Jumapili, 30 Juni 2024

Dhabihu iliyomachukizo kwa Bwana

 

Kumbukumbu 18:9-12 “Utakapokwisha kuingia katika nchi akupayo Bwana, Mungu wako usijifunze kutenda kwa mfano wa machukizo ya mataifa yale. Asionekane kwako mtu ampitishaye mwanawe au binti yake kati ya moto, wala asionekane mtu atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri,wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu. Kwa maana mtu atendaye hayo ni chukizo kwa Bwana; kisha ni kwa sababu ya hayo Bwana, Mungu wako, anawafukuza mbele yako.”


Utangulizi

Kaka zangu na dada zangu wapenzi katika Bwana, Leo tunachukua muda kuzungumzia kwa masikitiko makubwa Swala zima lenye kusikitisha na kutisha na linaloashiria kuwa jamii yetu bado tuko nyuma sana  na tuna safari ndefu sana ya kujiondoa katika ujinga na ufahamu finyu, kuhusu Mapenzi ya Mungu na upendo wake mkubwa kwa wanadamu, kwa kupambana na swala zima la mauaji ya wanadamu kwa dhana potofu za aina mbalimbali ambazo bado zinaendelea kujitokeza katika jamii, Dhana hizi ni pamoja na kutoa kafara za wanadamu, kuua wanawake vikongwe kwa kufikiri ya kuwa ni washirikina au wachawi, na mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi yaani watu wenye u-albino na kuwakata viungo vyao ili kuvitumia kwa ushirikina kwa kufikiri ya kuwa, viungo vya watu hao inaweza kusababisha mafanikio, vyeo, heshima na utajiri, Dhana hii ni dhambi na machukizo makubwa sana mbele za Mungu, na ni kinyume na Amri za Mungu na njia zake za kweli za kutuletea Baraka  wale wanaoamini katika njia ya ushirikina kwaajili ya kujiletea Heshima, vyeo, utajiri na mafanikio wamefuata njia ya mauti yao wenyewe.

Mithali 14:11-12 “Nyumba ya mtu mbaya itabomolewa; Bali hema ya mwenye haki itafanikiwa. Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, Lakini mwisho wake ni njia za mauti.”   

Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-


·         Dhabihu iliyomachukizo kwa Bwana!

·         Albino hafai kwa dhabihu

·         Njia ya kweli ya Mafanikio


Dhabihu iliyomachukizo kwa Bwana!

Ni muhimu kufahamu, kuwa ziko imani nyingi potofu na ambazo ziko kinyume na maagizo ya Mungu na mafundisho yake na imani hizo zinaelekeza kutoa dhabihu za kuua wanadamu kama kafara eti ili kuleta mafanikio ya kibiashara, cheo, heshima na utajiri kinyume kabisa na maagizo ya Mungu, imani hizi zimejikita pia katika kuwashambulia na kuwaua ili kwa kutumia damu zao na baadhi ya viungo watu hao waweze kutoa kafara kwa kuamini kuwa watajiletea mafanikio Jambo hilo ni chukizo kwa Mungu na ni kinyume kabisa na maagizo ya Mungu, na siku za karibuni watu hao wamekuwa wakiwashambulia watu wenye ulemavu wa ngozi wajulikanao kitaalamu kama Albinos, njia hiyo sio njia sahihi ya kuleta Baraka na mafanikio na badala yake inaleta laana, Hatuwezi kupata Baraka kwa kuziarifu amri za Mungu, na kwa kujikita katika ushirikina njia hiyo ni machukizo makubwa sana kwa Mungu:-

-          Kumbukumbu 12:28-32 “Maneno haya nikuagizayo yote yatunze na kuyasikiza, ili upate kufanikiwa na watoto wako baada yako milele, hapo uyafanyapo yaliyo mema na kuelekea machoni pa Bwana, Mungu wako. Bwana, Mungu wako, atakapoyakatilia mbali hayo mataifa mbele yako, huko uingiako kuyamiliki, nawe ukawatwaa, na kuketi katika nchi yao; ujiangalie, usije ukanaswa ukawafuata, wakiisha kuangamizwa mbele yako; wala usije ukauliza habari za miungu yao, ukisema, Mataifa haya waitumikiaje miungu yao? Nami nifanye vivyo. Usimtende kama haya Bwana, Mungu wako; kwani kila yaliyo machukizo kwa Bwana, ayachukiayo yeye, wameifanyia miungu yao; kwa maana hata wana wao na binti zao huiteketezea hiyo miungu yao ndani ya moto. Neno niwaagizalo lo lote liangalieni kulifanya; usiliongeze, wala usilipunguze.”

 

Mungu wa kweli, Mungu mwenyezi aliyeziumba mbingu na nchi Mungu wa Ibrahimu, na Isaka na Yakobo, alikuwa amewaokoa wana wa Israel kutoka utumwani Misri na kuwaleta katika inchi ya Mkanaani, Mungu alikuwa anataka wana wa Israel wafanikiwe kama anavyotaka wewe na mimi leo vile vile tufanikiwe, lakini Mungu aliwafundisha mojawapo ya njia ya mafanikio ni pamoja na kutenda yaliyo mema machoni pake ikiwa ni pamoja na kutokuwatoa wana wao na binti zao kafara au dhabihu kwa kuwaua na kuwateketeza kwa moto,  jambo hili Mungu alichukizwa nalo na ndilo ambalo watu walioishi Kanaani walikuwa wakiyafanya hayo na Mungu akachukizwa nao na kuwafutilia mbali.  Kwa hiyo kuwatoa wanadamu kama sadaka au dhabihu ni machukizo kwa Mungu. Lakini pia kukata viungo vya watu wenye u albino ni machukizo makuu.

 

2Wafalme 21:1-9 “Manase alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili alipoanza kutawala; akatawala miaka hamsini na mitano katika Yerusalemu, na jina la mamaye aliitwa Hefziba. Akafanya yaliyo mabaya machoni pa Bwana, sawasawa na machukizo ya mataifa, aliowafukuza Bwana mbele ya wana wa Israeli. Kwa maana akapajenga tena mahali pa juu alipopaharibu Hezekia baba yake; akamjengea Baali madhabahu, akafanya Ashera kama alivyofanya Ahabu mfalme wa Israeli. Akajiinama mbele ya jeshi lote la mbinguni na kulitumikia. Akazijenga madhabahu ndani ya nyumba ya Bwana, napo ndipo alipopanena Bwana, Katika Yerusalemu nitaliweka jina langu. Akajenga madhabahu kwa ajili ya jeshi lote la mbinguni katika behewa mbili za nyumba ya Bwana. Akampitisha mwanawe motoni, akatazama bao, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa Bwana, hata kumkasirisha. Akaiweka sanamu ya kuchongwa ya Ashera aliyoifanya ndani ya nyumba, ambayo Bwana alimwambia Daudi, na Sulemani mwanawe, Katika nyumba hii, na katika Yerusalemu, niliouchagua miongoni mwa kabila zote za Israeli, nitaliweka jina langu milele; wala sitawapotosha Israeli miguu watoke katika nchi niliyowapa baba zao; wakiangalia tu na kufanya sawasawa na yote niliyowaamuru, na kwa kuishika torati yote aliyowaamuru mtumishi wangu Musa. Walakini hawakusikia; naye Manase akawakosesha wafanye mabaya, kuliko mataifa Bwana aliowaharibu mbele za wana wa Israeli.”

 

Inawezekana katika jamii yetu watoto hao wasiteketezwe kwa moto, lakini matendo yanayofanyika ya kuwaua kuwakata baadhi ya viungo kwaajili ya sababu za kishirikina yanafanana kwa kiasi kikubwa na matukio ambayo yameorodheshwa katika machukizo mabaya ambayo Mungu anachukizwa  nayo sana, Matendo ya jinsi hii yalikuwa yakifanywa na wakazi wa Kanaani na ndio mojawapo ya sababu zilizopelekea Mungu kuwaondoa na kuwakataza Israel wasifanye kwa mfano wa matendo hayo ambayo kwa Mungu ni dhambi wafalme na watu wengi sana walioishi Kanaani walitegemea kufanya machukizo hayo kwaajili ya kuabudu miungu na kwaajili ya ushirikina wakifikiri kuwa watabarikiwa kwa kufanya mambo hayo.

 

2wafalme 3:26-27 “Naye mfalme wa Moabu alipoona ya kwamba ameshindwa vitani, alitwaa pamoja naye watu mia saba wenye kufuta panga ili wapenye hata kwa mfalme wa Edomu; wala hawakudiriki. Ndipo akamtwaa mwanawe wa kwanza, yeye ambaye angetawala mahali pake, akamtoa awe sadaka ya kuteketezwa juu ya ukuta. Kukawa hasira kuu juu ya Israeli; basi wakatoka kwake, wakarudi kwenda nchi yao wenyewe.”

 

Walawi 18:21 “Nawe usitoe kizazi chako cho chote na kuwapitisha kwa Moleki, wala usilinajisi jina la Mungu wako; mimi ndimi BWANA.”

 

Watu wote na ibada yoyote ile inayohusisha kuwatoa watoto wa kike au wa kiume na kuwateketeza, au kwa kukata viungo vyao na kwa njia zozote za kishirikina ibada za namna hiyo ziko kinyume na mapenzi ya Mungu na wote wanaofanya hivyo hufanya hayo kwa mashetani au mapepo na wanasababisha laana badala ya Baraka, nchi inalaanika na kutiwa unajisi na kuichochea hasira ya Bwana na kujitia utumwani kwa hiyo badala ya kuleta mafanikio wanayodhani, wanajiletea laana na sio wao tu na nchi zima inatiwa laama kwa sababu hizo uko ulazima wa viongozi wa dini, na imani zote na viongozi wa kimila na kisiasa kwa sababu zozote zile na kwa nia moja kusimama sawasawa na neno la Mungu na kukemea vikali swala zima la mauaji ya Albino na matendo yote ya ushirikina na upigaji ramli na utazamaji wa nyakati mbaya ambayo kimsingi yote yamekemewa katika maandiko  na ndio sababu kubwa ya mauaji ya wenye u albino na kukatwa kwa viungo

 

Zaburi 106:37-42 “Naam, walitoa wana wao na binti zao Kuwa dhabihu kwa mashetani. Wakamwaga damu isiyo na hatia, Damu ya wana wao na binti zao, Waliowatoa dhabihu kwa sanamu za Kanaani; Nchi ikatiwa unajisi kwa damu. Ndivyo walivyotiwa uchafu kwa kazi zao, Wakafanya uasherati kwa matendo yao. Hasira ya Bwana ikawaka juu ya watu wake, Akauchukia urithi wake. Akawatia mikononi mwa mataifa, Nao waliowachukia wakawatawala. Adui zao wakawaonea, Wakatiishwa chini ya mkono wao.”       

 

Albino hafai kwa dhabihu

Katika siku za miaka ya karibuni na hata majuzi hapa kumeibuka tena tabia za watu wenye mawazo ya kishirikina ambao wamekuwa wakiwaandama watu wenye ulemavu wa ngozi na kuwaua na kuwakata viungo vyao, kwa Imani za kishirikina wakifikiri kuwa wanaweza kujijengea umaarufu, kufanikisha biashara, kupata vyeo vya kisiasa na kutajirika au kujiletea mafanikio mbalimbali, lakini kama tulivyoona katika kipengele hapo juu, Dhabihu ya namna hiyo haipokelewi na Mungu aliye hai na ni dhabihu iliyo machukizo kwa Mungu, na Mungu mwenyezi amekataa kuwa yeye hapokei sadaka za aina hiyo, na hivyo maandiko yako wazi kuwa kazi hizo zinafanywa na washirikina, wachawi na wapiga ramli,  hata hivyo pia nataka kukazia wazi kuwa hata kama Mungu angelitaka sadaka za wanadamu, Mungu asingeliwatumia albino kwa dhabihu, kwa nini kwa sababu ualbino ni ulemavu wa ngozi na hivyo watu hao hawafai kwa dhabihu! Kama wasingelifaa kwa dhabihu kwa Mungu basi hawawezi kufaa kuwa dhabihu kwa miungu.

Ualbino ni changamoto ya kuzaliwa inayotokana na mvurugiko wa vinasaba vya kuzaliwa na kumfanya kiumbe anayezaliwa, kuzaliwa akiwa na changamoto ya ukosefu wa kemikali ya rangi ya ngozi ambayo kitaalamu inaitwa “Melanin” Kemikali hii ndiyo inayoamua kuwa mwili wa mwanadamu uwe na rangi gani katika ngozi, nywele na macho, kwa hiyo mtu mwenye ualbino kimsingi anakosa kirutubisho hicho na hivyo kumuweka katika mazingira yasiyo rafiki kwa jua, na hivyo kuweza kuandamwa na tatizo la saratani ya ngozi, Melanin pia ni kemikali inayohusika na kazi za uoni, na inapokosekana pia husababisha tatizo la uoni hafifu, ualbino hutokea kwa Waafrika, Wazungu, Waarabu na Waasia  na mara chache pia kwa baadhi ya wanyama. Neno Albino limetokana na neno la asili la kilatini Albus ambalo maana yake ni Nyeupe kwa hiyo watu hawa huwa na ngozi nyenye weupe usiokuwa wa kawaida, ualbino wenyewe sio ugonjwa lakini ni ulemavu wa ngozi, kwa hiyo kuna changamoto katika ngozi, nyele na macho inayowafanya wao wasiwe na ukamilifu kimaumbile, lakini wana akili, uwezo na hufanya kazi zao kama wanadamu wengine.  Kwa hiyo wao sio watu wenye ngozi nyeupe bali wao ni watu wenye ulemavu wa ngozi.

Kwa sababu ya ulemavu huu wao hawaingii katika kundi la wanyama au watu wanaotakiwa kutumika kwa dhabihu au kafara, Mwana kondoo wa kafara alitakiwa asiwe na maraka raka wala dosari ya aina yoyote ile nahii ilikuwa ikimzungumzia Yesu Kristo pekee ambaye alikuwa ni sadaka kamili isiyo na dhambi, Mwanakondoo wa sadaka ya dhabihu alikuwa na sifa zifuatazo ambazo kinabii zilimuhusu Yesu Kristo asiyekuwa na dhambi.

1.       Asiwe na Dosari -  Mwanakondoo wa Sadaka ya dhabihu alipaswa kuwa asiye na dosari wala doa la aina yoyote hii maana yake aliwakilisha ukamilifu na usafi ikiwakilisha picha ya Bwana Yesu pekee

 

Kutoka 12:5 “Mwana-kondoo wenu atakuwa hana ila, mume wa mwaka mmoja; mtamtwaa katika kondoo au katika mbuzi.”

 

2.       Alichaguliwa kwa uangalifu sana  kuhakikisha kuwa ni mkamilifu -  Mwankondoo wa sadaka ya dhabihu alichaguliwa kwa uangalifu mkubwa  ili kumpatia Mungu kitu kilicho bora, kumbuka sadaka hiyo pia ilitakiwa kuwa kondoo mume aliye mamilifu, hii maana yake ni kuwa haikutakiwa kuwa ya kike pia

                 

Walawi 1:10 “Na matoleo yake kwamba ni katika kundi, katika kondoo, au katika mbuzi, kuwa sadaka ya kuteketezwa; atatoa mume mkamilifu.”

               

3.       Sadaka ya dhabihu haikupaswa kuwa na ulemavu – Ulemavu unawakilisha mapungufu ya kawaida ya kibinadamu na wanyama kwa hiyo mnyama wa dhabihu hakupaswa kuwa mwenye ulemavu hii maana yake ni kuwa chochote chenye ulemavu hakiwezi kufaa kuwa sadaka ya dhabihu kwa Mungu au miungu

 

Kumbukumbu 17:1Usimchinjie Bwana, Mungu wako, ng'ombe wala kondoo aliye na kilema, wala neno ovu lo lote; kwa kuwa hayo ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako.”

 

4.       Dhabihu ya Albino sio dhabihu kamilifu – Mungu alitoa agizo kwamba dhabihu zinapaswa kuwa kamilifu, bila dosari, dhabihu yoyote iliyokuwa na dosari ilikuwa ni machukizo kwa Mungu, ile tu mtu kuwa Albino yaani kuwa na ulemavu wa ngozi, na ile tu kuwa Mungu amekataza mwanadamu asitolewe dhabihu tayari kuwatoa wanadamu na zaidi sana wenye ualbino ni kumtolea Mungu au miungu dhabihu isiyofaa, Mungu alikataa dhabihu za wanyama waliokuwa na ulemavu, na alikataa kutumikiwa na makuhani waliokuwa na ulemavu na hii itupe picha ya kuwa mwanadamu mwenye ualbino ni marufuku kutolewa dhabihu na sio wao tu ushirikina ni marufuku, nahata mwanadamu wa kawaida ni marufuku kutolewa dhabihu na kuabudu miungu au kuabudu mizimu, au kufuata maelekezo ya waganga, au wachawi haya yote ni machukizo kwa Bwana Mungu wetu na ni kinyume na maelekezo yake na mwelekeo wa kidhabihu.

 

Malaki 1:8 “Tena mtoapo sadaka aliye kipofu, si vibaya? Na mtoapo sadaka walio vilema na wagonjwa, si vibaya? Haya! Mtolee liwali wako; je! Atakuwa radhi nawe? Au atakukubali nafsi yako? Asema Bwana wa majeshi.”    

 

5.       Dhabihu ya Albino ni dhabihu ya udhalimu -  Mungu anachukizwa sana na watu wanaotoa dhabihu ya udhalimu, unapomtoa mtu huyu mwenye haki ya kuishi, huku ukiwa umedhulumu maisha yake hiyo ni dhambi, umeua na amri ya Mungu imesema usiue kwa hiyo huwezi kupata Baraka kwa kudhulumu maisha ya mtu hiyo ni dhambi na ni machukizo kwa Mungu, ni dhambi kwa sababu ni ushetani, ni ushirikina, mganga aliyeagiza ana dhambi, yeye aliyeagizwa ana dhambi na wale wanaohusika katika kuitekeleza dhabihu ya aina hiyo wana dhambi kwa hiyo huwezi kupata mafanikio na badala yake unavuna laana, sadaka hiyo inakuwa ni sadaka ya wasio haki na ni sadaka isiyotokana na melekezo ya kiungu ni sadaka au dhabihu ya watu wenye nia mbaya na moja kwa moja inakataliwa na Mungu. Huo ni uchawi na ushirikina kinyume na mapenzi ya Mungu, Kanisa ni lazima lisimame kinyume na uovu huu ambao sio sifa ukasikika katika jamii.  

 

Mithali 21:27 “Sadaka ya wasio haki ni chukizo; Si zaidi sana ailetapo mwenye nia mbaya!

 

6.       Dhabihu ya Albino ni dhabihu batili  -  Dhabihu ya watu wenye ualbino ni dhabihu ambayo haikuwahi kuagizwa na Mungu wala miungu wala hata mashetani, kwa hiyo ni machukizo na ni batili, kwa hiyo Mungu anachukizwa nazo, wala hazifurahii, watu wanaofanya hayo watapata laana badala ya Baraka wanazozifikiria kuwa watazipata, sio tu wanajiletea laana kwa familia zao lakini pia wanajiletea laana kwa taifa lao.

 

Isaya 1:10-16 “Lisikieni neno la Bwana, enyi waamuzi wa Sodoma; tegeni masikio msikie sheria ya Mungu wetu, enyi watu wa Gomora. Huu wingi wa sadaka zenu mnazonitolea una faida gani? Asema Bwana. Nimejaa mafuta ya kafara za kondoo waume, na mafuta ya wanyama walionona; nami siifurahii damu ya ng'ombe wala ya wana-kondoo wala ya mbuzi waume. Mjapo ili kuonekana mbele zangu, ni nani aliyetaka neno hili mikononi mwenu, kuzikanyaga nyua zangu? Msilete tena matoleo ya ubatili; uvumba ni chukizo kwangu; mwezi mpya na sabato, kuita makutano; siyawezi maovu hayo na makutano ya ibada. Sikukuu zenu za mwezi mpya na karamu zenu zilizoamriwa, nafsi yangu yazichukia; mambo hayo yanilemea; nimechoka kuyachukua. Nanyi mkunjuapo mikono yenu, nitaficha macho yangu nisiwaone; naam, mwombapo maombi mengi, sitasikia; mikono yenu imejaa damu. Jiosheni, jitakaseni; ondoeni uovu wa matendo yenu usiwe mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya;”

 

7.       Dhabihu ya kichawi au za watu wanaoabudu miungu mingi - Mungu anachukizwa na dhabihu zote za kishirikina zinazotolewa kwa miungu na ibada zote za kishirikina na sanamu zilizo kinyume na Imani ya kweli ibada hizo zote ni machukizo kwa Mungu

 

Yeremia 7:9-10 “Je! Mtaiba, na kuua, na kuzini, na kuapa kwa uongo, na kumfukizia Baali uvumba, na kuifuata miungu mingine ambayo hamkuijua; kisha mtakuja na kusimama mbele zangu katika nyumba hii, iitwayo kwa jina langu, na kusema, Tumepona; ili mpate kufanya machukizo hayo yote?

 

Mungu hataki ibada zenye michanganyo, ibada zote za namna hii zinaitwa ibada za kishirikina, kimsingi watu wanaotoa sadaka hizo au dhabihu hizi mbaya wana dini zao ambazo zinaweza kuwa zinamtaja Mungu na wakati huo huo wanashiriki maswala ya uchawi na uchafu mkubwa unaohusisha kuwaua watu wa Mungu.

Kwa hiyo kimsingi kwanza wote tunafahamu kuwa Mungu hakubaliani na sadaka ya dhabihu ya kuwatoa wanadamu, lakini pili tunakubaliana kuwa Mungu hapokei sadaka yenye dosari, au yenye kasoro au isiyokamilika, au isiyofaa, au yenye dosari au ulemavu wa aina yoyote, kwa msingi huo hata kama wanadamu wangekuwa wanatolewa dhabihu kwa Mungu basi mtu mwenye u albino hafai kwa dhabihu, sio hivyo tu hata mtoa dhabihu hakupaswa kuwa na ulemavu wa aina yoyote ile katika nyakati za agano la kale kwa hiyo kama sheria ya Musa ingelikuwa inafanya kazi hata sasa basi mwenye ualboni hangeweza kufaa kuwa mtumishi wa Mungu au kuhani, Hapa lengo langu sio kuwabagua wenye ualbino lakini nataka kunyesha kimaandiko ni namna gani Albino wasingeliweza kufaa kwa kafara

Walawi 21: 17-21 “Nena na Haruni, umwambie, Mtu awaye yote wa kizazi chako wewe katika vizazi vyao, aliye na kilema, asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake. Kwa kuwa mtu awaye yote aliye na kilema hatakaribia; mtu kipofu, au kiwete, au mtu aliye na pua iliyoharibika, au aliye na kitu kilichozidi vimpasavyo mwili, au mtu aliyevunjika mguu, au aliyevunjika mkono, au aliye na kijongo, au aliye kibeti, au aliye na kilema cha jichoni, au aliye na upele, au mwenye buba, au aliyevunjika mapumbu;mtu awaye yote wa kizazi cha Haruni kuhani aliye na kilema asikaribie kuzisongeza sadaka za BWANA kwa njia ya moto; ana kilema huyo asikaribie kusongeza chakula cha Mungu wake.”               

Lengo langu hasa ni nini hapo, kwa kawaida miungu mingi na hata shetani ameigiza kila kitu kutoka kwa Mungu mwenyezi, kwa hiyo kama unavyoona tabia ya Mungu mwenyezi kutaka kitu kisicho na mawaa wala doa wala dosari na wala kisicho na kilema; Hali kadhalika miungu na mashetani pia hutaka au hutembea katika kanuni hizo hizo kwa sababu hiyo, kwa kuwa watu wenye ualbino ni wanadamu kamili lakini wana ulemavu wa ngozi, kwa mujibu wa torati hawafai kwa dhabihu, Maana yake ni nini? Wale wanaowaua na kuwakata viungo watu wenye ulemavu wa ngozi, wanafanya makosa makubwa sana kwa sababu hakuna ibada ya aina yao inayoweza kukubalika na miungu ya aina yoyote.

Lengo langu ni nini hapa watu wenye changamoto ya ualbino wanapaswa kuachwa, na kuwa watu huru wasitishiwe kwa sababu zozote zile kwa sababu hawafai kwa huo ushirikina, lakini wanafaa katika jamii, mchango wao katika jamii unahitajika, Mungu hakuwaumba wao wawe maalumu kwaajili ya dhabihu hapana, waganga wanaotaka viungo vya watu wenye ulemavu wa ngozi ni waongo na kamwe hawajui kabisa kanuni za utendaji wa maswala ya kiroho yawe ya Mungu au ya kienyeji, wenye kushiriki zoezi hili ni washirikina kamili na ni wachawi na wapiga ramli na ni watu wasioelimika na waliopitwa na wakati au wako nyuma sana, wanasababisha mashaka, na huzuni na kuwafanya watu hao wa waishi kwa hofu, na wazazi wao na jamii isiwe mahali salama ni jambo la kusikitisha ya kuwa mtu mwenye tatizo anaongezewa tatizo badala ya kuwafariji na kulia nao katika changamoto hii ya ukosefu wa melanin katika maisha yao.

Namuomba Mungu kuwa tiba ya kuweza kurejesha melanini katika jamii hii igunduliwe lakini pia watu wa maombezi, tumuombe Mungu ili aweze kuwaponya watu wenye changamoto hii, aidha mimba zote na  watu wote walio wajawazito waombewe na kuwekwa katika mikono ya Bwana na wazingatie kanuni zote za kiafya na kitabibu ili kuzuia uwezekano wa kuzaliwa kwa watu wenye ulemavu huu.

Imani yangu ni kuwa kama sababu zinaanza kueleweka hatutashindwa kupata majibu ya kushughulika na changamoto hii, naungana na wanajamii wote duniani, na Afrika na katika ukanda wetu kukemea na kusimama kinyume na matendo yote ya kijinga ikiwepo tendo hili la kuwatoa walemavu wa ngozi na kuwafanya dhabihu kwa miungu nalaani kitendo hiki na wote wanaojihusisha na matendo haya na naiombea serikali kuwa ifanikiwe kumkamata kila mtu aliye kwenye mnyororo wa matendo haya maovu katika jamii, matendo haya ukiacha ya kuwa yanamuudhi Mungu lakini ni ishara ya jamii jinga isiyoelimika wala kustaarabika yanaposikilizika  katika masikio yetu matukio kama haya hasa katika nyakati za karibu na chaguzi za serikali za mitaa na serikali kuu, Mungu atuepushe na kuwa na jamii na viongozi wanaoamini katika ushirikina na Mungu awanyime mamlaka zozote zile zinazopatikana kwa njia ya kishirikina na wananchi wasimchague mtu yeyote yule anayekisiwa kujihusisha na ushirikina kwani hawezi kutuletea maendeleo ya kweli wakati yeye yuko nyuma kimaendeleo!

Naelezea haya kwa uchungu mkubwa kwa sababu sitaki kuamini kuwa katika jamii zetu bado tunao watu wanaosadiki mambo ya kijinga na huku wengine wakiwa ni viongozi wa kidini!, Hebu tuwaache ndugu zetu, kaka zetu na dada zetu wenye ualbino wawe huru waishi kwa Amani na utulivu, tuwaache wapambane na hali zao badala ya kuwaongezea maumivu mengine, na kila kiongozi wa ngazi yoyote kuanzia ya familia ahakikishe ya kuwa matendo haya hayatajwi na wala kusikika katika taifa letu, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kufunguka macho na kuondoka katiia ujinga huu katika jina la Yesu Kristo amen.

Njia ya kweli ya Mafanikio

1.       Mungu kwanza – Mungu aliahidi katika neno lake ya kuwa tukimtanguliza yeye na kumuweka yeye mbele yeye atayafanikisha maisha yetu, hakuna mafanikio ya kweli nje ya Mungu, Mungu ndiye mwenye neema ya kutufanikisha, hivyo ni muhimu kwetu kuutafuta kwanza ufalme wa Mungu na hakli yake naye na mengine tutazidishiwa.

 

Zaburi 84:11 “Kwa kuwa Bwana, Mungu, ni jua na ngao, Bwana atatoa neema na utukufu. Hatawanyima kitu chema Hao waendao kwa ukamilifu.”

 

Mathayo 6:33 “Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.”

 

Tunapomuweka Mungu mbele yeye hutupatia mahitaji yetu yote, na huu ni msingi mmojawapo muhimu wa mafanikio, Mungu ndiye anayetupa akili za kupata utajiri.

 

Kumbukumbu 8:18 “Bali utamkumbuka Bwana, Mungu wako, maana ndiye akupaye nguvu za kupata utajiri; ili alifanye imara agano lake alilowapa baba zako, kama hivi leo.”

 

2.       Utii kwa maagizo ya Mungu – Mafanikio ya kweli yana uhusiano mkubwa sana na utii kwa amri za Mungu au maagizo yake, tunapoyatii maagizo yake yeye hutuongoza na kutuletea Baraka kubwa ambazo zinatuletea mafanikio

Yoahua 1: 8 “Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali yatafakari maneno yake mchana na usiku, upate kuangalia kutenda sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; maana ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana.”

 

1Wafalme 2:1-3 “Basi siku ya kufa kwake Daudi ikakaribia, akamwusia Sulemani mwanawe, akasema, Mimi naenda njia ya ulimwengu wote; basi uwe hodari, ujionyeshe kuwa mwanamume; uyashike mausia ya Bwana, Mungu wako, uende katika njia zake, uzishike sheria zake, na amri zake, na hukumu zake, na shuhuda zake, sawasawa na ilivyoandikwa katika torati ya Musa, upate kufanikiwa katika kila ufanyalo, na kila utazamako;”  

 

3.       Mwamini Mungu, mtumainie yeye kwa moyo wako wote  – unapoamini katika Mungu kwa moyo wako wote na kudumisha uhusiano wake nay eye anakuwa msaada mkubwa katika kila aina ya dhuruba tunayokutana nayo

 

Mithali 3:5-7 “Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako mwenyewe; Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako; Mche Bwana, ukajiepushe na uovu.”

 

Warumi 8:32 “Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye?

 

4.       Kufanya kazi kwa bidii   - Maandiko yanatufundisha umuhimu wa kufanya kazi kwa bidi, na kwa uaminifu, Mafanikio hayaji kwa uvivu, bali ka juhudi na uaminifu na kujituma tunapofanya hivyo Mungu yeye hubariki kazi za mikono yetu hii ndio kanuni mojawapo muhimu ya kibiblia ya mafanikio na kwa uvumilivu

 

Mithali 10:4 “Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini; Bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha.”

               

Kumbukumbu 28:11- 12 “Bwana atakufanya uwe na wingi wa uheri, katika uzao wa tumbo lako, na uzao wa wanyama wako wa mifugo, na uzao wa nchi yako, katika nchi Bwana aliyowaapia baba zako kwamba atakupa. Atakufunulia Bwana hazina yake nzuri, nayo ni mbingu, kwa kutoa mvua ya nchi yako kwa wakati wake, na kwa kubarikia kazi yote ya mkono wako; nawe utakopesha mataifa mengi, wala hutakopa wewe.”

 

5.       Ni heri kutoa kuliko kupokea -  Matendo ya ukarimu kwa wengine na utoaji ni mojawapo ya njia inayofungua milango ya Baraka, wanadamu wote bila kujali Imani zao wanapoishi katiika kanuni hii wanabarikiwa, maandiko yanashuhudia kwamba ni vema kutoa na kutoa kwetu kunafungua mlango wa Baraka na mafanikio makubwa sana

 

Matendo 20:34-35 “Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”

 

Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.”

 

Matendo 10:1-4 “Palikuwa na mtu Kaisaria, jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu sadaka nyingi, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, Kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na sadaka zako zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu.”

 

Tunapoishi maisha ya ukarimu na kujitoa kwa watu wenye mahitaji tunamkopesha Mungu na kutuweka katika njia ya Baraka na mafanikio ya aina mbalimbali kutoka kwa Mungu

 

6.       Maombi na kudumisha uhusiano na Mungu – Kwa kuwa Mungu ndiye chanzo cha mafanikio ya kweli ni vema kwetu kuhakikisha ya kuwa tunadumisha uhusiano  wetu nay eye,  kwa kusali na kuomba, huku tukikumbuka ya kuwa wakati wote Mungu anatuwazia mema

 

Yeremia 29:11-13 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho. Nanyi mtaniita, mtakwenda na kuniomba, nami nitawasikiliza. Nanyi mtanitafuta na kuniona, mtakaponitafuta kwa moyo wenu wote.”

Hitimisho:

Ndugu zangu, Mafanikio ya kweli nay a kudumu yanapatikana kwa kuutafuta uso wa Mungu na kumpa yeye kipaumbele, kutii amri zake na kwa neema yake tukimtumaini yeye kwa moyo wetu wote na kufanya kazi kwa bidi, na kwa uaminifu, na kuonyesha matendo ya ukarimu kwa wengine Mungu atatupa mafanikio makubwa sana, Mafanikio ya kishirikina sio ya kudumu, na hayawezi kukupa Amani ya kweli, inasikitisha sana kuona au kusikia kuwa bado kuna watu wana akili za kizamani za wakati wa ujinga kwa kutoa sadaka ya viungo vya binadamu na zaidi sana wenye tatizo la Albinism kwa kuwaua na kuchukua baadhi ya viungo vyao hiyo haiwezi kutupa mafanikio ya kweli nay a kudumu, Mungu ametupa njia iliyo bora zaidi ni sadaka moja tu ya Mwanadamu aliyemwaga damu yake Msalabani ilitolewa kwa niaba yatu na hiyo tu ndiyominayokubaliwa na Mungu kwaajili ya mafanikio yote ya kimwili na kiroho kwa wanadamu wote ulimwenguni na sio vinginevyo:-

Isaya 53:4-6 “Hakika ameyachukua masikitiko yetu, Amejitwika huzuni zetu; Lakini tulimdhania ya kuwa amepigwa, Amepigwa na Mungu, na kuteswa. Bali alijeruhiwa kwa makosa yetu, Alichubuliwa kwa maovu yetu; Adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake, Na kwa kupigwa kwake sisi tumepona. Sisi sote kama kondoo tumepotea; Kila mmoja wetu amegeukia njia yake mwenyewe; Na Bwana ameweka juu yake Maovu yetu sisi sote.”

2Wakorintho 8:7-9 “Lakini kama mlivyo na wingi wa mambo yote; imani, na usemi, na elimu, na bidii yote, na upendo wenu kwetu sisi; basi vivyo hivyo mpate wingi wa neema hii pia. Sineni ili kuwaamuru, bali kwa bidii ya watu wengine nijaribu unyofu wa upendo wenu. Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwa ajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.”  
           

Jamii inapaswa kuelimisha watu na kukemea swala hilo vikali, Watu wenye ulemavu huu wa ngozi wamekuwa wakinyanyasika kwa sababu ya misimamo inayochangiwa na wagaganga wa kienyeji wenye madai kuwa uchawi unaohusisha viungo vya Albino una nguvu sana Imani hii potofu imechangia kwa kiasi kikubwa mauaji ya watu hao, n ahata kuchimbwa kwa makaburi yao na kukatwa viungo vyao, dhana hii inajitokeza zaidi katika mikoa ya Shinyanga na Mwanza, aidha watu wenye ualbino wananyanyasika wakati mwingine wakifikiriwa kuwa ni watu wasiotakiwa katika familia au jamii Ndugu zangu ni lazima tubadilike, utafiti mdogo unaonyesha kuwa Tanzania huenda labda ndio inchi inayoongoza kwa kuwa na albino wengi duniani, Hata hivyo wakati mwingine pia albino wametekwa na kusafirishwa mpaka katika inchi jirani, au kuuawa na wahusika kukimbilia katika inchi za jirani, ni aibu kwa Taifa lenye kuehsimika kama Tanzania kuwa na sifa ya mambo ya kijinga hivi, injili ihubiriwe na dini na imani za kweli zikifishwe katika maeneo yote ambayo yanazingirwa na imani hizi potofu. Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!      

Jumapili, 23 Juni 2024

Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria.


Yohana 4:1-10 “Kwa hiyo Bwana, alipofahamu ya kuwa Mafarisayo wamesikia ya kwamba, Yesu anafanya wanafunzi wengi kuliko Yohana, na kuwabatiza, (lakini Yesu mwenyewe hakubatiza, bali wanafunzi wake,) aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya.  Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria. Basi akafika kunako mji wa Samaria, uitwao Sikari, karibu na lile shamba ambalo Yakobo alimpa Yusufu mwanawe. Na hapo palikuwa na kisima cha Yakobo. Basi Yesu, kwa sababu amechoka kwa safari yake, akaketi vivi hivi kisimani. Nayo ilikuwa yapata saa sita. Akaja mwanamke Msamaria kuteka maji. Yesu akamwambia, Nipe maji ninywe. Kwa maana wanafunzi wake wamekwenda mjini kununua chakula. Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai.”



Utangulizi:

Leo tutachukua muda kujifunza mojawapo ya masomo ya Msingi sana katika Maisha na mafundisho ya Bwana wetu Yesu Kristo ili kujifunza jambo moja la msingi sana tunapofanya kazi ya kuieneza injili, na jambo hili lina uhusiano na kuvunja mipaka ya kijamii, kiimani, kidini, kisiasa, kiitikadi, kiadui na rangi, na kuhakikisha kuwa tunasambaza upendo wa Mungu kwa watu wote sawasawa na agizo kuu la Bwana wetu la kuihubiri injili na kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wake na kuwabatiza.

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”

Katika kujifunza somo hili muhimu lenye kichwa, Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria, ambalo kimsingi litazungumzia mazingira mazima ya mazungumzo ya Yesu na mwanamke Msamaria katika Yohana 4:1-42 pamoja na matokeo ya mazungumzo hayo kwa ujumla, tutaligawa somo hili katika vipengele vitatu muhimu:-

 

·         Uhusiano wa Wayahudi na Wasamaria.

·         Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria.

·         Matokeo ya kupita kwa Yesu pale Samaria

 

 

Uhusiano wa Wayahudi na Wasamaria.

Ni muhimu kuwa na ufahamu, kwamba moja ya safari Muhimu sana ambayo ina maswala mengi sana ya kutufunza ni pamoja na safari hii ya Yesu Kristo kupita katika jimbo la Samaria, Kimsingi katika wakati huu Yesu alikuwa amejipatia umaarufu mkubwa sana kuliko Yohana Mbatizaji, Na mafarisayo walianza kuchukizwa na Yesu kwa sababu walianza kupoteza umaarufu wao na mamlaka yao,  na hivyo hawakuwa na furaha sana na uwepo wa Yesu, kwa hivyo Yesu alilazimika kuondoka kwaajili ya kuepusha migogoro na mafarisayo ambao kimsingi walishaanza kutafuta namna na njama za kutaka kumuangamiza,kabla ya muda wake halisi wa kusulubiwa.

Yohana 4:1-3 “Kwa hiyo Bwana, alipofahamu ya kuwa Mafarisayo wamesikia ya kwamba, Yesu anafanya wanafunzi wengi kuliko Yohana, na kuwabatiza, (lakini Yesu mwenyewe hakubatiza, bali wanafunzi wake,) aliacha Uyahudi, akaenda zake tena mpaka Galilaya.”

Yesu alikuwa amekwishakuwa maarufu pande zote Uyahudi na Galilaya na jamii kubwa ya watu walikuwa wakimfuata kila aliko, kwa hiyo ili kupata nafasi ya kupumua aliazimia kupita Samaria (Alikuwa hana budi maana yake  ilikuwa lazima) Biblia ya kiingereza inatumia maneno “And he must needs go through Samaria”  neno Must needs katika kiyunani linatumika neno DEI  au DEON kwa kiingereza Necessary yaani ilikuwa ni muhimu, ilikuwa ni lazima, ilikuwa kuna jambo la msingi la kukutana nalo, kwa sababu maalumu, ikiwa ni pamoja na kupunguza kwa kiwango fulani mkakati wa mafarisayo kumuwinda na kutaka kumwangamiza, lakini kulikuwa na uhitaji wa kiungu.

Marko 3:6-10 “Mara wakatoka wale Mafarisayo, wakawa wakifanya shauri juu yake pamoja na Maherodi, jinsi ya kumwangamiza. Naye Yesu akajitenga, yeye na wanafunzi wake, akaenda baharini. Mkutano mkuu ukamfuata, kutoka Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu, na Idumaya, na ng'ambo ya Yordani, na pande za Tiro na Sidoni, mkutano mkuu, waliposikia habari za mambo yote aliyokuwa akiyatenda, wakamwendea. Akawaambia wanafunzi wake ya kwamba chombo kidogo kikae karibu naye, kwa sababu ya mkutano, wasije wakamsonga. Maana aliponya wengi, hata wote waliokuwa na misiba wakamrukia wapate kumgusa.”

Kwaajili ya hayo Yesu anakusudia kupita katikati ya Samaria, Samaria lilikuwa mojawapo ya jimbo kati ya majimbo makubwa matatu katika taifa la Israel, kusini kulikuwa na jimbo la Uyahudi (Yudea) na Kaskazini kulikuwa na jimbo la Galilaya, na katikati lilikuwepo jimbo la Samaria, kwa kawaida wayahudi halisi waliishi Yudea na Galilaya na wale wenye kuishika Imani sana walipotaka kwenda Galilaya au kuja Uyahudi hawakuthubutu kupita katikati ya Samaria kwani kufanya hivyo ilikuwa ni sawa na kujitia unajisi, na sababu kubwa ni kuwa kulikuwa na uhasama wa kihistoria kati ya Wayahudi na Wasamaria, hivyo Wayahudi walipokuwa wakienda Galilaya walilazimika kupita njia ndeefu kuzunguka nje ya Samaria kuliko kupita kati kati yake yaani Samaria ambayo kimsingi ilikuwa ndio njia fupi.

Wayahudi na Wasamaria walichukiana sana na hawakuwa hata na muda wa kuzungumza wao kwa wao, Sababu kubwa ni kuwa Wasamaria walikuwa ni Wayahudi hapo zamani, Lakini Israel ya kaskazini ilipovamiwa na Waashuru na watu wengi kuchukuliwa utumwani mwaka wa 722 KK.  Mfalme wa Ashuru aliwaleta wageni wengi sana kuikalia nchi ya Samaria, na wageni hawa walizaliana na waisrael waliobaki na hivyo kukazaliwa machotara wa kiyahudi na wageni na kwa sababu hiyo jamii hii ilianza kuabudu miungu na kujihusisha na tabia za mataifa wasio wayahudi.

2Wafalme 17:23-33 “hata Bwana akawaondoa Waisraeli wasiwe mbele zake, kama vile alivyosema kwa kinywa cha watumishi wake wote, manabii. Basi Waisraeli walichukuliwa mateka kutoka nchi yao wenyewe, waende nchi ya Ashuru, hata leo. Naye mfalme wa Ashuru akaleta watu kutoka Babeli, na Kutha, na Ava, na Hamathi, na Sefarvaimu, akawaweka katika miji ya Samaria badala ya wana wa Israeli; wakaumiliki Samaria, wakakaa katika miji yake. Basi ikawa, wakati ule walipoanza kukaa huko, hawakumcha Bwana; kwa hiyo Bwana akapeleka simba kati yao, nao wakawaua baadhi yao. Kwa hiyo wakamwambia mfalme wa Ashuru, wakasema, Wale wa mataifa uliowahamisha, na kuwaweka katika miji ya Samaria, hawaijui kawaida ya Mungu wa nchi; kwa hiyo amepeleka simba kati yao, na tazama, wanawaua, kwa sababu hawaijui kawaida ya Mungu wa nchi. Ndipo mfalme wa Ashuru akatoa amri, akasema, Mpelekeni mmojawapo wa makuhani, mliowachukua kutoka huko; aende akakae huko, akawafundishe kawaida ya Mungu wa nchi. Basi mmoja wa makuhani waliochukuliwa kutoka Samaria akaenda akakaa katika Betheli, akawafundisha jinsi ilivyowapasa kumcha Bwana. Lakini pamoja na hayo watu wa kila taifa wakajifanyia miungu yao wenyewe, wakaiweka katika nyumba za mahali pa juu, walipopafanya Wasamaria, kila taifa katika miji yao walimokaa. Watu wa Babeli wakafanya Sukoth-benothi kuwa mungu wao, watu wa Kutha wakafanya Nergali, watu wa Hamathi wakafanya Ashima, Waavi wakafanya Nibhazi na Tartaki; nao Wasefarvi wakawaunguza wana wao katika moto kwa Adrameleki na Anameleki, miungu ya Sefarvaimu. Basi hivyo wakamcha Bwana, nao wakijifanyia wengine wao kuwa makuhani wa mahali pa juu, ambao waliwafanyia dhabihu katika nyumba za mahali pa juu. Wakamcha Bwana, na kuitumikia miungu yao wenyewe, sawasawa na kawaida za mataifa ambao wao walihamishwa kutoka kwao.”

Kitendo cha wasamaria hawa kumwacha bwana na kuanza kutumikia miungu mingine kilijenga chuki kubwa sana kati ya wayahudi na wasamaria, lakini hata hivyo mpaka wakati wa Yesu baadhi walikuwa wanamwabudu Mungu wa kweli, lakini hata hivyo waliabudu katika mlima Gerizimu na ambapo pia palijengwa hekalu hapo, lakini wayahudi walilibomoa kabisa na hivyo kuongeza uhasama mkubwa baina yao, kwa hiyo uadui  wao ukawa mkubwa, Wayahudi waliwadharau sana Wasamaria, waliwaona kama watu waliopoteza utakatifu wao kwa kujichanganya na mataifa mengine, ambao walikuwa washirikina na wachawi na kamwe hawakuwahi wayahudi kufikiri kuwa Wasamaria wako sahihi, Mlima Gerizimu ni moja kati ya milima miwili iliyoko nchini Israel katika mji uitwao Nablus leo, lakini zamani paliitwa Shekemu, Neno Gerizim ni neno la kiarabu kumaanisha Jabal kwa kiibrania ni Argarizem  na mlima mwingine uliitwa Ebal.  Na wasamaria wengi waliishi chini ya mlima Gerizim, mlima huo ulifikiriwa kuwa mtakatifu.

Yohana 4:20 -23 “Baba zetu waliabudu katika mlima huu, nanyi husema ya kwamba huko Yerusalemu ni mahali patupasapo kuabudia. Yesu akamwambia, Mama, unisadiki, saa inakuja ambayo hamtamwabudu Baba katika mlima huu, wala kule Yerusalemu. Ninyi mnaabudu msichokijua; sisi tunaabudu tukijuacho; kwa kuwa wokovu watoka kwa Wayahudi.Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu.”

Uhasama baina ya wayahudi na wasamaria ukageuka kuwa uhasama wa kiimani, uhasama wa kiitikadi, uhasama wa ki ubaguzi, uhasama wa kisiasa na hata kijiografia,  Wasamaria waliamini vitabu vitano tu vya Musa na hawakutaka kuamini katika vitabu vingine hivyo walimtambua Musa tu na yule aliyetabiriwa na Musa tu yaani Masihi na yeye ndiye waliyekuwa wakimsubiria.

Kumbukumbu 18:15 “Bwana, Mungu wako, atakuondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zako kama nilivyo mimi; msikilizeni yeye.”          

Uhasama wao ulipelekea kuchukiana kiasi ambacho hata kijiografia ilikuwa ni ngumu sana kwa myahudi wa kawaida kupita katikati ya Samaria akielekea Galilaya na badala yake walilazimika kupita njia ndefu ya kuzunguka yaani kuizunguka Samaria badala ya kupita katikati ya Samaria, sasa basi kwa mara ya Kwanza baada ya miaka mingi sana ndio tunamuona sasa Yesu akilazimika kupita Samaria kwa sababu maalumu za kimkakati katika kuwahudumia watu

Naye alikuwa hana budi kupita katikati ya Samaria.

Yesu Kristo akiwa na moyo wa tofauti kabisa na wayahudi wengine Yeye aliona iko haja ya kupita katikati ya Samaria, sio tu kwa sababu, Mafarisayo walikuwa na mpango wa kumwangamiza, bali pia ziko sababu nyingi sana na mambo mengi sana ya kujifunza kutokana na ziara hii ya kijasiri ya Yesu Kristo! Ambayo ilikuwa ziara ya kimkakati katika kuifikisha huduma ya injili kwa watu waliokataliwa lakini pia kwaajili ya kutufunza maswala kadhaa muhimu sana

1.       Injili ni kwa watu wote – Yesu alikuwa amekuja ulimwenguni kwaajili ya watu wote na sio kwaajili ya Wayahudi peke yao, Kupita Samaria na kuzungumza na yule Mwanamke na hata matokeo yake kunadhihirisha wazi kuwa injili yake na habari njema zinamuhusu kila mmoja duniani, watu wenye ukomavu kiroho, na kisiasa, wanashinda kabisa mipaka ya kibaguzi na kuvuka mipaka ya kawaida ya kibinadamu  na kumuiita kila mmoja kushiriki neema ya Mungu bila kujali, itikadi, historia, ukoo, rangi, uchotara, siasa yake na kadhalika na zaidi ya yote kuufikia ulimwengu mzima hata kwa wale tunaofikiria kuwa ni maadui zetu.

 

Tito 2:11-13 “Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa; nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa; tukilitazamia tumaini lenye baraka na mafunuo ya utukufu wa Kristo Yesu, Mungu mkuu na Mwokozi wetu;”

 

Yohana 3:16 -17 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.”             

 

Kila mtu anayedai ya kuwa anamfuata Yesu hana budi kuhakikisha ya kuwa anawafikia watu wote bila ubaguzi, hubiri kila mahali, kuna watu wanadhani iko jamii ya watu Fulani tu ndio wanaohitaji injili Yesu aliivunja mipaka hiyo na anatufundisha kivitendo ya kuwa ni lazima injili imfikie kila mtu, awe Mwafrika, awe Mzungu, awe Muasia, awe Mwarabu, awe muislamu, awe mbudha, awe mhindu, awe Singasinga, awe Mjapani (Shintoism), awe Mchina (Taoism na Comfucianism) na kadhalika ni wajibu wetu kuhakikisha injili inapenya na kufika kila mahali hata kwa watu ambao tuna historia nao mbaya,  wanaotuchukia, hawatupendi, hawatukubali,  ni lazima tutafute njia ya kuwafikia kwa upendo. Ziara ya hii  ya Bwana iliweka Msingi kwa wanafunzi wa Yesu ambao baadaye walishuka Samaria  na kuhihubiri injili na Samaria ikaipokea injili na watu  wakatubu na wakajazwa Roho Mtakatifu na kukawa na uamsho mkubwa sana

 

2.       Kuleta Maridhiano – Pamoja na mafundisho kadhaa wa kadhaa Yesu kwa kupita kwake Samaria kama kiongozi mkubwa sana Duniani na mbinguni anatufundisha umuhimu wa Maridhiano, Yeye kwa kuonyesha mfano anaonyesha na kufunua ukweli mpya wa kiroho ya kuwa kupitia injili watu wake wanaweza kuonyesha upendo, yeye akiwa Myahudi wa mfano anaonyesha ya kuwa sio kuwa karanga moja ikioza ndio zote, anaonyesha ya kuwa Sasa yeye kama Myahudi halisi na wa kweli anavunja mipaka ya kibaguzi,  na kustawisha uhusiano na kuvunja ubinafsi na ubaguzi uliokuwepo kati ya Wayahudi na Wasamaria. Kila Mkristo aliyekomaa kiroho na mwenye ujuzi wa juu sana anaweza kuwa njia na daraja la kuwapatanisha watu kwa Mungu, hata bila ya kusubiri adui akunyenyekee, ni sisi ndio ambao tunaweza kuchukua hatua za kuvunja kuta za uadui na kuwafikia wengine, Kama Yesu asingelichukua hatua uadui kati ya wasamaria na wayahudi ungedumu, Lakini aliye na afya nzuri ya kiroho ndiye aliyekuwa wa kwanza kuuvunja uadui huo na jambo hili lilimshangaza mwanamke msamaria kwa sababu alijua sio kawaida Myahudi kuchukua hatua ngumu kama hii, na alijiuliza inakuwaje? Je wewe unasubiri adui yako ndio achukue hatua? Aje akunyenyekee na kukuomba? Yesu alikuwa wa kwanza kuchukua hatua na ikawashangaza sana wasamaria

 

Yoahana 4:9-10 “Basi yule mwanamke Msamaria akamwambia, Imekuwaje wewe Myahudi kutaka maji kwangu, nami ni mwanamke Msamaria? (Maana Wayahudi hawachangamani na Wasamaria.) Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai.”

 

Mungu anataka tuwashangaze wakati wote wale wanaojifikiria kuwa ni maadui zetu kwa kuwatendea mema, linapokuja swala la injili hakuna adui, hakuna mtu asiyestahili kufikiwa na upendo wa Mungu kwa sababu zozote zile, Kanisa ni lazima lijipange kuhakikisha kuwa injili inawafikia watu wote hata wale ambao tunadhani kuwa hawastahili, Wayahudi walikuwa ndio watu wa kwanza kuteuliwa na Mungu ili waweze kuwa Baraka kwa ulimwengu mzima, ingekuwa ni hasara kubwa sana kama wayahudi wangesahau wajibu wa kuvunja mipaka na kupeleka Baraka hizo kwa mataifa mengine, Na ashukuriwe Mungu kwamba Yesu kiongozi mkuu wa wokovu wetu anakuwa wa kwanza kuonyesha mfano huo kwa kuvunja mipaka ya kiadui, kibaguzi, kikabila, kidini, kitamaduni na kijimbo kwa kuifikisha injili kila mahali wakiwemo Wasmaria.

 

3.        Kufunua Mpango wa Mungu – Katika mpango wa Mungu kulikuwa na umuhimu sana wa ziara ya Yesu kule Samaria, nawe utakubaliana nami kuwa kulikuwa na mpango mahususi wa kiungu kwa Yesu kukutana na mwanamke huyu mjadala wao unatupa mafunzo makubwa sana kuanzia na mafundisho ya kweli na mpaka namna ya kuabudu na mafundisho sahihi ambayo yangeifaa sana jamii ya leo, Mazungumzo ya Kristo na mwanamke Msamaria yanatufunulia kweli kadhaa za muhimu katika Imani yetu kama tunavyoweza kuona

 

a.       Mungu ni Roho – Katika mazungumzo ya Yesu na Mwanamke Msamaria kuna mafundisho mengi ya msingi na moja ya Fundisho hilo ni kuwa Mungu ni Roho, Wayahudi waliamini kuwa sehemu sahihi ya kuabudu ni Yerusalem, na Wasamaria waliamini ya kuwa Mungu anapatikana katika Mlima Gerizimu, Lakini Yesu anaonyesha kuwa wakati sahihi unakuja ambapo watu watamuabudu Mungu sio kule Yerusalem wala kule Gerizimu, Lazima ufikie wakati watu wajue ya kuwa Mungu hapatikani katika mahekalu yaliyojengwa kwa mikono, wala hapatikani milimani, Mungu ni ROHO, mkao wako wa kiroho bila kujali uko wapi utamfanya Mungu akutembelee sawa na kiu uliyo nayo moyoni mwako, huitaji leo kwenda mahali Fulani kumtafuta Mungu kwani Mungu anapatikana kila mahali popote ulipo endapo tu utafungua moyo wako, Mungu yuko mahali kote na anapatikana kwa kila mtu amtafutaye kwa Moyo

 

Matendo 7:48-50 “Ila Yeye aliye juu hakai katika nyumba zilizofanywa kwa mikono, kama vile asemavyo nabii, Mbingu ni kiti changu cha enzi, Na nchi ni pa kuwekea miguu yangu; Ni nyumba gani mtakayonijengea? Asema Bwana, Au ni mahali gani nitakapostarehe? Si mkono wangu uliofanya haya yote?

 

Matendo 17:24-27 “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana wa mbingu na nchi, hakai katika hekalu zilizojengwa kwa mikono; wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kana kwamba anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na pumzi na vitu vyote. Naye alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja, wakae juu ya uso wa nchi yote, akiisha kuwawekea nyakati alizoziamuru tangu zamani, na mipaka ya makazi yao; ili wamtafute Mungu, ingawa ni kwa kupapasa-papasa, wakamwone, ijapokuwa hawi mbali na kila mmoja wetu.”

 

Ibada ya kweli haitegemei mahali, inategemea mkao wa Moyo wako, Mungu hawi mbali na yeyote anayemtafuta kwa dhati, uende milimani usiende, Yesu alitufundisha kupitia mwanamke huyu na kutupa kuelewa namna na jinsi inavyopaswa kumuabudu Mungu, Sio kwa sababu Ibrahimu na Isaka na Yakobo waliabudu katika mlima huo, basi na Mungu angepatikana katika mlima huo, Mungu ni Roho maana yake Mungu hapatikani katika namna ya asili kama wanadamu ambao wao wanafungwa na mipaka ya kijiografia, Mungu hana mwili kama huu wa kibinadamu, Yeye kwa kuwa ni roho hana mipaka na hivyo huwezi kumfungia Mungu katika mahali Fulani maalumu, kwani yeye yuko mahali pote na anapatikana kila mahali, kwa hiyo kupitia roho yako, na kujitoa kwako kwa moyo  unaweza kumpata Mungu  zaidi ya yote Msaada wa Roho Mtakatifu ndani yetu, yeye anayeweza kuiinua dhamiri yetu na kutuvuvia kumtafuta kwa msaada wake tunaweza kujiungamanisha na Mungu popote tulipo, ikiwa tu tunakuwa na dhamira ya kweli ya kumtafuta sawasawa na neno lake na kupitia Yesu ambaye ndiye ufunuo wa kweli, na zaidi ya yote ndani ya mwili wetu ambao ni hekalu la Roho Mtakatifu, Mungu anaweza kuwasiliana nasi na tunaweza kumuabudu yeye popote tulipo tukiamua tu kuwa katika roho na kumsikiliza kiibada

 

Yohana 14:6 “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” Yohana 17:17 “Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli.”

 

1Wakorintho 6:19-20 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe; maana mlinunuliwa kwa thamani. Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.”

 

b.      Maji ya Uzima – Mazungumzo ya Kristo na mwanamke huyu yalianzia kisimani, na yalianza kwa Yesu kuomba maji, Yesu aliomba maji ya kawaida, Na mwanamke huyu alisita kutokana na ubaguzi uliokuwepo, na mshangao na ndipo Yesu akajibu, akamwambia, Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, Nipe maji ninywe, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai.  Maji yaliyo hai kwa kimasai Engare Embuani, Katika lugha ya kiebrania linatumika neno “Mayim Chayim” yaani Mayim maana yake maji na Chayim maana yake uzima au uhai,  Hii ilikuwa na maana ya maji yasiyo na chumvi wala magadi, Maji masafi yanayotiririka  maji ya aina hiyo yaliaminiwa kuwa yalikuwa ni maji bora na safi na salama  na anayeweza kuwapa watu maji ya aina hiyo ilisadikiwa kuwa chanzo chake ni Mungu tu na ndio maana mwanamke Msamaria alimshangaa Yesu kuwa huenda ni mkuu kuliko Ibrahimu na Isaka na Yakobo waliowaachia kisima kile.

 

Yeremia 2:13 “Kwa maana watu wangu hawa wametenda maovu mawili; wameniacha mimi, niliye chemchemi ya maji ya uzima, wamejichimbia mabirika, mabirika yavujayo, yasiyoweza kuweka maji.”

 

Kwa hiyo Maji ya uzima yalikuwa yanawakilisha Mungu mwenyewe ambaye ndiye chanzo cha uhai na uzima wa wanadamu wote, Ni Mungu pekee ndiye anayeitwa kisima cha maji yaliyo hai au chemichemi ya maji ya uzima, Kwa hiyo kimsingi Yesu alikuwa anajitambulisha kuwa yeye ndiye chemichemi hiyo mya maji ya uzima. Na unapomuacha Mungu maana yake umeenda mbali na kisima cha maji yaliyo hai.

 

Yeremia 17:13 “Ee Bwana, tumaini la Israeli, wote wakuachao watatahayarika. Wao watakaojitenga nami wataandikwa katika mchanga, kwa sababu wamemwacha Bwana, kisima cha maji yaliyo hai.”

 

Katika lugha ya kiyunani (Greek) neno linalotumika kuelezea maji ya uzima ni “Hydor zōn” “Hydor” likiwa na maana ya maji na zōn ikiwa na maana ya Uzima Kwa hiyo Yesu alipozungumzia  maji yaliyo hai au maji ya uzima alikuwa anazungumzia kile chanzo cha uzima wa milele, Yesu alikuwa anamaanisha jambo kubwa sana zaidi ya kiu ya kawaida ya maji ya kimwili, Yesu alikuwa akizungumzia utoshelevu kwa kiu ya wale wanaomtafuta Mungu unatoka kwake na yeye ndiye chanzo hicho yeye ndiye anayetoa utoshelevu huo, kama mtu anahitaji utoshelevu wa kweli wa kiibada na kiimani basi Yesu ndiye halisi.

 

Yohana 4:13-14 “Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele.”

 

Kwa hiyo hapa Yesu anatumia mfano wa maji kuzungumzia kitu Fulani au chanzo Fulani ambacho ndio chanzo halisi cha maisha ya kiroho na uzima wa milele. Na ule uzima wa milele unaitwa ZOE kwa kiyunani ambalo kwa kiingereza ni God-Kind of life maisha ya umilele kama Mungu au maisha ya milele yanayotokana na kuungwa na Mungu. Ni dhahiri kuwa mwanamke yule ingawa alikuwa mwenye dhambi, lakini ndani yake alikuwa na kiu ya kutaka kumjua Mungu, na kiu ya kumuabudu Mungu, hakuwa kichwa tupu tu, alikuwa anajua pia kuwa masihi angekuja na angeweza kuleta majibu ya namna na jinsi iwapasavyo kuabudu, kiu yake ilikuwa imejibiwa kwa kuwa yeye aliyekuwa akisema naye alikuwa ndiye Masihi mwenyewe, na ndiye chanzo cha uzima na maji ya uzima, Kwa hiyo unaweza kuona kuwa ufunuo huu tusingeliupata kama Yesu asingelipita Samaria. Sio hivyo tu wale watu tunaoweza kuwaweka katika kundi la wat wasiofaa na tukawahukumu kama makahaba, au Malaya usije ukafikiri ya kuwa kichwani mwao hakuna kitu kabisa, au usije ukawahukumu na kufikiri kuwa hawastahili habari njema kila mwanadamu duniani bila kujali shetani amemuharibu kwa kiwango gani ndani yake iko kiu ya kumuhitaji Mungu na ni wajibu wetu kama wanafunzi wa Yesu kuyafikia makundi yote bila dharau kama za kifarisayo, na kuwapelekea injili hii ya uzima bila ubaguzi, wala kuwahukumu paleka habari njema kwao

 

c.       Nenda kamuite mumeo - Kuna kitu cha Ziada cha kujifunza tena na tena katika mazungumzo ya Yesu na Mwanamke Msamaria, Yesu alikuwa anayajua maisha ya Mwanamke huyu mwanzo mwisho,  na alikuwa anajua mahitaji yake ya kiroho, mwanamke huyu alikuwa anaishi maisha ya zinaa/alikuwa anaishi katika dhambi, Lakini alikuwa anajua maswala kadhaa ya kiroho, na ndio maana Yesu Hakumdharau hata kidogo alikuwa anataka kumsaidia na kuwasaidia na wengine katika siku za leo, Somo kuhusu maji ya uzima lilikuwa bado halijaeleweka kwa mwanamke huyu na alikusudia kubadilisha mada, Yesu akiwa anaelewa anachokifanya alimueleza nenda kamuite mumeo!

