Jumatano, 4 Juni 2025

Kwa hiyo hatulegei!

 

2Wakorintho 4:15-17 “Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe. Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana




Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika dunia hii iliyojaa changamoto, maumivu, majaribu, mateso, uonevu, dhuluma, kukosekana kwa haki, wivu, majungu na kuumizana, maneno ya kuumiza, na vita vya kila aina ni rahisi sana kwa baadhi ya watu hususani wale walio na moyo wa unyonge kulegea na kukata tamaa, na wakati huohuo kupoteza tumaini kwa sababu ya kuwako kwa vikwazo mbalimbali katika maisha, Paulo mtume yeye anasema na kutangaza kwa ujasiri “Kwa hiyo Hatulegei” ujumbe wake Paulo mtume kwa kanisa ni ujumbe wa matumaini na ushindi na nguvu kwa kila anayemwamini Yesu Kristo Bwana wetu, kwamba sisi ni watu wa tofauti na kamwe hakuna awaye yote aliyemwamini Yesu anayeweza kukata tamaa, au kuzimia moyo “Kwa hiyo hatulegei” tunaendelea kukaza mwendo kwa kadiri tunavyokutana na changamoto na majaribu ya namna mbalimbali.

Wafilipi 3:12-14. “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele; nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu.”

Leo basi tutachukua muda kujifunza sababu zilizopelekea Paulo mtume kuelezea “Kwa hiyo Hatulegei” na tutajifunza ujumbe huu kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo yafuatayo:-

·         Maana ya kutokulegea.

·         Sababu za kutokulegea.

·         Kwa hiyo hatulegei.

Maana ya kutokulegea:

2Wakorintho 4:15-17 “Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe. Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku. Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana

Neno kwa hiyo hatulegei katika Biblia ya kiyunani linasomeka “dio ekkakeō ou”  kwa hiyo neno hatulegei kwa kiyunani ni “ekkakeō”  ambalo kwa kiingereza linaweza kutafasirika to become weak, to fail, to faint, to become weary, or to fail in heart, or we do not give up. kwa hiyo kwa Kiswahili maana yake hatuwi dhaifu, hatushindwi, hatuzimii, hatuchoki, hatukati tamaa, hatuvunjiki moyo.

Maana yake hata pamoja na magumu kiasi gani tunayokutana nayo, hata pamoja na dhiki kubwa tunayokutana nayo, hata pamoja na changamoto kubwa tunazokutana nazo, hata pamoja na vipingamizi vikubwa tunavyokutana navyo iwe ni katika imani, iwe ni katika huduma, iwe ni ugumu katika jambo lolote unalokutana nalo, vyovyote vile visisitishe huduma yako, wokovu wako, ndoa yako biashara yako, juhudi zako katika masomo, uwezo wako wa kumtumainia na kumtegemea Mungu, utumishi wako, juhudi yako ya kupambana na umasikini, jitihada zako za kujikwamua, mpango wako wa biashara, mpango wako wa kilimo, mpango wako wa uwekezaji, mpango wako wa ufugaji, mpango wako wa maendeleo, na msimamo wako katika Bwana haupaswi kuzimia kwa sababu zozote zile kwa sababu ya ujuzi wako na maarifa yako ya kina kuhusu Mungu na kazi yake anayoifanya ndani yako! Kamwe Mungu hawezi kukuangusha! Kwa hiyo hatulegei

Hakuna jambo baya sana kama kuzimia, kukata tamaa, kuvunjika moyo, kuchoka, au kuwa dhaifu, adui mkubwa sana wa mwanaridha yoyote yule ni pamoja na kuzimia, au kulegea, kuvunjika moyo, kuogopa, wasiwasi na mashaka, na kufikiri kuwa umezidiwa, wakati wowote mwanadamu anapokata tamaa anazuia maendeleo yake, anatengeneza ugumu wa kushinda vikwazo na kutokusonga mbele mtu awaye yote aliyeokoka hapaswi kamwe kulegea, kulegea na kukata tamaa na kuzimia moyo kunaashiria kuwa uweza wako na nguvu zako ni chache, Jeshi lolote lile halina haja na Askari ambaye anazimia moyo au kukata tamaa.  Mithali 24:10 “Ukizimia siku ya taabu, Nguvu zako ni chache.”

Kulegea kunafananishwa na mwanamke aliyebeba mimba kwa miezi tisa akipitia shida na taabu mbalimbali kisha akaanza kusikia uchungu alafu muda wa kujifungua unafika wakati anataka kujifungua mwanamke huyu anachoka kusaidia kumsukuma mtoto ili atoke huo unakuwa wakati mgumu sana, unakuwa ni wakati wa dhiki, unakuwa ni wakati wa aibu, kuwa mwanamke huyu amebeba mimba lakini ameshindwa kuzaa, mwanamke huyu atashutumiwa kuwa alipoteza ujasiri na nguvu wakati wa kujifungua, kwa hiyo ni lazima Mwanamke asukume zaidi ili aweze kujifungua kama hakuna nguvu ya kuweza kujifungua maana yake hakuna nguvu ya kushinda kwa hiyo kushindwa kunakuja, aibu inakuja, fedheha inakuja, na jambo gumu zaidi linakabili:-

Isaya 37:1-3. “Ikawa mfalme Hezekia aliposikia hayo, alizirarua nguo zake, akajivika nguo za magunia, akaingia katika nyumba ya Bwana. Akamtuma Eliakimu aliyekuwa msimamizi wa nyumba yake na Shebna, mwandishi, na wazee wa makuhani, wamejivika nguo za magunia, waende kwa Isaya nabii, mwana wa Amozi. Wakamwambia, Hezekia asema hivi, Siku hii ni siku ya dhiki, na aibu, na matukano; maana watoto wa tayari kuzaliwa, wala hapana nguvu za kuwazaa.”

Kwa hiyo kulegea maana yake ni kuzimia, ni kukaribia kushindwa ni kukosa msaada, ni kuchoka, ni kupoteza nguvu ni uwezekano mdogo wa kushinda vikwazo na changamoto mbalimbali zinazokukabili, kwa hiyo watu wa Mungu au watu waliookoka hawalegei, hatukati tamaa, hatuvunjiki moyo, wala hatusitishi juhudi wakati wa mambo magumu tunasonga mbele kama askari wema na waaminifu walioko vitani na ziko sababu kadhaa za kutufanya tusilegee!

Sababu za kutokulegea.

1.       Kwa sababu tunaongezewa neema – Mst 15

 

2Wakorintho 4:15 “Kwa maana mambo yote ni kwa ajili yenu, ili neema hiyo ikiongezwa sana, kwa hao walio wengi shukrani izidishwe, na Mungu atukuzwe.”

 

Mtu wa Mungu anapopita katika changamoto za aina mbalimbali kwa kadiri ya  mateso na majaribu yanavyozidi Mungu aliyemfufua Bwana Yesu anatuongezea neema ya kupita kawaida ya kutusaidia kushinda majaribu, kwa hiyo ndani yetu moyo wa kukata tamaa unabomolewa na Neema inazidi na kutuinua juu zaidi, tunapewa neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.

 

Yakobo 4:5-6 “Au mwadhani ya kwamba maandiko yasema bure? Huyo Roho akaaye ndani yetu hututamani kiasi cha kuona wivu? Lakini hutujalia sisi neema iliyozidi; kwa hiyo husema, Mungu huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.”

 

Waebrania 4:16 “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

 

2Wakorintho 12:8-10 “Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke. Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu. Kwa hiyo napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.”

 

2.       Kwa sababu mtu wa ndani hachakai        Mst 16

 

2Wakorintho 4:16 “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku.”

 

Paulo mtume anasema hatulegei wala hatuishiwi nguvu wala kukata tamaa kwa sababu utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku, wakati kila mkristo anapokutana na majaribu na mateso na machungu ya aina mbalimbali utu wetu wa ndani unapata uzoefu na mabadiliko na ukuaji wa kiroho, kwa hiyo hata kama kwa nje tunaonekana kuchoka, kuugua na kuchakaa utu wetu wa ndani unafanywa upya na kuimarishwa katika imani kupitia uhusiano wetu na Mungu, Imani, maombi, neno la Mungu na uzoefu wa kiroho tunaoupata kila iitwapo leo, wakati wa majaribu unachangia kwamba akili zetu zinakuwa, ujuzi wetu unaongezeka, tunazidi kumjifunza Mungu kutoka katika pito moja kuelekea katika pito lingine  na kama ni hivyo sasa kukatatamaa kunatokea wapi, kuchoka kunatokea wapi, kupoteza nguvu kunatokea wapi, unafungwa gerezani, magereza inaachia, unapigwa mawe mpaka kufa unafufuliwa na unaendelea na injili, unapigwa bakora na kuteseka unazidi kuongezewa neema, unaviziwa getini unashushwa kwenye kikapu na injili inaendelea, utachokaje kwa mfano  unapata ujuzi unapata hekima unajengewa ujasiri na unagundua kuwa hakuna kitu kinaweza kukutenga na wewe na upendo wa Mungu

 

Warumi 8: 38-39 “Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

 

3.        Kwa sababu mateso ya sasa ni mepesi na ya muda tu. Mst 17

 

2Wakorintho 4:17 “Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana;”      

 

Paulo mtume anayaona mateso ya sasa na dhiki hizi ni nyepesi na za muda tu na kuwa dhiki hizi zinatutengenezea utukufu mkubwa sana na wa milele, watu waliookoka ni askari, askari ili awe na utukufu mkubwa na cheo kikubwa sana lazima akasotee katika chuo cha maafisa wa kijeshi ili kuongezewa nyota begani mwake, wakati wote dhiki huwa zinatujaribu na kutukomaza kupata ujuzi wa kiroho na kutufanya tuwe imara zaidi kwa sababu hiyo hatulegei tunapata uzoefu kutoka kwa dubu na simba ili kumpiga Goliathi.

 

Ayubu 23:10-12 “Lakini yeye aijua njia niendeayo; Akisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu. Mguu wangu umeshikamana sana na hatua zake; Njia yake nimeishika, wala sikukengeuka. Sikurudi nyuma kuiacha amri ya midomo yake; Nimeyatunza maneno ya kinywa chake zaidi ya riziki yangu,”

 

1Petro 1: 6-7 “Mnafurahi sana wakati huo, ijapokuwa sasa kwa kitambo kidogo, ikiwa ni lazima, mmehuzunishwa kwa majaribu ya namna mbalimbali; ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo.”

 

Paulo mtume alikuwa anaangalia hitimisho kubwa lenye utukufu mwingi baada ya dhiki hizi za muda mfupi, Kule mbinguni Mungu atamtukuza kila mmoja kwa kadiri ya neema na mapito aliyoyavumilia kwa sababu hiyo hatupaswi kuangalia hivi vinavyoonekana ambavyo ni vya muda mfupi bali tuviangalie vile vya milele, mateso na dhiki na maumivu ni vitu vinavyoonekana lakini thawabu na utukufu mkuu Mungu aliotuwekea ni kitu kisichoonekana kwa sasa lakini katika uzima wa milele kuna mambo makubwa yanakuja mbele yetu.

 

2Wakorintho 4:18 “tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”

 

4.       Kwa sababu huduma hii tumeipata kwa rehema Mst 1

 

2Wakorintho 4:1 “Kwa sababu hiyo, kwa kuwa tuna huduma hii, kwa jinsi tulivyopata rehema, hatulegei;”

 

Mungu aliyetuita katika wokovu na kisha kutupa wito wa kumtumikia ametuheshimu sana ni rehema kwa wewe na mimi kufanywa watumishi wa Mungu, angeweza kumtumia mwingine au hata kuwatumia malaika ambao ni wajumbe wake, lakini kwa rehema kubwa ametupa sisi huduma hii  tunawezaje kulegea? Tunawezaje kukata tamaa, Mungu ametukabidhi sisi kazi ya kuieneza injili ametupenda ametuhurumia ametuheshimisha tupeleke ujumbe wa Mwanae kwa watu wote, huduma hii ni ya rehema tu si kwa saababu tunastahili kwa hiyo kwa vipi tukate tamaa, kwa vipi tuzimie, kwanini tulegee?  Kama ni Mungu ameturehemu tumtumikie ni yeye mwenyewe ndiye atakayekuwa chanzo cha nguvu zetu , kwa sababu hiyo ni lazima tushinde vizuizi vyote na changamoto zote na kamwe tusizimie moyo, kazi yetu ni kazi njema na ni kazi ya Mungu kwa hiyo tusizimie, Yeye aliyetutuma ana mamlaka yote Mbinguni na duniani kwa sababu hiyo hatupaswi kamwe kuogopa!

 

Wagalatia 6:9-10 “Tena tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.”

 

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”         

 

Kwa hiyo hatulegei.

Ni muhimu maneno haya yakawa kauli mbiu katika utumishi wetu na maisha yetu ya wokovu, kila wakati unapohisi kuchoka au kuvunjwa moyo ni lazima tukiri kuwa Hatulegei, hatuzimii moyo hatuanguki, tunasonga mbele, kutokulegea kwetu ni ishara ya kuwa tunamjua Mungu kwa kina na mapana na marefu, na tunamwamini, Paulo alipokuwa anasema kuwa hatulegei yeye alikuwa anajua hakunamtu aliyepitia mateso kama yeye lakini hakuwahi kulegea hata siku moja.

2Wakorintho 11:23-33 “Wao ni wahudumu wa Kristo? (Nanena kiwazimu), mimi ni zaidi; katika taabu kuzidi sana; katika vifungo kuzidi sana; katika mapigo kupita kiasi; katika mauti mara nyingi. Kwa Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi; kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; katika kusafiri mara nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang'anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi. Baghairi ya mambo ya nje, yako yanijiayo kila siku, ndiyo maangalizi ya makanisa yote. Ni nani aliye dhaifu, nisiwe dhaifu nami? Ni nani aliyekwazwa nami nisichukiwe?  Ikinibidi kujisifu, nitajisifia mambo ya udhaifu wangu. Mungu, Baba wa Bwana Yesu, aliye mtukufu hata milele, anajua ya kuwa sisemi uongo. Huko Dameski liwali wa mfalme Areta alikuwa akiulinda mji wa Wadameski, ili kunikamata; nami nikatelemshwa ndani ya kapu, katika dirisha la ukutani, nikaokoka katika mikono yake.”

Mungu hatatuacha katika mapito ya aina yoyote ile aliahidi kuwa atakuwa pamoja nasi na kwa sababu hiyo atatutia nguvu kwa hiyo hata kama tunazingirwa na mazingira magumu kiasi gani hatutaangamia, wala hatutakata tamaa, kila jaribu linao mlango wa kutokea.

2Wakorintho 4:6-10 “Kwa kuwa Mungu, aliyesema, Nuru itang'aa toka gizani, ndiye aliyeng'aa mioyoni mwetu, atupe nuru ya elimu ya utukufu wa Mungu katika uso wa Yesu Kristo. Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu, wala si kutoka kwetu. Pande zote twadhikika, bali hatusongwi; twaona shaka, bali hatukati tamaa; twaudhiwa, bali hatuachwi; twatupwa chini, bali hatuangamizwi; siku zote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu, ili uzima wa Yesu nao udhihirishwe katika miili yetu.”

Kwa hiyo Hatulegei.

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumatano, 28 Mei 2025

Mleteni huku kwangu!


Mathayo 17:14-21 “Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, akampigia magoti, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]




Utangulizi:

Katika kifungu chetu cha msingi wa maandiko leo, tunakutana na kisa chenye kushangaza sana ambapo wanafunzi wa Yesu walishindwa kumsaidia kijana aliyekuwa anateswa na pepo wa kifafa, Baba wa kijana alileta mashitaka hayo kwa Yesu kwamba kijana wake amekuwa akisumbuliwa na pepo hao wa kifafa ambao wakati mwingine wamemtupa kijana wake katika maji na katika moto, na alipomleta kwa wanafunzi wake wao walishindwa kumtoa, Ndipo Yesu kwa uchungu mkubwa alitoa agizo lenye uzito “Mleteni huku Kwangu” agizo hili sio agizo la kawaida ni mamlaka ya kiroho yenye maana pana kwa kila mtu anayetafuta msaada wa kweli.

Mleteni Kwangu!

Ni muhimu kufahamu kuwa ni swala la kawaida kwamba kila mwanadamu anapopatwa na shida au changamoto zozote zile zikiwepo changamoto za kiafya huwa anatafuta msaada, na wakati mwingine wanadamu huwa na tabia ya kupeana taarifa wapi pa kwenda ili changamoto zako ziweze kutatuliwa, Baba wa kijana huyu anaonekana wazi kukosa Amani kwaajili ya afya ya mtoto wake ambaye alikuwa anasumbuliwa na Pepo wa kifafa, na huenda alihangaika sehemu nyingi sana kwaajili ya kujaribu kutatua hali ya kiafya iliyokuwa ikimkabili kijana wake, hatimaye huenda alisikia habari za Yesu, lakini wakati huu Yesu alikuwa mlimani pamoja na Petro na Yakobo na Yohana wanafunzi wengine walibaki, Mzee huyu aliwakabidhi wanafunzi wa Yesu changamoto za mwanae na wanafunzi walishindwa kushughulika nayo, Yesu alipofika baba wa kijana alitoa taarifa kwa Yesu na ndipo Yesu alipotoa amri “Mleteni huku kwangu

Kwanini aletwe kwa Yesu?

Watu wengi sana wanapopatwa na changamoto za namna mbalimbali kwa kawaida huwa hawampi Yesu nafasi ya Kwanza, na badala yake huanza kutumia akili zao za kawaida na za kibinadamu katika kutatua changamoto zinazowakabili na Yesu huwa anapewa nafasi ya mwisho, hii sio tu kwa wanadamu wa siku za leo, bali hata wakati Bwana Yesu alipokuwa duniani bado wako watu waliokuwa na changamoto mbalimbali walianza kupeleka changamoto zao kwa matabibu mbalimbali na kuingia gharama kubwa

Marko 5:25-29 “Na mwanamke mmoja mwenye kutoka damu muda wa miaka kumi na miwili, na kuteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, amegharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya aliposikia habari za Yesu, alipita katika mkutano kwa nyuma, akaligusa vazi lake;maana alisema, Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona. Mara chemchemi ya damu yake ikakauka, naye akafahamu mwilini mwake kwamba amepona msiba ule

Inawezekana umekuwa ukipitia changamoto za aina mbalimbali kama mwanadamu katika maisha yako ya kawaida, ni desturi na jambo la kawaida sana wanadamu kuomba ushauri kwa wanadamu wenzao na kuelezewa kuwa wajaribu hiki au kile, nenda hospitali hii au ile kamuone mwanasaikolojia huyu au yule, kamuone daktari huyu au yule, nenda kwa mganga huyu au yule, changamoto yako hii yuko mama mmoja huyo ni kiboko, changamoto yako hii inangekuwa kule Sumbawanga ingeshughulikiwa, tatizo lako hili lingekuwa kule Kwamsisi ni jambo dogo tu, changamoto yako hii ingekuwa kule Lamu - Mombasa sharifu angekusomea, hili tatizo lingepelekwa kule Korogwe kwa Semangube lingekuwa kama chai tu, hii kitu kuna wazee kule Kigombe Muheza inaisha na kadhalika na kadhalik wanadamu wanaweza kukupa ushauri wa kupeleka matatizo yako huku na kule na ukasumbuka sana kwaajili ya kutafuta uzima, na ikakugharimu sana, Mzee huyu ambaye alihangaika vile vile kwaajili ya kijana wake alipeleka changamoto yake huku na kule hospitali za kawaida zilishindwa, hospitali za rufaa zilishindwa na sasa akawaona wanafunzi wa Yesu ambao nao vile vile walishindwa!

·         Wanafunzi wa Yesu walishindwa – Bado walikuwa wanajifunza, Yesu alikuwa amewapa amri na mamlaka juu ya pepo, lakini walikosa namna na jinsi ya kuachilia nguvu za Mungu na kuitumia mamlaka hiyo kutoa Pepo, hii ni kwa sababu waliogopa, walishindwa kuamini na pia walikosa maisha ya kufunga na kuomba na hivyo mamlaka yao ilikuwa chini, Yesu aliwajulisha kuwa Pepo wana mamlaka za kijeshi na Pepo wa kifafa (aina hii) wana daraja la juu katika mamlaka za kipepo za kuwatesa wanadamu na kuwa wanaweza kutolewa kwa maisha ya kufunga na kuomba

 

Luka 10:17-19. “Ndipo wale sabini waliporudi kwa furaha, wakisema, Bwana, hata pepo wanatutii kwa jina lako. Akawaambia, Nilimwona Shetani, akianguka kutoka mbinguni kama umeme. Tazama, nimewapa amri ya kukanyaga nyoka na nge, na nguvu zote za yule adui, wala hakuna kitu kitakachowadhuru.”

 

Mathayo 17:17-21 “Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]

 

Maisha duni ya kufunga na kuomba, pamoja na upungufu wa Imani ya wanafunzi wa Yesu ilikuwa ni sababu ya kushindwa kwao kuwaamuru pepo hawa wa kifafa kumuachia kijana na kumuweka huru Yesu aliwajulisha baadae tatizo lililokuwako, kwa hiyo walishindwa kumsaidia, na mzazi aliwashitaki kwa Yesu.

 

·         Wanafunzi wa Yesu walikuwa wanadamu – watu wengi sana wanapokuwa na changamoto za aina mbalimbali katika maisha katika akili zao kichwani kwanza huanza kuwafikiri wanadamu, wanafikiria mtu atakayewapa muunganiko “connection” mtu wa kuwaunganishia, wanaelekeza mawazo yao na kuwategemea wanadamu na kama ilivyo ada Mungu anakuwa chagua la mwisho

 

Yeremia 17:5-8 “Bwana asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni tumaini lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda.”

 

·         Yesu ndiye suluhisho – Ziko shida ambazo madaktari wa kawaida hawawezi kushughulika nazo, ziko changamoto ambazo wanadamu hawawezi, ziko changamoto ambazo huwezi kuzidhibiti kwa mifumo ya kidini na kiserikali wala kwa uzoefu wako na maarifa yako bila kumkaribia Yesu Mwenyewe!

 

Yeye peke yake ndiye mwenye mamlaka yote mbinguni na duniani, hata wenye mamlaka na waliopewa mamlaka wanahitaji kumtegemea Yesu kila wakati, Yesu anapoagiza mleteni huku kwangu alikuwa anatualika wote kwamba changamoto yoyote kubwa au ndogo inayokukabili yeye anaweza kushughulika nayo, yeye ndiye mwenye mamlaka yote, jina lake lina kibali kila mahali, yeye ni mwisho wa matatizo zote, na kuwa kwake hakuna jambo lisilowezekana, hakuna linaloshindikana kwake, kila kitu ambacho kimeshindikana kipelekwe kwa Yesu, peleka watoto walioshindikana, peleka mke aliyeshindikana, peleka mume aliyeshindikana, peleka magonja na shida na changamoto zote zilizoshindikana kwa sababu Yesu sio wa kawaida !

 

Mathayo 28:18 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”

 

Ufunuo 1:8 “Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, asema Bwana Mungu, aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja, Mwenyezi.”

 

Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

 

Hakuna mafanikio ya kweli unayoweza kuyapata nje ya Yesu Kristo, yeye ndiye mwenye mamlaka yote, yeye ndiye mwanzo na mwisho Alfa na Omega, yeye kwa jina lake kila kitu kitapiga goti kiwe cha kuzimu, duniani au mbinguni, kila kitu kimetiishwa chini yake, mapepo yametiishwa chini yake magonjwa yametiishwa chini yake roho wote wachafu, falme mamlaka wakuu wa giza na majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho yametiishwa chini yake, hakuna shida ambayo yeye hawezi kuitatua, maarifa yako yanaweza kushindwa wagaganga wako wanaweza kushindwa, washauri wako wanaweza kukwama, dini yako inaweza kukwama, wanasaikolojia wako wanaweza kushindwa kukukwamua Lakini Yesu anasema na kutoa mwaliko leo Mleteni huku kwangu, Yako mambo katika maisha yako huwezi kuyashughulikia, unahangaika kwa sababu hujawahi kujaribu kwa Yesu, sikiliza mwito wa Mwana wa Mungu yeye anasema Mleteni huku kwangu, ni mke aliyeshindikana kwa ukorofi, mleteni huku kwangu, ni mtoto aliyeshindikana kwa ukorofi mleteni huku kwangu, ni mume aliyetekwa na makahaba mleteni huku kwangu, ni mlevi aliyepindukia kila mtu amemkataa mleteni huku kwangu, ni huduma yako haieleweki, mleteni huku Kwangu, ni magonjwa madakatari wameshindwa mleteni huku kwangu, ni mwenye nyumba mkorofi mleteni huku kwangu, ni bosi mwenye gubu mleteni huku kwangu, ni shida ya aina yoyote imekushika kooni Yesu anatoa mwaliko mleteni huku kwangu  Yesu habadiliki uwezo wake wa kutoa msaada bado uko pale pale yeye ni yeye yule jana leo na hata milele na hakuna jambo lililo gumu la kumshinda yeye.Hebu twende mbele za Bwana na kupeleka mahitaji yetu yote yaliyoshindikana kwake yeye ni mwema atatusaidia.

 

Waebrania 13:8 “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele.” Luka 1:37 “kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.”

 

Fanya uamuzi leo, wa kumkabidhi Yesu lolote linalokusibu na lolote libnalokusumbua katika maisha yako

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumanne, 20 Mei 2025

Yeye peke yake akanyagaye mawimbi ya bahari!


Ayubu 9:8-12 “Ambaye peke yake ni mwenye kuzitandika mbingu, Na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. Yeye afanyaye hizo nyota za Dubu, na Orioni, na hicho Kilimia, Na makundi ya nyota ya kusini.Atendaye mambo makuu yasiyotafutikana; Naam, mambo ya ajabu yasiyohesabika. Tazama, yuaenenda karibu nami, nisimwone; Tena yuapita kwenda mbele, nisimtambue. Tazama, yuakamata, ni nani awezaye kumzuia? Ni nani awezaye kumwuliza, Wafanya nini?



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa muujiza wa Bwana Yesu kutembea juu ya mawimbi ya bahari ya Galilaya haukuwa muujiza wa kawaida kama wengi tunavyodhani, muujiza huu wa aina yake kati ya miujiza mingi aliyoifanya Bwana Yesu huu umerokodiwa na injili tatu zisizo fanana kwa kusudi maalumu


Mathayo 14:22-33 “Mara akawalazimisha wanafunzi wake wapande chomboni na kutangulia mbele yake kwenda ng'ambo, wakati yeye alipokuwa akiwaaga mkutano.Naye alipokwisha kuwaaga makutano, alipanda mlimani faraghani, kwenda kuomba. Na kulipokuwa jioni, alikuwako huko peke yake. Na kile chombo kimekwisha kufika katikati ya bahari, kinataabika sana na mawimbi; maana upepo ulikuwa wa mbisho. Hata wakati wa zamu ya nne ya usiku Yesu akawaendea, akienda kwa miguu juu ya bahari. Wanafunzi walipomwona akienda juu ya bahari, wakafadhaika, wakisema, Ni kivuli; wakapiga yowe kwa hofu. Mara Yesu alinena, akawaambia, Jipeni moyo ni mimi; msiogope. Petro akamjibu, akasema, Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako juu ya maji. Akasema, Njoo. Petro akashuka chomboni, akaenda kwa miguu juu ya maji, ili kumwendea Yesu. Lakini alipouona upepo, akaogopa; akaanza kuzama, akapiga yowe, akisema, Bwana, niokoe. Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka? Nao walipopanda chomboni, upepo ulikoma. Nao waliokuwamo ndani ya chombo wakamsujudia, wakisema, Hakika wewe u Mwana wa Mungu.”


Marko 6:45-52 “Mara akawalazimisha wanafunzi wake wapande mashuani, watangulie kwenda ng'ambo hata Bethsaida, wakati yeye alipokuwa akiwaaga mkutano. Hata alipokwisha kuagana nao akaenda zake mlimani kuomba. Na kulipokuwa jioni mashua ilikuwa katikati ya bahari, na yeye yu peke yake katika nchi kavu. Akawaona wakitaabika kwa kuvuta makasia, kwa maana upepo ulikuwa wa mbisho; hata ilipopata kama zamu ya nne ya usiku akawaendea, akitembea juu ya bahari; akataka kuwapita. Nao walipomwona anatembea juu ya bahari, walidhani ya kuwa ni kivuli, wakapiga yowe, kwa kuwa wote walimwona, wakafadhaika. Mara akasema nao, akawaambia, Changamkeni; ni mimi, msiogope. Akapanda mle chomboni walimo; upepo ukakoma; wakashangaa sana mioyoni mwao; kwa maana hawakufahamu habari za ile mikate, lakini mioyo yao ilikuwa mizito.”


Yohana 6:16-21 “Hata ilipokuwa jioni wanafunzi wake wakatelemka baharini wakapanda chomboni, wakaanza kuivuka bahari kwenda Kapernaumu. Nako kumekwisha kuwa giza, wala Yesu hajawafikia. Na bahari ikaanza kuchafuka kwa kuvuma upepo mkuu. Basi wakavuta makasia kadiri ya maili tatu nne, wakamwona Yesu anakwenda juu ya bahari na kukikaribia chombo; wakaogopa.Naye akawaambia, Ni mimi, msiogope. Basi wakataka kumpokea chomboni; na mara hiyo chombo kikaifikilia nchi waliyokuwa wakiiendea.”


Muujiza huu wa Yesu Kutembea juu ya mawimbi ya bahari kimsingi ulikuwa ni muujiza maalumu wa kujifunua kwa wanafunzi wake mamlaka kubwa aliyokuwa nayo Yesu dhidi ya majanga ya asili na uweza wake wa kiungu, na ndio maana muujiza huu haukufanyika mbele ya watu wote isipokuwa wanafunzi wake peke yao kimsingi muujiza huu ulikuwa unamfunua Yesu kwa wanafunzi wake kwamba yeye ana upekee wa aina yake!


1.       Uwezo wake wa kiungu – Wanafunzi wake wote waliorekodi muujiza huu hawakuacha kutaja neno “NI MIMI” Msiogope, Yesu Kristo alitumia mara kadhaa neno NI MIMI au mimi ndimi moja kwa moja akijifunua kwa mamlaka na uweza wa kiungu sawa na mwokozi aliyemtokea Musa tayari kwa wokovu wa wana wa Israel kutoka utumwani kule Misri neno NI MIMI lilitumiwa na Mungu kujitambulisha yeye ni  nani wakati Musa alipopata wasi wasi kuhusu wovovu wa wana wa Israel mbele za Farao.


Kutoka 3:13-15 “Musa akamwambia Mungu, Tazama, nitakapofika kwa wana wa Israeli, na kuwaambia, Mungu wa baba zenu amenituma kwenu; nao wakaniuliza, Jina lake n'nani? Niwaambie nini? Mungu akamwambia Musa, MIMI NIKO AMBAYE NIKO; akasema, Ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli; MIMI NIKO amenituma kwenu. Tena Mungu akamwambia Musa, Waambie wana wa Israeli maneno haya, BWANA, Mungu wa baba zenu, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu; hili ndilo jina langu hata milele, nalo ni kumbukumbu langu hata vizazi vyote.”

 

Kwa kujitambulisha hivyo kwa wanafunzi wake Yesu ni sawa tu na anarudia namna Mungu alivyojitambulisha kwa Musa MIMI NDIMI, NI MIMI “I AM WHO I AM” jina hilo tafasiri yake ndio YHWH au Yahweh ambalo maana yake ni Mungu mwenye kujitosheleza na wa milele ni mwokozi kwa hiyo Yesu aliposema NI MIMI msiogope alikuwa anafunua mamlaka yake kamili ya uungu kwa wanafunzi wake

 

Kuna nguvu kubwa ya kupita kawaida nguvu ya uungu yenye uwezo zaidi ya wanadamu wa kawaida Yesu alipojitambulisha NI MIMI au MIMI NDIMI mwanafunzi wa Yesu Yohana katika injili yake anaonyesha jinsi majeshi ya wakamataji, yaani kikosi kilichotumwa kumkamata Yesu kilivyopata misuko suko mkubwa wakati Yesu alipojitambulisha kwao kwa usemi huo

 

Yohana 18:4-6 “Basi Yesu, hali akijua yote yatakayompata, akatokea, akawaambia, Ni nani mnayemtafuta? Wao wakamjibu, Ni Yesu Mnazareti. Yesu akawaambia, Ni mimi. Yuda naye aliyemsaliti alikuwa amesimama pamoja nao. Basi alipowaambia, Ni mimi, walirudi nyuma, wakaanguka chini.”

 

2.       Uweza wake juu ya maswala ya asili – Kristo Yesu alijifunua kupitia muujiza huu kuwa yeye anazo nguvu juu ya uumbaji na maswala yote ya asili, (Power over nature) kila janga la asili iwe ni matetemeko, iwe ni radi, iwe ni dhuruba, uwe ni upepo au bahari iliyochafuka Yesu ana uweza juu ya majanga ya asili, anauwezo wa kufanya yale yasiyowezekana kibinadamu ama yale yasiyofikirika injili zinaelezea kuwa mara Yesu alipopanda chomboni upepo na dhruruba vilikoma.

 

Mathayo 14:32-33 “Nao walipopanda chomboni, upepo ulikoma. Nao waliokuwamo ndani ya chombo wakamsujudia, wakisema, Hakika wewe u Mwana wa Mungu.”

 

Marko 6:49-51 “Nao walipomwona anatembea juu ya bahari, walidhani ya kuwa ni kivuli, wakapiga yowe, kwa kuwa wote walimwona, wakafadhaika. Mara akasema nao, akawaambia, Changamkeni; ni mimi, msiogope. Akapanda mle chomboni walimo; upepo ukakoma; wakashangaa sana mioyoni mwao;”

 

3.       Kutimiza unabii na kufunua uungu wake – Ayubu aliwahi kutabiri miaka 2,000 kabla ya Yesu kuwa ni Mungu peke yake mwenye kuzitandaza mbingu na kukanyaga mawimbi ya bahari, kwa hiyo kimsingi Yesu Kristo alikuwa anaufanya muujiza huu na maalumu alikuwa akitimiza unabii huu, kitabu cha Ayubu kiliandikwa yapata miaka 1000 kabla ya Yesu  na Yesu aliishi mnamo karne ya kwanza na kwa sababu hiyo kutoka Ayubu mpaka kuzaliwa kwa Yesu Kristo ilikuwa ni zaidi ya miaka 2,000. wanafunzi wa Yesu na watu wengine bila shaka walikuwa wamewahi kuyasoma maneno ya Ayubu na hivyo Kristo alipofanya muujiza huu walishangazwa sana na kujiuliza kuwa huyu ni mtu wa namna gani? Hata Pepo na bahari zamtii?

 

Mathayo 8:26-27 “Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga, enyi wa imani haba? Mara akaondoka, akazikemea pepo na bahari; kukawa shwari kuu. Wale watu wakamaka wakisema, Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?                 

 

Ayubu 9:8-12 “Ambaye peke yake ni mwenye kuzitandika mbingu, Na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. Yeye afanyaye hizo nyota za Dubu, na Orioni, na hicho Kilimia, Na makundi ya nyota ya kusini. Atendaye mambo makuu yasiyotafutikana; Naam, mambo ya ajabu yasiyohesabika. Tazama, yuaenenda karibu nami, nisimwone; Tena yuapita kwenda mbele, nisimtambue.Tazama, yuakamata, ni nani awezaye kumzuia? Ni nani awezaye kumwuliza, Wafanya nini?

 

Andiko hilo linafunua kuwa ni Mungu peke yake azitandaye mbingu na kukanyaga mawimbi ya bahari, kwa hiyo ni Dhahiri na ni wazi kuwa kitendo cha Yesu Kristo kutembea juu ya maji kwa kuyakanyaga mawimbi ya bahari alikuwa akiutimiza unabii huu, kwa hiyo muujiza unatufunulia ya kuwa Yesu hakuwa wa kawaida tu bali alikuwa na mamlaka ya uungu ndani yake, Bahari ilimtii, kanuni za kisayansi zilivunjika na Yesu alitembea juu ya maji, alikemea upepo na bahari na zikamtii.


Mambo ya Msingi ya kujifunza:

Kwanini Kristo anajifunua hivi kwa wanafunzi wake na kwa watu wote leo? Yesu hajifunui hivi kwa faida yake tu kwamba awe na sifa za uungu, Yesu anajifunua hivi kwetu leo ili kwamba wote tupate kumuamini kuwa yeye yuko pamoja nasi katika aina yoyote ya dhuruba, unapomuamini Yesu kwa kumfanya kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yako kumbuka muujiza huu haukuwa wa watu wote huu ulikuwa ni maalumu kwa wanafunzi wake ni muujiza maalumu kwa wale wanaomuamini yeye  kwa hiyo kwanza tunafunuliwa ya kuwa hatuko peke yetu, Wakati wanafunzi walipokuwa wakisumbuliwa na dhuruba na kujifikiri ya kuwa wako peke yao Yesu Kristo aliwatokea na kuingilia kati masumbufu yao, mashaka yao na wasiwasi wao, Leo tunajifunza ya kuwa muumba ulimwengu, mwenye nguvu juu ya majanga yote ya asili yeye ambaye Peke yake anaweza kukanyaga mawimbi ya bahari yuko pamoja nasi na atatutokea na atatuliza dhoruba zote zinazotukabili katika maisha yetu katika namna iliyo nyepesi sana na ya kushangaza, kwa hiyo hatuwezi kuogopa linapotokea janga la aina yoyote yeye ni kimbilio letu na nguvu zetu ona:-

Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”

Tunajifunza kuwa tunapaswa kumwangalia yeye kwa imani bila kuona shaka, Petro alipomtambua Yesu aliyekuwa anatembea juu ya dhuruba na kuomba atembee juu ya dhuruba Bwana alimpa kibali na aliweza, lakini pale alipoona shaka na kuanza kuangalia dhuruba mara alianza kuzama, tunajikumbusha au kukumbushwa kuwa wakati wa changamoto zozote za maisha ni lazima tuendelee kumtazama Yesu, Ni lazima tumwamini na kutambua ya kuwa yeye peke yake anaweza kutusaidia na kuwa tunapoliitia jina lake atatushika mkono

Waebrania 12:2- “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”

Waebrania 10:38-39 “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye.Lakini sisi hatumo miongoni mwao wasitao na kupotea, bali tumo miongoni mwa hao walio na imani ya kutuokoa roho zetu.”

Tunapomtazama Yesu ni muhimu kufahamu kuwa hakuna kuzimia na hakuna kuchoka wala kukata tamaa au kuingia mashaka, tunajifunza uweza mkubwa na mamlaka kubwa ya Yesu Kristo ili kwamba tupate kuamini na tukiisha kumwamini hakuna mtu awaye yote atakayetahayarika, Kama  Bwana wetu Yesu Kristo aliweza kupita sehemu hatarishi na akavuka salama tunajifunza kuwa sisi nasi tukimwangalia yeye tutapita sehemu hatarishi pamoja naye na tutavuka salama, maji na radi na vilindi vya bahari na dhuruba za kila namna vyote vina muogopa Mungu na kwa sababu hiyo hakuna jaribu liltakaloweza kusimama mbele yako lisishughulikiwe kwa jina la Yesu Kristo aliye hai.

Zaburi 77:16-20 “Ee Mungu, yale maji yalikuona, Yale maji yalikuona, yakaogopa. Vilindi vya maji navyo vikatetemeka, Mawingu yakamwaga maji. Mbingu nazo zikatoa sauti, Mishale yako nayo ikatapakaa. Sauti ya radi yako ikawa katika kisulisuli; Umeme uliuangaza ulimwengu. Nchi ilitetemeka na kutikisika; Njia yako ilikuwa katika bahari. Na mapito yako yalikuwa katika maji makuu; Hatua zako hazikujulikana. Uliwaongoza watu wako kama kundi, Kwa mkono wa Musa na Haruni.”

Hitimisho!

Leo nakutangazia kuwa  haijalishi unapitia changamoto ya aina gani, dhuruba ya aina gani, upepo wa aina gani, haijalishi madaktari wamekuambia nini, haijalishi kuwa una rufaa mkononi kwenda hospitali kubwa, haijalishi mapigo yako ya moyo yako juu au chini, haijalishi umevamiwa na virusi vya korona, au ukimwi, haijalishi vipimo vikubwa vimekuja na matokeo magumu kiasi gani, haijalishi una maadui waliojipanga kwa kiwango cha kukutishia, haijalishi unaogopa nini,  haijalishi una madeni ya kausha damu, na mikopo umiza, haijalishi wamekodi mganga gani akuroge, haijalishi kuna vikao gani vya majungu vimekukalia, haijalishi fitina na majungu, na mizengwe unayowekewa nakutangazia ya kuwa yuko yeye akanyagaye mawimbi, kila aina ya wimbi katika maisha yako litakanyagwa na kutulia tuli katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai, usiogope, usione shaka, usitikisike, usisitesite, usitetemeke, usikate tamaa, usilie, usiogope na kuwaza itakuwaje nakutangazia ya kuwa yuko akanyagae mawimbi ya bahari kila wimbi linalopita katika maisha yako Yesu atalikanyaga na litatulia kimya kwake yeye aliyezifanya mbingu na nchi katika jina la Yesu. 

“Kumbuka ni Yeye peke yake akanyagaye mawimbi ya bahari! Wokovu una yeye Mungu wetu!”

Tufani inapovuma

sana moyoni mwangu!

Huona pa kujificha 

Mkononi mwa Mungu.

 

Hunificha, hinificha, Adui hatanipata, Hunificha, hunificha mkononi mwake

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Alhamisi, 15 Mei 2025

Nguvu ya maombi!


Isaya 38:1-6 “Siku hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. Ikawa, neno la Bwana likamjia Isaya, kusema, Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako, asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu.”



Utangulizi:

Mojawapo ya njia ya kutuletea neema kubwa sana kutoka kwa Mungu ni pamoja na njia ya maombi, wote tutakuwa tunafahamu jinsi maombi yalivyo na nguvu kubwa sana, yana nguvu ya kuteremsha rehema na neema kutoka kwa Mungu hata wakati tunapopitia changamoto za aina mbalimbali katika maisha yetu, maombi yana uwezo wa kumfanya mwanamke aliye tasa kuwa na watoto wengi, maombi yana uwezo wa kusababisha adui kupigwa na ushindi kupatikana, maombi  yana uwezo wa kufungua utendaji wa miujiza na kuchochewa kwa karama, maombi yana uwezo wa kubatilisha hukumu ya kifo na kurejesha uhai, maombi yana uwezo wa kugeuza kesi, maombi yanauwezo wa kubatilisha kile Mungu amesema. Maombi yana uwezo wa kufungua magereza za kimwili na kiroho, Mungu ametupa maombi kama njia ya kufanya kazi na yeye na kumruhusu kufanya kazi duniani. Maombi yana nguvu isiyoweza kuelezeka katika changamoto yoyote unayokutana nayo duniani wewe tumia maombi.

Mathayo 7:7-11 “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?

Sisi ndio wenye maamuzi ya mwisho ya kuamua Mungu atafanya nini duniani kwa kutumia maombi, Hapa duniani sio eneo la utawala wa Mungu, ni eneo ambalo Mungu amewapa wanadamu kutawala, yeye utawala wake uko mbinguni, huko mapenzi yake yote hutimizwa kwa ukamilifu, lakini sivyo ilivyo duniani, ili kumpa Mungu kibali cha kufanya mambo duniani ni lazima tuombe, tunapoomba tunamruhusu Mungu kufanya yanayotakiwa yafanyike duniani kama yanavyofanyika mbinguni.

Zaburi 123:1-3 “Nimekuinulia macho yangu, Wewe uketiye mbinguni. Kama vile macho ya watumishi Kwa mkono wa bwana zao Kama macho ya mjakazi Kwa mkono wa bibi yake; Hivyo macho yetu humwelekea Bwana, Mungu wetu, Hata atakapoturehemu.”

Mwanzo 1:26-28 “Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi. Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”

Kupitia maombi tunaweza kumfungulia Mungu njia ya kututendea mambo makubwa na magumu tusiyoyajua, maombi yana uwezo mkubwa sana wa kubadilisha mambo na utendaji wa Mungu kutoka katika maisha ya mtu binafsi mpaka maswala ya kitaifa na ulimwengu kwa ujumla, tunapoomba tunamruhusu Mungu kuinguilia kati na kufanya jambo kwaajili yetu hapa duniani, tunaruhusu utawala wa kimbingu kuleta msaada wa haraka duniani.

-          Maombi yanaweza kumfanya tasa kuwa na watoto - Hana aliyekuwa mwanamke tasa, alipitia machungu na mateso na mashutumu kutoka kwa mke mwenzake, alinyanyasika hata pamoja na kupendwa sana na mumewe, lakini Penina mara kwa mara alimchokoza na kumkumbusha hali yake ya kukosa mtoto jambo ambalo lilimsikitisha sana na kumfanya kutembea kwa huzuni, Hana hata hivyo alifahamu kuwa njia pekee inayoweza kubadilisha hali yake ni maombi, hivyo alimimina maombi yake mbele za Mungu na hatimaye Mungu alisikia na kubadilisha hali yake aliyokuwa nayo, kutoka hali ya utasa kuwa mama wa watoto wengi.

 

1Samuel 1:1-6 “Palikuwa na mtu mmoja wa Rama, Msufi, wa nchi ya milima milima ya Efraimu, jina lake akiitwa Elkana, mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu, mwana wa Sufu, Mwefraimu naye alikuwa na wake wawili; jina lake mmoja akiitwa Hana, na jina lake wa pili aliitwa Penina; naye huyo Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakuwa na watoto. Na mtu huyo alikuwa akikwea kutoka mjini kwake mwaka kwa mwaka, ili kuabudu, na kumtolea Bwana wa majeshi dhabihu katika Shilo. Na wale wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi, makuhani wa Bwana, walikuwako huko. Hata siku ile ilipofika Elkana alipotoa dhabihu, kumpa mkewe Penina sehemu, akawapa na watoto wake wote, waume kwa wake, sehemu zao; lakini Hana humpa sehemu mara mbili; maana alimpenda Hana, ingawa Bwana alikuwa amemfunga tumbo. Ila mwenzake humchokoza sana, hata kumsikitisha, kwa sababu Bwana alikuwa amemfunga tumbo.”

 

1Samuel 1:10-20 “Naye huyo mwanamke alikuwa na uchungu rohoni mwake, akamwomba Bwana akalia sana. Akaweka nadhiri, akasema, Ee Bwana wa majeshi, ikiwa wewe utaliangalia teso la mjakazi wako, na kunikumbuka, wala usinisahau mimi mjakazi wako, na kunipa mimi mjakazi wako mtoto mume, ndipo mimi nitakapompa Bwana huyo mtoto siku zote za maisha yake, wala wembe hautamfikilia kichwani kamwe. Ikawa, hapo alipodumu kuomba mbele za Bwana, Eli akamwangalia kinywa chake. Basi Hana alikuwa akinena moyoni mwake; midomo yake tu ilionekana kama anena, sauti yake isisikiwe; kwa hiyo huyo Eli alimdhania kuwa amelewa. Ndipo Eli akamwambia, Je! Utakuwa mlevi hata lini? Achilia mbali divai yako. Hana akajibu, akasema, Hasha! Bwana wangu, mimi ni mwanamke mwenye roho ya huzuni, mimi sikunywa divai wala kileo, ila nimeimimina roho yangu mbele za Bwana. Usimdhanie mjakazi wako kuwa ni mwanamke asiyefaa kitu; kwa kuwa katika wingi wa kuugua kwangu na kusikitika kwangu ndivyo nilivyonena hata sasa. Ndipo Eli akajibu, akasema, Enenda kwa amani; na Mungu wa Israeli akujalie haja yako uliyomwomba. Naye akasema, Mjakazi wako na aone kibali machoni pako. Basi huyo mwanamke akaenda zake, naye akala chakula, wala uso wake haukukunjamana tena. Wakaondoka asubuhi na mapema, wakasali mbele za Bwana, kisha wakarejea na kufika nyumbani kwao huko Rama; Elkana akamjua mkewe Hana; naye Bwana akamkumbuka. Ikawa, wakati ulipowadia, Hana akachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; akamwita jina lake Samweli, akisema, Kwa kuwa nimemwomba kwa Bwana.”

 

Tunajifunza hapa kuwa maombi yana uwezo wa kubadilisha aibu kuwa heshima, yana uwezo wa kufumba vinywa vya maadui zetu, yana uwezo wa kunyamazisha wanaotubeza, yana uwezo wa kuifanya biashara yako kufanikiwa, mashamba kuzaa, mifugo yako kuongezeka, maisha yako kujawa na mafanikio, Huduma yako kutendeka kwa kiwango na kanisa lako linaloonekana kama tasa likawa kanisa lenye watu wengi, tunaweza kubadilisha hali yoyote inayotukabili iwe ni chungu kuwa furaha, Hana hakukubali kubakia vile alivyo lakini kwa kupitia maombi alibadilisha mwelekeo wa maisha yake na kurejesha heshima yake kama mwanamke kamili kwa njia ya maombi, Maombi yanaweza kubadilisha hatima yako na jina lako.

 

-          Maombi yanaweza kutuletea ushindi vitani - Maandiko yanaonyesha kuwa watu waliookolewa wako vitani, Paulo anasema kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama maana yake hatuna adui wa kimwili sisi, wala hatuwezi kumuhesabu mwanadamu awaye yote kuwa ni adui yetu, lakini adui zetu wako rohoni, ni mamlaka, ni falme ni wakuu wa giza na majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho, hao tunaweza kushughulika nao kwa njia ya kuomba peke yake, maombi yatatupa ushindi dhidi ya nguvu za giza popote.  

 

Waefeso 6:10-18 “Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani. Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama. Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. Tena ipokeeni chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote;”

 

Ushindi wetu hauwezi kupatikana kwa nguvu za mwili na akili za kibinadamu na ujanja ujanja ushindi wetu utapatikana kwa kumualika Mungu katika vita zetu kupitia maombi, wakati Musa alipokuwa jangwani wanaikabili Kanaani njiani waameleki walitokea na wakapigana na Israel neno la Mungu linatuambia kuwa Musa na Haruni na Huri walipanda mlimani  na huko Musa alinyoosha mikono yake kwa Mungu na Yoshua  na Israel walipata ushindi, Musa akishusha mikono Israel wanashindwa, watumishi wa Mungu ili tuweze kuwa na ushindi tusikubali kushusha mikono yetu, tuendelee kumuinulia Mungu mikono yetu na ushindi utakuwa upande wetu kwa Dhahiri hapo tunajifunza nguvu ya maombi, kwamba tunaweza kupata ushindi.

 

Kutoka 17:10-13 “Basi Yoshua akafanya kama Musa alivyomwambia, akapigana na Amaleki; na Musa na Haruni na Huri wakapanda juu ya kile kilima. Ikawa, Musa alipouinua mkono wake, Israeli walishinda; na alipoushusha mkono wake, Amaleki walishinda. Lakini mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa. Yoshua akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga.”

 

-          Maombi yanaongeza nguvu wakati wa upinzani – Nyakati za kanisa la kwanza Mitume walipoanza kuhubiri injili na kufanya miujiza, walikutana na upinzani, walikamatwa, waliwekwa gerezani, waliadhibiwa na walitishwa na walikatazwa wasizungumze lolote kwa jina la Yesu, kanisa lilipopata taarifa walijua ni namna gani wanaweza kuendelea na injili, walijua dawa ni kuomba na walipoomba mahali pale walipokuweko pakatikiswa wakajaa nguvu  za Roho Mtakatifu na kazi ya Mungu ikaendelea na neno la Mungu linaenea.

 

Matendo 4:21-31 “Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka; maana umri wake yule mtu aliyefanyiwa ishara hii ya kuponya ulipita miaka arobaini. Hata walipofunguliwa, wakaenda kwa watu wao, wakawapasha habari ya mambo yote waliyoambiwa na wakuu wa makuhani na wazee. Nao waliposikia, wakampazia Mungu sauti zao kwa moyo mmoja, wakisema, Mola, wewe ndiwe Mungu, ndiwe uliyefanya mbingu na nchi na bahari na vitu vyote vilivyomo; nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili? Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake. Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu Yesu, uliyemtia mafuta, ili wafanye yote ambayo mkono wako na mashauri yako yamekusudia tangu zamani yatokee. Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu. Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri.”

 

-          Maombi yanaweza kubadilisha mpango mbaya wa Serikali na wafalme – Mfalme Herode alikuwa na mpango wa kuwaangamiza viongozi wa kanisa, na alimkamata Yakobo na kumuua na alipoona imewapendeza wayahudi akamkamata na Petro ili naye amuuue vile vile, maandiko yanatueleza kuwa Kanisa lilimuomba Mungu kwa bidii kwaajili ya Petro aliyekuwa amefungwa na Mungu alijibu maombi kwa kumtuma malaika wake aliyemtokea Petro gerezani na kumfungua, hakuna mlango wowote mgumu utakaofungiwa au mnyororo wowote wa adui unaoweza kushindana na nguvu ya maombi, maombi yana nguvu dhidi ya wafalme, Maombi yana nguvu dhidi ya serikali, na yana nguvu dhidi ya magereza yoyote.

 

Matendo 12:5-11 “Basi Petro akalindwa gerezani, nalo kanisa likamwomba Mungu kwa juhudi kwa ajili yake. Hata wakati Herode alipotaka kumtoa, usiku ule ule Petro alikuwa analala katikati ya askari wawili, amefungwa minyororo miwili; walinzi mbele ya mlango wakailinda gereza. Mara malaika wa Bwana akasimama karibu naye, nuru ikamulika mle chumbani, akampiga Petro ubavuni, akamwamsha, akisema, Ondoka upesi. Minyororo yake ikamwanguka mikononi. Malaika akamwambia, Jifunge, kavae viatu vyako. Akafanya hivyo. Kisha akamwambia, Jivike nguo yako, ukanifuate. Akatoka nje, akamfuata; wala hakujua ya kuwa ni kweli yaliyofanywa na malaika; bali alidhani kwamba anaona maono. Na walipopita lindo la kwanza na la pili, wakaja hata mlango wa chuma wa kuingilia mjini, ukawafungukia wenyewe. Wakatoka nje, wakapita katika njia moja; mara malaika akamwacha. Hata Petro alipopata fahamu akasema, Sasa nimejua yakini ya kuwa Bwana amempeleka malaika wake na kunitoa katika mkono wa Herode na katika kutazamia kote kwa taifa la Wayahudi.”

 

-          Maombi yanaweza kufungua milango ya gereza – Paulo na Sila waliokuwa wakiihubiri injili walipata matokeo makubwa sana na watu wengi waliokolewa lakini baada ya kijakazi mmoja kutolewa pepo wa uaguzi bwana zake walikasirika na kuwafanyia ghasia kubwa sana na hivyo mitume waliwekwa gerezani, na kufungwa katika mikatale, tunaelezwa kuwa watu hawa waliimba na kumuomba Mungu usiku wa manane na mara walipofanya hayo tunaelezwa kuwa kila kifungo cha magereza kiliachia sio wao tu na wafungwa wote na matokeo makubwa ni kuwa hata mkuu wa gereza aliokolewa na familia yake yote, tunajifunza kuwa hakuna kifungo chochote kiwe cha kimwili, cha kiroho, cha gereza cha waganga wa kienyeji cha wachawi kinachoweza kusimama mbele ya maombi, hakuna mtu yeyote awe askari awe mfungwa ambaye maombi hayana nguvu za kumgusa, kuna nguvu ya ajabu katika kuomba kwa sababu hiyo kanisa tusipuuzie kuomba kwa kila jambo tuombe, omba kila unapokutana na changamoto yoyote ile omba omba omba!  

 

Matendo 16:25-31 “Lakini panapo usiku wa manane Paulo na Sila walikuwa wakimwomba Mungu na kumwimbia nyimbo za kumsifu, na wafungwa wengine walikuwa wakiwasikiliza. Ghafula pakawa tetemeko kuu la nchi, hata misingi ya gereza ikatikisika, na mara hiyo milango ikafunguka, vifungo vya wote vikalegezwa. Yule mlinzi wa gereza akaamka, naye alipoona ya kuwa milango ya gereza imefunguka, alifuta upanga, akataka kujiua, akidhani ya kuwa wafungwa wamekimbia. Ila Paulo akapaza sauti yake kwa nguvu, akisema, Usijidhuru, kwa maana sisi sote tupo hapa. Akataka taa ziletwe, akarukia ndani, akitetemeka kwa hofu, akawaangukia Paulo na Sila; kisha akawaleta nje akasema, Bwana zangu, yanipasa nifanye nini nipate kuokoka? Wakamwambia, Mwamini Bwana Yesu, nawe utaokoka pamoja na nyumba yako.”

 

-          Maombo yanaweza kubadilisha mpango wa maangamizo – Mungu mwenyewe alikuwa amemtuma Yona kwamba aende Ninawi na kuuonya mji ule na kuutangazia kuwa baada ya siku 40 ataungamiza, watu wa Ninawi na mfalme wao walipoambiwa kuhusu mpango huo walimgeukia Mungu wakafunga na kuomba na kumshawishi Mungu kubadili hukumu na Mungu akaghairi maangamizi aliyokuwa ameyakusudia, maombi ya toba yanaweza kubadilisha hukumu ya Mungu ya kitaifa na ya mtu mmoja mmoja na kusababisha neema na rehema za Mungu ziweze kumwagika kwetu.

 

Yona 3:4 -10 “Yona akaanza kuuingia mji mwendo wa siku moja, akapaza sauti yake, akasema, Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa. Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo. Habari ikamfikia mfalme wa Ninawi, naye akaondoka katika kiti chake cha enzi, akavua vazi lake, akajivika nguo za magunia, na kuketi katika majivu. Naye akapiga mbiu, akatangaza habari katika mji wa Ninawi, kwa amri ya mfalme na wakuu wake; kusema, Mwanadamu asionje kitu, wala mnyama wala makundi ya ng'ombe, wala makundi ya kondoo; wasile, wala wasinywe maji; bali na wafunikwe nguo za magunia, mwanadamu na mnyama pia, nao wakamlilie Mungu kwa nguvu, naam, na wageuke, kila mtu akaache njia yake mbaya, na udhalimu ulio mikononi mwake. Ni nani ajuaye kwamba Mungu hatageuka na kughairi, na kuiacha hasira yake kali, ili msiangamizwe? Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya. Basi Mungu akalighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda; asilitende.”

 

-          Maombi yana uwezo wa kubatilisha tangazo la kifo – Katika kifungu chetu cha msingi cha somo hili tunamuona nabii Isaya akitangaza mauti kwa Mfalme Hezekia, tangazo hilo nabii Isaya alikuwa amepewa na Mungu, lakini Hezekia alilipuuzia tangazo hilo na kugeukia ukutani aliomba kwa bidii na kwa kulia machozi na kumkumbusha Mungu matendo yake ya rehema hata alipokuwa akiomba katikati ya kuomba kwake Mungu alisema na nabii Isaya kwamba amemuongezea Hezekia miaka 15 ya kuishi kwake, kumbe kupitia maombi tunaweza kukata rufaa kwa Mungu kwaajili ya tangazo lolote la hukumu hata kama tangazo hilo au tamko hilo limetoka kwa Bwana mwenyewe! Tunaweza kumsihi Mungu kwa rehema zake na akafanya kwa maombi

 

Isaya 38:1-6 “Siku hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona. Basi Hezekia akajigeuza, akaelekeza uso wake ukutani, akamwomba Bwana, akasema, Ee Bwana, kumbuka haya, nakusihi, kwamba nimekwenda mbele zako katika kweli na kwa moyo mkamilifu, na kutenda yaliyo mema machoni pako. Hezekia akalia sana sana. Ikawa, neno la Bwana likamjia Isaya, kusema, Enenda ukamwambie Hezekia, Bwana, Mungu wa Daudi, baba yako, asema hivi, Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano. Nami nitakuokoa wewe, na mji huu, na mkono wa mfalme wa Ashuru, nami nitaulinda mji huu.”

 

Hitimisho.

 

Tunajifunza hapo kuwa hakuna jambo lolote lililo gumu lisiloweza kubadilishwa kwa maombi, kama watumishi wa Mungu waliotutangulia waliweza kubatilisha maswala kadhaa wa kadhaa katika maisha yao na huduma zao kupitia kuomba sisi nasi leo tunaweza kuliitia jina la Bwana Mungu wetu asiye badilika ambaye ni yeye yule jana leo na hata milele na tukashuhudia matokeo makubwa katika maisha yetu kwa sababu hiyo tusiache kuomba tudumu katika maombi siku zote za maisha yetu

 

Wakolosai 4:2-3 “Dumuni sana katika kuomba, mkikesha katika kuomba huku na shukrani; mkituombea na sisi pia, kwamba Mungu atufungulie mlango kwa lile neno lake, tuinene siri ya Kristo, ambayo kwa ajili yake nimefungwa

 

Karibu na wewe, Mungu wangu, Karibu zaidi Bwana wangu……

 

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Ijumaa, 9 Mei 2025

Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!


Kumbukumbu 33:24-27 “Na Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta. Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba; Na kadiri ya siku zako ndivyo zitakavyokuwa nguvu zako. Hapana aliyefanana na Mungu, Ee Yeshuruni, Ajaye amepanda juu ya mbingu ili akusaidie. Na juu ya mawingu katika utukufu wake. Mungu wa milele ndiye makazi yako, Na mikono ya milele i chini yako. Na mbele yako amemsukumia mbali adui; Akasema, Angamiza.”




Utangulizi:

Moja ya tahadhari inayotolewa kwa wahubiri wa neno la Mungu ni pamoja na kuhakikisha kuwa tunalitumia neno la Mungu kwa halali, Neno la Mungu linatahadharisha kuwa walimu wa neno la Mungu watapata hukumu iliyokubwa zaidi, kwa sababu hiyo ni muhimu kwa kila mtafasiri wa neno la Mungu kulitafasiri kwa halali neno la kweli ili watu wa Mungu wasipotoshwe na kujikuta wakipotezwa kwa kutokuwa na maarifa ya kuifahamu kweli ya neno la Mungu, na kanuni zake za kulitafasiri! Neno la Mungu likitafasiriwa kwa usahihi linaleta mwelekeo sahihi kwa watu wa Mungu. Tafasiri sahihi na njema kwa neno la Mungu huwajengea watu makuzi sahihi ya kiroho, kuikulia Imani sahihi na kujenga uhusiano imara na Mungu na kujiepusha na matumizi mabaya ya maandiko yatakayopelekea kuzuka kwa Imani potofu au Imani za kizushi na kuwafanya wadamu wasitimize kusudi sahihi la Mungu katika maisha yao!

2Timotheo 2:14-15 “Uwakumbushe mambo hayo, ukiwaonya machoni pa Mungu, wasiwe na mashindano ya maneno, ambayo hayana faida, bali huwaharibu wasikiao. Jitahidi kujionyesha kuwa umekubaliwa na Mungu, mtenda kazi asiye na sababu ya kutahayari, ukitumia kwa halali neno la kweli.”         

Yakobo 3:1-2 “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”

Kwa msingi huo basi leo nataka tuchukue muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu tafasiri ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta! Ili kwamba kila mwanafunzi wa Yesu Kristo aweze kuwa na ufahamu wa kutosha  na uliosahihi kuhusu fundisho linaloendelea mitaani ambapo kumekuwako na watumishi wa Mungu wanaowakanyagisha watu mafuta wakifikiri kuwa kwa kufanya hivyo wanaweza kusababisha mabadiliko ya maisha ya watu kiroho, kiuchumi na kimwili jambo ambalo sio sahihi,  na wakristo wengi sana wasomi kwa wasio wasomi lakini wasio na ujuzi kuhusu neno la Mungu wameshawishika kukanyaga mafuta halisi kwa kutumia tafasiri isiyo halisi ya neno la Mungu, tutajifunza somo hili Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta! Kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuafuatayo:-

 

·         Umuhimu wa kuzingatia kanuni za kutafasiri maandiko.

·         Tafasiri halisi ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

·         Jinsi ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

 

Umuhimu wa kuzingatia kanuni za kutafasiri maandiko.

Moja ya changamoto kubwa inayolikumba kanisa la Mungu katika nyakati za leo ni pamoja na kuweko kwa kundi kubwa la mashambulizi ya mafundisho ya uongo ambayo yamekuwa mwiba na usumbufu mkubwa katika kanisa la Mungu kwa miaka mingi, unaweza ukalichukulia swala hili kuwa ni swala la kawaida, lakini ni ukweli usioweza kupingika kuwa Mungu hafurahii watu wanaojitafasiria neno lake kama wapendavyo, Biblia ni kitabu cha Heshima kubwa sana ni neno la Mungu na kwa sababu hiyo haipendezi hata kidogo kila mtu tu akijitafasiria maandiko kama apendavyo kamwe huo sio mpango wa Mungu, Roho Mtakatifu ndiye mwandishi mkuu wa Biblia na bila shaka hangeweza kufurahia watu wajitafasirie neno lake kama watakavyo tu kwa mapenzi yao wenyewe!

2Petro 1:19-21 “Nasi tuna lile neno la unabii lililo imara zaidi, ambalo, mkiliangalia, kama taa ing'aayo mahali penye giza, mwafanya vyema, mpaka kutakapopambazuka, na nyota ya asubuhi kuzuka mioyoni mwenu. Mkijua neno hili kwanza, ya kwamba hakuna unabii katika maandiko upatao kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu. Maana unabii haukuletwa po pote kwa mapenzi ya mwanadamu; bali wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu.”

Mungu anachukizwa sana pale watu wanaposema kile ambacho yeye hajawahi kukisema, nakumbuka niliwahi kuwa na Muhasibu ambaye alikuwa akiandika jina langu katika namna ambayo mimi mwenyewe sikuwahi kuitwa hivyo, Mimi naitwa INNOCENT SAMUEL KAMOTE Lakini muhasibu wangu yeye alikuwa akiandika jina langu INNOCENT SAMWELI KAMMTTE  nililalamika mara kadhaa kuwa Jina langu unavyoliandika sivyo linavyopaswa kuwa lakini hata hivyo hakujali na aliendelea kuliandika jina langu katika namna hiyo hiyo aliyokuwa anataka yeye, mimi sio mwepesi wa hasira lakini hata hivyo nilianza kumtafasiri vibaya muhasibu huyu aliyekazania kuliandika jina langu katika namna anayoitaka yeye hata pamoja na kumuonyesha vitambulisho vyangu vilivyo na jina sahihi,yeye aliendelea kuliandika jina langu katika namna hiyo hiyo aliyoikubali yeye na hakukubali masahihisho, kimsingi nilianza kumchukia na kumuona kama mtu mwenye nia ovu kwa maslahi yangu kwani nafahamu kuwa dosari katika jina la mtu hasa ikiachwa hivyo katika documents muhimu linaweza kuwa na athari kubwa sana baadaye utakapohitajika kuthibitisha uhalisi wa mtu anayetajwa hapo na ukweli kuhusu jina lako, sio hivyo tu nilianza kuingia shaka kuhusu elimu yake na aidha akili zake, kwa hiyo sikuwa namfurahia tena, na alipoteza umuhimu wake kwangu, katika maumivu kama hayo ni ukweli ulio wazi kuwa Mungu anachukizwa sana watu wanapomnukuu vibaya tofauti na maana aliyokuwa anaikusudia kwenye neno lake, Mungu anataka neno lake lisemwe kwa uaminifu na kama mtu hataki aache, Mungu hataki kusingiziwa kwamba amesema kitu ambacho yeye hakukisema, iwe ni kwa misingi ya ndoto wala mafunuo anataka atendewe haki katika tafasiri halali kwa neno lake ili watu wake wasipotoshwe ona  

Yeremia 23:25-32.“Nimesikia waliyoyasema manabii wanaotabiri uongo kwa jina langu, wakisema, Nimeota ndoto; nimeota ndoto. Je! Mambo hayo yatakuwa katika mioyo ya manabii wanaotabiri uongo hata lini, manabii hao wenye udanganyifu katika mioyo yao wenyewe? Wanaodhania ya kuwa watawasahaulisha watu wangu jina langu kwa ndoto zao, wanazomhadithia kila mtu jirani yake, kama vile baba zao walivyolisahau jina langu, kwa ajili ya Baali. Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande? Basi kwa sababu hiyo mimi ni juu ya manabii hao, asema Bwana, wanaompokonya kila mtu jirani yake maneno yangu. Tazama, mimi ni juu ya manabii, asema Bwana, wanaotumia ndimi zao na kusema, Yeye asema, Tazama, mimi ni juu ya hao wanaotabiri ndoto za uongo, asema Bwana, na kuzisema, na kuwakosesha watu wangu kwa uongo wao, na kwa majivuno yao ya upuzi, lakini mimi sikuwatuma, wala sikuwapa amri; wala hawatawafaidia watu hawa hata kidogo, asema Bwana.”

Kwa msingi huo hatuwezi kulichezea neno la Mungu na kuruhusu litafasiriwe vyo vyote vile kama watu wanavyotaka, ziko kanuni zinazoongoza tafasiri halali kwa neno la Mungu, katika karne ya 20 wa NAZI wa Ujerumani waliona kuwa kuna uhalali wa kuwaangamiza wayahudi na kuwaua kwa sababu walitumia andiko la Mathayo 27:24-25 vibaya:-

Mathayo 27:24-25 “Basi Pilato alipoona ya kuwa hafai lo lote, bali ghasia inazidi tu, akatwaa maji, akanawa mikono yake mbele ya mkutano, akasema, Mimi sina hatia katika damu ya mtu huyu mwenye haki; yaangalieni haya ninyi wenyewe. Watu wote wakajibu wakasema, Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu.”

Tafasiri yoyote mbaya ya kimaandiko inaweza kuleta matokeo mabaya yasiyokusudiwa katika jamii wala yasiyo sawa na mapenzi ya Mungu, kama kila mwanadamu anapenda kunukuliwa vizuri basi Mungu anapenda kunukuliwa vizuri zaidi. Katika mtindo kama huo Madaktari wanafahamu athari zinazoweza kutokea endapo mtu atazidishiwa dozi au kupewa dozi chini ya kiwango wakati wa kumtibu mgonjwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha madhara ya usugu wa dawa au kumuumiza mgonjwa, kadhalika neno la Mungu linaagizwa litafasiriwe kwa halali na sio kwa maslahi ya mtu na mafunuo yake au ndoto zake, sio kila mtu ana sifa ya kuwa mtafasiri wa maandiko, na sio kila mtu anaweza kuelewa neno la Mungu bila msaada wa mtu mwingine, na wako watu Mungu amewaweka ili waifanye kazi hiyo ya kuelewesha wengine neno la Mungu ili malengo yake yaweze kufikiwa. Kwa hiyo usipuguze wala kuongeza neno.

Matendo 8:29-35 “Roho akamwambia Filipo, Sogea karibu na gari hili, ukashikamane nalo. Basi Filipo akaenda mbio, akamsikia anasoma chuo cha nabii Isaya; akanena, Je! Yamekuelea haya unayosoma? Akasema, Nitawezaje kuelewa, mtu asiponiongoza? Akamsihi Filipo apande na kuketi pamoja naye. Na fungu la Maandiko alilokuwa akilisoma ni hili, Aliongozwa kwenda machinjoni kama kondoo, Na kama vile mwana-kondoo alivyo kimya mbele yake amkataye manyoya, Vivyo hivyo yeye naye hafunui kinywa chake. Katika kujidhili kwake hukumu yake iliondolewa. Ni nani atakayeeleza kizazi chake? Kwa maana uzima wake umeondolewa katika nchi. Yule towashi akamjibu Filipo, akasema, Nakuomba, nabii huyu; asema maneno haya kwa habari ya nani; ni habari zake mwenyewe au za mtu mwingine? Filipo akafunua kinywa chake, naye, akianza kwa andiko lilo hilo, akamhubiri habari njema za Yesu.”

Kumbukumbu 4:1-2 “Na sasa, Ee Israeli, zisikilizeni amri na hukumu niwafundishazo, ili mzitende; mpate kuishi na kuingia na kuimiliki nchi awapayo Bwana, Mungu wa baba zenu. Msiliongeze neno niwaamurulo wala msilipunguze, mpate kuzishika amri za Bwana, Mungu wenu, niwaamuruzo.”  

Wakati mwingine ili mtu aelewe neno la Mungu anahitaji kuongozwa na wale ambao Mungu ameweka neema maaalumu ya kuwa wakufunzi wa neno la Mungu, kumbuka sisi ni wanafunzi wa Yesu na tunapaswa kujifunza kila iitwapo leo, tukiwa na moyo wa unyenyekevu na kuweka kiburi pembeni Mungu anaweza kutufundisha njia yake kwa usahihi zaidi.

Matendo 18:24-28 “Basi Myahudi mmoja, jina lake Apolo, mzalia wa Iskanderia, mtu wa elimu, akafika Efeso; naye alikuwa hodari katika maandiko. Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; na kwa kuwa roho yake ilikuwa ikimwaka, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu. Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi. Na alipotaka kuvuka bahari aende mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe, naye alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu. Kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo.”

Kwa hiyo wakristo tunakubaliana kuwa mtu anaweza kusoma neno la Mungu na asielewe bila uongozi, na pia mtu anaweza kuwa muhubiri lakini asihubiri kwa usahihi kama hajafundishwa vizuri na tunakubaliana kuwa maandiko yana kanuni zake katika kulitafasiri neno la Mungu ili yamkini liweze kutendewa haki katika tafasiri zake na kutumika kwa halali jambo ambalo linamfurahisha Mungu pia, tusiruhusu kitabu chetu kitakatifu kikatafasiriwa kama apendavyo mtu tu kwa mapenzi yake mwenyewe bali sawa na kanuni za kiungwana na kiungu sawasawa na mapenzi ya Mungu.  Kwa sababu hiyo ziko kanuni rahisi kumi zinazoongoza watu wa Mungu katika kutafasiri maandiko na ingawa hatutakuwa na muda wa kuzifafanua sana kwa undani lakini zinaweza kukupa mwanga wa namna ya kusimamia tafasiri njema na sahihi ya maandiko:-

1.       Lazima mtafasiri wa maandiko awe na Kanuni ya utii (The Principle of Obidience) – hii ni kanuni ya dhamiri njema, mtafasiri wa maandiko lazima ahakikishe kuwa ana moyo wenye dhamiri njema na kuwa mpango wake ni kumtii Mungu,  na kumtumikia kwa dhati, Kila mwanadamu mwenye utii kwa mapenzi ya Mungu na mwenye dhamiri njema Mungu humsaidia muelekeo wake wa moyo kuwa na uweza wa kuifahamu kweli na hata akikosea kwa sababu alikuwa na dhamiri safi rehema za Mungu huwa juu yake, kwa sababu Mungu akiiangalia nia yake anaona kuwa ni mtu mwenye mapenzi mema, Mungu hawezi kuwa radhi na mtu anayekusudia mabaya wakati wanapotaka kulitafasiri neno la Mungu, hata hivyo utii na dhamiri njema havitoshi peke yake vinaweza kutosha kwa Mungu anayechunguza mioyo lakini havitoshi kwetu kwa sababu tutajuaje kuwa ulikuwa na dhamiri njema iwapo fundisho lako limesababisha upotofu miongoni mwa jamii? Kwa hiyo kanuni ya utii inaweza kukuweka salama kwa Mungu tu lakini haikuachi salama kwetu sisi tuliosomea utaalamu wa kutafasiri maandiko haikuweki salama  kwa sababu neno la Mungu linasema Moyo una ugonjwa wa kufisha

 

Yeremia 17:9-10 “Moyo huwa mdanganyifu kuliko vitu vyote, una ugonjwa wa kufisha; nani awezaye kuujua? Mimi, Bwana, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake.”

 

Kwa hiyo wakristo wana haki ya kuyachunguza maandiko ili waone kama kile kinachohubiriwa na kusemwa ni kitu sahihi ama hapana! Hapo haijalishi anayehubiri ni nani na ana mamlaka gani lazima tumpime katika maandiko ili tuone yale anayotupa ndio mapenzi ya Mungu hasa, kinyume cha hapo tutakuwa tumekosa uungwana, watu wa Beroya hawakuwahi kujali kuwa Paulo ana mafunuo gani laiki waliyachunguza maandiko wajionee wenyewe kama mambio ndivyo yalivyo, usiamini katika moyo wa mtu.

 

Matendo 17:10-11 “Mara hao ndugu wakawapeleka Paulo na Sila usiku hata Beroya. Nao walipofika huko wakaingia katika sinagogi la Wayahudi. Watu hawa walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”                                

 

2.       Lazima mtafasiri wa neno la Mungu awe na uelewa kuhusu Kanuni ya uvuvio (The Principle of Inspiration) – hii ni kanuni inayomsaidia kujua kuwa kila andiko lenye pumzi ya Mungu linafaa kwa mafundisho, kwa hiyo tunaweza kuwafundisha watu neno la Mungu kwa njia nyepesi tu na kama tuna mapenzi mema tutawaelekeza watu wake katika mapenzi yake kwa kutumia neno la Mungu  kwa sababu lijna pumzi ya Mungu

 

2Timotheo 3:16-17 “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.”

 

Kanuni hii haitoshi ingawa kuna ukweli kuwa kila andiko lenye pumzi ya Mungu linafaa kwa mafundisho, lakini maandiko yanahitaji ulinganifu wa kina na ndio maana shetani pia alipoona Yesu anatumia maandiko naye akayatumia lakini si kwa nia nzuri kwa hiyo uko ulinganifu maalumu unaohitajika katika kujua andiko fulani linatumikaje na kwa wakati gani

 

Mathayo 4:5-7 “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu,akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako.”

 

3.       Lazima mtafasiri wa Maandiko pia awe na uelewa kuhusu Historia  na mazingira ya andiko (Mukhtadha) (Principle of Historical Context) – hapa mtafasiri anapaswa kujifunza historia ya Mazingira yanayozunguka andiko husika mfano historia ya mji wa Korintho, lugha zao, wakati ambapo neno linaandikwa, tamaduni zao, jamii yao na kadhalika , sio hivyo tu lazima mtafasiri aelewe kitu kilichoandikwa au kusemwa pamoja na maneno yote na maana zake zinazozunguka andiko husika, mazingira yaliyopelekea kutamkwa kwa maneno hayo huo ndio muktadha,  tafasiri hii inakulazima uwe msomi ili uweze kujua lugha za wakati ule, tamaduni za wakati ule, jamii ya wakati ule, na jinsi tunavyoweza kulitumia andiko hilo kwa sasa, lazima uwe na kamusi au ujuzi wa lugha za asili kwaajili ya kupata maana sahihi iliyokusudiwa na mwandishi

 

4.       Lazima mtafasiri aweze pia kufanya uchunguzi wa kimaandiko yaani “ajue yaliyomo” lugha zilizotumika misamiati iliyotumika na maana ya maneno yanayotumika,- (Principle of content) mfano lugha hiyo ni ya namna gani, maneno yake yana maana gani anaweza pia kwenda kwenye lugha za asili kama kiebrania, kiaramu, kiyunani na kilatini ili kupata matumizi ya lugha halisi ya wakati ule na jinsi inavyoweza kutumika katika wakati wa sasa, lazima uchunguze kuwa lugha hiyo ni ya kimafumbo au ya kawaida inaweza kutafasiriwa kama kawaida au inaweza kuwa fumbo? Na madhara gani yanaweza kujitokeza, ni lazima uwe na ujuzi kuhusu kitabu unachotaka kukitafasiri kama ni cha kinabii, kimashairi, kihistoria, sheria, nyaraka, au injili na msemaji alikuwa akizungumza na jamii ya watu wa aina gani, kwa wakati gani, kwa tamaduni gani na inaweza kutuhusu vipi sisi katika nyakati za leo, Lazima uwe na ujuzi kuhusu stori nzima, somo zima, wazo zima, mpangilio mzima, mtiririko mzima na nia nzima ya mwandishi na yote yaliyomo kabla na baada ya andiko husika.    

 

5.       Lazima mtafasiri pia wakati mwingine achukue “lugha rahisi” tu iliyoko kama ilivyo bila kutumia utaalamu kutafasiri japo kwa kufanya hivyo mtafasiri anaweza anaweza kujikuta yuko katika wakati mgumu kwa sababu sio kila lugha iliyotumika inaweza kuwa na maana hizo, ziko lugha za mficho, za kimashairi, za kimafumbo, za kinabii, na kadhalika  (The principle of simplicity) ziko Lugha au maana katika biblia ambazo hazihitaji tafasiri yoyote kwa hiyo ukizichukulia kama zilivyo bila kutafasiri unakuwa salama, huitaji kuyafanya mambo kuwa magumu, lakini yako maandiko ambayo yanahitaji kutokuchukuliwa kirahisi au kama yalivyo mfano:-

 

-          Jicho lako likikukosesha ling’oe – Mathayo 18:8-9 “Basi mkono wako au mguu wako ukikukosesha, ukate ukautupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima hali umepungukiwa na mkono au mguu, kuliko kuwa na mikono miwili au miguu miwili, na kutupwa katika moto wa milele. Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ukalitupe mbali nawe; ni afadhali kuingia katika uzima una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum ya moto.”

 

-          Je unaweza kulichukua andiko hilo hapo juu na kulitafasiri kama lilivyo? Je andiko hilo ni la kawaida au ni la kimafumbo? Sasa ukichukulia kila kitu kama kilivyoandikwa hutaweza kupata tafasiri sahihi ya andiko hilo hali kadhalika   neno na “Na achovye mguu wake katika mafuta”.  Haliwezi kuchukuliwa katika maana yake nyepesi au rahisi kama ilivyo hiyo ilikuwa lugha inayohitaji ufafanuzi, ukiichukulia kama ilivyo wajinga watakanyaga mafuta

 

6.       Lazima mtafasiri pia ajifunze kufanya ulinganifu wa kimaandiko (The Principle of Harmonisation) yaani ili uweze kufanya fundisho kutoka katika andiko basi andiko hilo liwe na mashahidi wawili au watatu, ni lazima ufanye ulinganifu wa fundisho unalotaka kulitengeneza kutoka katika ushahidi wa maandiko mengine (Combination of scriptures references) Biblia imekaa katika mfumo unaotegemeana sana kwa sababu hiyo huwezi kuchomoa uzi mmoja wa nguo kisha ukadai kuwa hii ni nguo, nguo kamili ni mfungamano wa nyuzi nyingi zinazoifanya nguo kuwa nguo kwa hiyo mzani wako wa ulinganifu wa maandiko utakusaidia kuwa na fundisho sahihi  na hupaswi kusingizia kila kitu kuwa kimetokana na ufunuo wa kiungu

 

Isaya 28:9-10 “Atamfundisha nani maarifa? Atamfahamisha nani habari hii? Je! Ni wale walioachishwa maziwa, walioondolewa matitini? Kwa maana ni amri juu ya amri, amri juu ya amri; kanuni juu ya kanuni, kanuni juu ya kanuni; huku kidogo na huku kidogo.”

 

2Wakorintho 13:1 “Hii ndiyo mara ya tatu ya mimi kuja kwenu. Kwa vinywa vya mashahidi wawili au watatu kila neno litathibitishwa.”

Kumbukumbu 19:15 “Shahidi mmoja asimwinukie mtu awaye yote kumshuhudia kwa uovu wo wote, wala kwa dhambi yo yote, katika makosa akosayo yo yote; jambo na lithibitishwe kwa vinywa vya mashahidi wawili, au watatu.”

 

7.       Lazima uwe na utaalamu wa kutosha kuhusu ulinganifu wa maswala ya agano la kale na agano jipya, (The Principles of Covenants) uwe na ufahamu kuwa ni mafundisho gani hasa yaliweza kuwahusu watu wa agano la kale na kwa wakati gani na  wale wa agano jipya, sheria zipi zilifaa kwa wakati ule na zipi hazifai kwa wakati huu na ni yapi mapenzi ya Mungu hasa kwa wakati wetu

 

Matendo 17:30-31 “Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”            

8.       Lazima uwe na utaalamu wa kujua ni mambo gani hasa yametimizwa katika ufalme wa Mungu na yale ambayo bado hayajatimizwa, Kanuni za ufalme wa Mungu (The Principle of the Kingdom) yako maswala kadhaa katika maswala yahusuyo ufalme wa Mungu ambayo yametimizwa na ambayo bado, kwa hiyo mtaalamu wa neno la Mungu anapaswa kuwa na uelewa huo.

 

9.       Lazima mtaalamu wa kutafasiri maandiko awe na ujuzi wa kina na wa kutosha kuhusu kutafasiri mifano ya ufalme wa Mungu (The Principle of Parables) mifano ya ufalme wa Mungu ina kanuni zake na taratibu zake na inabeba maana moja kubwa iliyokusudiwa na hivyo huwezi kuitafasiri kama unayefanya uchambuzi

 

10.   Lazima mtaalamu wa neno la Mungu awe na ujuzi wa kina kuhusu maswala ya unabii, (The Principle of Prophecy) ajue kuwa ni unabii gani umeshatimizwa na upi ambao bado haujatimizwa ili kujua ni namna gani anaweza kuyaweka sawa maswala ya kinabii asikosee au kwenda kinyume na zile kanuni za kimungu na ile tabia za unabii kujirudia kwa mfumo za zaidi ya mara moja.

Hizo hapo juu ni kanuni kumi muhimu zinazomuongoza mtafasiri wa maandiko kulitafasiri neno la Mungu kwa halali, sina muda mkubwa sana wa kuzielezea hapa kwa  kina lakini zinapatikana katika somo maalumu la kitheolojia linalohusika na namna na jinsi ya kuyatafasiri maandiko kwa halali somo hilo kitaalamu katika vyo vya Biblia linaitwa the “Principles of Biblical interpretations”  au “Hermaneutics”  the sientifical study of the methodological principles of interpretation of the Bible kwa Kiswahili hizo ni sayansi za ufundi na njia au kanuni za kimatumizi katiika kutafasiri maandiko au Biblia,  kwa hiyo watumishi wa Mungu wanaokuwa wameitwa na Mungu na kukubali kwenda katika vyuo vya Biblia hufundishwa masomo hayo kwa kusudi au lengo la kupunguza changamoto za kutafasiri vibaya maandiko, Uchungaji hausomewi, lakini yeye aliyeitwa anapaswa kuupeleka witio wake katika vyuo vya Biblia kwa walimu kwa kusudi la kuunoa wito wako ili uyatumie maandiko kwa halali au kwa mujibu wa kanuni kwa hiyo mtu anyezingatia kanuni hizo sasa anakuwa katika nafasi nzuri sasa ya kulitendea haki neno la Mungu kwa kuitafasiri Biblia katika njia iliyo njema, hairuhusiwi kutengeneza maana yako ya kibiblia kisha ukalisingizia andiko, to guide in “EISOGESIS”  na badala yake unatakiwa kutafuta maana iliyokusudiwa na mwandishi na kuiweka wazi kwa jamii unayoifundisha to guide out “EXEGESIS” wale wanaotafuta maana iliyokusudiwa na mwandishi kwa wakati wake kisha wakatafuta namna ya kuitumia maana ile kwa wakati huu wa sasa wako salama kabisa katika kulitafasiri neno la Mungu kwa usahihi, kwa hiyo tafasiri ya maandiko ni sayansi na sio swala la kukurupuka tu!

Sasa baada ya kujenga msingi huo wa ufahamu nataka twende moja kwa moja tukaaangalie sasa tafasiri ya kimaandiko kuhusu “Tafasiri halisi ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!” je andiko hili lilimaanisha nini kwa wakati wa Musa na linaweza kutafasiriwa vipi na linaweza kutendewa kazi katika mazingira yapi? Katika wakati wetu wa leo?

Tafasiri halisi ya Maana ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

Ni muhimu kwanza kufahamu kuwa andiko la msingi linatoka katika Kumbukumbu 33:24-25 “Na Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta. Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba; Na kadiri ya siku zako ndivyo zitakavyokuwa nguvu zako.”

Andiko hili kwa asili linatokana na lugha ya kiebrania kwa sababu ndio lugha ya asili iliyotumika kuandikia agano la kale tofauti na agano jipya ambalo kimsingi liliandikwa kwa lugha ya kiyunani sasa basi katika lugha ya kiebrania andiko hilo linasomeka namna hii:-

Âshr âmar âshr bârak bn râtsâh âch ţâbal regel shemen “24 âshr âmar âshr bârak bn râtsâh âch ţâbal regel shemen” kwa kiingereza ingetakiwa kusomeka Of Asher he said May Asher be most blessed of sons, may he be favorite among his brothers and bathe his feet in oil

KJV inasomeka hivi “And Asher he said, Let Asher be blessed with children; let him be acceptable to brethren, and let him dip his foot in oil”

SUV inasomeka hiviNa Asheri akamnena, Na abarikiwe Asheri kwa watoto; Na akubaliwe katika nduguze, Na achovye mguu wake katika mafuta.

Kwa asili andiko hili limetokana na Musa nabii ambaye alikuwa akitamka Baraka za aina mbalimbali kwa makabila 12 ya Israel sawa tu na jinsi Yakobo baba yao alivyowatabiria watoto wake kuhusu maswala yatakayowapata siku za mwisho kwa hiyo haya yalikuwa ni maneno ya kinabii  kutoka kwa Musa akiongezea yale yaliyotoka kwa Yakobo ona

Mwanzo 49:1-2 “Yakobo akawaita wanawe, akasema, Kusanyikeni, ili niwaambie yatakayowapata siku za mwisho. Kusanyikeni, msikie, enyi wana wa Yakobo, Msikilizeni Israeli, baba yenu.”

Mwanzo 49:20 “Asheri, chakula chake kitakuwa kinono, Naye atatoa tunu za kifalme.” Kimsingi Musa alikuwa akijazilizia Baraka zilizokuwa zimetamkwa na Baba yao Israel kwa kabisa zote 12 za wana wa Israel lakini linapokuja swala la kabila la Asheri inaonekana wazi kuwa Musa pamoja na Yakobo walikuwa wanalizungumzia kabila hili kama kabila ambalo Bwana angelibariki sana  kwa hiyo maneno “Thy feet in the oil or and let him dip his foot in Oil” au kwa KiswahiliNa achovye mguu wake katika mafutayana maana ya kinabii inayoashiria kuwa kabila la Asheri katika Israel ni kabila ambayo imetamkiwa kutembea katika utajiri mkubwa sana kwa chakula na tunu au madini  hiyo lugha inayotumika hapo ni lugha ya kinabii au pia inaweza kuitwa (figurative language) au figurative expression, yaani lugha ya mficho au lugha ya kimafumbo inayoashiria kuwa Asheri litakuwa ni kabila litakalokanyaga mafanikio makubwa sana, Asheri watakuwa una utajiri mkubwa wa mafuta ya mzeituni.

Nyakati za agano la kale mtu aliyekuwa anamiliki mafuta hasa yaliyotokana na mzeituni, alikuwa ni mtu ambaye anaweza kutengeneza fedha nyingi sana na kuwa vizuri kiuchumi, kwa nyakati zile, kwa hiyo lugha kubwa ya mafanikio na utajiri pia ililinganishwa na wingi wa mafuta ya mizeituni ambao mtu aliweza kuwa nao kama mtu angekuwa na mafuta ya kutosha angeweza kuyamudu maisha yake na kuondokana kabisa na madeni au kupoteza mali na rasilimali alizokuwa nazo, kuchovya mguu katika mafuta kulimaanisha ni kuwa juu ya Baraka zilizopitiliza, kabila la Asheri wanabarikiwa kuwa kabila lenye mafanikio na utajiri unaomwagika, pia mbaraka huu uliashiria kuwa mipaka ya kabila la Asheri itakuwa ni mipaka inayozingirwa na utajiri wa ardhi yenye rutuba na yenye kustawi mizeituni kwa wingi jambo ambalo litawapa utajiri wa mafuta. Kwa hiyo kuchovya mguu wake katika mafuta kunamaanisha kutembea katika mafanikio na maisha ya starehe, mafuta yalikuwa ni ishaya ya mafanikio makubwa nyakati za zamani kwa ichi za mashariki ya kati, ukibarikiwa kuwa uchovye mguu wako katika mafuta maana yake Mungu akufanikishe kwa njia rahisi na isiyo ya taabu.

2Wafalme 4:1-7 “Basi, mwanamke mmoja miongoni mwa wake za wana wa manabii alimlilia Elisha, akasema, Mtumishi wako mume wangu amekufa; nawe unajua ya kuwa mtumishi wako alikuwa mcha Bwana; na aliyemwia amekuja ili ajitwalie wana wangu wawili kuwa watumwa. Elisha akamwambia, Nikufanyie nini? Niambie; una kitu gani nyumbani? Akasema, Mimi mjakazi wako sina kitu nyumbani, ila chupa ya mafuta. Akasema, Nenda, ukatake vyombo huko nje kwa jirani zako wote, vyombo vitupu; wala usitake vichache. Kisha uingie ndani, ukajifungie mlango wewe na wanao, ukavimiminie mafuta vyombo vile vyote; navyo vilivyojaa ukavitenge. Basi akamwacha, akajifungia mlango yeye na wanawe; hao wakamletea vile vyombo, na yeye akamimina.Ikawa, vilipokwisha kujaa vile vyombo, akamwambia mwanawe, Niletee tena chombo. Akamwambia, Hakuna tena chombo. Mafuta yakakoma.Ndipo akaja akamwambia yule mtu wa Mungu. Naye akasema, Enenda ukayauze mafuta haya, uilipe deni yako; nayo yaliyosalia uyatumie wewe na watoto wako.”

Mtu alipokuwa amebarikiwa sana nyakati za agano la kale mafanikio yalionekana ni kama kukanyaga siagi au kumiminiwa mito ya mafuta, wakati huo ulikuwa unaitwa wakati wa ustawi mkubwa sana mfano Ayubu alipokuwa amebarikiwa sana kabla ya mapito yake alizikumbuka nyakati zake za Baraka kubwa na kuzitaja kama nyakati za kukanyaga siagi au kuoshwa hatua zako kwa siagi ona

Ayubu 29:4-6 “Kama nilivyokuwa katika siku zangu za kukomaa, Hapo siri ya Mungu ilipokuwa hemani mwangu; Wakati Mwenyezi alipokuwa akali pamoja nami, Nao watoto wangu walipokuwa wakinizunguka; Wakati hatua zangu zilipokuwa zikioshwa kwa siagi, Nalo jabali liliponimiminia mito ya mafuta!

Kwa hiyo katika andiko la msingi ni muhimu kila mwanafunzi wa maandiko akawa na uelewa kuwa hakuna mahali maaandiko yameagiza au kutoa amri au agizo la kukanyaga mafuta, andiko hili ni sehemu kamili ya maneno ya Baraka ya Musa kwa kabila kadhaa za Israel kabla ya kufa kwake, Musa alikuwa akifanya hivyo kama kiongozi wa kiroho kama ilivyokuwa kwa Israel au Yakobo ambaye ilipofika saa yake ya mwisho pia aliwaita watoto wake na kuwatamkia Baraka  kwa hiyo maneno  naNa achovye mguu wake katika mafuta yana uhusiano na Baraka ya moja kwa moja kwa kabila la Asheri  na ni lugha ya kinabii inayohusiana na mafanikio yao utajiri mkubwa ambao Mungu amewapa Kabila la Asheri, kabila hili lilibarikiwa sana kimwili, na kiroho na kwa maelezo ya marabi wa kiyahudi ni kuwa kabila hili pia lilikuwa na wanawake wazuri na waliokuwa na adabu na wala hawana maringo, kabila hili lilibarikiwa kwa utajiri, mafanikio na ongezeko kubwa lakini pia walibarikiwa kama watu ambao hawapigiki kirahisi vitani  na watakuwa na ulinzi wa uhakika Makomeo yako yatakuwa ya chuma na shaba  Asheri litakuwa ni kabila la watu wenye mafanikio makubwa sana na wingi wa mafuta unaashiria utajiri mkubwa sana wa Ardhi yenye kuzalisha mizeituni kwa wingi bna ambay ingewabeba kiuchumi.

Mafuta ya mzeituni nyakati za Biblia ilikuwa ni bidhaa adimu na ya thamani sana, mafuta yalitumika kwa kupikia, kuwashia taa, kutibu, kujipaka na kwa sababu mbali mbali kwa hiyo kabila hili kuwabarikiwa kiasi cha kukanyaga mafuta kulimaanisha wingi wa utajiri wa bidhaa hii adimu waliyokuwa nayo, kukanyaga mafuta au zabibu pia kulikuwa na maana ya kuendesha mtambo wa kukamulia Mafuta au zabibu kwaajili ya mvinyo, Mashine ya kutengenezea Zabibu au Mafuta ya mzeituni ilitengenezwa kwa mawe makubwa mawili ambapo jiwe moja kubwa lilikaa chini na jiwe moya lilikuwa juu na lile la juu lingesukumwa ili kusaga zaituni zilizovunwa na kuoshwa vizuri kisha zilikamuliwa katika mashinde (Shinikizo) na hivyo kuendesha mashine ya kukamua mafuta au Zabibu kwaajli ya juisi ya zabibu pia kuliitwa kukanyaka shinikizo

Isaya 63:1-2. “Ni nani huyu atokaye Edomu, Mwenye mavazi ya kutiwa damu kutoka Bosra? Huyu aliye na nguo za fahari, Anayekwenda katika ukuu wa uweza wake? Kwani mavazi yako kuwa mekundu, Na nguo zako kama za mtu akanyagaye zabibu? Nalikanyaga shinikizoni peke yangu; Wala katika watu hakuwapo mtu pamoja nami; Naam, naliwakanyaga kwa hasira yangu, Naliwaponda kwa ghadhabu yangu; Na mavazi yangu yametiwa madoa kwa damu yao, Nami nimezichafua nguo zangu zote.”          

Unaona kukanyaga Zabibu hapo maana yake ni kusaga zabibu kwaajili ya kupata juisi ya zabibu, na kukanyaga mafuta ya zeituni ni kukanyaga shinikio (Mashine za kizamani) za kukamulia mafuta ua mizabizu, kwa hiyi utaweza kuona kama Mungu alikuwa anamaaisha kuchovya mguu katika mafuta ni tukio halisi basi kukanyaka Zabibu nalo lingekuwa ni tukio halisi unaelewa?

 

Kwa hiyo Kabila la Asheri linatamkiwa na Musa kuwa kabila lenye wingi wa mafanikio na utajijiri wa mafuta ya zeituni na watu wasiopigika kirahisi, kabila la Asehri walikuwa na sifa njema sana nyakati za biblia kimwili na kiroho maana walitabiriwa kukubalika pia na kupata kibali kwa ndugu zao wakati Yesu alipokuwa anazaliwa mwanamke mmoja mcha Mungu aliyekuwa wa kiroho sana mwenye umri mkubwa sana na tabia njema na uvumilivu alijitokeza pia kutoa unabii kumuhusu Yesu Kristo mwanamke huyu maarufu alitokea kabila la Asheri ona

Luka 2:36-38 “Palikuwa na nabii mke, jina lake Ana, binti Fanueli, wa kabila ya Asheri, na umri wake ulikuwa miaka mingi, alikuwa amekaa na mume miaka saba baada ya uanawali wake. Naye ni mjane wa miaka themanini na minne; haondoki katika hekalu, ila huabudu usiku na mchana kwa kufunga na kuomba. Huyu alitokea saa ile ile akamshukuru Mungu, na wote waliokuwa wakiutarajia ukombozi katika Yerusalemu akawatolea habari zake.”

Kwa sababu hiyo ni muhimu wakristo wakawa na uelewa kuwa hakuna agizo la kibiblia la aina yoyote lile linaloamuru wanadamu wakanyage mafuta, hii ilikuwa ni lugha ya kinabii ya kumtakia mtu mafanikio hata kama utakuwa ulikanyaga mafuta mahali na ukaona mafanikio fulani kumbuka tu kuwa Mungu aliweza kukuhurumia tena alikuhurumia kwa sababu ya ujinga wako na kwa kufilisika kwako kimawazo na kwa tafasiri mbovu za kibiblia, na kwa sababu ya jina lake ambalo lilitajwa huko lakini, andiko hilo halina uhusiano wowote na kukanyaga mafuta kunakofanywa na watumishi kadhaa leo.  Maandiko hayajakakataza mtu kupakwa mafuta miguuni baada ya kunawa au kuoga, lakini hilo sio agizo la kibiblia kwamba tukanyage mafuta, Nayaweka haya hadharani kwa sababu nimeagizwa kuihubiri kweli, nimeagizwa kuwafungua watu akili ili watoke gizani na kumgeukia Yesu Kristo mzima mzima sawa sawa na mapenzi yake nimeagizwa kuweka kweli ya Mungu kwa uwazi kwa kusudu la kuleta uelewa ulio wazi ili watu waifahamu kweli na kweli iwaweke huru maandiko yanaonyesha wazi kuwa wakati wa Yoshua alipopiga kura ya kugawa ardhi watu wa kabila la Asheri walipata inchi yenye utajiri mkubwa wa madini pamoja na ustawi wa miti ya mizeituni na chakula cha kutosha, kwa hiyo unabii kuhusu kubarikiwa kwa kabila hilo la Asheri ulitimizwa!

Yoshua 19:24-31 “Kisha kura ya tano ilitokea kwa ajili ya kabila ya wana wa Asheri kwa kuandama jamaa zao. Na mpaka wao ulikuwa ni Helkathi, na Hali, na Beteni, na Akishafu; na Alameleki, na Amadi, na Mishali; nao ukafikilia hata Karmeli upande wa magharibi, tena ulifikilia hata Shihor-libnathi; kisha ukazunguka kuelekea maawio ya jua mpaka Beth-dagoni, nao ukafikilia hata Zabuloni, tena mpaka bonde la Iftaeli upande wa kaskazini hata Bethemeki na Neyeli; kisha ukatokea hata Kabuli upande wa kushoto; na Ebroni, na Rehobu, na Hamoni, na Kana, hata kufikilia Sidoni mkuu; kisha mpaka ulizunguka kuelekea Rama, na mji wa Tiro ulio na boma; kisha mpaka ulizunguka kuelekea Hosa; na matokeo yake yalikuwa baharini katika nchi ya Akzibu; na Uma pia, na Afeka, na Rehobu; miji ishirini na miwili, pamoja na vijiji vyake.Huu ndio urithi wa kabila ya wana wa Asheri kwa kuandama jamaa zao; miji hii pamoja na vijiji vyake.”

Tafasiri ya Kabila la Asheri kuchovya mguu wao katika mafuta inaweza kutafasiriwa leo kama kutembea katika Baraka za Mungu, kubarikiwa na kupata kibali kiroho, kiuchumi na wingi wa mafanikio, kufurahia neema ya Mungu na kuwa na mapito yasiyo na taabu na masumbufu, lakini kamwe andiko hilo haliwezi kutafasiriwa kama lisemavyo moja kwa moja kwa kufanya hivyo ni kufanya mambo ya kijinga kwani mnakanyaga chakula, kukanyaga chakula kunaleta laana kubwa sana  kwa hiyo Mwandishi au Musa hakuagiza watu wakanyage chakula au wakanyage mafuta mwandishi hajawahi kukusudia hivyo! Msipoelewa maneno ya Mungu mtakanyagishwa mpaka ugali, Bwana ampe neema kila mmoja kutembea katika Baraka za Mungu kama kabila ya Asheri katika jina la Yesu Kristo amen!

Jamani swala la kuchovya mguu katika mafuta tafasiri yake sio kukanyaka mafuta halisi, hii ni lugha ya kimafumbo yenye maana kuwa kabila la Asheri watafanikiwa sana kwa utajiri mwingi utakaopatikana kwao naomba ieleweke kwa njia hiyo!

Naomba niseme kwa kiingereza hapa labda nitaeleweka pia

My brothers and Sisters the phrase is not a literal instruction to dip feet in oil, but rather a metaphor for the tribe of Asher’s Prosperity and abundance of resouces available to them I beg to be understood in that way!

Jinsi ya kuchovya mguu wako katika Mafuta!

Kuchovya mguu wako katika mafuta maana yake ni kutembea katika Baraka za Mungu, matokeo ya kutembea katika Baraka za Mungu sio tukio linalokuja kama kufumba na kufumbua bali ni mchakato unaotokana na mtindo wa maisha ya kila siku, unaoendana na utii kwa Mungu. Badala ya kuwakanyagisha watu chakula watumishi wa Mungu wawafundishe watu jinsi ya kutembea katika Baraka za Mungu na kutembea katika Baraka za Mungu kuna kanuni zake.

Wakati Musa au Yakobo anawabariki kabla la Asheri kumbuka kuwa alikuwa amewasoma mtindo wao wa maisha tabia na mwenendo wao kwa Bwana, Imani yao, ushirika wao na kujitoa kwao katika maisha ya kila siku na safari ya kila siku ya maisha yao kwa hiyo Yakobo alipofikia mwisho aliwatabiria Asheri na Musa naye alipokuwa anafikia mwisho aliwatabiria Asheri Baraka nyingi sana kwa hiyo mtu awaye yote anayetaka Baraka za Mungu atapaswa kukanyaga katika kanuni za Mungu kwa kufanya yafuatayo katika maisha yake ya siku zote:-

1.       Ishi maisha ya utii kwa neno la Mungu – Baraka za Mungu huja kwetu pale tunapotii, huenda Musa alikuwa amewaangalia sana wana wa Asheri na kubaini kuwa walikuwa watii katika sheria za Mungu na sheria ya Mungu ilikuwa na ahadi kwamba kama mtu ataisikiliza sauti ya Bwana Mungu wake na kuyatunza maagizo yake basi Mungu angeamuru Baraka zije juu ya mtu huyu au kabila hiyo, utii wetu kwa Mungu katika mambo yote hata madogo madogo utawapelekea watu kufurahia matunda ya utii huo.

 

Kumbukumbu 28:1-2 “Itakuwa utakaposikia sauti ya Bwana, Mungu wako, kwa bidii, kutunza kuyafanya maagizo yake yote nikuagizayo leo, ndipo Bwana, Mungu wako, atakapokutukuza juu ya mataifa yote ya duniani; na baraka hizi zote zitakujilia na kukupata usikiapo sauti ya Bwana, Mungu wako.”

 

Isaya 1:19-20 “Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi; bali kama mkikataa na kuasi mtaangamizwa kwa upanga; maana kinywa cha Bwana kimenena haya.”      

 

2.       Ishi maisha  ya Imani – Mwamini na kumtegemea Mungu, hakuna namna iwayo yote mtu anaweza kuishi kwa imani bila kutii na kutegemea, tunaelezwa kuwa Mungu alimuahidi Ibrahimu Baraka lakini ili Baraka hizo ziweze kumjilia Ibrahimu yeye alimuamini Mungu na kutii na ikahesabiwa kwake kuna na haki, hakuna namna yoyote ile ambayo tunaweza kumpendeza Mungu pasipo Imani

 

Mwanzo 12:1-4 “BWANA akamwambia Abramu, Toka wewe katika nchi yako, na jamaa zako, na nyumba ya baba yako, uende mpaka nchi nitakayokuonyesha; nami nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa, na kukubariki, na kulikuza jina lako; nawe uwe baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa. Basi Abramu akaenda, kama BWANA alivyomwamuru; Lutu akaenda pamoja naye. Naye Abramu alikuwa mtu wa miaka sabini na mitano alipotoka Harani.”

 

Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”

 

Yeremia 17:5-8 “Bwana asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana. Maana atakuwa kama fukara nyikani, Hataona yatakapotokea mema; Bali atakaa jangwani palipo ukame, Katika nchi ya chumvi isiyokaliwa na watu. Amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni Tumaini Lake. Maana atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, Uenezao mizizi yake karibu na mto; Hautaona hofu wakati wa hari ujapo, Bali jani lake litakuwa bichi; Wala hautahangaika mwaka wa uchache wa mvua, Wala hautaacha kuzaa matunda.

 

3.       Ishi maisha ya utoaji – hakikisha kuwa unatoa kwa ukarimu na sio kwa sheria maandiko yanaonyesha kuwa Mungu huwabariki watu wake wote wanaotoa kwa moyo wa upendo na kwa ukarimu unapokuwa na moyo wa kuwasaidia wengine Mungu huamuru Baraka zake zikujie.

 

Matendo 20:34-35 “Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”            

 

Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa.”                                        

Hitimisho:

Kutembea katika Baraka za Mungu ni matokeo ya maisha endelevu yenye kudumisha uhusiano wako na Mungu, kumpenda Mungu kwa moyo wako wote, kumtii na kumtumikia huku ukiendelea kumuamini, Mungu sio mchoyo kwani yeye amekusudia kumbariki kila mtu na yuko tayari kumimina Baraka zake katika maisha yako ili hatimaye wewe nawe uchovye mguu wako katika mafuta yaani utembee katika Baraka za Mungu, wakristo ni lazima wakumbuke kuwa hakuna njia ya mkato, lakini iko njia ya mchakato, usikubali kudanganywa hata kama watu wanayatumia maandiko, kama kukanyaka mafuta ingekuwa ni njia halisi ya kibiblia ya kufunguliwa na kupata Baraka za Mungu wengi tungekanyaga mafuta hayo, lakini je tangu umenza kukanyaga mafuta halisi kuna badiliko lolote la kiroho, kiafya au kiuchumi? Watumishi wa Mungu tuamke na kutembea katika nuru kwani saa ya kutoka gizani imekwisha kuwadia asomaye na afahamu!, iwapo kukanyaga mafuta lingekuwa agizo halisi la kimaandiko, mitume wa Bwana wangefanya hivyo, na Yesu angeagiza hivyo, na ingekuwa rahisi tu tungekanyaga mafuta na kupata mafanikio lakini hakuna njia ya mkato kwa Mungu kanyaga njia halisi za mapenzi yake na utafanikiwa, kama bado hujamwamini Yesu tafuta kwanza ufaome wake na haki yake na mengine yote mtazidishiwa jiulize  je ni wapi Yesu ameagiza katika agano jipya? Tuchovye mguu katika mafuta?  Je Yesu alipowaosha wanafunzi wake miguu alikuwa akimaanisha na sisi tuoshane miguu? La hasha alikuwa akijibu swali la wanafunzi wake ni yupi aliye mkubwa na akajibu kwa vitendo ni yule atumikaye au anayewahudumia wengine, hebu tulitendee haki neno la Mungu na tusikubali kudanganyika kila tunachofundishwa duniani tuhoji na tujiulize kikoje katika maandiko na je ndivyo kilivyo? Imekuwaje wakristo wa kipindi hiki ambao ni wasomi na maarifa nyameongezeka wanadanganyika kwa njia rahisi? Do you think that to think critical is sin? Je unafikiri kwamba kufikiri kwa kuhoji au kujiuliza ni dhambi? Amka kuanzia sasa na jaribu kila fundisho au roho uone kama ndivyo ilivyo, Mafundisho huwa yana roho nyuma yake

Yohana 6:63 “Roho ndiyo itiayo uzima, mwili haufai kitu; maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima.”

1Yohana 4:1-4 “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani. Katika hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili yatokana na Mungu. Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu. Na hii ndiyo roho ya mpinga Kristo ambayo mmesikia kwamba yaja; na sasa imekwisha kuwako duniani. Ninyi, watoto wadogo, mwatokana na Mungu nanyi mmewashinda, kwa sababu yeye aliye ndani yenu ni mkuu kuliko yeye aliye katika dunia.”

                                 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!