Jumatano, 19 Septemba 2018

Tena mmeyasahau yale maonyo!



Waebrania 12:5-11tena mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana, Wala usizimie moyo ukikemewa naye; Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake. Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.


 

“Kila mmoja anapaswa kuchagua njia mojawapo kati ya mbili, maumivu ya Nidhamu au maumivu ya Majuto” – John Rohn

Utangulizi.

Ni muhimu kwa kila mmoja wetu kufahamu kwamba maisha yetu hayawezi kuwa na wingi wa furaha na amani  na hata mafanikio kama tutasahau kuishi kwa Nidhamu, ni ukweli ulio wazi kwamba Nidhamu ndio njia sahihi ya maisha, Nidhamu haina mipaka kila mtu anapaswa kuishi kwa nidhamu, Nidhamu haina mwenye pesa, au asiye na pesa, mwenye utajiri au asiye tajiri, swala la nidhamu linategemeana na jinsi mtu alivyofunzwa na anavyokubali kujifunza, Nidhamu ni tabia na haipatikani kwa kurithi, kwa msingi huo kila mmoja anaweza kujifunza kuishi kwa nidhamu na akafanikiwa katika maisha, wengi wa watu wenye mafanikio ya kiroho na kimwili, na maswala mengineyo yote ni wale waliofanikiwa kuishi na kuenenda kwa Nidhamu. Tunahitaji Nidhamu ili kuyafikia maono, tunahitaji nidhamu ili kutunza utajiri, tunahitaji nidhamu ili kuepuka matatizo,mtu akiwa na nidhamu ni kama ana stadi ya maisha iliyo ya juu zaidi, watu wanaofanya kazi kwa bidii na wenye vipawa vikubwa hawawezi kuwa na mafanikio makubwa kama hawatakuwa na nidhamu, yaani huwezi kuzungumzia huduma, maisha, kazi, kusoma, mtindo wa maisha, ubora wa shule au taasisi au chuo, au taifa, au michezo, au jeshi kama katika kila secta watu hawatakuwa wamejifunza kuishi kwa nidhamu.

“We don’t have to be smarter than the rest, we have to be more Displined than the rest” warren Buffet 
“Hatuhitaji kuwa bora kuliko wengine, tunahitaji kuwa na Nidhamu kuliko wote” Warren Buffet
“Everyone must choose one of two pain, the pain of Displine or the pain of regret” John Rohn
“Kila mmoja anapaswa kuchagua njia mojawapo kati ya mbili, maumivu ya Nidhamu au maumivu ya Majuto” – John Rohn
“He who lives without discipline dies without HONOR”
“Wanaoishi bila Nidhamu huwa wanakufa bila heshima”

Nidhamu inahitajika katika kila Nyanja, huwezi kuwa mwalimu Mzuri kama huna nidhamu, huwezi kuwa Dereva mzuri kama huna nidhamu, huwezi kuwa Mchungaji Mzuri kama huna nidhamu, huwezi kuwa daktari mzuri kama huna nidhamu, huwezi kuwa mwana siasa mzuri kama huna nidhamu, huwezi kuwa bondia mzuri kama huna nidhamu, huwezi kuwa mchezaji mpira mzuri kama huna nidhamu, nidhamu ni maisha kula, kuvaa, na hata kuishi ni nidhamu nidhamu ndio kila kitu, kuomba ni nidhamu, kufunga ni nidhamu kila kitu kinahitaji nidhamu
“Kama kuna somo kubwa ambalo ningependa Dunia nzima ijifunze jibu langu lingekuwa ni rahisi Nidhamu tu” – Rev. Kamote
“If there is a great subject that I would like the world to learn my answer could be simple Discipline”
Nidhamu ndio somo kuu na la kwanza ambalo wazazi walitufundisha Nyumbani, na walimu wanalikazia shuleni, na wakristo wameagizwa kulihubiri, Jamii yoyote ile ambayo unaweza kusema kuwa haijaelimika basi ni jamii wa watu wasio na nidhamu – Rev. Innocent Kamote

Maana ya neno Nidhamu.

Neno nidhamu maana yake ni mfumo wa kuwafunza watu, ili wawe watii, au wawe wenye tabia njema na mwenendo Mzuri, Ni malezi au makuzi yenye kuzingatia,  Maonyo, Sheria, Taratibu,mamlaka, uthabiti, weledi, uthibiti, Heshima, mwelekeo, wajibu, utii, kiasi na kujiongoza na kushikisha adabu kwa ujumla wake kuwa na Nidhamu.
Neno nidhamu pia linaweza kutumika kuelezea mafunzo maalumu yenye kumfanya mtu awe mtii kwa sheria tabia na mwenendo na kurekebishika pale inapohitajika, ni mafunzo, Mafundisho, Shule, kocha, elimisha, na hekimisha, na kumfanya mtu awe na uwezo wa kujidhibiti yaani “self control” au Marudia au nidhamu kwa kiingereza Displine. Kushikisha adabu au kunadhimisha na kutoa maonyo au adhabu ili kumrekebisha mtu kwa lengo la kumfanya awe thabiti. Kwa kiibrania kuna maneno mawili yanayotumika kumaanisha Nidhamu 1 ni “YASAR” (NIDHAMU AU KUADHIBIWA) NA “YAKACH” (MAONYO) yametumika maneno hayo katika Mithali 3:11 “Mwanangu usidharau Kuadhibiwa na Bwana wala usione taabu kurudiwa naye
Biblia katika Waebrania 12:5-11 inatuasa kwamba tumeyasahau yale maonyo ni maonyo gani haya ambayo Biblia inatuasa kutokuacha kuyasahahu? Ni swala la Nidhamu au Marudia Biblia ya kiingereza inasema hivi katika fungu hilo la maandiko
And have you completely forgotten this word of encouragement that addresses you as a father addresses his son? It says,
“My son, do not make light of the Lord’s discipline,
    and do not lose heart when he rebukes you,
because the Lord
disciplines the one he loves,
    and he chastens everyone he accepts as his son.”[
a]
Endure hardship as discipline; God is treating you as his children. For what children are not disciplined by their father? If you are not disciplined—and everyone undergoes discipline—then you are not legitimate, not true sons and daughters at all. Moreover, we have all had human fathers who disciplined us and we respected them for it. How much more should we submit to the Father of spirits and live! 10 They disciplined us for a little while as they thought best; but God disciplines us for our good, in order that we may share in his holiness. 11 No discipline seems pleasant at the time, but painful. Later on, however, it produces a harvest of righteousness and peace for those who have been trained by it.

Katika kifungu hiki utaweza kuona neno Marudia yaani Nidhamu katika Biblia ya Kiswahili SUV limetajwa mara saba (7) na katika Biblia ya kiingereza limetajwa mara kumi (10), Kama katika kifungu hiki tungeambiwa tutafute neno kuu yaani “key word” basi ni wazi kuwa neno kuu ni “Descipline” na “Marudia” isipokuwa mimi ningependa zaidi kutumia neno Nidhamu, au Maonyo Neno hili ni neno la Muhimu sana sana na ni neno la kutia moyo ambalo kanisa halipaswi kulisahau kamwe Nidhamu, Nidhamu Nidhamu.

Umuhimu wa kutokuyasahau yale Maonyo (Nidhamu).

Biblia inahitimisha katika kifungu hiki kwamba wakati tunafundishwa nidhamu au tunazoezwa nidhamu haionekani kuwa ni jambo lenye kufurahisha sana lakini ukiisha kuzoezwa nayo inaleta faida yaani matunda ya haki na amani, Ni kama maandiko yanataka kutuambia kuwa kuna faida kubwa sana kwa mtu aliyejifunza kukaa katika nidhamu, kuzingatia yale maonyo, ziko faida nyingi sana za kujitia nidhamu ambazo zinajibu swali kwa nini nidhamu ni Muhimu Waebrania 12:11Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani”

1.       Nidhamu itakupa kufikia malengo :- 

Kama mtu awaye yote ana ndoto ya aina yoyote na anakusudia kuifikia ni lazima awe na nidhamu, Ushuhuda wa kidunia unaonyesha kuwa watu wote waliofanikiwa katika kila Nyanja na hata kutimiza malengo yao katika maisha na kupata mafanikio makubwa walikuwa ni watu waliojifunza kukaa katika nidhamu, Nidhamu inatusaidia kufaulu masomo, kumaliza shule salama, kumaliza jeshi salama, kukaa katika kazi zetu salama, kufanya kazi zetu vema na kufikia malengo vizuri, Mtu awaye yote mwenye makusudi na mpango mwema atatulia na kufanya kazi kwa bidii kila siku ili kuyafikia malengo, ni nidhamu pekee inayoweza kumfikisha mtu kule anakokusudia, kinyume na nidhamu ni vigumu sana kwa mtu kuyafikia malengo, Biblia inaonyesha kuwa wana michezo wote huwa na tabia ya kujitia nidhamu ili kwamba waweze kushinda na kupata taji ya kile wanachokikusudia, mwanamichezo yoyote ambaye hana nidhamu au mwanjeshi yeyote ambaye hana nidhamu atapoteza malengo, Ubora wa mwanamichezo yoyote bila kujali kipawa alichonacho kama hana nidhamu, kuna uwezekano mkubwa sana wa kupoteza malengo au kutokuyafikia malengo

 1Wakoritho 9:25-27Na kila ashindanaye katika michezo HUJIZUIA KATIKA YOTE; (Maana yake hujitia nidhamu). basi hao hufanya hivyo kusudi wapokee taji iharibikayo; bali sisi tupokee taji isiyoharibika. Hata mimi napiga mbio vivyo hivyo, si kama asitaye; napigana ngumi vivyo hivyo, si kama apigaye hewa; bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.”

Napenda Biblia ya Kiingereza inavyosema hapaEveryone who competes in the games goes into strict training” unaweza kuona neno “STRICT TRAINING”

Ni wazi kuwa Paulo mtume hapo anazungumzia uhusiano wa kujitia nidhamu kwa wana michezo ili waweze kuwa washindi, na kwamba hata wale wanaotaka kwenda mbinguni hawana budi kujitiisha kujifunza kuishi kwa nidhamu ni nidhamu pekee itakayoweza kutusaidia kutoka na kufanikiwa. Ni watu wenye kujitia nidhamu tu watakaoweza kufika Mbinguni, ni wahubiri wanaojitia nidhamu ambao hawataweza kukataliwa baada ya kuwahubiri wengine.

2.       Nidhamu inaleta Heshima:-

Ni muhimu kufahamu kuwa tukiishi kwa nidhamu watu watatuheshimu, watu wengi sana wanapenda kuheshimika kutoka kwa wengine lakini njia nyepesi ya mtu kuheshimika ni kuishi kwa nidhamu, watu wengi au wote duniani humkubali na kumuheshimu mtu mwenye nidhamu, sababu kubwa ni kwamba ni kazi ngumu kuwa na nidhamu na kwa sababu hiyo ukiwa nayo watu watakuheshimu, ukifanya kazi kwa nidhamu, ukatimiza kazi zako kwa wakati, ukawepo unapotakiwa kuwepo kwa wakati, ni lazima utaheshimika, Mwanafunzi mwenye nidhamu anajiandaa vizuri, anafanya kazi alizozipewa kwa wakati na kwa sababu hiyo ni rahisi kwake kuyafikia malengo. Kwa ujumla utakuwa kielelezo na mfano wa kuigwa

1Timotheo 4:12Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio, katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”

Paulo mtume ni kama anamweleza Timotheo kuwa mtu asikudharau kwa sababu u kijana, lakini ni namna gani watu watakuheshimu? Ni kama utakuwa mfano yaani kielelezo, kwatika usemi, mwenendo, upendo imani na usafi, ni kama Paulo anamwambia Timotheo kuwa watu watakuheshimu bila kujali umri wako hata kama ni mdogo endapo tu utaishi kwa nidhamu. Binti au mwanamke, kijana au mwanaume anayejitia nidhamu anaheshimika katika jamii,

3.       Nidhamu itakupa Afya njema.

Jinsi na namna ya kutunza afya zetu pia ni swala linalohitaji nidhamu, namna tunavyokula, tunavyotumia chumvi, sukari au mafuta mengi sana na namna tunavyotumia dawa bila nidhamu au kwa nidhamu vina mchango mkubwa sana katika kuamua tuwe na afya ya namna gani, Lazima na ni muhimu kuoga vizuri, kufanya mazoezi, kutembea na kulala kwa wakati kwa ujumla mtindo wa maisha wenye kujitia nidhamu utaufanya mwili wetu na akili zetu kuwa njema na zenye afya nzuri wakati wote, magonjwa sugu hayatakuwa sehemu ya maisha yetu, kula kwa wakati funga kwa mpangilio mwema bila kuharibu mwili wetu kwa vile miili hii sio mali yetu wenyewe ni mali ya Mungu.

 1Wakoritho 6:19 “Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;”

4.       Nidhamu inaleta uthabiti na uwezo wa kujitawala.

Kwa ujumla nidhamu ina faida kubwa sana katika ujumla wa mtazamo wa maisha, inakuumbia uthabiti na kujitawala au kujiamini na inakuepusha na hali zote za uvivu, kila mtu mwenye nidhamu utaweza kuona hawezi kuwa mzembe wala kuzembea au kutegea kazi, inaleta ufanisi kujitawala na kuwa na kiasi, Mtu mwenye nidhamu anauwezo mkubwa sana wa kujizuia au kujitawala atakuwa makini katika kujua kile kinatakiwa kuzungungumzwa na wakati kinapaswa kuzungumzwa, anajua nini cha kuvaaa na wapi pa kuvaa, anajua namna anavyotakiwa kuenenda na kwa sababu hiyo hujiepusha sana na matatizo na hivyo kuwa na uhusiano mzuri na watu, Nidhamu na kujitawala ni mfano wa mji wenye boma kama mtu akikosa kujitawala anakuwa kama mji usio na boma usio na ukuta ni rahisi kuvamiwa na kubomlewa kwa maangamizi makubwa Mithali 25:28 “Asiyetawala roho yake Ni mfano wa mji uliobomolewa, usio na kuta.”  Kumbe kujitawala yaani nidhamu ni ulinzi wa hali ya juu, huwezi kupatwa na majanga na mashambulizi ya aina mbalimbali kama utajiyiisha katika nidhamu.

5.       Nidhamu inakwenda pamoja na ubora wa Elimu.

Elimu haiwezi kuwa bora kama hakuna swala la kukazia nidhamu, Lazima kila mwanafunzi ajifunze nidhamu, Nidhamu itamsaidia mwanafunzi kujifunza vema na kwa ufasaha darasani na kukamilisha silabasi nzima vema, Mwanafunzi hawezi kuwa mwanafunzi mzuri kama haamki kwa wakati, haogi, hanywi chai au kula kwa wakati na anayetoka toka hovyo bila sababu ya msingi, kwenda kujisaidia au kurejea nyumbani, ni nidhamu ndiyo itakayokufanya uwe na afya njema utulivu, heshima na adabu na kukua vema na kukuwezesha kujifunza, Hata kanisani haipendezi kuona watu wanatokatoka saa ya kujifunza neno la Mungu kisha eti wanaenda kujisaidia, au kusikiliza simu, iliyowekwa katika mtindo wa kimya eti kwamba una maswala Muhimu, Mungu anataka sikio lako na moyo wako ili akuonye na kukupeleka katika njia iliyonyooka Mithali 12: 1Kila apendaye mafundisho hupenda maarifa; Bali yeye achukiaye kulaumiwa ni kama mnyama”. Napenda zaidi Biblia ya kiingereza inavyoweka Msatari huu katika namna njema zaidi angalia “Whoever loves discipline loves knowledge, but he who hates reproof is stupid” hii ni kwa mujibu wa ESV, “Whoever loves discipline loves knowledge, but whoever hates correction is stupid”NIV, unaweza kuona so kwa lugha nyepesi inayokubaliana na somo langu ningeweza kusema Kila apendaye Maonyo, au (Nidhamu) anapenda maarifa (Elimu), lakini kila achukiaye maonyo ni mpumbavu, Kwa hiyo utaweza kuona kuwa hekima na maaruifa na elimu vinapatikana sambamba na Nidhamu au maonyo au marudia.

6.       Nidhamu inaleta furaha na amani.

Kuishi kwa nidhamu kunasaidia kufanya mambo yafanyike vema na kwa wakati, ingawa mambo mengine yanaweza kujitokeza na kuzuia lakini bado nidhamu inaweza kufanya mambo kufanyika kwa haraka na ufasaha  na hivyo kusababisha furaha na amani. Aidha biblia inaeleza kuwa kama mtoto amefunzwa vema atakustarehesha na kuifurahisha nafsi yako, lakini kama ameachiliwa atakuwa ni aibu kwa mama yake Mithali 29:15, 17 Fimbo na maonyo hutia hekima; Bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye., Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako”.

Makusudi ya Nidhamu katika mpango wa Mungu.

Ingawa neno nidhamu lina maana pana sana katika tafasiri yake kwa vila inahusu mambo mengi sana hata hivyo ni muhimu tukaangalia pia kwa kina makusudi ya nidhamu hasa katika mpango nwa Mungu, Maandiko ya Msingi yana mengi ya kutufunza kuhusu makusudi ya nidhamu katika mpango wa Mungu tunapoyaangalia maandiko ya msingi utaweza kuona kuna sababu kadhaa kama tano hivi ya makusudi ya Nidhamu katikia mpango wa Mungu

Waebrania 12:5-11tena mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana, Wala usizimie moyo ukikemewa naye; Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi? Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake. Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.

a.       Kwa kusudi la kurekebisha mwenendo usiofaa.

Biblia katika kitabu cha waebrania imeonya kuwa ni jambo la kutisha sana kuanguka katika mikono ya Mungu, yaani kuachana na neema na katika sura ya kumi na moja imekazia sana swala zima la mashujaa wa imani na kututaka tujifunze kupitia wao na kisha sura ya 12 inatutia moyo namna ya kufanya ili tuweze kufanikiwa kama wao kwa ufupi mashujaa wote wa imani walikuwa watu wenye nidhamu, na kutokana na kujitia nidhamu waliweza kufanikiwa na kuzirithi ahadi za Mungu
Kizazi cha ma hausegirl tulicho nacho leo, watoto wanalelewa boarding tangu wakiwa wachanga kwenye vituo vya day care, waliokosa malezi sahihi ya baba, wajomba mashangazi na wazazi wenye nidhamu nikizazi kilichopoteza muelekeo, kama kanisa halitakuwa  makini (Sirius) katika swala zima la nidhamu tutakuwa tumepoteza mwelekeo, ili tuweze kufanikiwa lazima turudi katika mpango wa Mungu wa kutoa maonyo kwa maneno na matendo YASAR (MARUDIA) YAKASH (MAKEMEO) Waebrania 12:5 “tena mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana, Wala usizimie moyo ukikemewa naye” hapa maneno yanayotumika Marudia au Makemeo yanakaziwa, haya maonyo yanataka wote wazazi na watoto kwa ujumla wasisahau wasichukulie kirahisi maonyo na makemeo ya Bwana yaani kutia nidhamu na kurekebisha tabia mbaya.

b.      Kwa kusudi la kuonyesha kujali na upendo.

Waebrania 12:6-9Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye. Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye? Basi kama mkiwa hamna kurudiwa, ambako ni fungu la wote, ndipo mmekuwa wana wa haramu ninyi, wala si wana wa halali. Na pamoja na hayo tulikuwa na baba zetu wa mwili walioturudi, nasi tukawastahi; basi si afadhali sana kujitia chini ya Baba wa roho zetu na kuishi?” Moja ya njia iliyo njema zaidi ya kuonyesha kuwa unamjali mtoto wako na kumpenda ni kuhakikisha kuwa wanakuwa na nidhamu, namna yoyote ile ya kumfanya mtoto ajisikie kuwa yuko salama kufanya na kuishi vyovyote atakavyo ni makosa makubwa sana ambayo yatatuletea huzuni kubwa lakini kama tutakubali kuumia wakati wa kuwatiisha na kuwafunza nidhamu basi ni wazi kuwa tutapata raha Mithali 29: 15, 17 “Fimbo na maonyo hutia hekima; Bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye, Mrudi mwanao naye atakustarehesha; Naam, atakufurahisha nafsi yako.” Hatuwezi kuwa na hekima kuliko maandiko wala hatuwezi kuwa na ufahamu kuliko Mungu, kama Mungu katika neno lake anataka tuchukue hatua stahiki dhidi ya watoto wetu ni wazi kuwa lazima kufanya kitu kwaajili ya watoto wote wa Mungu kwa upendo wenye kuonyesha kuwa tunajali badala ya kusubiri majuto ndio maana mwanafalsafa - John Rohn akasema   “Kila mmoja anapaswa kuchagua njia mojawapo kati ya mbili, maumivu ya Nidhamu au maumivu ya Majuto”  Tusipochukua hatua za kuishi kwa nidhamu maana yake tutajuata baadaye, na ndio maana Mungu katika mpango wake anatuonyesha upendo kupitia maonyo, Kama hatuna kuonywa ni dhahiri sisi tumekuwa wana wa haramu na maisha yetu yatajaa taabu na majuto mengi.

c.       Kwa kusudi la kufundisha utii

Tunapojifunza Nidhamu katika maisha yetu maana yake tunajifunza utii, tunajiweka katika neema ya Mungu, tunajifunza kutii kwa upendo, japo wakati wa mafunzo linaweza kuwa jambo lenye kuuma sana lakini linatupa matunda ya milele, mwanzoni itakuwa ni swala lenye kuumiza kwa nje lakini likihamia ndani linaleta ustaarabu wa kudumu, Biblia inasema katika Waebrania 12:11 “Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” Unaweza kuona kuwa kila adhabu, yaani nidhamu wakati wa kuijifunza haionekani kuwa ni furaha ni kama maumivu lakini ina faida kubwa baadaye.

d.  Nidhamu inatupa kuwa na Hekima 



Mungu ndiye chanzo cha Hekima na ni mkarimu kwa kila mmoja anasema katika Yakobo 1:5 “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.” Mojawapo ya njia ya kupokea hekima kutoka kwa Mungu ni pamoja na na kukubali maonyo, na hekima atakayotupa itatuongoza na kutusaidia kuwa waadilifu, watakatifu na kutuepusha na madhara ya kiroho Mithali 2:10-12 “Maana hekima itaingia moyoni mwako, Na maarifa yatakupendeza nafsi yako; Busara itakulinda; Ufahamu utakuhifadhi., Ili kukuokoa na njia ya uovu, Na watu wanenao yaliyopotoka;”, unaweza kuona hatimaye tutakuwa ytayari kumpenda Mungu na kumwabudu pasipo hofu, hatimaye kuingia katika uzima wa milele , Mungu anataka tuwe watakatifu na hivyo hututia nidhamu Waebrania 12:10Maana ni hakika, hao kwa siku chache waliturudi kama walivyoona vema wenyewe; bali yeye kwa faida yetu, ili tuushiriki utakatifu wake”. Yuda 1;21jilindeni katika upendo wa Mungu, huku mkingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo, hata mpate uzima wa milele.” 

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

0718990796

Alhamisi, 30 Agosti 2018

Maisha Bila Mipaka!


Warumi 8:38 -39.Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,  wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”


Utangulizi:

Nick Vujicic ni moja ya walemavu ambaye alizaliwa akiwa hana miguu wala mikono na wataalamu wa kitabibu walishindwa kuelewa sababu kuu ya ulemavu wake na hata namna ya kumtibu, lakini kwa sasa amejipatia umaarufu mkubwa sana duniani kutokana na bidii kubwa aliyo nayo na mafanikio makubwa sana katika maisha akiwa hana viungo hivyo muhimu yeye mwenyewe anasema Namnukuu  I was born without arms or legs and given no medical reason for this condition. Faced with countless challenges and obstacles, God has given me the strength to surmount what others might call impossible.” “Nalizaliwa pasi na mikono wala miguu na sikupewa sababu za kitabibu za kuzaliwa hivyo, Nimekumbana na changamoto nyingi na vikwazo, Mungu amenitia nguvu kupambana na hali ngumu ambazo wengine walizishindwa” Ni mwanzilishi wa shirika liitwalo Life without Limbs na Mwinjilisi mkubwa sana Duniani na pia ni Motivational speaker  ambaye aliweza kupitia vikwazo na magumu na kuvishinda kwa nguvu na tumaini lililo katika Kristo Yesu.

Siri kubwa ya mafanikio ya Mlemavu huyu Duniani ni “Mungu alimtia Nguvu” Kumbe kwa Mungu hakuna lisilowezekana, tunaishi katika misuguano na kujikuta tumezingirwa na mipaka pande zote dunia ikikulazimisha kusalimu amri na kuishia hapo ulipoishia au hapo ulipokatia tamaa kwa sababu hujatambua chanzo  cha nguvu zako, kwa hiyo dunia na mazingira na vikwazo vimekukwamisha hapo ulipo umeambiwa haiwezekani, haitowezekana, huwezi lolote, hustahili kitu hutoweza, ndugu zako walishindwa, Mfupa uliomshinda fisi wewe mbwa utauweza wapi.

Siri ya mafanikio.

Siri ya mafanikio ya watu kama kina Nick Vujicic  na wengineo ambao tunawasoma katika maandiko ni NGUVU ZA MUNGU nyuma ya maisha yao, Maandiko ni ufunuo wa Nguvu za Mungu, unaposoma na kuona shuhuda za watu kama kina Yusufu kutoka gerezani na kuwa mtu mwenye mamlaka kubwa duniani ni Matokeo ya Nguvu za Mungu, Unaposoma habari za kusisimua za kina Daniel na Hekima kubwa walizokuwa nazo na uwezo mkubwa katika kupambanua mambo ni kuwa siri kubwa ni Nguvu za Mungu, Roho wa Mungu alikuwa juu yake, hii ndio siri iliyowafanya waonekane kuwa ni wa kipekee.

Kila mtu Duniani Mungu alimuumba kwa kusudi, na moja ya kusudi la kuumbwa kwako ni ili ufanikiwe na kuwa Baraka kubwa kwa wengine pia, Lakini ni nguvu ya Mungu kiasi gani unayohitaji ndiyo itakayoamua hatima ya maisha yako, wengi tunaishi maisha yenye mipaka Lakini Mungu hakukusudia iwe hiyo! Hata kidogo, Mungu ametupa Nyenzo ya kutusaidia kufikia kiwango kikubwa na cha juu cha mafanikio Nguvu hizo ni Roho Mtakatifu.

·         Mwanzo 41:38-40Farao akawaambia watumwa wake, Tupate wapi mtu kama huyu, mwenye roho ya Mungu ndani yake? Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe.”

·         Daniel 5:10-12Basi malkia, kwa sababu ya maneno ya mfalme na ya wakuu wake, akaingia katika nyumba ya karamu; malkia akanena, akasema, Ee mfalme, uishi milele; fikira zako zisikufadhaishe; wala uso wako usibadilike. Yuko mtu katika ufalme wako, ambaye roho ya miungu watakatifu inakaa ndani yake; na katika siku za baba yako nuru na ufahamu na hekima zilionekana ndani yake; na mfalme Nebukadreza, baba yako, naam, mfalme, baba yako, akamfanya kuwa mkuu wa waganga, na wachawi, na Wakaldayo, na wanajimu;      kwa kuwa roho njema kupita kiasi, na maarifa, na ufahamu, na uwezo wa kufasiri ndoto, na kufunua maneno ya fumbo, na kufungua mafundo, zilionekana katika Danieli huyo, ambaye mfalme alimwita Belteshaza. Basi na aitwe Danieli, naye ataionyesha tafsiri.” 

·         1Wakoritho 2:4-5Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu,  ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu”.

     Paulo hakuhubiri Falsafa, hakutumia ushawishi wa kiakili lakini alifanikiwa sana katika injili kuliko wote kwa sababu alikuwa na Nguvu za Mungu

Kuishi bila Nguvu za Mungu ni kujiweka katika hatari kubwa sana, lakini ili tuweze kuwa washindi ni lazima tuishi katika uwepo na nguvu za Mungu, Mungu alituleta Duniani kama watu maalumu, alitukomboa ili tuwe Makuhani na Wafalme na watawala wa Dunia Ufunuo 5:10ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu ya nchi.” Mwanadamu ni kiumbe cha thamani sana, Mungu amewadhimisha wanadamu kuliko malaika lakini ili tuweze kuwa na mafanikio Duniani na kuitawala kama wafalme na makuhani hatuna budi kujiungamanisha na Nguvu za Mungu, Mungu hafurahii kutuona tukiishi kwa mipaka kwa ujumla hatukuumbwa ili tuje kuteseka na kufungiwa duniani bali Mungu alikusudia tuitawale dunia na kila kilichomo Haya yanawezekana tu kama tutajiachilia katika nguvu za Mungu na Roho wake hakuna jambo litakaloshindikana kwetu Zekaria 4:6-7.Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi. Nani wewe, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli utakuwa nchi tambarare; naye atalileta lile jiwe la kuwekwa juu kabisa pamoja na vigelegele vya, Neema, neema, ilikalie.”  Unaweza kuona sasa kama tunasumbuka katika Dunia hii, tumejawa hofu, tumejawa kukata tamaa, tumepoteza ujasiri, tunalia, tunaugua, tunaonewa kuna kitu hakiko sawa ni kwamba hatujatambua kuwa sisi ni akina nani na Mungu ametuandalia Nini? Yesu alianza kupata umaarufu mkubwa mara moja tu alipokaliwa na Roho wa Mungu na kumruhusu aongoze maisha yake 

Luka 4:1Na Yesu, hali amejaa Roho Mtakatifu, alirudi kutoka Yordani, akaongozwa na Roho muda wa siku arobaini nyikani14 Yesu akarudi kwa nguvu za Roho, akenda Galilaya; habari zake zikaenea katika nchi zote za kandokando.” 

Yesu anarejea akiwa amejaa nguvu za Mungu, na tangu tukio hili utaweza kuona umaarufu wake ulienea katika nchi zote za kandokando ya Israel, Wanafunzi wa Yesu walikuwa waoga walijifungia chumbani kwa siku kadhaa lakini alipokuja Roho Mtakatifu mambo yalibadilika waliupindua ulimwengu, Bila Roho Mtakatifu, bila neema na bila nguvu za Mungu tutaendelea kuwa wanyonge na kuishi katika kiwango cha chini cha maisha bila mafanikio na maisha yenye mipaka mingi.

Katika Warumi 8:38-39Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo,  wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Paulo Mtume anazungumza kwa ujasiri unaotokana na uzoefu wake akikazia kwa msisitizo mkubwa sana wa imani ya kitume kuwa yeye sasa kutokana na Mambo ambayo Mungu amemfunulia, kutokana na jinsi Mungu alivyoufunua upendo wake kwetu, yeye pamoja na wengine wote wenye kuamini Hakuna kitu kinaweza kututenga na upendo wa Kristo, Hili halitokani tu na ufunuo mkubwa alioupata bali kazi kubwa ambayo Mungu amewatendea wanadamu, kwa kutuchagua, kwa kutufanya kuwa wana wake, ametambua kuna usalama Mkubwa katika Kristo na kuwa ni vigumu sana jambo lingine lolote kupingana na kusudi la Mungu, hivyo yote yanayoogopewa na wanadamu hayawezi kuwa mpaka wa kututenganisha na Mungu

·         Kifo hakina ubavu – Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake
·         Maisha hayana ubavu– Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake
·         Mamlaka hazina ubavu– Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake
·         Serikali hazina ubavu– Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake
·         Malaika au mashetani – Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake
·         Mamlaka na falme– Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake
·         Mambo yaliyopo yaani sasa na yajayo– Haiwezi kuwa tishio la kuharibu kusudi la Mungu kwa sababu ya nguvu yake

Kama Nick ameweza kufanikiwa na hakuzaliwa akiwa na mikono wala miguu, bali kwa nguvu za Mungu ameweza kuwa mtu maarufu Duniani na kufanikiwa katika kuwatia moyo wengine wote, wanaofikiri kuwa wao si kitu, wanaofikiri kuwa hawawezi, Maandiko yanatutaka tuinue macho yetu na kumuangalia Mungu Nguvu zake zinatosha kutupeleka katika level nyingine na kutufanya tufanye mambo yasiyokuwa ya kawaida, Hakuna sababu ya kukata tamaa, tuitafute Nguvu ya Mungu, tuutafute upako na kufanya kazi zetu kwa bidii hakuna kitakachoweza kusimama na kuzuia kusudio la Mungu katika maisha yako, usikubali kukatishwa tamaa, usikubali hata kujikatisha tamaa, usikubali maneno yaliyonenwa juu yako, wao sio Mungu yuko Mungu mwenye uweza usio na mipaka hakuna wa kukuwekea mpaka Mungu amekupa uhuru wa kuyafurahi maisha katika nguvu zake, kaa katika hizo na utafurahia sana. Ziko sababu za kuishi maisha yasiyo na mipaka kutokana na upendo mkubwa sana wa Mungu wetu na mambo ambayo ametukarimia.

1.       Hakuna hukumu ya adhabu Rumi 8:1
2.       Roho wa aliyemfufua Kristo anaishi ndani yetu 11
3.       Roho anatuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa 26
4.       Mungu yuko upande wetu 31
5.       Aliweza kumtoa Yesu kwaajili yetu 32
6.       Hakuna wa kuwashitaki wateule 33
7.       Sisi ni washindi na zaidi ya kushinda 37

Nakuombea Mungu akuvike Nguvu zake ili usiishi katika mipaka uliyowekewa au kujiwekea Bali ujae nguvu za Mungu na uweza wake

Na. Mkuuwa wajenzi mwenye Hekima.
Rev. Innocent Kamote.

Jumatano, 29 Agosti 2018

Habari za Mapito ya Zamani!


Yeremia 6:16Bwana asema hivi, Simameni katika njia kuu, mkaone, mkaulize habari za mapito ya zamani, I wapi njia iliyo njema? Mkaende katika njia hiyo, nanyi mtajipatia raha katika nafsi zenu. Lakini walisema, Hatutaki kwenda katika njia hiyo.”



Kama Jamii yoyote itapoteza Historia, maana yake imepoteza Muelekeo” Rev Innocent Kamote Mkuu wa wajenzi mwenye hekima

Utangulizi. 

Ni muhimu kufahamu kuwa Maisha yetu hayawezi kuwa na furaha ya kweli kama mara kwa mara hatutajifunza kutokana na Historia, Historia ni mwalimu mkubwa sana wa kutusaidia kujua tunatoka wapi na tuko wapi na tunakwenda wapi, “Kama jamii yoyote itapoteza Historia, maana yake itapoteza muelekeo” Na mkuu wa wajenzi mwenye Hekima, Kwa msingi huo kuna umuhimu wa kujifunza kutokana na Historia, semi kadhaa za Kihistoria zinatusaidia kujua umuhimu wake
·         Historia sio mzigo katika kumbukumbu zetu bali ni Mwangaza wa Nafsi zetu lord Acton- History is not a burden on the memory but an illumination of the soul – Lord Action.
·         Mtu asiyejali Historia ni sawa na Kiziwi ni sawa na kipofu – Aldof Hittler  The man who has no sense of history, is like a man who has no ears or eyes. Adolf Hitler
·         Baada ya kufanya makosa au kuteseka, na kupoteza muelekeo Mtu mwenye akili huangalia nyayo zake – Napoleon - After making a mistake or suffering a misfortune, the man of genius always gets back on his feet. Napoleon
·         Tunasoma kutokakatika Historia kile ambacho Hatujakisoma katika Historia – Desmond Tutu - We learn from history that we don’t learn from history! Desmond Tutu
·         Raia wenzangu, Hatuwezi kuiepuka Historia Abrahamu Lincoln - Fellow citizens, we cannot escape history. Abraham Lincoln

Kama tunavyoweza kuona hapo juu, umuhimu wa Historia ni wazi kuwa neno la Mungu pia limeandikwa kwa makusudi ya kutukumbusha na kutufundisha kutokana na Historia Biblia inasema hivi :-  

1Wakoritho 10:1-11Kwa maana, ndugu zangu, sipendi mkose kufahamu ya kuwa baba zetu walikuwa wote chini ya wingu; wote wakapita kati ya bahari; wote wakabatizwa wawe wa Musa katika wingu na katika bahari; wote wakala chakula kile kile cha roho; wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo. Lakini wengi sana katika wao, Mungu hakupendezwa nao; maana waliangamizwa jangwani. Basi mambo hayo yalikuwa mifano kwetu, kusudi sisi tusiwe watu wa kutamani mabaya, kama wale nao walivyotamani.Wala msiwe waabudu sanamu, kama wengine wao walivyokuwa; kama ilivyoandikwa, Watu waliketi kula na kunywa, kisha wakasimama wacheze.Wala msifanye uasherati, kama wengine wao walivyofanya, wakaanguka siku moja watu ishirini na tatu elfu. Wala tusimjaribu Bwana, kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka.Wala msinung'unike, kama wengine wao walivyonung'unika, wakaharibiwa na mharabu. Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.” Kumbe kila mmoja anaweza kujifunza kitu kutokana na Historia.

Katika kifungu cha maandiko Yeremia 6:16 Mungu anatoa wito kwa wana wa Israel, yaani wayahudi kuuliza kwa habari za mapito ya zamani, yaani katika wakati huu kulikuwa na ukengeufu mkubwa na mmomonyoko mkubwa wa uadilifum watu walikuwa wakifuata njia zao wenyewe na hivyo walipoteza raha na amani ya kweli, Taifa, Kanisa, Jamii na kila mmoja anapaswa kuangalia njia zake na kujifunza kutokana na Historian a kuangalia njia za Zamani na kujikagua kama tuko sahihi au lah nini kimepoteza furaha tuliyokuwa nayo, ka sababu gani tupo hapo tulipo? Kwa nini hilo au lile linatokea? Nabii Yeremia alitumwa na Mungu kuwakubusha wayahudi kuifuata njia ile ili waweze kufanikiwa  

Yeremia 7:22-23Maana sikusema na baba zenu, wala sikuwaamuru kwa habari za sadaka za kuteketezwa na dhabihu, siku ile nilipowatoa katika nchi ya Misri; lakini naliwaamuru neno hili, nikisema, Sikilizeni sauti yangu, nami nitakuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu; mkaende katika njia ile yote nitakayowaamuru mpate kufanikiwa.”       

Unaweza kuona iko njia ya mafanikio ambayo Mungu aliwaonyesha Israel Tangu zamani lakini wao walikuwa wamekaidi kuifuata na hivyo maisha yao yalijaa taabu na kukosa raha na amani,  Hakuna namna yoyote ambayo tunaweza kuwa na amani ya kweli endapo tutakuwa nje ya njia ya kweli au kama tumeiacha njia ya Mungu, Kama Mungu anatupenda kwa dhati anachokifanya ni kuwatuma watumishi wake manabii wake kutukumbusha kurudi katika njia, Mungu anataka watu wake wajifunze kutokana na Historia Israel walipofanya vema na kuzishika nzjia za Mungu Mungu aliwarudia na kuwa pamoja nao, lakini walipofanya mabaya Mungu aliwaacha na walipata tabu sana
Sisemi kwamba kila taabu inasababishwa na kuacha njia ya Mungu hapana lakini kuna raha kupitia taabu huku ukiwa na Mungu, na kuna utungu mkubwa kupitia taabu huku ukiwa umemuacha Mungu, Katika nyakati hizi tulizo nazo pia Mungu ametupa njia ya kuifuata 

Yohana 14:6Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” 

Linapotokea jambo Gumu la kuumiza na kukatisha tamaa ni muhimu kuangalia Habari ya mapito ya zamani, baba zetu na watakatifu waliotutangulia walifanya nini? Wao walimtegemea Mungu hawakuzitegemea akili zao wenyewe, walimuweka Mungu mbele, walimfamya Mungu kuwa kinga yao, walimfanya yeye kuwa mtetezi wao, walimfanya kuwa ngao yao, walimfanya kuwa tumaini lao, walimgeukia yeye na kwa sababu hiyo walipata raha nafsini mwao, Historia inaonyesha kuwa Yesu hajawahi kumuangusha mtu aliyemtegemea  

Mathayo 11:28-29Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu;

Yesu amewahakikishia raha wale wote wanaoshikamana naye, Hakuna namna unaweza kujikwamua katika jambo lolote bila ya Yesu, Taifa jamii na kanisa kama tunataka kufanikiwa basi tunapaswa kuangalia njia zetu kama tumekengeuka tukajifunze habari za mapito ya zamani na kuangalia kwamba tunaenenda sawasawa au hapana? Tumfanye Yesu kuwa tegemeo letu, ngao yetu, kimbilio letu, mwamba wetu, tumaini letu na tukimtegemea yeye na kutii maelekezo yake tutapata raha nafisni mwetu, 
Tenzi namba 16 Kumtegemea Mwokozi kwangu tamu kabisa…………..

Na Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.

Jumatatu, 13 Agosti 2018

Bwana yu karibu na waliovunjika Moyo:-

Andiko la msingi: Zaburi 34:17-19Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa. Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote.”

 "Bwana yu Karibu na Waliovunjika Moyo, Na waliopondeka Roho Huwaokoa Zaburi 34:18"

Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa tuwapo duniani wanadamu tunazungukwa na changamoto nyingi, kwa kawaida Mungu ameruhusu tuweze kupitia nchangamoto za aina mbalimbali kwa makusudi mbalimbali, aidha ya kutufundisha ama kutufanya tukue kiroho, kihekima na kimaadili lakini wakati mwingine kwa sababu anazozijua yeye mwenyewe, hata hivyo wakati tunapopitia changamoto hizo, mara kadhaa wanadamu huwa tunakata tamaa, na tunaweza kujiuliza kama hivi Mungu anaona kweli? Hivi Mungu yupo? Kama yupo kwa nini anaachia jambo kama hili, kwa nini hakuzuia, kwa nini hakunitahadharisha mapema? Mbona yuko kimya Hivi yeye yupo kweli?tunaweza kufikiri kuwa Mungu ametuacha.

Katika nyakati hizi ngumu ndio nyakati ambazo ni rahisi kumuwazia Mungu kwa upumbavu, yaani kumfikiria Mungu kwa namna isiyofaa,Watakatifu waliotutangulia waliokuwa na ujuzi kuhusu Mungu walifahamu kuwa wanadamu wana changamoto nyingi maandi yanasema hivi kupitia Ayubu;-

Ayubu 14: 1Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke Siku zake za kuishi si nyingi, naye hujaa taabu.” 

Wote tunafahamu jinsi Ayubu alivyopitia majaribu na mateso Magumu lakini Biblia inatuambia kuwa Ayubu katika dhiki yake hakuwahi kumkufuru Mungu wala kumuwazia Mungu kwa upumbavu,

Ayubu 1:20-22Ndipo Ayubu akainuka, akalirarua joho lake, kisha akanyoa kichwa chake, na kuanguka chini, na kusujudia; akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; Bwana alitoa, na Bwana ametwaa; jina la Bwana na libarikiwe. Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.”

Hali kama hii ndio iliyomtokea mwandishi wa Zaburi hii, kwa mujibu wa masimulizi ya tamaduni za kiyahudi Zaburi hii imethibitika kuwa iliandikwa na Daudi, au moja ya viongozi wa kwaya wa Daudi, na mazingira ya uandishi wa zaburi hii ulitokana na tukio la Daudi kunusurika katika hatari mbaya iliyokuwa ikimkabili, Zaburi hii iliandikwa mara baada au kwa kusudi la kukumbuka namna Daudi alivyonusurika katika hatari ngumu katikati ya mfalme wa wafilisti alipokuwa akitafutwa na Sauli ili aweze kuuawa Katika Mazingira haya magumu Daudi aliweza kujifanya mwendawazimu ili kupata namna ya kuondoka mikononi kwa Akishi mfalme wa wafilisti.

1Samuel 21:10-15 Basi Daudi akaondoka, akakimbia siku ile, kwa hofu ya Sauli, akamwendea Akishi, mfalme wa Gathi. Nao watumishi wa Akishi wakamwambia, Je! Huyu siye yule Daudi, mfalme wa nchi? Je! Hawakuimbiana habari zake katika ngoma zao, kusema,Sauli amewaua elfu zake,Na Daudi makumi elfu yake. Naye Daudi akayatia maneno hayo moyoni mwake, akamwogopa sana Akishi, mfalme wa Gathi. Akaubadilisha mwenendo wake mbele yao, akajifanya mwenye wazimu mikononi mwao, akakuna-kuna katika mbao za mlango, na kuyaacha mate yake kuanguka juu ya ndevu zake. Ndipo huyo Akishi akawaambia watumishi wake, Angalieni, mwaona ya kuwa mtu huyu ana wazimu; basi, maana yake nini kumleta kwangu? Je! Mimi nina haja ya watu wenye wazimu, hata mmemleta kiumbe hiki ili aonyeshe wazimu wake machoni pangu? Je! Huyu ataingia nyumbani mwangu?

Ni katima Mazingira ya aina hii ndio Daudi alipoimba zaburi hii ya 34 akzizungumza maneno ya kushangaza sana hata baada ya tukio hili gumu namna hii Daudi aliweza kumsifu Mungu, alionyesha kuwa Mungu ni tumaini lake, hakutaka kulalamika alitaka watu wote wawe wanyenyekevu wamtumaini Mungu wamweleze shida zao na kuwa yeye atawaitikia kwa kuwa Ni Mungu aliye karibu na watu wake angalia maneno yake hiyo isiyo ndefu sana Zaburi 34:1-22

1. Nitamhimidi Bwana kila wakati, Sifa zake zi kinywani mwangu daima.
2. Katika Bwana nafsi yangu itajisifu, Wanyenyekevu wasikie wakafurahi.
3. Mtukuzeni Bwana pamoja nami, Na tuliadhimishe jina lake pamoja.
4. Nalimtafuta Bwana akanijibu, Akaniponya na hofu zangu zote.
5. Wakamwelekea macho wakatiwa nuru, Wala nyuso zao hazitaona haya.
6. Maskini huyu aliita, Bwana akasikia, Akamwokoa na taabu zake zote.
7. Malaika wa Bwana hufanya kituo, Akiwazungukia wamchao na kuwaokoa.
8. Onjeni mwone ya kuwa Bwana yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini.
9. Mcheni Bwana, enyi watakatifu wake, Yaani, wamchao hawahitaji kitu.
10. Wana-simba hutindikiwa, huona njaa; Bali wamtafutao Bwana hawatahitaji kitu cho chote kilicho chema.
11. Njoni, enyi wana, mnisikilize, Nami nitawafundisha kumcha Bwana.
12. Ni nani mtu yule apendezwaye na uzima, Apendaye siku nyingi apate kuona mema?
13. Uuzuie ulimi wako na mabaya, Na midomo yako na kusema hila.
14. Uache mabaya ukatende mema, Utafute amani ukaifuatie.
15. Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao.
16. Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani.
17. Walilia, naye Bwana akasikia, Akawaponya na taabu zao zote.
18. Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho huwaokoa.
19. Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana humponya nayo yote.
20. Huihifadhi mifupa yake yote, Haukuvunjika hata mmoja.
21. Uovu utamwua asiye haki, Nao wamchukiao mwenye haki watahukumiwa.
22. Bwana huzikomboa nafsi za watumishi wake, Wala hawatahukumiwa wote wamkimbiliao.

Unaweza kuona hatupaswi kukata tamaa wala kuvunjika Moyo katika mazingira yoyote, katika hali Ngumu zinazotukabili Mungu na aendelee kuwa Mungu wetu, tusimuwazie kwa Upumbavu tuendelee kuuona mkono wake, na kumtegemea yeye katika hali zozote, tusinungunike, bali afadhali kumlilia yeye, 

Manunguniko yanaondoa Baraka za Mungu, Manunguniko, yanamkasirisha sana Mungu, badala ya kulalamika na kunung’unika ni afadhali kumlilia yeye na kumhimidi yeye Daudi anasema atamhimidi Bwana kila wakati maana yake katika hali yoyote na Mungu yu Karibu na waliovunjika moyo na wanaonyenyekea kwake yeye huwakomboa huwahurumia na kuitikia kilio chao.
Mungu aitikie kilio chako Ndugu yangu, Mungu na awe karibu nawe Mungu asikupungukie Mungu asikufanye ukufuru Usivunjike moyo, wakati unapopita katika Magumu, Mungu yuko Karibu, Mungu hajatutupa wala hajakutupa wewe anakujali yuko Karibu nawe mtafute wakati huu wa dhiki yako atakutokea nawe utasadiki ya kuwa Mungu amenituma nikuhakikishie kuwa Yuko Karibu nawe Bila shaka atakufuta Machozi yako leo, BWANA YU KARIBU NA WALIOVUNJIKA MOYO, NA WALIOPONDEKA ROHO HUWAOKOA.

Na. Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima