Jumapili, 22 Machi 2026

Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu!


Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya maswala ya msingi sana yaliyowahi kutamkwa na Yesu Kristo alipokuwa akiwaandaa wanafunzi wake kwaajili ya kusulubiwa kwake ni pamoja na maneno haya “Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu” maneno haya yalisemwa masaa machache kabla kidogo ya kukamatwa na maadui zake, kimsingi maneno hayo yalikuwa yanamuhusu Shetani na utendaji wake na kuhusika kwake moja kwa moja katika swala zima la kusulubiwa kwa Yesu Kristo, ambapo Yesu alikuwa akiliona tukio hilo hilo kua ni tukio la ushindi  la hiyari na kuwa ingawa shetani atahusika katika kukamatwa na kusulubiwa kwa Yesu Kristo, Yesu Kristo alikuwa na tafasiri nyingine kuwa litakuwa ni tukio la kuokolewa kwa watu wengi Duniani na ushindi wa kiroho.

Yohana 12:31-33 “Sasa hukumu ya ulimwengu huu ipo; sasa mkuu wa ulimwengu huu atatupwa nje. Nami nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu. Aliyanena hayo akionyesha ni mauti gani atakayokufa.”

Yohana 13:26-27 “Basi Yesu akajibu, Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa. Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, Uyatendayo yatende upesi.”

Njama, mipango na usaliti pamoja na swala zima la kukamatwa kwa Yesu na mpango mzima wa kuteswa kwake na kusulubiwa msalabani kwa namna Fulani kulionekana kama kufaulu kwa mbinu za ibilisi kwani kuliratibiwa chini ya uwepo wa shetani, hata hivyo Yesu anatufungua katika kifungu hiki cha msingi kuwa mpango huo hauna madhara kwake na kuwa ni ushindi wa kiroho wa hali ya juu. Ni kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kutafakari kwa pamoja somo hili muhimu Yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu!, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele muhimu vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya neno mkuu wa ulimwengu huu.

·         Yuaja mkuu wa ulimwengu huu.

·         Wala hana kitu kwangu.

Maana ya neno mkuu wa ulimwengu huu.

Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”

Yesu Kristo aliyazungumza maneno hayo muda mfupi kidogo kabla ya kukamatwa kwake na kusulubiwa msalabani kwa mateso mabaya sana, maneno yake hayo yanatufunulia siri nzito kuhusu ushindi utakaoambatana na mateso yake, ushindi unaotokana na kuzizidi hila za shetani na njama zake; Maneno anayoyatumia hapo Mkuu wa ulimwengu huu yana maana gani hasa? Kimsingi neno yuaja mkuu wa ulimwengu huu wala hana kitu kwangu yanasomeka hivi katika lugha ya Kiyunani ona  “yáp archon toutou kósmos erchomai, kai echo oύ oudeis en emoi”  na katika kiingereza cha KJV ambayo ni literal translation Bible yaani ni biblia iliyotafasiriwa kwa mtindo wa neno kwa neno andiko hilo linasomeka hivi  “for the Prince of this world cometh, and hath nothing in me”  NIV yenyewe ambayo ni dynamic translation  inasomeka hivi “for the prince of this world is coming, He has no hold on me” kwa hiyo utabaini kuwa neno Mkuu wa ulimwengu huu au Prince of this world katika Kiyunani anaitwa “Archon” ambalo maana yeke hasa kwa Kiingereza ni “a person in authority” au “a magistrate” kimsingi Yesu alikuwa akimtaja shetani hapo ambaye anatajwa kama mwendesha mashitaka na ushawishi katika mfumo wa ulimwengu huu wa uovu “Ksómos”  taratibu zote za uovu za dunia zinaendeshwa na shetani kwa hiyo kutokana na kazi zake hizo anaitwa mtawala wa dunia hii, au mungu wa dunia hii au mkuu wa anga anayetamalaki falme na mamlaka za kiovu duniani.

Waefeso 2:1-3 “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi; ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine.”

Waefeso 6:10-12 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”

Ulimwengu wa uovu uko chini ya utawala na ushawishi na uendeshaji wa kishetani, changamoto na mapambano anayokutana nayo mwanadamu yanayopingana na maisha yetu ya kila siku na mafanikio yetu na uonevu ni matokeo ya kimwili ya kushindana kwetu katika ulimwengu wa kiroho wa utendaji wa shetani ambaye pia huitwa Mungu wa dunia hii.

2Wakorintho 4:3-4 “Lakini ikiwa injili yetu imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea; ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”

Kwa hiyo Yesu anayasema mambo hayo akiwaonyesha wanafunzi wake kuwa saa yake imewadia ya kwenda kupambana na mkuu wa ulimwengu huu, ni wakati wake sasa kwenda kufanya kazi ambayo kwa akili zake mawazo yake na mpango wake ni kuwa anakwenda kummaliza Yesu Kristo lakini Yesu Kristo katika hekima yake na mpango wake anaonyesha kuwa mpango na mkakati mzima wa ibilisi hautakuwa na mashiko kwake! 

Yuaja mkuu wa ulimwengu huu.

Kwa nini Yesu anatumia neno yuaja? Shetani alikuwa wapi na kwanini Yuaja? Neno yuaja katika Biblia ya kiyunani hapo kama tulivyoona linatumika neno “erchomai” ambalo kwa kiingereza ni “to come” au “to go” ambalo hasa linatumika kuelezea ujio halisi katika mwili  “a Physical movement” kama alikuwa akizunguka zunguka huko na kule katika ulimwengu wa roho sasa anakuja akiwa amejikamilisha kwa hiyo anakuja akijitokeza hadharani “to appear in public” “a physical arrival” kwa hiyo Shetani alikuwa amewapagaa rasmi Yuda, Viongozi wa dini, mahakama na askari wanakuja rasmi sasa kuendesha mateso na kufanya kazi ya kuua kupitia kusulubiwa kikatili, ni muhimu kuelewa hapo kuwa shetani anapokuja wazi kama alivyokuja wakati wa kumkamata Yesu maana yake ni wakati anapowavaa watu na watu hao sasa wanakuwa hawana huruma wanaingiwa na roho ya kikatili, roho mbaya inawakalia huruma ya kibinadamu inaondoka sasa wanakukusudia mabaya, kuharibu kusambaratisha na kuua!

1Petro 5:8-9 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze. Nanyi mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani, mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.”

Ayubu 2:7-8 “Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni.”

Yohana 10:10-11 “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo.”

Shetani anapokuja wazi wazi madhara yake yanaonekana wazi wazi, uharibifu mkubwa hutokea, wizi wa Afya mali na uvunjifu mkubwa wa maadili, mafarakano, ukatili uliopitiliza, anapokuja huwa anachinja ni tofauti na Yesu anapokuja, wakati Yesu anapokuja anaokoa, anakuja na uzima wa milele, shetani anapokuja anakuja na kufukuzwa kazi, anakuja na talaka, anakuja na uvamizi, anakuja kuleta hali mbaya, analeta usaliti, analeta mafarakano, kutokuelewana, anakuja na majungu, anakuja na matukio ya kuhuzunisha, hasara, na uhaini, mateso, dharau, matukano na kadhalika  hapo unapoona mambo mabaya yanakuandama kila kitu hakiendi ni kama una nuksi, mikosi na balaa ujue amekuja, Shetani anapokuja maana yake anakuja na kufikia kilele  cha utendaji wa kazi yake katika maisha yetu ataharibu kwa kiasi ambacho unaweza kufikiri kuwa Mungu hana huruma, utashuhudia utendaji wake wa kikatili ambao huwezi kulinganisha na siku au wakati mwingine wowote katika maisha.

Wala hana kitu kwangu.

Yohana 14:29-30 “Na sasa nimewaambia kabla halijatokea, kusudi litakapotokea mpate kuamini. Mimi sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa maana yuaja mkuu wa ulimwengu huu, wala hana kitu kwangu.”

Haleluya, habari njema ni kuwa Yesu alitoa taarifa hizo Yuaja mkuu wa ulimwengu huu lakini aliwathibitishia wanafunzi wake kuwa vyo vyote iwavyo hata kama anakuja na saa ile anayokuja inaonekana kuwa ni ya kutisha sana huyu jamaa hana kitu kwake!  Neno wala hana kitu kwangu linasomeka katika Kiyunani “kai echo oύ oudeis en emoi”  kwa kiingereza ESV as “No claim on me” NIV “nothing in me” NASB “ No power over me” KJV “and hath nothing in me” maana yake ni nini hasa anachokimaanisha Yesu ni kuwa pamoja na ujio wake huu wenye hatari wa kumsulubisha mwana wa Mungu Shetani hana udhibiti wowote juu ya Yesu, hana uhalali wowote, hana mamlaka yoyote, wala hausiki kwa lolote wala hana sehemu katika mpango wa Mungu wa ukombozi wa mwanadamu kupitia mauti ya Yesu msalabani Yesu haendi msalabani kwa sababu ya dhambi zake au makosa yake  anaenda kwa mpango wa Mungu kwa hiyari yake mwenyewe, kwani uwezo wa kuutoa uhai anao na uwezo wa kuutwaa anao, hakuna wa kumshitaki Yesu Kristo, uwezo huo uko kwenye mamlaka ya kimbinguni, na sio shetani wala serikali wala makuhani

Yohana 10:17-18 “Ndiposa Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena. Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu.”

Yohana 19:10-11. “Basi Pilato akamwambia, Husemi nami? Hujui ya kuwa mimi nina mamlaka ya kukufungua, nami nina mamlaka ya kukusulibisha? Yesu akamjibu, Wewe hungekuwa na mamlaka yo yote juu yangu, kama usingepewa kutoka juu; kwa hiyo yeye aliyenitia mikononi mwako yuna dhambi iliyo kubwa zaidi.”

Yohana 8:46-47 “Ni nani miongoni mwenu anishuhudiaye ya kuwa nina dhambi? Nami nikisema kweli, mbona ninyi hamnisadiki? Yeye aliye wa Mungu huyasikia maneno ya Mungu; hivyo ninyi hamsikii kwa sababu ninyi si wa Mungu.”

Waebrania 4:14-15 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu.Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.”

Kitendo cha Yesu kusulubiwa na kufa msalabani kwa mateso makali, hakikutokana na uwezo wa shetani bali ulikuwa ni mpango wa Mungu wa ukombozi wa mwanadamu, kimsingi shetani alihusika kwa upumbavu wake akiwatumia viongozi wa dunia hii waliopagawa na fikra zake, Lakini wakati anajihusisha katika mpango huu alijikaanga kabisa

1Wakorintho 2:6-9 “Walakini iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu; ila si hekima ya dunia hii, wala ya hao wanaoitawala dunia hii, wanaobatilika; bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu; ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu; lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao.”

Isaya 53:3-5 “Alidharauliwa na kukataliwa na watu; Mtu wa huzuni nyingi, ajuaye sikitiko; Na kama mtu ambaye watu humficha nyuso zao, Alidharauliwa wala hatukumhesabu kuwa kitu. Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona.”

Yesu alitaka tuelewe ya kuwa vita katika ulimwengu wa roho ni halisi, shetani yuko nyuma ya kila linalokupata anatumia usaliti, mateso na chuki lakini hata hivyo hana kitu kwa Yesu Kristo, sio tu kwa Yesu Kristo bali na kwa kila aaminiye kila mtu anayemkubali Yesu Kristo hapa duniani au ulimwenguni anakuwa kama Yesu kwa hiyo kama yeye alivyo ndivyo tulivyo, kwa hiyo kila yajapo mateso na dhiki za aina yoyote tunajua kuwa amekuja mkuu wa ulimwengu huu lakini hana kitu kwangu, zikija dhiki hivyo hivyo yakija magonjwa wewe jua yanakuja tu lakini hayana kitu kwako kwa sababu wewe ni kama alivyokuwa Kristo hapa duniani una Mungu aliye hai ndani yako

1Yohana 4:15-17 “Kila akiriye ya kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu, Mungu hukaa ndani yake, naye ndani ya Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake. Katika hili pendo limekamilishwa kwetu, ili tuwe na ujasiri katika siku ya hukumu; kwa kuwa, kama yeye alivyo, ndivyo tulivyo na sisi ulimwenguni humu.”

1Yohana 4:4 “Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”  

Ni kutokana na ushindi aliotupa Yesu Kristo pale msalabani una haki ya kumuambia shetani, magonjwa, dhiki, shida, changamoto kuwa najua umekuja lakini huna kitu kwangu, wachawi hawana madhara kwako, wambeya hawana madhara kwako, wafitini hawana madhara kwako chochote kinachokukabili hapa duniani fahamu amekuja tu lakini hana kitu kwako tembea katika ushindi huu tangu sasa tambua ya kuwa Yesu amekutetea amekufanya kuwa mshindi wa changamoto zozote zinazoendelea hapa duniani usikate tamaa wala usilie unapoteseka wala usimlaani Mungu na kumlaumu na kumuona kama amekuacha wewe tambua tu kuwa kama una Yesu kama una Mungu aliye ndani yako ni mkuu kuliko aliye katika dunia hii sema kila wakati na sema na kila changamoto ya kuwa najua kuwa yu aja mkuu wa ulimwengu huu kwa vyovyote vile hana kitu kwangu katika jina la Yesu Kristo kumbe kama alivyokuwa Yesu hapa ulimwenguni ndivyo tulivyo kwa sababu hiyi shetani hana kitu kwako na kwangu katika jina la Yesu Mwana wa Mungu aliye hai  ameen !        

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: