Jumapili, 30 Juni 2024

Na tuvuke mpaka ng'ambo


Marko 4:35-41 “Siku ile kulipokuwa jioni, akawaambia, Na tuvuke mpaka ng'ambo. Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. Ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia? Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu.  Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado? Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?


Utangulizi:

Kaka zangu, Dada zangu:- Ni muhimu kufahamu kuwa tunapaswa kuliamini kila neno, lililotoka katika kinywa cha Mungu bila kutia shaka yoyote hata kidogo! Wakati mwingine ni ngumu kufahamu kila hali inayokutokea katika maisha yako, kwanini jambo Fulani limechelewa, kwanini ulikutana na mwisho mbaya? Kwanini mligombana na ndugu yule, kwanini mtu yule alikufanyia ubaya? Kwanini maisha ni kama yamerudi nyuma, ni kama ulikuwa mbali na ni kama umerudishwa nyuma hatua mbili, Wakati mwingine Mungu hatuchukui katika kile tunachokitamani moja kwa moja, na wakati mwingine ili kuifikia ile hatima inayokusudiwa na Mungu, basi ni lazima, upitie katika changamoto kadhaa wa kadhaa. Neno la Mungu linaonyesha ya kuwa mambo yote hutenda kazi kwa kusudi la kutimiza mapenzi yake, hata hivyo yeye anapotamka haijalishi ni hali gani inajitokeza kati kati lakini neno la Mungu litasimama vile vile bila kujali mazingira, kwani Mungu hutumia mambo yote katika kuwapatia watu wake mema!

Warumi 8:28-30 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi. Na wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza.”

Wakati mambo yanapokuwa mazuri huwa tunafurahia,  na tunaweza kukubali na kumuona Mungu ni mwema lakini mambo yanapoenda mrama tunaweza kuchanganyikiwa na tunasahau kuwa Mungu ndiye bwana mipango mkubwa, wakati mwingine anaweza kukurejesha nyuma, ili kwamba akupeleke mbele zaidi, anaweza kufunga milango na kutulazimisha kubadilika, au kubadilisha mitazamo yetu, inawezekana tulijisikia poa pale tulipokuwa, lakini Mungu hakujisikia poa, kwa sababu anakitu kikubwa zaidi kwaajili yako na yangu, ana kitu ambacho akili zetu haziwezi kuelewa, Leo tutachukua muda kuchambua kwa kina na mapana na marefu Marko 4:35-41 chini ya kichwa “Natuvuke mpaka Ng’ambo” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

1.       Nguvu ya maneno ya Yesu.

2.       Natuvuke mpaka ng’ambo!

3.       Hamna Imani bado?

 

Nguvu ya maneno ya Yesu.

Marko 4:35-39 “Siku ile kulipokuwa jioni, akawaambia, Na tuvuke mpaka ng'ambo. Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. Ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia? Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu.”

Mojawapo ya jambo la Msingi tunalopaswa kufahamu ni kukubali ya kwamba maneno ya Bwana wetu Yesu yana nguvu ya ajabu sana kuliko tunavyoweza kufikiri, Yesu katika kifungu hiki anataka tuamini katika neno lake, na kujua ya kuwa akiagiza kitu au akisema kitu ni lazima kitatimia kama kilivyo bila kujali kuwa kutatokea nini mbele ya agizo lake au neno lake, Neno la Kristo likishatamkwa limetamkwa, neno lake linauwezo wa kugeuza machafuko kuwa Amani, kwa amri nyepesi tu Nyamaza na utulie, neno lake lina mamlaka ya kiungu, inayothibitisha kuwa yeye hakuwa tu Mwalimu wa kawaida bali alikuwa na mamlaka na amri, kila mtu aliyemsikiliza Yesu alikiri kuwa maneno yake na mafundisho yake hayakuwa ya kawaida bali yalijaa uwezo, yalijaa mamlaka, na yalikuwa amri, au sheria!

Luka 4:32 “wakashangaa mno kwa mafundisho yake, kwa kuwa neno lake lilikuwa na uwezo.”

Marko 1:21-22” Wakashika njia mpaka Kapernaumu, na mara siku ya sabato akaingia katika sinagogi, akafundisha.Wakashangaa mno kwa mafundisho yake; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye amri, wala si kama waandishi.”

Maneno hayo Uwezo, na Amri katika lugha ya kiyunani linatumika neno “Exousia” ambalo kwa kiingereza linaweza kuwa na maana ya Power, Authority, Right, Liberty, Jurisdiction and strength ambalo linaweza kuelezewa kama sense of ability, force capacity,  hii inaonyesha kuwa maneno ya Yesu yalikuwa na nguvu, yalionyesha ushawishi, uweza wa kuhukumu kimahakama, nguvu ya maamuzi, nguvu ya kutenda, nguvu ya kuleta matokeo,  Nguvu ya kisheria, amri ya kijeshi, matokeo ya kiserekali, hii maana yake ni nini Yesu anapotamka jambo, ni kama hakimu anapokuwa ametamka hukumu, na kinachofuata Polisi hupiga saluti na kumchukua mtuhumiwa na kumpeleka magereza, yaani kwa lugha nyingine mamlaka yake inapotamka mara moja kinachotokea ni utekelezaji halali wa Amri halali ya neno hilo, yaani amri yake ni ya kifalme anaposema kile kilichosemwa ni amri, ni sheria, ni mamlaka halali imetamka na hivyo ni lazima kitekelezwe kile kilichotamkwa! Yesu alikuwa anataka wanafunzi wake wafikie ngazi ya kuamini ya kuwa atakachokisema kitatimia au ni lazima kitimizwe bila kujali ni mazingira gani yanajitokeza mbele ya neno lake na mfano mkubwa wa kutufundisha hilo ni amri yake kwa wanafunzi wake pale alipowaagiza kuwa Na tuvuke mpaka ng’ambo.

Na tuvuke mpaka Ng’ambo

Marko 4:35-38 “Siku ile kulipokuwa jioni, akawaambia, Na tuvuke mpaka ng'ambo. Wakauacha mkutano, wakamchukua vile vile alivyo katika chombo. Na vyombo vingine vilikuwako pamoja naye. Ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji. Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia?

Yesu alipoamuru wanafunzi wake na kuwaambia na tuvuke mpaka Ng’ambo na kisha yeye mwenyewe akapumzika na kulala, kisha dhuruba zikaanza kukipiga chombo na wanafunzi wake wakaanza kuhangaika, kulikuwa na kitu cha muhimu cha kuwafunza na kutufunza ya kwamba je tunasadiki maneno yake ?  na je tunaweza kuyasadiki maneno yake hata tukiwa katika taabu?  Yeye amesema na tuvuke mpaka ng’ambo, amri ya mfalme ni sheria tayari mazingira yote yanaratibiwa kuhakikisha ya kuwa neno lake linatimizwa, kumbuka chochote anachokuambia Yesu kitakuwa vile vile kama alivyosema na sio vinginevyo.

Marko 11:13-23 “Akaona kwa mbali mtini wenye majani, akaenda ili labda aone kitu juu yake; na alipoufikilia hakuona kitu ila majani; maana si wakati wa tini. Akajibu, akauambia, Tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako. Wanafunzi wake wakasikia. Wakafika Yerusalemu, naye akaingia ndani ya hekalu, akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wakiuza na kununua ndani ya hekalu, akazipindua meza za wabadili fedha, na viti vyao wauzao njiwa; wala hakuacha mtu achukue chombo kati ya hekalu. Akafundisha, akasema, Je! Haikuandikwa, Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote? Bali ninyi mmeifanya kuwa pango la wanyang'anyi. Wakuu wa makuhani na waandishi wakapata habari wakatafuta jinsi ya kumwangamiza; maana walimwogopa, kwa sababu mkutano wote walishangaa kwa mafundisho yake. Na kulipokuwa jioni alitoka mjini. Na asubuhi walipokuwa wakipita, waliuona ule mtini umenyauka toka shinani. Petro akakumbuka habari yake, akamwambia, Rabi, tazama, mtini ulioulaani umenyauka.  Yesu akajibu, akamwambia, Mwaminini Mungu. Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng'oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake.”

Yesu aliwahi kuuambia mtini, tangu leo hata milele mtu asile matunda kwako, na katika macho ya nyama mtini ule ulionekana ni kama bado uko vile vile, Lakini Kristo hakuwa na shaka, asubuhi yake Petro aliuona ule mtini umenyauka toka shinani, na alimkumbusha Yesu maneno yake, Yesu aliwaonyesha ya kuwa sio maneno yake tu hata na ya kwetu tukiyatamka pasipo shaka huku tukimuamini Mungu yatatuklioa vile vile.             

Yohana 11:23-26 “Yesu akamwambia, Ndugu yako atafufuka. Martha akamwambia, Najua ya kuwa atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho. Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?

Yesu aliwahi kumwambia Martha kwa habari ya kaka yake Lazaro ambaye alikuwa amekufa na kuzikwa alimwambia ndugu yako atafufuka. Martha alianza kujieleza kwa mambo mengi, najua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho na kadhalika na kadhalika, mpaka wakati huu Martha alikuwa hajajua mamlaka ya neno la Yesu, Yesu anapotamka neno ni wajibu wetu kusadiki bila kujali ya kuwa kuna mazingira gani 

Yesu akiisha kutamka neno hata kama mazingira yanaonekana kukataa, au kutokukubali au kuonyesha matumaini hiyo haisaidii kulifanya neno lake lisiwe Dhahiri, changamoto zozote zitakazojitiokeza zinasaidia kutusafirisha kutufikisha katika kulitimiza neno la Bwana, Changamoto haziko hapo kutuzuia, lakini changamoto ziko pale kutupeleka katika kiwango cha juuu zaidi  lakini je tunaweza kumuamini yeye wakati mambo yanapoonekana kwenda ndivyo sivyo? Je tunaweza kuwa na Amani wakati mambo yanapoonekana kuwa sio?  Lazima tuamini katika kile alichokizungumza kumbuka yeye alisema na tuvuke mpaka ng’ambo hii maana yake ni kuwa tutafika nga’mbo hata bila kujali ni nini kinajitokeza katikati ya maneno ya Bwana Yesu ni kwa sababu ya tukio hili Yesu aliwakemea kuwa hawajaamini Bado kwa sababu wao walipoona changamoto waliogopa na kuanza kulia na kumuona mwalimu kama mtu asiyejali dhuruba walizokuwa wakizipitia lakini kimsingi Yesu alikuwa na utulivu mkubwa sana kwa sababu aliamini katika neno lake na kuwa hakuna jambo lolote linaweza kusimama kinyume na neno lake natuvuke mpaka ng’ambo.

Hamna Imani bado?  

Marko 4:39-41 “Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Upepo ukakoma, kukawa shwari kuu. Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado? Wakaingiwa na hofu kuu, wakaambiana, Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?

Yesu anaweza kutuagiza tuelekee mahali ambapo kuna changamoto, maandiko mengine yanasema akawashurutisha na tuvuke mpaka ngambo, ni wazi kuwa pale walipokuwepo walifurahia sana Baraka za Mungu na hawakutaka kuondoka, Palitendeka miujiza mingi, hata hivyo walihitaji kupumzika, na vilevioe kuwafikiwa watu wengine, hivyo aliwalazimisha wavuke Ng’ambo kwanini  lakini ?  Mungu hawezi kutulazimisha hivi hivi tu, anaweza kukuondoa katika eneo ambalo unakula raha na akataka uelekee eneo lingine lenye Baraka zake kubwa zaidi, wakati mwingine ni ngumu kuona na kufurahia maagizo ya kiungu na kuyaamini lakini Mungu hawezi kukulazimisha uende mahali ambapo, anajua utakutana na dhuruba ambazo zitayaangamiza maisha yetu, sababu kubwa ya kukutuma kwenye dhoruba ni kwa sababu anajua utatoboa na iko njia iliyonyooka, yeye ndiye anayefanya njia, na ni yeye ndiye anayeyaongoza maisha yako na yangu  hakuna sababu ya kujitahidi kuyaokoa maisha yetu,  hakuna sababu ya kuogopa,  wala kuhofia kama ilivyokuwa kwa wanafunzi wa Yesu, yeye anajua yupo na anajua kuwa ametamka neno lake na itakuwa salama  anajua pia anauwezo wa kunyamazisha kila aina ya dhoruba inayoyakabili maisha yako, Basi unachopaswa kukifanya wewe ni kuamini katika kile ambacho Mungu amekisema, upepo uliwaleta mahali pazuri zaidi ya kule jangwani walikokuweko

Yesu anapozungumza maneno yake hayawi bure yanatimiza makusudi yake makuu na hakuna kinachoweza kuzuia neno lake katika mazingira yoyote

Mawimbi  yanapokuja yanajaribu tu uwezo wetu wa kuamini, yanapima kwamba tunamuelewa Yesu kwa kiwango gani na tunayachukulia vipi maneno yake, Yesu alikuwa akiwafundisha wanafunzi wake kuamini katika maneno yake na mamlaka kubwa aliyokuwa nayo, Changamoto ni kipimo kuwa tunamsadiki yeye kwa kiwango gani, na sio hivyo tu changamoto hizo zinamfunua Yesu pia kwa undani zaidi, wanafunzi walikuwa wanamuona Yesu ni wa kawaida tu, lakini sasa sio tu aliwakema kwa kutokuamini kwao lakini alijifunua kwao katika kiwango cha juu zaidi, yeye aliukemea upepo na bahari na kuziamuru kunyamaza na kutulia na wanafunzi waliacha kuogopa hilo na sasa walimuogopa Yesu na kujiuliza kuwa huyu ni  mtu wa namna gani hata bahari na uepo unamtii ?

Hitimisho

Yesu aliwahoji wanafunzi wake Mbona mmekuwa waoga hamna Imani bado?  Nini maana yake muitikio wetu kwa neno la Kristo unapaswa kuwa usiojawa shaka na hofu wala kujali mazingira  hatuna budi kuendelea kuamini nguvu yake mamlaka yake na neno lake, tujue ya kuwa Mungu wakati wote ni mwema na kila anakotupeleka hutupeleka kwa kusudi lake,  anaposema kitu ni lazima tutii, lakini sio hivyo Yesu alikuwepo pale, wanafunzi wake walipaswa kuamini pia katika uwepo wake  hii inatukumbusha kuwa na Amani tunapokuwa katika uwepo wa Mungu  yeye yuko kwaajili yetu, neno lake sio tu linaleta utulivu wakati wa dhuruba lakini pia linatuhakikishia Amani ya maisha yetu, hivyo wajibu wetu kwa neno lake ni kuamini, kutii na kuwa na Amani katika uwepo wake.

 

Na Rev.Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: