2Wakorintho 4:15-17 “Kwa maana mambo yote
ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani
izidishwe, na Mungu atukuzwe. Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa
nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana
dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele
uzidio kuwa mwingi sana”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa katika
dunia hii iliyojaa changamoto, maumivu, majaribu, mateso, uonevu, dhuluma,
kukosekana kwa haki, wivu, majungu na kuumizana, maneno ya kuumiza, na vita vya
kila aina ni rahisi sana kwa baadhi ya watu hususani wale walio na moyo wa unyonge
kulegea na kukata tamaa, na wakati huohuo kupoteza tumaini kwa sababu ya kuwako
kwa vikwazo mbalimbali katika maisha, Paulo mtume yeye anasema na kutangaza kwa
ujasiri “Kwa hiyo Hatulegei” ujumbe
wake Paulo mtume kwa kanisa ni ujumbe wa matumaini na ushindi na nguvu kwa kila
anayemwamini Yesu Kristo Bwana wetu, kwamba sisi ni watu wa tofauti na kamwe
hakuna awaye yote aliyemwamini Yesu anayeweza kukata tamaa, au kuzimia moyo “Kwa hiyo hatulegei” tunaendelea kukaza
mwendo kwa kadiri tunavyokutana na changamoto na majaribu ya namna mbalimbali.
Wafilipi 3:12-14. “Si kwamba nimekwisha
kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate
kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu,
sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu;
nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo,
niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”
Leo basi tutachukua muda
kujifunza sababu zilizopelekea Paulo mtume kuelezea “Kwa hiyo Hatulegei” na tutajifunza ujumbe huu kwa kuzingatia
vipengele vitatu vifuatavyo yafuatayo:-
·
Maana ya kutokulegea.
·
Sababu za kutokulegea.
·
Kwa hiyo hatulegei.
Maana ya kutokulegea:
2Wakorintho 4:15-17 “Kwa maana mambo yote
ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani
izidishwe, na Mungu atukuzwe. Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa
nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana
dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele
uzidio kuwa mwingi sana”
Neno kwa hiyo hatulegei katika Biblia
ya kiyunani linasomeka “dio ekkakeō ou”
kwa hiyo neno hatulegei kwa kiyunani ni “ekkakeō” ambalo kwa kiingereza linaweza
kutafasirika to become weak, to fail, to
faint, to become weary, or to fail in heart, or we do not give up. kwa hiyo
kwa Kiswahili maana yake hatuwi dhaifu,
hatushindwi, hatuzimii, hatuchoki, hatukati tamaa, hatuvunjiki moyo.
Maana yake hata pamoja na magumu kiasi
gani tunayokutana nayo, hata pamoja na dhiki kubwa tunayokutana nayo, hata
pamoja na changamoto kubwa tunazokutana nazo, hata pamoja na vipingamizi
vikubwa tunavyokutana navyo iwe ni katika imani, iwe ni katika huduma, iwe ni
ugumu katika jambo lolote unalokutana nalo, vyovyote vile visisitishe huduma
yako, wokovu wako, ndoa yako biashara yako, juhudi zako katika masomo, uwezo
wako wa kumtumainia na kumtegemea Mungu, utumishi wako, juhudi yako ya
kupambana na umasikini, jitihada zako za kujikwamua, mpango wako wa biashara,
mpango wako wa kilimo, mpango wako wa uwekezaji, mpango wako wa ufugaji, mpango
wako wa maendeleo, na msimamo wako katika Bwana haupaswi kuzimia kwa sababu
zozote zile kwa sababu ya ujuzi wako na maarifa yako ya kina kuhusu Mungu na
kazi yake anayoifanya ndani yako! Kamwe Mungu hawezi kukuangusha! Kwa hiyo hatulegei
Hakuna jambo baya sana kama kuzimia,
kukata tamaa, kuvunjika moyo, kuchoka, au kuwa dhaifu, adui mkubwa sana wa
mwanaridha yoyote yule ni pamoja na kuzimia, au kulegea, kuvunjika moyo,
kuogopa, wasiwasi na mashaka, na kufikiri kuwa umezidiwa, wakati wowote
mwanadamu anapokata tamaa anazuia maendeleo yake, anatengeneza ugumu wa
kushinda vikwazo na kutokusonga mbele mtu awaye yote aliyeokoka hapaswi kamwe kulegea,
kulegea na kukata tamaa na kuzimia moyo kunaashiria kuwa uweza wako na nguvu
zako ni chache, Jeshi lolote lile halina haja na Askari ambaye anazimia moyo au
kukata tamaa. Mithali 24:10 “Ukizimia siku ya taabu,
Nguvu zako ni chache.”
Kulegea kunafananishwa na mwanamke aliyebeba
mimba kwa miezi tisa akipitia shida na taabu mbalimbali kisha akaanza kusikia
uchungu alafu muda wa kujifungua unafika wakati anataka kujifungua mwanamke
huyu anachoka kusaidia kumsukuma mtoto ili atoke huo unakuwa wakati mgumu sana,
unakuwa ni wakati wa dhiki, unakuwa ni wakati wa aibu, kuwa mwanamke huyu
amebeba mimba lakini ameshindwa kuzaa, mwanamke huyu atashutumiwa kuwa
alipoteza ujasiri na nguvu wakati wa kujifungua, kwa hiyo ni lazima Mwanamke
asukume zaidi ili aweze kujifungua kama hakuna nguvu ya kuweza kujifungua maana
yake hakuna nguvu ya kushinda kwa hiyo kushindwa kunakuja, aibu inakuja,
fedheha inakuja, na jambo gumu zaidi linakabili:-
Isaya
37:1-3. “Ikawa mfalme Hezekia aliposikia hayo,
alizirarua nguo zake, akajivika nguo za magunia, akaingia katika nyumba ya
Bwana. Akamtuma Eliakimu aliyekuwa msimamizi wa nyumba yake na Shebna,
mwandishi, na wazee wa makuhani, wamejivika nguo za magunia, waende kwa Isaya nabii,
mwana wa Amozi. Wakamwambia, Hezekia asema hivi, Siku hii ni siku ya dhiki, na
aibu, na matukano; maana watoto wa tayari kuzaliwa, wala hapana nguvu za
kuwazaa.”
Kwa hiyo kulegea maana yake ni
kuzimia, ni kukaribia kushindwa ni kukosa msaada, ni kuchoka, ni kupoteza nguvu
ni uwezekano mdogo wa kushinda vikwazo na changamoto mbalimbali zinazokukabili,
kwa hiyo watu wa Mungu au watu waliookoka hawalegei, hatukati tamaa,
hatuvunjiki moyo, wala hatusitishi juhudi wakati wa mambo magumu tunasonga
mbele kama askari wema na waaminifu walioko vitani na ziko sababu kadhaa za
kutufanya tusilegee!
Sababu za kutokulegea.
1.
Kwa
sababu tunaongezewa neema – Mst 15
2Wakorintho 4:15 “Kwa
maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao
walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe.”
Mtu wa Mungu
anapopita katika changamoto za aina mbalimbali kwa kadiri ya mateso na majaribu yanavyozidi Mungu
aliyemfufua Bwana Yesu anatuongezea neema ya kupita kawaida ya kutusaidia
kushinda majaribu, kwa hiyo ndani yetu moyo wa kukata tamaa unabomolewa na
Neema inazidi na kutuinua juu zaidi, tunapewa neema ya kutusaidia wakati wa
mahitaji.
Yakobo 4:5-6 “Au
mwadhani ya kwamba maandiko yasema bure? Huyo Roho akaaye ndani yetu hututamani
kiasi cha kuona wivu? Lakini hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema,
Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”
Waebrania 4:16 “Basi
na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema
ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”
2Wakorintho 12:8-10 “Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba
kinitoke. Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika
katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa
Kristo ukae juu yangu. Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba,
na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na
nguvu.”
2.
Kwa
sababu mtu wa ndani hachakai Mst 16
2Wakorintho 4:16 “Kwa
hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa
ndani unafanywa upya siku kwa siku.”
Paulo mtume
anasema hatulegei wala hatuishiwi nguvu wala kukata tamaa kwa sababu utu wetu
wa ndani unafanywa upya siku kwa siku, wakati kila mkristo anapokutana na
majaribu na mateso na machungu ya aina mbalimbali utu wetu wa ndani unapata
uzoefu na mabadiliko na ukuaji wa kiroho, kwa hiyo hata kama kwa nje
tunaonekana kuchoka, kuugua na kuchakaa utu wetu wa ndani unafanywa upya na
kuimarishwa katika imani kupitia uhusiano wetu na Mungu, Imani, maombi, neno la
Mungu na uzoefu wa kiroho tunaoupata
kila iitwapo leo, wakati wa majaribu unachangia kwamba akili zetu zinakuwa,
ujuzi wetu unaongezeka, tunazidi kumjifunza Mungu kutoka katika pito moja
kuelekea katika pito lingine na kama ni
hivyo sasa kukatatamaa kunatokea wapi, kuchoka kunatokea wapi, kupoteza nguvu
kunatokea wapi, unafungwa gerezani, magereza inaachia, unapigwa mawe mpaka kufa
unafufuliwa na unaendelea na injili, unapigwa bakora na kuteseka unazidi
kuongezewa neema, unaviziwa getini unashushwa kwenye kikapu na injili
inaendelea, utachokaje kwa mfano unapata
ujuzi unapata hekima unajengewa ujasiri na unagundua kuwa hakuna kitu kinaweza
kukutenga na wewe na upendo wa Mungu
Warumi 8: 38-39 “Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya
kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala
yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo
chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu
ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”
3.
Kwa sababu mateso ya sasa ni mepesi na ya muda
tu. Mst 17
2Wakorintho 4:17 “Maana
dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele
uzidio kuwa mwingi sana;”
Paulo mtume
anayaona mateso ya sasa na dhiki hizi ni nyepesi na za muda tu na kuwa dhiki
hizi zinatutengenezea utukufu mkubwa sana na wa milele, watu waliookoka ni
askari, askari ili awe na utukufu mkubwa na cheo kikubwa sana lazima akasotee
katika chuo cha maafisa wa kijeshi ili kuongezewa nyota begani mwake, wakati
wote dhiki huwa zinatujaribu na kutukomaza kupata ujuzi wa kiroho na kutufanya
tuwe imara zaidi kwa sababu hiyo hatulegei tunapata uzoefu kutoka kwa dubu na
simba ili kumpiga Goliathi.
Ayubu 23:10-12 “Lakini
yeye aijua njia niendeayo; Akisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu. Mguu wangu
umeshikamana sana na hatua zake; Njia yake nimeishika, wala sikukengeuka.
Sikurudi nyuma kuiacha amri ya midomo yake; Nimeyatunza maneno ya kinywa chake
zaidi ya riziki yangu,”
1Petro 1: 6-7 “Mnafurahi
sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa
kwa majaribu ya namna mbalimbali; ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo
ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto,
kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu
Kristo.”
Paulo mtume
alikuwa anaangalia hitimisho kubwa lenye utukufu mwingi baada ya dhiki hizi za
muda mfupi, Kule mbinguni Mungu atamtukuza kila mmoja kwa kadiri ya neema na
mapito aliyoyavumilia kwa sababu hiyo hatupaswi kuangalia hivi vinavyoonekana
ambavyo ni vya muda mfupi bali tuviangalie vile vya milele, mateso na dhiki na
maumivu ni vitu vinavyoonekana lakini thawabu na utukufu mkuu Mungu aliotuwekea
ni kitu kisichoonekana kwa sasa lakini katika uzima wa milele kuna mambo
makubwa yanakuja mbele yetu.
2Wakorintho 4:18 “tusiviangalie
vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu;
bali visivyoonekana ni vya milele.”
4.
Kwa
sababu huduma hii tumeipata kwa rehema Mst 1
2Wakorintho 4:1 “Kwa
sababu hiyo, kwa kuwa tuna huduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei;”
Mungu aliyetuita
katika wokovu na kisha kutupa wito wa kumtumikia ametuheshimu sana ni rehema
kwa wewe na mimi kufanywa watumishi wa Mungu, angeweza kumtumia mwingine au
hata kuwatumia malaika ambao ni wajumbe wake, lakini kwa rehema kubwa ametupa
sisi huduma hii tunawezaje kulegea?
Tunawezaje kukata tamaa, Mungu ametukabidhi sisi kazi ya kuieneza injili
ametupenda ametuhurumia ametuheshimisha tupeleke ujumbe wa Mwanae kwa watu
wote, huduma hii ni ya rehema tu si kwa saababu tunastahili kwa hiyo kwa vipi
tukate tamaa, kwa vipi tuzimie, kwanini tulegee? Kama ni Mungu ameturehemu tumtumikie ni yeye
mwenyewe ndiye atakayekuwa chanzo cha nguvu zetu , kwa sababu hiyo ni lazima
tushinde vizuizi vyote na changamoto zote na kamwe tusizimie moyo, kazi yetu ni
kazi njema na ni kazi ya Mungu kwa hiyo tusizimie, Yeye aliyetutuma ana mamlaka
yote Mbinguni na duniani kwa sababu hiyo hatupaswi kamwe kuogopa!
Wagalatia 6:9-10 “Tena
tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.”
Mathayo 28:18-20 “Yesu
akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.
Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la
Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru
ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”
Kwa hiyo hatulegei.
Ni muhimu maneno haya yakawa
kauli mbiu katika utumishi wetu na maisha yetu ya wokovu, kila wakati unapohisi
kuchoka au kuvunjwa moyo ni lazima tukiri kuwa Hatulegei, hatuzimii moyo
hatuanguki, tunasonga mbele, kutokulegea kwetu ni ishara ya kuwa tunamjua Mungu
kwa kina na mapana na marefu, na tunamwamini, Paulo alipokuwa anasema kuwa
hatulegei yeye alikuwa anajua hakunamtu aliyepitia mateso kama yeye lakini
hakuwahi kulegea hata siku moja.
2Wakorintho 11:23-33 “Wao ni wahudumu wa
Kristo? (Nanena kiwazimu), mimi ni zaidi; katika taabu kuzidi sana; katika
vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi. Kwa
Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa
kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi;
kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; katika kusafiri mara nyingi; hatari za
mito; hatari za wanyang'anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa
mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa
ndugu za uongo; katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika
njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi. Baghairi
ya mambo ya nje, yako yanijiayo kila siku, ndiyo maangalizi ya makanisa yote.
Ni nani aliye dhaifu, nisiwe dhaifu nami? Ni nani aliyekwazwa nami
nisichukiwe? Ikinibidi kujisifu,
nitajisifia mambo ya udhaifu wangu. Mungu, Baba wa Bwana Yesu, aliye mtukufu
hata milele, anajua ya kuwa sisemi uongo. Huko Dameski liwali wa mfalme Areta
alikuwa akiulinda mji wa Wadameski, ili kunikamata; nami nikatelemshwa ndani ya
kapu, katika dirisha la ukutani, nikaokoka katika mikono yake.”
Mungu hatatuacha katika mapito ya
aina yoyote ile aliahidi kuwa atakuwa pamoja nasi na kwa sababu hiyo atatutia
nguvu kwa hiyo hata kama tunazingirwa na mazingira magumu kiasi gani hatutaangamia,
wala hatutakata tamaa, kila jaribu linao mlango wa kutokea.
2Wakorintho 4:6-10 “Kwa kuwa Mungu,
aliyesema, Nuru itang'aa toka gizani, ndiye aliyeng'aa mioyoni mwetu, atupe
nuru ya elimu ya utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo. Lakini tuna hazina
hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si
kutoka kwetu. Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali
hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi;
siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao
udhihirishwe katika miili yetu.”
Kwa hiyo Hatulegei.
Na Rev. Innocent Samuel Kamote
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni