Jumapili, 31 Mei 2026

Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti!


Waefeso 3:14-17 “Kwa hiyo NAMPIGIA BABA MAGOTI, ambaye kwa jina lake ubaba wote wa mbinguni na wa duniani unaitwa, awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake katika utu wa ndani. Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo;”



Utangulizi:

Wote tunafahamu kuwa maombi ni moja ya njia ya muhimu inayotumiwa na watu wengi sana katika kuunganisha ulimwengu wa roho na mwanadamu, tunaweza kusema kuwa maombi ndio pumzi ya uhai wa kila anayeamini, maombi yana nguvu, maombi yanaweza kuombwa kwa staili, mikao na mitindo mbalimbali inayotajwa pia katika maandiko, kwa mfano kufumba macho, au kufumbua, kusimama au kukaa, kuinua mikono au kukunja, kulala kifudifudi, au kuketi kimya, kuomba kwa sauti au kimya, laniki pia kuna kuomba kwa kupiga magoti, hata hivyo pamoja na kuwa mwanadamu anaweza kumuomba Mungu kwa mitindo mbalimbali leo nataka kuzungumzia swala la kuomba kwa kupiga magoti, watu wengi wanataka kuomba maombi yenye matokeo, yenye nguvu, lakini hawajui njia, Neno la Mungu linazungumzia maombi ya kupiga magoti kwa njia na namna ya kipekee sana kuna nguvu ya ziada wakati mwanadamu anapomuomba Mungu au kumuabudu Mungu huku akiwa amepiga magoti.

Luka 22:39-43 “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, AKAPIGA MAGOTI AKAOMBA, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.”

Kumbe kuna matokeo katika maombi ya kupiga magoti,Kwa msingi huo basi leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu somo hili Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maana ya kupiga magoti kimaandiko.

·         Mifano ya watu walioomba kwa kupiga magoti.

·         Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti.

Maana ya kupiga magoti kimaandiko.

Neno kupiga magoti katika lugha ya Kiebrania linatumika kama neno “Barak” na kwa Kiyunani  linatumika neno “Gonypeteo” Neno “Barak” la Kiebrania maana yake ni Kupiga magoti, au kuonyesha unyenyekevu, kuonyesha heshima au kujishusha mbele ya mtu unayemuheshimu, mtu mkubwa au Mungu, kwa hiyo kwa ujumla wake kupiga magoti maana yake ni tendo la kuonyesha unyenyekevu mbele za Mungu, kutambua ukuu wake  na kukubali kuwa wewe na mimi tunamtegemea Mungu, kwa hiyo kupiga magoti ni tendo linalotakiwa kuanzia moyoni na kujitokeza kwa nje katika jinsi ya mwili, Neno la Mungu linatoa  wito wa kumuabudu  kwa kumsujudia na kwa kumpigia magoti Mungu wetu, Kumbuka imeandikwa utamwabudu na kumsujudia Bwana Mungu wake peke yake!

Zaburi 95:6-7 “Njoni, tuabudu, tusujudu, TUPIGE MAGOTI MBELE ZA BWANA aliyetuumba. Kwa maana ndiye Mungu wetu, Na sisi tu watu wa malisho yake, Na kondoo za mkono wake. Ingekuwa heri leo msikie sauti yake!

Kupiga magoti au goti katika Lugha ya Kiyunani linatumika neno “Gonypeteo” ambalo ni muunganiko wa maneno mawili ya kiyunani yaani “Gonu” na “Pipto”.  “Gonu” ikiwa na maana ya Goti na “Pipto” ikiwa na maana ya anguka au kuanguka kwa kiingereza “fall on Knee” au “Kneel down” au “Bow the knee” Hili ni tendo la kuonyesha, unyenyekevu na utii, au kukubali kuwa chini ya maelekezo ya Mungu, ni njia inayotumika katika maombi hususani nyakati za agano jipya kuonyesha heshima kwa Yesu Kristo, lakini ni ishara ya kuonyesha kuwa una hitaji la muhimu na zito na linalohitaji msaada wa haraka au kupewa kipaumbele cha aina yake.

Mathayo 17:14-18 “Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, AKAMPIGIA MAGOTI, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile.”

Kupiga magoti ni heshima kubwa na ni tendo la nje linalotoka moyoni lenye kuonyesha kuwa unakubali kunyenyekea kwa mwenye mamlaka, Maandiko yanaonyesha na kutabiri kuwa kwa Yesu Kristo kutokana na mamlaka kubwa sana aliyopewa kila goti la vitu vyote iwe ni mbinguni au duniani litapigwa kwake kwa sababu ya heshima kubwa aliyotunukiwa na Mungu Baba yake ona:-

Wafilipi 2:9-11 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ILI KWA JINA LA YESU KILA GOTI LIPIGWE, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.”

Mifano ya watu walioomba kwa kupiga magoti.

Neno la Mungu limejaa mifano kadhaa ya watu kadhaa wa kadha ambao waliomba kwa kupiga magoti na kupata matokeo makubwa sana katika maombi yao, kimsingi kabla ya kuangalia nguvu ya maombi ya kupiga magoti au umuhimu wa maombi ya kupiga magoti eneo hili linatuonyesha moja kwa moja matokeo nguvu na umuhimu wa kupiga magoti wakati wa kuomba.

1.       Yesu Kristo -  Alipokuwa katika wakati mgumu sana kibinamu wa kukabiliwa na mauti ya msalaba  na mateso yaliyojaa dhihaka na kuvunjiwa heshima kwa kuwa alitambua ni mauti ya aina gani na mateso ya aina gani yalikuwa yanamkabili, moyo wake na hisia zake zilijawa na maumivu makali ya kupita kawaida, alikuwa na wakati mgumu alikuwa na wakati wa vita kali ya kiroho, wakati huu alitumia maombi ya kupiga magoti na mbingu zilimtia nguvu kwani alitumiwa malaika kutoka mbinguni mara moja ili kumtia nguvu ona!

 

Luka 22:39-43. “Akatoka akaenda mpaka mlima wa Mizeituni kama ilivyokuwa desturi yake; wanafunzi wake nao wakafuatana naye. Alipofika mahali pale aliwaambia, Ombeni kwamba msiingie majaribuni. Mwenyewe akajitenga nao kama kiasi cha kutupa jiwe, AKAPIGA MAGOTI AKAOMBA, akisema, Ee Baba, ikiwa ni mapenzi yako, uniondolee kikombe hiki; walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke. Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia nguvu.”

 

Ukichunguza kwa kina tukio hili utagundua ya kuwa maombi ya kupiga magoti yanafaa sana wakati mwanadamu akiwa katika shinikizo zito na hali ngumu kihisia na mambo ya kutisha yanapokukabili au unapokuwa na vita kubwa, wakati huo utahitaji kujinyenyekeza zaidi kwa kupiga magoti lakini pia unaweza kuona matokeo ya kupiga magoti kwani Malaika wa Bwana kutoka mbinguni alimtokea na kumtia nguvu.

 

2.       Daniel – Kulikuwa na mswada mkali wa kiserikali uliopitishwa kukataza watu kuomba kwa mungu yoyote kwa muda wa mwezi mmoja na mtu ambaye angekiuka swala hilo angetupwa katika tundu la simba wakali wenye njaa, tunamuona Daniel hakubadilisha kabisa mfumo wa maisha yake ya maombi  na hata katika wakati huu wa sheria kali kiasi hicho la tishio la maisha na kifo kwa simba wakali aliendelea kuomba kwa kupiga magoti mara tatu kila siku akiwa mwaminifu kwa Mungu wake na matokeo yanaonekana simba hawakumuweza, Mungu aliwatuma malaika wake wakayafunga makanwa ya simba na hawakumdhuru.

 

Daniel 6:6-11 “Basi wale mawaziri na maamiri wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia hivi, Mfalme Dario, uishi milele.  Mawaziri wote wa ufalme, na manaibu, na maamiri, na madiwani, na maliwali wamefanya shauri pamoja ili kuweka amri ya kifalme; na kupiga marufuku, ya kwamba mtu ye yote atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme atatupwa katika tundu la simba. Sasa, Ee mfalme, piga marufuku, ukatie sahihi maandiko haya, yasibadilike, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi, isiyoweza kubadilika. Basi mfalme Dario akayatia sahihi maandiko yale, na ile marufuku. Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu;) AKAPIGA MAGOTI MARA TATU KILA SIKU, AKASALI, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake.”

 

Daniel 6:19-24 “Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. MUNGU WANGU AMEMTUMA MALAIKA WAKE, NAYE AMEYAFUMBA MAKANWA YA SIMBA, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu.”

 

3.       Petro – Mwanafunzi mmoja aliyekuwa mwema sana nyakati za Kanisa la kwanza huko Yafa kwa matendo yake mazuri kwa wajane na yatima aliyeitwa Thabita au Dorkas aliugua na kufa na walipokuwa wamemuosha walimuweka katika chumba na kumuita Petro, Petro alipokuja moja ya njia aliyoitumia kumuombea marehemu ilikuwa ni kwa maombi ya kupiga magoti na kwa kweli kwa kutumuia maombi hayo yaliyojaa unyenyekevu mkubwa maiti (Drkas aliyekuwa amekufa)alifufuka

 

Matendo 9:36-42 “Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha, tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa. Ikawa siku zile akaugua, akafa; hata walipokwisha kumwosha, wakamweka orofani. Na kwa kuwa mji wa Lida ulikuwa karibu na Yafa, nao wanafunzi wamesikia ya kwamba Petro yuko huko, wakatuma watu wawili kwake, kumsihi na kusema, Usikawie kuja kwetu.  Petro akaondoka akafuatana nao. Alipofika, wakampeleka juu orofani wajane wote wakasimama karibu naye, wakilia na kumwonyesha zile kanzu na nguo alizozishona Dorkasi wakati ule alipokuwa pamoja nao. Petro akawatoa nje wote, AKAPIGA MAGOTI, AKAOMBA, kisha akaelekea yule maiti, akanena, Tabitha, ondoka. Naye akafumbua macho yake, na alipomwona Petro akajiinua, akaketi. Akampa mkono, akamwinua; hata akiisha kuwaita wale watakatifu na wajane akamweka mbele yao, hali yu hai. Ikajulikana katika mji mzima wa Yafa; watu wengi wakamwamini Bwana.”

 

Ni kama tunajifunza hapo kuwa maombi ya kupiga magoti yanaweza kusababisha muujiza mkubwa sana na kuleta nguvu ya ajabu kwani sio tu mtu alifufuka lakini wengi pia waliosikia habari za tukio hilo katika mji huo na vitongoji vyake walimuamini Bwana kupitia muujiza ule, Unyenyekevu mkubwa kwa Mungu kwa njia ya kupiga magoti unaweza kufungua udhihirisho mkubwa sana wa nguvu za Mungu.

 

4.       Suleimani – alikuwa ni mfalme mwenye utukufu mkubwa na wa hali ya juu lakini hakuacha kuonyesha unyenyekevu kwa Mungu wake siku ya kuweka wakfu Hekalu alipiga magoti na kuomba maombi maalumu sana mbele ya watu wote bila kujali heshima yake na cheo chake jambo lililopeleka siku ile moto wa Mungu ukashuka na kuteketeza sadaka ya kutekeketezwa na utukufu wa Mungu ukashuka katika nyumba ya Mungu siku ile ilipokuwa inawekwa wakfu jambo lililosababisha makuhani kushindwa kutekeleza majukumu yao

 

2Nyakati 6:13-17. “(maana Sulemani alikuwa amefanya mimbari ya shaba, urefu wake mikono mitano, na upana wake mikono mitano, na kwenda juu kwake mikono mitatu, na kuisimamisha katikati ya ua; akasimama juu yake, AKAPIGA MAGOTI MBELE YA MKUTANO WOTE WA ISRAELI, AKAIKUNJUA MIKONO YAKE KUELEKEA MBINGUNI); akasema, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe, mbinguni, wala duniani; ushikaye maagano na rehema kwa watumishi wako, waendao mbele zako kwa moyo wao wote; uliyemtimizia mtumishi wako Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidi; naam, ulinena kwa kinywa chako, ukayatimiza kwa mkono wako, kama ilivyo leo. Sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, umfikilizie mtumishi wako Daudi, baba yangu, ahadi uliyomwahidia, ukisema, Hutakosa kuwa na mtu machoni pangu, wa kuketi katika kiti cha enzi cha Israeli; wakiwa tu watoto wako wataiangalia njia yao, ili kuiendea torati yangu, kama wewe ulivyokwenda mbele zangu.Basi sasa, Ee Bwana, Mungu wa Israeli, ulithibitishe neno lako, ulilomwambia mtumishi wako Daudi.”

 

2Nyakati 7:1-4. “Basi Sulemani alipokwisha maombi hayo, moto ukashuka kutoka mbinguni, ukateketeza sadaka ya kuteketezwa na dhabihu; utukufu wa Bwana ukaijaza nyumba. Wala makuhani hawakuweza kuingia nyumbani mwa Bwana, kwa kuwa utukufu wa Bwana umeijaza nyumba ya Bwana. Wakatazama wana wa Israeli wote, uliposhuka ule moto, utukufu wa Bwana ulipokuwapo juu ya nyumba; wakasujudu kifulifuli hata nchi sakafuni, wakaabudu, wakamshukuru Bwana, wakisema, Kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili zake ni za milele. Ndipo mfalme na watu wote wakatoa dhabihu mbele za Bwana.”

 

Ni kama tunajifunza hapo kuwa kumbe maombi ya unyenyekevu ya kumpigia Mungu magoti yanaweza kusababisha Mungu kushuka kwa utukufu na uwepo wake katika namna ambayo ni ya kipekee na ni nani asiyependa kuuona utukufu wa Bwana? Mungu alishuka na Mungu anaweza kushuka kwa kumpigia magoti

 

Stephano – Alikuwa anazingirwa na maadui na walikuwa wamekusudia kumuua baada ya kushindwa kwa hoja kutokana na ukinzani wa kidini, walimkasirikia sana Stephano, walimsagia meno na wakiwa wamekusudia kutaka kumuua na akiwa katika mateso na kukabiliwa na hali ya kifo alipiga magoti, aliwasamehe adui zake alimuona Yesu amesiamama tayari kumpokea na walipomkazia macho waliona uso wake ni kama wa malaika haya yanamtokea mtu huyu wa Mungu wa kipekee akiwa amepiga magoti na kumuomba Mungu

 

Matendo 6:8-15 “Na Stefano, akijaa neema na uwezo, alikuwa akifanya maajabu na ishara kubwa katika watu. Lakini baadhi ya watu wa sinagogi lililoitwa sinagogi la Mahuru, na la Wakirene, na la Waiskanderia, na la wale wa Kilikia na Asia, wakaondoka na kujadiliana na Stefano; lakini hawakuweza kushindana na hiyo hekima na huyo Roho aliyesema naye. Hata wakashawishi watu waliosema, Tumemsikia mtu huyu akinena maneno ya kumtukana Musa na Mungu. Wakawataharakisha watu na wazee na waandishi, wakamwendea, wakamkamata, wakampeleka mbele ya baraza. Wakasimamisha mashahidi wa uongo waliosema, Mtu huyu haachi kusema maneno ya kufuru juu ya mahali hapa patakatifu na juu ya torati; maana tumemsikia akisema kwamba Yesu huyo Mnazareti atapaharibu mahali hapa, na kuzibadili desturi tulizopewa na Musa. Watu wote walioketi katika ile baraza wakamkazia macho yao, wakamwona uso wake kuwa kama uso wa malaika.”

 

Matendo 7:57-60 “Wakapiga kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja, wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli. Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu. AKAPIGA MAGOTI, AKALIA KWA SAUTI KUU, BWANA, USIWAHESABIE DHAMBI HII. Akiisha kusema haya akalala. Na Sauli alikuwa akiona vema kwa kuuawa kwake.”

 

Paulo – Akiwa katika mafundisho na mkazo wa kiroho kwa wazee na washirika wa kanisa la Efeso wakati anakamilisha huduma yake huko hatimaye Paulo na wote waliokuwa wakimsindikiza walipiga magoti na kumuomba Mungu Neema kwa pamoja

 

Matendo 20:31-38 “Kwa hiyo kesheni, mkikumbuka ya kwamba miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mtu kwa machozi. Basi, sasa nawaweka katika mikono ya Mungu, na kwa neno la neema yake, ambalo laweza kuwajenga na kuwapa urithi pamoja nao wote waliotakaswa. Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu. Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami. Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea. ALIPOKWISHA KUNENA HAYA AKAPIGA MAGOTI, AKAOMBA PAMOJA NAO WOTE. Wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu, wakihuzunika zaidi kwa sababu ya neno lile alilosema, ya kwamba hawatamwona uso tena. Wakamsindikiza hata merikebuni.”

 

Tunajifunza hapa kuwa kupiga magoti pia inaweza kuwa ni hali ya kawaida ya maisha ya kila siku ya kumuomba Mungu kwa wakristo na viongozi wa kanisa, sio tu wakati wa changamoto lakini kwaajili ya kijiumbia tabia ya unyenyekevu tunaweza kuitumia njia hii kila wakati na Mungu akajali na kusikiliza dua zetu.

Yakobo Ndugu yake Bwana – Kwa mujibu wa masimulizi ya tamaduni za nyakati za kanisa la Kwanza inaelezewa kuwa Yakobo Ndugu yake Bwana alikuwa ni moja ya watu waliokuwa waombaji hodari sana kwa kupiga magoti, kiasi ambacho alipewa jina la Mtu mwenye magoti ya ngamia,  kwa mujibu wa maelezo ya mwanahistoria wa kanisa wa karne ya pili aliyeitwa Eusebius alinukuu maelezo ya Hegesippus yakieleza kuwa Yakobo ndugu yake Yesu alikuwa na tabia ya kupiga magoti hekaluni na kuomba kwa muda mrefu kiasi ambacho magoti yake yalishika sugu kama magoti ya ngamia, aliheshimiwa sana kwa sababu alisikika akiwaombea watu na kutubia dhambi zao, kwa kupiga magoti pembezoni mwa hekalu hii ilikuwa ni desturi yake ya maisha mpaka alipouawa kwa kupigwa mawe ambapo pia alipiga magoti na kuomba Baba uwasamehe, tunajifunza kwake kuwa kanisa pamoja na maombi mengine wakati mwingine ni vema kuwa na muda wa unyenyekevu na kukaa magotini kwa muda wa kutosha ili tuweze kupata rehema kwa Mungu wetu

Nguvu ya kuomba kwa kupiga magoti.

Kupiga magoti kama kutaanza kutokea ndani yaani moyoni ni moja ya silaha yenye nguvu sana katika maombi, sisemi kwamba kila anayepiga magoti maombi yake yanaweza kujibiwa, wala sisemi kuwa maombi ya kupiga magoti ni muhimu kuliko ya iana nyingine  lakini  nasema kile maandiko yamekionyesha swala Muhimu hapa ni kuvunjika moyo, ni kunyenyekea, ni kupondeka mbele za Mungu ishara yake ya nje ndio kupiga magoti, Kuna nguvu ya kusikilizwa na Mungu mtu anapokwenda mbele za Mungu au wakili wa Mungu kwa kuvunjika au kwa unyenyekevu ni  kama kunahusisha toba, unyenyekevu ibada na kuvunjiia vunjika mbele za Mungu, ni tendo ambalo likifanyika kuanzia moyoni linakupatia kibali na linaongezea neema hii ni kwa sababu Mungu huangalia moyo, kwa kupiga magoti kutoka moyoni unajitengenezea kibali kwa Mungu na kumfanya Mungu akuhurumie kwa haraka hitaji lako:-

2Wafalme 1:9-14 “Ndipo mfalme akatuma akida wa askari hamsini pamoja na hamsini wake, wamwendee Eliya. Akamwendea, na tazama, ameketi juu ya kilima. Akamwambia, Ewe mtu wa Mungu, mfalme asema, Shuka. Eliya akajibu, akamwambia yule akida wa hamsini, Ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, na ushuke moto kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na hamsini wako. Moto ukashuka, ukamteketeza, yeye na hamsini wake. Akatuma tena akida wa hamsini mwingine pamoja na hamsini wake, wamwendee. Akajibu, akamwambia, Ewe mtu wa Mungu, mfalme asema, Shuka upesi. Eliya akajibu, akamwambia, Ikiwa mimi ni mtu wa Mungu, na ushuke moto kutoka mbinguni, ukuteketeze wewe na hamsini wako. Moto wa Mungu ukashuka kutoka mbinguni, ukamteketeza, yeye na hamsini wake. Tena akatuma akida wa hamsini wa tatu, pamoja na hamsini wake. Yule akida wa hamsini wa tatu akapanda, AKAENDA AKAPIGA MAGOTI mbele ya Eliya, akamsihi sana, akamwambia, Ee mtu wa Mungu, nakusihi, roho yangu, na roho za watumishi wako hawa hamsini, ziwe na thamani machoni pako. Tazama, moto ulishuka kutoka mbinguni, ukawateketeza wale akida wa hamsini wawili wa kwanza pamoja na hamsini wao; laiti sasa roho yangu na iwe na thamani machoni pako. Malaika wa Bwana akamwambia Eliya, Shuka pamoja naye; usimwogope. Akaondoka, akashuka pamoja naye hata kwa mfalme.”

Akida hawa wa askari wa kikosi chenye askari 50 wa kwanza na wa pili  waliuawa kwa sababu ya tabia na mwenendo wao wa kutokujali mamlaka ya kiungu, walimuamuru Nabii ashuke na kumtii mfalme lakini nabii alikuwa anawakilisha mamlaka ya Mungu, na Mungu aliangalia kutoka moyoni  na kuwaona maakida hao kuwa kwa maneno na vitendo walikuwa hawana adabu,  wala moyo wa unyenyekevu, moyo wa akida wa 3 wa kikosi cha 50 mwengine yeye alikuwa na unyenyekevu wa hali ya juu sana na kwa sababu hiyo alipata neema kwa hiyo tabia ya kiburi kutoka moyoni inaweza kusababisha dua yako au yangu isisikilizwe na tabia ya unyenyekevu na kuvunjika kutoka moyoni huvutia neema ya Mungu, kwa hiyo kupiga magoti ni lazima kuwe kumetoka moyoni mtu anaweza kupiga magoti kwa nje lakini kwa nia na lengo la kudhihaki kama askari waliomsulubisha Yesu walivyomfanyia, walipiga magoti kwa dhihaka na sio kwaajili ya kunyenyekea bali kudhalilisha, hii ilikuwa ni jeuri ya wazi ya mwanadamu dhidi ya mwana wa Mungu ambaye kila goti litapigwa kwake

Mathayo 27:27-31 “Ndipo askari wa liwali wakamchukua Yesu ndani ya Praitorio, wakamkusanyikia kikosi kizima.Wakamvua nguo, wakamvika vazi jekundu. Wakasokota taji ya miiba, wakaiweka juu ya kichwa chake, na mwanzi katika mkono wake wa kuume; WAKAPIGA MAGOTI MBELE YAKE, WAKAMDHIHAKI, wakisema, Salamu, Mfalme wa Wayahudi! Kisha wakamtemea mate, wakautwaa ule mwanzi, wakampiga-piga kichwani. Walipokwisha kumdhihaki, wakalivua lile vazi, wakamvika mavazi yake, wakamchukua kumsulibisha.”

Mtu mwenye ukoma aliyechoshwa na hali ya kukaa na ukoma alimjia Yesu na kumpigia magoti akihitaji rehema za Mungu na kwa huruma kubwa sana, Yesu alimkubalia ombi lake kwa huruma na akatakakaswa ukoma kwa mamlaka

Marko 1:40-42 “Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa. Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika.”

Uko umuhimu wa kumuendea Mungu kwa heshima na unyenyekevu mkubwa, sisi hatuwezi lolote kwake yeye ni Muumba na sisis ni viumbe, kuokolewa kwetu kusitufanye sisi kujifikiri kuwa ni wa Muhimu sana na hata kama tutajifikiri kuwa ni wa Muhimu kwa Mungu wetu bado inatupasa kutambua kuwa yeye ni Bwana wa Mabwana na kuwa tukimuheshimu naye atatuheshimu, kupiga magoti ni ishara ya heshima kwa Mungu wetu naye anastahili, wote waliokwenda Mbele zake kwa unyenyekevu Mungu hakuwahi kuwaangusha na hii ndio nguvu ya kumuendea tukiwa tumepiga magoti mbele zake  kama ishara kutoka moyoni kuwa tunavunjika mbele zake, tu wanyonge mbele zake hebu kuanzia sasa jaribu kujifunza namna na jinsi tunavyopaswa kukaa magotini kwake

1Samuel 2:30 “Kwa sababu hiyo, Bwana, Mungu wa Israeli, asema, Ni kweli, nalisema ya kuwa nyumba yako, na nyumba ya baba yako itakwenda mbele zangu milele; lakini sasa Bwana asema, Jambo hili na liwe mbali nami; kwa maana wao wanaoniheshimu nitawaheshimu, na wao wanaonidharau watahesabiwa kuwa si kitu.”

Isaya 66:2 “Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema Bwana; lakini mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge, mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima 

Hakuna maoni: