe Bwana, Mungu wako,
aliyependezwa nawe, ili akuweke juu ya kiti cha enzi cha Israeli; kwa kuwa
Bwana amewapenda Israeli milele, kwa hiyo amekufanya kuwa mfalme, ufanye hukumu
na haki.”
Hitimisho:
Malikia wa
Sheba ni miongoni mwa wanawake mashuhuri wa kibiblia, alikuwa ni mwanamke mwenye ujasiri, uthubutu, busara
hekima na uaminifu, Yesu alimthibitisha kwa neno lake na kumtumia kama mfano wa
kuigwa na kutuonya kwamba ni lazima tumsikilize Yesu ambaye yeye ni Mwana wa
Mungu na kwa kumsikiliza Kristo tunajiokoa na hukumu ile ijayo, ni lazima
tufanye kila jitihada kujifunza na kuitafuta kweli kama alivyofanya Malikia wa
Sheba, tuache uvivu wa kujifunza neno la Mungu, tuache uvivu na kutokuacha
kuhudhuria ibada, tuutafute uwepo wa Mungu na kujifunza kutoka kwake kwa
gharama yoyote, tumtafute Yesu, tumtafakari, tujifunze kuhusu Yesu na wakati
mwingine tuingie gharama hata za kifedha kuyatafuta maarifa sahihi kuhusu Mungu
na Neema ya Mungu itatufunika na uwepo wake tutauona na kumhimidi Mungu kwa
upendo wake mkubwa kwetu.
Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni