Alhamisi, 5 Oktoba 2017

Mfululizo wa Masomo yahusuyo Hutuba za Kibiblia - "Homiletics".


UTANGULIZI


Homiletics ni somo linalohusu jinsi ya kuandaa na kupeleka ujumbe wa kibiblia kwa kufundisha au kuhubiri.
Tunajifunza somo hili kwa kusudi la kuwa wanenaji hodari na wazuri wa Neno la Mungu, Kuna njia kuu mbili tu za kuupeleka na kuuwasilisha ujumbe wa neno la Mungu ambao ni kuhubiri na kufundisha,  kwa kawaida hizi ni sehemu mbili  za sehemu moja ya huduma, Huduma ya mitume na Yesu Kristo ilijumuisha Kuhubiri na Kufundisha  ona Mathayo 4;23, Marko 1;21,27,28, Luka 4;44 na Matendo 18;4-5,11,18;19,19;8. Kuna waalimu wengi ambao hawahubiri ingawa wachungaji wote wana huduma ya Kuhubiri na kufundisha.  Katika somo hili tunajifunza jinsi ya kuwa wahubiri na wanenaji wazuri mbele za watu. Somo hili litamsaidia muhubiri kuwa na uwezo wa kuandaa vema mahubiri yake na kuyawasilisha lakini pia linakuandaa kuwa mnenaji hodari kila wakati unaposimama mbele za watu au kuzungumza nao kupitia vyombo vya habari na kadhalika.

     Somo kuhusu utungaji wa hutuba na namna ya kuwakilisha hutuba homiletics ni moja ya masomo ya muhimu sana katika jamii na katika Nyanja ya kibiblia  ni kupitia hutuba ndipo mtu anapoweza kujifunua na kujieleza yeye ni nini  na anataka nini, malengo yake ni nini, na kufanya tathimini ya nini kimefanyika na nini kinapaswa kufanyika, kwa msingi huo hutuba ina nafasi kubwa katika maisha yetu, watu wengi wametamka mambo ambayo hawangepaswa kuyatamka na kujikuta wakijilaani baadaye aidha waliyoyatamka yalikuwa ni matakwa yao binafsi na wakati mwingine hayana ukweli halisi  na kushindwa kujieleza hili ni moja ya matatizo yanayopelekea kuweko kwa  kwa watu mbalimbali na kushindwa kujieleza kumekuwa na mchango mkubwa sana wa magonjwa ya kiakili na wengine wanajikuta wakijitukana na kujilaumu kuwa wao ni wazembe, wabaya, hawafai, wao sio wema na haitakuja itokee wao kuwa wema kwa sababu ya majuto ya namna tu walivyoshindwa kujieleza na kupata aibu mbele ya hadahara aina hizi za maelezo hazitusaidii kuwa watu wanaostahili.Badala yake tunahitaji kuwa na bidii katika kujifunza kwani hakuna aliyezaliwa akiwa anajua kujieleza kwa msingi huo basi 

     Ni muhimu kujitambua wenyewe kwanza na kwa kujifahamu kuwa sisi ni watu wa namna gani na kisha baada ya kujitambua ndipo tuifanye kazi ya kujieleza vema na kuwakilisha mambo kwa uhakika, katika namna chanya na yenye ushawishi na hapo ndipo tunapoweza kuwa watu wenye uwezo wa kujieleza katika hutuba zetu yaani kutambua madhaifu yetu kwanza kisha kujifunza kuyadhibiti kisha kuingia katika ulingo wa kuwa wanenaji hodari na watoa hutuba wenye kujiamini na kujua kujieleza.

Lakini hutuba ni nini? Ni usemi kwa ufupi tunaweza kueleza kwa namna hiyo “it is just a speech” ni kuzungumza ni kutoa maelezo ni kujieleza kwa uhakika “Speaking to actuate” kuzungumza kunakochochea vitendo huu ndio msingi mkuu wa hutuba za Kikristo, Kuhutubu ni huduma kama ilivyo huduma ya uandishi ni huduma iliyoenea ulimwenguni kote kuliko huduma ya uandishi imebeinika kuwa wale wanaoandika wakati mwingine hutakiwa kuzungumza ingawa si kila anayezungumza hutakiwa kuandika  kwa hivyo kuhutubia ni huduma kamili kabisa  na ili kuishawishi jamii kupitia usemaji yaani hutuba inahitajika mbinu za kitaalamu na kujitoa katika kushughulika na maswala hayo ya kihutuba somo hili linashughulikia swala lote hilo la hutuba za kibiblia na hata zile zisizo za kibiblia ni  matumaini yangu kuwa utabarikiwa unapopitia somo hili na Mungu wa amani akubariki na kukupa moyo wa kujifunza katika jina la Yesu amen!.

SURA YA KWANZA: MUHUBIRI NA UJUMBE WAKE

Sifa za Kibiblia za Muhubiri
     Kabla ya kuanza shughuli ya kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu muhubiri anapaswa kuhakikisha kuwa anakuwa na sifa zinazohitajika za kibiblia, kuhubiri Biblia ni tofauti na hutuba nyingine za kisiasa au za kijamii,  kazi hii ya kuhubiri Biblia ni kazi ya Mungu na hivyo awaye yote anayeifanya ni lazima awe ameungwa na Mungu kwa maana nyingine hapa tunazungumzia wito wa kiutumishi kila mkristo anaweza kuhubiri na kufundisha Neno la Mungu kwa sababu Yesu aliagiza wakristo kufanya hivyo hilo ni jema lakini hata hivyo wako ambao Mungu amewaweka wakfu kwa ajili ya kuifanya kazi hii hawa ni wale walioitwa. Lakini penginepo mtu yu aweza kuuliza swali wito ni nini? Ni msukumo unaowekwa na Mungu kupitia Roho wake Mtakatifu kumuwezesha mtu aliyeokoka kusikia msukumo wa kufanya kazi ya ya Mungu na kukubali kuwa na wajibu wa kuwahubiri na kuwafundisha watu Neno la Mungu akisaidiwa na neema ya Mungu. Kuna aina kuu tatu za wito katika ukristo;-

Wito wa Jumla katika wokovu.
Wito huu ni wa jumla katika wokovu wito huu hutokea pale Mungu anapokuwa amemuokoa mtu kwa neema yake anapokuwa amemuamini Yesu Kristo na kumkiri akijutia dhambi zake na kupokea neema inayomuwezesha kukataa dhambi Tito 1;11 wito huu unaambatana na pumziko la kutolewa katika nira ya sheria Mathayo 11;28, ni wito unaohusu kuondoka gizani na kuja katika nuru kwa ajili ya maandalizi ya kuingia katika uzima wa milele 1Petro 2;9,1Timotheo 6;12 wito huu pia hujumuisha swala la kuishi maisha matakatifu 1Petro 15-16, wito huu kwa kiingereza ni “General call to the Salvation”. Wito huu ndio msingi wa aina nyingine za wito.

Wito wa jumla wa kumtumikia Mungu.
Wito huu unajumuisha pamoja na wito uliotangulia kuwa kila mtu aliyeitwa katika wokovu pia ameitwa kwa ajili ya kumtumikia Mungu, na Mungu anamtaka kila mtu aliyeokolewa amtumikie  wito huu ni wito wa jumla katika utumishi “General call to the service” wito huu unaanza mara tu baada ya kuokolewa Kutoka 7;16,8;1,20,9;1,13 agizo la kuhubiri na kufundisha ni la wakristo wote waliookolewa Mathayo 28;19-20 Matendo 8;1-4 na tunapata ushahidi kuwa nyakati za kanisa la kwanza washirika pia walihusika katika kuhubiri injili na hata kuanzisha baadhi ya makanisa wakimtumikia Mungu.

Wito maalumu wa Utumishi na maongozi.
Baada ya aina hizo za wito ambazo hutangulia ndipo sa wito huu maalumu wa maongozi huja huu ni wito maalumu kwa ajili ya utumishi “Special call to the service”ni wito ambao unaweza kugawanyika katika makundi makuu matano ya karama za kihuduma wito huu kibiblia unaanza kwa kutenga au kuweka wakfu kwa maneno haya “Mungu ameweka wengine “1Koritho 12;28 hawa ni mitume, manabii, wainjilisti, wachungaji na waalimu Waefeso 4;11 Hawa hawakujiweka wenyewe bali wamewekwa na Mungu na wamekubali kujinyenyekeza katika mpango wa Kristo kwa maisha yao yote waebrania 5;4. Kazi yao ikiwa ni kuwaandaa watu kwa makusudi ya kazi ya huduma itendeke na kuwakamilisha watu hata kufikia katika cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo katika tabiana mwenendo.

Jinsi Mungu anavyoita watu.
Nyakati za zamani katika vyuo vya Biblia kulikuwa na tabia ya kusikia shuhuda mbalimbali jinsi Mungu alivyowaita watumishi wake kuingia katika huduma  na unaposikiliza shuhuda hizo nyingine zinatisha kwani wengine wameitwa kwa kuisikia kabia sauti ya Mungu ikiwataka kufanya huduma hii na wengine walikuwa na shuhuda nyingine za kawaida unaposikia shuhuda hizi unaweza kufikiri kuwa labda aliyeitwa kwa kuisikia sauti ya Mungu kabisa ni maalumu sana kuliko wengine, au Yule ambaye Yesu amemtokea na kumuita n.k,Hapa jambo la msingi ni kujifunza kwamba Mungu huita watu kwa njia nyingi  na kwa namna mbalimbali kwa msingi huo ni upumbavu kujilinganisha na wengine kama maandiko yasemavyo 2Wakoritho 10;12 kila mwanadamu ni tofauti na mwingine  kwa sababu Mungu alikusudia iwe hivyo.

Na kwa kuwa kila mtu ni wa tofauti Mungu pia huita watu kwa njia tofauti na kila wito ni halisi na hakuna mtu anayeweza kudai kuwa ana wito sahii sana kuliko wa wengine kama ilivyo kwa wokovu.
·         Musa aliitwa kupitia Maono  kijiti kilichokuwa kinawaka Moto lakini hakliteketei Kutoka 3;1-10
·         Isaya alikua hekaluni akaona maono na kuitwa Isaya 6;1-9
·         Yeremia kupitia maono lakini tangu tumboni Mungu alikusuduia kumtumia Yeremia 1;1-19
·         Sauli aliitwa baada ya kupigwa mweleka alipokua akienda Dameski Matendo 9;1-20

·         Marko aliitwa kuwa masaidizi wa kwanza katika safari za kimisheni za Paulo na Barnaba Matendo 12;25 baadaye alikataliwa na Paulo kwa sababu alikuwa dhaifu kihuduma hata hivyo Barnaba aliendelea kumlea  na baadaye akafaa kwa huduma Matendo 13;13,15,37-38 na hata Paulo mtume alimihitaji sana baada ya kuona anafaa kwa huduma tena ndiye aliyeandika injili ya Marko. 2Timotheo 4;11. (Yoshua alikuwa mtumwa wa Musa Mungu akamuita kuwa kiongozi)
·         Elisha aliitwa kwa kutupiwa vazi na Eliya nakuamua kumfuata 2Wafalme 2;12-15.

Mungu anaita watu kwa njia mbalimbali na kwa namna nyingi inategemea tu mkao wako wa kiroho kisikia jinsi Mungu anavoita Roho wa Mungu yuko kila wakati yeye ndiye Bwana wa mavuno na huita watu kwa njia mbalimbali soma 1Koritho 2;14  Mambo ya kiroho yanajulikana kwa jinsi ya Rohoni ni wale walio kondoo wa Yesu wanaoweza kuisikia sauti yake Yohana 10;27  vyovyote iwavyo hakuna mwenye uwezo wa kudai au kuhukumu kuwa mwengine hakuitwa ni kazi ya Mungu kuita sio ya mtu.

Mungu aliyachagua mambo mapumbavu.
1Wakoritho 1;26-29 “Maana ndugu zangu  angalieni mwito wenu  ya kwamba si wengi wenye hekima ya mwilini, si wengi wenye nguvu, si wengi wenye cheowalioitwa, bali Mungu aliyachagua mambo mapumbavu ya dunia awaaibishe wenye hekima, tena alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu tena Mungu alivichagua vitu vinyonge vya dunia  na vilivyodarauliwa  naam vitu ambavyo haviko avibatilishe vile vilivyoko mwenye mwili awaye yote asije akajisifumbele za Mungu” unaona  Mungu katika hekima yake hachagui watu maalumu sana katika utumishi wake si kuwa Haiti kabisa wenye hekima lakini biblia inasema si wengi.. wakati mwingine Mungu aliwaita watu ambao kama ungeliwaona kwa macho yako wewe usingelikubali kuwaita na ndio maana tunaona kuwa hata Musa alipoitwa alijifahamu kuwa ana kigugumizi, Yeremia alijiona ni mtoto, Isaya alijiona kuwa ana midomo michafu hakuna aliyekua anafaa hata mmoja  Mungu hatuchagui kwa sababu tunafaa anachagua mtu mwenye uwezo wa kuibeba neema yake  watu ambao kwao Mungu atatukuzwa kupitia wao.Hata hivyo madhaifu hayo sio tiketi ya kukubali kukaa katika hayo bali ni kwaajili ya kuibeba neema ya Mungu.

MASWALA SITA YA LAZIMA ANAYOPASWA KUWA NAYO MUHUBIRI.
a.       Muhubiri anapaswa kuwa mtu asiyelaumika 1Timotheo 3;2
Hii ni sentensi ya ujumla inayofuatiwa na sifa zipatazo tisa ambazo muhubiri anapaswa kuwa nazo katika njia kuu mbili

·         Asiyelaumika katika macho yake mwenyewe maana yeke ni nini? Dhambi inatufanya tuwe waoga  juu yetu wenyewe huwezi kuhubiri jambo Fulani kwa ujasiri kama jambo hilo wewe mwenyewe umeshindwa kulifanyia kazi kwa mfano kma hutoi zaka huwezi kuhubiri kwa ujasiri kuhusu utoaji wa zaka  unaweza kujikaza kwa unafiki tu, hivyo kama muhubiri mwenyewe huna maadili ni ngumu kuhubiri maadili labda uwe farisayo ndipo uweze kuhubiri utakatifu kwa wengine  kuishi juu ya kiwango kunakuwezesha kuwa muhubiri mwenye viwango, jasiri na unayejiamini.
·         Asiyelaumika katika macho ya wengine maana yake ni nini? Biblia inasema katika Waebrania 12;13 “Mkaifanyie miguu yenu njia za kunyooka ili kitu kilicho kiwete kisipotoshwe bali afadhali kiponywe” Muhubiri anapokuwa mwenye kulaumika maana yake ni kuwa wale dhaifu ambao wana mfuata  wanakoseshwa na kuanguka  wataangalia mfano wa muhubiri na kuigiza tabia zakeau kuiacha imani kwa msingi huo muhubiri ni mfano wa maswala mema au maswala mabaya, Biblia  inaonyesha kuwa tuwe kielelezo katika usemi mwenendo imani na usafi 1Timotheo 4;12. Hii maana yake ni kuwa si kwamba muhubiri ataepuka kabisa kulaumiwa lakini lawama mbaya ni zile za kweli lawama hizi zinafananiswa na kujitia matope wewe mwenyewe lakini lawama ambazo hazina ukweli zinafananishwa na gari linalopita na kukumwagia matope.



Gari linalopita linaweza kukumwagia matope lakini baadhi ya watu hujipaka matope wao wenyewe. Mchungaji hapaswi kuwa na lawama za kweli lakini mchungaji hawezi kukwepa lawama za kusingiziwa, lawama hizi ni kama gari inayopita na kukumwagia matope, lawama ambazo hazina ukweli haziwezi kuwa na nguvu katika maisha yako. 


b.      Muhubiri anapaswa kuwa  Mume wa mke mmoja 1Tomotheo 3;2
Biblia inaposema awe mume wa mke mmoja katika Biblia ya kiyunani tafasiri yake inaweza kusomeka hivi kwa kiingereza “Be a One – woma man” yaani awe mwanaume wa mwanamke mmoja  huii maana yake sio lazima uoe na kuweka ndani lakini uwe mwaminifu kwa mkeo ndio tafasiri halali hapo  watu wanategemea kiongozi kuwa mtu mwenye maadili ndani ya ndoa yake pia ili kukubalika katika jamii
Mwanasisa Gary Hart alipendwa na wengi huko Marekani wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka 1984 alikuwa ni mwenye mvuto, mwenye elimu nzuri na maarufu sana  na alikuwa mnenejia hodari sana  mwenye uwezo mkubwa wa kushawishi na watu wengi walijua kuwa atakuwa raisi, baada ya muda ikagundulika kuwa hakuwa mwaminifu kwa mkewe na mara vyombo vya habari vikatangaza  ndugu huyo alipoteza ujasiri na  aliachana na kampeni za kisiasa kumbe hata watu wa kawaida nje ya kanisa wanahitaji mtu mwaminifu ni zaidi sana katika kanisa la Mungu. Mungu nyu aweza kusamehe dhambi yoyote inapofanyika na mtu akatubu lakini utakuwa umejichafulia kimaadili Mithali 6;32-33

c.       Muhubiri anapaswa kuwa Mwenye kiasi na Busara, mtu wa utaratibu 1Tomotheo 3;2
Kuwa na kiasi maana yake kuweza kujizuia kuhakikisha kuwa unakuwa sawia katika maeneo yote Usiiishi zaidi ya kiwango cha kawaida katika jamii yako, uwe na kiasi katika mazingira yote yanayokuzunguka, ishi vizuri na watu , usigombane au kupandisha hasira kupita kawaida  wala usipuuzie majukumu yako kuwa mtru unayeheshimika kwa matendo mema , hakikisha kuwa unazitawala tama zako kama mpanda farasi anapomtawala farasi kwa kutumia lijamu.

d.      Muhubiri anapaswa kuwa mkarimu 1Timotheo 3;2
Mtu mkarimu huwa pia ni mkaribishaji anakuwa mkarimu kwa watu na kuwahudumia hata kwa vinywaji waliookoka na wasiookoka watu wewngi wanaweza kuokolewa kupitia tabia zako za ukarimu 

e.      Muhubiri ni lazima ajue kufundisha 1Timotheo 3;2
Kuhubiri na kufundisha ni sehemu kuu mbili za huduma ya muhubiri, muhubiri pia ni mwalimu. Lakini huwezi kufundisha kitu ambacho hujajifunza kwa msingi huo muhubiri wakati wote anapaswa kuwa mwanafunzi wa Biblia na kwa maana nyingine hana mahafali, kufundisha kunahitaji zaidi ya maarifa ili uwe mwalimu mzuiri unapaswa pia kuwa mtu mzuri 2Tomotheo 2;24-25 “Tena haimpasi mtumwa wa bwana kuwa mgomvi , bali kuwa mwanana kwa watu wote awezaye kufundisha mvumilivu, akiwaonya watu kwa upole wao washindanao naye ili kama ikiwezekana Mungu awape kutubu na kuijua kweli”
 Kuweza kufundisha ni moja ya majukumu muhimu kwa mwalimu awaye tymwenye uwezo wa kufundisha anapaswa kuwa mnyenyekevu na mwanana mwema na kama utajiona kuwa bado humfananii Kristo hilo lisikupe shida endelea kumuomba Mungu na mwalimu mwema huendelea kuwa mwema  Mathayo 5;12. 

f.        Muhubiri ni lazima ajue kuisimamia nyumba yake 1Timotheo 3;4
Kiongozi wa kiroho anapaswa kuwa mwenye kuisimamaia nyumba yake vema na kutiisha watoto wake katika usatahivu, Eli ni moja ya mifano ya kiongozi wa kiroho aliyepoteza sifa  kutokana na kukosekana kwa maadili kwa watoto wake mwenyewe na kushindwa kuwasimamia  1Samuel 2-3, nyumba yake haikuwa mfano mzuri wa kiroho, Baadhi ya wahubiri wamejaribu kuwalazimisha wake zao au watoto wao mambo Fulani na matokeo yake wanavuna uasi na sio mahusiano mazuri , Mwanaume anatakiwa ajifunze kumpenda mkewe kama nafsi yake  na kama Kristo alivyolipenda kanisa  Waefeso 5;25 hapo ndipo uwezekano wa kuishi kwa amani naye unapotokea, wala watoto hutakiwi kuwalipukia kwa hasira lakini inakupasa  kuiwafundisha na kuwatika katika nidhamu  na kuwaelekeza katika njia za Bwana  Efeso 6;4 siku zote watoto huwa na mwitikio mwema kwa baba anayeshughulika nao vema  na kila unapopanda mbegu njema katika familia yako unazivuna
     Uwezo mkubwa wa kiongozi wa kiroho aliyekomaa ni namna gani anahusiana na familia yake  mtu anaposhindwa kuisimia nyumba yake vema atafanya kosa kama hilo wakati akishughulika na kanisa na Yule anayefanikiwa kushughulika vema na familia yake hali kadhalika hufanikiwa kwa kiwango kama hicho katika kuliongoza kanisa  Paulo alishughulika na waamini kama ambavyo baba anavyo shughulika na familia yake 1Thesalonike 2;11 ukiwa mwaminifu katika mambo madogo anaweza kuwa mwaminifu katika mambo makubwa pia Luka 16;10.

MASWALA MANNE AMBAYO MUHUBIRI HAPASWI KUWA.

a.       Muhubiri hapaswi kuwa mtumwa wa ulevi 1Timotheo 3;3
Kwa ujumla haipaswi kwa muhubiri kuonekana anakunywa pombe au hata kukaribia baa ulevi ni kama nyoka mwenye sumu kali kwa msingi huo muhubiri anapaswa kuwa mbali nayo Mithali 23;29-32 Biblia inakataza kulewa kwa mvinyo na badala yake inasisitiza swala la kujaa Roho Waefeso 5;18.

b.      Muhubiri hapaswi kuwa mgomvi wala mtu wa kujadiliana 1Timotheo 3;3
Siku zote hasira za mwanadamu haitendi haki ya Mungu Yakobo 1;20 “lakini hekima ishukayo kutoka juu ni ya amani, ya upole , tayari kusikiliza maneno ya watu imejaa rehema na matunda mema haina fitina, haina unafiki” Yakobo 3;17 ni muhimu kila mmoja kuomba ili kwamba Mungu atuumbie tabia ya upole na kuwa na maneno mem.

c.       Muhubiri hapaswi kuwa mpenda fedha  1Timotheo 3;3
Kuna hoja kadhaa kuhusu fedha baadhi wanahoji kuwa kukosekana kwa fedha ndio chanzo cha kila aina ya uovu lakini hii sio kweli kwani hata watu wenye fedha pia ni wenye dhambi, wala mtu haongezeki katika utakatifu kama anavyoongezeka katika fedha, wala fedha hazitufanyi tuwe wa Mungu au kiroho, Tatizo sio ukosefu wa fedha wala kuwa na fedha tatizo ni asili ya dhambi aliyonayo kila mwanadamu, kila mmoja anahitaji fedha  ni za muhimu situ kuwa tunahitaji fedha lakini tunastahili kuwa nazo  kila mtenda kazi anastahili ujira wake 1Tomotheo 5;18,1Koritho 9;9-11 lakini tunaaswa katika maandiko kuutafuta kwanza ufalme wa Mungu na hakli yake na mengine yote tutazidishiwa Mathayo 6;33 Abrahamu alikataa fedha alizopewa na mfalme wa sodoma aliona ni muhimu kutunza utakatifu wake na uhusiano wake na Mungu Mwanzo 14;23, dhambi kubwa ni kupedna fedha zaidi kuliko kumpenda Mungu Mathayo 6;24.

d.      Muhubiri  hapaswi kuwa aliyeongoka hivi karibuni 1Tomotheo 3;6
Dhambi mbaya kuliko zote ni kiburi  ni kwaajili hii ndio maana shetani alihukumiwa na kutupwa  Mithali 16;18, shetani alijivuna kwaajili ya nafasi aliyo nayo kama Malaika mkuu na hivyo alijivuna na kutaka kuwa juu ya Mungu Isaya 14;12-14 Yesu alimuona akianguka kutoka mbinguni Luka 10;18, si vema mkristo mchanga kuwekwa ju ya mamlaka ya kimaongozi katika kanisa anaweza kuanguka kutokana na  kujivuna au kiburi kwa msingi huo lazima kionngozi wa kanisa awe niu mtu aliye na Muda mrefu wa kutosha katika wokovu ili kwamba mizizi iende chini kwa kiasi cha kutosha kabla ya kuhimili upepo wa umaarufu

UMUHIMU WA KUJITAMBUA:
Kujitambua udhaifu wako;
Inapozungumziwa swala la kujitambua inazungumziwa kujitambua nguvu zako na udahaifu wako  na ni muhimu sana kujitambua udhaifu wako ili kwamaba ujue ni maeneo gani yanahitaji kuyaendeleza  na kutumia mbinu zitakazokusaidia katika kujitia nguvu  mara nyingi madhaifu ya kawaida katika kuhutubia yako katika mazingira makuu matatu.
·        Kuwa na misamiati michache
·        Kutamka vibaya maneno na kushindwa kueleweka
·        Kushindwa kujenga vizuri sentensi
Kwa kawaida matatizo ya jinsi hii yanajitokeza kwa wingi pale mtu anapotumia lugha ngeni lakini hata katika lugha hizi tilizozizoea kuna uwezekana wa matatizo ya aina hiyo kujitokeza kwa msingi huo ili muhubiri aweze kujiendeleza katika  kuwa meneji hodari anapaswa  kuhakikisha yafuatayo moja endeleza ujuzi kuhusu misamiati ili kwamba uwe na ujuzi wa maana ya maneno mengi sana ya kutosha  na anza kuitumia misamiati hiyo, Pili Endeleza uwezo wako wa kutamka maneno kwa kuzungumza na watu wenye ujuzi mzuri wa lugha  na hususani wataalamu na waalimu pia uwe na tabia ya kusikiliza sana vyombo vya habari, mwisho jenga namna ya kuunda sentensi zako vema  hususani katika maeneo ambayo unashindwa kuayatamka vema .

Jaribu kujichunguza mwenyewe.
Socrates Mwana falsafa wa kiyunani  wa zamani sana alisema  lazima ujitambue wewe mwenyewe  yaani ili kuufanyia kazi ushauri huu mzuri muhubiri anapaswa  kujifanyia uchunguzi wa kila unachokizungumza jifanyie uchunguzi mwenyewe jinsi unavyoona mambo na unavyowerza kuyaelezea  katika kujijadili wenyewe tutapata ukweli kujihusu hisia zetu  na jinsi tunavyojifahamu  na hapo ndipo tunapoweza kuweka malengo ambayo tunaweza kuyafikia kwa kujibadili sisi wenyewe  na ndipo tunaweza kuamua namna tunavyoweza kuendeeleza kujitoa katika hali ya udhifu kuelekea kwemnye kufanikiwa kuliko kukubwa kwa mfano ukimwambia mtu kuwa siwezi atakuifikiri kuwa huwezi lakini ukimwambia mtu unaweza naye ataanza kukufikiri kama mtu unayeweza  kwa msingi huo tufikie uwezo wa kutamka kamainavyotupasa kutamka.

Jifunze maswala yahusuyo namna ya kuhutubia.
Ili mtu aweze kuongeza uwezo wake katika kujieleza  anapaswa kujifunza  na kuendeleza uwezo wake wa kujieleza katika jamii, watu wengi sana wana  tatizo la kushindwa kujieleza  vizuri mbele za watu  hususani tunapokutana na watu au kutakiwa kukabiliana na kundi la watu na kujieleza, kumbuka kuwa kile tunachokisema na namna tunavyosema  ndivyo vitakavyotuamulia kukubalika kwa wengine kwa wakristo kuna uwezekano usitakiwe kusimama mbele za watu na kuzungumza na hadhara lakini kwa kuwa tuna ujumbe muhimu wa injili tunatakiwa kuwa tayari kwani kwaajili ya ujumbe tulio nao tutajikuta tunatakiwa kuupeleka kwa wengine hili linapaswa kututia moyo katika swala la kujifunza  kwa bidii kuwa wazungumzaji wazuri kwa kususdi la kuieneza injili.

Jifunze kuwa Jasiri au kujiamini.
Kama unataka jamii iamini kile unachokisema unapaswa kujiamini wewe mwenyewe, ujasiri au kujiamini sio jambo tunalprithi linahitaji kujifunza na eneo la kujifunza ni katika maisha yetu ya kila siku tunapoingiliana na watu, Fikiri vema kabla hujazungumza, hakikisha kuwa uko sahii  kasha zungumza kwa kujiamini  na wakati mwingine fanya zoezi la kuzungumza mahali pa siri kabla ya kuzungumza na hadhara, Unapokuwa mbele ya hadhira sio wakati wa kuamua nini cha kukisema na namna ya kusema kwa sababu wakati huo unahusika  na usemaji nah ii itakupa ujasiri na hadhira itahisi ujasiri wako.

Kujua kile kinachotarajiwa pia humpa mnenaji ujasiri
Muhubiri anapaswa kujua kuwa ni aina gani ya watu atazungumza nao, ukumbi gani atautumia kuzungumza na mahali atakapozungumzia na aina ya vyombo utakavyotumia kama ni vyombo au bila vyombo kujua maswala kadhaa ya mahali unapokwenda kuzungumza kutakupa ujasiri wakati wa kuzungumza.

Kuhusiana na wapi unakwenda kuzungumza
§  Pata habari za kutosha kuhusu ukumbu au chumba unachokwenda kuzungumza
§  Simu ya mtu ambaye anahusika na eneo unalokwenda kuzungumza na maelekezo kuhusu
§  Muda unaotakiwa kutumika kutoka ulipo mpaka katika eneo unakotakiwa kuzungumza

Kuhusiana na jamii ya watu unaokwenda kuzungumza nao
§  Historia ya jamii hiyo na jinsi walivyo
§  Mambo wanayopendelea na mshikamano walio nao
§  Idadi ya watu unaokwenda kuzungumza nao.

Kuhusiana na vyombo wanavyokwenda kuvitumia
§  Aina ya vyombo
§  Aina ya vyombo vya dharula
§  Aina  ya vipaza sauti kama ni vya waya au visivyo na waya
§  Ujuzi kama hutuba itakuwa inarekodiwa au haitarekodiwa
Si kila wakati utakuwa na ujuzi wa maswala haya yote na kadiri unavyokuwa na ujuzi kuhusu maswala hayo ndivyo na ujasiri wa namna ya kuzungumza unavyoongezeka, fahamu pia wale utakaokuitana nao na wale utakaotambulishwa kwao, Haklikisha kuwa umavaa vizuri kwa aajili ya matukio husika  na jiandae vema kwaajili ya ujumbe utakaoupeleka.
Wahubiri wengi sana wanaogopa kusimama katika mimbari kwa msingi huo basi ni muhimu kuchukua mazoezi ya kutosha kuhusu kuhutubu na maandalizi ya kutosha juu ya ujumbe unaohusika  haya yatakusaidia kupunguza hofu ya mimbari hata kama ni mara yako ya kwanza au ndo unaanza kazi ya kusimama mbele ya hadhara, lakini pia unaweza kufanya kazi ya kujiendeleza kiakili kuhusu  namna ya kundaa hali kiakili ya kuweza kupunguza hofu ya kusimama mbele ya hadhara
1.       Umeaalikwa au kukaribishwa kuhudumu kwa sababu una kitu cha ziada ambacho watu wanataka kukisikia kutoka kwako
2.       Ujumbe wako  ni wa muhimu sana  na ni zaidi ya namna unavyopaswa kuzungumza kwa sababu ya umuhimu huo hamu ya mtiririko wa kuukamilisha na kuufikisha kwa watu ndio lengo lako kuu
3.       Fahamu kuwa ni kawaida kwa kila mtu kuwa na hofu mwanzoni  unapoanza kuhutubu
4.       Hofu imezungumziwa sana kiasi cha kutiwa chumvi hivyo ipuuzie
5.       Unapo kuwa na uzoefu wa kuzungumza na kujiandaa kwa umakini sana na kuwa na ujuzi na somo lako utashangaa jinsi kazi ya kusimama katika mimbari inakuwa rahisi siku hadi siku

Jionyeshe kuwa una uwezo wa kufanya mambo vema
Unapokuwa unazungumza na watu kwa kawaida wakati huo huo ndio unajifunua utu wako kwao, kwa mfano endapo mnenaji anawaangalia wasikilizaji wake moja kwa moja  ina wasaidia wasikilizaji wake  kuwa mnenaji anazungumza kweli  au ni mkweli na unaposhindwa kuwaangalia usoni wanahisi kama unawadanganya kuwatazama wasikilizaji ni muhimu kwaajili ya sababu kubwa tatu
·         Kwanza wasikilizaji wanaona ya kuwa unajihushisha nao.

·         Pili macho yanazungumza kama jinsi ambavyo sauti inazungumza na viungo vingine
·          Macho yanakusaidia kutambua muitikio wa wasikilizaji wako na kuona kama wanaguswa au wanahisi kupotezewa muda , wamechanganyikiwa au wamekasirika  au wanakubaliana nawe
Mnenaji wakati wote anapaswa kuhakikisha kuwa anakuwa yeye ili kuepuka kuonekana ni kama muigizaji, wakati huo huo ni muhimu kwa mnenaji kuhakikisha kuwa ana orodhesha kwa mpangilio kile anachotaka kuwasilisha kwa jamii au wasikilizaji na wakati mwingine ili kile unachotaka kukisema kiweze kueleweka vema inakupasa kuweka mada yako katika mtindo wa maswali na majibu au unaweza kuielimisha jamii yako kwa mpangilio wa kutafuta kutatua tatizo lilioko kwa mfano

-          Zungumzia tatizo unalotaka kulitatua katika mfumo wa swali
-          Onyesha kweli kuhusu tatizo lenyewe
-          Onyesha njia za kutatua tatizo hilo
-         Tumia njia zinzoonekana kuwa suluhisho la tatizo
-         Fanya tathimini ili kuona kama njia iliyotumika kutatua tatizo inaweza kufaa kutumika tena ka tatizo kama hilo

Njia nyingine ya kujifanyia tathimini ni kuruhusu mijadala kutoka kwa jamii
Lakini kabla ya kufanya hilo ni muhimu kujiuliza mswali kadhaa yafuatayo
-          Je mchango kutoka kwa wasikilizaji unaweza kusaidia kusahihisha makosa?
-          Je mchango kutoka kwa wasikilizaji utaweka mambo sawia au utakuchanganya zaidi?
-          Je mchango kutoka kwa wasikilizaji utaleta vichekesho, vituko aui utaumiza?
-          Na kwa ufupi je mchango wao uatakuwa ni wenye kujenga au kubomoa?
Endapo utaridhika na matokeo yanayoweza kusababishwa na wachangiaji kutoka nje yaani katika jamii  basi sasa unaweza kuunda kundi hilo la kujadili na  yafuatayao yanaweza kufanywa na kiongozi wa mjadala

-          Anzisha mjadala
-          Waweke wahusika katika kujua mada husika
-          Chagua kweli kadhaa na kuzibainisha  kuhusiana na mada
-           Mpe kila mwanachama nafasi ya kushiriki mazungumzo
-          Saidia kutatua matatizo na kuepusha migogoro
-          Hitimisha kwa mukhtasari maendeleo ya kundi
Kwa kufanya mambo hayo hapo juu utakuwa umesaidia kukuza uwezo wa kufanya mambo na kujieleza mbele ya watu na wakati huo huo kuwa na uwezo wa kufanya mabo mengi kwa ubora.

Kuza uwezo wako wa kushawishi.
Wanenaji hodari na wakubwa duniani  ni wale ambao wamejifunza kuwa na uwezo  wa kujieleza kama walivyo  kwa kumaanisaha  na kujieleza kwa bidii na wengine walikuwa na uwezo kupitia unenaji wao kushawishi hata mambo ya kimataifa
-          Mnenaji mmoja aliyeitwa Savonarola  alitoa ujumbe wa kimapinduzi uliowafanya raia walioasi waovu katika karne ya 15 kubadilika na kuwa raia wema
-          Mnenaji Churchill alizungumza kwa hutuba yenye kuchochea kumwaga damu, kutoka jasho na kulia machozi  kwaajili ya taifa lake wakati wa vita vya pili vya dunia
-          Wanenaji hawa baadhi ya misemo yao imekuwa ni misemo ya kimapinduzi kwa miaka mingi hata leo kwa sababu ya unenaji wao wenye kuvutia , kutia moyo  na kutoa hoja za nguvu
-          Mnenaji aliye hodari kumbe anaweza kabisa kutoa hoja ambazo zinaweza kuishawishi  jamii na taifa  na kusababisha mageuzi lakini unenaji dhaifu unadhoofisha ushawishi wa mnenaji 

Hakikisha kuwa unatoka vizuri kulingana na mazingira
Unapokuwa umevaa vema na unatoka kuhutubia watu unakuwa na mvuto sana kwa watu kutaka kusikia kile unachokiwakilisha  hii ikiwa ni pamoja na namna unavyojieleza kwa msingi huo lazima muhubiri ujali nam,na unavyo vaa  kama utavaa vibaya hata kama una ujumbr mahususi si rahisi watu kuweza kuukubali au kupokelewa vema , unapovaa vibaya unakaa vibaya kirahisirahisi unadhgaraulika na hivyo kuufanya ujumbe wako pia usionekane wa maana utafiti unakubali kuwa wanenaji wanaovaa vizuri wana nafasi kubwa ya  kusikilizwa kuliko wasiojali wametoka vipi.
      
                      
Pichani anaonekana mnenaji mwenye madai ya kuwa na ujumbe Yesu anakupenda na kukujali sana lakini namna alivyotokea inasikitisha na kutatisha tamaa kiasi cha kuwafanya wapokeaji kuwa na mashaka kama Mungu anawapenda.

AMRI KUMI ZA MUHUBIRI WA BIBLIA
Utangulizi 
Abrahamu Lincon alikuwa ni Raisi wa Marekani  ambaye  alijipatia sifa kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwaachia huru watumwa wakati mmoja alisema “Ninavutiwa na muhubiri ambaye ni kama nyuki anayeuawa” kinachomvutia Lincon haikuwa kutembea madhabahuni au kuruka ruka  lakini muhubiri ambaye anahisia za ndani kwa kile anachokihubiri yaani  Passion
     Mama mmoja kikongwe alimwambia muhubiri mmoja mara baada ya kumaliza kuhubiri kwamba mchungaji nimehisi maumivu ya roho yak oleo asubuhi, ulimwengu unaambatana na muhubiri ambaye anahisia kali dhidi ya kile anachokihubiri , kwa maana hivyo Mchungaji au muhubiri anapaswa kuhubiri ujumbe ambao yeye mwenyewe unamgusa sana , vinginevyo  ujumbe huo hautakuwa na ushawishi kwa mtu yeyote Mtu mmoja Adam Clarke alisema “Jifundishe mwenyewe kufa klisha jiombee mwenyewe kufufuka” hili ni jambo la msingi sana Muhubiri ni lazima ahisi kile anachokihubiri ili kiweze kushawishi.

Amri kumi za Muhubiri.
1.       Onyesha ujasiri
Biblia inasema usiogope uwe na moyo mkuu Yoshua 1;9  Kila mtu anapatwa na tatizo la hofu hususani linapokuja swala la kusimama mbele za watuSauli alikuwa hivyo kabala ya kuwa mfalme, inaonekana pia Timotheo alikuwa hivyo 2Timotheo 1;7, lakini kwa kuwa Mungu amekuchagua kuwa mnenaji na kwa kuwa una kitu kwaajili ya watu usiogope kinene Matendo 13;15.
2.       Uwe safi na uvae vizuri.
Watu watahukumu aina ya ujumbe ulionao na jinsi ulivyo kama unatokea Porini au unahubiri porini basi si neno baya ukivaa kama Yohana mbatizaji, lakini kama unataka watu wapokee ujumbe wako vema unahitaji kuvaa vizuri si lazima mavazi yawe ya thamani sana , lakini yawe mavazi safi nay awe yamepigwa pasi
3.       Uwe na mikao mizuri
Ni muhimu kuhakikisha kuwa unakaa vizuri na unasimama vizuri hasa unapokuwa madhabahuni usikae kama mtu anayepunga upepo au mtu anaye jidai ukiwa umeweka mkono mfukoni na kusimama mbele ya madhabahu, hakikisha unasimama vema mabega yanakaa sawasawa na tumia miguu yote miwili wakati unasimama madhabahuni usifanye kama jamaa huyu katika kielelezo chini 


Usihubiri huku ukiwa umesimama kwa mguu mmoja kama mtu aliyeegamia mti Tumia kwa kivuli au aliyepanda daladala na kukosa siti.mikao ya aina hii huweza kueleweka vibaya na wasikilizaji wako, aidha si vema kuweka mikono mfukoni swala hilo linaweza kuonekana kama unajidai hususani hapa Afrika.

4.       Iheshimu madhabahu
Usikohoe kwa kubanja, au kutoasauti za kukoroma , kupnga kamasi au kuchokoa Pua, au kitendo chochote kigeni kinaweza kuondoa usikivu kwa utendaji wako madahabahuni, unaweza kufanya hayo unapokuwa umeketi  au inapokutokea fanya kwa neema na kuomba radhi kwani kumbuka watu wanakuangalia aidha kumbuka kuwa mpole madhabahuni usipande madhgabahuni kwa kiburi.

5.       Tumia sautuiyako vizuri
Sauti ni kama vyombo vya muziki inaweza kuwa laini na inaweza kuwa na kelele, inapendeza kuzungumza kwa saiuti kubwa kama kuna watu 20,000 lakini kama una watu 20 tumia sauti ya kawaida, Spergion alisema “sauti kubwa yenye kelele  haina nguvu kwani hugeuza majheshi ya maneno kuwa maneno ya kikundi yasiyo na maana” maana yake ni kuwa wakati mwingine maneno yenye maana katika ukurasa hupigiwa mstari ili kuonyesha umaana wake lakini kama maneno ya ukurasa mzima umepigiwa mstari maneno hayo hayana maana tena. Sivema kuanza na sauti kubwa na kuendelea nayo Muhubiri 10;10  kama chuma hakinoi itakusa kutumia nguvu kubwa zaidi., si kila wakati sauti kubwa ni sauti ya Mungu 1falme 19;11-13 kwa hiyo hata kama unahubiri polepole lakini kama maneno yako yana nguvu na upako yatasaidia kufikisha ujumbe.

6.       Tamka maneno yako vizuri
Maneno yako ndiyo ya muhimu na ya maana sana na ndiyo yanayotakiwa kusikiwa na watu hivyo ni muhimu yakitamkwa kwa ufasaha na vema zaidi Mathayo 5;2 Akafunua kinywa chake akawafundisha,  usizungumze na kusikika kama Nyuki, zungumza maneno yako wazi tamka vema  na acha nafasi kila unapokuwa umezunghumza neno uziyaunganishe kama charahani na wakti huo huo  epuka kutumia maneno ya kujazia “Gape filler” yaani maneno yenye kutafuta kujazia nafasi unapokuwa umekosa cha kusema  maneno haya ni kama vile Bwana asifiwe, haleluya n.k  na ni muhimu maneno hayo yakatumika mahali husika panapo mtukuza Mungu sio “Yuda akaenda akajinyonga Bwana asifiwe”!

7.       Tumia vema vihisisho muafaka
Ni muhimun kuhubiri bila ya kutumia vihisishi kuliko kuvitumia mahali ambapo sio muafaka, kwa mfano baadhi ya wahubiri huonyeha mikono lakini haiendani na kile anachokihubiri maana yake kama unaonyesha mbinguni juu basi mikono yako ionyeshe ju na sio vinginevyo kumbuka mwili unawasiliana.

8.       Zungumza kwa kutumia mikono.
Pampja na matumizi sahii ya mikono sio vema kutokuitumia mikono na kuamua kusimama kama askari, tumia mikono yako unapozungumza katika maeneo ya kuuliza msawali, kuheshabu, kuhaidi, kubariki, kuhairisha, kukaribisha, kukubali, kuonyesha furaha au huzuni n.k. sehemu nyingine za mwili zinasaidia kuonyesha muhubiri anahubiri nini lakini mikono ni zaidi.

9.       Kumbuka kuwa watu wanaangalia uso wako.
     Watu wataupokea ujumbe wako vema kama uatakuwa una uso laini wa kuliko uso mgumu, watu wengi hawapokei ujumbe kwa muhubiri mwenye uso wa jiwe, uso wa aina hiyo unachosha sana uso wa aina hii unatewngeneza hali ya kupingwa wakati wote, unaweza kusema maneno magumu bila kuwa na uso mgumu kwa msingi huo uwe mcheshi na uonekane mwenye kukubalika zaidi kuliko kuwa mgumu.
10.   Waangalie watu unaowahubiri.
Wako wahubiri wengine hawaangalii watu wanapohubiri utawaona aidha wanaangalia chini au juu tu , au wanazungumza na mahubiri yao yaliyoandikwa kwenye karatasi au kuiangalia Biblia tu  kwa ujumla hili sio jambo jema  hakikisha unawaangalia watu wako kwani macho yaweza kufanya m,akosa mengi wakati wa kuhubiri
Hakikisha kuwa unafanya bidii kuzingatia kanuni hizi kumi za muhubiri na hakikisha kuwa unawafurtahisha watu na ndipo, itakuwa vigumu watu makosa kwani wnafgurahishwa nawe hata kama una udhaifu kimwili basi hakikisha kuwa unanguvu katika ujumbe wako 2Koritho 10;10.



SURA YA PILI: MUHUBIRI NA VYANZO VYA MAHUBIRI

Utangulizi

Kila muhubiri anajua kuwa anapaswa kuhubiri lakini swala la kuchangua au nini cha kuhubiri huwa ni jambo gumu sana kwa wahubiri wengi, lakini inatupasa kulihubiri neno 2Timotheo 4;2 lakini ni sehemu gani ya kuhubiri  hapo ndipo inakuwa shughuli

     Kila mchungaji mwenye uzoefu anajua kuwa inapofika siku ya jumamosi na huku bado hujapata ujumbe au hujui nini cha kuhubiri  presha inakuwa juu sana  na shughuli ya kuchagua nini cha kuhubiri linakuwa swala gumu sana  hasa ikiwa hujui ni nini utakisema jumapili, katika baadhi ya madhehebu  huwa wanaaandaa mahubiri  ya kila juma pili na hivyo inakuwa rahisi kwa wachungaji wa madhehebu hayo kuwa na Muda wa kupumzika na  kulala vizuri usiku wa jumamosi, Swala hilo lina faida Fulani kwani muhubiri anakuwa na amani na inamsaidia namna ya kupangilia ujumbe wake 

Lakini kwa namna nyingine Mchungaji anapaswa kuwa wazi kwa Roho wa Mungu, katika somo hili pia nitakusaidia kupata kanuni kadhaa za kukusaidia kupata ujumbe na masomo mazuri kwaajili ya mahubiri yako

Masomo na mada
 Ni muhimu kufahaku kuwa hutuba nyingi zinzzohutubiwa na watu hususani za kibiblia  zinagusa maeneo muhimu  kama nane tu,  ambayo ni watu na vitu, maeneo na matukio, michakato na mawazo, matatizo na mipangoau suluyhisho
·         Kuhusu watu na vitu
Katika biblia tumebarikiwa kuwa na hadthi za watu mbalimbali kama Ibrahimu, Isaka na Yakobo au Yusufu, manabii kama Yeremia, Isaya na Daniel na nyingi ya hizi hadithi ziko katika Agano la kale na kwa kuzingatia kuwa kuna nukuu za kila aina ya hadithi katika Agano jipya pia na unapotumia itifaki ya Biblia utaweza kuona hadithi nyingi sana kupitia majina ya watu na maandiko yao wengi wa watu hao wana mabo mazuri na mabaya ambayo tunaweza kujifunza

§  Ibrahimu mfano katika Waebrania 11;8
§  Isaka mfano katika Wagalatia 4;28
§  Yusufu mfano katika Waebrania 11;22
§  Isaya mfano katika Marko 7;6-7
§  Yeremia mfano katika Mathayo 16;13-14
§  Daniel mfano katika mathayo 24;15

 Kwa hiyo kumbe kupitia watu tunaweza kupata jumbe mbalimbali za kutufunza mambo kadhaa katika Biblia  na pia tunazo habari za kina Stefano, Petro, Paulo Yesu na wengineo wengi ambao tuinaweza kujifunza vitu kutoka kwao, wengine walikuwa na maadui kama Eliya na Yezebel, wengine walikuwa mashujaa na walikuwa na madhaifu yao n.k haya yote ni ya muhimu kwaajili ya kutufunza sisi, wengi wa waliotajwa katika bilia walikuwa ni watu halisi na habari zilikuwa halisi ispokuwa katika baadhi ya mifano vingine vilitungwa kwa kusudi la kuleta somo Fulani hii hasa ni katika mifano , hadithi nyingine sio nzuri lakini ziko kwaajili ya kutufunza sisi kufanya vizuri na sio kurudia makosa yale,
Vitu pia vina sehemu kubwa katika kutufundisha  wanayama , ni vitu, Pepo ni vitu kwa mfano Yesu alitumia mfano wa maua ya mashambani Mathayo 6;28 kuweza kuwasilisha somo lake kuhusu kujali kwa Mungu.

·         Maeneo na matukio
Wakati mwingine kuna matukio yanayotajwa pamoja na maeneo au maeneo na matukio ya maeneo husika mara nyingi hutajwa pamoja katika maandiko haya nayo hutusaidia kupata vitu vya kutufundisha na vya kuhubiri mfano Yeriko na swala la ukuta Yoshua 6, Babel na swala la mnara Mwanzo 11;1-9, mlima wa faragha na Badiliko la Yesu Mathayo 17;1-8, anguko la mwanadamu na Bustani ya Edeni, Kana na muujiza wa maji kuwa Divai haya yote hutusaidia katika kupata jumbe za kuihubiri yaani maeneo na matukio

·         Michakato na mawazo
Michakato ni hatua zilizopitiwa au zilizofanyika kuonyesha jambo Fulani lilivyoweza kuja kutokea kuna aina hoiyo ya habai nyingi sana katika Biblia mfano Imani chanzo chake ni kusikia Warumi 10;9 na Matendo 2;38 , aidha kuna wazo la upendo wa Mungu, kuwekwa huru,  maadili n,k na maandiko yako kama Yohana 3;16, Ufunuo 6;10,16;5 zinazungumza kuhusu Mungu.

·         Tatizo na mipango
Kwa sababu watu wote hupatwa na matatizo mara nyingi basi ni muhimu kufahamu kuwa wakati mwingi jumbe zetu zitakuwa na malengo ya kuondoa matatizo yanayowakumba watu   baadhi ya matatizo hayo ni kama Dhambi, Magonjwa, vita matatizo ukimbizi, uchafuzi wa mazingira, umasikini, rushwa, kukoseka na kwa haki, dhuluma  na matatizo mengineyo chungu nzima
Sasa kama unahitaji kutatua matatizo hayo inakupasaa kuwa na mipango nah ii itakulazimu kupanga jumbe katika mtindo unaohusika na kushughulika na tatizo moja baada ya jingine

KANUNI KUMI ZA KUKUSAIDIA KUPATA JUMBE

Unapaswa kujitoa kila siku Daily devotions
·         Kila siku unapojitoa katika kuisoma Biblia na kuomba Roho wa Mungu anakuwa na kitun  cha kusema nawe hiki ni mbegu ya kuweza kukupatia au kustawisha ujumbe  na unapokuwa na Muda wa kutafakari ujumbe huo unakua na kama mchungaji unakuwa na shughuli kuliko kawaida ni ngumu kwako kupokea jumbe kutoka kwa Roho wa Mungu hivyo uinapaswa kubadili mwenendo

Unapaswa kuisoma Biblia yako kila siku
·         Kumbuka kuisoma Biblia yako mara kwa mara na unaweza kuisoma kwa mpangilio maalumu usiisome hovyohovyo, soma kifungu mara nyingi  katika njia tofauti toafauti , soma kwa kujiuliza maswali ili upate kuilewa   mfano mwandishi ni nani, walengwa ni akina nani, neno kuu ni lipi, tatizo kuu ni lipi na majibu ya tatizo hilo ni yapi yalitolewa  kisha ombea kile ambacho umekisoma kisha jitahidi kuelewa kile ulichokisoma 

Unapaswa kuwasoma watu wako
·         Baadhi ya jumbe zinapatikana kwa kuwasoma watu wako, wahubiri wanapaswa kuwasoma watu wao kama vile wanavyoisoma Biblia  ni makosa kujua watu waliishije nyakati za kanisa la kwanza kisha tukashindwa kuwatambua watu ambao tunaishi nao hakuna mtu anaweza kuwa mkweli kwa Biblia kama atashindwa kuyatumia  kwa watu husika tulio nao leo.

     Neno la Mungu lili tolewa kwa wanadamu na sio wanadamu kwa neno  Mahubiri yote mazuri ni yale yanayohusu tatizo la mwanadamu na kutoa suluhisho la Kiungu kutokana na neno la Mungu katika Biblia unapowasoma watu wako utyajua kuwa ni jumbe gani zinapaswa kuhubiriwa, jumbe hizo ni lazima zitokane na neno la Mungu  ingawa uvuvio kuihusu  ni ni cha kuhubiri unatokana na unavyowaona watu, huitaji kusikia sauti kama radi ili kujua kuwa Mungu anataka nini  kama unaona liko hitaji kwa watu huitaji kutafuta jambo lingine.

Epuka kuhubiri jumbe zenye utata
·         Ujumbe wowote ambao hauko wazi kimaandiko ni muhimu kujitahidi kuepuka kuhubiri jumbe hizo baadhi ya jumbe zenye utata wa kitheolojia katika Biblia ni pasmoja  na
Ø  Ubatizo wa wafu 1Koritho 15;29
Ø  Tofauti kati ya ufalme wa Mungu na ufalme wa mbinguni ingawa tunajua kua ni jambo moja
Ø  Malaika walioasi wasioilinda Enzi yao 2Petro 2;4
Ø  Malaika Mikaeli kugombania mwili wa Musa Yuda 1;9
Ø  Yesu kuhubiri Roho zilizokuwa kifungoni 1Petro 3;19
Jumbe hizi ni jumbe ambazo zina utata unaweza kuchangia wazo Fulani kuhusu lakini uzizifanye kuwa ni ujumbne wa somo
·         Ujumbe wowote ambao hauwezi kufanya kazi katika nyakati zetu  au katika jamii yetu mfano wa jumbe hizo ni kama
Ø  Salimianeni kwa busu takatifu
Ø  Kuvunja chombo cha dongo kilicho najisi Walawi 15;12
·         Ujumbe wowote ambao hautafasiri maandiko kwa halali.
Ø  Watu wanaotumia  vibaya Mithali 6;2 kukiri mambo mazuri tu Possitive Confession si kila wakati mafundisho hayo ni sahii
Ø  Biblia wakati mwingine inatutaka tuungame makosa yetu Yakobo 5;16, udhaifu wetu 2Koritho 12;9-10. Lkukosa kwetu hekima Yakobo 1;5 na kuugua kwetu Yakobo 5;14
Ø  Andiko linguine litumikalo vibaya ni pamoja na Yohana 11;26 Yeye aishiye na kuniamini mimi hatakufa kabisa andiko hili Yesu alikuwa akizungumzia Maisha ya kiroho Yesu alionyesha wazi kuwa tutakufa Yohana 16;1-3, 21;1
Chagua viini vikuu
Si vibaya kwa mchungaji kuhubiri jumbne za aina mbalimbali kwa msingi huo unaweza kuwa na masomo mengi na ya aina mbalimbali kulingana na aidha kuhubiri kuhusu misingi ya imani ya kipentekoste au imani ya kanisa mfano tunaamini katika maswala yafuatayo na kila swala ni somo au mafundisho unaweza kufundisha kuhusu mambo kadhaa yafuatayo
·         Maandiko yamevuviwa
·         Mungu mmoja wa kweli
·         Uungu wa Yesu Kristo
·         Anguko la mwanadamu katika dhambi
·         Wokovu wa mwanadamu
·         Maagizo makuu ya kanisa
·         Ubatizo wa Roho Mtakatifu
·         Ushahidi kuhusu ujazo wa Roho Mtakatifu
·         Mafundisho kuhusu Utakaso
·         Mafundisho kuhusu kanisa na wajibu wa kanisa
·         Mafundishoi kuhusu Huduma
·         Mafundisho kuhusu Tumaini lenye Baraka
·         Mafundisho kuhusu utawala wa miaka 1000 ya Kristo Duniani
·         Mafundisho kuhusu hukumu ya mwisho
·         Mafundisho kuhusu mbingu mpya na inchi mpya
Unaweza pia kuhubiri kuhusu, majaribu, maombi, msamaha, uwakili wema, kutembea kwa imani, namna ya kushinda hali ya kukata tamaa, tamaa, kuupenda ulimwengu, kuwa makini, matendo mema, Ndoa na nyumba na mengineyo mengi.
Hubiri kutoka katika Agano la kale pia
Baadhi ya wahubiri na wachungaji  hawalitendei haki agano la kale katika kuhubiri kwao, tunapaswa kuhubiri pia kutoka katika agano la kale  lakini hatupaswi kuhubiri kana kwamba tuko chini ya sheria za agano la kale wanaweza kuhubiri kutoka katika agano la kale mfano Kumbukumbu 28;7 wakati Biblia inasema katika Mathayo 10;23, si kila wakati adui atatukimbia kuna wakati inatupasa sisi kukimbia kwa maana hiyo muhubiri anapaswa kuwa na ujuzi wa kutosha katika somo linalohusu jinsi ya kutafasiri na kutumia kwa ahalali maandiko Hermeneutics, Wako wahubiri wengine wana lipuuzia kabisa agano la kale hawalihubiri kabisa, Agano jipya lina nukuu 1100 kutoka katika agano la kale, waamini wanapaswa kujifunza mambo mengi kutoka katika agano la kale wanapaswa kujua kuhusu
·         Habari ya uumbaji
·         Vivulikuhusu Kristo (Typology)
·         Masomo mbalimbali kuhusu watu wa agano la kale
·         Mambo makuu katika Zaburi
·         Hekima mbalimbali kutoka kwenye Mithali
·         Maswala ya manabii na unabii
·         Kanuni kadhaa za maisha kama amri kumi.
Endapo mchungaji au muhubiri atayazingatia hayo ataweza kuwa na masomo mazuri na mahubiri mazuri na hatakosa kitu cha kusema na kuhubiri kwa watu wake maandalizi ya mapema kuhusu jumbe kama hizi zitamfanya mtumishi wa Mungu kuwa na ujasiri wa kutosha anapokuwa anatoa hutuba
Kanuni nne za mwishoni zinauhusiano na mipango wakatiwa wa utoaji wa hutuba
Hakikisha kuwa unatoa mlo kamili.
     Ni muhimu kufahamu kuwa wako watu ambao hujifanya kuwa wanaongozwa na Roho lakini wakati huo huo wanapingana na maswala ya kupangilia jumbe, wanasahahu kuwa Roho wa Mungu naye anauwezo wa kuwasaidia katika kupanga namna watakavyo hubiri jumbe zao, kuto kuwa na mipango katika namna ya kuhubiri au jumbe za kuhubiri kunakuweka katika hali ya kujaribiwa kuhubiri jumbe zilezile na hapo ndipo inapokuwa sawa na kuwalisha watu wa chakula cha aina ileile inaweza kutushangaza kuwa inakuwaje mtu anayeongozwa na Roho Mtakatifu akashindwa kuongozwa kupangilia jumbe Roho wa Mungu aliweza kumpa Isaya jumbe kuhusu kuzaliwa kwa masihi miaka 750 kabla, Kanisani na chuo cha Biblia ni wapi pa kiroho zaidi?  Kwa kunena kiwazimu chuo cha Biblia ni pa kiroho zaidi, kwa sababu ndipo mahali panapoandaa wale wanaokuja kuchunga makanisa lakini katika vyuo vya Biblia Masomo hupangwa mapema kabla, na kama waalimu watashindwa kufanya maandalizi mapema basi kuna uwezekano wa kushindwa kufundisha masomo muhimu, kwa hiyo mipango ni muhimu, pamoja na kufunga na kuomba na Roho wa Mungu atatupaka mafuta tukipanga tunapanga na Roho Mtakatifu

Uwe na mipango kwaajili ya sikukuu
 Kila sikukuu inaweza kumsaidia muhubiri kuwa na somo kwa mfano kila sikukuu ya krismasi tunahubiri kuhusu kuzaliwa kwa masihi, pasaka tunahubiri kuhusu kufufuka kwa Yesu Kristo na kila sikukuu kama za uhuru na nyinginezo tunaweza kuwa na ujumbe maalumu wa sikukuu hiyo, kumbuka kuwa ni kiroho kupanga  kuwa na mipango kwaajili ya Mungu ni kwa muhimu sana Luka 12;13-21 watu wa jinga ni wale walio na mipango ya maisha bila Mungu, Yesu alihubiri au kufundisha maswala mengine kwa sababu alijua wanafunzi wake wanawaza nini Mathayo 20;20-28

Pangilia jumbe zako katika mtiririko unaofaa.
 Ni muhimu kuwa na mpangilio wa jumbe ambao una wiana unaweza kuwa na masomo kuhusu karama za kiroho 1Koritho 12 – 14. 

Kumbuka kufuata uongozi wa Roho Mtakatifu
Ni muhimu kupangilia jumbe zetu mapema lakini ni muhimu kupanga na Roho wa Mungu  au tunapokuwa tumepanga tuwe watu laini ambao tunaruhusu Roho wa Mungu kuingilia kati kile tulichokipanga  soma Matendo 16;9-18;28 mipango ni mizuri kama tutaruhusu Roho wa Mungu kupanga pamoja nasi

 AINA ZA MAHUBIRI (HOTUBA).

Ni muhimu kufahamu kwamba kuna malengo kila wakati mtu anapokusudia kuhubiri na kutoa hutuba iwe ya kawaida au ya Kibiblia, Kila aina ya mahubiri au hutuba ina makusudi, katika makusudi ya mawasiliano wasomi wamegawanya makusudi ya mahubiri au hutubia katika maeneo makuu Manne na ambayo ni Kufurahisha, kuelimisha au kujulisha, kushawishi na kuchochea, kila moja ina makusudi yake kama nitakavyo yaainisha wakati wa kuichambua moja baada ya nyingine

1.       Kufurahisha (to entertain).
Kufurahisha ni moja ya makusudi ya msingi ya hotuba aina hizi za hutuba hutolewa nyakati za  chakula cha jioni, kwenye sherehe kama harusi au wakati watu wana hisia za kuchoka au  wakiwa wamenuna  au kwa makusudi mengine madogo madogo bali wakati mwingine pasipo kuwa na sababu Hotuba hizi si nzuri sana katika msimamo wa Kikristo kwa sababu kila kitu katikia ukristo kimemaanishwa na hatuna muda wa mzaha  kwa msingi huo aina hizi za hutuba zinapotolewa katika mtazamo wa Kikristo  zinapaswa kulenga wakati huo huo jambo muhimu la kweli la kiroho na pia wakati wakristo wana pokuwa katika koinonia za kifamilia za kanisa au wakati wa mapimziko na kadhalika 

2.       Kuelimisha au kujulisha (to inform).
Aina hizi za hutuba wakati mwingine huitwa hutuba za kufunua mambo au jambo Expository speech kwa sababu inajengwa katika mfumo wa kutoa wazo kama unapofundisha darasani, au mijadala au muhubiri anapoelimisha kuhusu jambo Fulani, aina hizi pia hutolewa na kamati mbalimbali kwaajili ya kutoa taarifa Fulani ambayo imefanyiwa uchunguzi na kamati na wajibu wa kushughulikia utakuwa ni wa jamii husika,Ni muhimu kufahamu kuwa pia unapomtambulisha mtu aina hiyo ya hutuba inaweza kuangukia katika kundi hili au unapomuelekeza mtu au kuzungumzia maswala ya utalii kwa lengo la kutangaza, na pia unapochanganua vifungu Fulani katika maandiko yaani Biblia na kuvifanya kueleweka kwa wahusika  aina hizo za hutuba ni za kuelimisha au kujulisha. 

3.       Kushawishi (to Parsuade).
Ni hutuba zenye mlengo wa kushawishi katika hutuba kama hizi unatakiwa kutumia hoja ya nguvu logic  na kuinua hisia za watu, hutuba kama hizi hutumiwa zaidi na wainjilisti au wanasiasa wanapokuwa katika kampeni lakini hata wachungaji huzitumia aina hizi za hutuba  wanapokuwa wanawaita watu kuokoka, au kuchochea utoaji kwaajili ya jengo au jambo fulani kusudi hasa ni kuhitaji mwitikio wa mkutano  kukubaliana na muhubiri aina hizi za hutuba pia hutumiwa na wafanya biashara  au wakati wa kampeni ili kushawishi wapiga kura  au katika mtindo wa maandalizi kwaajili ya kuwa kiongozi baadaye, inaweza kutumika katika kushawishi uwekezaji na maswala mengineyo lakini kumbuka kusudi letu hapa ni hutuba za kibiblia. 

4.       Kuchochea (to actuate)
Aina hizi za hutuba hazina malengo ya kuushawishi mkutano kuona kuwa jambo hili ni zuri au baya  hapa unachojaribu kukifanya ni kuwafanya wafanye katika mtazamo wa kikristo aina hii ya hutuba inataka mtu ajikabidhi ajitoe afanye mfano Mathayo 4;19 Nifuateni nami nitawafanya ninyi kuwa wavuvi wa watu, hili ni jambo la kimaisha ni la kudumu ni la kila siku kwa hivyo wanafunzi walipoambiwa hivyo walitakiwa kuacha kila kitu na kutekeleza kile alichokisema na kukitenda kristo  aina hizi za hutuba kwa wakristo ni njema na zenye matokeo mazuri, kwa jamii ya kawaida aina hizi za hutuba  zina makusudi ya aidha kuwafanya watu waache au kupigana vita (mfano uwezo wa kumpiga tunao nguvu za kumpiga tunazo sababu za kumpiga tunazo tunataka dunia ituelewe hivyo) na mara nyingi hufanyika maamuzi ya muda mfupi wakati ya kikristo ni ya maisha yote.

Hotuba za kimatukio (Speech for Ocasions)
 Hizi ni hutuba zinazo husiana na matukio mbalimbali mfano Kukaribisha (Courtesy), na za kukubali makaribisho, hutuba za utambulisho introduction, hutuba za kutambua mchango wa mtu au kumuaga Tribute na kadhalika kwa kawaida hotuba za aina hii huwa ni fupi na sio ngumu sana  ingawaje ni za muhimu kwa watumishi kujifunza na kuwa na Ufahamu wa aina hizo za hutuba .

Hotuba za kukaribisha (Courtesy)
Kwa kawaida aina hii ya hutuba inapaswa kuwa yenye uzuri  na yenye kumfanya mgeni kukubalika kwa watu wanaomsikiliza inaweza kuwa mgeni wa kikristo au hata asiye mkristo lakini hilo halimfanyi mkristo kuwa sio mkaribishaji mzuri na kama umechaguliwa kwaajili ya kutoa aina hiyo ya hutuba ni muhimu  kwa mtoaji wa aina hiyo ya hutuba kujiuliza maswali yafuatayo kwaajili ya maandalizi

·         Kwa nini nitatoa hutuba hii?
·         Kwa kina nani ninatoa hutuba hii?
·         Je ninajua sifa gani kuhusu mtu nitakayemtambulisha au mtu ninayemzungumzia?
·         Je nitawakilisha vipi umuhimu wa  wa tukio hili la kihutuba
·         Hakikisha kuwa unatumia lugha nzuri badala ya kutoa maoni yako kuhusu mtu huyo na wakati huo huo hakikisha kuwa unapata usikivu wa kutosha kutoka kwa watu, watosheleze watu kuhusu utambulisho wako, wape picha ya kile wanachotarajia kukipata si lazima hatua hizi zizingatiwe kila wakati utakapotoa hutuba ya aina hii.

AINA ZA JUMBE ZA KIBIBLIA
Kuna aina nyingi sana za jumbe za kibiblia za kuhubiri kwa ujumla kuna aina kuu kama Nane za ujumbe ingawa tatu tu za jumbehizo hufundishwa sana katika vyuo vya Biblia.  Hebu kwanza tuziangalie jumbe zote kisha tutazungumzia zile ambazo hutumiwa sana katika vyuo vingi vya Biblia na kukaziwa sana

Aina za jumbe
·         Ujumbe unaotokana na andiko Textual Sermon
·         Ujumbe wa somo au mada Topical Sermon
·         Ujumbe unaotokana na alama kivuli kuhusu Kristo na mengineyo typical Sermon
·         Jumbe za vifungu zinazofunua kweli za kibiblia Expository Sermon
·         Jumbe kuhusu maisha ya watu Biographical Sermon
·         Jumbe za kuchimba na kuchanganua somo kwa undani Analytical Sermon
·         Jumbe za kuoanisha mambo au kulinganisha Analytical Sermon
·         Ujumbe wa kuchambua mstari kwa mstari, sura kwa sura na kitabu kwa kitabu Runing commentary Sermon.
Jumbe kuu ambazo huubiriwa sana hutumika sana na kusisitizwa sana katika vuyuo vya Biblia ziko Tatu kati ya hizo ni
1.       Ujumbe wa somo au mada Topical Sermon
2.       Ujumbe unaotokana na andiko Textual Sermon
3.       Jumbe za vifungu zinazofunua kweli za kibiblia Expository Sermon

Ujumbe wa somo au mada topical sermon
Huu ni ujumbe unaotokana na somo au wazo au kichwa ambacho aidha muhubiri anaamua au Roho wa Mungu anampa wazo  na baadaye unalipanga wazo hilo katika migawanyo yake Bila kutegemea mistari au kifungu cha kibiblia, somo lenyewe au wazo lenyewe ndio huwa kiini cha somo husika ujumbe wa somo hauitaji mstari kutoka katika Biblia kama kiini cha kuanzia bali unahitaji wazo la jumla la kibiblia  na ambalo litaungwa mkono na maandiko mbalimbali ya kibiblia  jumbe hizi hubeba kiini kimoja ambacho huwa kama mada  mtu anapokuwa anataka kuuzungumzia  kwa msingi huo basi ujumbe wa somo au mada unaweza kujengwa kwa mawazo mabalimbali na kisha yakawa na umbile toka katika maandiko mbalimbali ya Biblia mawazo hayo ni kama
-          Maana ya maombi
-          Nguvu ya maombi
-          Umuhimu wa kuomba
-          Matokeo ya maombi
-          Jinsi ya kuomba
-          Mifano ya watu waombaji
-          Maombi ya kufunga na kuomba
Kwa hiyo hapo somo kuu ni maombi lakini hata hivyo kila mgawanyo unaweza kuwa somo au unaweza kuwa somo au mada na ikazungumziwa kwa muda mrefu wa kutosha kwa hiyo wazo ni maombi lakini ndani yake unapata mambo mengi kuhusu maombi na yako maandiko mengi pia ya kutumia katika kufundisha juu ya maombi
Tatizo kuu la ujumbe wa somo ni kuwa ni rahisi kuisingizia Biblia kusema kile ambacho haija kisema au kutumia maandiko mahali ambapo si halali kwa andiko hilo kutumika na kwa sababu hiyo kukiuka kanuni za kutafasiri maandikokwa halali hata hivyo ni nzuri kwa watu wenye mapenzi mema, aina hii ya ujumbe hufananishwa na mbuzi ambaye hana kamba anakuwa huru kula kokote anakotaka kula.
Mfano wa ujumbe wa somo

SOMO: JINSI YA KUOMBA
Mstari wa Msingi Luka 11;1 “Ikawa alipokuwa mahali Fulani akiomba , alipokwisha mmoja katika wanafunzi wake alimwambia Bwana tufundishe sisi kusali kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake”
Mara tu baada ya mtu kuokoka  na kufanyika mtoto wa Mungu Yohana 1;12  inakuja shauku na hamu  kubwa ya mtu huyo kutaka kuwasiliana na Mungu aliye baba yake  wa Mbinguni. Mawasiliano hayo yanafanyika kwa njia ya maombi, Yesu kristo kiongozi mkuu wa wokovu wetu waebrania 2;10 alikuwa mwombaji mkuu, Alfajiri na mapema sana alikuwa anakwenda mahali pasipokuwa na watu  akawa anaomba Marko 1;35 Jioni pia alikuwa akifanya maombi Marko 6;46-47 wakati mwingine pia alikuwa akifanya maombi usiku kucha  Luka 6;12  Yesu alichukua muda mrefu wa kuomba mpaka akalia sana na machozi Waebrania 5;7 , hakukubali kutingwa sana na shughuli na kukosa muda wa kuomba, wakati mwingine hata katikati ya kilele cha shughuli zake  alikuwa akijiepusha  na kwenda mahali pasipokuwa na watu na kuomba Luka 5;15-16 wakati mwingine aliomba mpaka hari yake  au jasho lake likawa kama matone ya damu  yakidondoka katika inchi Luka 22;44 Mara nyingi aliwaambia wanafunzi wake waombe ili wasiingie majaribuni  halafu yeye akajitenga mbali kidogo nao na kuendelea kuomba , wanafunzi wake walipojaribu kuomba waliishiwa na maneno hata ikawa kwao vigumu kuomba hata kidogo Luka 22;39-41 Mathayo 26;40-41 na ndipo wanafunzi wake walipoona ni vema kumuomba awafundishe jinsi ya kuomba ni makusudi ya somo hili sasa kujifunza jinsi ya kuomba , Yesu kristo alikuwa muombaji na alikuwa ni kielelezo chetu Mtu awaye yote aliyeokoka hawezi kufika mbali katika wokovu wake kama  akiwa sio muombaji tutajifunza somo hili jinsi ya kuomba kwa kuzingatia vipengele vitano vifuatavyo
·         Mikao inayofaa kwa ajili ya maombi
·         Swala la kuomba kwa sauti kubwa
·         Swala la kuomba kwa kufumba macho au kufumbua macho
·         Umuhimu wa kuomba kwa jina la Yesu.
·         Matumizi ya sala ya Bwana katika Maombi

Mikao inayofaa kwa ajili ya maombi.
Wako watu wengi sana wanaofikiri kuwa wakati wote mtu anapotaka kumuomba Mungu ni lazima awe amepiga magoti, hii sio sahii kwani tunaweza kumuomba Mungu katika mikao tofauti tofauti  katika namna nyingine pia kutegemea na nafasi, Kupiga magoti ni jambo linalimfurahisha Mungu sana  wakati wa kuomba Isaya 45;23. Lakini hata hivyo kuna njia nyingi za kibiblia za jinsi ya kuomba zifuatazo ni baadhi ya njia zilizomo kwenye Biblia
a.       Kupiga magoti – Tunaona mifano katika Luka 22;41Yesu, Katika Daniel 6;10 Daniel, katika Zaburi 95;6 Daudi, katika Matendo ya mitume 7;60Stefano, katika Matendo 9;40Petro na katika  matendo 20;36,21;5 Paulo mtume na watu wengine.
b.      Kupiga magoti na kukunjua mikono kuelekea mbinguni – Mfalme Sulemani katika 1Wafalme 8;54, 2Nyakati 6;13, na pia Ezra kuhani katika Ezra 9;5.
c.       Kuinamisha kichwa  Mwanzo 24;26,Kutoka 4;31, 12;27 na 34;8
d.      Kuanguka kifulifuli uso kugusa Ardhi - Tunaona mfano wa Yesu Mathayo 26; 39. Yehoshafati 2Nyakati 20;18 Eliya 1wafalme 18;42,Yoshua katika Yoshua 5;14,Musa   na Haruni katika Hesabu 20;6
e.      Kusimama – Marko 11;25,Luka 18;11
f.        Kusimama na kukunjua mikono kuelekea mbinguni – 1Wafalme 8;22
Hizo zote hapo juu ni njia zinazo faa kwaajili ya kumuomba Mungu ni mazingira tu ndiyo yatakayoamua njia gani itumike, kwa mfano huwezi kupiga magoti ukiwa stendi ya mabasi au katika kanisa lisilo na sakafu Lakini kama mazingira ni mazuri na yanaruhusu kupiga magoti kufanya hivyo sio tatizo Daniel 6;10, wala sio busara kugusa uso chini mpaka utoke sugu ili watu wajue kuwa wewe ni muombaji maombi ya jinsi hii ni ya kinafiki Mathayo 6;1-5, Biblia inatufundisha kuwa mambo yote yatendeke kwa  uzuri na kwa utaratibu 1Koritho 14;40 kwa msingi huo inatupasa kuchagua  ni wapi na ipinjia ipi inafaa  na kuitumia kwa mfano ukiwa una usingizi ukapiga magoti ili kuomba ni rahisi kulala usingizi hapo njia sahii ni kusimama na kutembea huku unaomba itakusaidia kutokulala unaona.

Swala la kuomba kwa sauti kubwa
Kumekuwako na utata wa kitheolojia kuhusu kuomba kwa sauti kubwa ikifikiriwa kuwa kufanya hivyo ni kupayuka payuka kunakotajwa katika Mathayo 6;7-8 lakini tafasiri hiyo sio halali katika Biblia ya kiingereza King James Version ambayo ni tafasiri iliyo karibu na lugha za asili zilizoleta Biblia kwetu kiibrania na kiyunani Mathayo 6;7  husomeka hivi “But when ye pray use not vain repetitions as the heathen do” kwa msingi huo kupayuka payuka ni kurudia rudia maneno yale yale  kama kasuku  hii ilifanywa na mataifa kwa sababu hawajui kuomba  hawana maneno mengi ya kutosha kujieleza mbele za Mungu. Hivyo kuomba kwa kupaza sauti sio kupayuka Biblia imejaa mifano ya watu wengi ambao waliomba kwa kupaza sauti na hata kulia sana machozi kama alivyofanya Bwana Yesu Biblia inatoa ushauri wa kufanya hivyo
Waamuzi 2;4,21;21Samuel 30;3-4 Mithali 2;3-6 zaburi 77;1 Matendo 4;24  kuomba kimya kimya au kwa kupaza sauti kote ni sawa mbele za Mungu nako pia kunategemea na mzingira, kwa mfano sio busara kufanya hivyo kwenye nyumba ya kupanga  au mahakamani ukiwa kizimbani au wakati mumeo anayepinga wokovu akiwa chumbani anakusikia ukimuombea Niokoe na Mume huyu mkaidi anayepinga wokovu n.k. maswala kama hayo ungeweza kuyaomba kimyakimya Mathayo 7;6.

Swala la kuomba kwa kufumba macho au kufumbua macho.
Swala la kufumba macho au kufumbua ni swala linalohusiana na maswala ya kisaikolojia  kwa Mungu hakuna sharti Yeye huweza kuwasiliana na mwanadamu hata akiwa amelala usingizi kwa njia ya ndoto, na hii haina maana kuwa ukifumbua macho ndo kuna kitu utakiona  wakati mwingine mtu anaweza kuona maono akiwa amefumbua macho  na macho hutumika kuyaona maono hayo  lakini roho zetu huitwa zimezimia kwani tunakuwa hatuko katika hali ya kawaida  Matendo 10;9-12 wakati mwingine kufumbua macho kunaweza kusababisha kuingiza picha au mambo ambayo yatatutoa katika kuzingatia mwelekeo wetu kwa Mungu kwahiyo hili nalo ni swala la kisaikolojia na kimazingira kwa mfano kama unaendesha gari unaweza kuomba lakini sio kwa kufunika macho

Umuhimu wa kuomba kwa jina la Yesu.
Kuomba kibiblia ni kuomba kupitia jina la Yesu hili ni jambo la muhimu namna yoyote ya kutumia vitu vilivyochongwa au kutengenezwa kwa shaba, mbao, dhahabu , fedha n.k  na kuvisimamisha kati yetu na Mungu  na kuviangalia wakati wa kuomba na kuvitaja , kuvitumia, kuviangalia au kuvitafakari  na kufikiri kuwa vitafanikisha sala zetu hiyo ni ibada ya sanamu ambayo ni  machukizo makubwa mbele za Mungu Kutoka 20;4-5,1Yohana 5;21,1Wakoritho 10;14 Isaya 31;7, Sanamu yoyote au lozari na vitu vyote vya jinsi hiyo siyo sehemu ya maelekezo ya jinsi ya kuomba katika Biblia , Mungu ni Roho nao wamwabuduo au kumuomba wanapaswa kumuabudu katika roho na kweli na siyo kwa kutumia kitu chochote kinachoonekana Yohana 4;23-24, aidha ni muhimu kufahamu kuwa kuwaomba wafu pia ni chukizo kubwa mbele za Mungu Kumbukumbu 18;9-12, kuwaomba watakatifu ambao wamekwisha kufa kama Petro, Yohana, Paulo, Bikira Maria, Yusufu .n.k watuombee sio sahii kibiblia kila mmoja anapaswa kuomba mwenyewe na kuzungumza na Mungu kwa jina la Yesu na ukifanya hivyo anakusikia na kupokea dua zako, 

Kila mtoto wa Mungu ana haki sawa kabisa na mwenziwe anapoomba  kila aombaye hupokea Yohana 16;24, Luka 11;9-11 Biblia inaonyesha kuwa ni wawili tu wanaotuombea  hao ni Yesu Kristo na Roho Matakatifu nao hufanya hivyo bila sisi kuwaomba watuombee 1Yohana 2;1 Warumi 8;26-27 Tukifanya jinsi neno la Mungu linavyotuongoza na kulitii ndipo tutakapofanikiwa katika njia zetu Zaburi 119;9, aidha ni muhimu kufahamu kuwa kuwaombea wafu pia siyo sahii Biblia inasema katika Waebrania  9;27 kuwa mtu amewekewa kufa mara moja tu na baada ya kifo ni hukumu, tunaweza kuomba kwa ajili ya wale walio hai ili waokolewe kabla hawajafa lakini inapotokea mtu amekufa hakuna kinachoweza kubadilika 1Yohana 5;14-16

Maombi yetu ili yaweze kuwa na mafanikio inatupasa kumuomba Mungu baba kwa kupitia jina la Yesu Yohana 16;23, sio maelekezo ya Biblia kumuomba Mungu kupitia Mariam  kwa mawazo potofu eti ukipitia kwa mama wa Mungu  ndio utajibiwa kwa sababu kina mama wana huruma  ni muhimu kufahamu Kua Maria kamwe sio mama wa Mungu Mungu hana mama wala Baba hana mwanzo wa siku zake wala mwisho wa siku zake  hali kadhalika kwa Yesu Kristo hivyo hivyo Waebrania 7;3 Yesu hakuanzia maisha yake tumboni mwa Mariamu  yeye alikuwepo hata kabla ya Ibrahimu hajazaliwa Yohana 8;58, Yesu ndiye aliyeufanya ulimwengu Waebrania 1;2 katika Yesu kila kitu kiliumbwa  Wakolosai 1;13-17 Yeye ndiye aliyemuumba Musa Waebrania 3;1-4 na pia ndiye aliyemuumba Maria  na watu wote, aliyeumbwa hawezi kuwa mama wa aliyemuumba Biblia inaonyesha kuwa Maria mwenyewe alihusika katika kumuomba Mungu  pamoja na wanafunzi wa Yesu Matendo 1;4,12-14 Bikira Maria kamwe hawezi kujiita mama wa Mungu kinyume chake alijiita mjakazi wa Bwana  yaani mtumwa wa kike wa Bwana Biblia inasema katika Luka 1;38 “Mariam akasema Tazama mimi ni mjakazi wa Bwana” 

Matumizi ya sala ya Bwana katika Maombi
Mathayo 6;9-13 Yesu Kristo alipowafundisha wanafunzi wake kuomba aliwaelekeza kuomba kwa misingi inayojulikana kama sala ya Bwana, kimsingi hakuwa anamaanisha waitamke kama ilivyo na kuimaliza kama kasuku kama watu wengi wanavyofikiri , Biblia inaposema katika Mathayo 6;9 “Basi ninyi salini hivi baba yetu uliye mbinguni……” Tafasiri ya kiingereza ya King James Version inasema “After this manner therefore pray Ye” tafasiri ya kiingereza ya LIVING BIBLE inasema Pray alon these lines” Katika Luka 11;2 kwa msingi huo kinachozungumzwa hapa ni kuwa sala ya bwana ni mafundisho ya msingi ya kutumia katika maombi, kilichozungumzwa ni kuomba kupitia misingi hii kila tunapotaka kuomba Luka 9;54 Mathayo 20;20-22 Kutamka sala ya bwana kama ilivyo ingeweza kuchukua dakika mbili tu na isingelikuwa suluhisho la kufundisha maombi ambao wao walikuwa wakitaka kujifunza kuomba kwa muda mwingi wa kutosha  kama alivyokuwa akiomba Bwana Yesu  vinginevyo Yesu hangeshangazwa na wanafunzi wake kulala usingizi ikiwa sala Yenyewe ingeweza kuchukua dakika chache. Mafundisho mengi aliyokuwa akiyatoa Bwana Yesu Mara nyingi yalikuwa yakihitaji ufafanuzi Mathayo 13;36, na pia mafundisho ambayo wanafunzi waliweza kuyaelewa leo yanahitaji ufafanuzi  Mathayo 13;51 Mengine ambayo yalikuwa magumu kueleweka kwa wanafunzi kwa mfano habari za kuteseka kufa na kufufuka sio tatizo kubwa kueleweka leo Marko 9;30-32, Luka 24;44-45 na ndio maana kanisa linahitaji waalimu ambao wanaweza kufunuliwa na Roho wa Mungu  Neno lake ili kulilisha kanisa 1Wakoritho 2;10.

JINSI YA KUOMBA KWA KUTUMIA SALA YA BWANA.

Baba yetu uliye mbinguni.Mathayo 6;9.
Tunapokuja kumuomba Mungu inatupasa kufahamu kuwa Yeye ni baba yetu, kama unaweza kuwasiliana na baba yako wa duniani  anayejishughulisha na  na mahitaji yetu na kuyajali  ni muhimu kufahamu kuwa Hatupaswi kumuomba Mungu tukidhani kuwa yuko mbali ni lazima tuweke mawazo yetu kuwa Mungu ni baba yetu na kuwa yuko karibu mno tunapomuomba Zaburi 145;18,Zaburi 119;151 103;13 Fahamu kuwa ni baba mwenye upendo mwenye uwezo anayejishughulisha  sana na mambo yetu 1Petro 5;6-7  hatupaswi kufikiri kuwa yeye hatujali Zaburi 37;28 Isaya 49;14-16,1Wakoritho 10;10. Aidha uhusiano wetu na Mungu lazima uwe wa baba na mwana maana yake kama hujazaliwa mara ya Pili huwezi kuwa na uhusiano wa aina hiyo.

Misingi Saba ya kufuata katika maombi yetu Kama alivyotufundisha Yesu Kristo
1.       Jina lako litukuzwe Mathayo 6;9.
Maombi yetu yanapaswa kuanza kwa kumtukuza Mungu na kumsifu si busara kuanza kumimina shida tulizo nazo  mtukuze Mungu kwa uweza wake na uumbaji mfano Zaburi 104;5-28, mtukuze kwa wingi wa Rehema na huruma zake Zaburi 103;8 na pia unaweza kumtukuza kwa matendo yake makuu aliyokutendea Zaburi 106

2.       Ufalme wako uje Mathayo 6;9 Baada ya kuokolewa ujue kuwa umetolewa katika ufalme wa giza  au utawala wa shetani  hivyo inakupasa kuwakumbuka wengine omba watu waokolewe katika taifa lako, ombea wale wasio na mafundisho na kuombea kazi ya Mungu ikiwa ni pamoja na Bwana wa mavuno kupeleka watenda kazi katika kazi yake Waebrania 12;14 Mathayo 9;37-38.1Wakoritho 10;24,Wafilipi 2;4 Warumi 15;1

3.       Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni Mathayo 6;10 mapenzi ya Mungu kutimizwa  ni watu kuishi sawa na Neno lake tumuombe Mungu kwaajili ya serikali na wanaotawala duniani 1Timotheo 2;1-4,Mithali 21;1 ombea lolote lililo kinyume  na mapenzi ya Mungu  lililotawala duniani mambo kama rushwa, vita, njaa uonevu, kuzuia Neno la Mungu, kuenea kwa uislamu n.k

4.       Utupe leo riziki Yetu  Mathayo 6;11 Ni mapenzi ya Mungu baba yetu kuwa kila mtoto wake apate riziki yake kila siku  kuna riziki za aina nyingi  Afya Marko 7;25-27, Yeremia 30;17, 33;6 Chakula nguo  nazo ni aina za riziki Zaburi 37;25,1Timotheo 6;8 zaburi 34;10 pia unaweza kuomba kwaajili ya mahitaji ya wengine  na mahitaji mengine

5.       Utusamehe Deni zetu kama sisi nasi tunavyowasamehe wadeni wetu Mathayo 6;12  Deni zinazozungumzwa hapa ni makosa au dhambi  Luka 11;4  katika maombi Mungu anatutazamia tuangalie mahali tulipomtenda dhambi kwa kuwaza kusema na kutenda  kwani dhambi ni kizuizi cha maombi  lakini wakati huohuo tunapaswa kuwasamehe wengine au kupatana na watu tuliokosana nao Luka 17;4 kwani kama hatujasamehe  dhambi zetu pia zinakuwa ngumu kusameheka Mathayo 6;14-15.

6.       Na usitutie majaribuni lakini utuokoe na Yule mwovu kwa kuwa ufalme ni wako na nguvu na utukufu hata milele Mathayo 6;13, ni muhimu kufahamu kuwa Mungu hamjaribu mtu Yakobo 1;13-14 lakini shetani hatuwazii mema watu wa Mungu na ndiye ambaye anazunguka huko na huko akitafuta mtu ammeze 1Petro 5;8  Kwa kuwa Mungu ni mwenye nguvu zote inatupasa kumuomba atuokoe na mipango ya shetani  Luka 10;18-19Mathayo 18;18,Daniel 10;11-13 Kemea mipango yote ya shetani juu ya watu wote na kanisa pia kazi ya Mungu  na namna yoyote ya kuwazuia watu wasilielekee Neno la Mungu.

7.       Amina Mathayo 6;13 Neno hili amina maana yake ni na iwe hivyo, baada ya maombi amini kuwa imekuwa sawasawa na kuomba kwako Marko 11;24 Hivyo mshukuru Mungu kwa imani kwamba umepokea uliyoyaomba 1Thesalonike 5;18 Endelea kuwa mtu wa maombi Yeremia 33;3 penda pia kuwa mwenye kushiriki siku za maombi kanisani ambako uatajifunza kutoka kwa watu wenye uzoefu mkubwa wa kuomba na kupata changamoto. Mithali 27;17.

Ujumbe unaotokana na andiko Textual Sermon
Huu ni aina ya ujumbe ambao unatokana na maandiko yaani mistari kadhaa katika Biblia ambayo kitaalamu haipaswi kuzidi aya tatu, kichwa na migawanyo ya aina hii ya ujumbe hutokana na andiko hilo aina hii ya ujumbe ni nzuri na pia maandiko mengine sio mengi sana huweza kutumika katika kujenga au kuongeza nyama kwa aina hii ya ujumbe Aina hii ya ujumbe hufananishwa na Mbuzi mwenye kamba ndefu anakula kwa uhuru lakini sio mkubwa kama wa mbuzi wa ujumbe wa somo.
Mfano wa ujumbe wa andiko
Andiko Ezra 7;10
Ujumbe Moyo wa mtumishi wa Mungu
Somo makusudi ya moyo wa Ezra
1.       Alikusudia kulijua neno la Mungu, kila mtumishi wa Mungu anapaswa kuwa na moyo wa kujifunza kama ilivyokuwa kwa Ezra, huwezi kuwapa watu vitu, huwezi kuwa mwalimu mzuri huwezi kuelimisha watu au kufundisha somo lako kwa ujasiri kama hujajifunza kwanza Ezra alikuwa ni mafno wa kuigwa
2.       Alikusudia kutii yaani kulitendea kazi neno la Mungu, Matendo 1;1, 1Koritho 11;1 Ni vigumu kuwaambia watu kufanya jambo ambalo wewe hulifanyi  ili uweze kufanikiwa katika kuhudumu kwako ni lazima wewe mwenyewe kwanza uwe kilelelezo cha kutosha watu husoma zaidi matendo kuliko maneno Ezra aliamua kutenda kwanza Yesu alisema utoe boriti kwanza kabla ya kuondoa kibanzi katika jicho la ndugu yako
3.       Alikusudia kuwafundisha watu wa Mungu, Kristo ametuagiza kuwafanya mataifa yote kuwa wanafunzi wake na kuwafundisha kuyatii yote aliyo tuamuru, lakini kabla ya kuwaagiza wanafunzi wake kuifanya kazi hiyo yeye mwenyewe alikaa nao na kuwafundisha wao kwanza na ndio maana Ezra alijifunza kwanza kabla ya kuanza kuwafundisha wengine.

Sisi nasi inatupasa kuiga mfano wa Ezra katika maisha yetu ya kila siku Mungu akubariki
Aina za jumbe za andiko zinahitaji  kusoma kile kifungu ili ukielewe kwanza , Ufahamu historia ya wakati ule  na kuangalia nini kinahitajika leo ndipo ufanye Exegesis  na kutoa maana iliyofichwa katika lugha za wakati ule uvilete katika matumizi ya wakati huu  na kutumia hatua hizi pia zinahitajika kwa ujumbe wa Expository.

Jumbe za vifungu zinazofunua kweli za kibiblia Expository Sermon
Jumbe za aina hii mara nyingi huruhusu Biblia kujieleza yenyewe  na ndio ujumbe wenye kufanikiwa kwa juu kabisa kuhubiri kusudi la Mungu kwa wasikilizaji ni ujumbe ambao unachambua kifungu cha maandiko kwa kutafuta maana iliyokusudiwa na mwandishi kisha na kisha kuutumia kwa wakati ulioko katia ujumbe huu ni rahisi kwa muhubiri kushughulika hasa na kusudi la Mungu  ujumbe huu mara nyingi ni tofauti na textual yaani ujumbe wa andiko huu unagusa kifungu kizima  na kuanza kuzamisha kwa kuifunua kweli hivyo hufananishwa na Mbuzi mwenye kamba fupi lakini hula kwa kuzama chini zaidi aina hizi za jumbe ndizo zenye uwezo mkubwa kabisa wa kulifanya kanisa kukua na kuwa na ujuzi wa matumizi ya kweli kuhusu neno la Mungu kwa hiyo inasisitizwa kutumiwa zaidi makanisani na kokote.

Mfano wa ujumbe wa kifungu cha maandiko ni
                 SOMO;   UMUHIMU WA KUTUNZA UWEPO WA MUNGU
Mstari wa somo; 1Samuel 4; 12-22.
UTANGULIZI;
        Katika mistari hii tuliyoisoma  tunagundua habari zakusikitisha sana katika Historia ya Israel ambazo hazijawahi kutokea na huenda tukio hili linakumbukwa sana katika matukio yanayopaswa kukumbukwa, Israel walipigwa vibaya katika vita na wafilisti,  waliona njia pekee ya kuleta ushindi katika maisha yao ni kulileta sanduku la agano la Mungu katika uwanja wa vita na watu walishangilia sana maana chombo hiki muhimu na kitakatifu sana kilikuwa kinawakilisha Uwepo wa Mungu Asiyeonekana chombo hiki pia kilikuwa ndio moyo wa Ibada zao katika hema na Hekalu,  Sanduku la agano liliwakilisha uwepo wa Mungu ambaye ana historia ya kuleta ushindi dhidi ya maadui wa Israel hivyo hata inchi jirani ziliogopa sana maadui waliogopa waliposikia chombo hiki kinaletwa katika uwanjawa vita, kwani walijua yaliyotendeka kuanzia Misri na  sehemu zote ambazo Israel walipitia na kwa kweli kote ilikuwa ni ushindi katika kisa hiki kuna mambo muhimu ya msingi ya kujifunza kama ifuatavyo;-

·         Umuhimu wa kuutunza uwepo wa Mungu
·         Hasara za kuupoteza uwepo wa Mungu.
·         Kumlilia Mungu kwa ajili ya uwepo wake.

*      Umuhimu wa uwepo wa Mungu  Mstari wa 18a-,19
     Ujuzi wa mke wa Finehasi kuhusu uwepo wa Mungu unaonekana ulikuwa juu kuliko watu woote haiyamkini kuwa mwanamke huyu alikuwa mcha Mungu hata pamoja na kuwa mumewe alikuwa muovu, Yeye alifahamu kuwa sanduku kuchukuliwa mikononi mwa wenye dhambi hakuikuwa kitu cha kawaida katika Israel wote tunajua kuwa Eli alikufa ghafla aliposikia sanduku limetwaliwa, Mwanamke huyu naye aliingia katika hali ya kufa na kuzaa kwa uchungu ghafla kwa kusikia sanduku limetwaliwa  ikatika adhabu ambazo ni kubwa kuliko zote ni kutengwa na uwepo wa Mungu  Mwanzo 4;9-14, Kaini alijua kuwa uwepo wa Mungu ni ulinzi mkubwa sana na kuwa kama mtu atatengwa mbali na uwepo wa Mungu kifo ni halali yake, Daudi alijiombea alipokuwa anatubu dhambi zake katika Zaburi ya 51;11, alitambua jinsi uwepo wa Mungu ulivyokuwa wa Muhimu katika maisha yake,Musa alimwambia mungu yakuwa uwepo wako au uso wako usipokwenda pamoja nasi usitutoe kutoka mahali hapa ( Kutoka 33;1-4,14-15. ) uwepo wa Mungu pia uliitwa utukufu wa Mungu mwanadamu anapopungukiwa na utukufu wa Mungu.

*      Hasara za kuupoteza uwepo wa Mungu mstari wa 20-21.
Ujuzi wa mke wa Finehasi kuhusu sanduku la agano kwa baadhi ya wanawake wa Israel ulikuwa Tofauti wao walitafuta kumfariji kuwa jipe moyo  mkuu Usiogope maana umezaa motto mwanamume, wao walijua kuwa wanaweza kumtia moyo kwani hata kama mkwewe amekufa,mumewe amekufa Lakini alitakiwa ajipe moyo kwani yuko mtoto mwanamume huenda alikuwa mtoto wake wa kwanza na huenda angeendeleza kazi ya ukuhani kwani babu yake na baba yake walikuwa wamekufa hivyo alikuwa mtoto wa muhimu sana  Lakini mkewe finehasi aliona kuwa motto huyo hakuzaliwa kwa wakati unaofaa kwani utukufu ulikuwa haupo umeondoka hapa tunajifunza hasira za kupoteza uwepo wa Mungu
Hata kama tutasoma sana, kuwa katika dhehebu kubwa sana kuliko yote duniani au la kwanza  kutoka kwa mitume au tukawa madaktari auy tukaimba sana kama ndege au tukawa makuhani au mapadre au maaskofu wa dini kubwa sana Lakini kama dini hiyo imepoteza uwepo wa Mungu ni ikabodi haiwezi kuiwa na faida yoyote,ndoa zetu,watoto wetu na chochote kile kama uwepo wa Mungu hauko havina maana ni hasira kubwa  Daudi alifahamu kuwa kwa nabii samweli kuna uwepo aliamua kukimbilia huko akawa salama adui wakikutafuta wakijua kuwa umejificha katika uwepo wa Mungu utakuwa salama

*      Kumlilia Mungu kwa ajili ya uwepo wake.mstari wa 20-22
    Jambo la kushangaza na ambalo halikuwa jema kwa mke wa Finehasi  pamoja na kujua kuwa tatizo ni utukufu umeondoka badala ya kumlilia Mungu na kutubu ili uwepo wa Mungu urudi aliamua kufa tu na alikufa kweli wako watu ambao wanajua kuwa kanisa linapita katika hali ya kupoteza uwepo wa Mungu duniani Lakini badala ya kumlilia Mungu ili uwepo urudi nao wanaamua kufa badala ya kumlimlia Mungu na kutubu, wanakubali kuendana na hali halisi ya matukio shetani hata aacha kupigana nasi hata kama tuna uwepo wa Mungu au hauko na hata kama anaujuzi kuwa Mungu ana nguvu haachi kushindana nasi hivyo nasi tusiache kumpiga vita kwa gharama yoyote

UMUHIMU WA KUTUMIA NYENZO KWAAJILI YA MAANDALIZI YA UJUMBE
Kwa kawaida kila muhubiri anapaswa kuwa na nyenzo muhimu ambazo zitakusaidia katika kuandaa maomo ya kibiblia na kwa kawaida uandaaji huendana na utendaji kuhusu kanuni za kutafasiri maandiko hivyo katika kujiandaa pia muhubiri anatafasiri maandiko hivyo kazi hizi huenda pamoja nyenzo hizo ni kama ifuatavyo;-

A.            ROHO MTAKATIFU;
                1.            Ni nyenzo ya kwanza na ya Muhimu sana mtu awaye yote anayetaka kuwa mtafasiri mzuri wa Maandiko ni lazima akubali kujazwa Roho Mtakatifu kumbuka kuwa yeye ndiye aliyevuvia watu kuliandika neno na ni mwalimu anaweza kutukumbusha na kutufundisha kile ambacho Mungu amekikusudia kwetu hivyo lazima mtafasiri wa maandiko awe amejazwa Roho ikiwa wale waliokuwa mashemasi nyakati za kanisa la kwanza walizingatiwa kuwa wenye Roho je si zaidi sana wanaojitia katia kazi ya kuyatangaza Maandiko ona mfano wa Stefano Matendo 6;8-55 kwanini ni muhimu kuwa na Roho Mtakatifu?
                2.            Ni Mtafasiri mzuri
                                (a)          Ndiye Mwandishi wa Biblia  1Kor. 2:10-16, Yoh 14:26, 16:13
                                (b)          Anajua kile Ambacho Mungu anakijua

B.          HAKIKISHA KUWA UNA BIBLIA ZA MATOLEO TOFAUTI
1. Biblia ya Kiswahili na za aina mbalimbali za matoleo ya kiswahili cha kisasa        
                2. English Bible matoleo tofauti                   
3.Zile zilizoandikwa katika Lugha Tofauti Tofauti (Greek, Hebrew, Latin, Aramaic, etc.)
C.          UWE NA UJUZI KUHUSU AINA ZA MATOLEO YA BIBLIA
Kwa kawaida kuna matoleo makuu ya aina tatu za kibiblia zile zilizotafasiri neno kwa neno Literal translations, Zile zilizotafasiri kutokana na maana iliyokusudiwa,Dynamic Equivalent na zile tafasiri huru za lugha za kisasaau matoleo kwa watu maalum Free translation.
                     Literal translations          Dynamic Equivalence translations      Free translations
 

         KJV                  RSV,   Weymoth,                            NIV        JB            TEV,       MOFFAT, PHILIPS, LB
         NASB                                                                            NAB       NEB
                                                                                      NEB  GNB
 

           Neno kwa neno                                           Maana kwa maana                                    Tafasiri huru
B.                   UWE NA BIBLIA ZENYE MAFUNZO NDANI YAKE ; REFERENCE OR ANNOTATED
·         Uwe na Biblia zenye mafunzo Studies Bible Zinatoa maana ya baadhi ya aya:
(i)                  Mfano mzuri ni Full life study Bible (NIV)Biblia ya mafunzo ya uzima tele
(ii)                Life Application Bible (LB)
(iii)               Dake Bible
(iv)              Scafield Bible, etc.
C.                  COMMENTARIES: (Zenye uchambuzi wa mstari kwa mstari).
Baadhi ya Commentaries nzuri ni Pamoja na
               1.             Adam Clarke’s Commentary
                2.            The New International Commentary
                3.           The Evangelical Bible Commentary
               4.           Mathew Henry Commentary.
F.           CONCORDANCES   ITIFAKI
o   Itifaki yenye maneno yafananayo
o   Itifaki za maana ya meneno mfano  Malazi yawe safi -Ndoa
o   Mlinganio wa maneno yanayopatikana katika sehemu nyingine za Biblia.
o   Mfano Upendo upi? – Agape? Phileo? Storge? Eros?
o   Mahali lilipo neno Fulani
§  Mfano wa itifaki nzuri ni pamoja na ;-
                1.            Young’s Analytical Concordance
                2.            Strong’s Exhaustive Concordance etc.
               3.            Niv Exhaustive Concodance.
·         Kumbuka nyingine zina Kamusi za kiibrania na Kiyunani  Lexicons (=Dictionaries ).


Muhubiri asiyetumia nyenzo hutumia muda mrefu kuandaa ujumbe sawa na mtu anayejaribu kukata mti bila ya upanga kama jamaa huyu anayekata mti kwa kutumia nyundo itamgharimu kutumia muda mwingi  na mrefu sana kuliko anayetumia msumeno wa mashine Chainsaw 

B.                   VITABU VINAVYOHUSU TAMADUNI ZA KIBIBLIA & MASWALA YA UCHIMBAJI WA   MAMBO YA KALE
·         Hii itakusaidia kuufahamu na kuwa na ujuzi kuhusu mambo ya kale kama na maneno yaliyotumiwa kama Busu takatifu, Tundu la sindano na mambo mengineyo.
C.                  KAMUSI ZA BIBLIA NA ZA LUGHA ZA KAWAIDA & ENCYCLOPAEDIAS:
Zinafafanua maana ya maneno Mbalimbali kwa ajili ya maswala ya kibiblia na maswala ya kawaida
1.            Kamusi za kawaida ni pamoja na zile za Kiingereza na kiswahili
                (a)          English Language Dictionary
                (b)          Swahili Language Dictionary etc. (Kamusi)

2.            Kamusi za Biblia ni pamoja na zilizo maarufu kama zifuatazo nyingi ni za kiingereza
                (a)          Unger’s Bible Dictionary                                               
                (b)          Pictorial Bible Dictionary                                               
               (c)          Westminster Bible Dictionary                            
                (d)          Greek Lexicon & Hebrew Lexicon                                
3.              Kamusi za kitheolojia (Theological Dictionary).
       Kwa ajili ya kujifunza Mambo mbalimbali ya kitheolojia Mfano ni
1.              Baker’s Dictionary of Theology
4.            Encyclopedias,
                Mfano; - International Standard Bible Encyclopedia

D.                  MAFAFANUZI YA KIBIBLIA (BIBLE HANDBOOKS :)
·         Kwa ajili ya ufafanuzi wa Maswala mbalimbali, Vifungu, Maandiko, Tamaduni, Matukio ya kihistoria,  Ugunduzi wa maswala ya kale (archaeology), na kadhalika
Mfano
                1.            Halley’s Bible Hand Book
               2.           Unger’s Bible Hand Book

I.            MASOMO MBALIMBALI AU JUMBE MBALIMBALI (TOPICAL BIBLE).
·         Vitabu vinavyo weka mpangilio wa ufafanuzi wa masomo mbalimbali vikiwa na maandiko yoote husika sawa  book arranged according to different topics with all the texts related to each topic.
Mfano Nave’s topical Bible
J.             ATLASI ZA KIBIBLIA NA MSWALA YA KIHISTORIA  (BIBLE ATLASS) & HISTORY
Kwa ajili ya kutambua sehemu Mbalimbali na umbali kwa kilomita za mraba n.k na vipimo kama homeri, yadi, mwendo wa sabato, Ridhaa n.k
e.g.         1.            Baker’s Bible Atlas
                2.            The Oxford Bible Atlas
MPANGILIO WA HUTUBA AU MAHUBIRI
Makusudi ya Mpangilio
Karibu kila kitu ambacho tunakifahamu tumejifunza, kila mmoja kuna eneo Fulani hajui  kwa msingi huo si ajabu wanafunzi au washirika wakawa hawajui umuhimu wa mpangilio wa hutuba zao za kibiblia, kusudi kubwa la kupangilia ni ni kuweka mambo yaweze kwenda sawa kila moja ana kabati la nguo au wengi wa watu wana makabati ya nguo au hata masanduku, nguo zilizopangiliwa vema katika kabati ni rahisi sana kuziona na kuchagua ile unayoitaka kuliko nguo ambazo zimemwagwa tu katika kona ya nguo ndivyo ilivyo kwa jumbe zisizopangiliwa
Katika kupangilia unaweza kupangilia kwa kutumia herufi kubwa au ndogo na pia unaweza kutumia namba za kirumi, upangiliaji wa masomo unasaidia ujumbe kuweza kueleweka kulingana na mpangilio wake na mfuatano wa mawazo na ujenzi wa hoja unakuwa ni wenye mvuto kuliko ujumbe ambao hauja pangiliwa katika somo hili inashauriwa angalau ujumbe uonyeshe maeneo kama matano hivi kwa mfano huu utakaoonyeshwa chini mara baada ya maelezo kuhusu mpangilio wa ujumbe
Umuhimu wa kichwa cha ujumbe.
Kila aina ya ujumbe unaohubiriwa ni lazima uwe na kichwa, kazi kubwa ya kichwa cha ujumbe ni kumtaarifu msikilizaji kuwa ujumbe wako unahusu nini? Kichwa cha ujumbe ni kama kibao kinachotoa maelekezo kuwa tunakwenda wapi, lazima kichwa cha ujumbe kiwe na mvuto na kiwe kifupi na kiwe kinajenga mazingira ya watu kutaka kusikiliza kuwa ndani ya ujumbe kuna nini, kwa ufupi kichwa kinatakiwa kuwa ni mukhtasari wa kile ambacho muhubiri anakwenda kukihubiri na kinatakiwa kuwa katika hali nyepesi na iliyowazi hata ikitokea kuwa Muhubiri anakufa ghafla wasikilizaji watajua kuwa marehemu alitaka kuzungumzia nini, wako wahubiri wanaweka kichwa chenye utata sana au kutokuwa na kichwa cha ujumbe kabisa kiasi cha watu kushindwa kuelewa nini kinazungumzwa na wapi wanaenda
Utangulizi
Lengo kubwa la utangulizi ni kupata usikivu wa watu ni kama vile mchungaji amekwenda madhabahuni na mfuko na ndani ya mfuko huo kuna sauti za wanyama mbalimbali kila mtu atakodoa macho ili kutaka kujua  ni nini kimo ndani yake  hii ni kama kusudi la utangulizi, lakini sio tu kupata usikivu lakini pia kupata hamu na shauku ya kutaka au kupenda kile kinachofuata, utangulizi unatakiwa kurudisha akili zao katika somo  na kuwaondoa watu katika hali ya kulipinga neno na kukubali mabadiliko kumbuka kuwa tunahubiri ili kubadilisha maisha ya watu katika maeneo kadhaa mfano
·         Tunawahubiri wenye dhambi ili waokolewe na kumuamini Kristo
·         Tuanawahubiri wakristo ili wawe kama Kristo
·         Tunahubiri ili kubadili mitazamo na tabia mbaya na mafundisho mabaya
·         Tunahubiri kuondoa watu kutoka katika migandamizo, hali za kutokusamehe, kukata tamaa na kuondoka katika hali za uchungu.
Kwa msingi huo utangulizi unaweza kuanza kwa kichekesho, kuuliza swali, kufanya igizo Fulani au kuimba, shuhuda au mfano ili kuwafanya watu wafungue mioyo yao na kupokea ujumbe.


Tatizo linaloshughulikiwa
Ujumbe wa kibiblia unapaswa kujengwa katika misingi ya kuondoa tatizo kulingana na uhitaji wa watu ulioko au kulingana na mawazo ya watu lazima uwe hodari katika kupangilia kwako jumbe ni lazima uwe makini katika kuyachota mawazo ya watu wafanye watu kuwa na kiu ili wanywe maji wenyewe, huwezi kumlazimisha ngombe kunywa maji hata kama unaweza kumpeleka mtoni, lazima ujue kuwa watu wanahitaji nini  kisha utoekitu ambacho watu wale wanakihitaji, kwa mfano kama watu wanaogopa basi hofu inasababisha watu kuweka hela benk, kuweka walinzi kutembea wakiwa na hofu na kadhalika kwa hiyo unaonyesha tatizo la hofu katika jamii kisha kipengele cha suluhisho unatatua tatizo.
Picha zifuatazo zitakusaidia kuona umuhimu wa kufanya kile ambacho watu wanakitarajia na usilazimishe yale unayotaka wewe yawe.Wafanye watu kutamani mahubiri yako na kuwa na hamu na shauku ya kuyasikiliza kila siku kama wafanyavyo watu wanaoandaa vipindi vya tamthilia huandaa katika namana ambayo wateja wao hutamani kipindi kifike ili wakiangalie wahubiri nao wanapaswa kuwa werevu kuliko watu wa michezo ya kuigiza watu watamani wenyewe neno la Mungu na kuhudhuria mahubiri yako bila kuwalazimisha 



Suluhisho.
Katika kutoa suluhu Muhubiri anatoa suluhu ya matatizo husika kwa kuonyesha ni namna gani watu wanaweza kupata suluhu na ni njia gani wanaweza kuzitumia au vitendo gani wanapaswa kufanya, kwahiyo kama wana hofu unaweza kuwaelekeza kuiondoa kupitia maombi au kuwa na mawazo sahii na kutokuogopa ua kumshukuru Mungu na kadhalika na unaweza kutoa mifano
Matokeo
 Hapa muhubiri anaonyesha matokeo ya ujumbe wake endapo utafanyiwa kazi kwa mfano kwa swala la hofu Unaweza kuonyesha jinsi ambavyo utakuwa huru kutoka katika hofu na hautaogopa tena  na kuwa utatembea kifua mbele
Mwaliko
Muhubiri anachokifanya hapa ni kuwafanya wasikilizaji wake kukutana na Mungu kivitendo na kuwaombea ili wapokee neema ya kutoka katika tatizo walilo nalo Hapa muhubiri anaweza kuomba na wale wenye hofu ya kupita kawaida  na kuwafungua kwa maombezi ili waweze kuwa huru kutoka katika hofu.
Mpangilio wa ujumbe sasa unaweza kuonekana katika mtazamo huu
Kichwa cha ujumbe.
Hatua ya kwanza.  I. Utangulizi
Hatua ya pili.          II. Tatizo unaloshughulikia
A.      Kweli kuu
1.       Mfano kuhusu kweli kuu
2.       Mfano kuhusu kweli kuu
B.      Kweli kuu ya pili
1.       Mfano kuhusu kweli kuu ya pili
2.       Mfano kuhusu kweli kuu ya pili
Hatua ya Tatu.        III. Suluhisho la tatizo
A.      Kweli kuu ya kwanza
1.       Mfano wa kweli kuu
2.       Mfano wa kweli kuu
B.      Kweli kuu ua Pili
1.       Mfano kuhusu kweli kuu ya pili
2.       Mfano kuhusu kweli kuu ya pili
Hatua ya nne.          IV. Matokeo
Hatua ya tano.         V. Mwaliko wa madhabahuni au kuomba na kuhitimisha .


KITU CHA ZIADA KWA HUTUBA ZA KIBIBLIA (UPAKO)
Hotuba za watu wa Mungu ni tofauti na hutuba za wana siasa wa kawaida ni muhimu kufahamu kuwa kama muhubiri wa maneno ya Mungu atakosa upako mahubiri yake hayatakuwa tofauti na yale ya wana siasa, unapokosa upako unakuwa sawa tu na Samsoni asiyekuwa na nguvu kwa msingi huo ili hotuba zetu ziweze kuwa na kitu cha ziada upako ni wa muhimu nani lazima muhubiri autafute uso wa Mungu  na kuwa na mahubiri yenye nguvu na uweza wa kugusa na kubadilisha maisha ya watu

Ufahamu kuhusu upako
-          Upako sio uweza wa kibinadamu  1koritho 2;1-1-5,4;19-20
-          Upako haumfanyi mtu kuepuka kazi ngumu Matendo 8;26-30
-          Upako sio mbadala wa kutokwenda chuo cha Biblia kuwa na upako hakumaanishi kuwa wahubiri hawapaswi kuhudhuria katika mafunzo ya chuo cha Biblia 2Timotheo 2;2,Matendo 19;9-10 Badala yake upako wa Roho Mtakatifu unatupeleka kwenda chuo cha Biblia
-          Upako sio badala ya mwalimu  1Yohana 2;27, waefeso 4;11
-          Upako sio mwaliko wa kujitegemea, Paulo alipoitwa bado Roho wa Mungu alimuongoza kujitia chini ya viongozi waliomtangulia na kupata maelekezo ili kwamba kazi yake na maono yake yasiwe Bure Wagalatia 2;1-2 Kazi ya Mungu haiwezi kukamilika bila kushirikiana
Chanzo kikubwa cha imani ya  “Jesus Only” ni muhubiri Willium Branham ambaye alikuwa na upako wa kupita kawaida  akitumiwa kwa nguvu na ishara na miujiza  katika kazi ya uinjilisti lakini kwa bahati mbaya hakuwa na ushirika na mwili wa Kristo  yeye aliamini kuwa yeye ndiye kiongozi pekee  mwenye mamlaka ya mwisho  aliyeangaziwa kweli na hivyo alikataa wazo au fundisho kuhusu utatu wa Mungu  ambao kanisa limeamini kwa karibu na zaidi miaka 2000 na akasema anayepingana naye amekosa  na matokeo yake ilienea imani hii potofu ya Jesus Only warumi 12;3 kamwe upako haukufanyi wewe kuwa Bora kuliko wengine
-          Upako ni Neema ya Mungu inayompa mtu nguvu za kutumika kwa msaada wa Roho wa Mungu
-          Upako ni uweza wa Mungu katika maisha ya huduma na katika kuifanya kazi yake
-          Upako unatofautiana kwa viwango kati ya muhubiri na muhubiri kwa utii,1Koritho 12;4-11
-          Kuwa na upako sio alama ya kukomaa kiroho bali matunda ya roho Wagalatia 5;24
-          Upako ni lazima uendane na mwenendo au tabia njema sawa na viwango vya kibiblia
Upako na ujumbe
Ili jumbe zetu ziweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa ni lazima ziwe na upako, upako huongezeka kwa kadiri ya namna na jinsi tunavyojitoa kwa Mungu
·         Osward Chambers alijitoa kuutafuta uso wa Mungu na kuomba na kusoma neno la Mungu na alituma wamishionari 400 Duniani
·         John Wesley alikuwa akiomba masaa mawili kila siku asubuhi alitumiwa kuleta uamsho mkubwa sana uingereza
·         Martin Luther aliomba masaa mnne kila siku asubuhi na kusoma neno
·         Muhubiri David Yongg Cho hakutani na watu kwanza mpaka akutane na Mungu kwa saa tatu
Muhubiri anashauriwa kuwa na tabia ya kukaa miguuni kwa Mungu  na kujifunza kumuabudu yeye kwa kadiri ya neema unayopewa  na hapo utajifuza kumfahamu Yesu vema Luka 10;40-42, ni vema kutegemea upako zaidi kuliko kupeleka jumbe zetu  zikiwa kavu Yohana 16;37,Matendo 2;37,24;25, muhubiri mshuhuri katika historia za kanisa Charles Finney 1825 alikuwa ni mtu mwenye upako wa kupita kawaida aliitwa na shemeji yake katika kiwanda cha pamba  na alipoingia alikutana na binti mmoja aliyekuwa akidhihaki mara nyingi na kuzungumza mabaya juu yake  alipomuangalia binti alianza kulia na mara kila mtu alianza kulia  na kiwanda kizima kila aliyemwangalia alikuwa akilia na hatimaye waliomba na kuokolewa Upako ni zaidi ya uwezo wa kibinadamu Zekaria 4;6 unaleta matokeo yaliyokusudiwa.


UMUHIMU WA KUTUMIA MIFANO WAKATI WA KUHUBIRI
Mifano inaleta mwanga kwa watu kuweza kuelewa ujumbe wako vema kwa wepesi na kwa ubora zaidi kwa msingi huo inahsuriwa kuwa wahubiri watumie mifano katika jumbe zao, mifano ni njia ya Mungu ya kuwasiliana na mwanadamu, Mungu ndiye mwandishi wa biblia kupitia Roho wake  na katika biblia kuna mamia ya mifano  ambayo Mungu aliitumia ili kuwafundisha watu wake kitu kama alivyo mtuma nabii Hosea ili kuwasilisha ujumbe wake kwa Israel na tabia yao ya kuabudu miungu kwa msingi huo tunaona kuna umuhimu kwa wahubiri kuwa na ujuzi wa matumizi ya mifano katika mahubiri yao
Yesu Kristo alitumia mifano, inasemekana kuwa asilimia 52 ya injili ya luka ina mifano angeweza kuwasiliana apendavyo lakini alitumia mifano kwa sababu ina faida nyingi sana kama nitakavyoziorodhesha hapo chini, kila mara alizungumza kweli Fulani na kisha alitoa mifano, mfano katika Luka 12;13, 15, 22-33, kuhusu toba Luka 13;1-10, gharama za kumfuata 14;27, 28-30, 31-33, mwana mpotevu Luka 15, shilingi iliyopotea na kondoo.Mifano mingine aliyoitumia Yesu ni pamoja na mbwa mwitu, Mbweha, Ngamia, tai, njiwa, shomoro yaani mbayuwayu, jua , mwezi,  Anga, dunia,  mkulima, milima , bahari, upepo, udongo, mbegu, miti, miamba , samaki, yai, mikate, divai,  mvua , radi na mifano mingine mingi yoote aliitumia katika kuwasilisha kweli Fulani za kiroho.
Mifano inaweza kuwa
*      Hadithi
*      Miujiza
*      Uponyaji
*      Mgongano wa mawazo
*      Kuoanisha nyimbo
*      Mashairi mfano Matendo 17;28
*      Vitendawili
*      Mifano
*      Matukio mfano Luka 13;14
*      Kufananisha 
*      Maigizo
*      Grafu au takwimu
*      Matumizi ya picha
Kwa nini ni muhimu kutumia mifano?
-          Inaweka wazi
-          Inavutia
-          Inavuvia
-          Inarahisisha
-          Inasisimua
-          Ianakazia kweli
-          Inarudia kweli kwa undani zaidi
-          Inasababisha watu kukumbuka
-          Inagusa mioyo
-          Inashawishi watu kusikiliza
-          Inaburudisha
-          Inasisimua
-          Inasimama kama daraja
-          Ina shughulika na tatizo moja kwa moja
Ujumbe usio na mifano unafananishwa na barabara ambayo imenyooka moja kwa moja na haina hata kona hata hivyo wahubiri wengi sana hawana mifano ya kutosha na hivyo hukosa mifano kwa madai kuwa aidha muda ni mfupi au wanaona mifano ni kama jambo la kitoto, ai wengine huiona ni vigumu kueleza au haipatikani kwa urahisi, lakini inashauriwa kuwa na kitabu au faili la kutunzia mifano na unaweza kuiandaa katika mtindo wa herufi A-Z utaitunza kila unapoisikia

                              
Muhubiri mmoja alitumia mfano wa kijana na mbwa aliyekufa, kufundishwa habari ya msamaha, kijana alimpenda sana mbwa wake na siku aliyofariki mbwa huyo kijana alimuomba baba yake mbwa huyo azikwe lakini mkia uachwe nje, kila mara kijana alipomkumbuka mbwa wake alikwenda na kuuvuta mkia mwisho ikawa kila wakati kuna harufu mbaya baba yake alimshauri kijana Yule kufukia kabisa, nasi katika kusamehe hatupaswi kukumbushiana machungu yaliyopita msamaha lazima uendane na swala la kuachilia kila kitu kabisa, Kumbe mifano inasaidia somo kuwa wazi na kueleweka vema itumie kila iwezekanavyo.

Kanuni za kutumia mifano.
·         Hakikisha kuwa unakuwa mkweli unapotumia mifano
·         Usitumie mfano wa mtu mwingine kana kwamba tukio hilo limekutokea wewe
·         Usieleze katika mifano vitu visivyoweza kuaminika, asipunguze waka kuongeza chumvi
·         Uwe mwangalifu usitoe siri ya mtu  wala usitoe mifano inayoendana na tukio halisi lililofanyika kanisani, wala usitaje jina la mtu katika mifano tata
·         Jiandae usitumie mifano kama njia ya kupotezea muda wala usitumie muda mrefu kwa mifano
·         Usianze mfano kwa kusema huu ni mfano
·         Kuwa mbunifu kuhusu mifano, toa mifano ya kimatukio
·         Hakikisha kuwa ndani ya mifano kuna somo moja kuu linalosisitizwa.

SURA YA TATU: MUHUBIRI NA JAMII YAKE
Ujuzi kuhusu mawasiliano yasiyo na sauti
Kama itakuwa umewahi kumsikiliza muhubiri ambaye amesimama tu katika mahubiri yake bila kutikisa hata mkono bila shaka utakuwa hukuridhishwa na aina ya muhubiri wa jinsi hii na inakuwa vigumu pia kumsikia anasema nini? Mwenendo wa mwili una sehemu kubwa sana wakati wa kuhubiri unachangia kwa kiasi kikubwa  kuleta usikivu kwa jamii yako mwenendo huo wa mwili wako ndio unaitwa mawasiliano yasiyo na sauti Nonverbal communication mawasiliano yasiyo na sauti huwakilishwa  na maeneo makubwa manne
·         Muonekano wa uso wako
·         Matumizi ya mikono
·         Macho yako kama unawatazama watu au vinginevyo
·         Na muonekano wa hali ya hisia zako za ndani kwa nje

Muonekano wa uso wako
 Muonekano wa uso wako unaweza kuonyesha dhahiri  nini kinaendelea sawa kabisa na jinsi unavyoweza kuzungumza wanasaikolojia wanaamini kuwa karibu nusu ya  au zaidi ya athari za ujumbe wa mtu  kwa jamii yake unapokelewa kutoka usoni, uso ndio unaofunua ushawishi wa Mnenaji na kusaidia kukubalika kwa wazo lake hata kama mtu ameficha hisia zake ni rahisi kuziona hisia hizo usoni
Furaha na huzuni, Maumivu au uchungu, kushangaza au kuvutia, kuona huruma na kuguswa, upendo au chuki, kupenda au kutokupenda haya yote huweza kusomeka kupitia mawasiliano haya.

Matumizi ya mikono
Hapa tiunazungumzia sio tu swala la matumizi ya mikono bali pia mabega, kichwa na mwili mzima kwa ujumla vyote vinatakiwa kuonyesha kuwa uko katika kuwasiliana, wakati mwingine mwenendo wa mwili una tusaidia kusema hata kabla ya maneno na hivyo kukamilisha swala la mawasiliano.



Macho yako kama unawatazama watu au vinginevyo
Kama ilivyo kwa alama nyingine za mwili macho nayo ni ya muhimu sana katika mawasiliano unapaswa kuwaangalia wasikilizaji wako kwa sababu unapaswa pia kujua kinachoendelea na pia kitendo cha kuwaangalia moja kwa moja kinamaanisha kuwa mzungumzaji anazungumza na jamii yake jambo hili linasaidia katika maswala ya mawasiliano.
Maswala mengine yanayosaidia katika mawasiliano ni pamoja na vijichekesho au hata kuwa karibu na wasikilizaji wako

MAWASILIANO KATIKA MTINDO WA SAUTI
Sauti ni kama muziki inaweza kuwa laini au  kubwa  wakati wa kuwasiliana ni lazima uhakikishe kuwa unaitumia sauti yako vema  swala la utoaji wa sauti ni swala gumu sana  kwa sababu utoaji wa sauti unategemeana na  utendaji wa kazi wa viungo vingi sana , ili sauti iweze kutoka kuna viungo vinavyohusika katika utoaji wa sauti, Pua, taya, ulimi, meno, bomba la hewa, koo, mapafu na dayaframu
   Sauti iliyo nzuri  inaanza na upumuaji ulio mzuri pia  kwa msingi huo muhubiri unaweza kuwa na mazoezi ya kusaidia upumuaji wako ili wakati mwingine sauti iweze kutoka vizuri nunaweza kulala sakafuni na kuwekla kitu kizoto kati ya mapafu na tumbo kasha ukaanza kupumua taratibu na kuanza kutoa sauti za matamshi kama ha kasha  ho , pia unaweza kuchukua mazoezi kwaajili ya kuitoa sauti yako ili iweze kusikika  vuta pumzi ndani sana  mkisha anza kuiacxhia polepole na kutamka maneno yanayotakiwa kutamka kama ya kimaandiko jitahidi usitumia pua katika kuzungumza wala usiikoromeshe sauti yako

MASWALA YA USIKIVU
Kwa kawaida Muhubiri anapaswa kusikilizana na jamii yake wao wakusikie na wewe uwasikie hili linakuja hasa pale mzungumzaji atakapokuwa akijihusisha na maswala ya mijadala kama wasikilizaji hawakupati vizuri mara nyingi kunauwezekano wa wana jamii kutoa aina Fulani ya sauti hivyo hapo muhubiri unapaswa kuwa makini.

Wakati wa kusikiliza unapaswa kuzingatia
·         Uchaguzi – yaa ni kua na hali ya kuamua wapi usikilize kwani kuna sauti nyingi lakini wapi tunatoa usikivu ndipo panapoweza kutufanya tusikie

·         Kusudia - Mfano mtu anakuliza umesikia lazima ujiulize kusikia nini? Kila ambacho unakiulizia umesikia nini ndicho kilae ambacho mtu anakuwa amekikusudia  kwa hiyo katika kusikiliza uwe unakusudi

·         Uwe na ustadi
o   Lazimna uweze kutafuta wazo kuu katika kusikia kwako
o   Lazima ukumbuke uchambuzi wa ndani sana  wa kile kilichozungumzwa
o   Lazima ujue kwanini hoja au mada au kinachozungumzwa kinawakilishwa kwa njia hiyo
o   Lazima ujue maana ya maneno ambayo mzungumzaji anayatumia
o   Ujue kuhusianisha wazo la mneneji na kile anachokiwasilisha
o   Lazima uchambue au kufanya hukumu kuhusu mawazo ya mneneji
o   Lazima ujue kusudi kuu la mzungumzaji na kile anachokitarajia

·         Uwe makini
Hakuna mtu anayesikiliza wakati wote kile kinachozungumzwa na mneneji kukosa umakini ndio moja ya maadui wa kubwa wa kujifunza inasemekana mara nyingi ni nusu tu ya watu wanaweza kuelewa mnenaji anazunghumza nini na wengine wanapata juu juu tu na watoto wanakuwa kama viziwi kabisa hata ingawaje wanasikia unaweza kujifanyia utafiti kwa kuweka kaseti na kuwaomba watu wasikilize kasha waulize wameelewa nini? Kunahitajika umakini katika kusikiliza

MIJADALA
Mahubiri yanaweza kuwasilishwa pia kwa njia ya mijadala hususani wakati wa kuweko studio kwa njia ya redio au television na hata kanisani pia njia hii inaweza kutumika kuna aina nyingi za mijadala
Mijadala yenye kuhusisha watu wengi Panel
Hawa wanaweza kukaa katika mzunguko wa kuweza kutazamana au kuitazama jamii kwanmi jamii inahitaji kuona nyuso zenu lugha itakayotumika ni ya kuelimisha na yenye kuzingatia kuwa hapa mmnajadili sio mahubiri
Mijadala inayohusisha kuwasilisha kitu katika kikao symposium
Mijadala hii kila mmoja anakuwa ameandaliwa  kuwasilisha jambo Fulani  na kila mmoja atakuwa amepewa muda maalumu wa kuwasilisha  mada  kama ni somo litakuwa limegawanywa katika vipengele kadhaa na kila mmnenaji anakuwa na kipengele chake cha kuwasilisha

Makusudi ya mjadala
o   Kubadilishana mawazo
o   Kuchukua uamuzi
o    Kutafuta suluhu
o   Kutoa elimu
 Mijadala ni lazima iandaliwe vizuri, kila mmoja anapaswa kuonyesha ushirikiano na kunapaswa kuwako mwenye kiti wa mijadala anayejua kuendesha vizuri majadiliano hii inafanyika hivi kwa sababu makanisa yanabarikiwa na ni rahisi leo kuwa na vyombo vya habari kama tv na radio na kadhalika


SURA YA NNE: MUHUBIRI NA MASWALA YA VYOMBO VYA HABARI NA TAMADUNI TOFAUTI
Ujuzi kuhusu namna ya kuwasiliana katika Redio na Television
1.  Haya ni mawasiliano kwa njia ya vyombo vya habari “Media communication” Mahubiri kwa njia ya Redio na televisheni au mahubiri yaliyochapiswa huingia katika eneo la mawasiliano kwa njia ya habari mtindo huu wa mawasilianoi unaweza kuvuka tamaduni tofauti na kufika mbali
A. Vyanzo na Mchakato
1. Mchakato – tendo la redio au televisheni kupekleka ujumbe linaweza kuwa
i. Tendo la mtu Fulani pakee
ii. Tendo la matumizi ya mtandao
Mtandao wa kituo husika unakusudia au unaungana na vituop vingine kutuma ujumbe kwa wakati muafaka na kwa msingi huo watenda kazi wa Kikristo wanapata nafasi ya kluwahubiri maelfu kupitia vyombo vya habari
Vyanzo – Kuna vyanzo vingi sana vya kueneza habari na program za vyombo vya habari kama televisheni na redio kama unakusudia kuwa na matumizi ya vyombo hivi vya habari unaweza pia kuwa na vyanzo kama
Wahubiri mbalimbali wanaorusha vipindi
Waigizaji wanaoweza kufurahisha watu ili kuwavutia
Watenda kazi wa kiristo wanaoshughulikia maswala ya kurusha vipindi n.k.


Unapozungumza katika Redio au Televisheni
*      Hakikisha umeandaa ujumbe wako vilivyo kwa makusudi ya kukutana na mahitaji ya jumla ya wasikilizaji wako
*      Watu wana matatizo mengi na hivyo vipindi vyako view na uwezo wa kugusa mahitaji ya watu husika
*      Radio yako au televishenio yako inatakiwa iwe na mvuto wa kuwafanya wasikilizaji kupenda kusikiliza au kutazama
*      Kumbuka kama hawatafurahia wanachokisikia watazima au kubadilisha chaneli

 Maswala ya Fedha kwaajili ya vyombo vya habari
·         Uhakikishaji wa kupata fedha kwaajili ya vyombo vya habari kama Redio na Televisheni hufanyika katika namna nyingingi sana
o   Kwa kukusanya watu ambao watakuwa taryari kugharimia urushwaji wa vipindi
o   Kwa kuwatangazia wale wote wanaopenda kudhamini vipindi kwa makusudi ya kibiashara
o   Matangazo ya kibiashara  na kadhalika
 Program.
o   Hakikisha kuwa wanafaidika na kutangaza kwao kupitia tv yako au redio yako endapo inaweza kufika mbali kwa masafa yake
o   Hakikisha kuwa vipindi vyako vinakuwa na ubora mkubwa unaokusudiwa ili kuwavuta watu wengi sana kusikiliza ili wafanya biashara waweze kuvutwa kutangaza katika redio yako
o   Uwe na program nzuri za muziki za kuvutia zenye ujumbe mzuri ili kuvuta usikivu
o   Kumbuka kuwa wasikilizaji pia watakuwa wakiongezeka kutokana na umahiri wa vipindi vyako.

 Nguvu na Sheria
·         Redio na televisheni vina uwezo mkubwa sana wa kutawala mawazo ya watu kila tuachokiona na kukisikia kinavuvia akili zetu na upande mwingine wa kusikia na kuona  ni kunyonya kile tulichosikia na kuona  na kuyatumia
·         Maswala ya program za Kikristo katika vyombo vya habari yanatakiwa kuwa ya kweli nay a kivitendo ili kuvutia akili za watu
·         Uwe makini na kila aina ya ujumbe au kinachorushwa katika televisheni yako au redio
·         Jumbe na kila kinachorushwa kina nguvu sana ya kuchochea wema ama uovu kwa jamii husika
·         Ili kulinda ni vema kuamua muda wa kitu gani kinarushwa na saa ngapi nani anaweza kusikia na nani hawezi kusaikia  kitu kibaya kinaweza kusababisha wasikilizaji wako kuzima redio /televbisheni yako na kwenda kwengine
·         Televisheni na redio zina nguvu sana hata kwa watu wasiojua kusoma au kuandika
·         Maswaloa ya kuzungumzia dini hayana maana sana kwa jamii kwani watu wakati wote hutafuta majibu ya maswali ya matatizo yao na sio vinginevyo.

   Ujumbe wa Mawasiliano.
A.      Mawasiliano na wasikilizaji
                                                   i.      Ujumbe wa mawasiliano katika redio na televisheni unaweza kuwa wenye kuonekana au usio wa kuonekana kwa watu wote wawili yaani wasikilizaji na mtangazaji, unap[okuwa unatangazia kutoka studio watazamahji au wasikilizaji wanaweza wakawa hawakuoni kwa maana ya Redio
                                                 ii.      Kama ni vipindi vinavyochukuliwa kanisani ni rahisi kuwana wasikilizaji wako au wao wakakuona
                                                iii.      Lazima uwe makini katika kuhakikisha kuwa unajua namna ya kuiwasiliana na jamii hiyo ya watu hasa kama unatunmia redio wale wasiokuona unaweza kufanya mawasiliano nao kama mtu uonaye na kuwa fanya wwajisikie kama uko pamoja nao kwa upande wa televisheni yako mab ambayo yanaweza kusaidia wasikilizaji kujiona kama wako na wewe moja kwa moja kuliko redioni

Mambo mengine ya msingi ya kuzingatia.
*      Maandalizi mazuri ya vipindi ni muhimu yakafanyika kabla ya kipindi kuruishwa
*      Hakikisha kuwa una wataalamu au mafundi wakio hodari
*      Unapozungumza na watu moja kwa moja katika televisheni itazame kamera ili watazamaji waone kuwa sasa unazungumza nao
*      Uwe na kamera nzuri na vipaza sauti vilivyo na ubora kama una rekodi hakikisha kuwa unatumia vyombo safi.

Kwa habari ya Lugha
*      Tumia lugha nyepesi tu
*      Pangilia hotuba yako kwa mawazo yanayokubaliana ijulikane unatoka wapi kwenda wapi
*      Hakikisha kuwa unatamka wazi meneno yako
*      Tumia lugha ambayo inatumika na wasikilizaji wako na isiyo ya matusi
 



 

Hekima imejulikana kuwa na haki !


Luka 7:33 - 35Kwa kuwa Yohana Mbatizaji alikuja, hali mkate wala hanywi divai, nanyi mwasema, Ana pepo. Mwana wa Adamu amekuja, anakula na kunywa; nanyi mwasema, Tazama, mlafi huyu, na mnywaji wa divai, rafiki wao watoza ushuru na wenye dhambi. Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa watoto wake wote."
 


Utangulizi:-

Bill alikuwa ni mtu mwenye umri wa miaka ipatayo 40 na alikuwa akifanya biashara ya kuuza nguo, aliuza nguo za aina tofauti tofauti, kwatika miji na vijiji mbalimbali, siku zote alitumia punda kubeba mizigo ya nguo alizokuwa akiziuza.

Siku moja aliamua kumchukua kijana wake mwenye umri wa miaka 15 aliyeitwa Ron na kwenda naye katika miji na vijiji vilivyokuwa karibu,Punda alibeba behi mbili za nguo walizokuwa wakiuza, wote walikuwa na furaha kubwa sana Bill na Ron, baada ya kuuza na kufanya biashara kubwa sana na kupata faida , Bill alikuwa na furaha yeye na mwanaye ron na punda wao waliamua kurudi nyumbani.

Walitembea umbali mrefu sana mwishowe walichoka, wote watatu walitembea pole. Pole wakirejea nyumbani.

Watu wawili waliwaona wakiwa wamechoka sana, wakaanza kusema “angalia hawa wajinga wamechoka mbaya inavyoonekana, wana punda lakini kwanini mmojawao asipande juu ya punda wanapata shida ya bure hali wanaye punda si wangemtumia!”

Bill na Ron walisikia lililokuwa likizungumzwa na watu walke wawili kuhusu wao na Ron alimwambia baba yake apande juu ya Punda.

Alikubali na akakaa juu ya punda, lakini baada ya dakika chache Mzee mmoja alimuona Bill juu ya punda na akamwambia “we mzee huna hata huruma mwangalie kijana wako alivyochoka bado mdogo mno, wewe unapanda ju ya punda na unamuacha mtoto atembee ?”

Bill aliamua kumpandisha mwanae juu ya punda na wakaendelea na safari lakini baada ya muda kidogo Mgeni mmoja akapiga kelele akimkemea Ron “ weee bado ni kijana sana huwezi kutembea? Unaachaje mzee anatembea wewe kijana uko juu ya punda uvivu tu shuka haraka” 

Bill na mwanaye Ron walichanganyikiwa na wasijue nini cha kufanya, wakaamua wote wakae juu ya Punda na kuendelea ingawa punda alitembea kwa shida sana kwa vile uzito wao ulikuwa ukimuelemea.

Mtu mwingine akawaona kwa mbali akawakimbilia na kuwaambia kwa kupiga kelele akiwaambia Bill na mwanaye, hivi ninyi mna kichaa?inawezekanaje wote wawili mumpande punda mmoja je hamuwezi kutembea? Kwanini mnamtesa huyu mnyama?
Bill na Ron walishangaa sana wakanyamaza kimya kwa Muda.

Sio rahisi kumpendeza kila mtu, kila mmoja ana mawazo tofauti na maoni tofauti, ni vigumu kumpendeza kila mtu au kufuata wazo la kila mtu, wakati mwingine ni lazima kuamua kile tulichokiamua na kwa kweli fuata moyo wako na Mapenzi ya Mungu.

Mungu katika hekima yake amejaribu kwa kilanjia kuwapata wanadamu, alituma manabii kwa njia nyingi na kwa namna mbalimbali

Yohana mbatizaji alitumwa kwa Israel akihubiri mahubiri makali sana akiishi maisha ya kujikana, aliishi porini, akila nzige na asali ya mwituni, alivaa ngozi na singa za ngamia, hakuhudhuria sherehe za aina zozote, alionya kuhusu hukumu ya Mungu na kukemea dhambi akiwataka watu watubu na kugeuka kwa Mungu lengo kuu ikiwa ni kuwaleta watu kwa Yesu hata hivyo walisema ni kichaa ana pepo na hatimaye walimuua.

Yesu alikuja kwa kusudi la kuokoa alijichanganya na wenye dhambi alifanyika rafiki, alikula na kunywa naovyakula vyao vya kawaida na vinywaji vyao vya kawaida lakini hata hivyo walimuita mlafi.

Kristo anatufundisha kuwa Hekima ya Mungu imejulikana kuwa na haki kwa watoto wake, ni wazi tu kuwa kwa njia yoyote wanadamu hawapendi kuitikia wito wa Mungu aidha kwa kuwachezea au kwa kuwahuzunikia, ukiwaita kwa sherehe hawaji au ukiwaita kwa huzuni hawaombolezi,

Luka 7:31- 32. “Bwana akasema, Niwafananishe na nini watu wa kizazi hiki? Nao wamefanana na nini? Wamefanana na watoto walioketi sokoni na kuitana, wakisema, Tuliwapigia filimbi wala hamkucheza; tuliomboleza, wala hamkulia.”

Wanadamu hawana jema ukiwa mpole watasema huyu naye kazidi sana upole, ukiwa mkali watasema mmh huyu naye mkali mno, ni vema kila mmoja akatimiza kusudi la Mungu kama alivyokusudiwa na hii ndio hekima hatuwezi kuwa vile wanadamu wanavyotaka tuwe lakini tunaweza kuwa vile Mungu anavyotaka tuwe, Mungu alimuita Yohana kwa Kusudi lake na alimtuma Yesu vilevile kwa kusudi lake, hii ndio hekima ya Mungu, hatupaswi kujali watu wanasema nini timiza kusudi la Mungu uliloitiwa, Faida ya wito wako itaonekana baadaye.

Kikwete hawezi kuwa Magufuli na Magufuli hawezi kuwa Kikwete, Tulimuomba Mungu atupe Rais tumuachie atomize kusudi lile ambalo Mungu amempa kwaajili ya watanzania, iwapo Mungu angekuwa anataka mfumo uleule na aina ileile ya uongozi, angeachia mtu anayefanana na Kiwete atawale, hakuna anayeweza kusema yeye alikuwa Rais Mzuri zaidi ya mwingine kwa vile kila mmoja ameitwa kwa kusudi lake, Hali kadhalika katika Huduma, Mtume, Nabii, Mwinjilisti Mchungaji na Mwalimu, hakuna aliye mkubwa kuliko mwingine, kila mmoja anatimiza kusudi lake, Mtume hawezi kusema kuwa yeye ni mkuu kuliko Mwalimu kwa vile amefundishwa na mwalimu, Nabii, Mtume mwinjilisti wanalelewa na wachungaji Kanisani, ipi ni huduma iliyokuu ni ile inayohitajika kwa wakti huo. Na hii ndio hekima ya Mungu.

Sio rahisi kumpendeza kila mtu, kila mmoja ana mawazo tofauti na maoni tofauti, ni vigumu kumpendeza kila mtu au kufuata wazo la kila mtu, wakati mwingine ni lazima kuamua kile tulichokiamua na kwa kweli fuata moyo wako na Mapenzi ya Mungu.

Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekim.

Rev. Innocent Kamote.

Jumanne, 3 Oktoba 2017

Maombi yenye Nguvu!


Wafilipi 2:3-4Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake. Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine.”

 Musa Mtumishi wa Mungu mara kwa mara aliwaombea israel na kuwatanguliza wao kuliko yeye
 
Yakobo na Yohana walikuwa marafiki wa karibu sana, walikuwa majirani, walisoma pamoja kisha walikwenda chuoni pamoja na pia walipata kazi sehemu moja.

Siku moja waliamua kusafiri kwa meli kwenda katika visiwa vigeni, walianza safari yao na kuzunguka na meli na wakatokomea mbali sana, kwa bahati mbaya safari yao ilikumbwa na dhoruba kubwa sana kiasi ambacho meli waliyokuwa wakiitumia ilivunjika vunjika na baadhi ya abiria walikuwa, lakini hata hivyo Yakobo na Yohana walifanikiwa kuogelea kwa muda mrefu na kufikia moja wapo ya kisiwa kilichokuwa karibu.

Kisiwa hiki kilikuwa kama nyika tu hakukuwa na miti ya maana na Yakobo na Yohana waligundua kuwa hakuna uwezekano wa kuishi pale bila msaada wa Mungu, Hivyo waliamua kuomba Mungu aingilie kati, lakini waliambiana tuone ni maombi ya nani yatakuwa yenye nguvu? Yakobo aliamua kwena upane wa mashariki ya kisiwa na Yohana aliamua kwenda upande wa Magharibi wa kisiwa kila mmoja alidhamiaria kwenda kumuomba Mungu huko ili msaada utokee

Yakobo aliomba kwanza Mungu ampe chakula ili aweze kuishi, na mara akaona sahani ya chakula na matunda na mboga za majani na samaki, akaanza kula, 

Baada ya siku mbili aliomba apate mwanamke mzuri sana ili awe mke wake kwa vile alihisi upweke wa hali nya juu kule kisiwani, baada ya masaa machache kulikuwa na Meli iliyopata ajali karibu na kisiwa kile kwa mbali na ni mwanamke mmoja tu aliyeweza kupona katika ajali ile kwa kuogolea mpaka kisiwani na Yakobo alimpokea kama mke wake, sasa ikawa kila anachokiomba Yakobo anakipata.

Hatimaye kama mwezi mmoja ulipita tangu ajali ile ya meli itokee, Yakobo aliomba kutokee meli itakayomrudisha nyumbani yeye na mkewe, na kwa hakika ikatokea meli na kumchukua yeye na mkewe kurudi nyumbani.

Lakini walipokuwa wanakaribia kuingia katika lango  la meli, Yakobo alisikia sauti ikimwambia “Je unaondoka mwenyewe? Bila mtu muhimu katika maisha yako?” Yakobo alishangaa na kujibu hebu niambie unamaanisha nini ? mtu muhimu katika maisha yangu ni mke wangu na niko naye hapa!

Sauti ikamwambie mimi ndiye uliyekuwa ukiniomba na ndiye niliyekuwa nikijibu Maombi yako, ndiye niliyekupa chakula na kuyatunza maisha yako na hata huyo mke wako mimi ndiye niliyekupa, Yakobo alipiga magoti na kumwambia Mungu asante kwa fadhili zako zote.

Kisha Yakobo akamkumbuka Yohana ambaye alikuwa amekwisha sahau habari zake, na akajisikia vibaya 

Mungu akamwambia sikuwa najibu maombi yako kwa sababu ya wema wako, nilikuwa wakati wote nasikiliza maombi ya Yohana na kuyatimiza, Yohana wakati wote alikuwa akiomba ombi moja tu Mungu wangu tafadhali mkumbuke rafiki yangu Yakobo mtimizie kila anachokihitaji hayo ndio yalikuwa maombi ya Yohana wakati wote.

Yakobo alilia sana na alikimbia magharibi ya kisiwa kwaajili ya kumtafuta rafiki yake, alitambua kuwa alikuwa mbinafsi hakufikiri kuhusu wengine alijifikiria mwenyewe tu na kufurahia baraka zile, hata hivyo alipofika magharibi ya kisiwa hakumuona Yohana na Yakobo alimuuliza Mungu sasa yuko wapi Yohana Mungu akamwambia Nilimchukua na yuko name, Mtu mwenye moyo wa dhahabu kama Yohana anapaswa kukaa na mimi, lakini nitayatimiza maombi yake kama nilivyomuahidi.

Yakobo alijisikia vibaya sana na ndipo alipogundua kuwa rafiki yake ndiye aliyekuwa na maombi yenye nguvu kuliko yake, kwa sababu maombi yake, hayakuwa na hata chembe ya ubinafsi kama yak wake.

Maombi yenye nguvu ni maombi ambayo ndani yake hakuna chembe ya ubinafsi. Watu wakubwa katika maandiko hawajiombei wenyewe wanaombea wengine, Manabii waliokuwa rafiki wakubwa wa Mungu ni wale walioombea watu na sio kujiombea wenyewe, Mungu ampe neema kila mmoja wetu kuacha ubinafsi.

Kumbukumbu 9:18-20Nikaanguka nchi mbele za Bwana siku arobaini usiku na mchana, kama pale kwanza; sikula chakula wala kunywa maji; kwa sababu ya makosa yenu yote mliyokosa, kwa kufanya yaliyo maovu machoni pa Bwana, kwa kumkasirisha. Kwa kuwa niliogopa hasira na makamio aliyowakasirikia Bwana kutaka kuwaangamiza. Lakini Bwana alinisikiza wakati huo nao. Bwana akamkasirikia sana Haruni akataka kumwangamiza; nikamwombea Haruni naye wakati huo.”

1Samuel 7: 5-9Samweli akasema, Wakusanyeni Israeli wote Mispa, nami nitawaombea ninyi kwa Bwana. Wakakusanyika huko Mispa, wakateka maji na kuyamimina mbele za Bwana; wakafunga siku ile, wakasema huko, Tumemfanyia Bwana dhambi. Samweli akawaamua wana wa Israeli huko Mispa. Hata Wafilisti waliposikia ya kuwa wana wa Israeli wamekusanyika huko Mispa, mashehe wa Wafilisti walipanda juu ili kupigana na Israeli. Nao wana wa Israeli waliposikia, wakawaogopa Wafilisti. Wana wa Israeli wakamwambia Samweli, Usiache kumlilia Bwana, Mungu wetu, kwa ajili yetu, kwamba atuokoe na mikono ya Wafilisti. Ndipo Samweli akatwaa mwana-kondoo mchanga, akamtolea Bwana sadaka ya kuteketezwa nzima; Samweli akamlilia Bwana kwa ajili ya Israeli; Bwana akamwitikia.” 

Mafanikio yako wakati wote kumbuka kuwa kuna watu wanaoomba kwaajili yako na wala sio kwa sababu ya wema wako na Tunapoomba kwaajilin yaw engine Mungu hujishughulisha na mahitaji yetu pia.

Na Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.  

Jumapili, 1 Oktoba 2017

Ajidhaniaye kuwa amesimama na aangalie asianguke!


Andiko la Msingi:1Wakoritho 10:12Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”

Utangulizi:-

Ni muhimu kufahamu kuwa kifungu hiki cha maneno ya Paulo mtume kinafunga au kinahitimisha mfululizo wa maonyo muhimu sana aliyoyatoa Paulo mtume ambayo tunayapata kama somo kutoka kwa wana wa Israel

Kwamba kama mababa wa waisrael waliweza kufurahia neema maalumu ya kuokolewa kutoka Misri chini ya utawala wenye nguvu wa Farao, na kuona miujiza mingi na uwepo wa Mungu, bado waliweza kukataliwa na kuangamizwa jangwani, maiti zao ziliangukia katika jangwa zito, hawakuweza kufika na kuingia katika inchi ya ahadi, na kwa sababu hiyo kupitia wao tunajifunza kwamba watu wanaojikinai wenyewe na kufikiri kuwa wao ni maalumu sana na wenye kujiamini kupita kawaida na wenye kujivunia kipawa cha aina fulani, upendeleo wa aina fulani, na kumsanifu awaye yote hii ni moja ya dalili mbaya  inayoweza kumpelekea mtu katika anguko la aina yoyote!

Ujumbe:

Kulikuwa na mti mmoja mrefu sana unaojulikana kama mti wa mtiki na karibu yake kulikuwa na miti mingine iliyokuwa laini kama nyasi,

Mtiki ulianza kujisifu kwa nyasi kuwa mimi ni mzuri mrefu na ni mwenye nguvu sana kuliko ninyi, Nyasi ziliposikia ziliuonya mtiki na kuuamnbia rafiki yangu majivuno ya kupita kawaida ni hatari, Hata wenye nguvu huanguka siku moja

Mtiki ulizizarau nyasi, na kuendelea na kujisifu wenyewe!

Upepo mkali sana ulipuliza na mtiki ulisimama imara, na hata mvua kali ziliponyesha mtiki bado ulisimama imara na uliendelea kutanua majani yake, wakati wote huo nyasi na mbogamboga ziliinama kabisa, na mtiki ukawacheka sana nyasi na mboga mboga.

Siku moja kukatokea dhoruba kali sana msituni kama ilivyo desturi Nyasi ziliinama chini na kama kawaida yake mtiki haukukubali kuinama, Dhoruba iliendela kuwa kali sana kiasi ambacho mtiki haukuweza kustahimili tena, ukaishiwa na nguvu  ukaanguka chini, ulijaribu kwa nguvu zake kusimama na ikashindikana kabisa na huo ndio ukawa mwisho wa mti wenye kiburi, Mambo yalipokuwa sawa Nyasi zilisimama na kushangaa kuwa mtiki hauko na nyasi zilipoangalia vema ziligundua kuwa mtiki umeanguka!
Tunajifunza nini ?

Biblia inasema kijapo kiburi ndipo ijapo aibu, tena kiburi hutangulia uangamivu  Mithali 16:18Kiburi hutangulia uangamivu; Na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko”.  Biblia inaonya kuwa kila ajikwezaye atashushwa Mathayo 23:12Na ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.” Mithali 29:23 inasema “ Kiburi cha mtu kitamshusha; Bali mwenye roho ya unyenyekevu ataheshimiwa.” Baadhi ya wasomi wa kibiblia wanasema kuwa kiburi kinasababisha kutokujali ambako kunaongoza katika kufanya makosa makubwa ya kutisha na kushangaza na Wengine wanasema Mungu mwenyewe huwatia nidhamu watu wenye kujikinai wakijidhani wao ni bora kuliko neema ya Mungu kwa kuwaachilia wajikute katika matukio yatakayowanyenyekesha.

Iko mifano mingi sana Katika Historia ya dunia ambayo inaweza kutufunza jambokatika mitazamo hii, wote tumewahi kusikia au kuona habari ya Meli ya kifahari sana Duniani ijulikanayo kama TITANIC Meli hii ilitangwazwa na watengenezaji kuwa ni meli ISIYOWEZA KUZAMA kutokana na kujiamini huko kwa kupitakawaida meli hii haikuwa na meli ndogondogo za uokoaji, lakini kilichotokea kimetoa funzo katika Historia ya dunia

Matengenezo ya Titanic.

Meli ya Titanic ilianza kutengenezwa mwaka 1909. Kampuni iliyoagiza meli hiyo kutengenezwa ni White star, lengo la kampuni hii ilikuwa ni kuweza kushindana na kampuni ya Cunard line meli hii ndiyo maarufu kuliko zote katika historia ya dunia. TITANIC ilikuwa meli ya pili kwa ukubwa baada ya meli ya Olympic kwa wakati huo, meli ya tatu kwa ukubwa ilikuwa ni Britannic.

Titanic yaanza Safari.

Baada ya matengenezo yake kukamilika mwaka 1912 maandalizi ya kuanza safari yalianza.
Aprili 10, 1912 meli ya Titanic inaanza safari ikitokea Southampton- Uingereza kuelekea New York- Marekani. Huku ikipambwa na maneno yaliyo kuwa yameandikwa ubavuni mwake kwa ustadi mkubwa yakisomeka T I T A N I C Meli hiyo ilibeba watu wapatao 2,200 wengi wao wakiwa ni matajiri na baadhi ya watu walikuwa wakihamia Marekani kwenda kuanza maisha mapya. Kapteni wa meli hiyo alikuwa ni E.J.SMITH, Meli hii ilikuwa na eneo la Matajiri wa juu, wa kati na wa chini, ilikuwa na kumbi za starehe, viwanja vya michezo na basket ball, ilithibitishwa na wataalamu mbalimbali kama meli isiyoweza kuzama na yenye usalama wa hali ya juu duniani. Mmiliki wa meli alipohojiwa na vyombo vya habari kuhusu usalama wa meli hii alisema "Hata Mungu hawezi kuizamisha"

Titanic yaginga mwamba wa Barafu Baharini.

Aprili 14, 1912 saa 5:40 usiku, Titanic ikagonga mwamba wa barafu. Ilikuwa ni siku ya nne tu tangu ianze safari yake. Kapteni wa meli hii alikuwa amearifiwa kuwa kuna mwamba mbele yao, hivyo arijaribu kukwepa lakini alikuwa kachelewa ubavu wa meli uligonga kwenye mwamba wa barafu na kupasuka ndipo maji yakaanza kuingia ndani ya meli. Ni mashua 16 tu za uokoaji zilizokuwa ndani ya meli hiyo ambazo zingeweza kubeba watu 1,178 hata hivyo mashua nyingi hazikujaza watu na hivyo watu 705 tu ndiyo waliokolewa.

Titanic yazama.

Mnamo tarehe Aprili 15, 1912 saa 8:20 usiku TITANIC ilizama. Watu 1,500 hivi walipoteza maisha. Tangu saa hii histori mpya ya TITANIC yaanza kuandikwa. Ama kweli ni historia ya kusikitisha sana.

Ndugu yangu je wewe ni maalumu sana kama Titanic? Wewe je mgumu kama mtiki? Unajivunia nini Duniani? Mungu yuko nyuma yako anakuangalia, Yeye ni wa kutukuzwa na kuogopwa sana yeye ndiye aliyeshikilia kila kitu hatuna budi kuwa wanyenyekevu kama Nyasi na kukubali kuinama ili tuinuke tena!

Ajidhaniaye kuwa amesimama na aangalie asianguke!
Wa salaam

Na Mkuu  wa wajezni Mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.