 

Mwanamke huyu hakutaka kuzungumza kuhusu mumewe wa sasa wala aliyekuweko nyumbani kwa hiyo alidanganya kuwa hana mume! Ni Kama aliyekuwa anasema shiishi na mume, Lakini pamoja na kuwa mwanamke huyu alikuwa akijaribu kumdanganya Yesu, ni ukweli ulio wazi kuwa jibu lake lilikuwa ni kweli, kwanini? Mwanamke huyu alikuwa anaishi na mwanaume ambaye hakuwa mume wake kihalali, na kwa mujibu wa sheria za Kiyahudi kama mwanamke mume wake wa kwanza bado yuko hai, na mwanamke huyu akaishi na mwanaume mwingine maana yake mwanamke huyu anaishi katika uzinzi

 

Marko 10:11-12 “Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini.”

 

Warumi 7:2-3 “Kwa maana mwanamke aliye na mume amefungwa na sheria kwa yule mume wakati anapokuwa yu hai; bali akifa yule mume, amefunguliwa ile sheria ya mume. Basi wakati awapo hai mumewe, kama akiwa na mume mwingine huitwa mzinzi. Ila mumewe akifa, amekuwa huru, hafungwi na sheria hiyo, hata yeye si mzinzi, ajapoolewa na mume mwingine.”        

 

Hatuwezi kumdanganya Mungu kwa sababu zozote zile kwa sababu Mungu anajua kila kitu, Yesu alikuwa anamjua mwanamke huyu na asingeliweza kujificha, katika nyakati zetu leo, Ndoa za kikristo zinachukuliwa poa sana, wako watu wanafanya zinaa, zile za kuibia, lakini ziko zinaa zimepitishwa kiofisi, wako watu wamefungishwa ndoa kwenye makanisa ya kiroho, na wengine ni watu wanaoheshimika sana katika imani, watumishi wa Mungu na kadhalika leo wanaweza kusema kuwa ninawahukumu, mimi simuhukumu yeyote yule lakini Neno la Mungu linasimama leo na kutukumbusha wajibu wetu ya kuwa mwanaume na mwanamke wakristo kama uko kwenye ndoa nyingine na mumeo au mkeo bado yuko hai wewe una kesi ya kujibu kimaandiko  na kwa sababu hiyo, unapaswa kurudi kwa mkeo au mume au ukae hivyo hivyo bila kuoa au kuolewa kama yalivyo mfundisho ya Bwana ona, yeye Bwana amekataa kuwa hakuna sababu za mtu aliye katika Kristo kumuacha mkewe, Mungu haamini ya kuwa iko sababu inayoweza kupelekea wewe kama mwamini ukaacha ndoa yako halisi, au mkeo au mumeo halisi na ukapuuza lile agano na kuishi kinyumba, kama tu vile unavyoamini kuwa hakuna dhambi Mungu hawezi kusamehe, Basi Mungu naye anaamini hakuna dhambi inayoweza kusababisha wewe uachane na ndoa.

 

Mathayo 19:3-9 “Basi Mafarisayo wakamwendea, wakamjaribu, wakimwambia, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe kwa kila sababu? Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke, akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja? Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe. Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha? Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini.”

 

Safari ya Yesu katika mji wa Samaria pia ilijaa fundisho hili na inatukumbusha kuhakikisha ya kuwa tunaishi katika ndoa kwa usafi na mwenendo sawasawa na imani yetu katika Kristo na sio vinginevyo. Mungu ni Mungu wa utaratibu, inamshangaza Yesu Leo kuona watu wakiachana na wakati huo huo wakitaka kuoa tena au kuolewa tena ili hali wenzi wao wako hai, Katika eneo hili ni muhimu kujitafakari.

 

d.      Mavuno – Safari ya Bwana Yesu iliyo mlazimu kupita Samaria pia ilikuwa na faida kubwa kwa ufalme wa Mungu yaani kumvunia Bwana nasfi na roho za watu wengi sana, na hivyo kuzungumza na yule mwanamke ilikuwa ni chanzo tu cha kubadilisha moyo wake ili kisha aweze kuwaleta wasamaria wengi kwa Bwana

 

Yohana 4:27-38 “Mara hiyo wakaja wanafunzi wake, wakastaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke; lakini hakuna aliyesema, Unatafuta nini? Au, Mbona unasema naye? Basi yule mwanamke akauacha mtungi wake, akaenda zake mjini, akawaambia watu, Njoni, mtazame mtu aliyeniambia mambo yote niliyoyatenda. Je! Haimkini huyu kuwa ndiye Kristo? Basi wakatoka mjini, wakamwendea.  Huko nyuma wanafunzi wakamsihi wakisema, Rabi, ule. Akawaambia, Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi. Basi wanafunzi wake wakasemezana, Je! Mtu amemletea chakula? Yesu akawaambia, Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka, nikaimalize kazi yake. Hamsemi ninyi, Bado miezi minne, ndipo yaja mavuno? Tazama, mimi nawaambieni, Inueni macho yenu myatazame mashamba, ya kuwa yamekwisha kuwa meupe, tayari kwa mavuno.”

 

Yesu alikuwa na akili sana alifanya kazi ndogo kwa hekima iliyomletea matokeo makubwa sana, alimfundisha neno la Mungu mwanamke mmoja tu, lakini kupitia huyo alijikuta anazungumza na mji mzima, alikuwa akiwaza mavuno, na kwa kuvunja ukuta wa kiitikadi, kuvunja ukuta wa kiimani na kitamaduni na ubaguzi alifanikiwa kuwapata wengi nao wakamwamini hili lilikuwa ni jicho la Mavuno, Kristo anatukumbusha hapa kufanya kazi ya Mungu kwa akili sana na kuhakikisha ya kuwa tunamletea mavuno na katika kulitekeleza hili hatuna budi kufuata njia ya Mungu na kuacha kuwadharau watu, kwa sababu zozote zile, tuwaendee watu wa kila kabila na kila mila na tamaduni na kumzaliwa Bwana matunda, kwa kumletea mavuno hakuna mtu mbaya duniani ambaye hawezi kubadilishwa na neema  

 

Yohana 4:39-43 “Na katika mji ule Wasamaria wengi walimwamini kwa sababu ya neno la yule mwanamke, aliyeshuhudia kwamba, Aliniambia mambo yote niliyoyatenda. Basi wale Wasamaria walipomwendea, walimsihi akae kwao; naye akakaa huko siku mbili. Watu wengi zaidi wakaamini kwa sababu ya neno lake. Wakamwambia yule mwanamke, Sasa tunaamini, wala si kwa sababu ya maneno yako tu; maana sisi tumesikia wenyewe, tena twajua ya kuwa hakika huyu ndiye Mwokozi wa ulimwengu. Na baada ya siku mbili hizo akaondoka huko, akaenda Galilaya.”

       

Matokeo ya kupita kwa Yesu pale Samaria

Kupita kwa Bwana Yesu katika Samaria kulikuwa na ulazima sana kwa sababu ya mafunuo makubwa na ya muhimu ambayo tunayapata kupitia safari yake, Na zaidi ya yote kuokolewa kwa nafsi za watu wengi sana na kuhudumiwa kwa huruma za Mungu, Mungu ametufundisha maswala mengi sana na ya muhimu kupitia safari hii yenye mafanikio makubwa sana watu wa Samaria wengi zaidi walimuamini Yesu. Kanisa ni lazima tukumbuke Upendo wa Mungu na neema yake haina mipaka, tunaweza kuwafikia wengi bila kujali jamii zao, tamaduni zao, historia zao, ama tofauti zetu, Yesu alitufundisha namna ya kuvunja mipaka hiyo na kuwafikishia watu huduma inayowastahili

Wagalatia 3:28 “Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu

Matendo 10:34-35 “Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.”

Hitimisho

Nimuhimu kukumbuka kuwa injili ni kwa ulimwengu wote na kwa watu wote na kabila zote, Bwana anatufundisha kuhakikisha ya kuwa tunavunja vihunzi vyote  vya kijamii, kiutamaduni, kikabila, na kiimani au kidini na hata kidhehebu, na kuhakikisha ya kuwa tunahubiri upendo kivitendo, umoja na neema na msamaha wa Mungu kwa watu wote,  na kuwa inatupasa kuuiga mfano wake ili kuwafikia watu wote kwa upendo na huruma bila kujali tofauti zetu, Bwana ampe neema kila mmoja wetu kuvuka mipaka na vihunzi vya kibaguzi vinavyotufanya tusiwafikie watu au kuifikia jamii fulani kwa sababu zozote zile katika jina la Yesu ameen!, Aidha nakukumbusha kuwa Yesu aliongea na mwanamke huyu Kisimani yaani mahali ambapo hapawezi kuwa na maswala na wakati wowote mtu anaweza kuja, Yesu hakuongea na mwanamke huyu mafichoni, nalieleza hili mapema, mtu asione kuwa unaweza kuzungumza na mtu wa jinsi tofauti popote tu hapana, ili kujiepusha na kasfa na kusingiziwa kaa na ongea na mtu wa jinsi tofauti mahali pasipo na utata. Mungu akubariki sana kwa kufuatilia somo hili na kama umebarikiwa kumbuka kuwasiliana nami, uongezewe neema na Mungu akutunze!

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima