Jumatatu, 17 Juni 2024

Basi msiutupe ujasiri wenu !

 

Waebrania 10:32-36 “Lakini zikumbukeni siku za kwanza, ambazo, mlipokwisha kutiwa nuru, mlistahimili mashindano makubwa ya maumivu; pindi mlipotwezwa kwa mashutumu na dhiki, na pindi mliposhirikiana na wale waliotendewa hayo. Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang'anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo. Basi msiutupe ujasiri wenu, kwa maana una thawabu kuu. Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi.”




Utangulizi:

Ndugu zangu wapenzi!, Leo nataka tuchukue muda kutafakari kwa pamoja kifungu hiki muhimu Katika kitabu cha Waebrania 10:32-36, kifungu hiki bila shaka kinazungumza na moyo wa kila mmoja wetu,  na kina makusudi ya kumtia moyo na kumjenga kila Mkristo kwa ngazi yoyote ile ya kiroho, kuendelea kuwa na ujasiri katika Kristo, bila kujali ni aina gani ya mapito unapitia, na bila kujali kuwa mapito hayo yatadumu kwa muda mrefu kiasi gani, tunapopita katika changamoto nzito, mateso, fadhaa, fedheha, magumu, hatari na misukosuko ya aina yotote ile, kama tukisimama katika Kristo hatari hizo haziwezi kufua dafu na zitatuletea thawabu kubwa sana, lakini hatari kubwa zaidi kuliko hizo ni kuupoteza ujasiri wetu wakati mambo magumu yanapoendelea hata kutufikisha katika ngazi ya kushindwa kuendelea kujivunia wokovu tuliopewa na Bwana wetu Yesu Kristo au kujivunia Yesu mwenyewe.

Kitabu cha Waebrania ni kitabu chenye kuzungumzia theolojia zoefu ya kutembea na Kristo (Experimental Theology) ambapo Mwandishi ametumia uwezo wake mkubwa katika kuelezea ubora wa Yesu Kristo na kuonyesha hasara kubwa ya kumpoteza Yesu, au kuupoteza wokovu, kwa hiyo Mwandishi anatumia uzoefu wake kuwatia moyo wasomaji wake kuendelea kuwa na msimamo katika Kristo, bila kujali ni aina gani ya mapito wanaipitia kwani kwa kufanya hivyo watajipatia thawabu kubwa sana. Jambo hili linatuhusu sisi nasi tunaoishi katika siku za leo zilizo ngumu zaidi na zenye mapito mengi, Tutajifunza somo hili Msiutupe ujasiri wenu kwa kuzingatia vipengele vikuu vitatu vifuatavyo:-

 

·         Zikumbukeni siku za Kwanza (Mst 10:32-33)

·         Nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi (Mst 34)

·         Basi msutupe ujasiri wenu (Mst 35-36)

 

Zikumbukeni siku za Kwanza (Mst 32-33)

Waebrania 10:32-33 “Lakini zikumbukeni siku za kwanza, ambazo, mlipokwisha kutiwa nuru, mlistahimili mashindano makubwa ya maumivu; pindi mlipotwezwa kwa mashutumu na dhiki, na pindi mliposhirikiana na wale waliotendewa hayo.”

Mwandishi anawakumbusha Waebrania waliomuamini Yesu Kristo kukumbuka siku za Kwanza yaani siku za mwanzoni walipokuwa wamemuamini Bwana Yesu na kujua habari za wokovu, baada ya kuipokea injili, watu hawa walikuwa na uwezo mkubwa sana wakustahimili mashindano magumu, makubwa yaliyowaletea maumivu, wakati walipodhalilishwa yaani kutwezwa na kushutumiwa na kuteswa, kwa kupitia dhiki kwaajili ya Imani, sio hivyo tu Waebrania pia walisimama bega kwa bega na ndugu zao wote waliopitia mateso katika Imani wazi wazi bila kuogopa, hata katika macho ya wengine, walikuwa na umoja, na waliwahurumia wale ambao waliteseka kwa sababu ya Imani kama wao wakionyesha moyo mkubwa wa kuwatia moyo japo lilikuwa jambo la hatari sana, lakini walilifanya  huku wakifurahia miyoni mwao sawasawa na mafundisho ya Kristo na mitume.

Mathayo 5: 11-12 “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana ndivyo walivyowaudhi manabii waliokuwa kabla yenu.”

Matendo 5:40-41 “Wakakubali maneno yake; nao walipowaita mitume, wakawapiga, wakawaamuru wasinene kwa jina lake Yesu; kisha wakawaacha waende zao. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo

Walikuwa na ujasiri, mmoja alipoteseka walikubali kuteseka naye, na kumkingia kifua na kuwa tayari hata kuhatarisha maisha yao, waliishi sawasawa na injili ya Kristo na mitume na hawakuogopa lolote, walisimama kidete  walikubali kuumia pamoja na ndugu zao katika Bwana kama viungo katika mwili wa Kristo, Nyakati za agano jipya mtu alipokuwa amefungwa alipata mateso makali kama mtu anayetafuta kuuawa, kwa hiyo watu walioko gerezani walihitaji kutiwa moyo sana na kutembelewa na kujaliwa  na ndugu na jamaa na marafiki vinginevyo wangeweza kufa kwa kukata tamaa,  lakini sio hivyo tu ilikuwa ni hatari sana kama Mkristo angemtembelea mkristo mwenzake gerezani, kwenda kumtia moyo kwa kuwa kwa kufanya hivyo ni kama unakwenda kujishitaki mwenyewe kwa kosa lile lile lililomtia ndani mwenzako, na mara kwa mara waamini walikamatwa kwa tendo hilo tu la kuwatembelea wenzao magerezani, lakini pamoja na changamoto hizo zote Waebrania hawakuacha kusimama na wenzao waliokuwa magerezani wakikumbuka maneno ya Bwana kuhusu wafungwa pia

Mathayo 25:34-40 “Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu; kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha; nalikuwa uchi, mkanivika nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia. Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha? Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika? Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia? Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.”

Hawakupoteza ujasiri wao, walikuwa na imani kali sana katika Kristo, adui zao walikuwa na nguvu na walikuwa wengi, watu walipoteza ndugu zao, wengine walipoteza mali, ardhi zao, nyumba zao, familia zao na urithi wao, kumpokea Kristo katika familia za kiyahudi ilikuwa ni sawa na kujifuta kabisa katika kabila hilo mila na desturi, Lakini walikubali kupoteza kila kitu kwaajili ya Imani katika Kristo kwa nini walifanya hivyo waliamini Kuwa na Kristo ni kuwa na mali njema zaidi, kupoteza kila kitu kwaajili ya Kristo kungeleta furaha kubwa zaidi katika maisha yajayo.

Nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi (Mst 34)

Waebrania 10:34 “Maana mliwaonea huruma wale waliokuwa katika vifungo, tena mkakubali kwa furaha kunyang'anywa mali zenu, mkijua kwamba nafsini mwenu mna mali iliyo njema zaidi, idumuyo.”

Kama nilivyodokeza awali kuwa ilikuwa ni hatari sana kuonyesha matendo ya huruma dhidi ya wale waliokuwa kifungoni,  Lakini Waebrania waliokuwa wamempokea Yesu walionyesha matendo hayo ya huruma kwa wafungwa na wengine walioteseka, kuonyesha huruma kwa mtu aliyefungwa au anayeteseka kwaajili ya imani ilikuwa ni sawa tu na kuianika imani yako wazi wazi jambo ambalo lilipeleka nawe kuwa hatarini, Lakini hawa jamaa walikuwa tayari kwa lolote, walipokea mateso hayo kwa Imani na furaha kubwa, furaha yao haikuwa katika kupoteza walivyopoteza lakini ilikuwa katika Imani ya kuwa wamepoteza kwaajili ya Kristo na kuwa watapata thawabu iliyokubwa zaidi, walijua nafsini mwao kuwa iko mali mbinguni iko mali katika ulimwengu wa roho zaidi ya ile waliyopoteza na kuwa hizi walizopoteza ni za muda tu lakini kile watakachokipata ni cha milele, walihesabu kuwa mateso ya sasa si kitu kama utukufu ule utakaofunuliwa baadaye kwa Bwana wetu Yesu Kristo.

Warumi 8:18 “Kwa maana nayahesabu mateso ya wakati huu wa sasa kuwa si kitu kama utukufu ule utakaofunuliwa kwetu.”

2Wakorintho 4:17-18 “Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana; tusiviangalie vinavyoonekana, bali visivyoonekana. Kwa maana vinavyoonekana ni vya muda tu; bali visivyoonekana ni vya milele.”

Waebrania walijawa na imani hii, Mafundisho haya yalikuwa yamewakolea sana kwa hiyo waliwaza thawabu na malipo ya umilele watakayopokea kwa Mungu kuliko maswala ya muda mfupi ya dunia hii, haya ndio yalikuwa mawazo yao ya kwanza, hii ndio ilikuwa Imani yao ya kwanza, huu ndio ulikuwa ujasiri wao wa kwanza na huu ndo msingi wa Imani yao uliokuwa umejengwa na mitume nyakati za kanisa la Kwanza, kwa hiyo mwandishi anawakumbusha siku zile za kwanza! Walivyokuwa na msimamo huu mara baada ya kuokolewa kwao, kutiwa nuru.

Basi msiutupe ujasiri wenu (Msta 35-36)

Waebrania 10:35-36 “Basi msiutupe ujasiri wenu, kwa maana una thawabu kuu. Maana mnahitaji saburi, ili kwamba mkiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu mpate ile ahadi.”

Pamoja na mambo mazuri waliyokuwa nayo na moyo mkubwa wa uvumilivu na subira, Mwandishi wa kitabu cha Waebrania anaonya, na kutoa tahadhari kwamba wasije wakautupa ujasiri huu, Ujasiri huu ni upi?  Mstari huu katika Biblia ya kiingereza unasomeka hivi  “ So do not throw away your CONFIDENCE; it will be richly rewarded” Neno la kiingereza Confidence yaani ujasiri katika Kiyunani linasomeka “Parrhēsia” ambalo kiingereza tunapata neno Bluntness, assurance, bold, freely na confidence, sawa tu na neno, Kwa msimamo, kwa kujiamini, kwa ujasiri, kwa uhuru, kwa uaminifu.

Mwandishi alikuwa anaona wazi kuwa kama mateso haya yataendelea kwa muda mrefu na hali hii ya kuteseka itaendelea uko uwezekano wa waamini wa Kiebrania wakaanza kulegea na kupoteza uaminifu wao, wanaweza kuanza kupoteza ujasiri, kupoteza kujiamini, kupoteza msimamo  na kuanza kulegea  kwa hiyo anatoa wito kwamba wasiutupe ujasiri wao kwa sababu una thawabu kubwa sana, na kuwa waendelee kukaza, kuwa imara na kuamini.

Hakuna jaribu gumu duniani kama Kusubiri, kusubiri ndiko kunakowasumbua watu wengi, watu wengi sana wameiacha imani na kukosea kwa sababu walichoka kusubiri najua unaweza kusema mchungaji wewe hujui habari ya subira nisikilize najua sana na najua ugumu wa kusubiri na kuvumilia, yako mambo katika maisha yangu nimevumilia sana na nikamuona Mungu lakini yako mambo yalinishinda, yaliniumiza na yalinifanya ninung’unike, kwa hiyo naelewa habari ya subira na uvumilivu najua kilivyo kitu kigumu, hapa ndipo watu wengi sana wameutupa ujasiri wao, wamefarakana na imani, wamemuacha Yesu, kwa sababu tu walishindwa kusubiri, Imani yetu pia inajengwa katika kusubiri, Yusufu alisubiri miaka 13 mpaka ndoto zake kutimia, Mateso ya  Ayubu yalidumu kwa miaka 13 mpaka kupona na kurejeshewa kila alichokipoteza, Daudi aliusubiri ufalme kwa miaka karibu 14 huku akikataa kulazimisha awe mfalme kwa kumuua Sauli, Ibrahimu alimsubiria Isaka kwa miaka 25 na alishindwa kusubiri akajitafutia Ishamaeli wake, nimeona watu wengi sana wakishindwa kushika ujasiri wao mpaka mwisho japo mwanzoni walikuwa na imani, lakini pale Mungu alipoonekana anachelewa walichoka, Mungu leo anakutaka usichoke, anakutaka uwe na subira, anakutaka uendelee kuvumilia hatimaye utauona mkono wake yeye atakutokea tu, Mungu ameahidi Baraka kubwa sana za kimwili na kiroho kwa kila mwenye subira  na wakati tunaposubiri tuendelee kuyatenda mapenzi ya Mungu kwa uvumilivu mpaka mwisho ili tusipoteze thawabu yetu iliyokusudiwa na zaidi sana tuweze kuifikia ile ahadi ambayo kwayo Mungu ametuahidi, Mwandishi anaonyesha kuwa tunaweza kuifikia ahadi tukiisha kuyafanya mapenzi ya Mungu !

Ufunuo 2:3-5 “tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.”

Yakobo 5:10-11 “Ndugu, watwaeni manabii walionena kwa jina la Bwana, wawe mfano wa kustahimili mabaya, na wa uvumilivu.  Angalieni, twawaita heri wao waliosubiri. Mmesikia habari ya subira yake Ayubu, mmeuona mwisho wa Bwana ya kwamba Bwana ni mwingi wa rehema, mwenye huruma.”

Maandiko yanatuonyesha ya kuwa Mungu ni mwema tena ni mwingi wa rehema, na amejaa huruma hawezi kukuacha kama ulivyo, kubali kuendelea kuwa somo ili uwe ushuhuda mzuri, ziko baraka zinakusubiri, kaka zangu na dada zangu, tunakutana na majaribu mengi sana duniani majaribu ya kutisha na kutikisa yanaweza hata kutuondolea ujasiri wetu, lakini tusikubali kuibiwa thawabu zetu kumbuka uaminifu wa Mungu, kumbuka Kuwa Mungu ni mwema katika ahadi zake, watu wengi leo hawako tayari kuteseka kwaajili ya Kristo, wala hawataki kupoteza, wala kusubiri na kuvumilia  Yesu Kristo Bwana wetu ni kielelezo cha uvumilivu aliweza kuvumilia mapingamizi makuu sana kwaajili ya furaha iliyowekwa mbele yake, kaka zangu na dada zangu wapenzi natoa wito kwa kanisa na kila mtu anayesoma ujumbe huu tuvumilie, tuvumilie, tuvumilie, uvumilivu unalipa, Mungu hawezi kutuagiza kitu ambacho yeye mwenyewe hajawahi kukifanya tukishindwa kuvumilia na kuwa na subira maana yake tumeutupa ujasiri wetu, Yesu ni ujasiri wetu mkuu, Imani katika yeye ni ujasiri wetu mkuu hatupaswi kuupoteza tunapokutana na changamoto za aina mbalimbali, suluhu iko wazi kwamba tunapaswa kukumbuka imani yetu mwanzoni, ujasiri tuliokuwa nao mwanzoni wakati tulipomuamini Bwana Yesu, tuendelee kuvumilia na kuendelea kutenda mapenzi ya Mungu, na kuwa na subira kamwe tusiutupe ujasiri wetu una thawabu kubwa sana, ahadi za Mungu ni kweli, tuendelee kuamini katika ahadi zake, neno lake na kujua ya kuwa yeye ni mwaminifu tu naye atatenda lile tunalolisubiri kwa muda.

Waebrania 12:2-3 “tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”

Maombi!

Baba katika jina la Yesu;  tunakushukuru kwa somo zuri la mfano kutoka kwa Waebrania hawa, waliovumilia magumu kwa furaha wakiendelea kudumu katika Imani bila kujali ni magumu gani waliyapitia, sisi nasi utupe uvumilivu, na subira ili tuzione rehema zako na wema wako na baraka zilizofichika katika kipimo cha uvumilivu, kwa ulimwengu huu wa sasa na ule ujao,  wako wanaosubiri watoto, wako wanaosubiri kuolewa, wako wanaovumilia mateso na changamoto mbalimbali, wako wanaosubiri kazi, wako wanaoteseka kwa sababu wamekuamini, wako wanaosubiri kutoka kiuchumi na kufanikiwa katika maeneo mbalimbali, wako pia wanaosubiri kuinuliwa kihuduma; Baba Mtumwa wako ninawaombea kwa jina la Yesu Kristo, asante kwa sababu utatupa kuvumilia kwa neema na kila aliyewahi kushindwa kuvumilia msamehe na utupe neema ya uaminifu wako asante kwa sababu nimekuomba kwa ufupi nawe utafanya kwa urefu kwa kadiri ya wingi wa rehema zako, asante kwa sababu utafanya hivyo na kuzidi katika jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai ameen!

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!       

Jumatatu, 10 Juni 2024

Kupandishwa kwa mifupa ya Yusufu!


Mwanzo 50:24-26 “Yusufu akawaambia nduguze, Mimi ninakufa, lakini Mungu atawajia ninyi bila shaka, atawapandisha toka nchi hii, mpaka nchi aliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo. Yusufu akawaapisha wana wa Israeli, akasema, Bila shaka Mungu atawajia ninyi, nanyi mtaipandisha huko mifupa yangu. Basi Yusufu akafa, mwenye miaka mia na kumi; wakampaka dawa, wakamtia katika sanduku, huko Misri.”



Utangulizi:

Kaka zangu na dada zangu katika Kristo! Leo tunachukua Muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu kuhusu kutimizwa kwa mojawapo ya agizo la Muhimu sana la Yusufu kwa wana wa Israel, wote tunakumbuka habari za Mtu huyu Muhimu aliyeitendea mema familia yake na mataifa mengi kwa kuyaokoa na njaa kupitia uwezo wake mkubwa wa kiutawala na mipango chini ya Farao iliyoleta wokovu kwa wengi, Pamoja na kuwa ndugu zake walimfanyia vibaya lakini wote tunaukumbuka Moyo wa Yusufu jinsi ulivyokuwa mwema kwani hakuthubutu kulipa mabaya, alihesabu yaliyomkuta kama mapenzi ya Mungu, jambo lililopelekea kuwa mtu wa kuheshimiwa sana katika familia yake, Lakini akiwa anakaribia kufa mtu huyu aliwakusanya Israel wote na akiwa amezungukwa na wana wa Israel pamoja na wanae na wajukuu zake aliwaeleza habari za Muhimu sana na akazisisitiza kwa kuwaapisha kwamba ni lazima Bwana atawatokea tena na Bila shaka atawapandisha kutoka katika inchi hii Misri, na kuwa atawapandisha katika inchi ile aliyowaapia baba zao yaani Ibrahimu, Isaka na Yakobo, na ya kuwa wakati huo utakapowadia wahakikishe wanaipandisha Mifupa yake huko na aliwaapisha kuwa jambo hili ni lazima walitimize.

 Mwanzo 50:24-26 “Yusufu akawaambia nduguze, Mimi ninakufa, lakini Mungu atawajia ninyi bila shaka, atawapandisha toka nchi hii, mpaka nchi aliyowaapia Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo. Yusufu akawaapisha wana wa Israeli, akasema, Bila shaka Mungu atawajia ninyi, nanyi mtaipandisha huko mifupa yangu. Basi Yusufu akafa, mwenye miaka mia na kumi; wakampaka dawa, wakamtia katika sanduku, huko Misri.”

Tunaweza kujiuliza swala la msingi sana kwanini mtu huyu aliyekuwa na mafanikio makubwa sana kule Misri, aliyestawi sana na kuwastawisha ndugu zake wote lakini bado hataki kusahau inchi ya Urithi wa baba zake?  Yusufu alikuwa na ujuzi mkubwa sana kuhusu Mungu wa baba zake ya kuwa hakuna neno ambalo Mungu wetu ataahidi likaanguka bure yaani likapita bila kutimizwa, Yusufu anamjua wazi Mungu wa Ibrahimu na Isaka na Yakobo kuwa hakuna neno linalotoka katika kinywa chake ambalo liliwahi kuanguka bure, Mungu alikuwa ameahidi kwa kinywa chake Tangu zamani ya kuwa atawapa Israel Inchi ya Mkanaani, Nchi iliyojawa na maziwa na asali. Yusufu alikuwa na Imani kuwa neno hilo lazima litakuja kutimizwa, Hivyo hata kama yu katika hali ya kufa anajua kuwa Mungu atatimiza ahadi zake, Yusufu aliendelea kumuamini Mungu kwamba atawaokoa watu wake na kuwaondoa katika inchi ile ambayo wangetumikishwa kwa utumwa mzito ambao kimsingi pia waliujua kuwa utakuja na ya kuwa ni lazima atawaleta tena katika inchi ya ahadi. Nadhani Yusufu alikuwa anakumbuka kile ambacho Mungu alizungumza na baba zake Ibrahimu na Isaka na Yakobo.

Mwanzo 15:13-16 “BWANA akamwambia Abramu, Ujue hakika ya kwamba uzao wako utakuwa mgeni katika nchi isiyo yake, watawatumikia watu wale, nao watateswa muda wa miaka mia nne. Hata na taifa lile, watakaowatumikia, nitawahukumu; baadaye watatoka na mali mengi. Lakini wewe utakwenda kwa baba zako kwa amani, utazikwa katika uzee mwema. Na kizazi cha nne kitarudi hapa, maana haujatimia uovu wa Waamori bado.”

Tutajifunza somo hili kupandishwa kwa mifupa ya Yusufu kwa kuzingatia vipengele viwili vifuatavyo:-

1.      
  
Kwanini Mifupa ya Yusufu katika inchi ya Kanaani?

2.       Kupandishwa kwa mifupa ya Yusufu


Kwanini Mifupa ya Yusufu katika inchi ya Kanaani?

Yusufu aliinuliwa sana katika inchi ya Misri, alikuwa maarufu mno? Aliwasaidia wengi na kuheshimika sana na alipata mafanikio makubwa, aliwapa ndugu zake inchi ya Gosheni mahali ambapo Mto Nile unamwaga maji yake katika bahari ya Mediteraniani, ni eneo lenye rutuba na ustawi mkubwa sana kwa wana wa Israel na kwa kweli walifanikiwa sana, walimiliki mali nyingi mpaka wenyeji wao waliona wivu, waliongezeka sana walistawi na walikuwa na Nguvu,  Gosheni lilikuwa eneo lenye kufaa kwa malisho pia, unaweza kujiuliza kwanini Yusufu anawaapisha Israel na kuwahakikishia kuwa watakuja kuondoka na hivyo waikumbuke mifupa yake na kuipeleka katika inchi ya ahadi?

1.       Yusufu alikuwa amejifunza ya kuwa Mungu wa baba zake ni Muaminifu, Hakuna neno hata moja amewahi kuliahidi lisitimizwe bila kujali kuwa itachukua muda gani, Yeye mwenyewe alikuwa amejifunza uaminifu wa Mungu kwani Ndoto zile alizooteshwa na Mungu Japokuwa zilimpitisha katika mapito Mengi lakini zilikuja kutimia, alikuwa amejifunza kivitendo kwamba ni Mungu asiyeweza kusema uongo na ya kuwa neno lake haliwezi kwenda bure, uaminifu wake na fadhili zake ni za milele nazo hudumu kizazi hata kizazi!

 

Hesabu 23:19 “Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza?

 

Isaya 55:10 -11 “Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”

 

Kwa hiyo Yusufu alikuwa na uhakika wa Mungu wa baba zake ya kuwa hakuna kitu anaahidi kisha asikitimize, kwa hiyo tukio la kuagiza mifupa yake kuzikwa katika inchi ya kanaani ni wazi kuwa alikuwa na Imani ya kuwa wana wa Israel watatoka katika inchi ya utumwa na kuwa Mungu atawarejesha katika inchi ya ahadi.

 

Waebrania 11: 22 “Kwa imani Yusufu, alipokuwa amekaribia mwisho wake, alitaja habari za kutoka kwao wana wa Israeli, akaagiza kwa habari ya mifupa yake.”

 

2.       Yusufu anatumika kama alama ya kisayuni kwa wana wa Israel, Israel leo wametawanyika kila mahali duniani, na nafahamu na wote tu mashahidi kuwa wengi wamerudi nyumbani, wako pale Israel leo katika inchi ambayo dunia inachanganyikiwa kuhusu mustakabali wa inchi ile, Lakini Yusufu anawakumbusha Wayahudi wote duniani hata pamoja na mafanikio makubwa wanayoyapata kokote waliko duniani, wanaheshimika sana wanafanikisha inchi hizo huko waliko lakini ni lazima wakumbuke kuwa wao ni Wayahudi na kuwa Mungu anatoa wito kwao kurudi Nyumbani, kuchelewa kwao kurudi nyumbani kunachelewesha kutimia kwa unabii na mapenzi mengi ya Mungu, Mungu aliahidi kuwatawanya lakini vile vile Mungu aliahidi kuwa atawarudisha,

 

Kumbukumbu 30:4-6“Watu wako waliotawanyika wakiwako katika ncha za mbingu za mwisho, kutoka huko atakukusanya Bwana, Mungu wako; kutoka huko atakutwaa; atakuleta Bwana, Mungu wako, uingie nchi waliyomiliki baba zako, nawe utaimiliki; naye atakutendea mema, na kukufanya uwe watu wengi kuliko baba zako. Bwana, Mungu wako, atautahiri moyo wako, na moyo wa uzao wako, ili umpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, upate kuwa hai.”  

 

Haijalishi vizazi vingapi vimepita, haijalishi wana siasa  wa dunia wanawaza nini Lakini Israel ni Inchi ya ahadi kwa Ibrahimu, Isaka, Yakobo na Yusufu pia, kila anayeshindana na agizo hili anashindana na agizo la Mungu, Yusufu anaonyesha moyo wa kizalendo, anajitanabahisha kuwa Myahudi halisi nyumbani ni Israel, alijua kuwa Israel watakuwa watumwa, lakini Misri sio inchi salama kiroho wala sio kwao, ina miungu mingi inayoabudiwa, walipitia magumu mengi, watoto wao wa kiume waliuawa na Yusufu anaonyesha kwamba anatamani nyumbani na nyumbani halisi ni Israel sawasawa na Neno la Mungu kwa baba zao.

 

Mwanzo 15: 18-21 “Siku ile BWANA akafanya agano na Abramu, akasema, Uzao wako nimewapa nchi hii, kutoka mto wa Misri mpaka huo mto mkubwa, mto Frati, Mkeni, na Mkenizi, na Mkadmoni, na Mhiti, na Mperizi, na Mrefai,na Mwamori, na Mkanaani, na Mgirgashi, na Myebusi.”

 

Mwanzo 17:7-8 “Agano langu nitalifanya imara kati ya mimi na wewe, na uzao wako baada yako, na vizazi vyao, kuwa agano la milele, kwamba nitakuwa Mungu kwako na kwa uzao wako baada yako. Nami nitakupa wewe na uzao wako baada yako nchi hii unayoikaa ugeni, nchi yote ya Kanaani, kuwa milki ya milele; nami nitakuwa Mungu wao.”

 

Mwanzo 28:11-17 “Akafika mahali fulani akakaa huko usiku kucha, maana jua lilikuwa limekuchwa; akatwaa jiwe moja la mahali pale akaliweka chini ya kichwa chake, akalala usingizi pale pale. Akaota ndoto; na tazama, ngazi imesimamishwa juu ya nchi, na ncha yake yafika mbinguni. Tena, tazama, malaika wa Mungu wanapanda, na kushuka juu yake. Na tazama, BWANA amesimama juu yake, akasema, Mimi ni BWANA, Mungu wa Ibrahimu baba yako, na Mungu wa Isaka; nchi hii uilalayo nitakupa wewe na uzao wako. Na uzao wako utakuwa kama mavumbi ya nchi, nawe utaenea upande wa magharibi, na mashariki, na kaskazini, na kusini; na katika wewe, na katika uzao wako, jamaa zote za dunia watabarikiwa. Na tazama, mimi nipo pamoja nawe, nitakulinda kila uendako, nami nitakuleta tena mpaka nchi hii, kwa maana sitakuacha, hata nitakapokufanyia hayo niliyokuambia. Yakobo akaamka katika usingizi wake, akasema, Kweli BWANA yupo mahali hapa, wala mimi sikujua. Naye akaogopa akasema, Mahali hapa panatisha kama nini! Bila shaka, hapa ni nyumba ya Mungu, napo ndipo lango la mbinguni.”

 

Mwanzo 48:3-4 “Yakobo akamwambia Yusufu, Mungu Mwenyezi alinitokea huko Luzu, katika nchi ya Kanaani, akanibariki, akaniambia, Mimi hapa, nitakuongezea uzao wako, na kukuzidisha, nami nitakufanya uwe kundi la mataifa; kisha nitawapa wazao wako nchi hii baada yako, iwe milki ya milele.”

 

Israel ni ya Mungu, Israel (Kanaani) ni Mungu alimpa Ibrahimu na Isaka na Yakobo, kila anayetaka Israel isiwepo anashindana na agizo la Mungu, Wayahudi wenyewe wanapaswa kuwa mstari wa Mbele kutii agizo la Mungu ambalo Ibrahimu, Isaka na Yakobo walilitii, na Yusufu hakutaka kuwa sababu ya wayahudi kubakia Misri hivyo kwa kiapo aliwaapisha kwamba akifa haijalishi watakaa muda gani Misri, lakini Lazima Mungu ataitimiza ahadi yake naye hataki kubaki ugenini, huu ni moyo wa uzalendo mkubwa na nitoe wito kwa kila myahudi kokote aliko duniani wakumbuke Kanaani, kwa sababu Mungu ameagiza hivyo.

 

3.       Yusufu alikuwa ni Mwalimu mzuri sana, alitumia kifo chake na mifupa yake kuwa alama muhimu kwa kizazi na kizazi, kumbuka Tangu walipofika Misri Israel waliishi miaka karibu 430 na Yusufu aliishi miaka 110 tu lakini Fundisho lake na kazi yote ambayo Mungu aliifanya Yusufu alihakikisha kuwa kumbukumbu yake haitafutika alihakikisha kuwa kupitia mifupa yake kila kizazi kitakumbuka umuhimu wake, na uaminifu wa Mungu na unabii wake, Yeye aliagiza siku watakapoondoka Misri aliwaapisha wakumbuke mifupa yake hivyo kizazi na kizazi katika jamii ya wayahudi kila mmoja kabla hajafa alimkubusha mtoto wake kila nyumba kulikuwa na mafundisho ya kuwa Mungu atatutoa utumwani na atakapotimiza hilo kumbukeni mifupa ya Yusufu, kila familia ilionywa jamani jamani msisahau mifupa ya Yusufu, na ndio maana Musa alipotoka Misri  japo alikuwa wa kabila la Lawi hakusahau kamwe mifupa ya Yusufu, na Wana wa Israel hata alipokufa Musa huko jangwani bado wana wa Israel chini ya Yoshua walipewa inchi na walihakikisha wanaizika mifupa ya Yusufu huko Shekemu  nchini Israel yaani inchi ya mkanaani nchi ya ahadi.

 

Kutoka 13:19 “Musa akaichukua ile mifupa ya Yusufu pamoja naye; maana, alikuwa amewaapisha sana wana wa Israeli, akisema, Mungu hana budi atawajilia ninyi; nanyi mtaichukua mifupa yangu kutoka hapa pamoja nanyi.”

 

Yoshua 24:31-32 “Nao Israeli wakamtumikia Bwana siku zote za Yoshua, na siku zote za hao wazee walioishi baada ya kufa kwake Yoshua, hao walioijua kazi yote ya Bwana, aliyowatendea Israeli. Na hiyo mifupa ya Yusufu, ambayo wana wa Israeli walikuwa wameileta kutoka Misri, wakaizika huko Shekemu katika ile sehemu ya nchi, Yakobo aliyoinunua kwa wana wa Hamori, babaye Shekemu, kwa vipande mia vya fedha; nayo ikawa ni urithi wa wana wa Yusufu.”

 

Vizazi vingi vilikuwa vimepita Lakini Israel walikumbuka umuhimu wa Yusufu na agizo lake, walilishika walilitii na walilitimiza kama walivyoapishwa na Yusufu!

 

Kupandishwa kwa mifupa ya Yusufu!

 

Kupandishwa kwa mifupa ya Yusufu katika inchi ya kanaani kunatufundisha maswala kadhaa ya Muhimu sisi kama wakristo, huu ni mfano Muhimu sana wenye vitu vya kutufunza.

 

1.       Lazima tuendelee kumuamini Mungu na ahadi zake – iwe mvua iwe jua, iwe tumefanikiwa iwe hatujafanikiwa bado Mungu ni mwaminifu, Yusufu alikuwa amebarikiwa sana na alikuwa na mafanikio makubwa sana, lakini hii haikumfanya asahau uaminifu wa Mungu. Wala haikumfanya asahau kwao!  Alikuwa amejifunza kuwa Mungu ni mwaminifu na kila alisemalo litatimia aliamini kuwa Mungu atafanya alilolisema, Ni wangapi tunaamini katika kile ambacho Bwana amekisema? Yesu Kristo ni mwaminifu kila neno lake aliloliahidi litatimia kila kitu kitapita lakini maneno yake Bwana wetu Yesu hayatapita kamwe. Ni lazima kila mtu wa Mungu awe na Imani katika Neno la Mungu. Yesu Kristo anaitwa shahidi aliye mwaminifu, ni lazima tuziamini ahadi zake na kujua ya kila alilolisema atalitimiza.

 

Ufunuo 1:4-6 “Yohana, kwa yale makanisa saba yaliyoko Asia; Neema na iwe kwenu na amani, zitokazo kwake yeye aliyeko na aliyekuwako na atakayekuja; na zitokazo kwa roho saba walioko mbele ya kiti chake cha enzi; tena zitokazo kwa Yesu Kristo, shahidi aliye mwaminifu, mzaliwa wa kwanza wa waliokufa, na mkuu wa wafalme wa dunia. Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na milele. Amina.”     

 

2.       Yusufu alifikiri yajayo – Yusufu hakujifikiri yeye mwenyewe tu, alitaka kizazi na kizazi kimuelewe Mungu, hakuwa anafanya mambo kwaajili yake, tendo lake la kuamuru kwa nguvu na lazima yaani kwa kuwaapisha lilikuwa linaonyesha anawaza maisha zaidi ya maisha haya, kila Mkristo anapaswa kuhakikisha ya kuwa injili inarithishwa kwa kizazi kijacho kwa watu waaminifu ambao watafaa kuwafundisha na wengine, Israel walikuwa waaminifu kurudia tena na tena kiapo cha Yusufu kwao kwa kizazi kilichofuata waliogopa kupata madhara endapo hawatawashirikisha watu wengine, Injili yetu inapaswa kukabidhiwa watu wengine ili kizazi na kizazi kiweze kulijua neno la Mungu vile vile kama tulivyoagizwa tangu enzi za mitume

 

2Timotheo 2:2 “Na mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”

 

3.       Umuhimu wa inchi ya kanaani – Wakristo wanapaswa kuwa Mstari wa mbele kuelewa mapenzi ya Mungu kuhusu Israel ile nchi ni lango la Mbinguni, Baraka zote zilizokusudiwa duniani kwa wanadamu wote zinapitia Israel, kwa hiyo kila mmoja anapaswa kuwatendea mema wayahudi na kuwasaidia kurudi kwao na kuisimamia inchi yao, Wamarekani na Waingereza na Wafaransa na Wajerumani wanaijua siri hii, ni afadhali kukaa kimya linapokuja swala la Israel kuliko kuropoka ropoka Israel ni ya Mungu na amewapa wana wa Ibrahimu Milele, Waarabu wanapaswa kulijua hilo, Waafrika wanapaswa kulijua hilo, Wazungu wanapaswa kulijua hilo na zaidi sana Wakristo na kuwa watetezi wakubwa kwa wayahudi, Yusufu aliipa kipaumbele inchi ya Kanaani kwa sababu ni inchi waliyoahidiwa na Mungu, makao makuu ya Bwana wetu Yesu Kristo na serikali ya ufalme wake duniani itatawala kutokea Israel na Yerusalem yakiwa makao makuu yake, linaweza kuwa jambo la kusikitisha na la kushangaza mtu yeyote yule akisimama kinyume na Mapenzi ya Mungu kuhusu Israel, waarabu wanapaswa kukumbuka hilo ya kuwa endapo wanamuheshimu Mungu basi pia wakumbuke kuiacha Israel kwa wana wa Israel na waarabu kubakia katika mataifa mengine, vinginevyo Ibrahimu na Isaka na Yakobo na Yusufu watashangaa sana wakati wa Hukumu kukuta watu wengine wakiidai inchi ya kanaani kuwa yao kinyume na mapenzi ya Mungu mwenye nguvu sana !

 

Mathayo 5:34-35 “lakini mimi nawaambia, Usiape kabisa; hata kwa mbingu, kwa maana ndicho kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa nchi, kwa maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala kwa Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu.”

 

4.       Kuwaza kuhusu uzima wa milele – Swala la mifupa ya Yusufu liatukumbusha kuwa maisha yanaendelea hata baada ya kifo, kila mtu anapaswa kufikiri zaidi ya mazingira ya kawaida kwa sababu hata baada ya uzima huu uko uzima wa milele. Mungu ameahidi uzima wa milele kwa kila anayemuamini Yesu Kristo aliyetolewa pale msalabani kwa niaba ya watu wote watakaoamini ahadi hii ni ya kweli, kwa hiyo katika kuishi kwetu duniani pamoja na mafanikio yetu yote na umaarufu wetu wote tusisahau kujiwekeza katika uzima wa milele, Yusufu hakusahau inchi ya ahadi, Hatupaswi kusahau uzima wa umilele, hatuna budi kuwekeza katika uzima wa milele na kuamini ya kuwa Mungu atatufufua kutika kwa wafu na kutupa neema ya kuketi katika mkono wake wa kuume katika ufalme wake 

 

Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.”         

 

5.       Imani ni zaidi ya kawaida ya Muda – Ni swala la Muda tu, Yusufu hakujali kuwa Israel wataondoka lini Misri lakini alikuwa na Imani kuwa iko siku Mungu atawatokea, Nasema Mungu atakutokea bila kujali muda, kila mkristo anapaswa kukumbuka kumsubiri Mungu na kuishi kwa Imani, Mwamini Mungu biola kujali Muda, mwamini Mungu kuwa atafanya kitu, mwamini Mungu kuwa atakujibu, mwamini mungu kuwa atatkutokea, mwamini Mungu kuwa atafanya, Yusufu aliishi kwa Imani, aliamini katika maneno ya Mungu wa baba yake na babu zake alihesabiwa haki kwa Imani hii

 

Waebrania 10:38 “Lakini mwenye haki wangu ataishi kwa imani; Naye akisita-sita, roho yangu haina furaha naye.”         

 

6.       Agizo kuu – Agizo la Yusufu ambalo ilishikwa na kizazi na kizazi cha wana wa Israel ni fundisho kwa kanisa ya kuwa sisi nasi tunapaswa kulikumbuka agizo la Bwana wetu Yesu Kristo na kuihubiri injili duniani na kwa kila kiumbe, kama wana wa Israel vizazi na vizazi walilishika agizo la Yusufu, wakristo hawana budi kuhakikisha wanalishika agizo la Bwana Yesu, kuhakikisha kuwa kwa nguvu zetu zote tunarithisha injili au habari njema za wokovu  ulioletwa kwetu na Bwana wetu Yesu Kristo kwa kufa kwake Msalabani, Neno la Mungu ni lazima lienee na kurithishwa kwa watu wote Duniani na kwa vizazi vyetu vyote kwa kufanya hizi sisi nasi tutakuwa tumeipandisha mifupa ya Yusufu katika inchi ya kanaani, Musa hakuisahau mifupa, na hata Yoshua na wazee baada ya Yoshua walihakikisha Mifupa ya Yusufu inafika Shekemu inchi ya urithi wa wana Israel Efraimu na nusu ya Manase na Israel wote.  

 

Mathayo 28:18-20 “Yesu akaja kwao, akasema nao, akawaambia, Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.”               

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!      

Jumamosi, 8 Juni 2024

Who is Innocent Samuel Kamote?

 

Who is Innocent Samuel Kamote?


Rev. Innocent Samuel Kamote.


Innocent Samuel Kamote is a Tanzanian Pastor, Teacher, Author and Blogger known for his writings on Educational and Inspirational topics as well as motivational Speaker, He is also running the Blog DiraElimu@blogspot.com  where he shares various articles aimed at motivating and educating his readers.

His content includes discussion on Biblical teachings, Personal Growth, and practical advice on subjects like Defensive driving and learning techniques. Kamote’s works reflects a deep commitment to uplifting his community through thoughtful and meaning discourse.

He is well known for his nick name aka Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima, The name originated from

1Corinthians 3:10 "By the grace God has given me, I laid a foundation as an expert builder, and someone else is building on it. But each one should be careful how he builds"

So name Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima means Expert Builder or "Wise Master Mason" the intention of using this nick name is to inspire the Ministry of building the body of Christ 


Surname
: Kamote.

Given Names: Innocent Mkombozi Samuel

Birth Date: 25th June 1976. Friday

Place of Birth : Tanga, Tanzania

Tribe: Mbondei

Gender: Male

Address.   0718990796,ikamote@yahoo.com Pongwe, Tanga.

Phone Numbers. 0784394550, 0718990796

E-mail  Address.  ikamote@yahoo.com   and ikamote@gustudent.org .

Marital status. Marred to One wife 15th December 2001 Assemblies Of God City Center –Tanga

Religion: Born Again Christian:  On 15 th October 1992 Full Gospel Bible Fellowship Church

Spiritual Fathers: (Mantles)

§  Zachary Kakobe  1992 - 1996 FGBF Dar-es- Salaam

§  George Swenya   1996 – 1997 FGBF Tanga

§  Obadia Kilango   1997 – 1999 TAG Simanjiro Orkesumet

§  AGBC Dodoma  1999 -  2001 CBC.Central Bible College former AGBC.

Mantle and Models”: Bishop Zachary Kakobe - Tanzania, and Dr, Mensah Otabil from Ghana

Leadership Models: Retired District Commissioner. Samuel Jumaa Kamote.

Current Bishop: Tanzania Assemblies Of God; Dr. Barnabas Mtokambali.

Christianity teachings Foundations Assemblies Of God

Education Background:

·         January 1985- 1991 Changa Primary School/Kwalukonge Primary School – Tanga

·         Certificates of Christian religion in Anglican church for standard VII 1991

·         January 1992 – November 1992 Mbeya Artisans Technical school

·         1993 January -  1996 November Secondary School Makongo/Makongo High school Dar es Salaam

·       January 1999 – November 2001 Diploma in Bible and Church Ministry at Dodoma Tanzania Assemblies of God Bible College (AGBC).Now (CBC) Central Bible College.

·         November 2001 Certificate of Award for the outreaches Ministries at Dodoma 2001

·         January 2008 – November 2010 Bachelor of Arts in Bible and Theology (B.A.) Global University Springfield MO. USA.

·         February 8-12 /2010 Certificate of Participation on Understanding the Bible presented by Tree of Live Ministries Tanga, Christian Bible College February 2010.

·         January 2015- December 2017 Bachelor of Education Teacher Educator. teaching Philosophy and History from Open University of Tanzania (OUT)

Experiences:

·         Works as a Sunday school Teacher 1995 – 2010

·         Religion teacher for Primary and Secondary schools /youth leader 1997-1998 Simanjiro –Arusha.

·         Cell and prayer Group leader December 1996 - 1997, Full Gospel Bible Fellowship Church.

·         Part time teacher at Tanga Christian Bible College January 2003 - November 2007

·         Senior Pastor Tanzania Assemblies of God Pongwe – Tanga December 2001- September 2008

·         External Bible College Teacher – Assemblies of God - Kombezi 2003-2007

·         Licensed to cerebrate marriage from 2007 up to Now

·         Ordained Pastor from August 2004

·         AIDS & HIV. Seminar’s teacher and Youth Canceller/ speaker in CASFETA’S  Easter Conferences

·         Full time teacher teaching Staff at T.C.B.C from January 2010 – December 2012

·         Senior Pastor T.C.B.C. Church 2010 – 2012.

·         Chaplin, Bible Knowledge and Divinity Teacher at Living Stone Boys’ Seminary from January 2012- January 2023.

·         Headmaster Living Stone Boys’ Seminary from 18th Dec 2013- January 2023 with the following awards:-. 

1.    Best performing non government school 2015

2.    Best performing non government school 2016

3.    Best performing non government school 2017

4.    Best performing non government school 2018

·         Blogger of DiraElimu@blogspot.com

Traveling Experience:

 

Vision Trip to US June 2014 – visiting

·         University of Virginia, Georgetown University

·         New Post Office, Washington DC National Postal Museum

·         Library of Congress – Thomas Jefferson Building

·         Basilica of the National Shrine of the Immaculate Conception

·         Washington National Cathedral

·         Lincoln Memorial, Jewish Community Center, Naval Academy (Maryland)

·         The Kennedy Center

·         Capital, Vietnam veteran Memorial, Korean War veteran Memorial

·         Washington monument, White House,

·         New York Empire state and zero Ground

·         Tanzania House Washington

·         Open door Presbyterian Church

·         Kings Dominion, National Air Space and Museum,(NASM).

Vision Trip to Soul Korea March 2016 – visiting

·         Jomo Kenyatta International Airport

·         Southern-China airport Guangzhou China

·         Myeon - gdong. Ave

·         N Tower, Pohang Gods University

·         Yoido Full Gospel Church

·         National Museum of Korea –INCHEON

Other issues

·         Facebook writer @Innocent Kamote

·         Reached over  900,000 Readers through Blogger