Yohana 5:5-8 “Na hapa palikuwa na mtu,
ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya
kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu
wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu
mwingine hushuka mbele yangu. Yesu
akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende.”
Utangulizi:
Ni muhimu kufahamu kuwa wakati
mwingine hapa duniani mtu anaweza kukwama katika mambo fulani fulani tu
kwasababu ya kukosa mtu wa kukusaidia, inawezekana unahitaji matibabu ya tatizo
fulani la kiafya na linahitaji fedha nyingi lakini ukakosa mtu, au unatafuta
kazi mahali fulani na umehangaika kwa muda mrefu lakini ukaikosa kwa sababu tu
huna mtu, wako watu wengi sana wamekwama katika maisha na huduma na mambo
mbalimbali kwa sababu tu hawana mtu, usipokuwa na mtu hapa duniani wa
kukusaidia wakati mwingine unaweza kujikuta umekwama tu unaweza hata kupitia
katika mateso na kuwekewa zengwe kwa sababu huna mtu anayekufahamu.
Kutoka 2:8-10 “Basi akainuka mfalme mpya
kutawala Misri, asiyemjua Yusufu. Akawaambia watu wake, Angalieni, watu wa wana
wa Israeli ni wengi tena wana nguvu kuliko sisi. Haya! Na tuwatendee kwa akili,
wasije wakaongezeka; tena, ikitokea vita, wao nao wasije wakashikamana na adui
zetu na kupigana nasi, na kutoka katika nchi hii.”
Wana wa Israel waliteseka sana
kule Misri na kugeuzwa kuwa watumwa kwa mateso mazito kwa sababu hakukuwa na
mtu aliyewatambua, au asiyetambua mchango wa Yusufu huko nyuma, unapokosa mtu
anayekufahamu, anayekujua anayeweza kuwa msaada katika dunia hii ya sasa
unaweza kuteseka sana. Katika maandiko ya msingi tunasoma habari za mtu mmoja
ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja, lakini mtu huyu alikuwa
amepooza na alikuwa akitarajia kupokea uponyaji kutoka katika kisima kiitwacho Bethzatha mtu huyu amekuwa katika hali
hii ya mateso kwa miaka 38 na kwa sababu ya jambo hili alipoteza kila kitu
huenda aliishi kwa msaada wa wasamaria wema waliompa chakula lakini haja ya
moyo wake haikuweza kutimizwa kwa sababu ilihitaji mtu, na hakukuwa na mtu wa
kumjali kwa sababu watu walikuwa na watu wao, unaweza kuteseka kwa miaka mingi
sana kwa sababu tu hauna mtu, kuna watu wengi sana wamekwama kwa sababu hawana
mtu, jamii haikuoni, marafiki hawahusiki na wewe ndugu hawahusiki na wewe uko
peke yako na hakuna wa kukutoa kwa sababu huna mtu!
·
Katika
Birika la Bethzatha
·
Mimi sina
mtu wa kunitia birikani!
·
Kukosa
mtu sio kikwazo kwa Yesu
Katika Birika la Bethzatha
Yohana 5:2-9 “Na huko Yerusalemu penye
mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao
matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu,
viwete, nao waliopooza, [wakingoja maji yachemke. Kwa maana kuna wakati ambapo
malaika hushuka, akaingia katika ile birika, akayatibua maji. Basi yeye
aliyeingia wa kwanza baada ya maji kutibuliwa, akapona ugonjwa wote uliokuwa
umempata.] Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka
thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa
hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu,
Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati
ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu. Yesu akamwambia, Simama,
jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima, akajitwika godoro lake,
akaenda. Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo.”
Katika kisa hiki tunajifunza
habari za mtu mmoja aliyekuwa amepooza na kuteseka katika mateso hayo kwa muda
wa miaka 38 huku mtu huyu akihitaji
uponyaji kabla ya kukutana na Yesu, Neno la Mungu linatueleza kuwa kutokana na
haja ya moyo wake kuhitaji uponyaji alipelekwa mahali sahihi kabisa ambapo
angeweza kupata uponyaji wake mahali hapo ni katika Birika la Bethzatha, Kimsingi mahali hapo
palikuwa ndio mahali sahihi pa kupokea muujiza wake lakini hata hivyo hali yake
ilizidi kuwa mbaya na aliendelea kudhoofika siku hadi siku, kimsingi angefia
mahali ambapo alitakiwa kupokea uponyaji wake na kinyume chake zaidi aliendelea
kusota hapo bila ya msaada kwa nini?
“Bethzatha” lilikuwa ni jina
la Kiyunani la kisima maalumu cha uponyaji ambacho kwa lugha ya Kiebrania na
Kiaramu kiliitwa “Bethesda” kimsingi
jina hili ni muunganiko wa maneno mawili ya kiebrania Beth na Chesed au Hesed neno Beth ni nyumba House na neno Chesed/Hesed
ni Rehema Mercy kwa hiyo yanapounganishwa pamoja maneno hayo unapata neno Bethesda
ambalo maana yake ni nyumba
ya rehema (House of Mercy) hapa
palikuwa ni mahali pa ajabu sana kwani kisima hiki kilikuwa jijini Yerusalem
katika mlango uitwao Lango la kondoo, kisima hiki kilikuwa na matawi matano
ambapo maji ya mvua yalikingwa na kupelekwa katika visima vikubwa viwili hapo
kulikuwa na wakati kila siku Malaika wa Bwana alishuka na kuyatibua yale maji
na mtu anayekuwa wa kwanza kuingia kwa kuwahi huyu alipokea uponyaji, kwa
sababu hiyo wagonjwa wengi sana hususani vipofu, viwete na waliopooza
walikusanyika hapo na palikuwa na mashindano makali ya yule atakayefanikiwa
kuingia kwanza maji yanapotibuliwa alipona, jambo hili lilipelekea wengine hasa
wale waliokuwa dhaifu kusubiria hapo kwa miaka mingi, na kama ulikuwa na mtu
basi mtu huyo angelikusaidia kuingia kisimani kwa haraka kabla yaw engine na
ungepokea uponyaji na kuondoka zako, sasa hapa alikuweko mtu ambaye amesota kwa
miaka 38 na hana mtu wa kumsaidia, kimsingi tunapona kuwa mtu huyu alikuwa
mahali sahihi ambapo angepokea uponyaji na angeweza kuhurumiwa lakini kinyume
chake mambo hayakuwa hivyo badala ya kupata uponyaji na rehema aliendelea
kuteseka, aliendelea kusubiri mtu, mahali hapa pakawa mahali pa ushindani,
wenye nguvu walidumbukiza ndugu zao, wasio na nguvu na dhaifu walisubiri na
wengine walisubiri miaka wakakata tamaa, ndipo siku hii Yesu alikuja maalumu
kwaajili ya mtu huyu!
Yohana 5:6-7 “Yesu alipomwona huyu amelala,
naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa
mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji
yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.”
Mimi sina mtu wa kunitia birikani!
Tunaona kuwa changamoto kubwa
hapa ilikuwa ni mtu, hiki ni kilio cha watu wengi leo wanatamani kufanya mambo
fulani ya muhimu katika maisha yao lakini hawana mtu, unatamani kusoma lakini
huna mtu wa kukulipia ada, unatamani kupata kazi, Lakini huna mtu wa
kukuunganisha, unatamani kuanza huduma lakini huna mtu wa kukusapoti, unatamani
kurekodi studio lakini huna mtu, unahitaji kuchapa vitabu vyako lakini huna
mtu, unatamani, kuolewa au kuoa lakini hauna mtu, unatamani kufanya biashara
lakini huna mtu, unatamani, kupata kiti cha magurudumu lakini hauna mtu, unatamani
kwenda shule ya ufundi lakini hauna mtu, unatamani kupata dawa za gharama fulani
lakini huna mtu, unatamani kujiendeleza lakini huna mtu, unatamani
kujishughulisha na kilimo lakini huna mtu, unatamani kufungua ofisi yako lakini
huna mtu, unatamani kuanza biashara lakini huna mtu wa kukupa mtaji, unatamani
kulima lakini huna mtu, unatamani kufuga lakini huna mtu, unahitaji kufungua
ofisi ya ujuzi ulionao lakini huna mtu, mtu yule aliyepooza alikuwa hana mtu wa
kusimama naye, alikuwa hana mtu wa kumuinua, alikuwa hana mtu wa kumuunganisha
na fursa iliyokuwa mbele yake, una elimu sahihi kabisa lakini huna mtu, una
ujuzi sahihi kabisa lakini huna mtu, umesomea shughuli hiyo lakini huna mtu
kwaajili ya haya mtu huyu alikata tamaa, inasikitisha kuwa mtu huyu hakuwa na
watu watu walimsahau, watu walimuacha, watu hawakumtafuta watu
hawakujishughulisha naye, birikika lilikuwa sahihi, na maji yalikuwa sahihi
lakini tatizo lake ilikuwa mtu! Kumbe duniani unaweza ukapata shida kwa sababu
huna mtu, unaweza ukasota kwa sababu huna mtu, unaweza ukapoteza muda kwa
sababu huna mtu, Yesu aliitambua hali aliyopitia mtu yule na hivyo alikuja moja
kwa moja kwa mtu yule tena akijua hali halisi kwamba mtu huyu amekosa huduma
kwa sababu hana mtu tena ameteseka muda mrefu amelala pale amepigwa na baridi
na ameng’atwa na mbu, Godoro lale limechakaa, amesubiri muda mrefu, mpaka
amesahau kuwa anahitaji uzima yeye anaona sababu zake ni watu, unaweza kupita katika
hali ngumu sana duniani na wewe ukadhani ni kwa sababu ya watu, nisingelikuwa
hivi kama sio mtu, haya yote yamenipata kwa sababu ya watu, watu, mtu, watu,
mtu, watu, mtu, watu, mtu, hiki ndio kilio cha watu wengi sana, niko hivi
nilivyo leo kwa sababu watu au kwa sababu ya mtu! Nisingelikuwa hivi leo ila ni
kwa sababu ya mtu au watu!
Yohana 5:6-7 “Yesu alipomwona huyu amelala,
naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa
mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji
yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.”
Kukosa mtu sio kikwazo kwa Yesu
Ni muhimu kuelewa kuwa Yesu
alikuja moja kwa moja kwa mtu yule mwenye uhitaji, hatusomi kokote kuwa
alitaarifiwa habari zake lakini tunaona kuwa Yesu alikuwa na uelewa kamili,
alijua shida ya mtu yule na kwa sababu hiyo alikuja kumsaidia shida yake
ilikuwa uzima alikuwa nahitaji uponyaji lakini yeye alikuwa anaona watu, Yesu
alimwambia wataka kuwa mzima? Yesu alijua kuwa mtu huyu amekuweko kwenye nyumba
ya rehema na wala hakupata rehema, alikuwa karibu na birika, na maji lakini
havikuweza kumsaidia, malaika walitibua maji lakini hawakumsaidia mgonjwa
kuingia kwenye maji, Yesu alikuja kufanya uhamisho wa mtu yule kutoka
hospitalini kwenda nyumbani na kuendelea na shughuli zake, inawezekana
unahitaji mtu leo nakujulisha yuko mtu huyu ni Yesu
Yohana 5:6-9 “Yesu alipomwona huyu amelala,
naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa
mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji
yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.
Yesu akamwambia, Simama, jitwike godoro lako, uende. Mara yule mtu akawa mzima,
akajitwika godoro lake, akaenda. Nayo ilikuwa ni sabato siku hiyo.”
Kimsingi Yesu anaonyesha kuwa
anauwezo wa kuingilia mfumo na kufanya mambo nje ya mfumo, Mungu hafungwi na
njia za wanadamu wala njia ulizozizoea, Mungu anaweza kukufanyia jambo hata
bila ya msaada wa kibinadamu, Mungu anaweza kufanya jambo peke yake jambo lolote
ambalo wanadamu wameshindwa, Mungu haitaji mzunguko, wala hataki
kukuchelewesha, Mungu hutenda mambo kwa wakati, Mungu anaweza kugeuza mambo kwa
ghafla, dakika moja ya Yesu ni bora kuliko masaa elfu, ya kusubiria mtu, unapokuwa
hauna mtu kwa taarifa yako Yesu ndiye anakuwa mtu yule, yeye anachotaka ni wewe
kuamka na kuchukua hatua, kukosa msaada sio sababu za Mungu kushindwa kutimiza
kusudi lake, Mungu anaposema wewe chukua hatua yeye anapoona hakuna mtu huchukua hatua yeye
mwenyewe
Isaya 59:16 “Akaona ya kuwa hapana mtu,
akastaajabu kwa kuwa hapana mwombezi; basi, mkono wake mwenyewe ndio uliomletea
wokovu; na haki yake ndiyo iliyomsaidia.”
Zaburi 46:1-3 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio
na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa
ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake
yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake.”
Mungu anaweza kufanya yeye mwenyewe
bila msaada wa kibinadamu, Mungu anaweza kufungua njia bila connection za
wanadamu, wanadamu wanaweza kukusahau, lakini Mungu hawezi kukusahau wala
kukuacha, watu wanaweza kukupita lakini Mwokozi hatokupita kamwe, watu wanaweza
wasikuone lakini Mungu anakuona, unaweza kukaza macho yako kwa Mungu huko ndiko
unakoweza kutoka msaada acha kuwalaumu wanadamu mwangalie Yesu, mwambie Mungu
naomba unisimamie wewe mwenyewe, mwambie Mungu naomba muda wangu usipotezwe na
watu hata kama nimechelewa wewe ndiye msaada wangu mwambie Bwana njoo moja kwa
moja wewe mwenyewe naomba unikwamue hapa nilipo, kwaajili ya watu Eee bwana
unipe neema nisiwaangalia bali nikuone wewe na kila ninachikihitaji ee bwana
fupisha michakato hii unifanyie njia katika
jina la Yesu Kristo wa Nazareth aliye hai Aamen! kumbuka
Bwana ni mtu wa vita atakupigania katika vita yako
“Roho wa Bwana twakualika utawale, karibu Roho wa Bwana fanya mapenzi
ya Bwana”
Rev. Innocent Samuel Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni