Jumanne, 18 Aprili 2017

Malaika wa Pasaka!



Mstari wa Msingi: Marko 16:1-8, Mathayo 28:1-10

Hata sabato ilipokwisha, ikipambazuka siku ya kwanza ya juma, Mariamu Magdalene, na Mariamu yule wa pili, walikwenda kulitazama kaburi. Na tazama, palikuwa na tetemeko kubwa la nchi; kwa sababu malaika wa Bwana alishuka kutoka mbinguni, akaja akalivingirisha lile jiwe akalikalia. Na sura yake ilikuwa kama umeme, na mavazi yake meupe kama theluji. Na kwa kumwogopa, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu. Malaika akajibu, akawaambia wale wanawake, Msiogope ninyi; kwa maana najua ya kuwa mnamtafuta Yesu aliyesulibiwa. Hayupo hapa; kwani amefufuka kama alivyosema. Njoni, mpatazame mahali alipolazwa. Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka katika wafu. Tazama, awatangulia kwenda Galilaya; ndiko mtakakomwona. Haya, nimekwisha waambia. Wakaondoka upesi kutoka kaburini, kwa hofu na furaha nyingi, wakaenda mbio kuwapasha wanafunzi wake habari.  Na tazama, Yesu akakutana nao, akisema, Salamu! Wakakaribia wakamshika miguu, wakamsujudia. Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona.


              
Utangulizi:

Inaonekana wazi wakati wote Mungu anapokuwa na Tangazo muhimu sana kwa wanadamu, hutuma ujumbe wake kupitia Malaika, wakati mwingine Malaika wa habari muhimu alijitambulisha kwa jina na wakati mwingine Hakujitambulisha, vyovyote vile iwavyo malaika hao walileta ujumbe Muhimu kwa wanadamu mfano:- 

·         Mungu alituma Malaika kutangaza kuzaliwa kwa Samson Waamuzi 13
·         Mungu alituma Malaika kutangaza kuzaliwa kwa Yohana Mbatizaji Luka 1
·         Mungu alituma Malaika kutangaza kuzaliwa kwa Yesu Kristo Luka 2:8-11
·         Mungu alituma Malaika kushughulika na tatizo la Sodoma na Gomora Mwanzo 19
·         Mungu alimtuma Malaika wa Pasaka wakati wa Ukombozi wa wana wa Israel Misri 12:29

·     Na Mara hii Yesu anapofufuka Malaika wa Pasaka anakuja tena akiwa na ujumbe mzito ambao tutachukua Muda kuutafakari leo.

Malaika wa Pasaka anawatokea kinamama walikuja Kaburini wakiwa wamekata tamaa na wenye fadhaa kubwa sana, walitoka wakiwa hawajua hata ni nani atakayewaondolea jiwe waendelee na kazi ya kupaka mafuta mwili wa Yesu, lilikuwa ni jambo la hatari na lenye kuogopesha mno, lakini Malaika wa Pasaka alikuwa na ujumbe muhimu sana 

1.       Aliwaambia Msiogope.
Inawezekana kina mama waliokwenda Kaburini walishituka zaidi walipoona kijana huyu mwenye mavazi meupe, na waliogopa mno lakini ujumbe wa kwanza wanaoupokea kutoka kwa malaika wa pasaka ni kutokuogopa Mungu wakati wote anataka watu wake wasiogope na wawe na amani, wakati wote haijalishi tunazungukwa na mazingira ya namna gani, Malaika hakutaka kina mama na dunia nzima kwa ujumla itawaliwe na Hofu, hofu ni adui mkuu wa amani, kila mtu anayesheherekea Pasaka anapaswa kuwa Mbali na Hofu, Kama mauti ilimpata Yesu Kristo naye amefufuka hatupaswi kuogopa tena Milele Ufunuo 1:17-18, 2Timotheo 1:3, 8, Dunia ya leo imejawa na Hofu, Huko Syria hivi Karibuni Marekani imepiga Bomu kubwa sana kubwa mno, hali ya hofu inaongezeka , Hapa nchini kule Pwani Polisi kumi wameuawa ambao ni walizni wa amani nchini hii inaongeza Hofu, Kule Korea Kaskazini na Marekani wamekuwa na mikwara ya kustaajabisha wakitaka kupigana hali hizi zote zinaoneza hofu duniani na kuifanya Dunia isiwe mahali pa Amani ni lazima jitihada zifanyike katika kuhakikisha Amani inatawala Duniani na watu wanaondoka katika maisha ya hofu.

2.       Amefufuka Katika wafu.
Malaika anataka kuthibitisha kuwa Yesu alisulubiwa, na alikufa na kuwa amefufuka maana yake yu hai, Ufunuo 1:17-18 Yesu yu Hai milele na milele, kama kuna jambo ambalo shetani hapendi kulisikia ni ushahidi ulio wazi kuwa Yesu amefufuka, hii ndio tofauti yake na waanzilishi wote wa dini na falsafa mbalimbali duniani, wote waliandika historian a wakapita sivyo ilivyo kweke Yesu Kristo yeye yuko hai milele, ulikuwa ni ujumbe wa kutia moyo kwa kina mama hawa walikuwa wamenunua mafuta ya kuupaka mwili wa Yesu usizoe, aendelee kuwepokuwepo kaburini, Lakini Neno la malaika lilikuja kuondoa mashaka kwao na kuwajulisha kuwa hata mafuta yenu ya kumpaka Merehemu hayana kazi tena huyu mwanamume yu hai.Aidha malaika alikuwa amewakumbusha Maneno aliyoyasema Yesu kuwa atafufuka hii maana yake ni kuwa Yesu aliitimiza ahadi, viongozi wazuri ni wale wanaotimiza ahadi zao mara baada ya Uchaguzi kama ilivyo kwa Pombe Joseph Magufuli anatimiza ahadi nyingi sana alizowaahidi watanzania, lakini nitoe wito kwake kuendelea kudhibiti mfumo wa Bei ya chakula kwani imepanda mmno na kipato cha watanzania hakitoshelezi katika kukabiliana na kupanda kwa unga na vyakula vinginevyo.

3.       Hayuko Hapa
Malaika aliwaambia wanawake hawa wawe watalii wa kwanza wa kulitembelea Kaburi la Yesu lililotupu, aliwaambia Patazameni mahali walipomuweka, hata leo unaweza kwenda kupatazama mahali walipomuweka Hayupo tena, yuko Hai, Kaburi lake ni ushahidi wazi hata leo kuwa Yesu Kristo amefufuka na tayari yuko busy na majukumu ya kutuombea kama kuhani mkuu

4.       Nendeni Mkwawaambie wanafunzi wake na Petro
Habari njema kwa wanafunzi wote wa Yesu. Lakini pia maalumu kwa Petro, Petro na Yesu walikuwa tayari wameachana pabaya Petro alikuwa tayari amemkana Yesu Mara tatu wakati anasulubiwa Malaika ametumwa kulete ujumbe wa ufufuo kwa wanafunzi wote wa Yesu na maalumu kwa Petro pia, Mungu alitaka kuthibitisha kuwa ameshamsamehe Petro kabisa na kuwa sasa ana uhusiano naye mkubwa na wa kipekee zaidi, Habari njema za ufufuo zinawagusa hata wale ambao walikuwa wamemkana Yesu, Yesu kipakee anaonyesha kuhusika na rafiki zake wote na hata wale waliomkataa kivitendo na kwa kiapo

Malaika alikuwa na ujumbe uliobeba Kuondoa Hofu, Kuleta Matumaini, Msamaha na uthibitisho kuwa tutamuona Yesu aliyefufuka, Kila kiongozi wa kisiasa kuanzia ngazi ya kata anapaswa kuhakikisha wanainchi wanaishi mbali na Hofu, tuache kuwatisha wanainchi, Lazima kila kiongozi alete habari za matumaini na kututhibitishia hali halisi ya tumaini hilo Yesu alikuwa ni kiongozi aliyetoka tunmaini na alilithibitisha, aliposema yeye ni ufufuo na uzima alifuua wafu lakini pia alifufuka kwelikweli, aliweza kusamehe na kuwahesabu wale waliomkosea kama rafiki maalumu na sio maadui zake, viongozi wa leo hawapaswi kujenga hali ya uadui na raia wake, ahadi zake zilikuwa za kweli hakutoa matumaini hewa.

Na mkuu wa Wajenzi Mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.

Jumatatu, 3 Aprili 2017

Mwamba wenye Imara.

Andiko: 1Wakoritho 10:4 Biblia inasema “wote wakanywa kinywaji kile kile cha roho; kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuata; na mwamba ule ulikuwa ni Kristo.”

 Mji uliochongwa katika Mwamba huko Jordan unajulikana kama mji wa Petra yaani Mwamba

Utangulizi:

Ilikuwa mwaka wa 1763 wakati Mchungaji Rev.Augustus  Montague Toplady, Muhubiri wa Injili kutoka kijiji cha Blagdon Huko Mendip Hill Uingereza, alipokuwa akisafiri kwa shughuli za injili, alikumbwa na dhoruba kali sana njiani alijaribu kutafuta hifadhi katika moja ya miamba na kufanikiwa kuwa salama na ndipo baadaye alitunga wimbo MWAMBA WENYE IMARA au MWAMBA ULIOPASUKA ambao ni moja ya nyimbo kuu na za Muhimu sana kwa waanglikan na umekuwa maarufu katika tenzi za rohoni namba 58 na nyimbo za injili 30, wimbo huu ulichapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 1775 na gazeti moja la injili lililojulikana kama The gospel Magazine. Wimbo ulipendwa sana na Prince Albert ambaye aliagiza wimbo huo upigwe siku atakapokufa na ndipo ukawa maarufu sana wakati wa misiba hata ingawaje wimbo huu unamzunguzia Yesu kama Mwamba.
Mwamba wenye imara,
Kwako nitajificha,
Maji hayo na damu,
Yaliyotoka humu,
Hunisafi na dhambi,
Hunifanya mshindi.

Kwa kazi zote pia,
Sitimizi sheria,
Nijapofanya bidii,
Nikilia na kudhii,
Hayaishi makosa,
Ndiwe wa kuokoa. 

Sina cha mkononi,
Naja msalabani,
nili tupu, Nivike,
Ni mnyonge, nishike,
Nili mchafu naja,
Nioshe nisijafa.

Nikungojapo chini,
Na kwenda kaburini,
Nipaapo mbinguni,
Na kukwona enzini,
Roho yangu na iwe,
Rahani mwako wewe.


Mtunzi wa wimbo huu aliokoa maisha yake katika mwamba! Na kwa vile alikuwa muhubiri alielewa wazi kuwa Mwamba ulimwakilisha Yesu Kristo, Katika majira haya ya Pasaka ni muhimu kwetu kurudi katika maandiko na kutafakari kwa kina kwa nini Yesu anaitwa Mwamba? Watakatifu waliotutangulia walimfananisha Mungu na mwamba.

Biblia inamtaja wazi Mungu wetu kuwa ni Mwamba wa wokovu wetu

1.       Zaburi ya 18:2 Bwana ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia, Ngao yangu, na pembe ya wokovu wangu, na ngome yangu.

2.       Zaburi ya 62:1-2 Nafsi yangu yamngoja Mungu peke yake kwa kimya, Wokovu wangu hutoka kwake.  Yeye tu ndiye mwamba wangu na wokovu wangu, Ngome yangu, sitatikisika sana

3.       Zaburi ya 95: 1 Njoni, tumwimbie Bwana, Tumfanyie shangwe mwamba wa wokovu wetu.

Neno mwamba katika Biblia ya Kiebrania linatajwa kwa maneno makuu mawili yaani TSUR ambalo maana yake ni gema au pande kubwa la jiwe, na neno lingine ni SELA ambalo maana yake ni mlima au Jabali au ngome ya Jiwe, Kiyunani ni Peter na Petra
 
Kwa hivyo Biblia inapomtaja Kristo kama Mwamba inamaanisha SELA au PETRA Kila mmoja wetu anaweza kujua ujasiri anaojisikia akiwa juu ya mwamba unapokuwa juu ya mwamba au juu ya jabali unaweza kukaa kwa ujasiri, unaweza kurukaruka na hakuna wa kukubabaisha, mwamba huwa hautikisiki, haung’oki, hauogopi dhoruba na kama mtu atashindana na mwamba atavunjika vunjika na kama mtu ataangukiwa na mwamba atasagwasagwa!

Hakuna njia nyingine yoyote ambayo kwa hiyo tunaweza kuwa salama isipokuwa kumtegemea Yesu tu mtuni wa wimbo alionyesha kuwa ni kwa Damu yake yesu tu tunaweza kuwa salama, kwake tunaweza kujificha na kuutegemea ushidni, kazi njema , na matendo mema hayawezi kutuokoa ni zawadi ya Yesu Kristo pekee aliyekufa msalabani kwaajili yetu ndio inayoweza kututhibitishia usalama wetu, kwa jambo lolote lile ni lazima tuweke tegemeo letu kwa Bwana Yesu

Tunaweza kukutana na dhuruba za aina mbalimbali zenye kuhuzunisha Magonjwa na mateso, Matatizo ya kifedha na kiuchumi, Matatizo ya kifamilia, Huzuni na kukata tamaa jambo kubwa na la msingi la kufanya ni kumwangalia Yesu ni kumtegemea ni kujificha kwake yeye ndio nguvu yetu, na kimbilio letu ndiye mwamba imara 

Yeye aliahidi kuwa atalijenga kanisa lake juu ya mwamba na wala malango ya kuzimu hayatalishinda, ushindi ni wetu kama tu tutajificha na kuutegemea Mwamba.  

Mathayo 16: 13-18Basi Yesu akaenda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena Mwana wa Adamu kuwa ni nani? Wakasema, Wengine hunena u Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii.  Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?  Simoni Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni. Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda.”

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima.

Jumamosi, 25 Machi 2017

Ujumbe: Kataa kudhalilishwa kwa Jamii yako!



“Reject any insult in your society” 

Mstari wa Msingi: 2Samuel 10:1-5,17-19.

“Ikawa baadaye, mfalme wa wana wa Amori akafa, akamiliki Hanuni, mwanawe, mahali pake. Naye Daudi akasema, Nitamtendea wema Hanuni, mwana wa Nahasi, kama babaye alivyonitendea wema mimi. Basi Daudi akatuma kwa mkono wa watumishi wake, ili kumtuliza kwa habari za babaye. Wakaja watumishi wa Daudi katika nchi ya wana wa Amoni. Lakini wakuu wa wana wa Amoni wakamwambia Hanuni, bwana wao, Je! Waona ya kuwa Daudi amemheshimu babayo kwa kutuma kwako wafariji? Je! Daudi hakuwapeleka watumishi wake kwako ili kuuangalia mji, na kuupeleleza, na kuuangamiza? Basi Hanuni akawatwaa hao watumishi wa Daudi, akawanyoa nusu ya ndevu zao, akawakatia nguo zao katikati, hata matakoni, akawatoa waende zao. Watu walipomwambia Daudi habari hizo, akatuma watu kuwalaki; kwa sababu watu hao walikuwa wametahayarika sana. Mfalme akasema, Ngojeni Yeriko, hata mtakapoota ndevu zenu, ndipo mrudi.” 

“Alipoambiwa Daudi, akakusanya Israeli wote, akavuka Yordani, akaja Helamu. Nao Washami wakajipanga kinyume cha Daudi, wakapigana naye. Wakakimbia Washami mbele ya Israeli; naye Daudi akawaua katika Washami, watu wa magari mia saba, na wapanda farasi arobaini elfu, naye akampiga huyo Shobaki, jemadari wa jeshi lao, hata akafa huko. Na wafalme wote waliomtumikia Hadadezeri walipojiona kuwa wameshindwa mbele ya Israeli, walifanya amani na Israeli, wakawatumikia. Basi Washami wakaogopa kuwasaidia wana wa Amoni tena.”                
Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa Daudi alikuwa na kiongozi mwenye moyo wa ajabu sana, aliwapenda watu wake aliwapenda jirani zake, alipenda haki alilipa mema, lakini Daudi alichukia sana Udhalilishaji, Biblia inaonyesha katika kifungu tulichosoma Jinsi Israel walivyopigana vita na wana wa amoni na washami sababu kuu ikiwa ni Udhalilishwaji wa watumishi wake

Maana ya udhalilishaji
Neno udhalilishaji kwa kiingereza Insult au offend au embarrassing au abuse ni tendo au neno la kumfanya mtu ajione kuwa duni, ajione amedhalilishwa, amenyanyaswa, amefanywa duni na mnyonge,amefungwa au ametekwa au asiye huru, Daudi anaonekana kukataa kudhalilishhwa yeye na jamii yake 

Kuwanyoa watu nusu ndevu nyakati za Biblia lilikuwa ni tendo la unyanyasaji wa hali ya juu sana katika mashariki ya kati, kunyoa ndevu katika hali ya kawaida kulimaanisha una huzuni au msiba mkubwa Isaya 15:2,  Wanapanda juu hata Bayithi na Diboni, mpaka mahali palipo juu ili walie; juu ya Nebo na juu ya Medeba Wamoabi wanalia; Wana upaa juu ya vichwa vyao vyote; kila ndevu zimenyolewa.” Yeremia 41:5, “wakafika watu kadha wa kadha toka Shekemu, na toka Shilo, na toka Samaria, watu themanini, nao wamenyoa ndevu zao, na kurarua nguo zao, nao wamejikata-kata, wakichukua sadaka na ubani mikononi mwao, ili wazilete nyumbani kwa Bwana. aidha katika Biblia na nyakati za Biblia kuwachania wat nguo zao makalioni lilikuwa ni jambo la kuaibisha lililomaanisha ninyi ni wafungwa au mateka wa vita na zawadi yenu ni kuaibishwa tu Isaya 20:4. “vivyo hivyo mfalme wa Ashuru atawachukua uchi, wafungwa wa Misri, na watu wa Kushi waliohamishwa, watoto kwa wazee, hawana viatu, matako yao wazi, Misri iaibishwe.”

Yesu Hatakubali uaibishwe!

Daudi angekubali jambo hilo maana yake anagekuwa amekubali aibu na huzuni, amekubali salamu za kuaibishwa kwake na jamii yake, Daudi alikataa kudhalilishwa alimtuma Yoabu kupanga vita na kupambana kwa gharama yoyote.

Moyo wa Daudi ni kama wa Yesu Kristo, shetani amekusudia kumuweka kila mmoja wetu katika aibu kubwa ya maisha haya lakini na wengine si ajabu kuwa ameshatuaibisha lakini Kristo Yesu ka Ilivyo kwa Daudi hawezi kuvumilia wewe na mimi tudhalilishwe au tuingie katika aibu, na tumkimbilie yeye atatihufadhi na kutuondolea aibu yetu yote.

Daudi alikuwa anatambua siri ya kuikimbia aibu yetu ni kumkimbilia Mungu tu, kusudi kubwa la shetani ni kutuaibisha katika maisha yetu ni kutufanya tutahayari, ni kutufanya tujione duni wanyonge hatufai masikini na mateka katika ufalme wake.

Lakini leo tunaye wa kumkimbilia yeye ni Mwana wa Daudi na tumkimbilie yeye tusiaibike milele Zaburi 31:1, “Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele. Kwa haki yako uniponye,” Zaburi 71:1-71. Nimekukimbilia Wewe, Bwana, Nisiaibike milele.  Kwa haki yako uniponye, uniopoe, Unitegee sikio lako, uniokoe. Uwe kwangu mwamba wa makazi yangu, Nitakakokwenda sikuzote. Umeamuru niokolewe, Ndiwe genge langu na ngome yangu.  Ee Mungu wangu, uniopoe mkononi mwa mkorofi, Katika mkono wake mwovu, mdhalimu, Maana ndiwe taraja langu, Ee Bwana MUNGU, Tumaini langu tokea ujana wangu.  Nimekutegemea Wewe tangu kuzaliwa, Ndiwe uliyenitoa tumboni mwa mama yangu, Ninakusifu Wewe daima. Nimekuwa kitu cha ajabu kwa watu wengi, Na Wewe ndiwe kimbilio langu la nguvu.”

Wayahudi leo hawako Tayari kupoteza Taifa lao

 "Wayahudi waliokimbilia Masada walikuwa tayari kufa kuliko kwenda utumwani"

Mwaka wa 70 askari wa Rumi walikusudia kuwauwa wayahudi wote kutokana na uasi wao, warumi waliamua kupita mji kwa mjia kuhakikisha kuwa wanawaua wayahudi mpaka mwaka 73 kijiji cha mwisho kuvamiwa na kuzingirwa kilikuwa ni kijiji cha Masada wayahudi waliokimbilia huko inakisiwa walikuwa 960 hivi kwa pamoja waliamua “KULIKO KWENDA UTUMWANI NI AFADHALI KUFIA KATIKA INCHI YETU”

Hitimisho!

·         Shetani siku zote anaandaa mpango wa kutuaibisha
·         Mungu siku zote anamawazo mema juu yetu
·         Watumishi wa Daudi walipoaibishwa walikimbia kurudi kwa Daudi mfalme wao
·         Sisi hatuna budi kukimbia na kurejea kwa Bwana wetu Yesu ili atutetee
·         Daudi alikuwa na tabia ya kumkimbilia Mungu ili asiaibishwe
·         Sisi nasi wakati wote tumkimbilie Bwana wetu Yesu hii ndio namna pekee ya kukataa aibu katika maisha yetu. 

Mkuu wa Wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.
0784394550
0718990796

Jumanne, 14 Machi 2017

Hazina katika vyombo vya Udongo.


Mstari wa Msingi: 2 Wakoritho 4:7Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu wala sio kutoka Kwetu


Utangulizi:-

Ni muhimu kwa kila mmoja wetu kujitambua na kujifahamu kuwa tumeumbwa kwa njia ya jabu sana, na hivyo ni vema katika maisha yetu tukampa Mungu utukufu siku zote na kumshukuru yeye anayetuwezesha na kuyashikilia maisha yetu, Maandiko yanatufananisha sisi kwa Mungu kama viumbe dhaifu sana yaani tumeumbwa kwa udongo, sisis ni kama chombo cha udongo katika mikono ya Mungu na Mungu baba yetu ndiye mfinyanzi kwa maana hiyo imetupasa kuishi na kuendena kwa unyenyekevu mkubwa, vipawa na akili na karama Mungu alizowekeza ndani ya Mwanadamu ni hazina sio ya kujivunia bali ni kwaajili ya utukufu wa Mungu.



Vyombo vya Dongo:

2 Wakoritho 4:7Lakini tuna hazina hii katika vyombo vya udongo, ili adhama kuu ya uwezo iwe ya Mungu wala sio kutoka Kwetu” tunaweza kuutafasiri mstari huu katika lugha nyepesi ya mkuu wa wajenzi hivi “Lakini kuna vitu vya thamani kubwa sana vimewekwa katika vyombo vya dhaifu vya udongo, ili utukufu na sifa kuu iwe ya Mungu wala sio kutoka kwetu”

Kwa nini Paulo mtume anazungumza maneno mazito namna hii na je yana maana gani kwetu? Ni muhimukwanza tukawa na ufahamu wa kutosha kuhusu vyombo vya dongo, Vyombo vya udongo anavyozungumza Paulo Mtume ni vyombo vilivyotengenezwa kwa udongo wa mfinyanzi na kuumbwa na mfinyanzi kwa ustadi kulingana na makusudi na matakwa ya mfinyanzi husika, Mara baada ya kufinywangwa vyombo hivyo vilichomwa kwa moto ili kuweza kuvifanya imara, baada ya hatua hiyo vingeweza kupakwa rangi na kuchorwa maua ya aina mbalimbali ya kupendeza na kuwa na muonekano mzuri sana

Nyakati za Biblia zamani sana vyombo vya udongo vilitumika kwa kusudi pia la kuhifadhi au kuficha hazina au vitu vyenye thamani sana, mfano halisi ni kuwa watu wa kale waliwahi kuhifadhi katika vyungu magombo ya chuo cha nabii isaya na vitabu vingine vya ngozi vilivyotumika zamani, Mfano halisi ni katika bonde la Qumran yaliwahi kuokotwa magombo ya ngozi yaliyokuwamo katika vyombo vya dongo vya kale, vijana wa kiislamu waliokuwa wakichunga Kondoo walikuwa wakirusha mawe huenda ni katika lengo la kutafuta kondoo, walisikia mlio Fulani wa chungu katika pango, walipofika kumbe ni chungu au mitungi iliyoundwa kwa dongo na ndani yake kulikuwa na ngozi zilizokuwa na maandishi, wao wakiwa hawajui maandishi hayo walitaka kuzitumia ngozi hizo kutengenezewa viatu, Mafundi waligundua kuwa yalikuwa ni maandiko matakatifu waliyapeleka kwa Kanisa na yakahifadhiwa chuo cha nabii Isaya kwa mfano kilipatikana kamili kama ilivyo Biblia katika magombo hayo.

Kutokana na mtazamo huo Paulo mtume anatukumbusha katika 2 Wakoritho 4:7 kuwa wanadamu tunafanana sana na vyombo hivyo vya udongo, karama, akili na vipawa alivyotupa Mungu ni hazina tu iliyohifadhiwa katika vyombo dhaifu sana vya dongo, vyombo ambavyo ni dhaifu na vinaweza kuvunjika wakati wowote na kwa njia rahisi “very delicate” ukweli huu haupingiki kwa sababu biblia iko wazi kuwa wewe na mimi tuliumbwa kwa Udongo Mwanzo 2:7 Biblia inasema “. BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Unaona? Mpendwa wewe na mimi ni mavumbi yaani ni udongo tu! Mungu analijua vema sana umbo letu na kukumbuka kuwa sisi ni mavumbi Zaburi 103:14 Biblia inasema Kwa maana Yeye anatujua umbo letu, Na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” Je unajua kuwa Mungu anakumbuka kuwa sisi tu mavumbi? Ndio ni muhimu kukumbuka lakini pamoja na kuwa Mungu ametuumba kwa udongo ameweka vitu vya thamani kubwa ndani yetu ambavyo hata Malaika hawana!

Kutokana na jinsi Mungu alivyotuumba kwa thamani kubwa kiasi hicho ingawa ni dhaifu sana lakini ameweka vitu vya thamani na ujuzi wa hali ya juu na karama na vipawa ndani yetu, Hata hivyo Mungu anatuonya katika neno lake kuendelea kumuheshimu yeye na kujihadhari na majivuno ya aina yoyote na kuenda mbele zake kwa unyenyekevu mkubwa na kumrudishia yeye utukufu, heshima na adhama kwa sababu yeye ni mfinyanzi na sisi ni kama vyombo hivyo dhaifu mikononi mwake Isaya 45:9Ole wake ashindanaye na Muumba wake! Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je! Udongo umwambie yeye aufinyangaye; Unafanya nini? Au kazi yako, Hana mikono?” Unaona ni maonyo makali kutoka kwa Mungu kupitia Nabii Isaya hatuwezi kuwa Jeuri kwa Mungu mimi na wewe ni kama Kigae Biblia inasema ole wetu kama tutashindana na Muumba! Isaya 64:8 “Lakini sasa, Ee Bwana, wewe u baba yetu; sisi tu udongo, nawe u mfinyanzi wetu; sisi sote tu kazi ya mikono yako.” Hatuwezi kushindana na Mungu Baba yetu inatupasa kuwa wanyenyekevu mno kwani sisi ni udongo na Mungu baba yetu ni mfinyanzi tu sisi ni dhaifu Mungu na atusaidie tusijivune kwa jambo lolote.

 "Paulo Mtume alikuwa dhaifu katika mwili lakini alijaa Neema na Kweli alikuwa kama Malaika"

Hazina katika vyombo vya udongo!

Paulo mtume anapozungumzia Hazina katika vyombo vya udongo alikuwa na maana pana zaidi ingawa msingi wake mkubwa ni jinsi Mungu alivyowekeza siri zake katika mioyo yetu, siri ya injili, Paulo anazungumzia nguvu na uwezo wa Mungu, vipawa na karama ambazo zimewekezwa ndani ya mtu kiasi ambacho mtu akisikia habari zako anaweza kudhani kuwa wewe ni jitu kubwa sana
Paulo alikuwa na ujuzi wa nguvu za Mungu na udhaifu wa mwili wa binadamu ambao ni kama udongo Mungu alimtumia Paulo mtume kwa miujiza ya viwango vya kupita kawaida Biblia inatoa majumuisho tu ya huduma ya Paulo na jinsi Mungu alivyomtumia kwa kusema 

·         Matendo 19:11Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida;”
·         Licha ya Mungu kumtumia Paulo kwa mijuiza mikubwa ya kupita kawaida lakini ni wazi kuwa Mtume Paulo ndiye mtume aliyefanya kazi kuliko mitume wote kama maandiko yanenavy 1Wakoritho 15:10 Lakini kwa neema ya Mungu nimekuwa hivi nilivyo; na neema yake iliyo kwangu ilikuwa si bure, bali nalizidi sana kufanya kazi kupita wao wote; wala si mimi, bali ni neema ya Mungu pamoja nami.
·         Licha ya Paulo kutumiwa na Mungu na kufanya kazi kuliko mitume wote yeye alipewa mafunuo makubwa sana kuliko mtume yala mtumishi yeyote Paulo alipelekwa mpaka Mbingu ya tatu akaonyeshwa mambo mazito na meneno mazito ambayo mengine ni magumu kuyaeleza angalia 2Wakoritho 12:2-4 “Namjua mtu mmoja katika Kristo, yapata sasa miaka kumi na minne, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua). Mtu huyo alinyakuliwa juu mpaka mbingu ya tatu.  Nami namjua mtu huyo, (kwamba alikuwa katika mwili sijui; kwamba alikuwa nje ya mwili sijui; Mungu ajua); ya kuwa alinyakuliwa mpaka Peponi, akasikia maneno yasiyotamkika, ambayo haijuzu mwanadamu ayanene”.
·         Paulo Mtume alikuwa Mwombaji, alikuwa akinena kwa lugha kuliko mtu yeyote, alikuwa na karama zote alikuwa na uwezo wa kuimba mpaka malango ya gereza yanafunguka, aliombea watu wa kila aina na kuponya wenye magonjwa, Paulo alikuwa Msomi ni Daktari wa Sheria aliyebobea na kadhalika 

Lakini pamoja na vipawa alivyokuwa navyo hakusahau kuwa yeye ni mavumbi alitambua kuwa Mungu ameweka hazina katika vyombo vya udongo tu na Historia ya kanisa inaeleza kuwa Paulo mtume ndiye aliyepatwa na majaribu mengi zaidi na mateso mengi zaidi kwaajili ya Kristo na injili, inasemakana kuwa Paulo mtume hakuwa jitu kubwa alikuwa ni mwembamba sana mwenye matege na nyele zake zilikuwa zimejinyonganyonga kama mmanga, aidha alikuwa na udhaifu katika mwili wake alikuwa anaumwa na pia alikuwa na macho dhaifu sana 2Wakoritho 12:7-9 Biblia inasema hivi “.Na makusudi nisipate kujivuna kupita kiasi, kwa wingi wa mafunuo hayo nalipewa mwiba katika mwili, mjumbe wa Shetani ili anipige, nisije nikajivuna kupita kiasi. Kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke. Naye akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu. Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu yangu”. 

Unaweza kuona! Paulom mtume alikuwa na mwili dhaifu na pia macho dhaifu aliomba kuondolewa tatizo hilo lakini Mungu alimwambia ni neema yangu tu inakutosha ili asiwe na Majivuno, Wagalatia 4:13-15 Lakini mwajua ya kuwa naliwahubiri Injili mara ya kwanza kwa sababu ya udhaifu wa mwili; na jaribu lililowapata katika mwili wangu hamkulidharau wala kulikataa, bali mlinipokea kama malaika wa Mungu, kama Kristo Yesu.  Ku wapi, basi, kule kujiita heri? Maana nawashuhudu kwamba, kama ingaliwezekana, mngaling'oa macho yenu, mkanipa mimi”.  Paulo mtume alikuwa na udhaifu katika mwili wake pamoja na kuombea wengi Mungu aliyaachia kwaajili ya utukufu wake ni kwaajili ya haya Paulo anaona kuwa Mungu ameweka hazina katika vyombo vya udongo.

Ndugu msomaji wangu hatuna cha kujivunia? Tunapaswa kuwa wanyenyekevu, tunapaswa kumpa Mungu utukufu, lakini hata kama ni wadhaifu hatuna hiki ama kile hiyo haipunguzi thamani ya kuumbwa kwako mfinyanzi ameliweka kusudi lake ndani yako usikate tamaa lakini kumbuka kuwa sisi ni binadamu ni daifu na Mungu ni mwenye nguvu ni mfinyanzi na tuishi mbali na majivuno ya aina yoyote tuwapo ulimwenguni

Mungu alimtuma Musa licha ya kuwa na kigugumizi, alimtumia Elisha licha ya kuwa na Upara, alimtumia Daudi licha ya kuwa na umri mdogo na kudharaulika hata kwa baba yake, acha kujidharau kwa sababu zozote zile 

Kumbuka kuwa asili ya nguvu zetu, uzuri wetu, ujuzi wetu, heshima yetu na mali zetu zimetokana na Mungu muumba wetu. Ukiyajua nhayo heri wewe ukiyatenda

Na mkuu wa wjenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote