Jumapili, 5 Oktoba 2025

Namjua anayeishika kesho!


Mathayo 6:31-34 “Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”



Utangulizi:

Mojawapo ya tatizo kubwa la kiroho na kisaokolojia linalowakumba wanadamu ni pamoja na tatizo la kuogopa kesho au wakati ujao, tatizo la kuhofia kuhusu kesho au wakati ujao kisakolojia linaitwa “Chronophobia” au “time anxiety”  hofu ya wakati hususani wakati ujao ambayo kitaalamu inafafanuliwa kama “a type of anxiety that involves  worrying about tomorrow or future”  yaani ni aina ya msongo wa mawazo unaohusisha kuogopa au hofu kuhusu kesho au wakati ujao,  Neno Chronophobia ni muunganiko wa maneno mawili ya kiyunani “Chronos” yaani muda na “phobos” yaani hofu kwa hiyo wanadamu wengi wanasumbuliwa na hofu kubwa sana kuhusu itakuwaje kesho, katika Afrika wanawake wengi huongoza kwa hofu hii na ndio maana wengi huogopa kufiwa na waume zao na utawasikia wakisema kuna leo na kesho hali itakuwaje? Na wakati mwingine watu huogopa kuwa huenda kuna jambo baya litawatokea na watu wengi wanaogopa magumu, wengine huogopa muda kwa kufungwa gerezani, masikini huogopa kwamba kesho itakuwaje, matajiri huogopa kufilisika, wenye vyeo huogopa kuviachia, wafanya biashara huogopa hasara, Wengine huogopa muda kwa kufikiri kuwa wamekawia katika maisha, Tatizo la hofu linaweza kuwako katika pembe nyingi,  Ingawa tatizo hili linaweza kuwa la kawaida lakini kuna wanadamu wengine tatizo hili huwa kubwa zaidi kwao na linaweza kufikia hatua likaathiri Imani yao na ni kwa sababu hii Neno la Mungu linamtaka kila mmoja wetu kutokuogopa kuhusu kesho au wakati ujao na badala yake kumtegemea Mungu.

Mathayo 6:34 “Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”

Kwa nini neno la Mungu linatuonya kutokuogopa kesho? Hii ni kwa sababu Mungu ndiye anayeishika kesho, kesho yako na wakati wako ujao uko mikononi mwa Mungu na ukilitambua hilo huwezi kuogopa lolote, Kwa msingi huu basi leo tutachukua muda kujifunza kwa kina na mapana na marefu juu ya somo hili “Namjua anayeishika kesho” kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Hofu ya wanadamu kuhusu kesho.

·         Neno la Mungu linasemaje kuhusu kesho.

·         Namjua anayeishika kesho.


Hofu ya wanadamu kuhusu kesho.

Mathayo 6:25-34 “Kwa sababu hiyo nawaambieni, Msisumbukie maisha yenu, mle nini au mnywe nini; wala miili yenu, mvae nini. Maisha je! Si zaidi ya chakula, na mwili zaidi ya mavazi? Waangalieni ndege wa angani, ya kwamba hawapandi, wala hawavuni, wala hawakusanyi ghalani; na Baba yenu wa mbinguni huwalisha hao. Ninyi je! Si bora kupita hao? Ni yupi kwenu ambaye akijisumbua aweza kujiongeza kimo chake hata mkono mmoja? Na mavazi, ya nini kuyasumbukia? Fikirini maua ya mashamba, jinsi yameavyo; hayafanyi kazi, wala hayasokoti nami nawaambia, ya kwamba hata Sulemani katika fahari yake yote hakuvikwa vizuri kama mojawapo la hayo. Basi, ikiwa Mungu huyavika hivi majani ya kondeni, yaliyopo leo, na kesho hutupwa kalibuni, je! Hatazidi sana kuwavika ninyi, enyi wa imani haba? Msisumbuke, basi, mkisema, Tule nini? Au Tunywe nini? Au Tuvae nini? Kwa maana hayo yote Mataifa huyatafuta; kwa sababu Baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa. Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.”

Katika hutuba yake ya mlimani Mwalimu wetu mkuu na mwokozi wa maisha yetu Yesu Kristo hakuacha kuzungumzia swala zima la hofu ya wanadamu kuhusu kesho, wanadamu wengi masikini kwa matajiri wote wanakabiliwa na hofu kuwa itakuwaje kesho au maisha ya baadaye, hofu hii inaweza ikawa sio tu kwa mahitaji ya kawaida nitakula nini na nitavaa nini, lakini inaweza kuwa zaidi ya hapo, itakuwaje nikifiwa na mume, itakuwaje nikifukuzwa kazi, itakuwaje nikifilisika, itakuwaje nikidaiwa kodi, itakuwaje nikiachwa! Itakuwaje nikiugua? Itakuwaje nikishindwa uchaguzi, itakuwaje nikifeli, nini kitatokea, itakuwaje uchumi ukiyumba? Na kadhalika hofu hii ni tatizo kubwa la kiroho na kisaikolojia na Mungu analijua vema, anajua kuwa hofu hizi zinaweza kumpelekea mtu akakosa Amani, akapoteza usingizi, na hatimaye akapoteza Imani na matumaini na Ndio maana Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kwamba hawapaswi kuogopa kuhusu kesho kwa sababu Baba wa mbinguni anajua mahitaji yetu na ndiye anayeishika kesho!.

Neno la Mungu linasemaje kuhusu kesho.

Neno la Mungu linatufundisha ya kuwa ni Mungu ndiye mwenye uwezo wa kudhibiti kesho ya kila mmoja wetu, na hakuna mwanadamu ambaye anaweza kujisumbua kuhusu kesho yake na akafanikiwa bila neema na kibali cha Mungu, hofu yako wasiwasi wako na hata maandalizi yako hayawezi kukuhakikishia kesho iliyo salama na kamili bila Mungu, kwa sababu kesho haiko katika mikono ya mwanadamu bali iko katika mikono ya Mungu mwenyewe, wako watu ambao walijisumbua sana kuhusu kesho na neno la Mungu likawatumia kama mifano ya kutuonya kuwa huwezi kufanya kitu kuhusu kesho na ukajithibitishia usalama bila ya Mungu! Kesho iko kwenye mapenzi ya Mungu! Mungu ndiye anayeishika kesho ili mwanadamu asiwe na kiburi, Tancredo Neves alikuwa mgombea urais wa Brazili mwaka 1985 wakati wa kampeni zake alisema nikipata kura 500,000 tu kutoka kwenye chama changu hakutakuwa na wa kuzuia nisiwe Rais hata Mungu hataweza kunizuia, Kwa kweli alipata kura hizo na akashinda uchaguzi, lakini aliugua ghafla na utumbo ulijikunja akafariki siku moja kabla ya kuapishwa kuwa raisi Tarehe 21/4/1985. Lazima kila mmoja kwa unyenyekevu akubali kuwa kesho iko mikononi mwa Mungu na sio mikononi mwa mwanadamu.

Yakobo 4:13-15 “Haya basi, ninyi msemao, Leo au kesho tutaingia katika mji fulani na kukaa humo mwaka mzima, na kufanya biashara na kupata faida; walakini hamjui yatakayokuwako kesho. Uzima wenu ni nini? Maana ninyi ni mvuke uonekanao kwa kitambo, kisha hutoweka. Badala ya kusema, Bwana akipenda, tutakuwa hai na kufanya hivi au hivi.”

Luka 12:15-20 “Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo. Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana; akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu. Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu. Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi. Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?               

Maandiko yanatuonya wazi kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kudai kwa sababu zozote zile kwamba anaweza kuwa na uhakika wa kesho, na hata hivyo hatupaswi kuiogopa kesho pia, lakini kesho iko katika mikono ya Mungu na kwa sababu hiyo neno la Mungu linatuonya kuiacha hofu ya kesho katika mikono ya Mungu, badala yake tunatiwa moyo kumuamini Mungu na kumtegemea yeye kwaajili ya mahitaji yetu ikiwepo kesho yetu,  Neno la Mungu halitutii moyo kuogopa kuhusu kesho kwaajili ya mahitaji yetu, wala halituhakikishii kuwa tunaweza kutengeneza usalama wetu wa kesho kwa kujilimbikizia ua kujiwekea akiba au kwa kutafuta sana kunakoambatana na hofu ya kesho na pia hakuna mwanadamu awaye yote wa ngazi yoyote ile anayeweza kujithibitishia kuwa na kesho iliyo njema nje ya uweza na mamlaka ya Mungu Mwenyewe. Kwa sababu hiyo hatupaswi kujivuna au kujisifia lolote kuhusu kesho!

Mithali 27:1-2 “Usijisifu kwa ajili ya kesho; Kwa maana hujui yatakayozaliwa na siku moja. Mwingine na akusifu wala si kinywa chako mwenyewe; Mtu mgeni wala si midomo yako wewe.”

Neno la Mungu linaonyesha wazi kuwa mwenye kesho ni Mungu tu, siku moja tu inaweza kuzaa jambo na likabadilisha kila kitu katika maisha yetu, kwa sababu hiyo hatuna budi kuishi kwa unyenyekevu na kwa kumtegemea Mungu pake yake, hatupaswi kuiogopa kesho kama tunamwamini Mungu na wala hatupaswi kujihami kuhusu kesho kama iko mikononi mwa Mungu hii maana yake ni nini? Maana yake ni kuwa Mungu ndiye anayeishika kesho na ukimjua yeye hutaweza kuishi maisha ya hofu ya aina yoyote ile, ukiwa na uhakika kuwa kesho yako iko kwake!

Namjua anayeishika kesho.

Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna hofu wala woga utakaokutawala endapo tu utagundua kuwa ni Mungu ndiye anayeishikilia kesho yako, Mungu anaweza kubadilisha mambo kwa usiku mmoja tu, ukitambua kuwa ni Mungu ndiye anayeishikilia kesho yako hakuna mwanadamu atakayekutisha wala kukutetemesha kuhusu yajayo, kesho yako haiko katika mikono ya wanadamu, iko katika mikono ya Mungu, ukimjua yeye anayeshika kesho hautaogopa mabadiliko ya aina yoyote ile, utamtegemea yeye ambaye ni ngome iliyo imara  naye hatakuangusha, Mwandishi wa Zaburi hakuwahi kuogopa mabadiliko yoyote yale kwa sababu alikuwa anamjua Mungu na kutambua ya kuwa ndiye anayeshikilia kila kitu kwa hiyo lolote litokee haliwezi kututisha kwa sababu yeye Mungu ndiye mwenye kesho yake!

Zaburi 46:1-7 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema. Mataifa yalighadhibika, falme zikataharuki; Alitoa sauti yake, nchi ikayeyuka. Bwana wa majeshi yu pamoja nasi, Mungu wa Yakobo ni ngome yetu.”

Mungu wetu ni Mungu asiyebadilika, Yeye ni Yeye yule jana leo na hata milele, Yu hai, na bado anaendelea kubarikia watu wake, anaendelea kulinda watu wake, anakomboa watu wake, bado ni mtawala wa mbingu na nchi majira na nyakati, ziko mkononi mwake, hajawahi kupoteza nguvu zake wala uwezo wake Yeye bado ni Bwana Mungu aliyeziumba mbingu na nchi na bahari na vyote vilivyomo, Ndiye aliyeigawa bahari ya Shamu, akamzika Farao na majeshi yake, akawalisha watu wake kwa mana, akawanywesha maji kutoka katika mwamba, akawapigania dhidi ya adui zao, akatimiza ahadi zake kwa kuwapa nchi ya Mkanaani, nguvu zake hazijawahi kupungua, alimfufua Lazaro, alimtoa Petro na Paulo na Sila gerezani, hakuna nguvu inaweza kupingana naye, Yeye ndiye anayeishika kesho, kesho yako haiko kwa waganga wa kienyeji, kesho yako haiko kwa bosi wako, kesho yako haiko kwa wenye mamlaka au cheo, kesho yako haiko kwa wachawi, kesho yako haiko kwa wapiga ramli kesho yako inashikwa na Mungu aliye hai, muumba wa mbingu na nchi, uaminifu wake unazidi kizazi hata kizazi na yeye anatuwazia mema na yeye habadiliki ni Yeye Yule jana leo na hata milele, Hakuna mtu anayeweza kuichafua kesho yako, hakuna mtu anaweza kuizibia kesho yako, kesho yako iko katika mikono ya Mungu, ukimjua anayeishika kesho yako hutaogopa, hakuna wa kukurudisha nyuma, tunaweza tusijue lolote kuhusu kesho, lakini tunaweza kumjua anayeishika kesho! Naye ni mwenye nguvu!

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako maana yake unaweza kumuamini yeye kuhusu kesho yako na kutokuogopa wakati ujao ukijua ya kuwa anatuwazia mema na ana mpango mzuri kwaajili yako:-

Yeremia 29:11 “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako maana yake hupawi kuogopa endapo unazingirwa na maadui pande zote na wanakukusudia mabaya hawawezi kutimiza mpango wao kwa sababu mpango wao sio mkuu kama wa yule anayeishika kesho:-

Zaburi 31:13-15 “Maana nimesikia masingizio ya wengi; Hofu ziko pande zote. Waliposhauriana juu yangu, Walifanya hila wauondoe uhai wangu. Lakini mimi nakutumaini Wewe, Bwana, Nimesema, Wewe ndiwe Mungu wangu. Nyakati zangu zimo mikononi mwako; Uniponye na adui zangu, nao wanaonifuatia.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako maana yake ni yeye anayeweza kukulinda kwa nguvu zake na mkono wake kiasi kwamba hutakuwa na lolote la kuogopa, hutaogopa wachawi, hutaogopa Shetani, hutaogopa, laana, hutaogopa wanaoukutishia maisha Imani na tumaini litakuwa kubwa kwa Bwana Mungu wako na hutaogopa vita wala majeshi makubwa ya adui yajapojipanga kupigana nawe kwa sababu yuko anayeishika kesho yako!

Zaburi 27:1-5 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake. Mradi atanisitiri bandani mwake siku ya mabaya, Atanisitiri katika sitara ya hema yake, Na kuniinua juu ya mwamba.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yetu tunajengewa uhakika na matumaini ya kuwa anajishughulisha sana na mambo yetu, atakutana na mahiaji yetu, na tutaishi kwa kujiamini bila kuogopa tukijua ya kua kesho ni ya Baba mwenye upendo na rehema ataishughulikia, sina ada italipwa, sina chakula nitakula, sina nguo nitavaa, sina raha nitapewa, nina mizigo itapumzishwa, nina madeni yatalipwa, sioni njia ataniongoza, naona giza atakuwa nuru!

Kumbukumbu 8:11-16 “Jihadhari, usije ukamsahau Bwana, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na sheria zake, ninazokuamuru leo. Angalia, utakapokuwa umekula na kushiba, na kujenga nyumba nzuri na kukaa ndani yake; na makundi yako ya ng'ombe na kondoo yatakapoongezeka, na fedha yako na dhahabu yako itakapoongezeka, na kila kitu ulicho nacho kitakapoongezeka; basi hapo moyo wako usiinuke, ukamsahau Bwana, Mungu wako, aliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa; aliyekuongoza katika jangwa lile kubwa lenye kitisho, lenye nyoka za moto na nge, nchi ya kiu isiyokuwa na maji; aliyekutolea maji katika mwamba mgumu, aliyekulisha jangwani kwa mana, wasiyoijua baba zako; apate kukutweza, apate kukujaribu, ili kukutendea mema mwisho wako.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yako, maana yake ni kuwa haitakuja utishike na kuweweseka kwa sababu yeye yuko siku zote, alikuwako tangu mwanzo, habadiliki, hageuki wala hana kigeugeu, wala kwake hakuna kubadilika badilika Yeye ni Yeye yule jana leo na hata milele  Waebrania 13:8 “Yesu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele.”

Yakobo 1:17 “Kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili, hutoka juu, hushuka kwa Baba wa mianga; kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeuka-geuka.”

Kama Mungu ndiye anayeishika kesho yetu basi ni wazi kuwa hakuna jambo lolote lile linaloweza kututenga na upendo wake, hakuna wa kutuhukumu, hakuna wa kututishia maisha, hakuna wa kututishia kuhusu kesho, hakuna wa kutupunguzia kitu, hakuna wa kutupokonya ushindi, hakuna wa kututisha kwa maana kesho iko mikononi mwake

Warumi 8:31-39 “Basi, tuseme nini juu ya hayo? Mungu akiwapo upande wetu, ni nani aliye juu yetu? Yeye asiyemwachilia Mwana wake mwenyewe, bali alimtoa kwa ajili yetu sisi sote, atakosaje kutukirimia na mambo yote pamoja naye? Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 28 Septemba 2025

Kuishi zaidi ya maneno!


Zaburi 109:1-3. “Ee Mungu wa sifa zangu, usinyamaze, Kwa maana wamenifumbulia kinywa; Kinywa cha mtu asiye haki, cha hila, Wamesema nami kwa ulimi wa uongo.  Naam, Kwa maneno ya chuki wamenizunguka, Wamepigana nami bure.”




Utangulizi:

Wote tutakuwa tunafahamu nguvu kubwa iliyoko katika maneno, maneno yana nguvu!, yana nguvu kubwa kiasi cha kuweza kujenga, yana nguvu kubwa kiasi cha kuweza kubomoa, yana uwezo wa kuponya, yana uwezo wa kujeruhi, yana uwezo wa kutia moyo, yana uwezo wa kuvunja moyo, Neno la Mungu linasema kuwa maneno yana uwezo wa kuleta mauti au kuleta uzima unaona!

Mithali 18:20-21 “Tumbo la mtu litajazwa matunda ya kinywa chake; Atashiba mazao ya midomo yake. Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake.”

Leo nataka tuzungumzie kile ambacho Roho Mtakatifu anataka nikizungumzie kwaajili ya watu wake anaotaka kuwasaidia na hii ni kuishi zaidi ya maneno hasi, Ujumbe huu ulinijia kwa lugha ya kiingereza “Beyond the negative words” lakini mimi nahudumia watu wanaozungumza Kiswahili, kwa hiyo nimeUita ujumbe huu Kuishi zaidi ya maneno!, Kila mtu aliyemwamini Mungu anapaswa kuishi zaidi ya maneno, hususani maneno hasi yaani yale yanayokuja kwetu kupitia Shetani na mawakala wake ambao wanatutupia maneno ili tuishi kwa mipaka, ili tukate tamaa, ili tuvunjike moyo, ili tushindwe, ili tuogope, ili tusiendelee, ili tutawalike, ili kutuonea na kutujeruhi, ili kuondoa ujasiri wetu, ili ususie na kadhalika, Roho Mtakatifu amenituma nikutie moyo kwamba unaweza kuishi zaidi ya maneno, na kuwa wako watakatifu waliotutangulia ambao kimsingi walishi zaidi ya maneno na wakapata ushindi na kusonga mbele katika maisha yao ya kawaida na ya kiroho Ishi zaidi ya maneno, Tutajifunza somo hili kuishi zaidi ya maneno kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·         Maneno ya kuvunja moyo.

·         Wanadamu na maneno ya kuvunja moyo.

·         Kuishi zaidi ya maneno


Maneno ya kuvunja moyo.

Mojawapo ya namna na jinsi Shetani anavyowashambulia watu wa Mungu ni pamoja na kuwashambulia kwa maneno, hususani maneno ya kuvunja moyo, Shetani anaweza kuwatumia watu yaani mawakala wake, na wanaweza kuwa na sura yoyote ile, wanaweza kuwa ni waamini wenzako, waimbaji wenzako katika kwaya, watumishi wenzako, wakristo wenzako ndugu au watu wa karibu na wakati mwingine watu wa ulimwengu huu watakurushia maneno ya kukuvunja moyo, ili ujihoji kama unastahili, uwe na mashaka, uwe na wasiwasi hata kuhusu ahadi za Mungu, watakuhukumu, watakujaza woga na hofu, watashambulia imani yako, watakuvunja moyo, wataiba furaha yako. Shetani anaweza kutumia marafiki, maadui na jamii na wakati mwingine hata moyoni mwako unaweza ukajihukumu! Kwamba labda wewe sio bora sana, wewe sio mwema sana, labda wewe huwezi kufanikiwa, hutoboi, au Mungu amekuacha, maneno haya yatakushambulia kama mshale yakitafuta kukuvunja moyo na kukukatisha tamaa na unaweza hata kudhani kuwa labda wokovu kwako hauna maana au Mungu hana msaada kwako, Kristo Yesu alishambuliwa kwa maneno wakati akiwa msalabani katika hali ya mateso.

Luka 23:35-37 “Watu wakasimama wakitazama. Wale wakuu nao walikuwa wakimfanyia mzaha, wakisema, Aliokoa wengine; na ajiokoe mwenyewe, kama ndiye Kristo wa Mungu, mteule wake. Wale askari nao wakamfanyia dhihaka, wakimwendea na kumletea siki, huku wakisema, Kama wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi, ujiokoe mwenyewe.”

Luka 23:38-39 “Na juu yake palikuwa na anwani; HUYU NDIYE MFALME WA WAYAHUDI. Na mmoja wa wale wahalifu waliotungikwa alimtukana, akisema, Je! Wewe si Kristo? Jiokoe nafsi yako na sisi.”

Mathayo 27:39-43 “Nao waliokuwa wakipita njiani wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa vyao, wakisema, Ewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe nafsi yako; ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu, shuka msalabani. Kadhalika na wale wakuu wa makuhani wakamdhihaki pamoja na waandishi na wazee, wakisema, Aliokoa wengine, hawezi kujiokoa mwenyewe. Yeye ni mfalme wa Israeli; na ashuke sasa msalabani, nasi tutamwamini. Amemtegemea Mungu; na amwokoe sasa, kama anamtaka; kwa maana alisema, Mimi ni Mwana wa Mungu.”

Neno la Mungu linaonya na kukemea, likitaka wanadamu wawe na matumizi mazuri ya ulimi yaani maneno kwani yanaweza kusababisha madhara makubwa sana, uharibifu wa aina nyingi sana duniani na hata vita kubwa duniani zilianza na ulimi tu, talaka, majungu makazini, kufukuzwa watu kazi, kuharibia wengine maisha kumesababishwa kwa kiwango kikubwa na ulimi, yaani maneno maneno yameumiza wengi, yameua wengi, yamefarakanisha wengi, yamechongea wengi na kuleta uharibifu katika maisha ya wengi kiroho, kiakili, kiuchumi, kisaikolojia na kadhalika.

Yakobo 3:5-6 “Vivyo hivyo ulimi nao ni kiungo kidogo, nao hujivuna majivuno makuu. Angalieni jinsi moto mdogo uwashavyo msitu mkubwa sana. Nao ulimi ni moto; ule ulimwengu wa uovu, ule ulimi, umewekwa katika viungo vyetu, nao ndio uutiao mwili wote unajisi, huuwasha moto mfulizo wa maumbile, nao huwashwa moto na jehanum.”             

Wanadamu na maneno ya kuvunja moyo

Hebu tuwe wakweli tu maneno ya kuvunja moyo ni sehemu ya maisha ya Mwanadamu, tunaishi katika ulimwengu uliooza na kuharibikwa kwa dhambi, kwa sababu hiyo aidha watu kwa kupenda au hata kwa kutokupenda, kwa kudhamiria au hata kwa kutokudhamiria, watapiga domo, watapiga umbeya, wanadamu ni wambeya wanadamu ni waongo wanadamu wana maneno yaliyojaa sumu, wanadamu wana maneno, wanadamu ni wazushi, watu wana maneno watu wanazungumza bhana maneno ya kuumiza, maneno ya kubomoa, maneno ya kukosesha watu wanasengenya, ukiwa mwema utasengenywa, ukiwa mbaya utasengenywa, vyovyote uwavyo kila mwanadamu anasemwa mahali fulani na wakati mwingine wanazungumza maneno yanayoumiza sana, wanazungumza maneno ya kuharibu, wanazungumza vitu vya kuharibu usalama wako, wanakuweka uchi, wanakuwekea mipaka, wanaharibu maisha, na wakati mwingine wanatumiwa wazi wazi na adui Shetani kuumiza na kukatisha tamaa wengine na hata waliookoka huingia katika mtego huu na hata sisi wenyewe tunaweza kujifikiri vibaya kama hatutaacha kujitazama katika mtazamo wa Mungu, kwa ujumla ndimi za wanadamu zimejaa sumu, yaani watu wana maneno yenye madhara na wanaweza kuzungumza bila kujifikiri, hawafikiri madhara, hawafikiri mauti wanatumiwa tu na yule shetani, ukitenda mema watasema, ukitenda mabaya watasema ni mawakala wa Shetani.

Zaburi 140:1-3. “Ee Bwana, uniokoe na mtu mbaya, Unihifadhi na mtu wa jeuri. Waliowaza mabaya mioyoni mwao, Kila siku huondokesha vita. Wamenoa ndimi zao kama nyoka, Sumu ya fira i chini ya midomo yao.”

Kwa hiyo utakubaliana nami kuwa maneno ya kukatisha tamaa ni sehemu ya maisha ya kila siku na ya kawaida katika ulimwengu huu wa watu wasio wakamilifu, Mwandishi wa Zaburi amewahi kulalamika kuwa wakati mwingine hata rafiki zetu wa karibu wanaweza kutunenea mabaya, watu tunaosali nao pamoja, marafiki na hata ndugu, yaani yeyote anaweza kutumiwa! Haijalishi ni nani!

Zaburi 55:12-14 “Kwa maana aliyetukana si adui; Kama ndivyo, ningevumilia. Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye; Kama ndivyo, ningejificha asinione. Bali ni wewe, mtu mwenzangu, Rafiki yangu, niliyejuana nawe sana. Tulipeana shauri tamu; na kutembea Nyumbani mwa Mungu pamoja na mkutano.”

Warumi 3:10-14 “kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Hakuna mwenye haki hata mmoja. Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja. Koo lao ni kaburi wazi, Kwa ndimi zao wametumia hila. Sumu ya fira i chini ya midomo yao.Vinywa vyao vimejaa laana na uchungu.”

Endapo hutajifunza na kuelewa kwa kina na mapana na marefu Neno la Mungu unaweza kusumbuka sana, lakini ukielewa kuwa tuko Duniani na Dunia imejaa wazushi na waongo na waharibifu na wasema vibaya na waumizaji hutaweza kuishi zaidi ya maneno “Beyond the negative words” Lakini ashukuriwe Mungu atupaye kushinda Roho Mtakatifu atatuwezesha kuishi zaidi ya maneno, Maneno ni aina ya vita, ambayo Shetani anaitumia, kama ilivyo katika ulimwengu wa kawaida mabondia na wapiganaji kabla ya kupigana huanza na tambo za maneno au propaganda hii ni vita ambayo watakatifu waliotutangulia waliifahamu na kujua namna na jinsi ya kuipigana, kwa nini Shetani hutumia vita vya maneno kuwashambulia watu wa Mungu hii ni kwa sababu:-

-          Unashambuliwa ili ujisahau kuwa wewe ni nani – anataka usahahu kuwa wewe ni chagua la Mungu na Mungu amekuumba kwa jinsi ya ajabu, amekuumba kwa kusudi na kwa ushindi na kukuita kwenye kusudi lake kwa sababu hiyo ni lazima Shetani akushambulie, akushitaki.

 

Zaburi 139:13-14Maana Wewe ndiwe uliyeniumba mtima wangu, Uliniunga tumboni mwa mama yangu, Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa Kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, Na nafsi yangu yajua sana,”

 

1Petro 2:9-10 “Bali ninyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu; ninyi mliokuwa kwanza si taifa, bali sasa ni taifa la Mungu; mliokuwa hamkupata rehema, bali sasa mmepata rehema.”

 

-          Unashambuliwa ili utoke katika kusudi la Mungu – Maneno yanaweza kukutia mashaka na kukufadhaisha ili ikiwezekana yakutoe katika mpango na mapenzi ya Mungu au kusudi ambalo kwalo Mungu amekuitia

 

Nehemia 4:1-3 “Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe.”              

 

-          Unashambuliwa kwaajili ya kuidhoofisha Imani – Maneno yanaweza kutumika kama njia ya kukuvunja moyo, ili ushindwe kulitimiza kusudi la Mungu kwa Imani na kurudi katika mashaka Israel walipokuwa wanakaribia kuingia katika inchi ya Kanaani wapelelezi kumi walitumiwa na shetani wakwavunja moyo watu kwa maneno yao na watu wakakubali kuvunjika moyo.

 

Hesabu 13:31-33Bali wale watu waliopanda pamoja naye wakasema, Hatuwezi kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi. Wakawaletea wana wa Israeli habari mbaya ya ile nchi waliyoipeleleza, wakasema, Ile nchi tuliyopita kati yake ili kuipeleleza, ni nchi inayowala watu wanaoikaa; na watu wote tuliowaona ndani yake ni watu warefu mno. Kisha, huko tuliwaona Wanefili, wana wa Anaki, waliotoka kwa hao Wanefili; tukajiona nafsi zetu kuwa kama mapanzi; nao ndivyo walivyotuona sisi.”

 

Hesabu 14:1-3 “Mkutano wote wakapaza sauti zao wakalia; watu wakatoka machozi usiku ule. Kisha wana wa Israeli wote wakamnung'unikia Musa na Haruni; mkutano wote wakawaambia, Ingekuwa heri kama tungalikufa katika nchi ya Misri, au, ingekuwa heri kama tungalikufa katika jangwa hili. Mbona Bwana anatuleta mpaka nchi hii ili tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu watakuwa mateka; je! Si afadhali turudi Misri?”                           

Kuishi zaidi ya maneno;

Ili kila mtu duniani awe na amani ya kweli na ushindi dhidi ya maneno ya kukatisha tamaa na kuumiza moyo tunayokuta nayo duniani basi inatulazimu kuishi zaidi ya maneno hasi, na ili uweze kuishi zaidi ya maneno unapaswa kuishi kwa kuliangalia Neno la Mungu linasema nini juu yako na sio kile watu wanachokisema, wewe na mimi sio matokeo ya kile watu wanasema wewe na mimi ni matokeo ya kile Mungu anachokisema Neno la Mungu lina nguvu kuliko nyundo ivunjayo mawe vipande vipande, Neno la Mungu ni moto mkali wenye nguvu ya kuumba!

Yeremia 23:28-29 “Nabii aliye na ndoto, na aseme ndoto yake; na yeye aliye na neno langu, na aseme neno langu kwa uaminifu. Makapi ni kitu gani kuliko ngano? Asema Bwana. Je! Neno langu si kama moto? Asema Bwana; na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?”

Watakatifu waliopata ushindi katika kila vita waliyokutana nayo ya maneno walijikita katika Neno la Mungu na ujuzi wao kuhusu Mungu, ukawafanya wawe washindi, wale walioogopa maneno walinywea lakini wale walioliangalia neno la Mungu na kile Mungu ameahidi hawakuogopa

a.       Daudi na Gloiath – Walipigana vita vya maneno kwanza kabla ya kuingia katika vita halisi, Goliathi aliogopewa sana sio tu kwa sababu ya ukubwa wake lakini pia kwa sababu ya maneno yake hasi ambayo yalitisha sana na watu wote wakaogopa na pia walimkimbia ilikuwa ni aibu kubwa sana. Lakini Daudi alifahamu namna ya kushughulika naye. Daudi alikutana na maneno mengi ya kukatisha tamaa lakini yeye aliishi zaidi ya maneno! Ona:-

 

1Samuel 17: 1-11 “Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti.Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

 

1Samuel 17:24-28 “Na watu wote wa Israeli walipomwona yule mtu wakakimbia, wakaogopa sana. Watu wa Israeli wakasema, Je! Mmemwona mtu huyu aliyepanda huko? Hakika ametokea ili awatukane Israeli; basi, itakuwa, mtu yule atakayemwua, mfalme atamtajirisha kwa utajiri mwingi, naye atamwoza binti yake, na kuifanya mbari ya baba yake kuwa huru katika Israeli. Daudi akaongea na watu waliosimama karibu, akisema, Je! Atafanyiwaje yeye atakayemwua Mfilisti huyo, na kuwaondolea Israeli aibu hii? Maana Mfilisti huyu asiyetahiriwa ni nani hata awatukane majeshi ya Mungu aliye hai? Nao watu wakamjibu vivyo hivyo, wakisema, Ndivyo atakavyofanyiwa mtu yule atakayemwua. Naye Eliabu, mkubwa wake, alisikia hapo alipoongea na watu; na hasira yake Eliabu ikawaka juu ya Daudi, akasema, Mbona wewe umeshuka hapa? Na kondoo wale wachache umemwachia nani kule nyikani? Mimi nakujua kiburi chako, na ubaya wa moyo wako; maana umeshuka ili upate kuvitazama vita.”

 

1Samuel 17:32-33 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake.”

 

1Samuel 17:37 “Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe.”

 

1Samuel 17:42-46Hata Mfilisti alipotazama huku na huku, akamwona Daudi akamdharau; kwa kuwa ni kijana tu mwekundu, tena ana sura nzuri. Mfilisti akamwambia Daudi, Je! Mimi ni mbwa hata umenijia kwa fimbo? Mfilisti akamlaani Daudi kwa miungu yake. Mfilisti akamwambia Daudi, Njoo huku kwangu; nyama yako nitawapa ndege wa angani na wanyama wa mwituni. Ndipo Daudi akamwambia yule Mfilisti, Wewe unanijia mimi na upanga, na fumo, na mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la Bwana wa majeshi, Mungu wa majeshi ya Israeli uliowatukana.Siku hii ya leo Bwana atakuua mkononi mwangu, nami nitakupiga, na kukuondolea kichwa chako, nami leo nitawapa ndege wa angani na wanyama wa nchi mizoga ya majeshi ya Wafilisti, ili kwamba dunia nzima wajue ya kuwa yuko Mungu katika Israeli.”

 

Daudi ni mfano wa watu ambao hawakukubali kuishi kwa maneno ya kukatisha tamaa kama angeyasikiliza aibu kubwa ingelipata taifa zima la Israel, lakini aliishi zaidi ya maneno alimkiri Mungu mwenye nguvu aliyeweza kumuokoa yeye na wanyama wakali wakiwepo simba na dubu akitambua ya kuwa Mungu huyu na neno lake ana nguvu kuliko maneno na umbile la adui

 

b.      Hanna na Penina – Hana alipata maneno ya kuumiza na kukatisha tamaa kutoka kwa Penina kwa sababu Hana hakuwa na watoto, alichokozwa na kusemwa vibaya kwa maneno hasi Penina alifanya hivyo mwaka kwa mwaka mpaka Hana aliacha kula na kusikitishwa sana naye

 

1Samuel 1:6-7 “Ila mwenzake humchokoza sana, hata kumsikitisha, kwa sababu Bwana alikuwa amemfunga tumbo. Tena mumewe akafanya hivyo mwaka kwa mwaka, hapo yule mwanamke alipokwea kwenda nyumbani kwa Bwana, ndivyo yule alivyomchokoza; basi, kwa hiyo, yeye akalia, asile chakula.”

 

Hata pamoja na maneno ya kuumiza na kukatisha tamaa Hana alifamya uamuzi wa kuishi zaidi ya maneno yeye aliongeza kasi kwenye maombi na kumlilia Mungu na Mungu hakumuangusha kwani alimjibu na kumpa mtoto Samuel na watoto wengine, kinywa cha Hana kilizungumza lugha nyingine kwa furaha

 

1Samuel 2:1-10 “Naye Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka katika Bwana, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia wokovu wako; Hakuna aliye mtakatifu kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna mwamba kama Mungu wetu. Msizidi kunena kwa kutakabari hivyo; Majivuno yasitoke vinywani mwenu; Kwa kuwa Bwana ni Mungu wa maarifa, Na matendo hupimwa na yeye kwa mizani. Pinde zao mashujaa zimevunjika, Na hao waliojikwaa wamefungiwa nguvu. Walioshiba wamejikodisha ili kupata chakula, Na hao waliokuwa na njaa wamepata raha. Naam, huyo aliyekua tasa amezaa watoto saba, Na yeye aliye na wana wengi amedhoofika. Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu. Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake. Yeye atailinda miguu ya watakatifu wake; Bali waovu watanyamazishwa gizani, Maana kwa nguvu hakuna atakayeshinda; Washindanao na Bwana watapondwa kabisa; Toka mbinguni yeye atawapigia radi; Bwana ataihukumu miisho ya dunia; Naye atampa mfalme wake nguvu, Na kuitukuza pembe ya masihi wake.”

 

Kaka zangu na dada zangu Mungu anatutaka tuishi zaidi maneno, hatuishi kwa sababu ya maneno ya watu tunaishi kwa sababu ya neno la Mungu, ushindi wa maisha yetu umefungwa katika neno la Mungu na sio katika maneno ya wanadamu sisi ni washindi na zaidi ya kushinda. Hakikisha katika maisha yako unajaa neno la Mungu ili kila neno utakaloshambuliwa uwe unajibu lake katika neno la Mungu Ni neno la Mungu tu litakaloulinda moyo wako na mashambulizi ya shetani, litaiweka sawa akili yako litakulinda na kukuhifadhi  maneno ya kukatisha tamaa hayatakuwa na nguvu kwa mtu aliyejaa neno la Mungu ushindi wako utakuwa kama Daudi dhidi ya Goliati na Hana dhidi ya Penina, au Nehemia na akina Sanbalati, jifiche katika neno la Mungu imba ahadi zake kumbuka hakuna silaha itakayofanyika juu yako ambayo itafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka dhidi yako katika kuhukumu utauhukumu kuwa mkosa na huu ndio urithi wa watumishi wa Mungu!

 

Isaya 54:17 “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia.Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako. Tazama, nimemwumba mhunzi avukutaye moto wa makaa, akatoa silaha kwa kazi yake; nami nimemwumba mharibu ili aharibu. Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.”

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 21 Septemba 2025

Heri aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba!


Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”




Utangulizi:

Moja ya maneno ya msingi sana yanayohitimisha hutuba maarufu ya Bwana Yesu, maarufu kama Hutuba ya Mlimani ni pamoja na mfano wa mjenzi mwenye hekima na yule mjenzi mpumbavu, ambao ni mfano alioutumia Yesu Kristo kukazia hutuba yake kuonyesha umuhimu wa kusikia na kulitendea kazi neno lake, kimsingi kulitendea kazi neno kunajenga msingi imara sana wa kiroho, msingi usiotikisika  katika maisha ya kila mwanafunzi wa Yesu, uwezo wa kustahimili  majaribu na magumu, Lakini pia usalama wa kukaa ndani ya Yesu,  sawa na nyumba iliyojengwa juu ya mwamba ambayo inakuwa na uwezo wa kustahimili dhuruba za aina mbalimbali na kukaa kwa usalama na kudumu.

Luka 6:47-49 “Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake. Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri. Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa.”           

Kimsingi neno la Mungu linampa umuhimu mkubwa mtu anayelitendea kazi neno la Mungu, na mfano huu Yesu aliutoa sawa na tu na agizo linalotutaka tuwe watendaji wa neno na sio wasikiaji, moja ya changamoto kubwa katika nyakati za leo, sio kukosekana kwa mafundisho au watu kuisikia injili lakini changamoto kubwa iko kwamba ni nani analifanyia kazi neno la Mungu, uwezo wetu wa kusikia hauko katika kusikia bali kutenda Wayahudi wanaita agizo hilo SHEMA yaani SIKIA Israel.

Marko 12:29-30 “Yesu akamjibu, Ya kwanza ndiyo hii, SIKIA, Israeli, Bwana Mungu wetu ni Bwana mmoja; nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote.”

Mathayo 21:28-32 “Lakini mwaonaje? Mtu mmoja alikuwa na wana wawili; akamwendea yule wa kwanza, akasema, Mwanangu, leo nenda kafanye kazi katika shamba la mizabibu. Akajibu akasema, Naenda, Bwana; asiende. Akamwendea yule wa pili, akasema vile vile. Naye akajibu akasema, Sitaki; baadaye akatubu, akaenda. Je! Katika hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya babaye? Wakamwambia, Ni yule wa pili. Basi Yesu akawaambia, Amin nawaambia, watoza ushuru na makahaba wanatangulia mbele yenu kuingia katika ufalme wa Mungu. Kwa sababu Yohana alikuja kwenu kwa njia ya haki, ninyi msimwamini; lakini watoza ushuru na makahaba walimwamini, nanyi hata mlipoona, hamkutubu baadaye, ili kumwamini.”

Yakobo 1:22-25 “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo. Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.”

Kimsingi maandiko yote na mifano yote hapo inatolewa kusisitiza ujumbe mmoja wa kulifanyia kazi neno la Mungu, yaani kulitenda au kuliishi, Mtu anayelitendea kazi neno la Mungu huyu anafananishwa na mtu aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba imara na kwa sababu hiyo dhoruba za kimwili na kiroho na kiakili na kisaikolojia na mafundisho potofu, haziwezi kumdhuru kwa sababu amejengwa juu ya Mwamba, Leo tutachukua muda kujifunza juu ya somo hili Muhimu, Heri aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba na kuliangalia somo hili katika vipengele vitatu vifuatavyo:-


·         Maana ya neno Mwamba.

·         Heri aliyejenga nyumba yake juu ya Mwamba. 

·         Jinsi ya kujijenga juu ya Mwamba.


Maana ya neno Mwamba.

Ni muhimu kufahamu kuwa moja ya msamiati muhimu sana ambao umetumika mara nyingi katika neno la Mungu ni pamoja na neno MWAMBA, Neno Mwamba tunalolisoma katika maandiko kwa mujibu wa muktadha wake mara nyingi limetajwa kwa Lugha ya Kiebrania kama neno Sela’, Cá¿¡r na KÄ“phÄ«m, sawa na maneno KÄ“phas na Pétra katika Lugha ya Kiyunani  Katika Kiingereza tunapata maneno Rock au neno Solid Foundation kwa Kiswahili Mwamba au Msingi imara, Pamoja na neno hili kutumika kitaalamu katika maswala ya miamba na ujenzi, katika uhalisia wake, katika Lugha ya kinabii mara nyingi neno Mwamba lilitumika kumtaja Mungu mwenyewe, Kristo au neno la Mungu:-

2Samuel 22:1-4 “Basi Daudi akamwambia Bwana maneno ya wimbo huu, siku ile Bwana alipomwokoa mikononi mwa adui zake zote, na mkononi mwa Sauli; akasema, Bwana ndiye jabali langu, na ngome yangu, na mwokozi wangu, naam, wangu; Mungu wa MWAMBA wangu, nitamwamini yeye; Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, mnara wangu, na makimbilio yangu; Mwokozi wangu, waniokoa na jeuri. Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa; Hivyo nitaokoka na adui zangu.”

Zaburi 71:1-3 “Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele. Kwa haki yako uniponye, uniopoe, Unitegee sikio lako, uniokoe. Uwe kwangu MWAMBA wa makazi yangu, Nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru niokolewe, Ndiwe genge langu na ngome yangu.”

Isaya 17:10 “Maana umemsahau Mungu wa wokovu wako, wala hukuukumbuka MWAMBA wa ngome yako; kwa sababu hiyo ulipanda mashamba yapendezayo, na kutia ndani yake mizabibu migeni.             

Zaburi 61:1-3 “Ee Mungu, ukisikie kilio changu, Uyasikilize maombi yangu. Toka mwisho wa nchi nitakulilia nikizimia moyo, Uniongoze juu ya MWAMBA nisioweza kuupanda. Kwa maana ulikuwa kimbilio langu, Ngome yenye nguvu adui asinipate.”

Kumbukumbu 32:3-4 “Maana nitalitangaza Jina la Bwana; Mpeni ukuu Mungu wetu. YEYE MWAMBA, kazi yake ni kamilifu; Maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili.”

1Wakorintho 10:4 “wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea MWAMBA wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo.”

Unaona kwa msingi huo katika lugha ya kinabii, Neno la Mungu halizungumzii Mwamba wa kawaida au jiwe la kawaida au Msingi mgumu bali inamzungumzia Mungu mwenyewe na sifa zake alizonazo za Uimara, Uthabiti, Usalama na Uwepo wake wa milele, Mungu anapowaita watu wake yaani Kanisa anakuwa amewajenga juu ya Mwamba, na kwa sababu hiyo Shetani hana uwezo, wala kuzimu hakuna uwezo wowote wa kulishinda Kanisa lake, kwa sababu amelijenga juu yake yeye Mwenyewe

Mathayo 16:17-18 “Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya MWAMBA huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”

Waefeso 2:20-22 “Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni. Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana. Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho.”               

Watu waliomwamini Bwana Yesu wamejengwa juu ya Mwamba ambaye ni Yesu Kristo mwenyewe, na Neno lake, Mtu akilitendea kazi neno la Mungu anafananishwa na mtu aliyejenga nyumba yake juu ya MWAMBA yaani Kristo na neno lake, huyu anakuwa amejijenga juu ya msingi imara usiotikisika, kwa ujumla neno la Mungu linazungumzia maisha yaliyojengwa juu ya Mungu, Kristo wake na Neno lake ambalo halibadiliki, pamoja na na jina lake lenye nguvu, maisha ya aina hii humfanya mtu aishi kwa amani kwa sababu anamjua sana Mungu kwa hiyo hata apitie dhuruba za aina yoyote duniani, dhuruba hizi haziwezi kumtikisa hata kidogo, Kwa hiyo ili mtu awe imara katika maisha haya hana budi, kujijenga katika kumjua sana Mungu, kumfahamu sana Yesu Kristo huu ni ndio utajiri unaoweza kutuhakikishia usalama wa maisha ya kiroho na kimwili!

Yohana 17:2-3 “kama vile ulivyompa mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”

Ayubu 22:21 “Mjue sana Mungu, ili uwe na amani; Ndivyo mema yatakavyokujia.”       

Heri aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba.

Neno Heri maana yake ni Baraka kubwa sana au amebarikiwa mtu yule aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba, Hapa Mungu hamaanishi kujenga nyumba halisi, hapa anamaanisha mtu ambaye maisha yake amewekeza juu ya Mungu, Juu ya Kristo na juu ya Neno la Mungu au jina lake,  mtu wa aina hii Maandiko yanaonyesha kuwa mtu aliyejijenga katika Kristo, kujikita katika kumfahamu Yesu Kristo, kulijua neno lake na kuishi sawa na neno lake  huyu ni mtu asiyeweza kuyumbishwa na lolote hapa duniani na kuzimu pia, Kumbuka wala malango ya kuzimu hayataliweza hii maana yake mtu aliyejijenga katika kumjua Mungu maishani mwake hawezi kutikiswa hata kidogo!

Ni mtu asiyeweza kuyumbishwa – Kwa kawaida Mwamba huwa hauyumbishwi, ni jiwe lenye msimamo, ni gumu ni la kudumu ni la milele, huwezi kulitikisa unaweza kukimbilia juu ya MWAMBA au chini yake na ukawa salama kwa hiyo ukijijenga juu ya Yesu na juu ya neno lake na jina lake lililo takatifu sana unahakikishiwa usalama na uwepo wa kudumu na kutokuonolewa au kutikiswa kwa sababu zozote zile, si kuwa hutapitia magumu kabisa lakini hata ukipitia hayatakutikisa kabisa! Si kuwa hutapatwa na majaribu lakini yakikupata hatutatikiswa, sababu uko juu ya mwamba

Mathayo 7:25 “mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba.”

Mtu aliyejikita katika kumjua Mungu, aliyejikita katika kulijua neno lake mtu anayemtegemea Mungu katika kila jambo sio kuwa hatakutwa na dhuruba, sio kuwa mafuriko hayatampiga, sio kuwa pepo hazitavuma juu yake, hii ikimaanisha kuwa atapitia katika moto, atapita katika dhiki, atapita katika maji, atapigwa na pepo zinazovuma lakini kwa kuwa amejikita juu ya mwamba hakuna kitakachoweza kuufarakanisha uwepo wake na Yesu.

Zaburi 46:1-5 “Mungu kwetu sisi ni kimbilio na nguvu, Msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso. Kwa hiyo hatutaogopa ijapobadilika nchi, Ijapotetemeka milima moyoni mwa bahari. Maji yake yajapovuma na kuumuka, Ijapopepesuka milima kwa kiburi chake. Kuna mto, vijito vyake vyaufurahisha mji wa Mungu, Patakatifu pa maskani zake Aliye juu. Mungu yu katikati yake hautatetemeshwa; Mungu atausaidia asubuhi na mapema.”

Zaburi 27:1-4 “Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, Nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, Nimhofu nani? Watenda mabaya waliponikaribia, Wanile nyama yangu, Watesi wangu na adui zangu, Walijikwaa wakaanguka. Jeshi lijapojipanga kupigana nami, Moyo wangu hautaogopa. Vita vijaponitokea, Hata hapo nitatumaini. Neno Moja nimelitaka kwa Bwana, Nalo ndilo nitakalolitafuta, Nikae nyumbani mwa Bwana Siku zote za maisha yangu, Niutazame uzuri wa Bwana, Na kutafakari hekaluni mwake

Zaburi 23:4 “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.”

Isaya 43:1-2 “Lakini sasa, Bwana aliyekuhuluku, Ee Yakobo, yeye aliyekuumba, Ee Israeli, asema hivi, Usiogope, maana nimekukomboa; nimekuita kwa jina lako, wewe u wangu. Upitapo katika maji mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha; uendapo katika moto, hutateketea; wala mwali wa moto hautakuunguza.”

Ulinzi wa kudumu – Nyakati za agano la kale watu wengi sana walitafuta usalama katika miamba, walifahamu kuwa kama kukitokea janga lolote lile mahali salama ni kwenye JABALI au kwenye MWAMBA, ni MWAMBA ndio ulimpa mtu ulinzi na usalama wa kudumu kwa hiyo ujenzi pia unaozingatia usalama unajengwa juu ya Mwamba na sio vinginevyo.

Zaburi 18:1-6 “Wewe, Bwana, nguvu zangu, nakupenda sana; Bwana ni JABALI langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu wangu, MWAMBA wangu ninayemkimbilia, Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu. Nitamwita Bwana astahiliye kusifiwa, Hivyo nitaokoka na adui zangu. Kamba za mauti zilinizunguka, Mafuriko ya uovu yakanitia hofu. Kamba za kuzimu zilinizunguka, Mitego ya mauti ikanikabili. Katika shida yangu nalimwita Bwana, Na kumlalamikia Mungu wangu. Akaisikia sauti yangu hekaluni mwake, Kilio changu kikaingia masikioni mwake.”

Mtu aliyejijenga juu ya mwamba ana ulinzi wa kudumu, Maagano ya Mungu wetu sio ya siku moja ni agano la kudumu ni agano la milele, kwa hiyo mtu akimtumainia Yesu Kristo ana ulinzi wa kudumu, Yesu hafanyi jana tu yeye ni wa siku zote jana, leo na hata milele, ulinzi wake ni wa milele, msamaha wake ni wa milele, fadhili zake ni za milele hakuna kitu kitakachoweza kututenga na upendo wake, hatujamjia Yesu kwa majaribio bali tumemjia yeye kwa sababu anastahili kujiliwa, yeye ni usalama wetu wa milele kwa jambo lolote lile na kwa jaribu lolote lile!

Warumi 8:33-39 “Ni nani atakayewashitaki wateule wa Mungu? Mungu ndiye mwenye kuwahesabia haki. Ni nani atakayewahukumia adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea. Ni nani atakayetutenga na upendo wa Kristo? Je! Ni dhiki au shida, au adha, au njaa, au uchi, au hatari, au upanga? Kama ilivyoandikwa, ya kwamba, Kwa ajili yako tunauawa mchana kutwa, Tumehesabiwa kuwa kama kondoo wa kuchinjwa. Lakini katika mambo hayo yote tunashinda, na zaidi ya kushinda, kwa yeye aliyetupenda. Kwa maana nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.

Usalama wa milele – Ni mwamba ndio humuhakikishia mtu usalama wa milele, kwa hiyo mtu akijijenga juu ya mwamba anajihakikishia Msamaha, na uzima kulindwa dhidi ya hatari zozote zile ziwe za kimwili na kiroho, mwamba unakupa Amani hata kutokee mafuriko au pepo zinazovuma kama umejenga juu ya mwamba utalala usingizi mtamu

Waebrania 10:10-14 “Katika mapenzi hayo mmepata utakaso, kwa kutolewa mwili wa Yesu Kristo mara moja tu. Na kila kuhani husimama kila siku akifanya ibada, na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi; ambazo haziwezi kabisa kuondoa dhambi. Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake. Maana kwa toleo moja amewakamilisha hata milele hao wanaotakaswa.”

Yohana 10:27-29 “Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. Baba yangu aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote; wala hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu.”

Jinsi ya kujijenga juu ya mwamba.

Tumeona faida kubwa sana na Baraka za mtu aliyejenga juu ya Mwamba, hata hivyo ni muhimu kwetu kujifunza kwa kuhitimisha ili kuangalia kuwa tunawezaje kujijenga juu ya mwamba?

1.       Kumtegemea Mungu – Kwa kuwa Mungu ndiye Mwamba maisha ya mtu anayemtegemea Mungu hayategemei mabadiliko ya hali ya hewa au mambo, sisi tunaye Mungu asiyebadilika, Sifa mojawapo ya mwamba ni kutokubadilika, miaka nenda miaka rudi mwamba hubakia vile vile, siku zote, Mwamba ni mgumu una nguvu, mwamba ni wa milele, mwamba ni wa kudumu, mwamba ni ngome, mwamba ni wa kuaminiwa, mwamba ni wa kutumainiwa mwana unaweza kumlinda mtu dhidi ya adui, mwamba unakubeba.

 

Zaburi 62:1-8 “Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake. Yeye tu ndiye MWAMBA wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Hata lini mtamshambulia mtu, Mpate kumwua ninyi nyote pamoja? Kama ukuta unaoinama, Kama kitalu kilicho tayari kuanguka, Hufanya shauri kumwangusha tu katika cheo chake; Huufurahia uongo. Kwa kinywa chao hubariki; Kwa moyo wao hulaani. Nafsi yangu, umngoje Mungu peke yake kwa kimya. Tumaini langu hutoka kwake. Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana. Kwa Mungu wokovu wangu, Na utukufu wangu; MWAMBA wa nguvu zangu, Na kimbilio langu ni kwa Mungu. Enyi watu, mtumainini sikuzote, Ifunueni mioyo yenu mbele zake; Mungu ndiye kimbilio letu.”

 

2.       Kudumu Katika maombi na ibada – Maombi na ibada, kusoma neno la Mungu, kusikiliza mahubiri mbalimbali, kujisomea neno la Mungu kulijadili na kujifunza kunatutengenezea ukaribu wenye nguvu na Mungu na kwa sababu hiyo kwa kufanya hivyo tunajiimarisha juu ya mwamba, tunakuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu, kujitoa kwa Mungu “Devotions” kunatushikamanisha na Mwamba na kwa sababu hiyo sio rahisi kwetu kuyumbishwa kwa namna yoyote ile na mtu yeyote na fundisho lolote!

 

Yeremia 33:1-3 “Tena, neno la Bwana likamjia Yeremia mara ya pili, hapo alipokuwa akali amefungwa katika uwanda wa walinzi, kusema, Bwana alitendaye jambo hili, Bwana aliumbaye ili alithibitishe; Bwana ndilo jina lake; asema hivi, Niite, nami nitakuitikia, nami nitakuonyesha mambo makubwa, magumu usiyoyajua.”

 

3.       Kulitendea kazi neno la Mungu – Kristo ameonyesha wazi kuwa kulitendea kazi neno lake kunafananishwa na kujenga juu ya mwamba na kutokulitendea kazi neno lake kunafanyanishwa na kujenga kwenye mchanga, kwa msingi huo hatuna budi kulitendea kazi neno la Mungu kwa kadiri ya neema ili kuimarisha uhusiano wetu na Mungu wetu na kumuelewa au kumjua yeye kwa kina na mapana na marefu.

 

Mathayo 7:24-27 “Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya MWAMBA; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.”

 

4.       Kuishi maisha ya toba – Ni maisha ya toba pekee yanayoweza kumsaidia mtu kudumisha uhusiano wake na Mungu, watu wengi sana wanafikiri kuwa ujumbe kuhusu toba ni ujumbe kwa wasiookoka lakini ukweli ni kuwa ujumbe wa toba unalihusu Kanisa na unawahusu watu wa Mungu, Hakuna namna yoyote ile tunaweza kubaki katika Mwamba yaani Yesu Kristo bila kuwa na toba neno toba katika kiyunani ni “Metanoia” maana yake kugeuka na kuacha njia mbaya, toba inawahusu watu wa Mungu kugeuka na kuacha njia zao mbaya!

 

2Nyakati 7:14 “ikiwa watu wangu, walioitwa kwa jina langu, watajinyenyekesha, na kuomba, na kunitafuta uso, na kuziacha njia zao mbaya; basi, nitasikia toka mbinguni, na kuwasamehe dhambi yao, na kuiponya nchi yao. Sasa macho yangu yatafumbuka, na masikio yangu yatasikiliza maombi ya watu waombao mahali hapa.”

 

Ufunuo 2:2-5 “Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo; tena ulikuwa na subira na kuvumilia kwa ajili ya jina langu, wala hukuchoka. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.”

 

Ufunuo 2:13-15 “Napajua ukaapo, ndipo penye kiti cha enzi cha Shetani; nawe walishika sana jina langu, wala hukuikana imani yangu, hata katika siku za Antipa shahidi wangu, mwaminifu wangu, aliyeuawa kati yenu, hapo akaapo Shetani. Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli, kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini. Vivyo hivyo wewe nawe unao watu wayashikao mafundisho ya Wanikolai vile vile. Basi tubu; na usipotubu, naja kwako upesi, nami nitafanya vita juu yao kwa huo upanga wa kinywa changu.”

 

5.       Kuishi maisha Matakatifu – Mungu wetu ni Mtakatifu, hii sifa ya utakatifu ni sifa yake yeye na hakuna awaye yote mwingine ambaye anasifa hii, Yeye kama Mwamba moja ya sifa yake ni utakatifu, kwa hiyo ili mtu aweze kuwa salama juu ya mwamba huu, maana yake maisha matakatifu yanamhusu, na hakuna njia ya mkato, nyakati tulizo nazo imekuwa ngumu sana kusikia watu wakihubiri utakatifu lakini wito wa Mungu kwa kanisa lake ni pamoja na kuishi maisha matakatifu ili kujihakikishia usalama kwa Mungu wetu.

 

2Samuel 2:1-2 “Naye Hana akaomba, akasema, Moyo wangu wamshangilia Bwana, Pembe yangu imetukuka katika Bwana, Kinywa changu kimepanuka juu ya adui zangu; Kwa kuwa naufurahia wokovu wako; Hakuna aliye MTAKATIFU kama Bwana; Kwa maana hakuna ye yote ila wewe, Wala hakuna MWAMBA kama Mungu wetu.”

 

Isaya 6:1-3 “Katika mwaka ule aliokufa mfalme Uzia nalimwona Bwana ameketi katika kiti cha enzi, kilicho juu sana na kuinuliwa sana, na pindo za vazi lake zikalijaza hekalu. Juu yake walisimama maserafi; kila mmoja alikuwa na mabawa sita; kwa mawili alifunika uso wake, na kwa mawili alifunika miguu yake, na kwa mawili aliruka. Wakaitana, kila mmoja na mwenzake, wakisema, MTAKATIFU, MTAKATIFU, MTAKATIFU, ni Bwana wa majeshi; dunia yote imejaa utukufu wake.”


Walawi 20:26 “Nanyi mtakuwa watakatifu kwangu mimi; kwa kuwa mimi BWANA ni MTAKATIFU nami nimewatenga ninyi na mataifa, ili kwamba mwe wangu.”

 

1Petro 1:15-16. “bali kama yeye aliyewaita alivyo MTAKATIFU, ninyi nanyi iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote; kwa maana imeandikwa, Mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.”

Heri yule aliyejenga Nyumba yake juu ya Mwamba, maana yake heri mtu yule aliyewekeza maisha yake kwa Mungu wetu na Kristo wake na Neno lake na jina lake, Mtu wa namna hii ana maisha thabiti yasiyoyumbishwa na dhuruba, wala pepo wala mafuriko wala changamoto za aina yoyote na ana uhakika wa uzima wa milele, Neno la Mungu linatoa wito kwetu kuwekeza katika kristo kwa usalama wa uhakika wa maisha yetu!.

 

Na. Rev. Innocent Samuel Kamote.

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumapili, 14 Septemba 2025

Urithi wa Mtoto wa kike!


Hesabu 27:1-4 “Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.”



Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika Jamii nyingi zamani na hata siku hizi, Mwanamke hakupewa nafasi kubwa katika urithi wa mali za baba yake hususani ardhi, Kulikuwa na sheria na mila nyingi zinazompa upendeleo mtoto wa kiume na kumpuuzia mtoto wa kike, Hapa Masaini Loiborosoit A, Wilayani Simanjirio, Mkoani Manyara niliko pia nimeikuta mila hii miongoni mwa jamii ya Kimaasai, Mila, Desturi na Sheria kama hii vilevile lilikuweko katika jamii ya Kiyahudi wakati wa Torati ya Musa, Lakini kupitia mabinti jasiri sana wana wa SELOFEHADI  yaani Mala, Noa, Hogla, Milka na Tirsa  wao waliwahi kutoa hoja mbele ya Musa na kuhani mkuu Eleazari na kisha hoja ikapelekwa kwa Mungu na Mungu akalazimika kubadilisha sheria na kutoa kibali kwamba watoto wa kike wana haki ya kurithi kama ilivyo kwa watoto wa kiume, ujasiri wao na uthubutu wao wa kuweza kumkabili Musa na hatimaye Mungu kubadili sheria kwaaji yao unaonyesha kuwa mabinti hawa walikuwa na ujasiri usiokuwa wa kawaida “uncommon boldness” katika tafiti zangu wakati wa maandalizi ya somo hili nilimuona mtu mmoja akiwaita mabinti hawa “Change Makers” yaani waleta mabadiliko, Hoja yao ilikuwa na mashiko jambo lililopelekea Mungu kubadili sheria kwaajili ya watoto wa kike

Hesabu 27:5-8 “Basi Musa akaleta neno lao mbele ya Bwana Bwana akanena na Musa, na kumwambia, Hao binti za Selofehadi wananena lililo haki; kweli utawapa milki ya urithi pamoja na ndugu za baba yao; nawe utawapa urithi wa baba yao. Kisha utanena na wana wa Israeli, na kuwaambia, Mtu akifa, naye hana mwana wa kiume, ndipo utampa binti yake urithi wake.”

Leo basi tutachukua muda kujifunza kwa njia ya uchambuzi somo hili Urithi wa Mtoto wa kike kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

 

·         Sheria isiyozingatia haki

·         Kuvunjwa kwa sheria isiyozingatia haki

·         Urithi wa mtoto wa kike

                 

Sheria isiyozingatia haki

Sheria ya Musa pamoja na Mila nyingi na Desturi za zamani zilikuwa zimezoeleka ya kwamba urithi wa mali pamoja na ardhi ulikuwa unaelekezwa kwa watoto wa kiume pekee, mtoto wa kiume wa kwanza akipokea urithi mara dufu yaani mara mbili kuliko wengine na wengine kwa kadiri ya sehemu zao, watoto wa kike hawakuhesabiwa, na kuwa kama mtu angefariki dunia bila kuwa na mtoto wa kiume basi mali zake zingerithiwa na Ndugu zake wa karibu na mabinti wangeolewa tu na kuwa na jina la familia nyingine, kimsingi pia wangeachwa bila kurithi lolote

Kumbukumbu 21:15-17 “Akiwa mtu yuna wake wawili, mmoja ampenda, mmoja hampendi, nao wamemzalia watoto, ampendaye na asiyempenda wote wawili; na yule mzaliwa wa kwanza akiwa ni wa mke asiyependwa; ndipo itakapokuwa ya kwamba siku atakayowarithisha wanawe alivyo navyo, asimweke mwana wa ampendaye kuwa mzaliwa wa kwanza mbele ya mwana wa asiyempenda, naye ndiye mzaliwa wa kwanza huyu; lakini amkubali mzaliwa wa kwanza mwana wa yule asiyempenda, kwa kumpa mafungu mawili katika vyote alivyo navyo; kwa maana ndiye mwanzo wa nguvu zake; haki ya mzaliwa wa kwanza ni yake yeye.”

Kwa hiyo Mwanzoni Mila na Desturi na Sheria za Kiebrania hazikuwa zimemfikiria hata kidogo mtoto wa kike, Sheria hii ilikuwa ni Sheria isiyozingatia haki, ilisababisha huzuni kwa mabinti kwani mali hususani ardhi ya baba yao ingekwenda kwa ndugu zake na wao wangeachwa mikono mitupu, Binti za wana wa Selofehadi yaliwakuta haya, na bila shaka waliyafikiri kwa kina na kuona kuwa hakuna haki hapo na sheria hiyo ni kandamizi kwao wakadai haki hiyo

Hesabu 27:1-4 “Wakati huo wakakaribia hao binti za Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, wa jamaa za Manase mwana wa Yusufu; na majina ya hao binti za Selofehadi ni haya; Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakasimama mbele ya Musa, na mbele ya Eleazari kuhani, na mbele ya wakuu, na mkutano wote, mlangoni pa hema ya kukutania, wakasema, Babaetu alikufa nyikani, naye hakuwamo katika mkutano wa hao waliojikutanisha kinyume cha Bwana katika mkutano wa Kora; lakini akafa katika dhambi zake mwenyewe; naye alikuwa hana wana wa kiume. Kwa nini basi jina la babaetu kufutwa katika jamaa zake kwa sababu alikuwa hana mwana wa kiume? Tupe sisi urithi pamoja na ndugu zake babaetu.”

Mabinti wa Selofehadi walihuzunika kuona kwakuwa baba yao hakuwa na mtoto wa kiume, basi ndugu zake baba yao wangerithi mali na ardhi yake na mabinti zake wakiepo wangeachwa bila kitu, lakini baada ya kuchukua hatua za kijasiri na kumkabili Musa na Musa akamuuliza Mungu huo ukawa mwisho wa sheria kandamizi dhidi ya wanawake.

Tunajifunza kutoka kwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa kwamba tunaweza kubadili lolote lisilo la haki kwa ujasiri na lolote lililo kandamizi kwa njia ya maombi na Mungu akasikiliza, Sheria na Kanuni yoyote iliyokinyume na lile tunalolihitaji na linalosimama kama haki yetu mbele za Mungu inaweza kuingiliwa kati kwa Sheria ya Kanuni ya kuomba kwa Mungu, Mabinti hawa kwa imani na ujasiri walimkabili Musa na Musa aliomba kwa Mungu na Mungu akabadili sheria, tunaweza kuomba lolote kwa jina la Yesu kwenda kwa Baba yetu wa Mbinguni na kubadilisha Sheria na Kanuni, Mila na Desturi kandamizi na uhuru wetu ukapatikana katika jina la Yesu Kristo.

Kuvunjwa kwa sheria isiyozingatia haki

Habari ya mabinti hawa inatufundisha kuwa tunaweza kubadili sheria, endapo tu tutasimama katika haki, na tunajifunza ya kuwa maombi yana nguvu ya kubadili sheria mila na desturi ambazo hazitutendei haki katika ulimwengu wa roho na mwili, wakati habari hii ikizungumzia kubadilishwa kwa sheria iliyopelekea wasichana au wanawake katika familia kuwa na haki ya kisheria ya kurithi, lakini tunajifunza pia kuwa tunaweza kubadili sheria za mila na desturi za aina yoyote ile kwa njia ya maombi ikiwa sheria hiyo au mila hizo au kanuni hizo hazijazingatia haki

Esta 4:15-16 “Basi Esta akawatuma ili wamjibu Mordekai, Uende ukawakusanye Wayahudi wote waliopo hapa Shushani, mkafunge kwa ajili yangu; msile wala kunywa muda wa siku tatu, usiku wala mchana, nami na wajakazi wangu tutafunga vile vile; kisha nitaingia kwa mfalme, kinyume cha sheria; nami nikiangamia, na niangamie.”  

Daniel 6:10-26 “Hata Danieli, alipojua ya kuwa yale maandiko yamekwisha kutiwa sahihi, akaingia nyumbani mwake, (na madirisha katika chumba chake yalikuwa yamefunguliwa kukabili Yerusalemu ;) akapiga magoti mara tatu kila siku, akasali, akashukuru mbele za Mungu wake, kama alivyokuwa akifanya tokea hapo. Basi watu hao wakakusanyika pamoja, wakamwona Danieli akiomba dua, na kusihi mbele za Mungu wake. Ndipo wakakaribia, wakasema mbele ya mfalme katika habari ya ile marufuku ya mfalme; Je! Hukuitia sahihi ile marufuku, ya kwamba kila mtu atakayeomba dua kwa Mungu awaye yote, au kwa mtu awaye yote, katika muda wa siku thelathini, ila kwako, Ee mfalme, atatupwa katika tundu la simba? Mfalme akajibu, akasema, Neno hili ni kweli, kama ilivyo sheria ya Wamedi na Waajemi isiyoweza kubadilika. Basi wakajibu, wakasema mbele ya mfalme, Yule Danieli, aliye mmoja wa wana wa wale waliohamishwa wa Yuda, hakujali wewe, Ee mfalme, wala ile marufuku uliyoitia sahihi, bali aomba dua mara tatu kila siku. Basi mfalme aliposikia maneno haya alikasirika sana, akakaza moyo wake ili kumponya Danieli; akajitaabisha kumwokoa hata jua likachwa. Ndipo watu wale wakakusanyika pamoja mbele ya mfalme, wakamwambia mfalme, Ee mfalme, ujue ya kuwa ni sheria ya Wamedi na Waajemi, lisibadilike neno lo lote lililo marufuku, wala amri yo yote iliyowekwa na mfalme. Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli. Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba.Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno. Basi mfalme akafurahi sana, akaamuru wamtoe Danieli katika lile tundu. Ndipo Danieli akatolewa katika lile tundu, wala dhara lo lote halikuonekana mwilini mwake, kwa sababu alikuwa anamtumaini Mungu wake. Mfalme akaamuru, nao wakawaleta wale watu waliomshitaki Danieli, wakawatupa katika tundu la simba, wao, na watoto wao, na wake zao; na wale simba wakawashinda wakaivunja mifupa yao vipande vipande, kabla hawajafika chini ya tundu. Ndipo mfalme Dario akawaandikia watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, waliokaa juu ya uso wa dunia; Amani na iongezeke kwenu. Mimi naweka amri, ya kwamba katika mamlaka yote ya ufalme wangu watu watetemeke na kuogopa mbele za Mungu wa Danieli; maana yeye ndiye Mungu aliye hai, adumuye milele, na ufalme wake ni ufalme usioharibika, na mamlaka yake itadumu hata mwisho.”              

Tunaona katika mifano kadhaa hapo juu ya kuwa maombi yana uwezo wa kuingilia kati sheria za kawaida na mila za kawaida na hata za Mungu na kubadilisha mambo, mabinti hawa wenye ujasiri waliomkabili Musa kwa maombo yao na ufuatiliaji waliweza kusababisha mabadiliko ya sheria, walimrudisha Musa kwa Mungu na Mungu akafanya mabadiliko ya sheria kwaajili yao na wengine hata leo, kwa tukio lao Mungu alibadili kanuni na kuamua kuwapa haki

Luka 18:1-7 “Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu sikuzote, wala wasikate tamaa. Akasema, Palikuwa na kadhi katika mji fulani, hamchi Mungu, wala hajali watu. Na katika mji huo palikuwa na mwanamke mjane, aliyekuwa akimwendea-endea, akisema, Nipatie haki na adui wangu. Naye kwa muda alikataa; halafu akasema moyoni mwake, Ijapokuwa simchi Mungu wala sijali watu,lakini, kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa kunijia daima.Bwana akasema, Sikilizeni asemavyo yule kadhi dhalimu. Na Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu kwao?

Mungu atampa haki yake kila mtu anayemkomalia katika maombi, Mungu aliwapa haki mabinti wa Selofehadi ya Kuwa kama mtu akifa bila mwana wa kiume basi urithi wake utapewa binti zake, asipokuwa na binti au mwana wa kiume basi watepea ndugu zake walio karibu na sheria hii ikawa agizo la kudumu kwa Israel hata leo, haya yakawa mapinduzi makubwa na ya kipekee kwa sababu kupitia wao na kwa mara ya kwanza katika mila na desturi za Kiyahudi wanawake walihesabika kuwa warithi halali wa mali na ardhi ya baba zao. Sio hivyo tu Mungu aliongezea baadaye kwamba ili mali hizo zisitawanyike kutoka kwenye kabila lao basi mabinti hao waolewe ndani ya koo zao ili urithi usihame kutoka kabila moja hadi lingine na hii haikuwanyima haki ya kurithi bali ilihifadhi urithi ule ndani ya ukoo na ndani ya kabila husika bila kutawanyika kwa jina na mali za Muhusika

Hesabu 36:1-10 “Kisha wale wakuu wa nyumba za mababa ya jamaa ya wana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, katika jamaa za wana wa Yusufu, wakakaribia, na kunena mbele ya Musa, na mbele ya wakuu walio juu ya nyumba za mababa ya wana wa Israeli; wakasema, Bwana alimwagiza bwana wangu awape wana wa Israeli nchi kwa kupiga kura iwe urithi wao; tena bwana wangu aliagizwa na Bwana awape binti za Selofehadi ndugu yetu huo urithi wa baba yao. Wakiolewa na watu wa wana wa hizo kabila nyingine za wana wa Israeli, ndipo urithi wao utatwaliwa na kuondolewa katika urithi wa baba zetu, na hiyo kabila watakayotiwa ndani yake itaongezewa urithi wao; basi urithi huo utaondolewa katika kura ya urithi wetu. Tena itakapokuwapo hiyo yubile ya wana wa Israeli, ndipo urithi wa hiyo kabila ambayo wamekuwa ndani yake utaongezewa huo urithi wao; hivyo urithi wao utaondolewa katika urithi wa kabila ya baba zetu. Basi Musa akawaagiza wana wa Israeli kama neno la Bwana lilivyokuwa, akasema, Kabila ya wana wa Yusufu imenena yaliyo haki. Bwana ameagiza neno hili katika habari ya binti za Selofehadi, akasema, Na waolewe na waume wawapendao; lakini na waolewe katika jamaa ya kabila ya baba zao. Hivyo hapana urithi wo wote wa wana wa Israeli utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa wana wa Israeli watashikamana kila mtu na urithi wa kabila ya baba zake. Na kila binti atakayemiliki urithi katika kabila yo yote katika wana wa Israeli, ataolewa katika jamaa moja ya kabila ya baba yake, ili wana wa Israeli wapate kumiliki kila mtu urithi wa baba zake. Hivyo hapatakuwa na urithi uwao wote utakaotoka kabila hii kwenda kabila hii; kwa kuwa kabila za wana wa Israeli zitashikamana kila mmoja na urithi wake mwenyewe. Basi hao binti za Selofehadi wakafanya kama Bwana alivyomwagiza Musa;”

Urithi wa mtoto wa kike

Moja ya fundisho lingine la msingi na la Muhimu tunalojifunza kutoka kwa mabinti wa Selofehadi ni kuwa tunajifunza namna Mungu anavyotaka sheria ya urithi wa mtoto wa kike kuzingatiwa, Ni kama neno la Mungu olinatoa wito kwa jamii kutokuwapuuzia watoto wa kike katika maswala mbalimbali ya kijamii, Kamwe jamii haipaswi kufikiri kuwa Mwanamke ni kiumbe wa daraja la chini, Haki zao zimendikwa katika Torati na zimethibitishwa na Mungu mwenyewe. Jamii inapaswa kuondoa dhana potofu ya kufikiri kuwa mwanamke hastahili urithi na kupingana na hilo ni kupingana na mpango wa Mungu, watoto wa kike wapewe kila wanachistahili katika familia zao, ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha, kupinga ukatili na ubaguzi wa kijinsia, kutokuwatahiri wanawake na yote yanayowanyima haki kutokana na maumbile yao na kuwa jamii inapaswa kuacha mila na desturi za kizamani ambazo ni kandamizi.

Katika nyakati za agano jipya Mwanamke ana haki na mwanaume, Mtumwa na muajiri, Myahudi na Myunani wote wana haki sawa za kiroho, Kwa hiyo anapomuamini Yesu wote wanaonekana kuwa wamoja katika Kristo

Wagalatia 3:27-29 “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo. Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu. Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi.”

Habari ya mabinti wa Selofehadi ni fundisho la kipekee kwamba Mungu ni mtetezi wa haki ya wote walio dhaifu na wanyonge na wale wanaokandamizwa katika jamii, ni somo kwamba Mungu hakubaliani na mila na desturi zinazowanyima haki wengine kwa sababu fulani fulani, kila mwanadamu ana nafasi yake na heshima yake mbele za Mungu na kila mwanadamu anastahili kushiriki Baraka zote za Mungu, Urithi wa mwanamke ni agizo la Mungu na sio upendeleo, Lakini ili urithi ubaki katika kabila lao na jina la baba yao lisipotee waliolewa na binamu zao, kimsingi baadaye watoto hao mabinti walikabidhiwa urithi ulioahidiwa na Musa mtumishi wa Mungu katika nchi ya Mkanaani

Yoshua 17:3-4 “Lakini Selofehadi, mwana wa Heferi, mwana wa Gileadi, mwana wa Makiri, mwana wa Manase, hakuwa na wana waume ila binti; na majina ya hao binti zake walikuwa wakiitwa Mala, na Noa, na Hogla, na Milka, na Tirsa. Nao wakakaribia mbele ya Eleazari, kuhani, na mbele ya Yoshua, mwana wa Nuni, na mbele ya mashehe, wakasema, Bwana alimwamuru Musa kutupa sisi urithi kati ya ndugu zetu; basi kwa kuiandama hiyo amri ya Bwana akawapa urithi kati ya ndugu za baba yao.”

Desturi ya kuwanyima watoto wa kike urithi hususani wa Ardhi imeleta mafarakano katika jamii nyingi duniani, ni Sheria,  Mila na Desturi ambayo imeleta ubaguzi wa kijinsia, lakini hiki ambacho Mungu alikifanya baada ya mabinti wa Selofehadi kimeleta mtazamo mpya wa kijamii na usawa wa kijinsia, hivyo sio tu swala la ardhi lakini watoto wasomeshwe na wasiozwe katika hali ya utoto, lakini wajaliwe na kutunzwa na kuhudumiwa kama watoto wengine, Katika sheria za kislamu watoto wa kike hupewa urithi japo ni nusu ya kile wanapewa wanaume, Lakini wale wenye mila mbovu zinazo-mbagua mtoto wa kike wafahamu tu kuwa Mungu anawathamini nao vilevile kama anavyothamini watoto wa kiume hivyo ni wakati sasa kwa jamii kubadilika ni wakati wa mabunge kutunga sheria zenye kuzingatia uaswa wa kijinsia na kuondoa mila potofu na kandamizi katika jamii na kuachia zile zenye manufaa  

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima