Jumatatu, 25 Mei 2026

Yawafaa ninyi Mimi niondoke!

 


Yohana 16:7-13 “Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu. Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu. Kwa habari ya dhambi, kwa sababu hawaniamini mimi; kwa habari ya haki, kwa sababu mimi naenda zangu kwa Baba, wala hamnioni tena; kwa habari ya hukumu, kwa sababu yule mkuu wa ulimwengu huu amekwisha kuhukumiwa. Hata bado nikali ninayo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili hivi sasa. Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Yesu Kristo alikuwa anazungumza maneno haya mwishoni kabisa mwa huduma yake akiwa amewaaga wanafunzi wake ya kuwa yeye ameikamilisha kazi aliyotumwa kuifanya na kuwa anarudi kwa Baba, Yesu alikuwa amewaeleza wanafunzi wake kuwa atasulubiwa, kufa na kufufuka, na kuikamilisha kazi ya ukombozi wa mwanadamu, na baada yake nini kingelifuata. Yesu anaonyesha kwa uwazi umuhimu wa kuja kwa Roho Mtakatifu, hili lilikuwa ni jambo la muhimu sana kwani lingeondoa hofu ya wanafunzi wake na kuifanya kazi ya Mungu kupanuka kwa kina zaidi na hivyo kuondoka kwake kulikuwa na faida zaidi kuliko hasara ambayo wanafunzi wake walikuwa wakiifikiria, Yesu alikuwa anafahamu changamoto ambazo zingewakabili wanafunzi wake baada yake na hivyo alitaka kuwathibitishia kuwa uwepo wa Roho Mtakatifu utakuwa na umuhimu zaidi na suluhu kwa hofu yao

Yohana 14:16-17 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”

Kimsingi Yesu Kristo alilizungumzia swala na ujio wa Roho Mtakatifu kama swala muhimu sana  na hitaji la msingi katika maisha ya kiroho ya  wanafunzi wake na kila aaminiye  baadaye na huduma, Yesu alitaka wanafunzi wake wawe na uelewa mpana kuhusu umuhimu wa Roho Mtakatifu na kuonyesha wazi kuwa hatuwezi kwa namna yoyote ile kuishi duniani na kutimiza kusudi la Mungu bila msaada wa Roho Mtakatifu na nguvu zake mwenyewe, kwa msingi huo katika msimu huu wa juma la Pentekoste tutachukua  muda kutafakari kwa kina na mapana  na marefu umuhimu wa Roho Mtakatifu katika maisha yetu, na kujumuika kwa pamoja katika maombezi ya ubatizo wa Roho Mtakatifu na  hivyo tutajifunza somo hili “Yawafaa ninyi mimi niondoke” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:

·         Yawafaa ninyi mimi niondoke

·         Kazi za Roho Mtakatifu Duniani

·         Ubatizo wa Roho Mtakatifu

Yawafaa ninyi mimi niondoke!

Kimsingi Roho Mtakatifu ametolewa na Mungu Baba yetu ili akae nasi milele na kuikamilisha ile kazi iliyoanzishwa na Yesu Kristo hapa duniani, Yesu alikuwa hana budi kuteswa na kufa msalabani kisha kufufuka siku ya tatu na kupaa kwenda mbinguni mpaka wakati ulioamriwa, Ujio wa Roho Mtakatifu ulikuwa ni wa Muhimu sana kwa sababu kuweko wa Yesu Duniani katika mwili wa kibinadamu kulimpa mipaka ya kihuduma na alilazimika kuweko mahali pamoja kwa wakati mmoja lakini kwa kitendo cha kupaa na kurudi kwa Baba angetoa ruhusa kwa Roho Mtakatifu kuja na kukaa na sisi daima  na kuuleta uwepo wa Mungu kwa kila mmoja kokote aliko Duniani, Kutokana na umuhimu wa Roho Mtakatifu, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake kutokuianza kazi ya Mungu kwanza mpaka wamepokea ubatizo wa Roho Mtakatifu ambaye angewageuza,  kuwapa nguvu na kuwafanya kuwa mashahidi wake

Matendo 1:4-8 “Hata alipokuwa amekutana nao aliwaagiza wasitoke Yerusalemu, bali waingoje ahadi ya Baba, ambayo mlisikia habari zake kwangu; ya kwamba Yohana alibatiza kwa maji, bali ninyi mtabatizwa katika Roho Mtakatifu baada ya siku hizi chache. Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme? Akawaambia, Si kazi yenu kujua nyakati wala majira, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe. Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

Luka 24:46-49 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa pamoja naye kwa zaidi ya miaka mitatu na nusu, wakijifunza maarifa elimu na uwezo wa kufanya huduma lakini pamoja na yote haya Yesu anawaamuru wasitoke kufanya lolote mpaka wapokee ahadi ya Baba, hii ilikuwa na maana iliyo wazi ya kuwa Elimu, ujuzi na maarifa pekee hautoshi, uzoefu hautoshi, vipawa vya kibinadamu havitoshi ili tuwe wanafunzi wa Yesu waliokamilika tunamuhitaji sana Roho Mtakatifu. Uwepo wa Roho Mtakatifu ambaye haonekani kwa macho katika maisha ya wanafunzi wa Yesu ni wa muhimu zaidi kuliko uwepo wa Yesu katika hali ya mwili, Roho Mtakatifu asingeliweza kuja kama Yesu angeendelea kubaki, Kupaa kwa Yesu Kristo, na kutukuzwa kwake mbinguni kungeruhusu ujio wa Roho Mtakatifu ambaye uwepo wake ungesababisha uwepo wa Mungu kukaa ndani ya kila mwamini kokote aliko duniani, lakini pia kazi ya kutukuzwa kwa Yesu Kristo Duniani  ingeanza kupitia Roho Mtakatifu sawasawa na jinsi ambavyo Yesu ametukuzwa Mbinguni.

Kazi za Roho Mtakatifu Duniani

-          Roho Mtakatifu ni Msaidizi mwingine – Yesu Kristo alikuwa anafahamu kuwa Wanafunzi wake wangekabiliwa na changamoto kali  na kubwa na upinzani mkali wa aina mbalimbali na wangekata tamaa hasa baada ya kuondoka kwake, Yeye alipokuwa pamoja nao alikuwa ni mtetezi mkubwa sana wa wanafunzi wake na mashambulizi yote ya adui yalielekezwa kwake, Kuondoka kwake Yesu Kristo ilikuwa sababu ya huzuni nyingi sana hofu na mashaka na walikata tamaa, Yesu aliwaahidi kuwa atawaletea msaidizi mwingine

 

Yohana 14:16-17 “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu.”

 

Neno Msaidizi mwingine katika lugha ya kiyunani (Koine Greek) linasomeka kama “Paraklētos” ambalo maana yake Msaidizi, mtetezi, mfariji, mshauri au mtu anayesimama karibu na wewe kwa kusudi la kukutetea wakili (Advocate) Kazi hii inafanywa na Roho Mtakatifu kwa kila mtu aliyemuamini hata leo, kwa sababu hiyo kila mtu aliyeokoka anamuhitaji yeye kama uwepo wa Mungu katika maisha yetu ya kila siku.

 

-          Roho Mtakatifu anauwezo wa kubadilisha maisha – Wanafunzi wa Yesu Kristo walikuwa wanahitaji mabadiliko makubwa ya maisha yao, wengine walikuwa waoga, wasiojiamini, wenye ukali, wenye kisasi, wasioweza kusamehe na walihitaji mabadiliko makubwa sana, Roho Mtakatifu ndiye njia inayohusika katika mfumo mzima wa kubadili maisha ya mtu na kumfanya afae kwa kazi ile ambayo Mungu anaihiitahi katika maisha, ni pale tu Roho wa Mungu anapokuwa juu ya mtu kwa ubatizo ndipo anapoweza kubadilisha maisha ya mtu huyo na kumfanya afae kwa matumizi ya kazi ya ufalme wa Mungu.

 

1Samuel 10:5-7 “Baada ya hayo utafika Gibea ya Mungu, hapo palipo na ngome ya Wafilisti; kisha itakuwa, utakapofika mjini, utakutana na kundi la manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, wenye kinanda, na tari, na kinubi, na filimbi mbele yao, nao watakuwa wakitabiri; na roho ya Bwana itakujilia kwa nguvu, nawe utatabiri pamoja nao, nawe utageuzwa kuwa mtu mwingine. Basi, hapo ishara hizi zitakapokutukia, fanya kama uonavyo vema; kwa kuwa Mungu yu pamoja nawe.”

 

Wagalatia 5:16-25 “Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. Lakini mkiongozwa na Roho, hampo chini ya sheria. Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”

 

Ubatizo wa Roho Mtakatifu unatubadilisha maisha na kutufanya au kutusaidia kuishi maisha matakatifu siku hadi siku, kutembea katika Roho Mtakatifu kutayafanya maisha yetu yaachane na zile hali za mwili na kuruhusu ukomavu na kuzaliwa kwa matunda ya Roho Mtakatifu katika maisha yetu na kumlingania Yesu.

 

-          Roho Mtakatifu hutuvika uwezo au Nguvu kutoka juu – Kuihubiri injili na kuishi maisha ya ushuhuda kunahitaji nguvu za Mungu, Mungu anapowatuma watu katika ulimwengu huu anawavika nguvu kwa sababu kuna nguvu za upinzani ambazo tutakabiliana nazo duniani nguvu hii  tunayovikwa na Roho wa Mungu katika lugha ya kitaalamu ya maandiko ya agano jipya inaitwa “Dunamis” hili ni neno la Kiyunani (Koine Greek) ambalo lina maanisha uwezo, nguvu za Mungu, Nguvu zenye matokeo na mamlaka, nguvu hii husaidia waamini kukabiliana na upinzani wa anaina yoyote na kuwa tayari hata kufa kwaajili ya jina la Bwana na kwaajili ya ufalme wa Mungu, Wale waliokuwa na hofu na woga waliweza kutiwa nguvu na kuwa majasiri mara baada ya kubatizwa katika Roho Mtakatifu, tutakuwa na uwezo wa kukabiliana na upinzani wa aina yoyote na kuwa tayari hata kufa kwaajili ya jina la Bwana kama tutabatizwa kwa Roho Mtakatifu.

 

Luka 24:46-49 “Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya. Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

 

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

 

-          Roho Mtakatifu atatuongoza katika kweli yote – Kweli yote ya Mungu haiwezi kueleweka kwa akili za kawaida peke yake, Lakini Roho Mtakatifu ni Mwalimu, yeye ni mwandishi wa neno la Mungu, ni Mwalimu na anaweza kutupa ufunuo wa kweli,  lakini sio hivyo tu Roho Mtakatifu atatukumbusha katika maswala yote muhimu na ya msingi katika mafundisho ya Yesu Kristo, Yeye hufanya kazi ya kutufunulia maswala yote kuhusu Mungu na mapenzi yake, Katika ulimwengu huu kila mtu anadai anayo kweli lakini ni kazi ya Roho Mtakatifu ambaye anaitwa Roho wa kweli kuufunua ukweli halisi sawasawa na ufunuo wa neno la Mungu.

 

Yohana 14:26 “  Lakini huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia.”

 

1Wakorintho 2:10-14 “Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho Huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu, Maana Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu. Lakini sisi hatukuipokea roho ya dunia, bali Roho atokaye kwa Mungu, makusudi tupate kuyajua tuliyokirimiwa na Mungu.  Nayo twayanena, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yanayofundishwa na Roho, tukiyafasiri mambo ya rohoni kwa maneno ya rohoni. Basi mwanadamu wa tabia ya asili hayapokei mambo ya Roho wa Mungu; maana kwake huyo ni upuzi, wala hawezi kuyafahamu, kwa kuwa yatambulikana kwa jinsi ya rohoni.”

 

-          Roho Mtakatifu humshuhudia Yesu Kristo – Kumshuhudia Yesu Kristo katika lugha ya asili ya kiyunani linatumika neno “martureō ambalo kwa kiingereza ni sawa na  neno “giving evidence”, au “well report about me”, maana yake ni kuwa Roho Mtakatifu atathibitisha ukweli kuhusu Yesu Kristo ni nani au ataelezea vizuri kuhusu Yesu Kristo, ana ushahidi wa kina kuhusu Yesu Kristo, kwa hiyo kama Mwalimu wa kweli atawaelekeza watu kumjua Yesu Kristo kwa kina zaidi ya alivyojulikana kwa wakati ule, na anavyoelezewa katika maandiko, atamuinua Yesu Kristo atathibitisha mafundisho yake kwa hiyo huduma yoyote ya kiroho au inayoongozwa kiroho haitakuwa na malengo ya kumuinua mtu bali itakuwa inamuinua Yesu Kristo, huduma yoyote ambayo haimuinui Yesu Kristo inahitaji kupimwa , na mtumishi yoyote ambaye hamuinui Yesu hatuna budi kumwangalia kwa makini na nabii yeyote ambaye anajitukuza yeye kuliko Kristo naye ni wa kuangaliwa kwa makini, ukiona imani yoyote inamuinua yeyote zaidi ya Kristo basi ni imani yenye mashaka.

 

Yohana 15:26 “Lakini ajapo huyo Msaidizi, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia.”

 

1Wakorintho 12:3Kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika Roho wa Mungu, kusema, Yesu amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu.”

-          Roho Mtakatifu hutoa nyenzo za kutendea kazi – Ziko nyenzo za kutendea kazi ya Mungu ambazo hutolewa na Roho Mtakatifu ni maarufu sana kama karama za Roho Mtakatifu, hizi husaidia kurahisisha kazi ya Mungu na kulithibitisha neno na kuufaidia mwili wa Kristo, bila karama na utendaji wa Roho Mtakatifu kupitia karama hizo maneno yetu yatakuwa ni maneno yasiyo na uthibitisho au yanaweza kuwa kama hekima tu za wanadamu (Yaani Falsafa) au maneno ya kushawishi, lakini litakuwa ni neno lenye kuthibitishwa

 

1Wakorintho 2:4-5 “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za nguvu, ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali katika nguvu za Mungu.”

 

1Wakorintho 12:7-11 “Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye.”

 

-          Roho Mtakatifu ni njia ya kurahisisha ukomavu wa kiroho – Roho Mtakatifu anahusika katika kuzaliwa kwetu mara ya pili, lakini pia anahusika katika kusaidia ukomavu wetu wa kiroho, endapo Mkristo atakomaa kiroho matendo yote ya mwili yanapukutika na matunda ya kiroho yanaanza kujichomoza katika maisha ya mwamini, Roho Mtakatifu hatoi karama tu bali anatoa na matunda ambayo kimsingi hutuumbia tabia kama ya Kristo

 

Wagalatia 5:22-25 “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria. Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”

 

-          Roho Mtakatifu hutupa hekima ya utawala na maamuzi – Ili dunia iweze kuongozwa vema na maamuzi yaweze kufanyika kwa haki bila upendeleo wala kuumiza watu tunamuhitaji Roho Mtakatifu ambapo yeye hutoa hofu ya Mungu, haki, ufahamu, ushauri, uweza na maarifa yatakayosaidia kuujenga ufalme wa Mungu na kuiongoza dunia katika haki.

 

Isaya 11:1-5 “Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda. Na roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana; na furaha yake itakuwa katika kumcha Bwana; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonya kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya. Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia.”

 

Matendo 6:3-4 “Basi ndugu, chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.”

 

-          Roho Mtakatifu hutupa nguvu za kukabiliana na uchawi – Katika ulimwengu huu tulio nao ziko nguvu kubwa mbili zinazotawala, nguvu za Mungu na nguvu za Giza, ili mwanadamu wa kawaida aweze kuwa na nguvu za Mungu zinazoweza kukabiliana na nguvu za giza ni lazima abatizwe katika Roho Mtakatifu, nguvu za Mungu kwetu ziko pia kwaajili ya kukabiliaana na nguvu pinzani  mfano

 

Matendo 13:6-12 “Walipokwisha kupita katikati ya kisiwa chote mpaka Pafo, wakaona mtu mmoja, mchawi, nabii wa uongo, Myahudi jina lake Bar-Yesu; mtu huyu alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mtu mwenye akili. Yeye liwali akawaita Barnaba na Sauli waje kwake, akataka kulisikia neno la Mungu. Lakini Elima, yule mchawi (maana ndiyo tafsiri ya jina lake), akashindana nao, akitaka kumtia yule liwali moyo wa kuiacha ile imani. Lakini Sauli, ambaye ndiye Paulo, akijaa Roho Mtakatifu, akamkazia macho, akasema, Ewe mwenye kujaa hila na uovu wote, mwana wa Ibilisi, adui wa haki yote, huachi kuzipotoa njia za Bwana zilizonyoka? Basi, angalia, mkono wa Bwana u juu yako, nawe utakuwa kipofu, usilione jua kwa muda. Mara kiwi kikamwangukia na giza, akazunguka-zunguka na kumtafuta mtu wa kumshika mkono na kumwongoza.Ndipo yule liwali, alipoyaona yaliyotendeka, akaamini, akiyastaajabia mafundisho ya Bwana.”

 

2Timotheo 3:8 “Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani.”

 

1Wafalme 18 :21-24 “Naye Eliya akawakaribia watu wote, akanena, Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini? Bwana akiwa ndiye Mungu, mfuateni; bali ikiwa Baali ni Mungu, haya! Mfuateni yeye. Wale watu hawakumjibu neno. Ndipo Eliya akawaambia watu, Mimi nimesalia, mimi peke yangu, nabii wa Bwana; lakini manabii wa Baali ni watu mia nne na hamsini. Kwa hiyo na watutolee ng'ombe wawili; wao na wajichagulie ng'ombe mmoja, wamkate-kate na kumweka juu ya kuni, wasitie moto chini; nami nitamtengeza huyo ng'ombe wa pili, na kumweka juu ya kuni, wala sitatia moto chini. Nanyi ombeni kwa jina la mungu wenu, nami nitaomba kwa jina la Bwana; na Mungu yule ajibuye kwa moto, na awe ndiye Mungu. Watu wote wakajibu wakasema, Maneno haya ni mazuri.”                              

 

Ubatizo wa Roho Mtakatifu.

Fahamu ya kuwa anayebatiza kwa Roho Mtakatifu Ni Bwana Yesu mwenyewe, Na ubatizo huu ni mpango wa Mungu, ni ahadi ya Mungu kwa waaminio kwa hiyo kila mmoja anastahili kupokea kwa Imani na kufungua moyo wake kuhakikisha kuwa maisha yake yanajaa na kufunikwa na uwepo wa Mungu Roho Mtakatifu sawa na neno lake lisemavyo:-

 

a.       Mathayo 3:11 “Kweli mimi nawabatiza kwa maji kwa ajili ya toba; bali yeye ajaye nyuma yangu ana nguvu kuliko mimi, wala sistahili hata kuvichukua viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto.”

 

b.       Ubatizo huu ni ahadi ya Mungu mwenyewe kwa kila mtu amwaminiye

Yoel 2:28 “Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili; na wana wenu, waume kwa wake, watatabiri, wazee wenu wataota ndoto, na vijana wenu wataona maono;”

               

Luka 24:49 “Na tazama, nawaletea juu yenu ahadi ya Baba yangu; lakini kaeni humu mjini, hata mvikwe uwezo utokao juu.”

 

Matendo 2:38-39 “Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie.”

 

c.       Lazima uwe na nia ya kutumika – Ubatizo wa Roho Mtakatifu ni kwaajili ya utumishi, Roho wa Mungu anatabia ya kutaharakisha watu kwaajili ya utumishi, Pale tunapokuwa tayari kwa huduma na kukubali kutumika huku na huko Roho Mtakatifu atakuwa radhi nasi, Ubatizo huu hauwafai watu ambao wakataa tu, unawafaa watu ambao wako tayari kwa kazi kwa sababu Roho Hatakupa kutulia

 

Waamuzi 13:24-25 “Basi yule mwanamke akamzaa mtoto mwanamume akamwita jina lake Samsoni, mtoto huyu akakua, Bwana akambarikia. Roho ya Bwana ikaanza kumtaharakisha katika Mahane-dani, katikati ya Sora na Eshtaoli.”

 

Yeremia 47:6-7 “Ee upanga wa Bwana, Siku ngapi zitapita kabla hujatulia? Ujitie katika ala yako; Pumzika, utulie. Utawezaje kutulia, Ikiwa Bwana amekupa agizo? Juu ya Ashkeloni na juu ya pwani, Ndipo alipoyaamuru hayo.”

 

d.       Kwa maombi bila kuchoka – Kama itatokea hujabatizwa katika Roho mtakatifu wakati Fulani huo usiwe mwisho au mwanzo wa kukata tamaa maandiko yanatutia moyo kuendelea kung’ang’ania mpaka tumpokee Roho Mtakatifu, aidha huwezi kupokea Roho Nyingine zaidi ya kile unachokiomba, iko dhana ya watu kufikiri kuwa ukiwekewa mikono wakati wa maombi utapokea roho Nyingine, Mungu atakupoa sawasawa na kuomba kwako

 

Luka 18:9-13 “Nami nawaambia, Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa. Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Maana ni yupi kwenu aliye baba, ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe au samaki, badala ya samaki atampa nyoka? Au akimwomba yai, atampa nge? Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?

 

e.       Lazima uwe na imani

Maswala yote ya kiroho yanapokelewa kwa Imani, wakati wote mtu akiwa na mashaka hawezi kupokea kitu kutoka kwa Mungu, kwani pasipo Imani haiwezekani kumpendeza Mungu, kwa hiyo Mtu anayemuhitaji Roho wa Mungu ni lazima aombe kwa Imani,

 

Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”

 

Wagalatia 3:2 “Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?

 

f.         Kuna umuhimu wa kuomba kwa kupaaza sauti – watu wanaoomba kimyakimya maombi ya ubatizo wa Roho Mtakatifu ni vigumu sana kujazwa maandiko yanaonyesha kuwa wale waliobatizwa katika Roho Mtakatifu walikuwa wakiomba kwa sauti ya kusikika kubwa na ndio maana walijazwa na wakasikika wakisema kwa lugha nyingine

Zaburi 81:10 “Mimi ndimi Bwana, Mungu wako, Niliyekupandisha toka nchi ya Misri; Fumbua sana kinywa chako nami nitakijaza.”

 

Matendo 10:45-46 “Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu,”

 

Kwa hiyo baada ya kujifunza namna hii na kusikia neno la Mungu kuhusu Ubatizo wa Roho Mtakatifu unapaswa kuamini na kuyatendea kazi yale yote ambayo umeyasikia na ninakuhakikishia hutakuwa kama ulivyo.

Yesu alisisitiza juu ya ahadi hii ya ujio wa Roho Mtakatifu kwa sababu

Roho Mtakatifu ni Msaidizi mwingine, Roho Mtakatifu ana uwezo wa kubadilisha maisha, Roho Mtakatifu hutuvika uwezo au Nguvu kutoka juu, Roho Mtakatifu atatuongoza katika kweli yote Roho Mtakatifu humshuhudia Yesu Kristo, Roho Mtakatifu hutoa nyenzo za kutendea kazi, Roho Mtakatifu ni njia ya kurahisisha ukomavu wa kiroho, Roho Mtakatifu hutupa hekima ya utawala na maamuzi, Roho Mtakatifu hutupa nguvu za kukabiliana na uchawi, kuna na mambo mengine mengi sana ambayo kibinadamu hatuwezi kuyatakeleza bila msaada wa Roho Mtakatifu hivyo ubatizo wa Roho Mtakatifu unabaki kuwa nyenzo Muhimu sana kwa kanisa tangu jana leo na hata milele. Uongezewe neema unapochukua majukumu ya kulitendea kazi neno la Mungu kivitendo, wako katika utumishi.

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye hekima             

Hakuna maoni: