Jumatatu, 10 Oktoba 2022

Vazi la Yusufu!


Mwanzo 37:23-24Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.


Utangulizi:

Mojawapo ya viongozi wa kiroho ambao habari zao zimeandikwa kwa urefu sana katika maandiko ni pamoja na Yusufu, Yusufu anahesabika kama moya ya mababa wa Israel, ukiacha Abrahamu, Isaka na Yakobo, yeye ndio sababu kubwa kwa wana wa Israel kushuka Misri, kuna mambio mengi sana ya kujifunza katiika maisha ya Yusufu lakini moja wapo ya jambo la msingi na la muhimu sana tunalotaka kulizungumzia leo tena kwa kina ni pamoja na Vazi la Yusufu, vazi lake na nguo zake zinaonekana kuwa na mvuto wa kipekee na vilevile kuwa sababu ya mapito yake kuna nini kilipelekea hawa watu kumtenda machungu kisa kikianzia kwenye vazi? Maandiko yanasema hivi;-

Mwanzo 49:22-24 “Yusufu ni mti mchanga wenye kuzaa, Mti mchanga wenye kuzaa karibu na chemchemi, Matawi yake yametanda ukutani. Wapiga mishale walimtenda machungu, Wakamtupia, wakamwudhi, Lakini upinde wake ukakaa imara, Mikono yake ikapata nguvu, Kwa mikono ya Mwenye Enzi wa Yakobo; Kwa jina la mchungaji, yeye jiwe la Israeli,”

Maandiko hayatuambii kuwa Yusufu aliwakosea Ndugu zake, lakini yaonekana wazi kuwa ndugu zake walichukizwa naye na sababu kubwa inaweza kuwa ni wivu wenye uchungu na hasira kali juu yake, lakini Bwana alikuwa pamoja naye, matukio ya aina hii yanaweza pia kuwako katika jamii inayotuzunguka leo, tunaweza kujikuta katika wakati mgumu sana kwa sababu ya mafanikio ya aina mbalimbali na wakati mwingine kwa sababu ya kusudi la Mungu lililoko ndani yetu!  Na anayepingana na kusudi hilo kwa vyovyote vile ni adui Shetani ambaye wakati mwingine anaweza kuwatumia watu tena watu wa karibu.

Vazi la Yusufu!

Kisa cha kusikitisha cha maisha machungu ya Yusufu kinaanzia na namna Yusufu alivyonunuliwa na kuvishwa vazi la thamani kubwa sana na baba yake biblia inaelezea vazi hilo katika

Mwanzo 37:3-4 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani.”

Maandiko yanaelezea kuhusu kanzu hii ndefu, na matoleo mengine ya kibiblia yanaitaja kama nguo yenye rangi nyingi, vazi hili la thamani lilikuwa ni vazi la gharama kubwa na kwa mujibu wa historia ya kibiblia lilikuwa ni vazi lililoweza kumtambulisha mtu kuwa ni mwana mfalme au mwana wa kifalme (Prince au Princess)

2Samuel 13:18 “Naye alikuwa amevaa kanzu ndefu; kwa kuwa kwa nguo hizo huvikwa binti za mfalme waliokuwa wanawali. Ndipo mtumishi wake akamleta nje, akafunga mlango nyuma yake.”

Kanzu hii au vazi kinabii ilikuwa inaashiria kuwa Israel au Yakobo amekusudia kumpa heshima kubwa na ya tofauti mwanaye aliyeitwa Yusufu, na kuanza kumfunza Yusufu kuwa mtawala na mfalme, Vazi hili alilotengenezewa na baba yake lilikuwa ni ishara ya upendeleo, neema na heshima maalumu aliyokuwa ametunukiwa Yusufu aidha na baba yake au na Mungu lakini kwa vile baba yake alikuwa nabii alikuwa anaashiria kuwa Yusufu hakuwa mtu wa kazi ngumu yeye alikuwa ni msimamizi na mwangalizi na kazi zake ni usimamizi kwani vazi lile halikuwa vazi la kazi bali vazi la kitawala! Lilikuwa ni vazi la kibali, kupendwa na neema ya Mungu

Vazi maalumu kwa Yusufu!          

Kwa nini Yakobo alimtengenezea Yusufu vazi maalumu? Maandiko yanaonyesha kwanza kabisa Kuwa Yakobo alimpenda Raheli sana kuliko Lea, jambo hili linaweza kuwa lilionekana wazi kwa watoto wa Yakobo ambao waliona wazi kuwa mama zao hawakupendwa kama alivyopendwa mama yake Yusufu,

Mwanzo 29:30-31 “Akaingia kwa Raheli naye, akampenda Raheli kuliko Lea, akatumika kwa ajili yake miaka saba mingine. BWANA akaona ya kwamba Lea hakupendwa, naye akafungua tumbo lake; bali Raheli alikuwa hazai.”

Unaona kwa hiyo ni wazi kuwa kutokana na Yakobo kumpenda sana Raheli kuliko Lea ilikuja kuwa rahisi vilevile kwa Yakobo kumpenda Yusufu kuliko watoto wengine japo hii ni dhana tu ya kibiblia na kitheolojia  

Mwanzo 30:22-24 “Mungu akamkumbuka Raheli; Mungu akamsikia, akamfungua tumbo. Akapata mimba, akazaa mwana, akasema, Mungu ameondoa aibu yangu. Akamwita jina lake Yusufu, akisema, BWANA aniongeze mwana mwingine.”

Raheli alipokuja kumzaa Yusufu pia alimpa jina Yufufu ambalo maana yake Bwana ameniondolea aibu yangu, kwa msingi huo kinabii pia mtoto huyu alikuwa anahusika na kuondoa aibu ya mama yake wote tutakuwa tunakumbuka kuwa mara baada ya anguko la Mwanadamu katika bustani ya Edeni Adamu na Eva walijisikia aibu, walijiona wako uchi na Mungu aliwatengenezea vazi ili kuifunika aibu yao au kuwaondolea aibu kumbuka

Mwanzo 3:21 “BWANA Mungu akawafanyia Adamu na mkewe mavazi ya ngozi, akawavika.” Yakobo alichokifanya kwa Mwanaye Yusufu, na jina alilopewa Yusufu na Vazi alilotengenezewa baadaye na Yakobo yalikuwa na maana sawa na kile Mungu alimfanyia Adamu na mkewe kwa kuwavika mavazi ya kuwaondolea aibu, maana yake Mungu aliwapa Heshima iliyokuwa imepotea na vilevile Yusufu kutengenezewa vazi lile maalumu ilikuwa ni Ishara ya Heshima kubwa kwake!,  na kinabii ni kijana ambaye angekuja kuiondolea aibu familia yake na kuiifadhi wakati wa dhiki, ukiacha heshima hii kijana huyu alikuwa mwadilifu na alijifunza mambo mengi kuhusu Mungu kutoka kwa baba yake na mara kwa mara ndiye aliyekuwa akitoa ripoti ya taarifa ya watoto wote wa Yakobo kwa  na kwa bahati mbaya wengi wao hawakuwa na tabia njema mwanzoni  ukilinganisha na Yusufu ona,

Mwanzo 37:2 “Hivi ndivyo vizazi vya Yakobo. Yusufu, aliyekuwa mwenye miaka kumi na saba, alikuwa akichunga kondoo pamoja na ndugu zake; naye alikuwa kijana pamoja na wana wa Bilha, na wana wa Zilpa, wake wa baba yake. Yusufu akamletea baba yao habari zao mbaya.”

Kwa hiyo utaweza kuona kutokana na usafi wa Yusufu, alionekana kama kikwazo kikubwa cha matendo maovu ya kaka zake, pia alionekana kama mbeya kwa sababu angeleleza taarifa zao mbaya walizokuwa wakizifanya, achilia mbali Ndoto zake za kiutawala ambazo zilikuja kuongeza chuki kubwa kwani sio tu, baba yake alikusudia kumuheshimu sana Yusufu, lakini sasa inaonekana kuwa hata Mungu alikuwa amekusudia kumuheshimu sana Yusufu kuliko nduguze na kumuinua juu kiutawala ona.

Mwanzo 37:5-11 “Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia; akawaambia, Tafadhalini, sikieni ndoto hii niliyoiota. Tazama, sisi tulikuwa tukifunga miganda shambani, kumbe! Mganda wangu ukaondoka ukasimama, na tazama, miganda yenu ikazunguka ikainama mbele ya mganda wangu. Ndugu zake wakamwambia, Je! Kweli wewe utatumiliki sisi? Nawe utatutawala sisi? Wakazidi kumchukia kwa ajili ya ndoto yake, na kwa maneno yake. Akaota tena ndoto nyingine, akawaambia ndugu zake, akasema, Angalieni, nimeota ndoto nyingine; na tazama, jua na mwezi na nyota kumi na moja zikaniinamia. Akawaambia baba yake na ndugu zake; baba yake akamkemea akamwambia, Ni ndoto gani hii uliyoiota? Je! Mimi na mama yako na ndugu zako tutakuja tukusujudie hata nchi? Ndugu zake wakamhusudu; bali baba yake akalihifadhi neno hili.”

Ndoto za Yusufu ulikuwa ni unabii maalumu kutoka kwa Mungu kuwa Mungu angemuheshimu sana Yusufu na kuwa kwa vyovyote vila angekuja kuwatawala nduguze, sawa tu na baba yake alivyomtengenezea vazi maalumu, ni wazi kuwa Mungu alikuwa amekusudia kumuheshimu Yusufu, kila mmoja wetu kuna jambo ambalo kwalo Mungu amekusudia kukufanya maalumu kuliko wengine kuna heshima ambayo Mungu ameikusudia kwako wakati wote Mungu ana mpango mwema kwaajili yako

Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”

Hata hivyo ni Muhimu kufahamu kuwa kama Mungu baba yetu wa Mbinguni amekusudia kutuheshimisha sisi, ieleweke wazi kuwa shetani atapambana kwa kila namna kuhakikisha ya kuwa heshima hiyo inaharibiwa vazi la heshima ambalo Mungu anataka kukuvisha linaweza kuwa sababu kubwa sana ya vita vyako duniani lakini kumbuka wakati wote kusudi la Mungu ndilo litakalosimama

Kuharibiwa kwa vazi la Yusufu!

Tumejifunza na kuona kuwa vazi hili tayari kinabii linaashiria heshima ambayo Mungu amekusudia Kumpa Yusufu, lakini vilevile ni heshima ambayo Mungu amekusudia kumpa kila mmoja wetu, ni muhimu kufahamu kuwa kusudi kubwa la ibilisi au shetani ambaye ni adui wa makusudi yote ya Mungu ndani yetu ni pamoja na kupambana na ile Heshima ambayo Mungu ameikusudia katika maisha yetu, na hii ni kutaka kuiharibu na kuichafua ile heshima ili yamkini aweze kupambana na kusudi la Mungu lililoko ndani yetu, ona mfululizo wa matukio magumu unaambatana na maisha ya Yusufu yote yakilenga kuharibu vazi lake kusalitiwa, kuchukiwa bila sababu, kupanwa kuuawa au kuuzwa uhamishoni  na jambo la kwanza ilikuwa ni kumbua lile vazi.

Mwanzo 37:23-24 “Ikawa Yusufu alipofika kwa ndugu zake, wakamvua Yusufu kanzu yake, kanzu ile ndefu aliyoivaa, wakamtwaa wakamtupa katika birika; na hiyo birika ilikuwa tupu, hamna maji.”

Unaweza kuona chuki dhidi ya Yusufu haikuwa juu yake mwenyewe tu lakini ilikuwa na juu ya ile kanzu, vita kali ilikuwa dhidi ya vazi la Yusufu, na Nduguze hawakuishia hapo tu walihakikisha kuwa wanaliharibu vazi lile na kumtumia salamu baba yake ili yamkini naye aweze kujuta kwa kumuandalia Yusufu vazi kama lile ona

Mwanzo 37:31-34 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi.”

Unaona kimsingi chuki, na husuda juu ya Yusufu kwa ndugu zake haikutokana na nafsi zao tu kwani wao walimalizia hapo, lakini ni wazi kuwa chuki hii inatoka kwa yule adui, adui hana mpango mwema na vazi la Yusufu la aina yoyote ile fikiria kuwa ameuzwa ugenini utumwani, huko nako hakuna mtu anayeijua historia yake wala ndoto yake na kwa vile Mungu alikuwa amemkusudia kuwa msimamizi na kiongozi anajikuta utumwani ananunuliwa na Potifa naye anamfanya kuwa mtu mkubwa katika nyumba yake ona  

Mwanzo 39:1-18 “Basi Yusufu akaletwa mpaka Misri naye Potifa, akida wa Farao, mkuu wa askari, mtu wa Misri, akamnunua mkononi mwa hao Waishmaeli waliomleta huko. BWANA akawa pamoja na Yusufu, naye akasitawi; naye alikuwa katika nyumba ya bwana wake, yule Mmisri. Bwana wake akaona ya kwamba BWANA yu pamoja naye, na ya kuwa BWANA anafanikisha mambo yote mkononi mwake. Yusufu akaona neema machoni pake, akamtumikia. Naye akamweka awe msimamizi juu ya nyumba yake, na yote yaliyomo akayaweka mkononi mwake. Ikawa tokea wakati alipomweka awe msimamizi juu ya nyumba yake, na vyote vilivyomo, BWANA akabariki nyumba ya yule Mmisri kwa ajili ya Yusufu. Mbaraka wa BWANA ukawa juu ya vyote alivyokuwa navyo katika nyumba, na katika shamba. Akayaacha yote aliyokuwa nayo mkononi mwa Yusufu; wala hakujua habari za kitu cho chote chake, ila hicho chakula alichokula tu. Ikawa baada ya mambo hayo, mke wa bwana wake akamtamani Yusufu, akamwambia, Lala nami. Lakini akakataa, akamwambia mke wa bwana wake, Tazama, bwana wangu hajui kitu kilichowekwa kwangu nyumbani, na vyote alivyo navyo amevitia mkononi mwangu. Hakuna mkuu katika nyumba hii kuliko mimi, wala hakunizuilia kitu cho chote ila wewe, kwa kuwa wewe u mkewe. Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?  Akawa akizidi kusema na Yusufu siku baada ya siku, lakini hakumsikia alale naye, wala aongee naye. Ikawa, siku moja, akaingia nyumbani atende kazi yake, wala hapakuwa na mtu katika watu wa nyumbani humo ndani; huyo mwanamke akamshika nguo zake, akisema, Lala nami. Yusufu akaiacha nguo yake mkononi mwake, akakimbia, akatoka nje. Ikawa alipoona ya kwamba amemwachilia nguo yake mkononi mwake, naye amekimbia nje, akawaita watu wa nyumbani mwake, akasema nao, akinena, Angalieni, ametuletea mtu Mwebrania atufanyie dhihaka. Ameingia kwangu, ili alale nami, nikalia kwa sauti kuu. Ikawa, aliposikia ya kuwa nimepaza sauti yangu na kulia, aliiacha nguo yake kwangu, akakimbia, akatoka nje. Basi akaiweka ile nguo kwake hata bwana wake aje nyumbani. Naye akamwambia kama maneno hayo, akisema, Yule mtumwa Mwebrania uliyemleta kwetu, aliingia kwangu anidhihaki. Ikawa nilipopaza sauti yangu, nikalia, akaacha nguo yake kwangu akakimbia nje.”

Unapoendelea kufuatilia maisha ya Yusufu hata kule ugenini utakubaliana nani kwamba sio ndugu zake tu, lakini ni shetani anahusika kufuatilia vazi la Yusufu kwani hata watu wasiomjua wageni bado waliendelea kuandama nguo au vazi jingine la Yusufu katika nyumba ya Potifa ili waharibu kile ambacho Mungu amekikusudia,  makusudi ni kuwa maisha ya Yusufu yawe matatani na asipate nafasi kabisa ya kulitumikia shuri la Mungu, vazi la pili la yusufu linaingia matatani sasa Yusufu ana mavazi ya kifungwa gerezani hata hivyo bado neema ya Mungu ilikuwa pamoja naye hata akiwako kule gerezani  kwa kuwa yeye ana karama ya usimamizi ona

Mwanzo 39:21-23 “Lakini BWANA akawa pamoja na Yusufu, akamfadhili, akampa kibali machoni pa mkuu wa gereza. Mkuu wa gereza akawatia mkononi mwa Yusufu watu wote waliofungwa, waliomo gerezani; na yote yaliyofanyika humo ndiye aliyeyafanya. Wala mkuu wa gereza hakuangalia neno lililoko mkononi mwa Yusufu; kwa kuwa BWANA alikuwa pamoja naye. BWANA akayafanikisha yote aliyoyafanya

Yusufu katika vazi jipya

Hata pamoja na mapito yote aliyoyapitia Yusufu Bado Mungu alikuwa Pamoja naye, Mungu atakuwa pamoja nasi wakati wote katika kuhakikisha ya kuwa mpango wake unatimizwa kwetu, Yusufu hatimaye aliweza kutumia kipawa chake kutafasiri ndoto na hatimaye alitafasiri ndoto ya Farao ambayo ilimpatia nafasi kubwa sana na akalitimiza kusudi la Mungu

Mwanzo 41:39-44 “Farao akamwambia Yusufu, Kwa kuwa Mungu amekufahamisha hayo yote, hapana mwenye akili na hekima kama wewe. Basi wewe utakuwa juu ya nyumba yangu, na kwa neno lako watu wangu watatawaliwa. Katika kiti cha enzi tu nitakuwa mkuu kuliko wewe. Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake. Akampandisha katika gari lake la pili alilokuwa nalo. Na watu wakapiga kelele mbele yake, Pigeni magoti. Hivyo akamweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akamwambia Yusufu, Mimi ni Farao, na bila amri yako, mtu asiinue mkono wala mguu katika nchi yote ya Misri.”

Kumbe wote tunaweza kukubaliana wazi kuwa vazi la Yusufu lilikuwa lina uhusiano mkubwa sana na nafasi aliyokuwa nayo, Mungu alikuwa amekusudia kutimiza kusudi Fulani ndani yake Sasa sio baba yake tu wala sio Mungu pekee farao pia anamvika mavazi Yusufu kutoka gerezani saa anavikwa mavazi ya kifalme anapewa na mamlaka ili aweze kutimiza hivyo kusudi kubwa la Mungu

Mambo ya kujifunza kutoka katika vazi la Yusufu

1.       Vazi la sifa njema – Yusufu alitengenezewa vazi la kwanza na Baba yake kwa sababu alikuwa ni mtoto mwenye sifa njema kuliko wengine alipata kibali kwa baba yake, alipata neema ni vazi la upendeleo, ni sifa hii njema iliyoweza kuinua chuki na ibilisi alikusudia kuiharibu,

 

Mwanzo 37:3-4 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani.”

 

Yusufu alifanyiwa hila nyingi sana za kibinadamu kupitia ndugu zake lakini tunajifunza ya kuwa kusudi la Bwana ndilo litakalosimama, ikiwa Mungu amekukusudia Heshima hata iwe gerezani heshima yako itabaki pale pale

 

Mithali 19:21 “Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; Lakini shauri la Bwana ndilo litakalosimama.”Mavazi yake yalichafuliwa lakini Mungu alimvisha mavazi ya Kimisri na kumuinua juu akitumia farasi wa farao na Pete ya farao, Nataka nikuhakikishie ya kuwa ukisimama na Mungu hakuna mtu atafanikiwa katika hila yake ya aina yoyote.

 

2.       Vazi la utumwa – Ni ukweli ulio wazi kuwa vazi la Yusufu ilichanwa chanwa na kuharibiwa na kuchafuliwa kwa damu na Yakobo alionyeshwa ili atambue kama kanzu ile ni ya mwanaye Mwanzo 37:31-34 “Wakaitwaa kanzu ya Yusufu, wakachinja mwana-mbuzi, na kuichovya kanzu katika damu. Wakaenda nayo ile kanzu ndefu, wakamletea baba yao, wakasema, Tumeona hii; basi, utambue kama kanzu hii ni ya mwanao, ama siyo. Akaitambua, akasema, Ndiyo kanzu ya mwanangu, mnyama mkali amemla; bila shaka Yusufu ameraruliwa. Yakobo akararua mavazi yake, akajivika gunia viunoni, na kumlilia mwanawe siku nyingi.”

 

Yusufu alipata vazi lingine huko utumwani alinunuliwa kama mtumwa wa amrijeshi mkuu wa farao alivikwa mavazi ya kitumwa ili amtumikie mtu, lilikuwa vaza la anasa na lilikuwa vazi la tama lakini Yusufu aliishinda tamaa, aliushinda ulimwengu, alimuheshimu Mungu hata katika mazingira magumu nay a ugenini, Mungu huwaheshimu wale wanaomuheshimu  Yusufu alimuheshimu Mungu kila alipokuwepo, alitambua ya kuwa anapaswa kuwa mwaminifu kwa wanadamu na kwa Mungu pia, aliikataa dhambi nimtendeje Bwana Mungu wangu dhambi kubwa namna hii, aliamua kumuheshimu Mungu katika maisha yake alijihami na ubaya wa kila namna na kwa sababu hiyo hatimaye kwa uvumilivu mkubwa alivuna matunda yake yaliyokusudiwa

 

1Samuel 2:30 “Kwa sababu hiyo, Bwana, Mungu wa Israeli, asema, Ni kweli, nalisema ya kuwa nyumba yako, na nyumba ya baba yako itakwenda mbele zangu milele; lakini sasa Bwana asema, Jambo hili na liwe mbali nami; kwa maana wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu.”

 

3.       Vazi la Heshima – lolote linalotokea katika maisha yetu liko chini ya utawala wa Mungu hata pale watu wanapotutendea uovu na hila tukumbuke tu ya kuwa Mungu ndiye anayetawala, Pamoja na mapito yote uaminifu na uvumilivu ulimleta Yusufu katika heshima kubwa sana alivikwa mavazi ya kifahari na kuinuliwa na watu wote kuinamaa mbele zake ona

 

Mwanzo 41:41-42 “Farao akamwambia Yusufu, Tazama, nimekuweka juu ya nchi yote ya Misri. Farao akavua pete yake ya muhuri mkononi mwake, akaitia mkononi mwa Yusufu; akamvika mavazi ya kitani nzuri, na kumtia mkufu wa dhahabu shingoni mwake.”

Hitimisho:

Mungu anao mpango Madhubuti wa kumuheshimu kila mmoja wetu, ni wajhibu wako kuhakikisha ya kuwa unatunza sifa njema ulizonazo, huku ukitambua ya kuwa, Shetani atakupiga vita akiwatumia watu, jilinde na kuhakikisha kuwa unaendelea kuyatunza maisha yako, haijalishi ni mapitio magumu kiasi gani unayapitia.haijalishi uko sehemu ya ugenini ambako watu hawakuoni kumbuka ya kuwa Mungu anakuona na anataka wewe umuonyeshe heshima na Mungu atakuwa pamoja nawe  Mpango wake Mungu ni kutaka kukuheshimu na Mungu analo vazi, anao farasi anayo mavazi na anao watakaokutangaza pale utakapoitunza heshima inayokusudiwa kwako na Mungu na wazazi wako na ulimwengu , Bado Mungu anamkusudia kila mmoja wetu kuvikwa mavazi ya heshima kubwa

Esta 6:7-10 “Basi Hamani akaingia. Mfalme akamwambia, Afanyiziwe nini yule ambaye mfalme apenda kumheshimu? Hamani akasema moyoni mwake, Ni nani ambaye mfalme apenda kumheshimu kuliko mimi? Basi Hamani akamwambia mfalme, Yule ambaye mfalme apenda kumheshimu, na aletewe mavazi ya kifalme ambayo mfalme amezoea kuyavaa, na farasi ambaye mfalme humpanda mwenyewe, ambaye ametiwa taji ya kifalme kichwani; na yale mavazi na yule farasi akabidhiwe mkononi mmojawapo wa maakida wa mfalme aliye mstahiki; ili makusudi amvike yule ambaye mfalme apenda kumheshimu, na kumrakibisha juu ya farasi kuipitia njia kuu ya mjini, na kupiga mbiu mbele yake, kusema, Hivyo ndivyo atakavyofanyiziwa mtu yule ambaye mfalme apenda kumheshimu. Basi mfalme akamwambia Hamani, Hima! Twaa mavazi na farasi kama ulivyosema, ukamfanyizie vivyo hivyo Mordekai, Myahudi, aketiye mlangoni pa mfalme; lisipungue neno lo lote katika yote uliyoyasema.” Ni ahadi ya Mungu kwamba kila mtu atakayeshida tapata heshima kubwa sio hapa duniani tu bali na mbinguni pia

Ufunuo 3:5 “Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe, wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele ya malaika zake.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumatatu, 3 Oktoba 2022

Haki yako ya Mzaliwa wa Kwanza!

Waebrania 12:16-17 “Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja. Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), ijapokuwa aliitafuta sana kwa machozi.”



Utangulizi

Haki ya Mzaliwa ni haki ya kimila, kitamaduni na kiroho anayoipata mtu kutokana na kuzaliwa au mfululizo wa kuzaliwa kwake, Haki hizi zinaweza kumpa mtu, kwa mfano uraia kutokana na mahali ulipozaliwa au walipozaliwa wazazi wake, au kupokea sehemu ya mali na heshima kutoka katika familia yake kufuatana na mpangilio wa kuzaliwa kwake. Haki hii inaweza pia kumpatia mtu urithi wa kifalme kama anatokea katika familia za kifalme!

Katika maandiko Haki ya mzaliwa ilihusiana moja kwa moja na kijana wa kiume aliyezaliwa kwanza katika familia kuwa na haki ya kurithi mali au heshima na mamlaka ya baba yake mara mbili zaidi kuliko watoto wengine, Katika Israel, Kwa mfano kila mtoto alipokea sehemu fulani ya urithi wa mali za baba yake lakini mtoto wa kwanza alipokea mara mbili zaidi kuliko wengine pamoja na uongozi wa Familia.

Mwanzo 48:21-22 “Israeli akamwambia Yusufu, Angalia, mimi ninakufa, lakini Mungu atakuwa pamoja nanyi, naye atawarudisha mpaka nchi ya baba zenu. Nami nimekupa wewe sehemu moja zaidi kuliko ndugu zako, niliyoitwaa katika mikono ya Waamori, kwa upanga wangu na upinde wangu.”

Haki ya kuzaliwa kwanza kwa kawaida ilipaswa kuwa ya Mzaliwa wa kwanza hata kama umezaa na mwanamke usiyempenda, mtoto wa kwanza alihesabika kama mwanzo wa nguvu zako yeye ni Malimbuko ya uzao wako  kwa hivyo maandiko yaliagiza kutazamwa kwa jicho la tofauti kwa mzaliwa wa kwanza katika familia ona  

Kumbukumbu la Torati 21:15-17 “Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa; ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu; lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.”

Neno Mzaliwa wa kwanza katika Lugha ya kiyunani ilihusiana zaidi na mfululizo wa kimamlaka kutoka juu kwenda chini mfululizo huu unaitwa itifaki, neno la kiyunani linalotumika kuelezea kuhusu mzaliwa wa kwanza ni “PROTOTOKOS”ambalo maana yake ni wa kwanza katika cheo, kwa hiyo mamlaka ya uzaliwa wa kwanza ingeweza kuhama hata kwa mtoto mwingine kama kijana wa kwanza hangekuwa na nidhamu, au angefanya mambo ya kipuuzi

Vita vya uzaliwa wa kwanza.

Katika ulimwengu wa kiroho shetani anapigana sana vita  na haki za mzaliwa wa kwanza kwa sababu Mzaliwa wa kwanza ndiye anayekuwa mlango wa Baraka kwa ndugu zake wote, kila mzaliwa wa kwanza alikuwa ni mali ya Mungu ona Hesabu 3:12-13 “Mimi, tazama, nimewatwaa Walawi na kuwatoa kati ya wana wa Israeli badala ya wazaliwa wa kwanza wote wafunguao tumbo katika wana wa Israeli; na hao Walawi watakuwa wangu; kwa kuwa hao wazaliwa wa kwanza wote ni wangu; katika siku ile niliyowapiga wazaliwa wa kwanza wote katika nchi ya Misri nikajiwekea wakfu wazaliwa wa kwanza wote wa Israeli, wa wanadamu na wa wanyama; watakuwa wangu; mimi ndimi Bwana.”

Kwa kuwa wazaliwa wa kwanza ni mali ya Mungu ni urithi wa Mungu, ni Makuhani, ni viongozi wa ibada, ni warithi wa Baraka za kifamilia, ni ishara ya mafanikio ya familia ni nguvu ya familia ni akiba, ni mtazamo wa baadaye wa familia nan i mali ya Mungu, kamwe shetani hangeweza kufurahia na kupenda kuona mpango wa Mungu unapitia kwa wazaliwa wa kwanza kwa hiyo kuna vita katika ulimwengu wa roho kwaajili ya wazaliwa wa kwanza, shetani angefurahia kuharibu kila mzaliwa wa kwanza kiadilifu, kitaaluma na kimafanikio ili kudhoofisha familia ambazo Mungu amekusudia kuzibarikia, kwa hiyo kila mzaliwa wa kwanza anapaswa kujua kuwa iko vita katika maisha yake.

Ni muhimu kufahamu kuwa kuupata urithi, kungehitaji uvumilivu mkubwa na mapambano ya hali ya juu, shetani anafahamu kuwa kuna urithi uolioko mbele yako na hivyo atahakikisha kuwa anapambana kwa kadiri awezavyo ili ikiwezekana upoteze, vita kati ya Mungu na Farao kule Misri kimsingi ilikuwa ni vita ya kugombea Mzaliwa wa Kwanza, Israel ni taifa ambalo lina haki ya mzaliwa wa Kwanza miongoni mwa mataifa ya dunia, lakini Farao hakutaka kuwaachia alitaka wawe watumwa wake awatumikishe hivyo kimsingi kulikuwa na vita kali kwaajili ya kumgombea mzaliwa wa kwanza  na ndio maana Mungu alimuonya Farao kumuachia Israel kwani vinginevyo angwewaadhibu wazaliwa wa kwanza wote wa mwanadamu na mnyama katika taifa la Misri ili Israel auweze kuwa huru ona

Kutoka 4:22-23 “Nawe umwambie Farao, BWANA asema hivi, Israeli ni mwanangu mimi, mzaliwa wa kwanza wangu; nami nimekuambia, Mpe mwanangu ruhusa aende, ili apate kunitumikia, nawe umekataa kumpa ruhusa aende; angalia basi, mimi nitamwua mwanao, mzaliwa wa kwanza wako.”  

Mzaliwa wa kwanza alikuwa ni mlinzi wa mali au urithi wa mali za wazee wao kizazi hata kizazi na walipaswa kuhakikisha kuwa haki ile inatunzwa kwa gharama yoyote ili isipotee Shetani angetamani wakati wote Mzaliwa wa kwanza apoteze,

1 Wafalme 21:1-3 “Ikawa baada ya hayo, Nabothi Myezreeli alikuwa na shamba la mizabibu katika Yezreeli, karibu na nyumba ya kifalme ya Ahabu mfalme wa Samaria. Ahabu akasema na Nabothi, akamwambia, Nipe shamba lako la mizabibu nilifanye shamba la mboga, maana ni karibu na nyumba yangu; nami nitakupa badala yake shamba la mizabibu lililo zuri zaidi; au ukipenda, nitakupa fedha sawasawa na thamani yake. Nabothi akamwambia Ahabu, Bwana apishe mbali nikupe wewe urithi wa baba zangu

 Kila mtu aliyemwamini Bwana Yesu kuwa bwana na Mwokozi ni mzaliwa wa kwanza, na una haki na Baraka zilezile zilizokusudiwa kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, kwa msingi huo Mwandishi wa kitabu cha waebrania alikuwa akiwaasa Wakristo wa kiyahudi, kutokurudia nyuma na kuiacha imani kwani kufanya hivyo kungekuwa hakuna tofauti na mwesherati au mtu asiyemcha Mungu kama ilivyokuwa kwa Esau.

Jinsi ya kuilinda haki ya mzaliwa wa Kwanza.

Kwa kuwa haki ya mzaliwa wa kwanza ni jambo linaloweza kuponyoka kutoka katika mikono ya mtu mmoja kwenda kwa mwingine  na tumeona wazi kuwa shetani kama mpinzani hangependa kuona makusudi ya Mungu yakitimizwa kwa wazaliwa wa kwanza hatuna budi kuhakikisha ya kuwa unailinda haki hiyo kwa gharama yoyote, Maandiko yanatuonya kuwa asiwepo mweshatari, wala mtu asiyemcha Mungu kama Esau aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwaajili ya chakula kimoja hii ina maana gani? Maana yake ni kuwa Esau sio kuwa alifanya uasherati lakini lugha inayotumika hapo inamaanisha kubadilisha kitu kikubwa sana na cha thamani kwa kitu kidogo sana kisicho na tamani, tabia ya aina hii inafananishwa na uasherati, uashetari unaweza kumuharibia mtu thamani yake na heshima yake kwa muda mfupi sana, maandiko yanatutaka tulinde kila kitu ambacho tunakiweka katika idadi ya vitu vya thamani sana duniani. Mambo yanayohitaji kupewa kipaumbele yapewe kipaumbele, Mfano watu wanapokuja shuleni, wazazi wanakuwa wamewekeza fedha ambazo wanazitafuta kwa hali na mali, ili mwanafunzi asome, lakini inasikitisha sana kama mwanafunzi badala ya kusoma yeye akawa anapoteza Muda na kucheza huku anapoteza fedha ya wazazi wake na kuharibu maisha yake ya baadaye kwa njia za kiupuuzi, mtu anaweza kufanya jambo la kijinga tu na likamkosesha kazi,  wakati wote tuyape kipaumbele maswala ambayo ni ya muhimu katika maisha yetu na kujihami na mambo yasiyo ya msingi, majukumu yoyote unayopewa hapa dunaini hakikisha kuwa unayatimiza na kuyatetendea haki kwa kujituma kwa gharama kubwa, mwenendo wako na uadilifu wako na tahadhari ni za muhimu sana katika kuhakikisha kuwa unatunza sana kile ambacho Mungu anakitarajia katika maisha yako! Biblia imejaa mifano ya watu waliopoteza haki yao ya uzaliwa wa kwanza kwa njia za kipuuzi na za kusikitisha sana ona :-

-          Mwanzo 9:20-26 “Nuhu akaanza kuwa mkulima, akapanda mizabibu; akanywa divai, akalewa; akawa uchi katika hema yake. HAMU, baba wa Kanaani, akauona uchi wa baba yake, akawaeleza ndugu zake wawili waliokuwa nje. Shemu na Yafethi wakatwaa vazi, wakalitanda mabegani mwao wote wawili, wakaenda kinyumenyume, wakaufunika uchi wa baba yao; na nyuso zao zilielekea nyuma, wala hawakuuona uchi wa baba yao. Nuhu akalevuka katika ulevi wake, akajua mwana wake mdogo alivyomtendea. Akasema, Na alaaniwe Kaanani; Atakuwa mtumwa kabisa kwa ndugu zake. Akasema, Na atukuzwe BWANA, Mungu wa Shemu; Na Kaanani awe mtumwa wake.”

-           

-          Mwanzo 49:3-4 “REUBENI, u mzaliwa wangu wa kwanza, Nguvu zangu, na malimbuko ya uwezo wangu. Umewapita wengine kwa ukuu na kwa nguvu. Umeruka mpaka kama maji, basi usiwe na ukuu, Kwa sababu ulikipanda kitanda cha baba yako, Ukakitia unajisi; alikipandia kitanda changu.”

-           

-          Mwanzo 25:29-32 “Yakobo akapika chakula cha dengu. ESAU akaja kutoka nyikani, naye alikuwa amechoka sana. Esau akamwambia Yakobo, Tafadhali, unipe hicho chakula chekundu nile, kwa kuwa ninazimia mimi. Kwa hiyo walimwita jina lake Edomu.Yakobo akamwambia, Kwanza niuzie leo haki yako ya mzaliwa wa kwanza. Esau akasema, Tazama, mimi ni karibu kufa, itanifaa nini haki hii ya uzazi?

Pigania urithi wako !

Wako watu wanaotajwa kama Mashujaa walioishi wakati wa Daudi watu hawa walikuwa Hodari sana katika kuutetea urithi wa bwana na kuhakikisha kuwa watu wengine wanafaidiaka kwa ujasiri wao, ni imani yangu Kuwa Mungu atakusaidia wewe na mimi tuweze kupigania kile ambacho Mungu ametukabidhi kwa gharama yoyote

2Samuel 23:8-12 “Haya ndiyo majina ya mashujaa aliokuwa nao Daudi; Yashobeamu Mhakmoni,mkuu wa maakida ;huyo aliliinua shoka lake juu ya watu mia nane waliouawa pamoja.Na baada yake kulikuwa na Eleazari, mwana wa Dodai, Mwahohi, mmojawapo wa wale mashujaa watatu waliokuwa pamoja na Daudi; walipowatukana Wafilisti waliokuwa wamekusanyika huko ili kupigana, na watu wa Israeli walikuwa wamekwenda zao; huyo aliinuka, akawapiga Wafilisti hata mkono wake ukachoka, na mkono wake ukaambatana na upanga; naye Bwana akafanya wokovu mkuu siku ile; nao watu wakarudi nyuma yake ili kuteka nyara tu. Na baada yake kulikuwa na Shama, mwana wa Agee, Mharari; nao Wafilisti walikuwa wamekusanyika huko Lehi, palipokuwapo konde lililojaa midengu; nao watu wakawakimbia Wafilisti; ila huyo alisimama katikati ya konde lile, akalipigania, akawaua Wafilisti; naye Bwana akafanya wokovu mkuu.”

 

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima!

Jumanne, 20 Septemba 2022

Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima !


1Wafalme 12:6-7 “Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa?  Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.”



Utangulizi:

Mojawapo ya maombi yanayompendeza sana Mungu ni pamoja na kuomba Hekima, Mfalme Suleimani mara alipotawazwa kuwa mfalme wa Israel, Mungu alimtokea na kumtaka amuombe lolote alitakalo, katika namna ya kushangaza sana Mfalme Suleimani aliomba Hekima jambo ambalo lilimpendeza sana Mungu hata akamjalia na mambo mengine mengi sana ambayo hakuyaomba ona:-

1Wafalme 3:5-13 “Na huko Gibeoni Bwana akamtokea Sulemani katika ndoto ya usiku; Mungu akamwambia, Omba utakalo nikupe. Sulemani akasema, Umemfanyia mtumwa wako Daudi baba yangu fadhili kuu, kadiri alivyoenenda mbele zako katika kweli, na katika haki, na katika unyofu wa moyo pamoja nawe; nawe umemwekea na fadhili hii kubwa, maana umempa mwana wa kuketi kitini pake kama ilivyo leo. Na sasa, Ee Bwana, Mungu wangu, umenitawaza niwe mfalme mimi mtumwa wako badala ya Daudi baba yangu; nami ni mtoto mdogo tu; sijui jinsi inipasavyo kutoka wala kuingia. Na mtumwa wako yu katikati ya watu wako uliowachagua, watu wengi wasioweza kuhesabiwa, wala kufahamiwa idadi yao, kwa kuwa ni wengi. Kwa hiyo nipe mimi mtumwa wako moyo wa adili niwahukumu watu wako, na kupambanua mema na mabaya; maana ni nani awezaye kuwahukumu hawa watu wako walio wengi? Neno hili likawa jema machoni pa Bwana, ya kuwa Sulemani ameomba neno hili. Mungu akamwambia, Kwa kuwa umeomba neno hili, wala hukujitakia maisha ya siku nyingi; wala hukutaka utajiri kwa nafsi yako; wala hukutaka roho za adui zako; bali umejitakia akili za kujua kuhukumu; basi, tazama, nimefanya kama ulivyosema. Tazama, nimekupa moyo wa hekima na wa akili; hata kabla yako hapakuwa na mtu kama wewe, wala baada yako hatainuka mtu kama wewe. Na mambo yale usiyoyaomba nimekupa, mali na fahari, hata hapatakuwa na mtu katika wafalme kama wewe, siku zako zote.”

Kila siku katika maisha yetu tunakabiliwa na swala la kufanya uamuzi, Hakuna jambo gumu sana duniani kama kufanya uamuzi, maamuzi yetu tunayoyafanya leo yanaweza kuwa na faida kubwa sana katika siku zetu zote za maisha yetu na ya watu wengine, lakini vilevile yanaweza kutugharimu na kusababisha machungu katika maisha yetu au hata na ya wengine kwa hiyo ni muhimu sana kumuomba Mungu atupe Hekima.

Yakobo 1:5 “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.”

Katika kifungu cha maandiko ya msingi, tulichosoma tunamuona Mwana wa mfalme Sulemani aliyeitwa Rehoboamu akiwa anakabiliwa na wakati wa kufanya maamuzi kwa mustakabali wa taifa lake mapema tu katika siku za mwanzoni mwa utawala wake.

1Wafalme 12:1-5 “Rehoboamu akaenda Shekemu; maana Israeli wote walikuwa wamekwenda Shekemu, ili kumfanya mfalme. Ikawa Yeroboamu mwana wa Nebati alipopata habari (maana alikuwa akaliko Misri, huko alikokimbilia awe mbali na mfalme Sulemani; Yeroboamu akakaa huko Misri, wakapeleka watu kwenda kumwita); basi Yeroboamu na jamii yote ya Israeli wakaenda, wakamwambia Rehoboamu, wakasema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu; basi sasa utupunguzie utumwa mzito tuliotumikishwa na baba yako, na lile kongwa zito alilotutwika, nasi tutakutumikia. Akawaambia, Enendeni zenu hata siku ya tatu, kisha mnirudie tena. Watu wakaenda zao.”

Wana wa Israel wanaonekana ya kuwa walikuwa tayari kabisa kumtumikia mfalme Rehoboamu baada ya baba yake Suleimani, lakini walikuwa na ombi kwamba wawarahisishie maisha maana wakati wa baba yake hali ilikuwa ngumu sana walielemewa na kodi na utumwa mzito uliowanyima furaha, Suleimani alikuwa amewatumikisha watu sana kwa utumwa mzito na Kodi kwaajili ya fahari ya ufalme wake, Mfalme Rehoboamu aliwapa Muda ili kwamba aweze kulitafakari ombi lao, jambo hili au hatua hii ilikuwa njema kwani hakufanya haraka alikuwa na utulivu na hii ni hatua nzuri kila wakati tunapotaka kufanya maamuzi, hatupaswi kufanya maamuzi kwa kufuata mihemko, ni muhimu kutulia na ikiwezekana kuwa na wakati wa kumuomba Mungu ili kwamba atupe hakima ya kufanya maamuzi mema yanayokusudiwa, Mungu akitupa hekima yake tutakuwa na mafanikio makubwa sana yaani matunda mema kwa sababu hekima ya Mungu ni safi, ya amani, ya upole, na inasikiliza watu hekima hii ina rehema, na ina matunda mema haina fitina wala haina unafiki imetajwa hivyo katika maandiko;-

Yakobo 3:17-18 “Lakini hekima itokayo juu, kwanza ni safi, tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina unafiki. Na tunda la haki hupandwa katika amani na wale wafanyao amani.”

Tunapotafakari haya tutaliangalia somo hili katika vipengele vitatu vifuatavyo:-

1.       Ushauri wa wazee na ushauri wa vijana

2.       Umuhimu wa kufanya maamuzi yenye busara

3.       Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima

Ushauri wa wazee na ushauri wa vijana.

Kuna kitu cha kujifunza tunapoangalia maamuzi yaliyofanywa na mfalme Rehoboamu, Maamuzi yake yanaletwa kwetu na neno la Mungu ili tuweze kujifunza maswala halisi yanayoweza kujitokeza kwetu katika maisha  Mfalme Rehoboamu alipotulia ili atake ushauri, alipata ushauri kutoka katika makundi makuu mawili, kundi la kwanza lilikuwa kundi la wazee hawa walikuwa ni watu waliokuwa na uzoefu na ujuzi (Experience) walikuwa wameona utawala uliopita wa wakati wa baba yake walijua mazuri na machungu ya utawala huo, kwa kawaida Biblia inapotaja wazee wakati mwingine huwa inazungumzia UZOEFU hawa walitoa ushauri wao  kama hivi ona

 1Wafalme 12:6-7 Mfalme Rehoboamu akataka shauri kwa wazee waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani, baba yake, alipokuwa hai, akasema, Mwanipa shauri gani ili niwajibu watu hawa? Wakamwambia wakasema, Ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa leo, na kuwatumikia, na kuwajibu, na kuwapa maneno mazuri, basi watakuwa watumishi wako daima.”

Kundi hili ni kundi la watu wanaojua wapi tunatoka na wapi tunakwenda, maandiko yanaonyesha kuwa walikuwa ni washauri pia wa Mfalme Suleimani, maandiko yanasema waliokuwa wakisimama mbele ya Sulemani alipokuwa hai, hawa waliona ukatili aliokuwa nao Sulemani na ukali wake hunda kuna mambo walishauri na Sulemani kwa ubabe wake alikataa, na sasa anapokuja mfalme mpya walimshauri kwamba akubali kuwa mtumwa yaani mtumishi awajali watu awatumie watu lakini vilevile azungumze nao vizuri, awape majibu akutane na haja za mioyo yao, na kuwapa maneno mazuri, walimwambia akifanya hivyo watu hawa watamtumikia daima.  

Kundi la Pili lilikuwa kundi la vijana, vijana katika lugha ya kinabii ni watu wasio na uzoefu, hawana ujuzi wa kutosha wa kupambanua mambo, wao walikuwa ni machipukizi bado hawana mizizi kundi hili wao walimpa mfalme ushauri wa kuongeza ukatili na kutokuwahurumia watu

1Wafalme 12:8-11 “Lakini akaliacha shauri lile la wazee, walilompa, akataka shauri kwa wale vijana waliokua pamoja naye, na kusimama mbele yake. Akawaambia, Mwanipa shauri gani ili tuwajibu watu hawa, waliosema nami, wakinena Utufanyie jepesi kongwa lile alilotutwika baba yako? Na wale vijana waliokua pamoja naye wakamwambia, wakasema, Uwaambie hivi watu wale waliokuambia, wakisema, Baba yako alilifanya zito kongwa letu, bali wewe utufanyie jepesi, uwaambie hivi, Kidole changu cha mwisho ni kinene kuliko kiuno cha baba yangu. Basi kama vile baba yangu alivyowatwika kongwa zito, mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge.”

Mfalme Rehoboamu kwa bahati mbaya alifuata ushauri wa vijana maana yake alifuata ushauri wa watu wasio na uzoefu, wajanja wajanja ambao kimsingi walikuwa wakitarajia nafasi kadhaa katika utawala mpya hivyo wasingekuwa na jipya zaidi ya kumpamba mfalme na kumpa maneno ambayo walifikiri yangeweza kuwa na tija katika jamii matokeo yake wana wa Israel waligawanyika makundi makundi na inchi ya Israel ikapoteza umoja na kuvunjika katika falme mbili

1Wafalme 12:12-16 “Basi, Yeroboamu na watu wote wakamfikia Rehoboamu siku ya tatu, kama mfalme alivyoamuru, akisema, Mnirudie siku ya tatu. Mfalme akawajibu watu wale kwa ukali, akaliacha shauri lile wazee walilompa; akawajibu kama vile walivyomshauri vijana, akasema, Baba yangu alilifanya zito kongwa lenu, bali mimi nitaongeza kongwa lenu; baba yangu aliwapiga kwa mijeledi, bali mimi nitawapigeni kwa nge. Basi mfalme hakuwasikia wale watu; maana jambo hili lilitoka kwa Bwana, ili alitimize neno lake, Bwana alilomwambia Yeroboamu mwana wa Nebati kwa kinywa cha Ahiya Mshiloni. Basi Israeli wote walipoona ya kuwa mfalme hakuwasikia, hao watu walimjibu mfalme, wakasema, Tuna sehemu gani katika Daudi? Wala hatuna urithi katika mwana wa Yese. Haya! Nendeni zenu hemani kwenu, enyi Israeli; sasa itunze nyumba yako mwenyewe, Ee Daudi. Hivyo Israeli wakaenda zao hemani kwao.”

Umuhimu wa kufanya maamuzi yenye busara

Ni jambo la kusikitisha sana kuwa Nchi ya Israel iligawanyika na watu walivunjika Moyo, mfalme hakuwajibu watu kwa upole na badala yake aliwajibu watu kwa ukali na watu wakavunjika moyo kila mmoja akarejea nyumbani kwake,  Siku zote katika maisha yetu hatuna budi kuhakikisha ya kuwa tunafanya maamuzi ambayo yanampendeza Mungu maamuzi ambayo kwa namna yoyote ile hayatakuja yawaumize watu na kuwakatisha tamaa, tusifanye uamuzi wowote wenye kuaibisha watu au kudhalilisha, au kuumiza, tusifanye kwa mihemko yetu wala kwa ubinafsi wetu wala kwa kutaka makuu, Mungu anatutaka watu wote tuwe na maamuzi yenye busara, watu wa Mungu hawapaswi kuwa kama watu wa dunia hii, katika kanuni za kimungu kuwatumikia watu ndio hatua ya juu zaidi itakayotupa heshima kwa Mungu, Bwana Yesu ametufundisha kuwa namna hiyo

Mathayo 20:25-28 “Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha. Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu; na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu; kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

Kumbe ni kanuni ya kibiblia kabisa ya kuwa  tunapaswa kuwatumikia watu kwa maana nyingine tuwe wanyenyekevu na jambo hili litatupa faida kubwa sana katika maisha yetu, Wazee walikuwa wamemshauri Rehoboamu namna njema ya kufaulu walimtaka awe mnyenyekevu kwa watu, awe mpole azungumze nao kwa amani awe mtumwa na kuwa watu wangemtumikia daima, kumbe katika maisha yetu tukitaka kufanikiwa tukubali kuwa watumwa, tujinyenyekeze, tutii wazee, tusikilize wakubwa, tusikilize walimu, tusikilize wazazi, na walezi, tusikilize wale wenye uzoefu wanatuambia nini  na wakati wote tukatae hali ya kujifanya mabwana:-

1Petro 5: 1-3 “Nawasihi wazee walio kwenu, mimi niliye mzee, mwenzi wao, na shahidi wa mateso ya Kristo, na mshirika wa utukufu utakaofunuliwa baadaye; lichungeni kundi la Mungu lililo kwenu, na kulisimamia, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari kama Mungu atakavyo; si kwa kutaka fedha ya aibu, bali kwa moyo. Wala si kama wajifanyao mabwana juu ya mitaa yao, bali kwa kujifanya vielelezo kwa lile kundi.”

Ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima!.

Huu ndio ushauri mwema kutoka katika mapenzi ya Mungu, wazee walimshauri Rehoboamu kwamba ukikubali kuwa mtumishi wa watu hawa watakutumikia daima, hii ndio kanuni ya msingi ya kibiblia na ina faida nyingi sana kwa mujibu wa maandiko;-

1.       Ukijinyenyekesha utainuliwa juu sana, unapokubali kuwa mtumwa Mungu atakuinua juu mno utapanda katika viwango na watu wote watakutumikia ona Wafilipi 2:5-11 “Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu;  tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba. Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba. Hii ni kanuni huru ya kibiblia Zaburi 147:6 “Bwana huwategemeza wenye upole, Huwaangusha chini wenye jeuri.” Bwana wetu Yesu Kristo alikubali kuwa mtumwa, aliwatumikia watu, kumbuka alikuwa sawa na Mungu alikini alijinyenyekeza moyo wake ulijikita katika kumtumikia Mungu na watu wake na hivyi Mungu alimuinua juu sana na kumpa jina lipitalo majina yote na kutukuzwa sana mbinguni na duniani.

2.       Kujinyenyekeza kunaongeza Neema ya Mungu, 1Petro 5:5-6 “Vivyo hivyo ninyi vijana, watiini wazee. Naam, ninyi nyote jifungeni unyenyekevu, mpate kuhudumiana; kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu neema. Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake;” Hakuna jambo baya duniani kama kupungukiwa neema, Mungu wetu ana upendo mkubwa sana aukipata neema mbele zake utafanikiwa katika maisha yako, lakini kiburi ni sumu ya neema, kama tukishindwa kujinyenyekesha haraka sana Mungu ataondoa neema yake kwetu! Na hivyo tutajisikia vibaya na kupatwa na aibu.

3.       Kujinyenyekeza kunaleta kukubaliwa na kujikweza kunaleta kukataliwa Luka 18:9-14 “Akawaambia mfano huu watu waliojikinai ya kuwa wao ni wenye haki, wakiwadharau wengine wote. Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali, mmoja Farisayo, wa pili mtoza ushuru. Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi, wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.” Yakobo 4:10 “Jidhilini mbele za Bwana, naye atawakuza.” 3Yohana 1:9 “Naliliandikia kanisa neno, lakini Diotrefe, apendaye kuwa wa kwanza kati yao, hatukubali.”

4.       Mungu huwasikiliza wanyenyekevu 2Nyakati 34:27 “kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe umejinyenyekeza mbele ya Mungu, uliposikia maneno yake juu ya mahali hapa, na juu ya wakaao, ukajinyenyekeza mbele zangu, na kuyararua mavazi yako, na kulia mbele zangu; mimi nami nimekusikia, asema Bwana.”

5.       Unyenyekevu unaleta hekima na kutufanya tukubali kufundishika ona Zaburi 25:9 “Wenye upole atawaongoza katika hukumu, Wenye upole atawafundisha njia yake”. na Mithali 11:2 “Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu; Bali hekima hukaa na wanyenyekevu.”

6.       Huepusha hasira ya Mungu na kutupa wokovu ona 2Nyakati 32:26 “Hata hivyo Hezekia akajinyenyekeza kwa ajili ya huku kutukuka kwa moyo wake, yeye na wenyeji wa Yerusalemu, hata haikuwajia hasira ya Bwana siku za Hezekia.” na Zaburi 149:4 “Kwa kuwa Bwana awaridhia watu wake, Huwapamba wenye upole kwa wokovu.

7.       Ukijishusha utakuwa mkubwa katika ufalme wa Mungu Mathayo 18:4 Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.”    

Kama Rehoboamu angejinyenyekeza angeweza kupata thawabu kubwa na nyingi zinazotajwa katika mandiko, Bwana na ampe neema kila mmoja wetu kujifunza umuhimu wa kunyenyekea na kujishusha ili tuweze kuona faida na uzuri wa kanuni za kimungu sawa na namna Mungu anavyokusudia katika Maisha yetu na tukumbuke siku zote ya kuwa ukikubali kuwa mtumwa utatumikiwa Daima.

Rev. Innocent Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Alhamisi, 15 Septemba 2022

Kuhani mkuu kwa Mfano wa Melkizedek


Zaburi 110:1-4 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako.  Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki.”



Utangulizi

Maandiko yanamuonyesha Yesu Kristo kama ni Nabii mkubwa na aliyebora zaidi kuliko Musa, lakini pia ni Kuhani mkuu aliye bora zaidi kwa mfano wa Melkizedeki unaweza kuona poia katika Waebrania 6:20 “alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu, amekuwa kuhani mkuu hata milele kwa mfano wa Melkizedeki.” Tunapojifunza somo hili kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki tutazingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Tofauti ya nabii na kuhani

·         Wajibu wa kikuhani.

·         Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki

Tofauti ya Nabii na kuhani

Neno la Mungu linatufundisha tofauti kubwa iliyoko kati ya nabii na kuhani, kwa kawaida hawa wote ni watumishi wa Mungu, na huwa wanaitwa ama kuteuliwa na Mungu mwenyewe ona Kumbukumbu 18:18 “Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe, nami nitatia maneno yangu kinywani mwake, naye atawaambia yote nitakayomwamuru.” Unaona ni Mungu ndiye anayeinua nabii na kuweka neno lake ndani yao ili aseme kwa niaba yake na kuwafundisha watu wa Mungu njia zake nan i Mungu mwenyewe anayechagua kuhani ona Waebrania 5:1-4 “Maana kila kuhani mkuu aliyetwaliwa katika wanadamu amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu, ili atoe matoleo na dhabihu kwa ajili ya dhambi; awezaye kuwachukulia kwa upole wao wasiojua na wenye kupotea, kwa kuwa yeye mwenyewe yu katika hali ya udhaifu; na kwa sababu hiyo imempasa, kama kwa ajili ya watu, vivyo hivyo kwa ajili ya nafsi yake mwenyewe, kutoa dhabihu kwa ajili ya dhambi. Na hapana mtu ajitwaliaye mwenyewe heshima hii, ila yeye aitwaye na Mungu, kama vile Haruni.” Unaweza kuona hawa wote huteuliwa au kuitwa na Mungu, Nabii yeye huchaguliwa na Mungu ili awe msemaji kwa niaba ya Mungu Neno nabii katika Lugha ya kiibrania huwakilishwa kwa maneno makuu matatu ambayo ni NABI, ROEH, na HOZEH

Nabi – Maana yake ni Msemaji, au mtangazaji Hawa ni wasemaji au wanenaji wanaosukumwa na Roho wa Mungu kuyasema mapenzi ya Mungu kwa msukumo na wivu mkali wa kiungu, lakini pia ni walimu wa neno la Mungu kwa ufupi ni wasemaji kwa niaba ya Mungu, ni wasemaji wa Mapenzi ya Mungu

Roeh – Maana yake ni waonaji, au wafunuaji wao hitwa na Mungu na kuwawezesha kuona mambo yaliyofichika na kuyasema au kuonya au kutangaza au kufundisha mapenzi ya Mungu baada ya kufunuliwa na Mungu, mwisho wa siku nao ni wasemaji kwa niaba ya Mungu

Hozeh – Ni msahuri au mwenye hekima ambao kazi yao ni kufikiri na kutoa ushauri kwa niaba ya Mungu kwa watu wake ni wenye uwezo wa kutambua kama ujumbe ni wa kiungu au la walitumika sana kuwashauri wafalme ili watende sawasawa na mapenzi ya Mungu

Katika kiyunani Prophet ni mtu anayezungumza jambo kwa niaba ya mwingine kwa hivyo wao husema au kutafasiri jambo kwa niaba ya Mungu, ili watu wa Mungu wajue mapenzi ya Mungu katika maisha yao hivyo kwa vyovyote vile manabii ni walimu wa neno la Mungu, ni walimu kwa niaba ya Mungu ni wajumbe kwa niaba ya Mungu, Mungu anapotaka kuyafunua mapenzi yake kwa wanadamu.

Kuhani kwa upande mwingine ni mwanaume anayechaguliwa na Mungu kuwawakilisha wanadamu kwa Mungu, wao ni wasemaji wa wanadamu kwa Mungu, wana wana kibali maalumu cha kumfikia Mungu, na kuzungumza au kutenda kwa niaba ya wanadamu kwa Mungu , hata hivyo hii haiachi ukweli kuwa nao ni walimu wa nenola Mungu kwa watu wa Mungu, lakini mafundisho yao ni tofauti nay ale ya manabii, wakati manabii wanakazia uadilifu, hali safi ya kiroho na wajibu wetu kwa Mungu, Makuhani wao hushughulika na njia sahihi za kumuendea Mungu.

Wajibu wa kikuhani.

Huduma ya kikuhani kwa kawaida kihistoria ilianzishwa na Mungu kwa wana wa Israel baada ya kutoka katika inchi ya Misri, baada ya maelekezo ya Mungu kwa Musa katika mlima wa Sinai, Kutoka 28:1 “Nawe umlete Haruni ndugu yako karibu nami, na wanawe pamoja naye, miongoni mwa wana wa Israeli, ili anitumikie katika kazi ya ukuhani. Haruni, na Nadabu, na Abihu, na Eleazari, na Ithamari, wana wa Haruni.” Makuhani hawa walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili waweze kuwawakilisha wanadamu kwa Mungu kwa hiyo sifa zao zilikuwa

1.       Walichaguliwa kutoka miongoni mwa wanadamu ili kuwawakilisha wanadamu

2.       Walichaguliwa na Mungu mwenyewe

3.       Walifanya kazi ya Mungu kwa niaba ya wanadamu, kwa mambo yote ya wanadamu ya kidini ili kumfikia Mungu

4.       Walikuwa na kazi ya kutoa sadaka za kuteketezwa kwaajili ya watu kwa Mungu

5.       Walikuwa na wajibu wa kuwaombea watu kwa Mungu

6.       Walikuwa na wajibu wa kuwabariki watu wa Mungu

Kwa msingi huo katika maandiko iko wazi kabisa kuwa wajibu wa kikuhani ulikuwa ni kutoa sadaka zakuteketezwa, kuwaombea watu, na kuwabariki watu kwa jina la Mungu, hata hivyo kazi zote hizi zilizokuwa zikifanywa na makuhani bado zilikuwa zinaashiria kuwa siku moja atakuja kuhani mkuu aliye bora zaidi huyu ndiye ametabiriwa kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki “Zaburi 110:1-4 “Neno la Bwana kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, Hata niwafanyapo adui zako Kuwa chini ya miguu yako.  Bwana atainyosha toka Sayuni Fimbo ya nguvu zako. Uwe na enzi kati ya adui zako; Watu wako wanajitoa kwa hiari, Siku ya uwezo wako; Kwa uzuri wa utakatifu, Tokea tumbo la asubuhi, Unao umande wa ujana wako. Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki.” Huyu atakuwa ni masihi ambaye hangetoka katika ukoo wa kikuhani bali katika kabila nyingine ya Yuda na ukoo wa Daudi ukuhani wake huyu utakuwa wa milele kuhani huyu vilevile ataketi katika kiti cha enzi cha Daudi milele na milele, kuhani huyu atakuwa ni mfalme na wakati huo huo kuhani kama ilivyokuwa kwa Melkizedeki, Kuhani huyu atakuwa bora zaidi ya wale wa agano la kale kutoka kabila ya walawi, Huyu ni Yesu Kristo ambaye anafanya kazi zilezile zilizokuwa zikifanywa na makuhani katika agano lililo bora zaidi Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Waebrania 7:24-25 “bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.”  Kwa msingi huo tunaona kwamba Mungu ametupa kuhani aliyebora zaidi kutoka nje ya kabila la walawi, ambaye ni kuhani na mfalme sawa na ilivyokuwa kwa Melkizedeki

Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki

Yesu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki ina faida gani kwetu?  Kama wakristo? Yako mambo kadhaa ya muhimu na msingi yenye faida kwetu kwa kristo Yesu kuwa kuhani mkuu kwaajili yetu.

1.       Tunaweza kupatanishwa na Mungu

 

Kwa sababu ya kazi aliyoifanya Yesu Kristo pale msalabani kama Kuhani mkuu ametupatanisha na Mungu 2Wakoritho 5:18-20 “Lakini vyote pia vyatokana na Mungu, aliyetupatanisha sisi na nafsi yake kwa Kristo, naye alitupa huduma ya upatanisho; yaani, Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake, asiwahesabie makosa yao; naye ametia ndani yetu neno la upatanisho. Basi tu wajumbe kwa ajili ya Kristo, kana kwamba Mungu anasihi kwa vinywa vyetu; twawaomba ninyi kwa ajili ya Kristo mpatanishwe na Mungu.”

 

Wakolosai 1:19-20 “Kwa kuwa katika yeye ilipendeza utimilifu wote ukae; na kwa yeye kuvipatanisha vitu vyote na nafsi yake akiisha kufanya amani kwa damu ya msalaba wake; kwa yeye, ikiwa ni vitu vilivyo juu ya nchi, au vilivyo mbinguni.”

 

Dhambi ilisababisha uadui kati yetu na Mungu, sote tulikuwa tumefarakanishwa na Mungu lakini kupitia Kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki Neema ya Mungu imekuwa juu yetu na uadui uliokuweko kati yetu umevunjwa wote tunajua kuwa maovu huwa yanatufarikisha kwa Mungu

 

Isaya 59:1-2 “Tazama, mkono wa Bwana haukupunguka, hata usiweze kuokoa wala sikio lake si zito, hata lisiweze kusikia; lakini maovu yenu yamewafarikisha ninyi na Mungu wenu, na dhambi zenu zimeuficha uso wake msiuone, hata hataki kusikia.”

 

Lakini kupitia Mwokozi wetu Yesu Kristo hakuna uadui tena kati yetu na Mungu Warumi 5:8:-11 “Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi. Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye. Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake. Wala si hivyo tu, ila pia twajifurahisha katika Mungu kwa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa yeye sasa tumeupokea huo upatanisho.”            

 

2.       Tunaweza kumfikia Mungu kwa Maombi tukiwa na ujasiri

 

Sasa tunaweza kumuomba Mungu kwa ujasiri kwa sababu ya kazi kubwa ya ukuhani aliyoifanya Bwana wetu Yesu, Mwanzoni ilikuwa ngumu kumfikia Mungu na kumuomba bila kuhani mkuu kutuombea kwanza kwa kutoa sadaka ya dhambi zake na zetu ndio tupate kibali cha kumfikia Mungu na ujasiri wa mioyo yetu, Lakini kupitia ubora wa sadaka aliyoitoa kuhani huyu mkuu kwa mfano wa Melikizedeki sasa tunaweza kabisa kumuendea Mungu kwa ujasiri na kumuomba moja kwa moja ikifahamika ya kuwa tunaye mwombezi na mpatanishi mbinguni Warumi 8:33-34 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.” Waebrania 7:24-25 “bali yeye, kwa kuwa akaa milele, anao ukuhani wake usioondoka. Naye, kwa sababu hii, aweza kuwaokoa kabisa wao wamjiao Mungu kwa yeye; maana yu hai sikuzote ili awaombee.” Tunaoujasiri ya kuwa Mungu anasikia maombi yetu na kuwa atatujibu sawa na mapenzi yake kwanini kwa sababu mwanzoni ilikuwa ngumu Yohana 9:31 “Twajua ya kuwa Mungu hawasikii wenye dhambi; bali mtu akiwa ni mcha Mungu, na kuyafanya mapenzi yake, humsikia huyo.”

 

3.       Tunapata amani nafsini mwetu

 

Jambo lingine bora zuri na la amani ni kuwa tunapata amani katika dhamiri zetu hii pia ni kutokana na kazi kubwa aliyoifanya Bwana wetu Yesu Kristo pale Msalabani, Waebrania 4:14-16 “Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.  Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

4.       Sisi sasa ni makuhani pia.

 

Moja ya faida kubwa tunayoipata katika ukuhani wa Yesu Kristo, ni pamoja na sisi kuwa tunaushiriki huo ukuhani hivyo kila aaminiye ni kuhani 1Petro 2:9-10 “       Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

Ufunuo 1:4-6  Yohana, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia; Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi; tena zitokazo kwa Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele. Amina.”

 

Raha ya aina yake kuwa na kuhani mkuu wa kipekee mwenye Baraka zetu zote za kimwili na kiroho!

 

Rev. Innocent Kamote.

 

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jiwe la Kukwaza Katika Sayuni !


1Petro 2:6-8 “Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika.  Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni. Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa ni kwanini mtume Petro anamtaja Yesu Kristo kama jiwe la kukwaza? (Stumbling block) Hili linaweza kuwa jambo lenye kushangaza sana, kwa sababu kwa lugha rahisi hauwezi kudhani kuwa Mungu angeweza kukusudia Kristo Yesu awe jiwe la Kukwaza pia, Katika hali ya kawaida tunapomuelezea Yesu Kristo kama jiwe la Pembeni na lenye heshima inaweza kueleweka vema zaidi, lakini hata hivyo kama tutaelewa kile kinacho maanishwa katika maandiko tunaweza kutoka tukiwa na amani ya kutosha sana kumuhusu Yesu Kristo na sisi tuliomuamini. Tutajifunza somo hili kwa kuzinagatia vipengele vifuatavyo vikuu viwili vifuatavyo:-

·         Maana ya jiwe la kukwaza.

·         Jiwe la kukwaza katika Sayuni. 

Maana ya jiwe la kukwaza.

Kibiblia neno jiwe la kukwaza au kukwaza maana yake ni kukosesha kwa hila kwa kiingereza ni Stumbling Block yaani ukwazo, au makwazo ambalo kwa kiibrania husomeka kama neno Miksol na kwa kiyunani ni Skandalon ambalo maana yake ni kukosesha au kutegea mtu ili aanguke na kupata madhara au jambo lolote linaloweza kufanyika na kumfanya mtu afanye dhambi au apatikane na madhara na kuhukumiwa sawa na kumuwekea mtu mtego ili aingie hatiani 

Zaburi 140:4-5 “Ee Bwana, unilinde na mikono ya mtu asiye haki; Unihifadhi na mtu wa jeuri; Waliowaza kuzipotosha hatua zangu. Wenye kiburi wamenifichia mtego na kamba; Wametandika wavu kando ya njia; Wameniwekea matanzi.”

Jambo hili kimaandiko sio jambo jema na Katika lugha ya kinabii kukosesha mtu au kumkwaza mtu kulihesabika kuwa ni tukio baya, hasa linapofanyika kwa mtu asiye na hatia, Mungu aliwaagiza makuhani kutokuweka kwazo kwa mtu asiye na ufahamu au asiyeona (kipofu) kwani kufanya hivyo lilionekana kuwa jambo baya na la kikatili sana  

Walawi 19: 14 “Usimlaani kiziwi, wala usitie kwazo mbele ya kipofu, bali umche Mungu wako; Mimi ndimi BWANA.”

Kimsingi maandiko haya yalikuwa na maana ya kutokusababisha makwazo kwa watu wanaohitaji kuelekezwa au kufahamishwa, kwa hiyo kimsingi maonyo haya yanawahusu walimu wa neno la Mungu kwamba wasitumie ufahamu wao kuwapotosha watu kwa hila kwa kufanya hivyo kungeleta hukumu iliyokubwa sana au ya kutisha ona

 Mathayo 18:6 “bali atakayemkosesha mmojawapo wa wadogo hawa waniaminio, yamfaa afungiwe shingoni jiwe kubwa la kusagia, na kutoswa katika kilindi cha bahari.

Unaweza kuona maandiko yanatangaza hukumu kubwa sana kwa mtu atakayekosesha wengine au kwa lugha nyingine anayesababisha makwazo au kwa lugha nyingine kufundisha watu uongo au kumtia mwenye haki hatiani

Yakobo 3:1-2 “Ndugu zangu, msiwe waalimu wengi, mkijua ya kuwa mtapata hukumu kubwa zaidi. Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi. Mtu asiyejikwaa katika kunena, huyo ni mtu mkamilifu, awezaye kuuzuia na mwili wake wote kama kwa lijamu.”  

Kwa msingi huo unaweza kupata picha ya wazi kuwa kukosesha au kukwaza kamwe kibiblia halikuweza kuhesabiwa kuwa  la jambo zuri bali ni tukio baya na lililoambatana na maonyo makali dhidi ya wale wote wanaosababisha makwazo ya aina yoyote ile :-

Luka 17:1-2 “Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa.  

Sasa ni katika namna ya kushangaza sana unaweza kustaajabu kuona kuwa ujio wa Masihi Bwana wetu Yesu Kristo unatajwa vilevile kuambatana na Heshima kwa wale watakaomwamini lakini vilevile na kukwaza  kwa wale watakaomkataa au kutokumuelewa na kutokumuamini hii maana yake ni nini hilo sasa linatuleta kutafakari kipengele kinachofuata kama ifuatavyo:-         

Jiwe la kukwaza katika sayuni

Ni muhimu kufahamu kuwa kuja kwa Yesu Kristo duniani, kulitabiriwa na manabii na kuwekwa wazi kuwa Yesu angekuja kwa makusudi makuu mawili, yaani kuokoa wengi  na kuwapa heshima kubwa lakini vilevile kukwaza wengi hasa wale wasiomuamini au wasiomuelewa na kumkubali na kusababisha hukumu kubwa sana kwao, 

Yohana 3:16 -18 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye. Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.”

Kwa msingi huo ujio wa Yesu Kristo una maswala makubwa mawili ya msingi kwa wanaomuamini na kwa wasiomuamini, wanaomuamini hawatatahayarika lakini kwa wale wasiomuamini watapata hukumu watakutana na mambo magumu sana sawa na alivyotabiri nabii isaya ona.  

Isaya 28:16 “kwa ajili ya hayo Bwana, MUNGU, asema hivi, Tazama, naweka jiwe katika Sayuni, liwe msingi, jiwe lililojaribiwa, jiwe la pembeni lenye thamani, msingi ulio imara; yeye aaminiye hatafanya haraka.”

Swala hili lilielezwa mapema katika maandiko lakini vilevile nabii mwingine alimuelezea Mariamu mama yake Yesu waziwazi mara baada ya kuzaliwa na walipokuwa wamempeleka kijana Yesu Hekaluni kwa kubarikiwa ona katika

Luka 2: 25-34 “Na tazama, pale Yerusalemu palikuwa na mtu, jina lake Simeoni, naye ni mtu mwenye haki, mcha Mungu, akiitarajia faraja ya Israeli; na Roho Mtakatifu alikuwa juu yake. Naye alikuwa ameonywa na Roho Mtakatifu ya kwamba hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana. Basi akaja hekaluni ameongozwa na Roho; na wale wazazi walipomleta mtoto Yesu ndani, ili wamfanyie kama ilivyokuwa desturi ya sheria, yeye mwenyewe alimpokea mikononi mwake, akamshukuru Mungu, akisema, Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, Kwa amani, kama ulivyosema; Kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako, Uliouweka tayari machoni pa watu wote; Nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, Na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.  Na babaye na mamaye walikuwa wakiyastaajabia hayo yaliyonenwa juu yake. Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.”

Kuna maneno kadhaa ambayo watafasiri wa biblia ya Kiswahili waliyachanganya au kuyanukuu vibaya hasa katika mstari wa 34 hapo ambao katika biblia ya Kiswahili Union Version unasomeka hivi Simeoni akawabariki, akamwambia Mariamu mama yake, Tazama, huyu amewekwa kwa kuanguka na kuinuka wengi walio katika Israeli, na kuwa ishara itakayonenewa.” Mstari huo katika biblia ya  kiingereza  ya NIV yaani New International version unasomeka hiviThen Simeon blessed them and said to Mary, his mother: This child is destined to cause the Falling and rising of many in Israel, and to be a sign that will be spoken againstkwa hiyo kwa tafasiri yangu mimi kifungu hiki kilitakiwa kusomeka Simeoni akawabarikia na kumwambia Mariam, mama yake, Mtoto huyu hatima yake itasababisha kuanguka (Kujikwaa) na kuinuka (kuokolewa) kwa wengi katika Israel  na kuwa Ishara itakayonenwa kinyume  unaona Kwa msingi huo Petro anamuelezea Yesu katika pande hizo mbili ya kuwa ni jiwe zuri sana la thamani na heshima kwa wale walimuamini lakini vilevile ni jiwe la kukwaza kwa wale waliomkataa na wasiomuelewa, au waliompuuzia, Wakati wote Yesu alipokuwa duniani na kufanya kazi yake  makundi mawili yalitokea wale waliomuamini na wale wasiomuamini na wale wasiomuamini Kristo wamepata hasara kubwa sana Yohana 6:54-62 Petro anatoa ushauri kwa waamini waendelee kumfuata Yesu kwa sababu yeye ni jiwe lililo hai, ni jiwe teule, ni jiwe lenye heshima na kwa kufanya hivyo hakuna mtu atakayetahayari au atakayeaibika kwa kumtegemea Yesu. 

1Petro 2:4-9 “Mmwendee yeye, jiwe lililo hai, lililokataliwa na wanadamu, bali kwa Mungu ni teule, lenye heshima. Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya Roho, ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. Kwa kuwa imeandikwa katika maandiko Tazama, naweka katika Sayuni jiwe kuu la pembeni, teule, lenye heshima, Na kila amwaminiye hatatahayarika. Basi, heshima hii ni kwenu ninyi mnaoamini. Bali kwao wasioamini, Jiwe walilolikataa waashi, Limekuwa jiwe kuu la pembeni.Tena, Jiwe la kujikwaza mguu, na mwamba wa kuangusha, Kwa maana hujikwaza kwa neno lile,wasiliamini,nao waliwekwa kusudi wapate hayo. Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu;    
    

Petro anakazia katika ujumbe wake sawa na neno la Mungu kwa vinywa vya manabii ya kuwa tumchague Yesu, yeye ni jiwe lenye heshima ni teule limendaliwa na Mungu baba kwaajili ya ukombozi wetu na kwamba ni fahari kumuamini Yesu na kumkubali na kuwa yeye hatatukataa na kuwa hatutatahayari, yesu hatamuangusha mtu awaye yote anayemtumaini na kumwendea yeye wakati wowote hata tuwapo majaribuni, hatatuangusha kwa hiyo ukimuamini Yesu na kumtegemea katika maisha yako kutoboa katika jambo lolote kuko nje nje lakini ukimpuuzia Yesu aibu na makwazo na hukumu zinakungoja ona katika maandiko:- 

Warumi 9:33 “kama ilivyoandikwa, Tazama, naweka katika Sayuni jiwe likwazalo, na mwamba uangushao; Na kila amwaminiye hatatahayarika.”  

Kumwamini Yesu kunalipa na kuliwapa faida kubwa wale waliomsadiki, lakini wale wanaojifanya wana hekima na akili na wanaomtambua Yesu kama mtu wa kawaida watajikwaa, watu hawajikwai kwa Yesu tu wanajikwaa hata kwa neno lake na kukataa ujumbe wake hata leo, Yesu hatambuliki kwa historia ya kibinadamu tu na hekima ya kibinadamu tu huwezi kumtambua Yesu kwa hisia tu, au kwa ujuzi wako binafsi, wako watu waliojikwaa kwa sababu walimuona Yesu kuwa ni wa kawaida tu wakitimia akili zao na hekima ya kibinadamu watu wengi wataingia dhambini na hatimaye kuingia mtoni kwa sababu ya kutumia fahamu zao katika maswala ya kiungu, wako watu wenye dharau kubwa sana kuhusu Mungu, na mambo ya Mungu huonekana kama ya kipumbavu kwao, na wengine hulichukulia neno la Mungu kwa mazoea tu  jambo hili litawagharimu gharama kubwa sana kwa sababu watajikwaa na ukijikwaa hukumu itakupasa 

Marko 6:1-3 “Akatoka huko, akafika mpaka nchi ya kwao; wanafunzi wake wakamfuata. Na ilipokuwa sabato, alianza kufundisha katika sinagogi; wengi waliposikia wakashangaa, wakisema, Huyu ameyapata wapi haya? Na, Ni hekima gani hii aliyopewa huyu? Na, Ni nini miujiza hii mikubwa inayotendeka kwa mikono yake? Huyu si yule seremala, mwana wa Mariamu, na ndugu yao Yakobo, na Yose, na Yuda, na Simoni? Na maumbu yake hawapo hapa petu? Wakajikwaa kwake.” 

Hatuwezi kumtambua Yesu kwa akili za kawaida na ujuzi wa kawaida Yesu alikuja ili wanyenyeevu watu waliovunjika moyo waweze kumkubali na watu wenye kiburi waweze kukataliwa Yesu ataendelea kuwa jiwe la kukwaza kwa watu wote wanaojidhani kuwa wana hekima ya mwilini na watu wote wenye kiburi na wale wanaojihesabia haki na ndio maana Yesu alipokuja duniani Mafarisayo ambao  walifikiriwa kuwa ndio wenye Haki waliumbuliwa na kujulikana kama wanafiki, wale waliokuwa wakiitumainia haki yao wenyewe waliumbuka na kujiona kuwa sio kitu kila mtu anayejitumainia na kujiamini mwenyewe Yesu kama jiwe la kukwaza litawasaga tikitiki, watu wasio na akili huitegemea akili yao wenyewe, lakini Yesu ameifanya hekima ya dunia hii kuwa ni upuuzi na kuifanya kuwa si kitu ni kupitia kumwamini Yesu tu tunaweza kuokolewa na kuhesabiwa haki kutoka kwa Mungu, kila anayemuami Yeye hatatahayari wala hatakwazika lakini kila anayejitumainia atakwazika na kukengeuka na kuingia katika hukumu ya Mungu. Mungu hawezi kueleweka kwa hekima ya kibinadamu, wengi waliokosa Baraka za Mungu ni wale waliopuuzia neno la Mungu na kuona kama Yesu hana maana lakini wale wanaomkubali wanazijua nguvu zake na uwezo wake 

1Wakoritho 1:18-19 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu. Kwa kuwa imeandikwa, Nitaiharibu hekima yao wenye hekima, Na akili zao wenye akili nitazikataa.”   
              

Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima