Jumapili, 5 Juni 2016

Ujumbe: Makusudi ya Bwana Hayawezi Kuzuilika!



Ayubu 42:1Ndipo Ayubu akamjibu BWANA na Kusema Najua ya kuwa waweza Kufanya Mambo yote  Na ya makusudi yakohayawezi kuzuilika.”

 Ayubu alielewa Kuwa makusudi ya Mungu hayawezi kuzuilika
 
Watu wengi sana Duniani wanaishi Maisha ya huzuni na kukata tamaa kwa sababu ya kutokuwa na ujuzi wa kutosha kuhusu Mungu na makusudi ya Mungu katika maisha yao, Na huuzunika zaidi wanapopitia katika Magumu, masumbufu na Mateso ya aina mbalimbali wakati mwingine ikiwa ni magonjwa, kuchukiwa na hata kutendewa mambo mabaya au kupatwa na Mabaya, Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu katika mambo yoote (Mema au mabaya) anaweza kuyatumia katika kutimiza Mpango wake mwema katika maisha Yetu. 

Warumi 8:28Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema yaani wale walioitwa kwa kusudi lake

Andiko la msingi linatoka katika kitabu cha Ayubu ni kitabu cha kifalsafa kinachojadili dhana kuhusu Mateso kwa wanadamu na Mtazamo wa Mungu, wote tunajua kuwa Ayubu alipatwa na Mateso na mitihani migumu ya kupita kawaida, Muda Hautoshi kuangalia ni hasara gani na mateso gani aliyapitia, lakini wote tunajua kuwa Ayubu hakutenda dhambi, na hata kama angetenda Mungu ni wa rehema na hawezi kutulipa mabaya kwa sababu ya ubaya wetu, Rafiki za Ayubu walimlaumu Ayubu na kumtetea Mungu walionyesha wazi kuwa haiwezekani Mateso hayo yampate Ayubu kama Ayubu hakuwa na Makosa, aidha Ayubu alijitetea sana kuwa hakuna makosa aliyoyafanya, Ayubu ingawa hakufanya dhambi lakini alimlaumu Mungu katika kiwango cha kufikia kuonyesha Kiburi na kuonyesha kuwa Mungu hayuko sawa, ni kama alikuwa akimhoji Mungu kwa nini niyapitia haya
Kutokana na majibu ya Mungu kwa Ayubu hatimaye Ayubu alitambua

1.      Mungu huruhusu mambo yote yatupate kwa makusudi yake mema
2.      Kila jambo ambalo Mungu uliruhusu litokee katika maisha yetu katika hekima yake Mungu huruhusu kwa makusudi
3.      Hata mateso ya Mwanadamu na mapito magumu yana maana katika kusudi la Mungu

Kwa sababu hiyo basi ni muhimu kwetu kuamini kuwa Mungu anaweza kufanya mambo yote, Kuamini kuwa kama tunatembea katika Makusudi ya Mungu basi hakuna cha kutuzuia, wala mtu wa kuzuia kusudi la Mungu kwetu katika maisha yetu.

Ni muhimu kwetu tu kutambua makusudi ya Mungu katika maisha yetu, na kutambua kuwa hakuna jambo linalotokea kwa Bahati mbaya “Socrates alisema maisha yasiyotafakariwa Hayafai kuyaishi” mimi nasema “Kuishi maisha yasiyo na kusudi nikupoteza mwelekeo” Mungu ametuumba kwa Makusudi na ni lazima makusudi hayo yatimizwe.

Mungu akikusudia Jambo katika maisha yako hakuna anyeweza Kulibatilisha

Mungu huyabatilisha Mashauri ya watu waovu Dhidi yako

Yusufu alipewa Ndoto yale yalikuwa ni Makusudi ya Bwana katika maisha yake hata hivyo alipitia changamoto za aina mbali mbali, tunapopitia hayo ni muhimu kutambua kuwa Kusudi la Mungu haliwezi kubatilika.

Daudi alipakwa mafuta kwa kusudi la Kuwasaidia Israel kama Mfalme, Sauli alitaka kumuua mara kadhaa alimtupia mkuki ili kuharibu kusudi na mpango wa Mungu lakini hatimaye Daudi alimiliki na kutawala

Musa alikuwa auawe katika mpango mbaya wa mfalme wa Misri aliyeamuru watoto wa kiume wauawe, Mungu katika hekima yake alimfanya Musa huyohuyo alelewe ikulu na kuwa salama zaidi
Kiko mifano mingi inayothibitisha kuwa Makusudi ya Mungu hayawezi kuzuilika, Adui zetu wanapotufikiria mabaya Mungu hutufikiria mema au kutumia ubaya wao kutuletea mambo mema.

Zaburi 33:10-11“Bwana huyabatilisha Mashauri ya mataifa, Huyatungua makusudi ya watu, Shauri la Bwana lasimama milele. Makusudi ya moyo wake vizazi na vizazi”

Mithali 21:30 - 31 “Hapana Hekima wala ufahamu, wala shauri juu ya Bwana, farasi huwekwa tayari kwa siku ya vita Lakini bwana ndiye aletaye wokovu” 

Isaya 8:10 “ Fanyeni Shauri pamoja nalo litabatilika, Semeni neno, Lakini halitasimama kwa maana Mungu yu pamoja nasi”

Mungu akikusudia hakuna anayeweza kubatilisha
 
Isaya 14:27 “Maana Bwana wa majeshi amekusudia, naye ni nani atakayelibatili? Na Mkono wake uliionyooshwa ni nani atakayegeuza nyuma?

Hata wanadamu wafanye hila bado kusudi la Mungu ndio litakalo simama
 
Mithali 19:21 “Mna hila nyingi moyoni mwa mtu, Lakini Shauri la Bwana ndilo Litakalosimama”

Paulo Mtume alikuwa amekusudia kuuona na Rumi pia
Warumi 1:15 “Kwa hiyo kwa Upande wangu mimi ni tayari kuihubiri injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi” 

Lakini Wayahudi walikusudia kwa kila namna kuharibu mpango na makusudi ya Paulo, walitaka kumuua kabla hajafika Rumi Angalia
 
Matendo 23:12-15 “Kulipopambauka,Wayahudi wakafanya mapatano, wakajifunga kwa kiapo kwamba hawatakula wala hawatakunywa hata wamwue Paulo.  Na hao walioapiana hivyo walipata zaidi ya watu arobaini. Nao wakaenda kwa wakuu wa makuhani na wazee, wakasema, Tumejifunga kwa kiapo tusionje kitu hata tumwue Paulo. Basi sasa ninyi pamoja na wazee wa baraza mwambieni jemadari amlete chini kwenu, kana kwamba mnataka kujua habari zake vizuri zaidi; na sisi tu tayari kumwua kabla hajakaribia.  
        
Angalia je hila zao zilifanikiwa?
Matendo 23: 11 “.Usiku ule Bwana akasimama karibu naye, akasema, Uwe na moyo mkuu; kwa sababu, kama ulivyonishuhudia habari zangu Yerusalemu, imekupasa kunishuhudia vivyo hivyo Rumi nako.”

Ni muhimu kufahamu kuwa kama unatembea katika kusudi la Mungu basi hakuna anayeweza kuzuia kusudi hilo na kamwe hupaswi kukata tamaa unapoona mambo magumu, vikwazo na hila za ibilisi na mipango ya kukukatisha tamaa hila na matendo mabaya ya watu dhidi ya ndoto zako hakuna muda wa kumlaumu mtu au kutafuta mchawi ni nani, jambo moja unalopaswa kulitambua ni kuwa “Makusidi ya Mungu hayawezi kuzuilika” Mungu amekupa nguvu na mamlaka ya kubatilisha hata Mashauri ya Adui zako hata kama mashauri hayo yanaonekana kana kwamba yanatoka kwa Mungu angalia.

 2Samuel 16:23, Na shauri lake Ahithofeli alilokuwa akilitoa siku zile lilikuwa kama mtu aulizapo kwa neno la Mungu, Ndivyo yalivyokuwa mashauri yake Ahithofeli kwa Daudi na Kwa Absalom”

Daudi alitambua kuwa Ahithofeli alikuwa mtu mashuhuri kwa Ushauri na ushauri wake ilikuwa kama kuuliza kwa Mungu na Ahithofeli  alipokuwa ameasi kwa Daudi Dua za daudi kwa Mungu ilikuwa ni kuilaani karama ya ushauri ya Ahithofeli na kuibatilisha 

2Samuel 15:31 “Mtu mmoja akamwambia Daudi ya Kwamba Ahithofeli yu katika hao walioambatana na Absalom, Daudi akasema Ee Bwana nakusihi Uligeuze Shauri la Ahithofeli liwe Batili”

Ni muhimu kwa kila mmoja wetu kumsihi Mungu ili mashauri mabaya yanayotolewa dhidi yatu yaweze kuwa Batili, mawazo mabaya yanayotolewa dhidi yetu yabatilike maneno mabaya yanayotolewa dhidi yako yabatilike Bwana na abatilishe manuizo yote ya wachawi na laana zote na kila mpango ambao sio makusudi ya Bwana dhidi ya maisha yetu katika Jina la Yesu Amen.

Ujumbe na Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.

Hakuna maoni: