Marko 5:35-40 “Hata alipokuwa katika kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu? Lakini Yesu, alipolisikia lile neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu. Wala hakumruhusu mtu afuatane naye, ila Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye Yakobo. Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu. Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana.”
Utangulizi:
Kila mwanadamu mwenye akili
timamu huwa anakuwa na ndoto na matarajio kadhaa wa kadha katika maisha,
wengine huwa na matarajio makubwa wengine ya wastani na wengine ya kawaida tu
katika maisha, kwa kawaida matarajio fulani yasipofikiwa au kutimia katika
maisha husababisha msongo mkubwa wa mawazo na wakati mwingine kupoteza kabisa
matumaini, matarajio hayo wakati mwingine yanaweza kuwa ya wazi na wakati
mwingine yanaweza kuwa ya siri lakini kwa vyo vyote vile yasipofikiwa anayeumia
zaidi ni yule aliyekuwa na matumaini hayo. Neno la Mungu lasema
Mithali 13:12 “Kilichotarajiwa kikikawia
kuja, moyo huugua. Bali haja ya mtu ikipatikana, ni mti wa uzima.”
Hali hii ilimkuta mtu mmoja
muhimu sana katika maandiko, huyu anatajwa kama mojawapo ya wakuu wa sinagogi
ambaye alimwendea Yesu wakati binti yake mdogo akiwa katika hali ya kufa, ili
yamkini ikiwezekana Yesu aweze kumuhudumia na kuokoa uhai wake aendelee na
maisha naye
Marko 5:22-24 “Akaja mtu mmoja katika wakuu
wa sinagogi, jina lake Yairo; hata alipomwona, akaanguka miguuni pake, akimsihi
sana, akisema, Binti yangu mdogo yu katika kufa; nakuomba uje, uweke mkono wako
juu yake, apate kupona, na kuishi. Akaenda pamoja naye; mkutano mkuu
wakamfuata, wakimsonga-songa.”
Akiwa katika safari ya kuelekea
kumhudumia Yesu alisongwa songwa na watu wengi waliokuwa wakihitaji huduma na
zaidi sana tukio la mwanamke mmoja aliyekuwa anatokwa na damu kwa muda wa miaka
13 liliingilia kati na kwa sababu hiyo kuchelewesha safari ya Yesu kufika kwa
Yairo, Akiwa katika huduma za dharula zilizokuwa zinaingilia kati, katika huduma
za Yesu hapa linakuja kundi la watu na kumpasha habari Yairo kwamba asiendelee
kumsumbua Mwalimu kwani binti yake amekwisha kufa!
Marko 5:35 “Hata alipokuwa katika kunena,
wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako amekwisha
kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?”
Unapopiga picha ya kile
kilichokuwa kinaendelea katika moyo wa Yairo utaweza kugundua kuwa kwa vyovyote
vile moyo wake uliugua zaidi na nguvu zake zilimuishia na huenda alikata tamaa,
hali kama hii huwapata baadhi yetu pale
yale tunayoyatarajia yanapoonekana kutokuwa na uwezo wa kutimia tena, hali ya
kupoteza matumaini inatokea, ndoto zinapokufa, mambo yanapoonekana kutokwenda
kama vile tulivyotarajia, afya inapokuwa hatarini, kazi inapoonekana kufika
mwisho, mkataba unapoonekana kusimama, kazi uliyoitarajia inapoonekana kufikia
mwisho, mchongo unaousikilizia unapoota mbawa, uchumba unapovunjika, mtaji
unaposambaratika, mkopo unaposhindwa kulipwa, hasara katika biashara, mavuno
usiyoyatarajia na kadhalika wakati huu matumaini huonekana kutoweka na hiyo iko hivyo katika mtazamo wa
Binadamu Yesu anakuambia usilie kuna
matumaini
·
Mungu huona tofauti na wanadamu.
·
Kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu
· Mtoto hajafa amelala tu
Mungu huona tofauti na wanadamu
Matarajio ya kila mwanadamu
anapopitia changamoto mbalimbali ni
pamoja na suluhu ya haraka, kukosa faraja kukumbana na mipaka na kutamani
kuondoka katika maumivu yanayotusibu, wakati Mungu mtazamo wake ni wa muda
mrefu, wa kutukuza kiroho kutukomaza na kutaka tuuone utukufu wake lakini zaidi
sana kuimarisha uhusiano wetu na yeye milele, wanadamu tunaona changamoto kama
vikwazo njiani wakati Mungu anaona
vikwazo kama njia ya kuonyesha nguvu na utukufu wake, upendo wake na namna
anavyotujali lakini pia kunyamazisha
kelele za kipinzani, wakati watu wanaona mauti kama jambo gumu sana na mwisho
wa kila kitu, Yesu anaona mauti ni kama usingizi tu
Isaya 55:8-9 “Maana mawazo yangu si mawazo
yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. Kwa maana kama vile mbingu
zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia
zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”
Wakati mwanadamu anawaza kuwa
amefika mwisho, Mungu ndio kwanza anaanza jambo, wakati wanadamu wanafikiri
kuwa haiwezekani, Mungu anaona kivingine wakati mwanadamu anaona mauti na
ukavu, Mungu anaona uhai na upako, Mungu hatendi kazi kwa hisia bali kwa imani!
Ezekiel 37:1-3 “Mkono wa Bwana ulikuwa juu
yangu, naye akanichukua nje katika roho ya Bwana, akaniweka chini, katikati ya
bonde; nalo limejaa mifupa; akanipitisha karibu nayo pande zote; na tazama,
palikuwa na mifupa mingi katika ule uwanda! Nayo, tazama, ilikuwa mikavu sana.
Akaniambia, Mwanadamu, je! Mifupa hii yaweza kuishi? Nami nikajibu, Ee Bwana
MUNGU, wajua wewe.”
Mungu alipomuonyesha Ezekiel bonde
lililokuwa limejaa mifupa ya wafu na iliyokuwa imekauka sana katika maono yale
yeye hakujua kuwa uko uwezekano wa mifupa ile kufanywa hai, hivi ndivyo
inavyokuwa wakati mwanadamu anapopitia mambo magumu na hivyo ndivyo ilivyokuwa
katika moyo wa Yairo wakati akitarajia uponyaji wa binti yake anapokea taarifa
kuwa asimsumbue Mwalimu (Rabbi)
kwani binti yake amekwisha kufa, matumaini yake na ya wale waliomletea taarifa
yalikuwa yametoweka na sasa kilichokuwa kinasubiriwa ni mipango ya mazishi ya
binti wa miaka 12 akiwa anawaza hilo hata hivyo Yesu alikuwa anaona mambo kwa
njia nyingine tofauti sana na mtazamo wa kawaida, alimtia moyo Yairio aamini tu
asiogope na sio hivyo tu hata alipofika naye kwenye nyumba ya msiba na
kuwakataza watu waache kelele za maombolezo kwani mtoto amelala tu wao
walimcheka na kumdhihaki wakidhani labda huenda Yesu hajui hata maiti au mtu
aliyekufa
Marko 5:35-36. “Hata alipokuwa katika
kunena, wakaja watu kutoka kwa yule mkuu wa sinagogi, wakisema, Binti yako
amekwisha kufa; kwani kuzidi kumsumbua mwalimu?Lakini Yesu, alipolisikia lile
neno likinenwa, akamwambia mkuu wa sinagogi, Usiogope, amini tu.”
Marko 5:38-39. “Wakafika nyumbani kwa yule
mkuu wa sinagogi, akaona ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha
kuingia, akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali
amelala tu.”
Je wewe unaona nini katika ndoto
zako, unaona nini kazini kwako, unaona nini katika ndoa yako, uchumba wako,
biashara zako, na maisha yako kwa ujumla, wakati unaona kuwa umefikia mwisho
Mungu kwake yeye anaona ndio kwanza mwanzo unaanza, wakati wewe unaona giza
yeye ndio kwanza kumekucha kile kinachoonekana kama mwisho kwako ni mapumziko
ya muda tu, kamwe usikubali taarifa na tafasiri za watu ziwe tafasiri ya Mungu
juu ya maisha yako! Mwangalie Yesu tu.
Kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu
Walipofika nyumbani kwa Yairo
kulikuwa na kelele, waombolezaji walikuwa wameshajaa tayari, na walilia kwa
sauti kuu ya maombolezo na ngoma za maombolezo zilikuwa tayari
zimeshawekwa wakati wao wakifanya
maombolezo kweli kweli Yesu alikuwa anaona wanafanya ghasia, na aliwakemea na
kuwataka waache ghasia zao, wakati mwingine unapokuwa katika wakati mgumu watu
wanaokuzunguka wanaweza kuongezea balaa katika majanga yaliyokupata kwani hata
kama wewe ulikuwa na matumaini wao wanayafifisha zaidi, kila mmoja anajua kuwa
mwisho wa maisha ya mwanadamu ni kifo na kila mtu anaelewa kuwa kifo ndio
mwisho wa mambo yote na kwa sababu hiyo waliendelea na maombolezo na masikitiko
na vilio ambavyo Yesu aliona kuwa wanafanya ghasia na alipowanyamazisha
walimcheka sana, watu na mazingira yanayokuzunguka yanaweza kusema kuwa wewe
uwezi tena, wanaweza kusema muda wako umeisha, wanaweza kusema hii ndio
imetoka, Lakini Yesu ni kama alikuwa anamwambia Yairo usisikilize sauti za
makelele na ghasia za watu wewe sikiliza sauti ya Yesu kelele za watu
hazibadilishi mpango wa Mungu kamwe
Marko 5:38-43. “Wakafika nyumbani kwa yule mkuu wa sinagogi, akaona
ghasia, na watu wakilia, wakifanya maombolezo makuu. Alipokwisha kuingia,
akawaambia, Mbona mnafanya ghasia na kulia? Kijana hakufa, bali amelala tu.
Wakamcheka sana. Naye alipokwisha kuwatoa nje wote, akamtwaa babaye yule kijana
na mamaye, na wale walio pamoja naye, akaingia ndani alimokuwamo yule kijana.
Akamshika mkono kijana, akamwambia, Talitha, kumi; tafsiri yake, Msichana,
nakuambia, Inuka. Mara akasimama yule kijana, akaenda; maana alikuwa amepata
umri wa miaka kumi na miwili. Mara wakashangaa mshangao mkuu. Akawaonya sana,
mtu asijue habari ile; akaamuru apewe chakula.:”
Yesu alimshika mkono aliyekufa na akamwambia msichana nakuambia inuka, Yesu alitumia maeneno ya Kiaramu “Talitha kum” akimaanisha msichana amka, Yesu hakupiga makelele wala hakutaka kufanya muujiza huu kama maonyesho, alikuwa kazini kuwasaidia watu wenye uhitaji, alikuwa kazini kuahirisha msiba, alikuja kusaidia watu, yuko tayari kukusaidia na yuko tayari kukushika mkono, haijalishi moyo wako umepata ganzi kwa kiasi gani wala hijalishi umevunjika moyo kwa kiwango gani, haijalishi umefikia mwisho wa nguvu zako yeye akikushika mkono uhai utakurudia wakati watu wanadhani imekwisha Yesu anasema inuka, hakuna hali yoyote ile isiyoweza kubadilishwa na Mungu, tumaini lako na ndoto zako haziwezi kuzikwa mbele za Yesu Krito wa Nazareth aliye hai, wakati watu wanafikiri kuwa hali yako itadumu Yesu anaiona hali yako ni ya muda tu kwa sababu hiyo usilie, wala suiogope, acha kutazama mazingira, wala hali yako wala kushindwa kwako kwa Yesu hakuna kitu kinakufa yeye anauwezo wa kuamsha na leo ataliamsha kwenye maisha yako kila jambo linaloonekana kuwa limekufa na watu wameanza kuzomea wakifikiri mwishi umefika, kwa Yesu Kesi yako sio mwisho, kwa Yesu amini tu usiogope kelele za watu hazibadilishi mpango wa Mungu
Mtoto hajafa amelala tu
Katika uwepo wa Mungu kifo ni
jambo la muda na sio la milele, wala sio mwisho wa mambo, na ndio Maana Kristo
katika mtazamo wake huona kifo kama usingizi tu, wakati wanadamu wanaona ndio
mwisho wa kila kitu, Yesu anakiona kifo kama suingizi tu, sio tatizo kubwa yeye
ndio huo ufufuo!
Yohana 11:11-14 “Aliyasema hayo; kisha,
baada ya hayo, akawaambia, Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda
nipate kumwamsha.Basi wale wanafunzi wakamwambia, Bwana, ikiwa amelala, atapona.Lakini
Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena
habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa.”
Yesu alikuwa akionyesha mamlaka
yake kama mwana wa Mungu kuwa anao uwezo wa kufufua na ana mamlaka dhidi ya
kifo, ni yeye ndiye anayeshikilia funguo (Mamlaka) ya kifo na uzima kwa hiyo yeye
anauwezo wa kuwaamsha waliokufa kama anavyoamsha mtu usingizini, Mungu anatumia
usemi huu kuwatia moyo wanadamu kuwa kile wanachokiona kama uzito kwake yeye ni
chepesi kuliko wanavyofikiri, wanadamu wanapopoteza tumaini wakati wote
wanapaswa wakumbuke kuwa yuko Mungu ambaye kwake mambo ni mepesi tu na ndio
maana Yesu aliamua kuwatuliza waombolezaji na kuwafukuzilia mbali na kuwaamuru kuacha
ghasia, aidha Yesu alikuwa anataka kuficha mamlaka yake isijulikane na watu
nguvu za Mungu sio kwaajili ya maonyesho bali ni kwaajili ya kuwasaidia watu
wenye uhitaji, Yesu alikuwa amekuja kuahirisha msiba amkuja kuondoa ghasia
Yesu alichelewa wakati akiwa
njiani kumhudumia mtoto wa Yairo ili kutoa muda wa kifo cha mtoto na habari za
kifo ziweze kumfikia Yairo nan a majirani na ndugu na jamaa pia waombolezaji wajikusanye na kufika na kuanza kuomboleza, wataalamu wa kifo
wathibitishe kuwa mtoto amekufa, mwili uoshwe na watu wasubiri amri ya mazishi
kutoka kwa baba mzazi wa binti Yairo
Mathayo 9:23-26 “Yesu alipofika nyumbani
kwa yule jumbe, aliona wapiga filimbi, na makutano wakifanya maombolezo,
akawaambia, Ondokeni; kwa maana kijana hakufa, amelala tu. Wakamcheka sana.
Lakini makutano walipoondoshwa, aliingia, akamshika mkono; yule kijana
akasimama. Zikaenea habari hizi katika nchi ile yote.”
Mungu anapotaka kufanya mambo ya
kushangaza huonekana kama amechelewa ili nguvu zake zionekane kwamba muda sio
tatizo kwa Mungu, waombolezaji wakuzunguke ili jina la Mungu litukuzwe, wakati
mwingine wambeya watapata habari ya yale yaliyokukuta na watasengenya na kusema
Mungu atawaacha wazungumze kuwa jamaa amefikia mwisho mambo yake yameharibika kwisha habaru yake hawezi
kuinuka tena na kadhalika, kisha atafanya muujiza na hapo kila mtu atajua kuwa Mungu ana uwezo
anza kuchangamka ndugu yangu kwa sababu mtoto hajafa amelala tu, kinachokutokea
ni kwaajili ya utukufu wa Mungu, yanakutokea ili majirani wapate taarifa, ili
ndugu na jmaa wajue ili wasengenyaji wasema wakati wanakuza habari zako hapo
anatikea mwanaume anaitwa Yesu anatangaza kuwa msifanye ghasia hapa mtoto
hajafa amelala tu !
Yesu pia alkuwa akidhihirisha
nguvu zake dhidi ya uumbaji kile anachokitamka ndicho kinachokuwa ni vizuri
watu wakaamini katika neno la Mungu kuliko kuzitegemea akili zao wenyewe, Neno
la Yesu lina nguvu kwa hiyo anapotamka kuwa ndoto zako hazijakufa zimelala tu
ataamsha kila kinachoonekana kufa katika maisha yako, kwa uweza wake wa uumbaji,
Yesu alimwamsha binti Yairo ataamsha kila kitu chako kinachoonekana kufa katika
maisha yako na watu wanakudhihaki
watazuibwa vinywa vyao, anza kuchangamka kwa sababu mtoto hajafa amelala tu,
anza kuzungumza lugha ya Bwana Yesu achana na lugha za waombolezaji hizo ni kelele
tu mtoto hajafa amelala tu !
[Korajabasta, para-kashata,
roboboboso-kolotam katerrishetapapapa, kastabastariango, korabashandara-kasto,
Yesukarabastanda-ding, koroposhotorabalistakarasto, taraka san sando pang-k-satostamanifesto,
roborborboroshosta karabasa]
Mtoto hajafa amelala tu, kila kinachoonekana
kufa katika maisha yako Katika jina la Yesu Kristo nakutamkia uzima naifukuza
roho ya mauti naachilia uzima kila mahali katika mwili wako, katika ndoa yako,
katika nyuimba yako, katika familia
yako, katika biashara yako, kazini kwako, katika afya yako nakutangazia uzima
katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai amen! Mungu akutunze!
Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye hekima
.jpg)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni