Jumapili, 17 Mei 2026

Kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu!


Zaburi 27:1-3. “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Neno la Mungu yaani maandiko matakatifu yanakiri kupitia mwandishi wa zaburi hii ya kuwa Bwana akiwa nuru na wokovu wetu, haijalishi kuwa maadui zetu na watesi wetu hata wawe wengi kiasi gani na hata wajipange vipi, watajikwaa na kuanguka, hii maana yake ni kuwa kumtegemea Mungu kunasababisha tuendelee kubaki wenye nguvu hata kama kuna mashambulizi makali ya adui kutoka kila kona, Zaburi hii pia inafunua Nguvu za Mungu ambazo maadui walipaswa kujiuliza kwanza katika mipango yao kuwa Mungu yuko na nani kabla ya kuanza kujipanga dhidi yetu kwa mashambulizi yoyote yale, Hakuna mtu mwenye hati miliki ya Mungu ati!

2Samuel 5:17-18 “Na hao Wafilisti waliposikia kwamba wamemtia Daudi mafuta ili awe mfalme juu ya Israeli, Wafilisti wote wakapanda kumtafuta Daudi; naye Daudi akapata habari, akashuka akaenda ngomeni. Basi Wafilisti walikuwa wamekuja na kujitawanya bondeni mwa Warefai. Basi Daudi akauliza kwa Bwana, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti? Utawatia mkononi mwangu? Naye Bwana akamwambia Daudi, Panda; kwa kuwa hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.”

Ni makosa makubwa sana kupigana vita, kupanga maovu, na kumshambulia kumsema vibaya na kumchafua, mtu ambaye hujui kama ana Mungu au hana, katika vita vya kiroho ni lazima ujue kuwa unayepigana naye ni mwenye haki au mwovu, kama unayepigana naye Mungu yuko upande wake utakufa vibaya, utasambaratika, utaporomoka, utafutika  na hautakuwepo tena kwa kosa la kipuuzi kama hilo lisilozingatia kanuni na utendaji wa Mungu! Watakatifu waliotutangulia Hasa Daudi ambaye alikuwa mtaalamu wa vita alijifunza kuwa Bwana akiwa upande wako atakusaidia, na wanaokuchukia watashindwa na kusambaratika vibaya, Historia yao itafifia na watatoweka duniani!

Zaburi 118:6-8 “Bwana yuko upande wangu, sitaogopa; Mwanadamu atanitenda nini? Bwana yuko upande wangu, msaidizi wangu, Kwa hiyo nitawaona wanaonichukia wameshindwa. Ni heri kumkimbilia Bwana Kuliko kuwatumainia wanadamu.”

Leo basi kwa uzito mkubwa tutatafakari pamoja somo hili muhimu lenye kichwa Kujikwaa kwa watesi wangu na adui zangu, ambalo linakazia ushindi wa ajabu unaowapata watu wa Mungu dhidi ya adui zao, na tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vifuatavyo:-



·         Maana ya kujikwaa kwa watesi.

·         Siri ya kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu.

·         Kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu!


Maana ya kujikwaa kwa watesi.

Zaburi 27:1-3. “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Ni muhimu kufahamu kuwa neno linalotumika katika Lugha ya Kiebrania kuelezea watesi ni “Tzoreri” au “Oyevai” ambalo kwa Kiingereza ni enemies au oppressors, au adversaries, Maadui, watesaji, watu wanaotaka kukusababishia mabaya katika maisha au wanaofurahia wewe upatwe na mabaya au wanaopanga mipango mibaya juu yako na wenye kutaka kuchafua au kuharibu kibali ulichonacho  hawa ndio wanaitwa watesi an maadui watu ambao hawakufurahii na wanakupinga hawataki mafanikio yako au wanaogopa wewe kufanikiwa hawa Bwana ameahidi katika neno lake kuwa wanapodhamiria kukufanyia mambo yao au hata kama watafanya mambo yao hatimae watajikwaa

Kujikwaa hasa ni nini? Neno linalotumika kuelezea kujikwaa katika lugha ya Kiebrania ni “Kāshal” ambalo maana yake ni kudhoofishwa, kupoteza nguvu, kurudishwa nyuma, kushindwa kusimama, kukutana na kizuizi, kukutana na kikwazo, kukosa uwiano, kuzimia chini ya shinikizo, kuanguka kwa namna isiyotegemewa kwa kiingereza “stumble” au “Fall” kwa hiyo mtu awaye yote anayepambana na watu wa Mungu au mtu wa Mungu anaweza akaanguka na asiinuke tena, huku sio tu kujikwaa kimwili, lakini ni kuanguka kwa mfumo mzima wa adui, kusambaratika kwa mipango, na mifumo ya utendaji wa maadui kupitia nguvu na msaada wa Mungu kwa mtumishi wake.

Zaburi 18:36-40 “Umezifanyizia nafasi hatua zangu, Na miguu yangu haikuteleza. Nitawafuatia adui zangu na kuwapata, Wala sitarudi nyuma hata wakomeshwe. Nitawapiga-piga wasiweze kusimama, Wataanguka chini ya miguu yangu. Nawe hunifunga mshipi wa nguvu kwa vita, Hunitiishia chini yangu walioniondokea. Naam, adui zangu umewafanya wanipe visogo, Nao walionichukia nimewakatilia mbali.”

Siri ya kujikwaa kwa watesi wetu na adui zetu

Neno la Mungu linafunua siri kubwa ni kwa nini maadui hawakufanikiwa, kwanza maadui hawa walikuwa na chuki kubwa na ya kiwango cha juu, walikuwa wamekusudia kuharibu kabisa au kufutilia mbali hawa hawakuwa maadui wa kawaida bali watu waliodhamiria mabaya na katika kudhamiria kwao mabaya walikuwa kama watu wanaokaribia kula nyama kwa uchu hii ni lugha ya kuonyesha tamaa mbaya ya kusababisha uharibifu mkubwa kwa mtu au watu wa Mungu. Walikuwa ni watesi waliokusudia mabaya lakini walijikwaa, Mipango yao iliharibika, uharibifufu uliwapata kwa ghafla, hofu iliwaingia, akili zao zilipigwa na wakachanganyikiwa, maamuzi yao yaligeuzwa kuwa makosa, roho zao ziliingia hatiani, dhamiri zao ziliwasuta, ushindi wako mtu wa Mungu utageuka kuwa ushuhuda kwao, Mwandishi anaeleza kuwa yeye Bwana ni Nuru yake na wokovu wake, haogopi

Zaburi 27:1-3 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini.”

Mungu anapokuwa upande wako hakuna anayeweza kusimama kinyume na wewe, adui awaye yote anapokukaribia anakutana na nguvu za Mungu zisizokuwa za kawaida na bila kujielewa wanaanza kupoteza mwelekeo, Mungu hakuwahi kuacha watu wake waonewe, kila anayejipanga kupigana na mtu wa Mungu atashughulikiwa mpaka wajue ya kuwa wewe una Mungu, kama walidhani wao ndio wana Mungu basi Mungu ataonyesha ni kina nani aliwachagua kwaajili ya utukufu wake, adui watapata somo kali ambalo watasimuliana kizazi na kizazi wataelewa ya kuwa kushindana na Mungu ni kujitafutia kifo, ni kupoteza umaarufu, ni kuangamia na kupotea, ni kujifuta katika ramani ya dunia

Zaburi 103:14-15 “Hakumwacha mtu awaonee, Hata wafalme aliwakemea kwa ajili yao. Akisema, Msiwaguse masihi wangu, Wala msiwadhuru nabii zangu.”

Isaya 54:14-17 “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia. Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako.Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”

1Samuel 2:9-10 “Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake.”                           

Kujikwaa kwa watesi wangu na adui zangu!

Maandiko yanatuthibitishia ya kwamba kila mtu anayekukusudia mabaya juu yako au anayekukaribia kwa nia ovu Mungu atampa kupoteza mwelekeo, wanaopanga mabaya dhidi yako watakosea hatua zao, wanaotaka kukuangusha au kukupoteza wao ndio watakaopotea, hii ni sheria ya kiroho kama Mungu yuko upande wako, adui anapokuja na kukushambulia au kukukaribia ataharibiwa na uwepo wa Mungu, hili sio tukio la bahati mbaya ni tukio la uhakika, wewe na mimi tutamshukuru Mungu kwaajili ya matendo yake makuu atakayotutendea na anayoendela kuyafanya akihukumu kwa haki dhidi ya wale wanaotuchukia, na kujipanga kinyume nasi wao na kila anachojivunia itakuwa historia  

Zaburi 9:1-4 “Nitamshukuru Bwana kwa moyo wangu wote; Nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu;Nitafurahi na kukushangilia Wewe; Nitaliimbia jina lako, Wewe Uliye juu. Kwa sababu adui zangu hurudi nyuma; Hujikwaa na kuangamia mbele zako. Kwa maana umenifanyia hukumu na haki Umeketi kitini pa enzi ukihukumu kwa haki.”

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima


Hakuna maoni: