Jumapili, 4 Desemba 2016

Mungu wa Kisasi Uangaze!



Andiko : Zaburi 94:1-3

“1. Ee Bwana, Mungu wa kisasi, Mungu wa kisasi, uangaze, 2. Mwenye kuihukumu nchi, ujitukuze, Uwape wenye kiburi stahili zao. 3. Bwana, hata lini wasio haki, Hata lini wasio haki watashangilia?



Utangulizi:

Je wewe umewahi kuona watu wakidhulumiwa? Umewahi kuona mahali haki haitendeki? Je hujawahi hata kusikia mahali watu wakionewa, wakiteswa, wajane na yatima na hata wageni au wakimbizi na wanyonge wakikandamizwa na kuonelewa huku wale wanaofanya dhuluma wakishangilia na kufurahi? Na hata wakidharau kuweko kwa Mungu na utetezi wake?

Jambo hili ndio hali halisi katika zaburi hii iliyoandikwa na Daudi, Hatuwezi kujua kuwa Daudi wakati huu alikuwa ameshuhudia nini katika mazingira yake, lakini kile anachokizungumza na kukililia katika zaburi hii kinafunua wazi aidha jambo ambalo amelishuhudia katika uzoefu wake wa maisha ama limewahi kumkuta, vyovyote vile iwavyo maswala haya yanaikumba hata jamii inayotuzunguka leo na Biblia hapa kupitia kinywa cha Mfalme Daudi ambaye pia Roho wa Kinabii alikaa ndani yake kuna mswala kadhaa muhimu ya kujifunza ambayo tutajifunza katika vipengele vifuatavyo:-

·         Kumuita Bwana kwaajili ya Haki (Zaburi ya 94:1-4)
·         Kushitaki kile wanachikifanya wadhalimu (Zaburi 94:5-7)
·         Kushangazwa na ujinga wa wadhalimu (Zaburi 94:8-11)
·         Baraka za kupitia katika magumu (Zaburi 94:12-13, 14-15)
·         Hatima ya kucheza na mwenye haki (Zaburi 94:16-23)

Kumuita Bwana kwaajili ya Haki (Zaburi ya 94:1-4)

Daudi anaiimba Zaburi hii katika mtazamo wa watu wanaoonewa, wanoteswa na kudhulumiwa na kutokutendewa haki watu hao wakimuangalia Mungu kama Jaji mkuu mwenye uwezo wa kutoa hukumu ya mwisho, wakati wengine wote wameshindwa kutoa msaada, Daudi anamuonyesha Mungu kuwa ndio mahakama ya juu zaidi tunayoweza kukata rufaa na tena mahakama hii ya juu zaidi inauwezo wa kutulipia Kisasi, Daudi anamtaka Mungu huyu mwenye uwezo wa kulipiza kisasi dhidi ya maadui zetu  aangaze, yaani aangalie kila kinachofanyika na kutoa haki

Wewe na mimi tumewahi kushuhudia kile ambacho Daudi alikishuhudia na kukililia katika Zaburi hii, inawezekana umewahi kushuhudia mume akifariki na kuacha mjane na yatima na Ndugu wa Mume wakiingilia kati na kudhulumu mali za yatima na kumuacha mjane huyo akiwa mikono mitupu wakiishi maisha ya dhiki, tumewahi kushuhudia wanawake wakorofi wakipora mali za waume zao na kujimilikisha, ndugu jamaa na hata watoto wakigombea hati za viwanja, kadi za magari, watu wakichongeana makazini na kusababisha wenngine wafukuzwe kazi, na kushangilia mafanikio ya anguko la mwingine, watu wakichafuana kwa faida na maslahi yao wenyewe na hila za aina nyingi zikifanyika duniani zinazofanana na hayo

Biblia inatufundisha kuwa endapo tumezulumiwa kila tunachokistahili na hakuna wa kututetea pako mahali ambapo tunaweza kudai haki zetu, Yesu alifundisha kwa msisitizo kuhusu madai ya haki zetu kwa Jaji mkuu wa majaji wote duniani, Mfalme wa wafalme mwenye uwezo sio tu wa kutoa haki bali pia kulipiza kisasi kwa watakaotudhulumu 

Luka 18: 1-81. Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. 2. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. 3. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. 4. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu, 5. lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima. 6. Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. 7. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao? 8. Nawaambia, atawapatia haki upesi;”

Daudi anamuomba Mungu haki iweze kupatikana, Yesu anatufundisha kuendelea Kumuomba Mungu mpaka haki yetu iweze kupatikana Yeye ni Jaji mkuu, ni Hakimu wa Dunia nzima, tunaweza kuimuendea yeye kwa ujasiri atupatie haki yetu, hatuhitaji kulalamika Yuko Mungu wa kisasi mwenye kuihukumu inchi na kuwapa stahili zao wenye kiburi, Yeye atawahukumu watu wote na pia ndiye mwenye kulipiza kisasi kwa wadhalimu na ndiye anayeteua majaji Warumi 13:4

Biblia inatufundisha kuwa tunapodhulumiwa tumuombe Mungu na kumsihi aangazie kile kinachoendelea, Hatupaswi kutumia njia yoyote ile yenye kutaka kujilipia kisasi wenyewe ni muhimu kumuachia Mungu yeye ndiye atakayetulipia kisasi.

 Warumi 12:19Wapenzi, Msijilipizie kisasi, Bali ipisheni ghadhabu ya Mungu; maana imeandikwa Kisasi ni juu yangu mimi nitalipa anena Bwana

Kushitaki kile wanachikifanya wadhalimu (Zaburi 94:5-7)

Daudi mwandishi wa Zaburi anaendelea kumwambia Mungu kilie wanachokifanya wadhalimu, wote tunajua kuwa Mungu anafahamu kila kinachoendelea lakini Daudi anataka kufafanua, kuchamganua kile ambacho ameona kinaendelea na anataka Mungu akiangazie 

5. Ee Bwana, wanawaseta watu wako; Wanautesa urithi wako; 6. Wanamwua mjane na mgeni; Wanawafisha yatima. 7. Nao husema, Bwana haoni; Mungu wa Yakobo hafikiri.”

Daudi anaelezea jinsi sifa ya wadhalimu hao walivyo, hawana huruma, wana kiburi na wanazungumza kwa kejeli na kiburi cha hali ya juu, hawajali hata kile wanachokizungumza, wanazungumza vibaya na wengine, sio watu wa dini wala hawamjali Mungu, wanajiamini wanajitegemea, wanavunja watu mioyo, wanagawa watu, wanawaua watu,hawajali huyu mjana wala yatima, wanajisemesha kuwa nani atatwatetea nani atawaokoa na uwezo walio nao ni makatili, hawajali wageni wala wakimbizi, Daudi aliwasoma vema maadui hawa na kuwaona jinsi walivyo wabaya na wakatili na alieleza Moyo wake kwa Mungu kuwahusu, wako watu Duniani ni wabaya na hawana haya unaweza kujiuliza ni roho ya namna gani waliyonayo na usipate majibu kwamba wanaongozwa na ibilisi au vipi wakati mwingine unaweza kuona ukatiliwao unazidi hata ule wa ibilisi mwenyewe Mungu atulinde na watu wa aina hii 

Kushangazwa na ujinga wa wadhalimu (Zaburi 94:8-11)

8. Enyi wajinga miongoni mwa watu, fikirini; Enyi wapumbavu, lini mtakapopata akili? 9. Aliyelitia sikio mahali pake asisikie? Aliyelifanya jicho asione?         10. Awaadibuye mataifa asikemee? Amfundishaye mwanadamu asijue? 11.  Bwana anajua mawazo ya mwanadamu, Ya kuwa ni ubatili.”

Daudi anashangwazwa na jinsi wadhalumu hao walivyojawa na roho ya udanganyifu wanafanya uovu mkubwa kwa kujiamini kiasi cha kupofuka macho na kuwa wajinga na wasiofikiri wala kuwa na akili Daudi anauzoefu kuwa Mungu Jaji mkuu atafanya kitu haiwezekani Yeye aliyemuumba mwanadamu awe na sikio kisha yeye mwenyewe asisikie, Yeye aliyemuumba mwanadamu kuwa na jicho kisha asiione yanayotendeka, yeye anayeshikisha watu adabu asikemee udhalimu unaoendelea, yeye anayewafundisha wanadamu sheria na jinsi iwapaswavyo kuenenda asijue uharibifu unaoendelea, anahitimisha kuwa Mungu anayajua mawazo ya wanadamu na anatambua kuwa ni ya ubatili

Wako watu wameharibika mioyo kiasi cha kutokutambua kuwa yuko Mungu anayeona na kusikia, wako watu wanafanya uovu kana kwamba wao ndio Miungu na hakuna awaye yote aliye juu yao, Daudi anasema huu ni ujinga wa watu na unaweza kufanywa na watu wasiofikiri, tena anawaita wapumbavu na anajiuliza ni lini watakapopata akili

Baraka za kupitia katika magumu (Zaburi 94:12-13, 14-15)

12. Ee Bwana, heri mtu yule umwadibuye, Na kumfundisha kwa sheria yako; 13. Upate kumstarehesha siku za mabaya, Hata asiye haki atakapochimbiwa shimo.14. Kwa kuwa Bwana hatawatupa watu wake, Wala hutauacha urithi wake, 15. Maana hukumu itairejea haki, Na wote walio wanyofu wa moyo wataifuata.

Daudi anatumia mistari hii kumuita heri mtu anayepitia katika majaribu kwake yeye kupitia katika hali ngumu ni kuadibishwa na Mungu ni kufundishwa sheria na kanuni za Mungu na kuwa hatima ya Mungu ni kuja kutupa starehe wakati wa mabaya na kuwa mwisho wa adui upon a tutawaona adui zetu wakizikwa wakichimbiwa shimo, Daudi aonyesha ya kuwa Mungu hatawatupa watu wake hawezi kutuacha maana kila anayemcha yeye ni urithi wake, ana uhakika kuwa Mungu atafanya hukumu atarejea  na haki itapatikana na waliowanyofu wa moyo watanufaika nayo

Dhuluma zinazoendelea Duniani hazitadumu, uko wakati Mungu atakomesha , atahukumu kwa haki na kuwasterehesha wote walioonewa na mwisho wa wabaya tutauona Ndugu yangu kama asemavyo Daudi na kama lisemavyo neno la Mungu Bwana hatawatupa watu wake hawezi kuuachia Urithi wake 

Hatima ya kucheza na mwenye haki (Zaburi 94:16-23)

16. Ni nani atakayesimama Kwa ajili yangu juu ya wabaya? Ni nani atakayenisaidia Juu yao wafanyao maovu? 17. Kama Bwana asingalikuwa msaada wangu, Nafsi yangu kwa upesi ingalikaa penye kimya. 18. Niliposema, Mguu wangu unateleza; Ee Bwana, fadhili zako zilinitegemeza. 19. Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, Faraja zako zaifurahisha roho yangu. 20. Je! Kiti cha udhalimu kishirikiane nawe, Kitungacho madhara kwa njia ya sheria? 21. Huishambulia nafsi yake mwenye haki, Na kuihukumu damu isiyo na hatia. 22. Lakini Bwana amekuwa ngome kwangu, Na Mungu wangu mwamba wangu wa kukimbilia. 23. Naye atawarudishia uovu wao, Atawaangamiza katika ubaya wao, Naam, Bwana, Mungu wetu, atawaangamiza

Mwandishi wa zaburi anahitimisha kwa kuuliza swali nani atasimama kunitetea dhidi ya adui zangu? Na ni atanisaidia dhidi ya waovu au wadhalimu? Kisha anaonyesha kuwa Bwana ni Msaada na kama asingelikuwa msaada waovu waneipoteza nafsi yake, Lakini fadhili za Bwana ni njema na zilimtegemeza Mungu alifanyika faraja kubwa  pamoja na udhalimu wanaoufanya Mungu akikimbiliwa anakuwa mwamba na atawarudisha waovu hawezi kukaa nao kiti kimoja atawaangamiza katika ubaya wao na hakika atawaangamiza 

Ni muhimu kufahamu kuwa Mungu anaona kila aina ya uonevu unaoendelea katika ulimwengu, inatupasa kukata rufaa na kudai haki zetu kwa dua sala na maombi, Mungu atatutetea, ataingilia kati jambo kubwa la msingi ni kumwambia mlipiza kisasi aangaze Tumuombe Mungu wa kisasi aangaze amulike aangalkie aone atazame na kukemea kila aina ya ubaya , uovu  na udhalimu wa watu walioota sugu walioharibika mioyo wasiojali wanaodhulumu, wanaoibia watu wakidhani kuwa hakuna utetezi dhidi ya wanyonge Bwana ana aliangalie jambo hilo na kulikemea Katika Jina la Yesu Kristo mwana wa Mungu aliye hai

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima!

+255718990796

Jumanne, 15 Novemba 2016

Kumuweka Bwana mbele Daima!



Andiko la Msingi: Zaburi 16:8

Nimemweka Bwana mbele yangu daima, Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu, sitaondoshwa.

Utangulizi:

Zaburi hii ni zaburi iliyotungwa na kuimbwa na Daudi, Ni zaburi ya kimasihi hasa kutokana na unabii unaomuhusu Yesu Kristo moja kwa moja, hata hivyo kupitia zaburi hii bado kuna mambo ya muhimu ya kujifunza kutokana na maisha ya Daudi, na uwezo wake aliokuwa nao katika kumtegemea Mungu na faida zake Daudi anatufunulia siri mojawapo kubwa ya ushindi na mafanikio yake katika kudumisha uhusiano na Mungu, katika mstari huu wa nane kuna maswala ya msingi matatu ya kujifunza

·         Kumuweka Bwana mbele Daima
·         Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu
·         Sitaondoshwa!

Kumuweka Mungu mbele Daima.

Moja ya siri kubwa ya ushindi katika maisha ya Daudi ilikuwa ni pamoja na kumuweka Mungu mbele, Katika biblia ya kiingereza neno kumuweka Mungu mbele linasomeka hivi “I have set the Lord always before meNeno “SET” la kiingereza linalotumika hapo liko sawa na neno la kiebrabia “SAWA” kwa msingi huo tafasiri rahisi ya mstari wa aya hiyo katika kiingereza inaweza kusemeka hivi “I have equally set” ambalo katika Kiswahili tunaweza kutumia neno Nimekwenda sambamba na Mungu, au nimetembea sawasawa na Mungu, au kwenda pamoja na Mungu, au kuendenda kwa jinsi ya Mungu lugha hii ya kibiblia ndiyo ambayo imetumika katika Mwanzo 5:22,24 ikionyesha jinsi “Henoko akaenda pamoja na Mungu” kwa hiyo duniani kuna aina tatu za mwenendo, kwa jinsi ya Mungu, kwa jinsi ya kishetani na kwa jinsi ya kibinadamu.

1Wakoritho 3:3 “Kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini, maana ikiwa kwenu kuna husuda, na fitina Je si watu wa tabia ya mwilini; tena mnaendenda kwa jinsi ya kibinadamu

Daudi alidhamiria katika maisha yeke kuenenda kwa jinsi ya Mungu siku zake zote. Hakutaka kuendenda kwa jinsi nya mwili wala ya kishetani aliamua maisha yake yote kumuweka Mungu mbele hii ilikuwa siri ya maisha ya ushindi kwa daudi siku zote za maisha yake.

Kwa kuwa yuko kuumeni kwangu.

Mkono wa kuume yaani mkono wa kulia kama unavyojulikana sana kwa lugha ya Kiswahili ni kuwekwa mahali pa Heshima kubwa sana, ni sawa na kutawala pamoja, au kukaa katika meza ya kifalme, kuamua pamoja naye, kula pamoja naye kushauriana na kufanya maamuzi ya pamoja, hivyo mtu alipomuweka mtu mkono wake wa kuume maana yake kumuweka mahali pa heshima kubwa
 2Samuel 9:1-9, “1. Kisha Daudi akasema, Je! Amesalia mtu mmoja katika nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema kwa ajili ya Yonathani? 2. Palikuwa na mtumishi mmoja wa nyumba ya Sauli, jina lake Siba, basi wakamwita aende kwa Daudi; na mfalme akamwuliza, Wewe ndiwe Siba? Naye akasema Mimi, mtumwa wako ndiye. 3. Mfalme akasema, Je! Hakuna hata sasa mtu ye yote wa nyumba ya Sauli, nipate kumtendea mema ya Mungu? Siba akamwambia mfalme, Yonathani anaye mwana hata sasa, aliye na kilema cha mguu. 4. Mfalme akamwambia, Yuko wapi? Siba akamwambia mfalme, Tazama, yumo katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. 5. Basi mfalme Daudi akatuma watu, akamwondoa katika nyumba ya Makiri, mwana wa Amieli, katika Lo-debari. 6. Basi Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli akaenda kwa Daudi, akaanguka kifudifudi, akasujudu. Daudi akasema, Mefiboshethi! Naye akaitika, Mimi hapa, mtumwa wako! 7. Daudi akamwambia, Usiogope, maana bila shaka nitakutendea mema; kwa ajili ya Yonathani, baba yako, nami nitakurudishia mashamba yote ya Sauli, baba yako; nawe utakula chakula mezani pangu daima. 8. Akasujudu, akasema, Mimi mtumwa wako ni nini, hata ukamwangalia mbwa mfu kama mimi? 9. Ndipo mfalme akamwita Siba, mtumwa wa Sauli, akamwambia, Mali yote yaliyokuwa ya Sauli na ya nyumba yake nimempa mwana wa bwana wako. 10. Nawe utamlimia nchi hiyo, wewe, na wanao, na watumwa wako; nawe utamletea mwana wa bwana wako matunda yake, apate chakula ale; lakini Mefiboshethi, mwana wa bwana wako, atakula chakula mezani pangu sikuzote. Basi huyo Siba alikuwa na wana kumi na watano na watumwa ishirini. 11. Ndipo Siba akamwambia mfalme, Mimi, mtumwa wako, nitatenda hayo yote kama bwana wangu, mfalme, alivyoniamuru. Na kwa habari za Mefiboshethi, mfalme alisema, Atakula mezani pangu, kama mmojawapo wa wana wa mfalme. 12. Huyo Mefiboshethi alikuwa na mwana mdogo, jina lake akiitwa Mika. Na watu wote waliokaa nyumbani mwa Siba walikuwa watumwa wa Mefiboshethi. 13. Basi Mefiboshethi akakaa Yerusalemu; maana alikuwa akila chakula sikuzote mezani pa mfalme; naye alikuwa na kilema cha miguu yote miwili.

Watu wa nyakati za agano jipya walifahamu vizuri umuhimu wa swala hili, swala la kumuweka mtu mkono wa kuume lilimaanisha kumuheshimu mtu huyo kwa kiwango kikubwa na cha hali ya juu, katika serikali kumuweka mtu mkono wa kuume ni sawa na kumfanya kuwa makamu wa rais, wana wa  Zebedayo kupitia mama yao waliwahi kumuomba Yesu wapewe nafasi hii lilikuwa ni ombi la ajabu sana ambalo gharama yake ilikuwa ni kupitia mateso na aibu ileile aliyoipitia Yesu Kristo  Mathayo 20:20-23

Biblia inasema:- 20. Ndipo mama yao wana wa Zebedayo akamwendea pamoja na wanawe, akamsujudia, na kumwomba neno. 21. Akamwambia, Wataka nini? Akamwambia, Agiza kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja mkono wako wa kuume, na mmoja mkono wako wa kushoto, katika ufalme wako. 22. Yesu akajibu akasema, Hamjui mnaloliomba. Je! Mwaweza kunywea kikombe nitakachonywea mimi? Wakamwambia, Twaweza. 23. Akawaambia, Hakika mtakinywea kikombe changu; lakini kuketi mkono wangu wa kuume na mkono wangu wa kushoto, sina amri kuwapa, bali watapewa waliowekewa tayari na Baba yangu.”

Aidha kumuweka mtu mkno wa kuume maana yake ni kumfanya kuwa msaada wako, na ngao yako au mlinzi wako au mtetezi wako.

Daudi kutokana na kumtegemea kwake mungu na kutembea naye alikuwa na uhakika kuwa Mungu yuko mkono wake wa kuume ndiye anayemshauri, ndiye anayemlinda na ndiye anayemtegemea na kwa sababu hiyo alikuwa na uhakika kuwa hatoondoshwa.

Sitaondoshwa!

Kutokuondoshwa kunakotajwa mahali hapo, maana yake ni kuwa salama, kutokusumbuliwa na maadui, kutokuogopa, kutokutikiswa, kulindwa dhidi ya maadui, kuokuingia matatani, kutokuwamo taabuni Zaburi 10:6, kudumu milele Zaburi 15:5, kutokutetemeshwa Zaburi 46:5, Hutotikisika
Kwa ufupi Daudi anatufundish.

1.       Kumuweka Mungu mbele siku zote za maisha yetu
2.       Kumfanya kuwa ngao yetu
3.       Kumfanya kuwa kinga yetu
4.       Kumfanya kuwa tegemeo letu
5.       Kumfanya kuwa mwangalizi wetu
6.       Kumueshimu na kutembea naye
Na tukiyafanya hayo
1.       Tutakuwa na furaha
2.       Hatutatikisika milele
3.       Mungu atakuwa tegemeo letu na ngao yetu

Taifa lolote, chama chochote, mtu yeyote na taasisi yoyote kama tumedhamiria kumuweka Mungu mbele katika maisha yetu mafanikio ni lazima, furaha ya Bwana ndio nguvu zetu, amani ya Mungu ndio nguvu yetu kubwa sana, kama ukimuweka Mungu, katika mitihani, katika maisha ya kila siku, katika kazi zetu, katika ndoa zetu, katika dua zetu na ibada na maombi yetu kila kitu mfanye Mungu kuwa mkono wako wa kuume na utakuwa msindi na zaidi ya kushinda.

Hivi karibuni katika uchaguzi wa Marekani watu wengi sana walishangazwa na matokeo ya uchaguzi huo uliompa Ushindi mkubwa Muheshimiwa Donal Trump wa Republican na ambaye ni kama alikuwa hakubaliki wala kuongoza katika kura za Maoni, na kuking'oa chama cha Democtratic lakini siri kubwa ya Ushindi wa Trump bila kujali madhaifu yake alimuweka Mungu mbele, wakati Democratic walifanya maovu yafuatayo

1. Waliondoa Amri kumi na alama ya Biblia iliyowekwa na George Washington kutoka ikulu ya Marekani

2. walifungisha ndoa za jinsia moja kwa wafanyakazi wa ikulu ya Marekani
Makamu wa Rais wa Marekani wa Chama cha Democratic Joe Biden akifungisha ndoa ya Mashoga ambao ni wafanyakazi wa ikulu ya Marekani jijini Washington DC

3. Uhusiano na Israel wakati wa utawala wa Obama na Chama chake cha  Democratic ulipoa na ulikuwa wa kinafiki

Sriri ya ushindi wa Donal Trump wa Republican

1. Alumuweka Mungu mbele na kuchukizwa na uovu unaofanyika Washington DC ikulu


2. Ana uhusiano mzuri na Israel na ameahidi kuhamisha ubalozi wa Marekani kutoka Tel Aviv Jaffa kwenda Mji mkuu wa milele wa kiyahudi Yerusalem


3 baada ya kuteuliwa alifanyiwa maombi na watumishi wa Mungu kuonyesha kumtanguliza Mungu katika kila jambo
Katika mifano hii iliyohai utakuwa umejifunza kwamba kumuweka Mungu mbele na kumuheshimu kutakufanya usiondoshwe milele


Rev. Innocent Kamote
“Mkuu wa Wajenzi mwenye hekima”

Jumapili, 30 Oktoba 2016

Bwana atasimama pamoja nawe!


Andiko: 2 Timotheo 4:16-18
 
16. Katika jawabu langu la kwanza hakuna mtu aliyesimama upande wangu, bali wote waliniacha; naomba wasihesabiwe hatia kwa jambo hilo. 17. Lakini Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie Mataifa yote; nami nikaokolewa katika kinywa cha simba. 18. Bwana ataniokoa na kila neno baya, na kunihifadhi hata nifike ufalme wake wa mbinguni. Utukufu una Yeye milele na milele. Amina

Kuokolewa katika kinywa cha Simba 

Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Nyakati za kanisa la kwanza wakristo walipitia vipindi mbalimbali vya Mateso na kulikuwa na aina kuu mbili za maadui, walikuweko maadui wa nje wa kanisa na wa ndani, wote walikuwa ni hatari sana, katika mwaka wa 54-68 baada ya Kristo Mateso ya Kanisa yaliongezeka sana na ndugu wengi katika Kristo waliuawa, kwani mfalme katili zaidi kuliko wote alitawala aliyejulikana kama “NERO CLAUDIUS” wakati huu ulikuwa wakati mgumu sana na hasa kwa viongozi wa Kanisa na washirika pia, Paulo mtume wakati huu aliandika waraka wake wa mwisho ili kumtia moyo Timotheo kuendelea kusimamia kanisa la Mungu bila kuogopa Mateso.

Licha ya Paulo mtume kumtia moyo Timotheo lakini vilevile alijitia Moyo yeye mwenyewe ingawa wakati huu alifahamu kuwa atakufa na kuwa huduma yake ilikuwa imefika mwisho, lakini aliandika waraka huu akiwa kifungoni Rumi na mtawala Nero akiwa hataki kabisa kusikia Injili ikihubiriwa, lakini hata wakristo na ndugu waliokuwa pamoja na Mtume Paulo walikimbia na hakuna mtu alitaka kusimama upande wake hivyo wakati huu Paulo alivunjika moyo na kukata tamaa lakini katika mistari hii hapo juu kuna mambo Muhimu ya kujifunza kutoka kwake

·         Lakini Bwana alisimama Pamoja nami
·         Kuokolewa katika kinywa cha Simba
·         Kuokolewa na kila neno baya.

Lakini Bwana alisimama Pamoja nani

Paulo ingawa alikuwa anajua kuwa mwisho wake umekaribia na kuwa sasa anamiminwa "2Timotheo 4:6-7" hakutaka Timotheo akate tamaa yeye alikuwa na ujuzi kamili ya kuwa Bwana angesimama pamoja naye, Mungu kusimama pamoja naye halikuwa jambo geni katika maisha ya huduma yake, Mara kadhaa kila alipokutana na jambo gumu hata kukaribia kutaka kufa Yesu alikuwa Pamoja naye, Neno KUWA PAMOJA, AU KUWA KARIBU kwa Kiyunani ni “PARISTEMI” kiingereza chake place beside, put at disposal, to present, to stand before, to provide, or come to aid or present offer na standing near, tafasiri rahisi ya Kiswahili ni “KUWEPO KWA KUSUDI LA KUSAIDIA” Neno kama hilo limetumika mara kadhaa katika huduma ya Paulo 

Matendo 23:11Usiku ule Bwana akasimama karibu naye, akasema, Uwe na moyo mkuu; kwa sababu, kama ulivyonishuhudia habari zangu Yerusalemu, imekupasa kunishuhudia vivyo hivyo Rumi nako.”

Matendo 27:23 - 25 “23. Kwa maana usiku huu wa leo malaika wa Mungu yule ambaye mimi ni wake, naye ndiye nimwabuduye, alisimama karibu nami, 24. akaniambia, Usiogope, Paulo, huna budi kusimama mbele ya Kaisari; tena, tazama, Mungu amekupa watu wote wanaosafiri pamoja nawe. 25. Basi, wanaume, changamkeni; kwa sababu namwamini Mungu, ya kwamba yatakuwa vile vile kama nilivyoambiwa.

Ni kawaida ya Mungu kuwepo karibu nasi na kutoa msaada pale tunapohitaji msaada wake ama pale watu wengine wanapokuwa wameshindwa kutoa msaada, Inaonekana wazi kuwa alipokuwa Gerezani Bwana alimtia nguvu, Mungu ataendelea kututia nguvu mpaka dakika ya mwisho

Kuokolewa katika kinywa cha Simba

Paulo mtume anazungumza jambo lingine lililokuwa likiwakabili watu wa nyakati za Kanisa la kwanza na Bwana pia alimuokoa nalo na hii ilikuwa ni kuokolewa katika kinywa cha samba, Nyakati za Kanisa la kwanza wakati wa mateso kulikuwa na samba wa aina tatu waliokuwa wakilisumbua kanisa

·         Simba wa kawaida wanyama – Hawa walikuwa wakitumika kuwatesa wakristo kila mtu aliyesimama kuihubiri injili na kumkiri Yesu kuwa ni Bwana kama akikamatwa auwakikamatwa walitupwa viwanjani na kufunguliwa simba wenye njaa na kuwatafuna wakristo, watu wengi katika maombi yao waliomba waokolewa na simba hao, huenda Paulo mtume pia alimuomba Mungu akaokolewe na simba wakristo wengi waliomba muujiza utokee kama Daniel lakini walitafunwa hivyo hofu kubwa iliingia 

·         Simba aliwakilisha mtawala wa Rumi – Nero Claudio alikuwa ni mtawala katili aliyeuawa wakristo wengi bila Huruma na hivyo wakristo wengi walimuogopa na walitumia jina simba pia kama lugha ya mficho dhidi ya mtawala katili

·         Simba aliwakilisha Shetani  - katika wakati huu kwa kweli shetani alikuwa amekasirika kama simba akipania kabisa kuisambaratisha injili kwa kulisambaratisha kanisa sura ya shetani ilionekana wazi kupitia Nero na simba halisi waliokuwa wakitumiwa kama njia ya mateso 1Petro 5:8Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.” Kukesha ni kuomba Yesu alisema Ombeni ili msije mkaingia majaribuni

Kuokolewa na kila neno baya 

Ni muhimu kufahamu kuwa mitume kamwe hawakuwa wanaogopa kufa lakini walikuwa wanaogopa kusalitiwa na watu wa baya ndani ya injili “deliver me from every evil work” Neno baya au evil katika kiyunani ni “PONEROS  ambalo kiingereza chake ni  The negative moral quality of a person or action opposed to God and his goodness” Paulo alijiombea kuwa asije akamkosea Mungu akapoteza Ufalme wa mbinguni, Paulo alijiombea kumaliza vizuri mwendo wake, kuvipiga vita vilivyo vizuri vya imani, alijiombea asinenwe vibaya asichafuke kwaajili ya injili, Mungu na awe karibu na kila mmoja wetu na kutupa msaada na kutuokoa na kinywa cha simba na kutuokoka na kila neno baya.

Na. Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Alhamisi, 27 Oktoba 2016

Mabaya hayatakupata wewe!



Mstari wa Msingi: Zaburi 91:10
 
Mabaya hayatakupata wewe, wala tauni haitakaribia hema yako!”


Utangulizi:

Zaburi hii ni mojawapo kati ya Zaburi zilizotungwa na kuandikwa na Daudi, Inaonekana wazi kabisa zaburi hii ikizungumzia pigo la ugonjwa wa Tauni, ambayo Mungu aliipiga Israel kuokana na kosa la Daudi kuwahesabia wanajeshi wake na kusahau kuwa ushindi unatoka kwa Mungu, katika wakati huu Mungu aliruhusu malaika wake na kuua watu wapatao 70 elfu kwa muda mfupi sana kutoka Dani mpaka Beersheba na sasa malaika wa Bwana alikuwa anaelekea kuuharibu Yerusalem  unaweza kuona vema habari hii katika 2Samuel 24: 10-17

10. Ndipo moyo wake Daudi ukamchoma baada ya kuwahesabu hao watu. Naye Daudi akamwambia Bwana, Nimekosa sana kwa haya niliyoyafanya; lakini sasa, Ee Bwana, nakusihi uuondolee mbali uovu wa mtumishi wako; kwani nimefanya upumbavu kabisa. 11. Na Daudi alipoondoka asubuhi, neno la Bwana likamjia nabii Gadi, mwonaji wake Daudi, kusema, 12. Nenda, ukanene na Daudi, Bwana asema hivi, Nakuwekea mambo matatu; katika haya uchague moja, nikutendee hilo. 13. Basi Gadi akamwendea Daudi, akamweleza, akamwambia, Basi, miaka saba ya njaa ikujie katika nchi yako? Au miezi mitatu ukimbie mbele ya adui zako, huku wakikufuatia? Au siku tatu iwe tauni katika nchi yako? Fanya shauri sasa, ufikiri, ni jawabu gani nimrudishie yeye aliyenituma. 14. Naye Daudi akamwambia Gadi, Nimeingia katika mashaka sana; basi sasa na tuanguke katika mkono wa Bwana; kwa kuwa rehema zake ni nyingi; wala nisianguke katika mkono wa wanadamu. 15. Basi Bwana akawaletea Israeli tauni tangu asubuhi hata wakati ulioamriwa; nao wakafa watu toka Dani mpaka Beer-sheba sabini elfu. 16. Lakini huyo malaika aliponyosha mkono wake kuelekea Yerusalemu ili auharibu, Bwana akaghairi katika mabaya, akamwambia huyo malaika mwenye kuwaharibu watu, Yatosha, sasa ulegeze mkono wako. Naye yule malaika wa Bwana alikuwako karibu na kiwanja cha kupuria cha Arauna, Myebusi.17. Daudi, alipomwoma malaika aliyewapiga watu, akanena na Bwana, akasema, Tazama, ni mimi niliyekosa, ni mimi niliyepotoka; lakini kondoo hawa, wamefanya nini? Mkono wako na uwe juu yangu, na juu ya nyumba ya baba yangu.”

Baada ya tukio hili la kutisha la watu kupigwa kwa tauni, ambalo linaonekana kumuuma moyo sana Daudi, aliamua kumuomba Mungu na ingawa haiku wazi alikuwa anaombea nini lakini bila shaka alijiombea yeye na wakazi wa mji wa Yerusalem na hasa alikuwa anaomba kwa mji wa Yerusalem na maombi yake yalikuwa na uhakika kuwa Mungu hawezi kuipiga Yerusalem, kutokana na uzoefu wake Daudi anaonyesha mambo ya msingi makuu mawili

1.       Kuutafuta uwepo wa Mungu siku zote za masiha yetu Mstari wa 1-9  Katika Mistari hii Daudi alikuwa anaonyesha umuhimu wa kuwa na uhusiano usioonekana na Mungu “AKETIYE MAHALI PA SIRI PAKE ALIYE JUU ATAKAA KATIKA UVULI WA MWENYEZI” Daudi anasisitiza kuwwa na uhusiano usioonekana kati yetu na Mungu, Ukristo wetu sio tu ule unaoonekana, tunapoomba maombi ya kanisani kwa pamoja ni vema lakini uhusiano wetu na Mungu ni zaidi ya maombi ya kanisani, uko uhusiano wa siri kukaa katika uwepo wake  Mathayo 6:2.-4, 7-8.16-18.  Daudi anaonyesha kuwa mtu atakayedumisha uhusiano wa siri na Mungu na kukaa naye katika namna ambayo wengine wanaweza wasijue, Na kumtegemea Mungu, Mungu atakufanyia haya  Zaburi 91:3-9
·         Atakuokoa na mtego wa Mwindaji
·         Mungu atakufunika kwa mbawa zake  na utapata nkimbilio
·         Hutakuwa na hofu ya aina yoyote
·         Mapigo kama tauni na magonjwa ya kutisha  na vita hutaviogopa
·         Hata watu elfu na kumi elfu walianguka mapigo kwao hayatakukaribia wewe
·         Macho yako yataona mwisho wa wabaya

2.       Mabaya hayatakupata wewe.

Ni muhimu kufahamu kuwa Mabaya yanayozungumzwa hapa kama Pestilence (Magonjwa yasio na tiba), au plague (Mapigo ya hukumu) kama biblia nyingi za kiingereza zilivyoandikwa, Biblia ya kiebrania inatumia neno “NEGA ambalo maana yake ni KURUDIWA, au KUADHIBIWA au KUPUNGUKIWA NA NEEMA YA MUNGU, neno hili lina maana kuwa Mungu hatazuia majaribu yasitupate lakini, lakini Mungu hatatuadhibu, au anapotuadhibu hataacha tuangamiie katika mkono wake, atatutisha lakini hataacha tauni disaster zikaribie Hema yako, yaani amakazi yako hayatapigwa Daudi alikuwa anajua kuwa Mungu anaweza kupiga miji Mingine lakini ni vigumu kuruhusu Yerusalem kupigwa , haitakaribiwa ni makazi yake matakatifu, ukifanya masikani na Mungu, Mungu akifanya makazi kwako hakuna mabaya yatakayokupata, Mungu atatuma malaika zake wakulinde, Yeye ana Rehema nyingi hata anapotuadhi,

Mungu hatatuadhibu
Mungu hahatuondolea neema
Hatatupungukia
Hatoondoa rehema zake
Ikiwa tutaimarisha uhusiano wetu wa siri na yeye
Ikiwa tutautafuta uwepo wake, atatuhifadhi, hata wengine wakianguka ka maelfu yao sisi tutabaki salama
Ikiwa Mungu aliwaokoa watu wengi sana katia Biblia wasipatwe na mabaya kuna ushahidi wa
 kutosha kimaandiko kwamba Mungu hatakuacha upatwe na Mabaya 

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa Wajenzi mwenye hekima!