Jumatatu, 27 Juni 2022

Imani ya kuhamisha Milima !


1Wakorintho 13:1-3 “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.”



Utangulizi:

Imani imekuwa ni mojawapo ya jambo Muhimu sana ambalo limeelezewa kwa ajabu katika maandiko, Imani imetumiwa na mashujaa wote wa imani tunaowasoma katika maandiko kama nyenzo ya kipekee sana ambayo iliwaletea matokeo makubwa sana katika maisha yao

Waebrania 11:32-35 “Nami niseme nini tena? Maana wakati usingenitosha kuleta habari za Gideoni na Baraka na Samsoni na Yeftha na Daudi na Samweli na za manabii; ambao kwa imani walishinda milki za wafalme, walitenda haki, walipata ahadi, walifunga vinywa vya simba, walizima nguvu za moto, waliokoka na makali ya upanga. Walitiwa nguvu baada ya kuwa dhaifu, walikuwa hodari katika vita, walikimbiza majeshi ya wageni. Wanawake walipokea wafu wao waliofufuliwa. Lakini wengine waliumizwa vibaya hata kuuawa, wasikubali ukombozi, ili wapate ufufuo ulio bora;”

Maandiko yanasema pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu, mtu awaye yote anayemuendea Mungu ni lazima aamini kuwa Mungu yupo na kuwa huwapa thawabu wale wawamtafutao Waebrania 11:6 “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza; kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao.”     Kwa msingi huo basi ni muhimu kufahamu kuwa mashujaa wote wa imani tunaowasoma katika maandiko, pamoja na mambo mengine vilevile walimuamini Mungu katika kiwango cha imani ya juu sana kiasi cha kukubalika kwa Mungu, Abraham kwa mfano alipojaribiwa na Mungu kumtoa Isaka kwa imani alikubali, yeye aliamini ya kuha hata akimkata kichwa Mungu atamfufua tena kutoka kwa wafu na atarejea na mwanaye  Waebrania 11:17-19 “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa, akamtoa Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea hizo ahadi alikuwa akimtoa mwanawe, mzaliwa pekee; naam, yeye aliyeambiwa, Katika Isaka uzao wako utaitwa, akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu; akampata tena toka huko kwa mfano.”

Aina za imani!

Katika agano jipya iko imani iokoayo, imani hii ni kumuamini Bwana Yesu kwa kukubali kazi aliyoifanya pale msalabani, na kwamba alikufa na kufufuka imani hii hutupa zawadi ya wokovu, imani hii kila mmoja anaweza kuipata kwa kumkubali Yesu kuwa bwana na mwokozi

Warumi 10:9-12 “Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu. Kwa maana andiko lanena, Kila amwaminiye hatatahayarika. Kwa maana hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao;”

Vilevile iko imani inayotokana na kuwepo kwa karama ya Roho Mtakatifu, ambayo huitwa neno la Imani au neno la mamlaka hii imetajwa katika 1Wakoritho 12:4-11 “Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule. Tena pana tofauti za huduma, na Bwana ni yeye yule. Kisha pana tofauti za kutenda kazi, bali Mungu ni yeye yule azitendaye kazi zote katika wote. Lakini kila mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye.” Karama ya imani ni karama kwa mtu aliyeokoka kumuwezesha mtu huyo kuwa na uwezo wa kutamka neno na likawa au likasababisha muujiza mfano 1Wafalme 17:1 “Basi Eliya Mtishbi, wa wageni wa Gileadi, akamwambia Ahabu, Kama Bwana, Mungu wa Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake, hakutakuwa na umande wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu.” Hapa Eliya anatamka kwa neno la Mungu na kile anachokitamka kinakuwa vilevile, Elisha pia alitamka kuuzwa kwa chakula kwa bei nafuu wakati kulikuwa na njaa kali haijawahi kutokea njaa ambayo ilipelekea hata watu kula watoto wao 2Wafalme 6:24-30 24. “Ikawa baada ya hayo, Ben-hadadi mfalme wa Shamu akakusanya majeshi yake yote, akakwea akauhusuru Samaria. Njaa ikawa kuu huko Samaria; na tazama, wakauhusuru, hata kichwa cha punda kikapata kuuzwa kwa vipande themanini vya fedha, na kibaba cha mavi ya njiwa kwa vipande vitano vya fedha. Ikawa mfalme wa Israeli alipokuwa akipita ukutani, mwanamke mmoja akamwita akisema, Unisaidie, bwana wangu, mfalme.  Akasema, Bwana asipokusaidia, nikusaidieje mimi? Ya sakafuni, au ya shinikizoni? Mfalme akamwambia, Una nini? Akajibu, Mwanamke huyu aliniambia, Mtoe mtoto wako, tumle leo, na mtoto wangu tutamla kesho.Basi, tukamtokosa mtoto wangu, tukamla; nikamwambia siku ya pili, Mtoe mtoto wako, tumle; naye amemficha mtoto wake. Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya huyo mwanamke, aliyararua mavazi yake; (naye alikuwa akipita juu ya ukuta;) na watu wakaona, na tazama, alikuwa amevaa magunia ndani mwilini mwake.”  Wakati hali halisi ikiwa ngumu kwa kiasi hicho Elisha anatamka kuwa kesho panapo saa hii chakula kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli ona 2Wafalme 7:1-10, “Elisha akasema, Lisikieni neno la Bwana; Bwana asema hivi, Kesho panapo saa hii, kipimo cha unga mzuri kitauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, langoni pa Samaria. Basi yule akida, ambaye mfalme alikuwa akitegemea mkono wake, akamjibu yule mtu wa Mungu, akasema, Tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akamwambia, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula. Basi walikuwapo watu wanne wenye ukoma, penye lango la mji; wakasemezana, Mbona tunakaa hapa hata tufe?  Tukisema, Tutaingia mjini, mjini mna njaa, nasi tutakufa humo; nasi tukikaa hapa, tutakufa vile vile. Haya! Twende tukaliendee jeshi la Washami; wakituhifadhi hai tutaishi; wakituua, tutakufa tu. Basi wakaondoka kabla ya mapambazuko, ili waende mpaka kituo cha Washami; na walipofika mwanzo wa kimo cha Washami, kumbe! Hapana mtu. Kwa maana Bwana alikuwa amewasikizisha Washami kishindo cha miendo ya magari, na kishindo cha farasi, kama kishindo cha jeshi kubwa; wakaambiana, Tazama, mfalme wa Israeli amewaajiri wafalme wa Wahiti, na wafalme wa Wamisri, waje wapigane nasi. Kwa hiyo wakaondoka, wakakimbia kungali giza bado, wakaziacha hema zao, na farasi zao, na punda zao, na kimo chao vile vile kama kilivyokuwa, wakakimbia wapate kujiponya nafsi zao. Basi wale wenye ukoma walipofika mwisho wa kituo, waliingia katika hema moja, wakala, na kunywa, wakachukua fedha, na dhahabu, na mavazi, wakaenda wakavificha; wakarudi, wakaingia katika hema ya pili, vile vile wakachukua vitu, wakaenda, wakavificha. Ndipo wakaambiana, Mambo haya tufanyayo si mema; leo ni siku ya habari njema, na sisi tunanyamaza; mkingoja hata kutakapopambazuka, madhara yatatupata; basi twende tukawaambie watu wa nyumba ya mfalme. Basi wakaenda, wakawaita mabawabu wa mji; wakawaambia, Tulifika kituo cha Washami, na tazama, hapana mtu ye yote huko, wala sauti ya mtu, ila farasi wamefungwa, na punda wamefungwa, na hema zao kama walivyoziacha.”  Kisha ikawaje ona neno la Mungu alilolisema Elisha lilitimizwa vilevile kama alivyotamka 2Wafalme 7:16-20 “Basi watu wakatoka, wakaziteka nyara hema za Washami. Ikawa kipimo cha unga mzuri kikauzwa kwa shekeli, na vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, sawasawa na neno la Bwana. Naye mfalme akamweka yule akida, ambaye alitegemea mkono wake, awasimamie watu langoni; na watu wakamkanyaga langoni, akafa; kama alivyosema yule mtu wa Mungu, aliyenena hapo mfalme alipomshukia. Ikatukia kama vile yule mtu wa Mungu alivyomwambia mfalme, Vipimo viwili vya shayiri kwa shekeli, na kipimo cha unga mzuri kwa shekeli, ndivyo vitakavyokuwa kesho, panapo saa hii, katika lango la Samaria; na yule akida akamjibu mtu wa Mungu, akasema, Sasa tazama, kama Bwana angefanya madirisha mbinguni, je! Jambo hili lingewezekana? Akasema, Angalia, wewe utaliona kwa macho yako, lakini hutakula. Ikampata vivyo hivyo, kwa kuwa watu wakamkanyaga langoni, akafa.”   

Mungu anatutaka tuwe na imani, tujiungamanishe naye katika kiwango cha kuwa na imani ya kuhamisha milima, kimsingi Mungu hafurahii sana kuona wakristo wanashindwa jambo, Yesu aliwakemea wanafunzi wake mara kwa mara kwa sababu walikuwa wanakosa imani hii

Mathayo17:15-20 “Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.”          

Sasa ni imani ya namna gani inahitajika ili kuhamisha milima Yesu anasema mkiwa na imani ndogo tu kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu ondoka hapa nao utaondoka huitaji imani kubwa sana unahitaji imani kidogo sana katika Mungu kukuletea ushindi na kutoa matamshi yenye mamlaka ya kiungu na mara moja utaweza kuona dunia ikishikishwa adabu

Mathayo 13:31-32 “Akawatolea mfano mwingine, akisema, Ufalme wa mbinguni umefanana na punje ya haradali, aliyoitwaa mtu akaipanda katika shamba lake; nayo ni ndogo kuliko mbegu zote; lakini ikiisha kumea, huwa kubwa kuliko mboga zote, ikawa mti, hata nyuni wa angani huja na kukaa katika matawi yake.”

Kumbe kiasi cha imani kinachohitajika ni kidogo tu nah ii ni kuonyesha kuwa watu wengi hawana imani, Mungu arupe kuwa na imani, Musa alikuwa mtu wa imani na alipokuwa akitamka jambo wakati mwingine hata kabla, hajaliomba Mbingu ziliweza kutekeleza matakwa yake ona:-

Hesabu 16:28-32 “Musa akasema, Kwa jambo hili mtajua ya kwamba Bwana amenituma, ili nifanye kazi hizi zote; kwa kuwa mimi sikuzifanya kwa akili zangu mwenyewe. Kama watu hawa wakifa kifo cha sikuzote, kama watu wote wafavyo, au kama wakipatilizwa kwa mapatilizo ya watu wote; hapo basi Bwana hakunituma mimi. Lakini Bwana akiumba kitu kipya, na hiyo nchi ikifunua kinywa chake na kuwameza, pamoja na wote walio nao, nao washukia shimoni wali hai; ndipo mtatambua ya kwamba watu hawa wamemdharau Bwana Basi ilikuwa, hapo alipokwisha kusema maneno haya yote, nchi iliyokuwa chini yao ikapasuka; nchi ikafunua kinywa chake, na kuwameza, na watu wa nyumba zao na wote walioshikamana na Kora, na vyombo vyao vyote.”

Matamshi haya ya kimamlaka yatatuletea ukombozi, mkubwa sana katika maisha yetu Mungu ataifanya dunia ijuie na ifahamu ya kuwa yuko Mungu, mwenye nguvu na mamlaka nay a kuwa neno lake haliongopi kamwe, wakristo tuinuke na kuwa waombaji na kuitafuta mamlaka hii ili kushikisha adabu watu wasio na uelewa kuhusu Mungu

Ni milima ya namna gani inayozungumzwa hapa?

Niliwahi kumsikia mwanatheolojia mmoja mkubwa sana na msomi akizungumzia kuwa Yesu alipokuwa akizungumzia mlima au milima alikuwa akizungumzia mlima halisi au milima halisi, ni ukweli ulio wazi kuwa lugha inayozungumzwa kibiblia ni lugha ya kinabii,  na kinabii maandiko yanapozungumzia mlina yanamaanisha kikwazochochote kigumu, jambo lolote lililogumu, kwa hiyo inahitajika wazo la kinabii na kimaandiko kujua kuwa Yesu aliposema utahamisha mlima au Paulo mtume anapozungumzia imani ya kuhamisha milima wote kwa pamoja katika mioyo yao na jamii ya wale waliokuwa wakizungumza nao walielewa alikuwa anazungumzia vikwazo vinavyoinuka juu ya mtu, au jaribu au jambo gumu unaweza kuona, Milima hii ni vikwazo vya namna mbalimbali vinavyoweza kujitokeza katika maisha yetu, lolote linalozuia breakthrough au mpenyo katika maisha yako, upinzani, magonjwa, kifo, Magumu, yanayoonekana hayawezekani, na hali zenye utata katika maisha yetu hizi zote zinaweza kuitwa mlima ona

 Zakaria 4:6-7 “Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi. Nani wewe, Ee mlima mkubwa? Mbele ya Zerubabeli utakuwa nchi tambarare; naye atalileta lile jiwe la kuwekwa juu kabisa pamoja na vigelegele vya, Neema, neema, ilikalie.”

Unaona lugha ya kinabii kamwe haimaniishi kuwa mlima unaotajwa ni mlima halisia HAPANA Mungu hawezi kupinga ana kanuni yake ya kimaumbile kumbuka wakati anaumba ulimwengu alihitimisha kwa kusema tazama kila kitu ni chema, sisi tu nao uwezo wa kuchagua ni mahali gani pa kuishi unaweza kuamua kuishi bondeni au mlimani kwa kadiri ya uumbaji wa kiungu, hatusomi katika historia wala shuhuda kuwa kuna mtu aliweza kuondoa mlima mahali, lakini kwa lugha ya kinabii mlima ni changamoto ngumu zinazikinzana na maisha yetu ya kila siku

Isaya 40:3-5 “Sikiliza, ni sauti ya mtu aliaye, Itengenezeni nyikani njia ya Bwana; Nyosheni jangwani njia kuu kwa Mungu wetu. Kila bonde litainuliwa, Na kila mlima na kilima kitashushwa; Palipopotoka patakuwa pamenyoka, Na palipoparuza patasawazishwa; Na utukufu wa Bwana utafunuliwa, Na wote wenye mwili watauona pamoja; Kwa kuwa kinywa cha Bwana kimenena haya.”

Unaona? milima hapa sio halisi ndugu zangu, milima inayotajwa hapa ni lugha ya mficho (Figurative) kama nilivyosema awali ni imani pekee ndiyo inayoweza kutuondolea mambo magumu ya kuyasawazisha hii maana yake yala yaliyoinuka juu yetu yanakuwa si kitu tena mbele yetu, kwa hiyo hakuna kitakachoweza kusimama mbele yako kutoka kwa mwaname au mwanamke kama utakuwa na imani

Marko 11:22-24 “Yesu akajibu, akamwambia, Mwaminini Mungu. Amin, nawaambia, Ye yote atakayeuambia mlima huu, Ng'oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yoyote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.

Mathayo 21:21-22. “Yesu akajibu, akawaambia, Amin, nawaambia Mkiwa na imani, msipokuwa na shaka, mtafanya si hilo la mtini tu, lakini hata mkiuambia mlima huu, Ng'oka, ukatupwe baharini, litatendeka. Na yo yote mtakayoyaomba katika sala mkiamini, mtapokea.”

Lugha hiyo pia ni lugha ya kukazia (hyperboles)kuonyesha namna na jinsi imani isivyoshindwa kitu na kuwa tunapomuamini Mungu na hata tunapomuomba Mungu kwa imani ni lazima tuamini na kusadiki kuwa lazima kutakuwepo matokeo makubwa sana.

Je imani yetu inaweza kuhamisha milima?

Ndio wakati wote tunapokuwa na imani imani hufanya mambo makubwa sana, lakini kuna maswala kadhaa ambayo yakikosekana katika maisha yetu tunaweza kuona mambo yakiwa ndivyo sivyo! Mathayo 17:14-21 1 “Nao walipoufikia mkutano, mtu mmoja akamjia, akampigia magoti, akisema, Bwana, umrehemu mwanangu, kwa kuwa ana kifafa, na kuteswa vibaya; maana mara nyingi huanguka motoni, na mara nyingi majini. Nikamleta kwa wanafunzi wako, wasiweze kumponya. Yesu akajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, kilichopotoka, nitakaa pamoja nanyi hata lini? Nitachukuliana nanyi hata lini? Mleteni huku kwangu. Yesu akamkemea pepo, naye akamtoka; yule kijana akapona tangu saa ile. Kisha wale wanafunzi wakamwendea Yesu kwa faragha wakasema Mbona sisi hatukuweza kumtoa? Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu. [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]

Wanafunzi wa Yesu walishindwa kumtoa pepo na Yesu aliwaonyesha sababu za kushindwa kwao, na kwanza aliwakemea mara kadhaa kwa sababu ya kukosa imani, kutia shaka, kuogopa jambo ambalo ni kinyume na imani.

Marko 4:40  Akawaambia, Mbona mmekuwa waoga? Hamna imani bado?”

Marko 9:19 “Akawajibu, akasema, Enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni kwangu.”

Mathayo 14:31 “Mara Yesu akanyosha mkono wake, akamshika, akamwambia, Ewe mwenye imani haba, mbona uliona shaka?

hawakuwa na imani kabisa kuna maswala kadhaa ambayo yakikosekana kwako hutawexa kuona Baraka za kiutendaji katika imani

1.       Ukikosa imani

2.       Ukiacha kuomba

3.       Ukiacha kufunga

4.       Ukiacha kulitumia neno la Mungu

Siri kubwa ya ushindi na imani inayoweza kuleta matokeo inakaa katika maswala hayo niliyoyataja ukiwa na tabia hizo unaweza kuondoa mlima wowote unaoweza kujitokeza katika maisha yako, Mathayo 17:21 “[Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]” Lakini kama inavyoelezwa katika maandiko ya kwamba silaha za vita vyetu zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome 2Wakoritho 10:4 (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;) ni kukosa muda wa kuomba, kusoma neno la Mungu na kufunga ndiko kunakotuletea changamoto kuwa gumu katika maisha, tunapofanyia kazi maombi, neno na kufunga tunaifanya imani yetu kukomaa na kuwa kali sana  na kwa sababu hiyo hakuna mlima unaowezxa kusimamam mbele yetu neno la Mungu ambalo ni upanga war oho utarahisisha sana kazi yetu ya kuhamisha milima kwa haraka wakati wote Yesu alikema kukosekana kwa imani na mambo yanayoweza kuifanya imani kuwa imara ni hayo

Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Jumapili, 19 Juni 2022

Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu !

Zaburi 23:1-6Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza. Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake. Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji. Waandaa meza mbele yangu, Machoni pa watesi wangu. Umenipaka mafuta kichwani pangu, Na kikombe changu kinafurika.  Hakika wema na fadhili zitanifuata Siku zote za maisha yangu; Nami nitakaa nyumbani mwa Bwana milele.”



Utangulizi:

Moja ya zaburi maarufu zaidi duniani labda kuliko zaburi zote ni zaburi ya 23, Zaburi hii imetumiwa sana na Wayahudi na Wakristo katika ibada na maombi lakini vilevile kwaajili ya kujenga imani, Kiini kikuu cha zaburi hii ni yale maneno Bwana ndiye Mchungaji wangu maneno haya yanazigusa jamii nyingi sana Duniani, Hata huko Mesopotamia, Inasemekana kuwa Mfalme Hammurabi katika mojawapo ya hutuba yake muhimu sana aliyowahi kuitoa alihitimisha kwa kusema “Mimi ndiye Mchungaji ninayehakikisha usalama na mafanikio ya watu wangu, utawala wangu utakuwa wa haki, wenye nguvu hawatawaonea wanyonge, na hata yatima na wajane watatendewa kwa haki” maneno ya kiongozi huyu wa zamani sana yalikuwa maarufu na huenda yakawa yalichangia mtunzi wa Zaburi hii kuyachanganua kwa kina katika uimbaji wake kwa kusudi la kutambua uhusiano wake na Mungu.

Zaburi hii ina mistari michache sana lakini yenye kubeba maana pana sana na hatuwezi kwa somo moja kama hivi kugusia kila neno linalozungumziwa na zaburi hii, Hata hivyo leo Mwalimu mkuu Roho Mtakatifu anatupeleka kuutazama mstari wa tano (5) katika zaburi hii ya (23) ili tuweze kujifunza kile ambacho Mungu amekikusudia kwetu .

Katika Zaburi 23:5 Daudi anasema “WAANDAA MEZA MBELE YANGU, MACHONI PA WATESI WANGU maneno haya peke yake yanaashiria uhusiano mkubwa sana na wa karibu ulioko kati yake na Mungu, lakini sio hivyo tu mstari huu unafunua heshima kubwa sana ya kifalme ambayo mwandishi anapewa na Mungu, kwani kumbuka kuwa anayeandaa meza hapa sio Daudi bali Mungu anamuandalia Daudi meza hivyo kimsingi mahali hapa pana maana pana na kubwa sana ambayo inaweza kumfaa kila mmoja wetu leo!

Ni muhimu kufahamu kuwa katika taratibu za kifalme, unapomualika mtu ambaye unamuheshimu sana katika utawala wako basi mgeni huyo rasmi labda ni rais au mfalme wa taifa lingine kama alikuja aidha kwa mazungumzo au kwa mualiko wa serikali yako au ziara ya kuimarisha uhusiano basi inapofika jioni kiongozi huyo mualikwa huandaliwa chakula maalumu ambacho huitwa dhifa ya kitaifa kwa kusudi la kusalimiana, kubadilishana mawazo, kufarijiana, kutiana moyo kujenga mahusiano, kufurahi na kisha kula pamoja, na unapokuwa umemualika kiongozi huyo mfalme au Rais aliyemualika mfalme mwingine anapaswa vilevile kuhakikisha kuwa anatoa na huduma zote ikiwemo ulinzi mkali na hata kama ana ulinzi wake, Kwa msingi hata kama ana maadui katika taifa lake au mataifa yanayomzunguka hawawezi kumgusa akiwemo katika himaya yako na itakuwa ni aibu kubwa sana kushindwa kuimarisha ulinzi wa mgeni wako huyu wa heshima endapo atauawa mbele yako, Dhifa hii kwa kawaida huonyesha kuwa umempa heshima ya juu sana mgeni wako! Na haya ni maswala muhimu katika mambo ya kidiplomasia.

Mwaka 1969 Mwenyekiti wa chama cha ukombozi wa Msumbiji Edward Mondlane aliuawa makao makuu ya chama cha FRELIMO yaliyokuwa jijini Dar es salaam baada ya kuletewa kikapu cha zawadi ya kitabu alichokuwa akikifungua kwenye nyumba ya rafiki yake wa kimarekani aliyeitwa Betty King, bomu lililipuka na kumuaa na mpaka leo haujajulikana aliuawa na nani ingawa inahisiwa ni wapinzani wa ukomonisti, hii inatufundisha kuwa mtu anaweza kuuawa hata mahali anakodhania kuwa ni salama!

Mungu aliwahi kuwapa heshima ya kidiplomasia na kuwaandalia meza wazee 74 wanaoheshimika sana katika Israel akiwemo Musa na haruni ingawa maandiko hayaelezei kwa kina ilikuwaje kuwaje ona lakini waliandaliwa meza mbinguni

Kutoka 24:9-11 “Ndipo akakwea juu, Musa, na Haruni, na Nadabu, na Abihu, na watu sabini miongoni mwa wazee wa Israeli; wakamwona Mungu wa Israeli; chini ya miguu yake palikuwa na kama sakafu iliyofanyizwa kwa yakuti samawi, kama zile mbingu zenyewe kwa usafi wake. Naye hakuweka mkono wake juu ya hao wakuu wa wana wa Israeli; nao wakamwona Mungu, wakala na kunywa.”

Hii ilikuwa ni neema kubwa na heshima ya juu zaidi kuwahi kutokea!, Daudi anaonyesha kuwa alikuwa ana uhusiano na Mungu wa karibu mno na anadhihirisha wazi kuwa neema ya Mungu ilikuwa juu yake kiasi cha kualikwa katika uwepo wa Mungu na kuandaliwa meza, huku Mungu akimlinda dhidi ya adui zake  na kumhakikishia usalama, huku akiendelea kuonyesha wema wake kwake, Daudi alikuwa mtu wa vita kwa hiyo alikuwa na maadui wengi sana, lakini kwa heshima hii aliyopewa na Mungu, hakuna adui anaweza kumgusa watamuona tu maana ameketi kwenye meza ya mwenye nguvu na hakuna mtu wa kumgusa kwa gharama yoyote.

Jambo hili pia vilevile licha ya kumhusu Daudi, lakini pia linaihusu Israel yote, nchi ya mkanaani haikuwa ya Israel kwa asili, lakini ilikuwa ni Mungu aliyemuahidi Ibrahimu kuwa atawapa, kwa msingi huo basi Israel wamealikwa katika nchi ya Mkanaani, Mwenyeji wao ni Mungu, Israel kule kaskazini inapakana na nchi ya Lebanon, na Syria, magharibi inapakana na Jordan na kusini iko Misri na eneo la wafilisti pale Palestina (Ukanda wa Gaza) kwa kawaida  wote tunafahamu namna na jinsi Israel inavyostawi na jinsi inavyokuwa na nguvu kubwa sana ya kijeshi, huku tukifahamu kuwa inazungukwa na adui pande zote na ambao wangetamani ifutwe mara moja, lakini wako salama kwa sababu wameandaliwa meza machoni pa watesi wao mwenyeji aliyewaalika ni Mungu.

Jambo hili vilevile linaweza likalihusu kanisa kwani kanisa limepewa kazi ngumu ya kuipeleka injili lakini kwa mfano wa kondoo na mbwa mwitu, aliyetualika kuihubiri injili alisema atakuwa pamoja nasi hata ukamilifu wa dahari. Haijalishi kuwa ni changamoto za aina gani tunapitia yeye mwenyewe anajua kuwa ametutuma kama kondoo katikati ya mbwa mwitu!.

Mathayo 10:16-20 “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua. Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga; nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa. Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu.”

Hata hivyo pamoja na hatari zote zinazoweza kumzunguka mtu mmoja mmoja au Israel au kanisa au wewe kumbuka Zaburi hii ya 23 ina maana panasana katika maisha yako yenyewe inaaanza kwa kusema Bwana ndiye Mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu, Na katika kuandaliwa meza kumbuka kuwa ni Mungu mwenyewe ndiye aliyekualika na ni yeye ndiye aliyekuheshimisha kwa hiyo zaburi hii inataka tuwe na ujasiri uliopitiliza na kutokuogopa!.

Zaburi hii inamtia nguvu kila mmoja kujua ya kuwa Mungu yuko pamoja nasi, na kuwa hatutapungukiwa na kitu, na kuwa lazima tuwe na ujuzi kuwa Mungu yuko pamoja nasi na kuwa hatatupungukia wala hatatuacha, haijalishi tunapitia maswala gani magumu au laini hata yawe mazingira yenye kutishia amani yetu na usalama wetu, Mungu atajishughulisha na kutupatia mahitaji yetu huku akituhakikishia usalama wetu.

Wafilipi 4:19 “Na Mungu wangu atawajazeni kila mnachokihitaji kwa kadiri ya utajiri wake, katika utukufu, ndani ya Kristo Yesu.”

Mungu anapotuandalia meza kazi yetu ni kusubiri tu, hatupaswi kuwa na wasiwasi kama ilivyo kwa wageni wengine unatulia tu mwenyeji wako anajua unachohitaji na anaweza kukuuliza akuletee kinywaji gani, unapokuwa unaandaliwa meza haupambani ukae wapi, haupambani ule nini,   haupambanii usalama wako ni yeye aliyekualika anajua unayoyahitaji kwa msingi huo unapaswa kuwa na utulivu, huwezi kujiandalia mwenyewe  ni aibu umealikwa sebuleni kwa mtu kisha unaanza kufungua friji, unaingia jikoni, unaulizia matunda na kadhalika  Hapana haipaswi kuwa hivyo kwani yeye anayeandaa meza ataleta kila tunachiokihitaji, Israel walipokuwa wanaalikwa katika inchi ya kanaani mwenyeji wao aliwapa maji, aliwapa na mana wakala na aliwapa kware walipolilia.

Kutoka 16:14-16 “Na ulipoinuka ule umande uliokuwa juu ya nchi, kumbe! Juu ya uso wa bara kitu kidogo kilichoviringana, kidogo kama sakitu juu ya nchi. Wana wa Israeli walipokiona, wakaambiana, Nini hiki? Maana hawakujua ni kitu gani. Musa akawaambia, Ndio mkate ambao BWANA amewapa ninyi, mle. Neno hili ndilo aliloagiza BWANA, Okoteni ninyi kitu hicho kila mtu kama ulaji wake ulivyo; kichwa pishi, kama hesabu ya watu wenu ilivyo; ndivyo mtakavyotwaa, kila mtu kwa ajili ya hao walioko hemani mwake.”

Daudi kwa zaburi hii alikuwa anamuamini Mungu ana ujasiri katika Mungu anamjua Mungu kuwa hawezi kumuangusha yeye atatupa mahitaji yetu kwa kadiri ya neema ya uhitaji wetu maandiko yanaema katika  Waebrania 4:16 “Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.”

Mungu ndiye mwenyeji amemkaribisha mgeni kwenye dhifa maana yake ni nini kila kitu kimekwisha kuandaliwa kwaajili yake, ni yeye ndiye aliyetupa mwaliko sisi sio wazamiaji, hivyo tunamtegemea yeye kwa mahitaji yetu yote ya kimwili na kiroho na muhimu zaidi atatulinda Mungu sio tu atatupatia kila tunachikihitaji katika ulimwengu huu lakini kama Mungu atakuwa pamoja nasi milele

2Petro 1:3 “Kwa kuwa uweza wake wa Uungu umetukirimia vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa, kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe.”

Kwa msingi huo Zaburi ya 23:5 inapandisha chati ya mwamini ambaye amealikwa katika karamu ya mwana kondoo na katika uwepo wa Mungu uhakika wa wema na fadhili za Mungu kutufuata siku zote za maisha yetu na kukaa katika uwepo wake milele

 

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima.

Jumanne, 14 Juni 2022

Kaburi liko wazi!

Luka 24:1-3 “Hata siku ya kwanza ya juma, ilipoanza kupambazuka, walikwenda kaburini, wakiyaleta manukato waliyoweka tayari. Wakalikuta lile jiwe limevingirishwa mbali na kaburi, Wakaingia, wasiuone mwili wa Bwana Yesu.”


Utangulizi: 

Moja ya mambo ambayo wanadamu wengi sana huyaogopa duniani ni pamoja na Kaburi, au eneo la makaburini, sehemu nyingi sana duniani na katika jamii nyingi duniani kumekuwepo na hofu ya aina Fulani ambapo watu huogopa sana kaburi au makaburini, lakini sio hivyo tu hata pamoja na kuweko kwa hofu ya kifo, bado watu wengi wanahofia tukio la kuzikwa wakifikiri ni moja ya tukio gumu, au wakidhani kuwa wanaweza kuzikwa wakiwa na fahamu zao, au wakifikiri itakuwaje kama itatangazwa kuwa nimekufa kwa bahati mbaya kisha nikashituka nikiwa kaburini hofu ya aina hii imekuwepo kwa miaka mingi, katika lugha ya kiyunani (Greek) hofu hii ya kisaikolojia kwa kiyunani inaitwa TAPHOPHOBIA  neno hilo ni neno la kiyunani lenye muunganiko wa maneno makuu mawili TAPHO – ambalo maana yake ni Kaburi (Grave) na PHOBIA – Maana yake hofu, kwa hiyo neno TAPHOPHOBIA maana yake ni hofu ya kaburi, kwa hiyo kimsingi watu wengi sana wanaogopa kifo lakini hata hivyo ni ukweli uliowazi kuwa watu wengi wanaogopa zaidi kaburi, kwa hiyo kuna hofu ya kifo na kuna hofu ya kaburi, au hofu ya kufikia mwisho!, sasa basi ni muhimu kufahamu kuwa kufufuka kwa Yesu, sio tu kunatusaidia kutokuogopa kifo lakini vilevile kunatusaidia kutokuogopa nguvu za kaburi au kuzimu! Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu vifuatavyo:-

·        
  
Kuzikwa kwa Yesu Kristo.

·         Umuhimu wa kaburi lililo wazi.

·         Kaburi liko wazi.

Kuzikwa kwa Yesu Kristo.! 

Mara kadhaa tumezungumzia sana kuhusu Mateso ya Bwana wetu Yesu, na huenda wahubiri wengi hawajawahi kuzungumzia kuhusu kuzikwa kwa Yesu Kristo, lakini ni muhimu sana kuuthibitishia ulimwengu kuwa Kristo alizikwa, kuzikwa kwa Yesu Kristo ni moja ya jambo, Muhimu sana katika injili kwa sababu Manabii waliliona  na kulitabiria pia kama walivyotabiria mambo mengine. 

Isaya 53:8-9 “Kwa kuonewa na kuhukumiwa aliondolewa; Na maisha yake ni nani atakayeisimulia? Maana amekatiliwa mbali na nchi ya walio hai; Alipigwa kwa sababu ya makosa ya watu wangu. Wakamfanyia kaburi pamoja na wabaya; Na pamoja na matajiri katika kufa kwake; Ingawa hakutenda jeuri, Wala hapakuwa na hila kinywani mwake.” 

Unaweza kuona Isaya nabii aliyeishi miaka 700 kabla ya Kristo, alitabiri kuhusu kuzikwa yaani kufanyiwa kaburi kwa Yesu Kristo, Hili ni jambo la msingi sana kama sehemu ya injili unapozungumzia mateso ya Kristo na hata kufufuka kwake basi tukio la kuzikwa ni la muhimu na ni sehemu ya injili ambayo hata Paulo Mtume alikabidhiwa ona 

1Wakorintho 15:1-4 “Basi, ndugu zangu, nawaarifu ile injili niliyowahubiri; ambayo ndiyo mliyoipokea, na katika hiyo mnasimama, na kwa hiyo mnaokolewa; ikiwa mnayashika sana maneno niliyowahubiri isipokuwa mliamini bure. Kwa maana naliwatolea ninyi hapo mwanzo yale niliyoyapokea mimi mwenyewe, ya kuwa Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, kama yanenavyo maandiko; na ya kuwa alizikwa; na ya kuwa alifufuka siku ya tatu, kama yanenavyo maandiko;” 

Unaweza kuona kumbe unabii na injili vyote vinakazia swala zima la kuwa Yesu alizikwa, mtu akifa hilo ni jambo lingine na akizikwa hilo ni jambo lingine, Neno kuzikwa katika kiingereza linatumika neno “Burial” au “Interment” au “inhumation” ambalo maana yake ni hatua ya mwisho kabisa ya kuwepo duniani kwa kuuweka mwili wa Mwanadamu chini au kuuchoma (Cremation) au kuufungia na kuhitimisha huzuni au huruma kwa kumuweka mtu au mwili wake na kuufunika kabisa, kwa hiyo licha ya kufa ukizikwa maana yake umetoweka kabisa, kibinadamu imethibitika na kukubalika kuwa huwezi kuweko tena, Hivyo Yesu alizikwa maana yake ilithibitishwa kuwa hawezi kuweko tena kabisa duniani, lakini na pamoja na tendo hilo, serikali ya kirumi iliweka walinzi ili kuhakikisha kuwa pale alipozikwa hakuna kitu kinaweza kubatilika. Kimsingi jamii inapomzika mtu maana yake imekubali kuwa asiweko tena kabisa duniani! Sasa Yesu alizikwa lakini sio kuzikwa tu na ulinzi uliwekwa kuhakikisha kuwa amezikika. 

Mathayo 27:62-66 “Hata siku ya pili, ndiyo iliyo baada ya Maandalio, wakuu wa makuhani, na Mafarisayo wakamkusanyikia Pilato, wakasema, Bwana, tumekumbuka kwamba yule mjanja alisema, alipokuwa akali hai, Baada ya siku tatu nitafufuka. Basi amuru kwamba kaburi lilindwe salama hata siku ya tatu; wasije wanafunzi wake wakamwiba, na kuwaambia watu, Amefufuka katika wafu; na udanganyifu wa mwisho utapita ule wa kwanza. Pilato akawaambia, Mna askari; nendeni mkalilinde salama kadiri mjuavyo. Wakaenda, wakalilinda kaburi salama, kwa kulitia lile jiwe muhuri, pamoja na wale askari walinzi.” 

Asee sio tu kuwa mtu amekufa hapa lakini AMEZIKWA na hata maziko yake yanawekewa ulinzi kwa siku tatu, kuhakikisha kuwa hafufuki mtu, ndio maana katika nguvu ya injili hatuwezi kamwe kupuuzia swala la kuzikwa “ALITESWA, AKAFA AKAZIKWA…”  Wako watu katika maisha yako sio tu unapokuwa umesitawi inawapa shida sana, na watatamani uharibikiwe, upotee na ikiwezekana historia yako ifutike na usambaratike kabisa wanaweza hata kulinda hata taarifa zako zisisambae watakuchafua ikiwezekana usisimame milele hawa wanataka kukufuta “inhumation” “Cremation” kuhakikisha kuwa hauko tena hata tuta lako la kaburi lisiweko, ni kama kwa kaburi la Colonel Muammar Gadafi, au Osama Bin Laden wameuawa na makaburi yao yamefutika hawako kabisa, waliochukizwa nao hawakutaka hata wazikwe katika hali ya kawaida, wawe wamefutika hivyo ndivyo adui za Kristo Yesu walivyotaka iwe, kwa hiyo kuzikwa, kutoweka kusahaulika ni sehemu ya injili unaposema Yesu aliteswa, akafa usiseme tu akafufuka siku ya tatu kumbuka alizikwa! 

Umuhimu wa Kaburi lililo wazi. 

Kufufuka kwa Yesu Kristo ndio moja ya muujiza Mkubwa sana katika ukristo, kama Yesu hangelifufuka imani yetu ingekuwa ni imani potofu na ya hovyo kabisa kuliko zote, nisikilize ni kufufuka kwa Yesu Kristo pekee kunakotuthibitishia uwezo wa Mungu kwamba hatuwezi kukata tamaa katika jambo lolote lile, Kaburi lililo wazi ni ushahidi ulio wazi wa kutimizwa kwa unabii wa Mfalme Daudi ya Kwamba Mungu hatamuacha Mtakatifu wake aone uharibifu

Zaburi 16:10 “Maana hutakuachia kuzimu nafsi yangu, Wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu.”

Kaburi lililo wazi ni ishara iliyowazi ya ushindi unaobainisha kuwa Mungu anauwezo wa kufufua hata pale mtu anapofikia hatua ya kuzikwa, Yesu yuko hai nani wazi kuwa nguvu ileile iliyomfufua Yesu Kristo ina uwezo wa kufufua lolote katika maisha yetu ambalo linaonekana kama linataka kufa na hata kama limekufa machoni pa watu, Bado ana uwezo wa kulifufua.

Warumi 8:11 “Lakini, ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu” 

Nyakati za zamani sana alama ya wakristo ilikuwa sio msalaba ilikuwa ni kaburi lililowazi, kaburi lililo wazi ni ishara ya kuwa Yesu amefufuka na kuwa Mauti haimuwezi, ni ishara kwetu kuwa hakuna mtu anaweza kuifuta historia ya kuwepo kwa masihi, ni ushahidi kwetu kuwa Mungu wetu yu hai na ana nguvu, ni ishara kwetu kuwa hata kama watu watakukusudia ufutike hawataweza kukufuta wewe juu ya uso wa dunia, Kaburi lilowazi ni ushahidi kuwa yuko mwenye mamlaka mmoja tu mwenye ufunguo ambao akifunga hakuna afunguaye wala akifungua hakuna awezae kufunga mwenye mamlaka ya kufisha na kuhuuisha ni Yesu pekee! 

Ufunuo 1:17-18 “Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa. Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu.” 
     

Kaburi liko wazi!

Msikilizaji wangu mpendwa nimepewa mamlaka ya kukutangazia ya kuwa kaburi liko wazi, tutaweza kupitia kila aina ya changamoto tuwapo duniani, kila aina ya mawimbi na mateso na matukano na dharau za watu, watu wanaweza kupanga mikakati ya kishetani katika kuhakikisha kuwa tunapotea na kutoweka na kuwa historia yetu inafagiliwa na kufutiliwa mbali na tunazikwa na kaburi zetu zinawekewa muhuri kuhakikisha ya kuwa hatuchomoki lakini nataka nikutangazie kuwa kaburi liko wazi, hakuna mahali ambako mkono wa Mungu hauwezi kufika na kukuchomoa, alimezwa Yona na nyangumi na nyangumi akamtapika, alimezwa Yesu na Kaburi na kaburi likamtapika, aliwekwa Danieli katika tundu la simba na makanwa ya simba yakazuibwa, walitupwa Daniel, Shadrak na Abednego na katika tanuri ya moto yaani kaburi la moto ili wafanyiwe “Cremation” lakini mauti ilishindikana nakutangazia kwa jina la Yesu Kristo hakuna mauti katika kazi yako, hakuna mauti katika masomo yako, hakuna mauti katika ndoa yako, hakuna mauti katika biashara yako, hakuna mauti katika sifa zako, hakuna mauti katika familia yako hakuna mauti kokote kule itakayokuweza! Ndio maana kaburi liko wazi, kaburi lililo wazi ndio kiini cha injili inayotuthibitishia kuwa Yesu yu hai, mtetezi wetu yu hai hajafa naye atasimama juu ya nchi apate kututetea, kila mauti inayokusudiwa, katika kila sehemu ya maisha yako naitangazia kuwa Kaburi liko wazi, mwambie shetani kaburi liko wazi, mwambie adui yako kaburi liko wazi, kaburi lililo wazi ni ishara ya kuwa kuna maitumaini kila wakati na kuwa Mungu hatatuacha tuone uharibifu wa namna yoyote! Na badala yake tutawaona adui zetu wakitoweka kwa haraka.!

 

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!



Jumapili, 22 Mei 2022

Kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako !


Mwanzo 26:12-22 “Isaka akapanda mbegu katika nchi ile, akapata mwaka ule vipimo mia kwa kimoja, BWANA akambariki. Na mtu huyu akawa mkuu, akazidi kusitawi, hata akawa mkuu sana. Akawa na mali ya kondoo, na mali ya ng'ombe, na watumwa wengi. Hao Wafilisti wakamhusudu. Na vile visima vyote walivyochimba watumwa wa baba yake, siku za Ibrahimu babaye, Wafilisti walikuwa wamevifukia, wakavijaza kifusi. Abimeleki akamwambia Isaka, Utoke kwetu, maana wewe una nguvu sana kuliko sisi. Basi Isaka akatoka huko akapiga kambi katika bonde la Gerari, akakaa huko.  Isaka akarudi akavichimbua vile visima vya maji walivyovichimba siku za Ibrahimu babaye; maana wale Wafilisti walikuwa wamevifukia baada ya kufa kwake Ibrahimu; naye akaviita majina kufuata majina alivyoviita babaye. Watumwa wa Isaka wakachimba katika lile bonde, wakapata kisima cha maji yanayobubujika. Wachungaji wa Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema, Maji haya ni yetu. Ndipo akakiita jina la kile kisima Eseki, kwa sababu waligombana naye. Wakachimba kisima kingine, wakagombania na hicho tena. Akakiita jina lake Sitna. Akaondoka huko akachimba kisima kingine, wala hicho hawakukigombania. Akakiita jina lake Rehobothi, akasema, Kwa kuwa sasa BWANA ametufanyia nafasi, nasi tutazidi katika nchi.”


 

Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kuwa katika ulimwengu tulionao ni watu wachache sana tena wenye ukomavu wa kifikra wanaoweza kustahimili pale mtu mwingine anapobarikiwa, na wako wengi wenye kushangaza katika upande wa pili ambao hawawezi kuvumilia pale Mungu anapokubariki, Baraka za Mungu kwetu zina tabia ya kuvutia umati mkubwa sana wa watu, lakini pia zinauwezo wa kuvutia maadui kwa upande mwingine, kwa msingi huo kila mmoja anapokuwa amebarikiwa na mbaraka wa Mungu na mbaraka huo ukamtajirisha ni lazima aelewe kuwa atakuwa na maadui na hawa ni wale ambao hawawezi kuvumilia Baraka zako na hivyo wakati mwingine tunaweza kujikuta tunavuna Baraka lakini tunapata na changamoto za Baraka hizo, kimsingi Mungu katika mapenzi yake kamili alikusudia kuwa Baraka zake zisilete huzuni iwayo yote ona Mithali 10:22 “Baraka ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.”   Lakini kwa sababu tuko duniani wakati mwingine Baraka hizo zitaambatana na huzuni au udhia kutokana na watu wanaotuzunguka kushindwa kustahimili kishindo cha Baraka za Mungu kwetu, ni muhimu kufahamu kuwa watu wanaweza kushindwa kustahimili Baraka za Mungu kwetu katika mazingira yafuatayo-

1.       Wakati mwingine Mungu anapotutakabali.

Watu wengine wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zetu tunapotakabaliwa na Mungu, kutakabaliwa na Mungu katika lugha ya kiingereza ni “When God looked us with favor” ni tukio la kukubalika kiibada Mungu kukubali au kusikiliza maombi yetu na dua zetu, wengine wanachukizwa kwa nini huyu amesikilizwa na Mungu, kwanini huyu ameolewa mie bado, kwanini huyu amejenga mie bado, kwa nini huyu ana mashamba mimi bado, kwa nini huyu ana watoto mimi bado wako watu wanashindwa kuvumilia wanapoona Mungu amekutakabali, wanaweza kuona wivu, wanaweza kukukasirikia na wanaweza hata kukuua.

 

Mwanzo 4:1-8 “Adamu akamjua Hawa mkewe; naye akapata mimba, akamzaa Kaini, akasema, Nimepata mtoto mwanamume kwa BWANA.  Akaongeza akamzaa ndugu yake, Habili. Habili alikuwa mchunga kondoo, na Kaini alikuwa mkulima ardhi. Ikawa hatimaye Kaini akaleta mazao ya ardhi, sadaka kwa BWANA. Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana. BWANA akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde. Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani] Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua.”

 

Habili alipoteza maisha kwa sababu ya kutakabaliwa na Mungu, kaini alijawa na wivu wenye uchungu na kumkusudia nduguye mabaya, unaweza kukusudiwa mabaya, unaweza kupigwa vita kwa sababu una huduma nzuri, unaweza kupigwa vita kwa sababu unahubiri vizuri, kwa sababu unaimba vizuri, kwa sababu una sura nzuri, kwa sababu uko vizuri katika kila eneo kwa nini inafanyika hivyo ni kwa sababu wako watu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

               

2.       Wakati mwingine tunapopata kibali kuliko wao.

 

Watu wengine wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zako kwa sababu tu unakibali, unakubalika kuliko wao, kwa sababu ya wao kujiona duni “inferiority complex” kutokana na kukubalika kwako wataanza kukuchukia na kukuonea wivu na hata kukupiga vita kwanini kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako ona

 

Mwanzo 37:3-5 “Basi Israeli akampenda Yusufu kuliko wanawe wote, maana ni mwana wa uzee wake, akamfanyia kanzu ndefu. Ndugu zake wakaona ya kuwa baba yao anampenda kuliko ndugu zake wote, wakamchukia, wala hawakuweza kusema naye kwa amani. Yusufu akaota ndoto, akawapa ndugu zake habari, nao wakazidi kumchukia;”

 

Ndugu zake Yusufu walipoona kuwa Yusufu anapendwa zaidikuliko wao, na baba yake amemnunulia nguo nzuri anapiga pamba kali kuliko wao,  wanabadilishana mawazo na mzee Yakobo, Yusufu anatoa taarifa kwa baba yake kuhusu kila kitu nyumbani jamaa wakahisi anapendelewa walishindwa kuvumilia Baraka hii ya kibali na wakazidi kumchukia sana, wako watu wanaweza kuchukizwa nawe kwa wazi au mioyoni mwao na wakawa wanaumia tu kwa sababu wewe unapendwa, kwa sababu wewe una kibali, una kibali kazini, unakibali kwa bosi, una kibali kikubwa na ni Mungu amesababisha kibali hicho na wanaokuzunguka wakashindwa kuvumilia Baraka zako na wanaanza kuchukizwa nawe na kukuonea wivu kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

3.       Wakati mwingine tunapopewa sifa zaidi kuliko wao

 

Watu wengine wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zako kwa sababu tu umesifiwa kuliko wao unaupiga mwingi katika jamii kuwazidi, unaposifiwa zaidi au sana kuliko wao, wao wanaaza kujiona duni na kupoteza kujiamini na hivyo wanaweza kukuonea wivu na kujenga uadui na kuanza kukupiga vita tangu waliposikia sifa zako kwanini watafanya hivyo kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

1Samuel 18:6-9 “Hata ikawa, walipokuwa wakienda, hapo Daudi aliporudi baada ya kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika miji yote ya Israeli, kwa kuimba na kucheza, ili kumlaki mfalme Sauli; wakatoka na matari, na shangwe, na vinanda. Nao wale wanawake wakaitikiana wakicheza, wakasema, Sauli amewaua elfu zake, Na Daudi makumi elfu yake. Basi Sauli akaghadhibika sana, na maneno haya yakamchukiza; akasema, Wamempa Daudi makumi elfu, na mimi wamenipa elfu tu; kuna nini tena awezayo kupata, isipokuwa ni ufalme? Sauli akamwonea Daudi wivu tangu siku ile     

 

Unaona ni Daudi ambaye kwa nia njema alikuja kumpiga Goliath ambaye alikuwa ni adui wa taifa zima alisumbua ati kwa hiyo shujaa wa wafilisti alipigwa na Daudi ambaye ndani yake kulikuwa na upako wa kiungu ambao ulimwezesha kuwatetea wana wa Israel na jina la Mungu likatukuzwa watu walipomsifu tayari Sauli alimuonea wivu na kuanza uadui na Daudi, wako watu wanaweza kuanzisha uadui na wewe na wakakuchukia na kukupiga vita lakini sababu kubwa ni kuwa hawawezi kuvumilia Baraka zako!, angalia kuwa Sauli akimuwa mfalme na Daudi alikuwa mchunga kondoo tu, dunia ni yenye kushangaza kwa sababu wakati mwingine mtu mkubwa na mwenye nguvu kuliko wewe anakupiga vita wewe uliye mdogo kwa nini kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

4.       Wakati Mwingine tunapopandishwa Cheo.

 

Wako watu ambao wanaweza kushindwa kuvumilia Baraka zako kwa sababu eti wewe umekuwa mkubwa kuliko wao kwa sababu wewe una cheo kikubwa kuliko wao, unajua watu wanadhani cheo ni kuukata au kuuchinja au kuula, lakini Mungu huwa anatupa majukumu ili tuwatumikie watu hivyo kutokana na Baraka za kiungu Mungu anaweza kusababisha uinuliwe juu sana na ukawa na sifa njema lakini jambo la kushangaza ni kuwa wako watu hawataweza kustahimili kuinuliwa kwako na kwa sababu hiyo wataanza kupanga mikakati ya kibinadamu kabisa ili wakumalize kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

Daniel 6:1-5 “Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake. Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake.”

 

Unaona watu wanapata taabu sana kwa sababu una cheo na unaupiga mwingi katika mamlaka uliyo nayo kwa hiyo zinatafutwa sababu ili wakukamate, uweze kutiwa hatiani, Daniel alianza kutafutia namna hii iko kila mahali, iwe ni makazini, au makanisani, na kwenye taasisi mbalimbali kuna watu ni waroho wa Madaraka wanatafuta kila linalowezekana wakuangushe tu na hawajisikii vizuri wewe ukitamalaki! Kwa nini  kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

5.       Wakati mwingine kwa sababu unajenga.

 

Wako watu wengine kwa sababu wewe uko kwenye ujenzi unajenga basi wivu unawainuka na wanatamani kupingana na kile unachikifanya, wakati nakumbuka nilipokuwa najenga nyumba yangu, wachwi walikuja na kufanya uchawi wao wa kusotea huu ni uchawi wa kuhakikisha kuwa nyumba inadumaa na haiwezi kujengeka kama unaishia kwenye linta inakuwa ni kwenye linta tu, lakini mimi nilimtegemea Mungu hata baada ya wachawi kusotea na kuacha kinyesi kwenye nyumba ile, nilimuomba Mungu na ujenzi ukaenda kwa kasi sana na nikafanikiwa na ndipo wachawi walipokuja waziwazi na kugombana na mimi kwa hasira kali sana kwa nini kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zangu, Nehemia alipokuwa anaujenga ukuta wa Yerusalem maadui wa wayahudi walitoa maneno ya kufuru kwa sababu Nehemia na wayahudi walikuwa kwenye ujenzi ona

 

Nehemia 4:1-8 “Lakini ikawa, Sanbalati aliposikia ya kwamba tulikuwa tukiujenga ukuta, akaghadhibika, akaingiwa na uchungu sana, akawadhihaki Wayahudi. Akanena mbele ya nduguze na mbele ya jeshi la Samaria, akisema, Wayahudi hawa wanyonge wanafanyaje? Je! Watajifanyizia boma? Watatoa dhabihu? Au watamaliza katika siku moja? Je! Watayafufua mawe katika chungu hizi za kifusi, nayo yameteketezwa kwa moto? Basi Tobia, Mwamoni, alikuwa karibu naye, akasema, Hata hiki wanachokijenga, angepanda mbweha, angeubomoa ukuta wao wa mawe. Sikia, Ee Mungu wetu; maana tunadharauliwa; ukawarudishie mashutumu yao juu ya vichwa vyao, ukawatoe watekwe katika nchi ya uhamisho; wala usiusitiri uovu wao, wala isifutwe dhambi yao, mbele zako; kwa maana wamekukasirisha mbele ya hao wanaojenga. Basi tukaujenga ukuta; nao ukuta wote ukaungamanishwa kiasi cha nusu ya kimo chake; maana watu walikuwa na moyo wa kufanya kazi. Lakini ikawa, Sanbalati, na Tobia, na Waarabu, na Waamoni, na Waashdodi, waliposikia ya kuwa kazi ya kuzitengeneza kuta za Yerusalemu inaendelea, na ya kuwa mahali palipobomoka panaanza kuzibwa, basi wakaghadhibika mno; wakafanya shauri wote pamoja kuja kupigana na Yerusalemu, na kufanya machafuko humo.”

 

Unaona kuna watu wanaweza kutoa maneno ya kejeli kwako, au hata kughadhibika na kufanya machafuko lakini ukiangalia sababu kubwa ni kua hawawezi kuvumilia Baraka zako, wala usishangae, wala usifadhaike they can’t handle your blessing  wakati mwingine utajenga nyumba watasema ni nyumba basin i kakibanda tu ili mradi wakukatishe tama usiogope ni kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!

 

6.       Wakati mwingine ili wakunyamazishe

 

Kuna watu wakati mwingine hawafurahii kuona ukivuma au ukisifiwa au jina lako likiwa na nguvu, au ukishangiliwa hivyo kutokana na wivu wanatamani wakunyamazishe, wanapoona unafanya vizuri unakubalika na una nafasi kubwa sana sifa zako zinaenea kila mahali utashangaa wanakunyamazisha au wanataka hata na watu wanaokusifia wanyamaze ona

 

Luka 19:37-40 “Hata alipokuwa amekaribia matelemko ya mlima wa Mizeituni, kundi zima la wanafunzi wake walianza kufurahi na kumsifu Mungu kwa sauti kuu, kwa ajili ya matendo yote ya uwezo waliyoyaona, wakasema, Ndiye mbarikiwa Mfalme ajaye kwa jina la Bwana; amani mbinguni, na utukufu huko juu. Baadhi ya Mafarisayo waliokuwa katika mkutano wakamwambia, Mwalimu, uwakanye wanafunzi wako. Akajibu, akasema, Nawaambia ninyi, wakinyamaza hawa, mawe yatapiga kelele.”

 

Unaona wakati mwingine unaweza kujikuta unanyamazishwa ziko namna nyingi watu watataka wakunyamazishe kwa sababu sifa zako zinaenea na kukua kwa kasi na wanajisikia vibaya hawawezi kustahimili, kwa nini hii ni kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako.!

 

7.       Wanataka uwasujudie

 

Kuna watu wengine huwa wakipata cheo tayari wanageuka kuwa miungu watu na wanataka uwatetemekee na kuwasujudia na ikiwa hutetemeki wala kuwasujudia wanachukia sana na hiyo inaweza kuwa sababu ya kuanzisha mapambanao na wewe, na hata kukuangamiza ona

 

Esta 5:9-13 “Basi Hamani alitoka siku ile kwa furaha na ukunjufu wa moyo; lakini Hamani alipomwona Mordekai mlangoni pa mfalme, ya kwamba hasimami wala kutetemeka mbele yake, alijaa ghadhabu juu ya Mordekai. Walakini Hamani akajizuia, akaenda zake nyumbani kwake; akatuma kuwaita rafiki zake na Zereshi mkewe. Naye Hamani akawasimulia habari za fahari ya mali zake, na wingi wa watoto wake, nayo mambo yote pia ambayo mfalme amemfanikisha katika hayo, na jinsi alivyompandisha juu ya maakida na watumishi wa mfalme. Zaidi ya hayo Hamani akasema, Naye malkia Esta hakumkaribisha mtu ye yote pamoja na mfalme katika karamu aliyoiandaa, ila mimi peke yangu; hata na kesho pia nimealikwa naye pamoja na mfalme. Bali haya yote yanifaa nini, pindi nimwonapo yule Mordekai, Myahudi, ameketi mlangoni pa mfalme?

 

unaona ni kwanini Hamani pamoja na fahari yake aliyokuwa nayo alikuwa hajisikii raha ? kwa sababu alikuwa anataka asujudiwe, wako watu wanataka watetemekewe, wababaikiwe kwa sababu tu eti wana madaraka makubwa wa kutetemekewa ni Mungu tu yeye ndiye mwenye destiny Hatima ya maisha yetu, na sio mwanadamu

 

Esta 3:1-6 “Baada ya hayo mfalme Ahasuero alimwongezea cheo Hamani bin Hamedatha, Mwagagi, akampandisha, akamwekea kiti chake juu ya maakida wote waliokuwapo pamoja naye. Nao watumishi wote wa mfalme, walioketi mlangoni pa mfalme, wakainama na kumsujudia Hamani, maana ndivyo alivyoamuru mfalme kwa habari zake. Bali Mordekai hakuinama, wala kumsujudia. Basi watumishi wa mfalme walioketi mlangoni pa mfalme wakamwambia Mordekai, Mbona wewe waihalifu amri ya mfalme? Ikawa, waliposema naye kila siku asiwasikilize, wakamwarifu Hamani, ili kuona kama mambo yake Mordekai yatasimama; maana alikuwa amewaambia ya kuwa yeye ni Myahudi. Hata Hamani alipoona ya kwamba Mordekai hainami wala kumsujudia, alighadhibika sana. Akaona si shani kumtia mikono Mordekai peke yake; maana wamemjulisha kabila yake Mordekai; kwa hiyo Hamani alitaka kuwaangamiza Wayahudi wote waliokuwa wakikaa katika ufalme wote mzima wa Ahasuero, yaani, watu wake Mordekai.”

 

Umeona wako watu wanadhani wewe huwaheshimu kwa sababu huwasujudii sie wengine ni wayahudi tunaheshimu kila mtu lakini hatuabudu watu, tunamwabudu Mungu peke yake kama maandiko yalivyotuelekeza Luka 4:8 “Yesu akajibu akamwambia, Imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake  wakati mwingine visa na mikasa huinuka kwa sababu watu wanataka kuabudiwa, mtu unamuheshimu laki ni anataka kuvuka mipaka ya kiheshima na kwenda mbali zaidi, Mordekai aliyekuwa myahudi alikuwa amejifunza kuwa mwanadamu wa kawaida muheshimu lakini wakumuinamia  na kumtetemekea ni Mungu peke yake anayestahili kuabudiwa na kusujudiwa wengine wakiona hufanyi hivyo hawawezi kuvumilia kwa sababu hauabudu mwanadamu.!

 

8.       Wakati mwingine kwa sababu unatumiwa na Mungu kuliko wao

 

Kuna watu wakati mwingine hawafurahii kuona namna Mungu anavyokutumia katika karama na vipawa mbalimbali kuliko wao na kwa sababu hiyo watajisikia wivu moyoni na wakati mwingine watazusha maneno ya uwongo kwa kusudi la kukuchafulia huduma yako, wanaweza kusema unafanya mioujiza kwa kutumia nguvu za giza, wanaweza kusema wewe ni freemason, wanaweza kusema wewe ni mchawi, anaweza kusema wewe ni imani potofu, hutumii jina la Yesu na kadhalika hiii yota inafanyika kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka na upako ambao Mungu ameweka ndani yako ona

 

Mathayo 12:22-24 “Wakati ule akaletewa mtu mwenye pepo, kipofu, naye ni bubu; akamponya, hata yule bubu akanena na kuona. Makutano wote wakashangaa, wakasema, Huyu siye mwana wa Daudi? Lakini Mafarisayo waliposikia, walisema, Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo

 

Unaona Mafarisayo hawakufurahia Yesu kukubalika kutokana na ishara na miujiza aliyokuwa akiifanya, sisis nasi Yesu alituambia kuwa Mwanafunzi hawezi kumpita Mwalimu wake maana yake yale majaribu ambayo Mwalimu aliyapitia sisi nasi tutayapitia na kuzidi, tumetumwa kama Kondoo katikati ya mbwa mwitu, lazima adui wa Baraka za kiungu ndani yetu watajitokeza na kuleta kila aina ya upinzani katika jambo lolote ambalo kwalo Mungu ameweka mkono wake usiogope jambo kubwa na la msingi la kukumbuika ni kuwa hawawezi kuvumilia Baraka zako!

Tumeona katika Mstari wetu wa Msingi kuhusu baba yetu wa Imani nabii Isaka ya kuwa Mungu alimbariki upeo, ilikuwa kuna njaa katika nchi ya kanaani na ilikuwa ni kawaida kuwa kukiwa na njaa kama ilivyokuwa wakati wa Ibrahimu baba yake, wao walikimbilia Misri kwa sababu ya chakula, hata hivyo Mungu alimuonya Isaka kuwa asishuke kwenda Misri, na Mungu akaweka Baraka zake, Isaka na baba yake Ibrahimu walikuwa ni wataalamu wa kuchimba visima, walifahamu namna na jinsi ya kuchimba maji, na huenda pia Isaka alikuwa na ujuzi wa kumwagilia, njaa ilipokuwa kali yeye alipanda mbegu na bila shaka alimwagilia hivyo Mungu alimbariki na akampa kuvuna mara mia lakini sio hivyo tu mali yake iliongezeka na umaarufu wake ukawa mkubwa mno, hivyo akastawi na kuwa mtu mkubwa sana, wafilisti walianza kuona wivu, kila kisima alichokichimba wao walikigombea na kukifukia au kudai kuwa ni cha kwao, Biblia imeweka wazi kuwa wafilisti WAKAMHUSUDU yaani maana yake waluiona wivu tena wivu wenye uchungu, Isaka alikuwa mpenda amani hivyo aliwaachia na kuchimba kingine lakini walifanya fitina hii ama ile na mwisho wakaona haya Isaka akachimba na kingine na wakapata Maji na wakakiita kisima kile REHOBOTHI maana yake sasa Bwana ametufanyia nafasi, Isaka aliteseka kwa sababu ya Baraka zake, yako mateso mengine unayapitia na changamoto nyingine unazipitia sio kwa sababu umemkosea Mungu bali kwa sababu Mkono wa Mungu uko juu yako na wanaokuzunguka hawawezi kustahimili wala kuvumilia aina ya upako ulio nao, aina ya huduma uliyo nayo aina ya Baraka ulizoanazo, aina ya uimbaji unaoimba, aina ya mavazi unayovaa, aina ya uzuri ulio nao na kila aina ya Baraka kwa kawaida ina tabia ya kuvutia watu na maadui kwa nini ulipobarikiwa wengine walikukimbia ni kwa sababu hawawezi kuvumilia Baraka zako!, wako ambao hawatavumilia wewe kuzaa, hawatavumilia wewe kuolewa, hawatavumilia we kuwa na mtoto, hatawatavumilia wewe kufanikiwa au kua na ustawi wa aina yoyote ilekatika jamii kwa nini kwa sababu wako watu watakupoenda na kukusoegelea lakini wako wengine hawataweza kuvumilia Baraka zako! Bwana Mungu wa Baba zangu Ibrahim, Isaka na Yakobo na akufanyie nafasi, ili ufurahie Baraka zako bila usumbufu kutoka kwa maadui katika jina la Yesu nakuombea amen!

 

Na Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Jumapili, 8 Mei 2022

Mfalme juu ya Punda


Mathayo 21:1-5Hata walipokaribia Yerusalemu, na kufika Bethfage, katika mlima wa Mizeituni, ndipo Yesu alipotuma wanafunzi wawili akiwaambia, Enendeni mpaka kijiji kile kinachowakabili, na mara mtaona punda amefungwa, na mwana-punda pamoja naye; wafungueni mniletee. Na kama mtu akiwaambia neno, semeni, Bwana anawahitaji; na mara huyo atawapeleka. Haya yote yamekuwa, ili litimie neno lililonenwa na nabii, akisema, Mwambieni binti Sayuni Tazama, mfalme wako anakuja kwako, Mpole, naye amepanda punda, Na mwana-punda, mtoto wa punda.”


Utangulizi:

Ni muhimu kufahamu kwamba tukio la Yesu Kristo kupokelewa kwa shangwe jijini Yerusalem, lilikuwa ni tukio la kipekee sana lililofanywa na watu, sawa kabisa na namna watu wanavyompokea mfalme, tukio hili halikuwa tukio la bahati mbaya kwani vilevile lilikuwa ni sehemu ya kutimizwa kwa maandiko ya kinabii kuhusu kuja kwa mfalme wa kipekee ambaye angejibu mahitaji yote ya wanadamu Nabii Zekaria alilitabiri tukio hili miaka 400 kabla ya kuzaliwa kwa Yesu ona;-

Zecharia 9:9Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda.”

Swali moja kubwa ambalo wanafunzi wengi wa maandiko hupenda kujiuliza ni kwamba, iko wazi kuwa Yesu alipokelewa Yerusalem kwa shangwe kubwa sana watu walimfurahia kwa matawi ya mitende na hata kutandaza nguo zao njiani, lilikuwa ni tukio la kipekee sana ambalo hakuna mfalme amewahi kufanyiwa,Mungu roho Mtakatifu aliinua mioyo ya watu na wakasangilia kwa nguvu sana kuingia kwa Maishi pale Sayuni, lakini swali kubwa kwanini mfalme huyu awe amepanda punda?  Hili ndio swali kubwa na la Muhimu kwa kila mmoja wetu kujiuliza na kutafuta majibu.

Wafalme huja na Majibu ya mahitaji ya watu!

Moja ya Kazi kubwa sana ya wafalme wa zamani na labda huenda hata sasa ilikuwa ni pamoja na kutawala mfalme alipaswa kuwa na majibu ya aina yoyote dhidi ya mahitaji ya watu wake, wafalme walitakiwa kutatua changamoto zilizowakabili watu hata kuamua kesi za aina mbalimbali mfano;- 

1Wafalme 3:16-28 “Ndipo wanawake wawili, makahaba, walimwendea mfalme, wakasimama mbele yake. Na mwanamke mmoja akasema, Ee bwana wangu, mimi na mwanamke huyu tunakaa katika nyumba moja; nami nalizaa nilipokuwa pamoja naye nyumbani. Kisha, siku ya tatu baada ya kuzaa kwangu, ikawa mwanamke huyu naye akazaa; na sisi tulikuwa pamoja; hapakuwa na mtu mwingine pamoja nasi nyumbani, isipokuwa sisi wawili tu. Na mtoto wa mwanamke huyu akafa usiku, maana alimlalia. Akaondoka kati ya usiku, akamwondoa mtoto wangu ubavuni pangu, mimi mjakazi wako nilipokuwa usingizini, akamweka kifuani pake, na mtoto wake mwenyewe, aliyekuwa amekufa, akamweka kifuani pangu. Nilipoondoka asubuhi nimnyonyeshe mtoto wangu, kumbe? Amekufa. Hata asubuhi nilipomtazama sana, kumbe! Siye mtoto wangu niliyemzaa. Ndipo yule mwanamke wa pili akasema, Sivyo hivyo; bali mtoto wangu ndiye aliye hai, na mtoto wako ndiye aliyekufa. Na mwenzake akasema, Sivyo hivyo; bali mtoto wako ndiye aliyekufa, na mtoto wangu ndiye aliye hai. Ndivyo walivyosema mbele ya mfalme.  Ndipo mfalme akasema, Huyu anasema, Mtoto wangu yu hai, na mtoto wako amekufa. Na huyu anasema, Sivyo hivyo; bali mtoto aliyekufa ni wako, na mtoto aliye hai ni wangu. Mfalme akasema, Nileteeni upanga. Wakaleta upanga mbele ya mfalme. Mfalme akasema, Mkate mtoto aliye hai vipande viwili, kampe huyu nusu, na huyu nusu. Ndipo mwanamke yule, ambaye mtoto aliye hai ni wake, akamwambia mfalme kwa maana moyoni mwake alimwonea mtoto wake huruma, akasema, Ee bwana wangu, mpe huyu mtoto aliye hai, wala usimwue kamwe. Lakini yule mwingine akasema, Asiwe wangu wala wako; na akatwe. Ndipo mfalme akajibu, akasema, Mpe huyu wa kwanza mtoto aliye hai, maana yeye ndiye mama yake. Na Israeli wote wakapata habari za hukumu ile aliyoihukumu mfalme wakamwogopa mfalme; maana waliona ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake, ili afanye hukumu.”

Wafalme walitakiwa kujibu hoja zozote ngumu za watu wao waliowatembelea kuhitaji msaada katika maeneo mbalimbali ya maisha yao 1Wafalme 10:1 “Na malkia wa Sheba aliposikia habari za Sulemani juu ya jina la Bwana, alikuja ili amjaribu kwa maswali ya fumbo.” Biblia ya kiingereza inatumia maneno “she came to test her with HARD questions       Hata hivyo Mfalme Suleimani pia aliweza kutoa majibu ya maswali yote aliyouliza malikia wa Sheba. Hata hivyo maandiko pia yanatueleza kuwa kuna wakati ambapo wafalme walikosa majibu na uwezo wa kutatua changamoto kadhaa na hivyo walilia, na kufunga na kuvaa magunia au kurarua mavazi yao. Angalia kwa mfano:-

2Wafalme 6:25-30 “Njaa ikawa kuu huko Samaria; na tazama, wakauhusuru, hata kichwa cha punda kikapata kuuzwa kwa vipande themanini vya fedha, na kibaba cha mavi ya njiwa kwa vipande vitano vya fedha. Ikawa mfalme wa Israeli alipokuwa akipita ukutani, mwanamke mmoja akamwita akisema, Unisaidie, bwana wangu, mfalme. Akasema, Bwana asipokusaidia, nikusaidieje mimi? Ya sakafuni, au ya shinikizoni? Mfalme akamwambia, Una nini? Akajibu, Mwanamke huyu aliniambia, Mtoe mtoto wako, tumle leo, na mtoto wangu tutamla kesho. Basi, tukamtokosa mtoto wangu, tukamla; nikamwambia siku ya pili, Mtoe mtoto wako, tumle; naye amemficha mtoto wake. Ikawa, mfalme alipoyasikia maneno ya huyo mwanamke, aliyararua mavazi yake; (naye alikuwa akipita juu ya ukuta;) na watu wakaona, na tazama, alikuwa amevaa magunia ndani mwilini mwake.”

Unaona kwa msingi huo Mfalme alikuwa na kazi ngumu ya kutatua changamoto za maisha ya watu,  ukiacha swala la kutatua changamoto ya maisha ya watu, mfalme pia alitakiwa kuwa mtu wa vita na mwenye uwezo wa kutwatetea watu wake dhidi ya adui zao kwa kupigana kwa silaha na kwa uwezo wa kujihami, wafalme walipaswa kuwa watu wa vita, Heshima ya mfalme ilikuwa kupitia uwezo wake wa kuamua mambo na kuwapigania watu wakena kuwashindia dhidi ya adui zao, mfano

 1Samuel 17:1- 11. Wakati huo Wafilisti walikusanya majeshi yao kwa vita, nao wakakusanyika huko Soko, ulio mji wa Yuda, wakatua kati ya Soko na Azeka, katika Efes-damimu. Naye Sauli na watu wa Israeli wakakusanyika, wakatua katika bonde la Ela, nao wakapanga vita juu ya hao Wafilisti. Wafilisti wakasimama juu ya mlima upande huu, na Waisraeli wakasimama juu ya mlima upande huu, napo palikuwa na hilo bonde katikati. Ndipo akatoka shujaa katika kambi ya Wafilisti, aliyeitwa Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shibiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega; yake. Na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. Naye akasimama, akawapigia kelele majeshi ya Israeli akawaambia, Mbona mmetoka kupanga vita? Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama akiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana.”

Mfalme juu ya Punda !

Sasa moja ya tukio la kushangaza ni kuwa pamoja na kuwa wafalme walikuwa ni watu waliotakiwa kujibu hoja na mahitaji ya watu ya aimna mbalimbali na kuwashindia watu vita dhidi ya adui zao, ni muhimu kufahamu kuwa wafalme walipotaka kuonyesha nguvu zao na ukuu wao wakati wote walitumia farasi katika kusafiri kwao, Farasi ilikuwa ni alama ya vita na ufahari na utajiri, kwa hiyo kila mfalme aliyekuwa anataka kuonyesha ufahari wake alitumia farasi, farasi ni mnyama anayeonyesha uhodari, wakati punda ni mnyama anayeonyesha huduma,  kama watu walikuwa wakijivuna walijivunia magari yao ya farasi kwani hayo ndio yalikuwa yakidhihirisha nguvu na uwezo wao

Zaburi 20:1-9 “Bwana akujibu siku ya dhiki, Jina la Mungu wa Yakobo likuinue. Akupelekee msaada toka patakatifu pake, Na kukutegemeza toka Sayuni. Azikumbuke sadaka zako zote, Na kuzitakabali dhabihu zako. Akujalie kwa kadiri ya haja ya moyo wako, Na kuyatimiza mashauri yako yote. Na tuushangilie wokovu wako, Kwa jina la Mungu wetu tuzitweke bendera zetu. Bwana akutimizie matakwa yako yote. Sasa najua kuwa Bwana amwokoa masihi wake;Atamjibu kutoka mbingu zake takatifu.Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu. Wao wameinama na kuanguka, Bali sisi tumeinuka na kusimama. Bwana, umwokoe mfalme, Utuitikie siku tuitayo.”

Watu wanachohitaji ni kuokolewa kutoka katika changamoto zinazowakabili, haijalishi mfalme anakuja namna gani, anaweza akaja na magari ya farasi lakini akawa hana majibu ya kutosheleza mioyo ya watu wake Zekaria alitabiri kuwa anakuja mfalme mnyenyekevu, mpole hana majivuno wala majigambo wala hana nia ya kutafuta kiki au ufahari yeye anakuja na wokovu anakuja na kifurushi kitakachotuletea amani ni mfalme wa tofauti mwenye uwezo wa kutatua changamoto za watu kwa kiwango kikubwa sana yeye anatabiriwa kuwa angekuja akiwa amepanda punda na mwana punda mtoto wa punda, hii ilikuwa ni ishara madhubuti ya kumtambua mfalme huyo mwenye nguvu zote lakini mnyenyekevu!

 Zakaria 9:9-10 “Furahi sana, Ee binti Sayuni; Piga kelele, Ee binti Yerusalemu; Tazama, mfalme wako anakuja kwako; Ni mwenye haki, naye ana wokovu; Ni mnyenyekevu, amepanda punda, Naam, mwana-punda, mtoto wa punda. Na gari la vita nitaliondoa liwe mbali na Efraimu, na farasi awe mbali na Yerusalemu, na upinde wa vita utaondolewa mbali; naye atawahubiri mataifa yote habari za amani; na mamlaka yake yatakuwa toka bahari hata bahari, na toka Mto hata miisho ya dunia.”

Maandiko yanaonyesha kuwa mfalme huyu

o   Atakomesha vita

o   Silaha za vita kama upinde utaondolewa mbali

o   Hatakuja na majeshi

Yeye atatangaza amani kwa mataifa yote na ufalme wake utakuwa ni wa dunia nzima, Luka 2:14 “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.” Mfalme atakayeingia Yerusalem, yaani katika mlima wa Sayuni akiwa juu ya Punda, ni simple but powerful ni mnenyekevu na mpole lakini ana majibu yote yeye atatoa suluhu ya mahitaji yetu yote na hivyo tunachopaswa kusema ni Hosana mwana wa Daudi, mfalme mwenye majibu ya wokovu wako haji na vifaru, haji na ufahari wowote anakuja na mwana punda, humble but very powerful, huyu ndiye mfalme aliyetabiriwa na Zekaria na Mathayo anatudhihirishia kuwa Yesu ndiye mfalme huyu ambaye amekuja kulitimiza andiko, ana hekima kuliko suleimani na ana nguvu kuliko Daudi, yeye atatupigania na hakuna kinachoweza kusimama mbele yake yeye ndiye mtetezi wa adui zetu na mkombozi wetu dhidi ya unyonge si mwingine ni Yesu !

Rev. Innocent Kamote

Mkuu wa wajenzi Mwenye Hekima!

Jumatatu, 2 Mei 2022

Shika sana ulichonacho!


Ufunuo 3:10-12 “Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi. Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako. Yeye ashindaye, nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, wala hatatoka humo tena kabisa, nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya.”


Utangulizi:

Wito unatolewa kwa kanisa na kila mwanadamu mmoja mmoja kushika sana au kwa lugha nyingine kutunza sana kile alichonacho, asije mtu akaitwaa taji yako, Hii ni kwa sababu kuja kwa Yesu kunakaribia, lakini sio hivyo tu kuna misukumo mingi sana duniani na nguvu kubwa ya upinzani ambayo iko kinyume na kile ambacho Mungu amekubarikia kwacho katika maisha haya, Yesu Kristo alikuwa akizungumza na kutoa ujumbe wake kwa makanisa saba yaliyokuwepo katika Asia ndogo huko uturuki, akiyaonya na kuwatia moyo katika maswala mbalimbali na hapa anazungumza na kanisa la Filadelfia ambalo kimsingi lilikuwa na mambo mazuri ukilinganisha na mengine na Yesu anawataka wajitunze, wawe makini ili wasije wakapoteza kile walicho nacho ambacho ni kizuri, kimsingi sina mpango wa kuzungumzia Makanisa yale saba,wala nyakati zile saba za historia ya kanisa kwani vyote vinaweza kutumika kuzungumza na kanisa, lakini Mpango wangu ni kuzungumza na wewe au na hata mimi mwenyewe, ya kwamba mara kadhaa Mungu ametubariki kwa mambo mengi mazuri, mfano, Kazi nzuri, Ndoa nzuri, kibali, mambo mema, vipawa, kujulikana, na kadhalika ziko zawadi nyingi na nafasi nyingi nzuri ambazo Mungu ametubarikia nazo katika maisha yetu lakini wengi wetu huwa tunajikuta nafasi zile, vipawa vile, zawadi zile na Baraka zile hatuna uwezo wa kuzitunza, au tunazipoteza kabisa hii ni kwa sababu shetani anavutiwa sana na kila jambo jema ambalo Mungu amewekeza katika maisha yetu na hivyo anakusudia kutuharibia, wakati mwingine tunapambana kufa na kupona na kumwaga jasho letu jingi kwaajili ya jambo Fulani lakini unapokuja wakati wa mavuno adui anakuja na kutuharibia na kuvuruga kabisa mpango wa Mungu katika maisha yetu, hapa ndipo mahali Yesu anatutaka tushike sana kile tulichonacho!  Hali mkama hii iliwasumbua sana Israel wakati wa waamuzi kabla Gideoni hajaitwa ona!;- 

Waamuzi 6:2-6,11 “Mkono wa Midiani ulikuwa na nguvu juu ya Israeli; tena kwa sababu ya Midiani wana wa Israeli walijifanyia hayo mashimo yaliyo milimani, na hayo mapango, na hizo ngome. Basi ikawa, hapo Israeli walipokuwa wamepanda mashamba, Wamidiani wakakwea, na Waamaleki, na hao wana wa mashariki; wakakwea juu yao; wakapanga marago juu yao, na kuyaharibu hayo maongeo ya nchi, hata ufikapo Gaza, wala hawakuacha katika Israeli riziki ziwazo zote; kondoo, wala ng'ombe, wala punda. Kwa maana walikwea na ng'ombe zao na hema zao, wakaja mfano wa nzige kwa wingi; wao na ngamia zao pia walikuwa hawana hesabu; nao waliingia katika hiyo nchi ili kuiharibu. Israeli walitwezwa sana kwa sababu ya Wamidiani; nao wana wa Israeli wakamlilia Bwana. Malaika wa Bwana akaenda akaketi chini ya mwaloni uliokuwa katika Ofra, uliokuwa mali yake Yoashi, Mwabiezeri; na mwanawe Gideoni alikuwa akipepeta ngano ndani ya shinikizo, ili kuificha machoni pa Wamidiani.”

Unaona shetani atasubiri umetaabika sana na pale unapokuwa unatarajia kuwa utapumzika utagundua kuwa ndio kwanza vita inaanza upya na ni kama hakuna kulala na endapo utajisahau shetani atachukua mateka kila kitu na kukuacha ukiwa unalia na kulalamika wakati kilikuwa mikononi mwako na kiko kwenye uwezo wako!

o   Maana ya neno taji

o   Shika sana kile ulichonacho!

Maana ya neno taji:

Neno taji katika lugha ya kiyunani linasomeka kama neno “STEMMA” kwa kiibrania ni “TIARA” ambayo maana yake ni kwa kiingereza “Top”, au “Climax”, au “The highest” au “Uppermost point” au “surface of something”, au “Exeed”  kwa hivyo neno taji maana yake ni kilele cha ubora, ni ile hali ya kuwa juu, kama ni nyota kuwa na mwangaza mkubwa zaidi kuliko wengine, au hali ya kuwa na kitu cha ziada kinachozidi wengine, ni kilele cha furaha yako, kwa hiyo neno la Mungu linatuonya kutunza kile kilichobora ambacho Mungu ametupa kwa sababu adui yetu shetani hawezi kufurahia kile ulicho nacho au kile ambacho ndio shauku yako uweze kukifikia, Mungu anatutaka kutokudharau na kufikiri kuwa kile tulichonacho sio bora wakati kuna watu wanatamani ukipoteze ili wakipate, kwa msingi huo ni muhimu kufahamu kuwa tunapokuwa duniani tuko kwenye uwanja wa vita ambapo kuna mapambano ambapo, kile ulichonacho ambacho wewe unaweza kuwa huujali na wala haumshukuru Mungu ya kuwa unacho kuna wengine wanakitamani na watapigana wakipate kwa msingi huo lazima ujue namna ya kukitunza taji yako inaweza kuchukuliwa na akapewa mtu mwingine ona:-

2Samuel 12:29-31 “Basi Daudi akawakusanya watu wote akaenda Raba, akapigana nao, akautwaa. Kisha akamnyang'anya mfalme wao taji toka kichwani pake; na uzani wake ulikuwa talanta ya dhahabu, nayo ilikuwa na vito vya thamani ndani yake; akavikwa Daudi kichwani. Akazitoa nyara za huo mji, nyingi sana. Naye akawatoa watu waliokuwamo, akawaweka kwenye kazi ya misumeno, na sululu za chuma, na mashoka ya chuma, akawatumikisha, tanuuni mwa matofali ndivyo alivyoifanya miji yote ya wana wa Amoni. Kisha Daudi akarudi na watu wote Yerusalemu.”

Ni muhimu kukumbuka kuwa kile unachokitamani wewe kuna na wenzako wanakitamani na kama utakuwa dhaifu kuna watu watapita mbele yako na watakichukua, usifikiri kuwa kuna mtu atakubeba au kukuhurumia, hakuna wa kukubeba lazima wewe mwenyewe upambane, Mungu anaweza kuachilia Baraka Fulani, lakini ni jukumu letu sisi kulinda, ukitegemea wanadamu wakubebe kumbuka nao wana mahitaji yao watakuacha utasota sana watapita mbele yako na watachukua kile wewe unatamani kuwa nacho na kukuacha unalalamika tu

Yohana 5:2-7 “Na huko Yerusalemu penye mlango wa kondoo pana birika, iitwayo kwa Kiebrania Bethzatha, nayo ina matao matano. Ndani ya hayo jamii kubwa ya wagonjwa walikuwa wamelala, vipofu, viwete, nao waliopooza, [wakingoja maji yachemke. Kwa maana kuna wakati ambapo malaika hushuka, akaingia katika ile birika, akayatibua maji. Basi yeye aliyeingia wa kwanza baada ya maji kutibuliwa, akapona ugonjwa wote uliokuwa umempata.] Na hapa palikuwa na mtu, ambaye amekuwa hawezi muda wa miaka thelathini na minane. Yesu alipomwona huyu amelala, naye akijua ya kuwa amekuwa hali hiyo siku nyingi, alimwambia, Wataka kuwa mzima? Yule mgonjwa akamjibu, Bwana, mimi sina mtu wa kunitia birikani, maji yanapotibuliwa; ila wakati ninapokuja mimi, mtu mwingine hushuka mbele yangu.”

Wakati wote unaweza kuona kama kuna kitu unakitamani ni lazima uchukue hatua wewe mwenyewe na usisubiri mwanadamu aje akusaidie, lazima upambane kuhakikisha kuwa unafikia kilelelcha furaha yako au hakikisha kuwa unamuita Yesu na kumuomba akusaidie haja ya moyo wako!.

Mungu anapokuwa amekubariki kwa kitu Fulani adui wakati wote anavutiwa na kitu hicho, na atainuka kupigana na kitu ambacho Mungu anataka au amekufanyia, wakati wote adui  atakuja wakati mambo yanapokaribia kuwa mazuri, baada ya wewe kutaabika sana ndipo anapokuja kuteka na kumbuka wakati wote utakuwa mwenyewe ukipambana ukifanikiwa watu wengi sana watakuzunguka, ukifeli kila mmoja atakukimbia, watu hawatakushambulia kwa sababu uko kama wao watakushambulia kwa sababu una taji, una kitu cha ziada umewazidi, una mambo mazuri, una nyumba nzuri, una gari nzuri, una cheo kizuri, una mshahara mzuri, una mafanikio, una kibali, una mvuto, una mke mzuri, una mume mzuri, una kipato kizuri, unazalisha mazao, unafanya vizuri, au hata una umbo zuri, kaa duniani na usifanye lolote lile uone kama kuna atakayepambana na wewe, watu watakushambulia kwa sababu una mafanikio na Mungu ameweka mkono wake kwako kwa hiyo utapigwa vita ili uwaondokee hawataki uwe una ushuhuda wa Baraka za Mungu kwako!

Daniel 6:1-4 “Ilimpendeza Dario kuweka juu ya ufalme maliwali mia na ishirini, wawe juu ya ufalme wote; na juu yao akaweka wakubwa watatu, na Danieli alikuwa mmoja wao; ili maliwali hawa watoe hesabu kwao, mfalme asipate hasara. Basi Danieli huyo alipata sifa kuliko wakubwa na maliwali, kwa kuwa roho bora ilikuwa ndani yake; naye mfalme akaazimu kumweka juu ya ufalme wote. Basi mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake.”     

Unaona wakati wote unapokuwa na kitu cha ziada wewe ndio utakuwa unatafutwa, ili ushuhuda wa Mungu kuwa amekutendea mema uweze kupotea kwa sababu wengine watasikia na kumtukuza Mungu kwa yale ambayo Mungu amekufanyia sasa adui akufurahie kwa sababu gani? Shetani akufurahie wewe kwa lipi?

Shika sana ulichonacho!

Ni jukumu lako kuhakikisha kuwa wakati wote unapambana kulinda kile ambacho Mungu amekubariki kwacho, Baraka za Mungu katika maisha yetu zinavutia maadui hivyo wakati wote lazima ujifunze kujihami na kujilinda Yesu aliliambia kanisa la Filadelfia kuwa kwa kuwa umeishika sana subira yangu nani nitakulinda, ziko kanuni ambazo kwazo zinauwezo wa kutulinda

1.       Lazima tutumaini Mungu na kumtegemea yeye Zaburi ya 91:1-9 “Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, Na katika tauni iharibuyo. Kwa manyoya yake atakufunika, Chini ya mbawa zake utapata kimbilio; Uaminifu wake ni ngao na kigao. Hutaogopa hofu ya usiku, Wala mshale urukao mchana, Wala tauni ipitayo gizani, Wala uele uharibuo adhuhuri, Ijapo watu elfu waanguka ubavuni pako. Naam, kumi elfu mkono wako wa kuume! Hata hivyo hautakukaribia wewe. Ila kwa macho yako utatazama, Na kuyaona malipo ya wasio haki.  Kwa kuwa Wewe Bwana ndiwe kimbilio langu; Umemfanya Aliye juu kuwa makao yako.”

 

2.       Uwe mwaminifu Daniel 6:16-22 “Basi mfalme akatoa amri, nao wakamleta Danieli, wakamtupa katika tundu la simba. Mfalme akanena, akamwambia Danieli, Mungu wako unayemtumikia daima, yeye atakuponya. Likaletwa jiwe, likawekwa mdomoni mwa lile tundu; naye mfalme akalitia muhuri kwa muhuri yake mwenyewe, na kwa muhuri ya wakuu wake, lisibadilike neno lo lote katika habari za Danieli. Kisha mfalme akaenda nyumbani kwake, akakesha usiku kucha, akafunga; na vinanda havikuletwa mbele yake; na usingizi wake ukampaa. Asubuhi mfalme akaondoka mapema, akaenda kwa haraka mpaka penye lile tundu la simba. Naye alipolikaribia lile tundu, akamlilia Danieli kwa sauti ya huzuni; mfalme akanena; akamwambia Danieli, Ee Danieli, mtumishi wa Mungu aliye hai, je! Mungu wako, unayemtumikia daima, aweza kukuponya na simba hawa? Ndipo Danieli akamwambia mfalme, Ee mfalme, uishi milele. Mungu wangu amemtuma malaika wake, naye ameyafumba makanwa ya simba, nao hawakunidhuru; kwa kuwa mbele zake mimi nalionekana kuwa sina hatia; tena, mbele yako, Ee mfalme, sikukosa neno.”            

 

3.       Usikubali kupeleka ibada kwa mwanadamu, maandko yako wazi kuwa amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu na kumfanya mwanadamu kuwa kinga yake, wokovu wa kweli kwetu hautoki kwa mwanadamu mtumaini Mungu na kumtegemea yeye tu naye atakusaidia

 

Daniel 3:12-27 “Wako Wayahudi kadha wa kadha uliowaweka juu ya mambo ya wilaya ya Babeli, yaani, Shadraka, na Meshaki, na Abednego; watu hawa, Ee mfalme, hawakukujali wewe; hawaitumikii miungu yako, wala kuiabudu ile sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha. Basi Nebukadreza akatoa amri kwa hasira na ghadhabu, waletwe hao Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Basi wakawaleta watu hao mbele ya mfalme. Nebukadreza akajibu, akawaambia, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, je! Ni kwa makusudi hata hammtumikii mungu wangu wala kuisujudia sanamu ya dhahabu niliyoisimamisha? Basi sasa, kama mkiwa tayari wakati mtakapoisikia sauti ya panda, na filimbi, na kinubi, na zeze, na santuri, na zomari, na namna zote za ngoma, kuanguka na kuisujudia sanamu niliyoisimamisha, ni vema; bali msipoisujudia, mtatupwa saa iyo hiyo katika tanuru iwakayo moto; naye ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu? Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakajibu, wakamwambia mfalme, Ee Nebukadreza, hamna haja kukujibu katika neno hili. Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa na tanuru ile iwakayo moto; naye atatuokoa na mkono wako, Ee mfalme. Bali kama si hivyo, ujue, Ee mfalme, ya kuwa sisi hatukubali kuitumikia miungu yako, wala kuisujudia hiyo sanamu ya dhahabu uliyoisimamisha.Ndipo Nebukadreza akajaa ghadhabu, na sura ya uso wake ikabadilika juu ya Shadraka, na Meshaki, na Abednego, basi akatoa amri watie moto ile tanuru mara saba kuliko desturi yake ya kutiwa moto. Kisha akawaamuru baadhi ya watu mashujaa wa jeshi lake kuwafunga Shadraka, na Meshaki, na Abednego, na kuwatupa katika ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. Basi watu hao wakafungwa, hali wamevaa suruali zao, na kanzu zao, na joho zao, na mavazi yao mengine, wakatupwa katikati ya ile tanuru iliyokuwa ikiwaka moto. Basi kwa sababu amri ya mfalme ilikuwa ni kali, na ile tanuru ilikuwa ina moto sana, mwako wa ule moto ukawaua wale watu waliowashika Shadraka, na Meshaki, na Abednego. Na watu hao watatu, Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakaanguka, hali wamefungwa, katikati ya ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Ndipo Nebukadreza akastaajabu, akainuka kwa haraka; akanena, akawaambia mawaziri wake, Je! Hatukutupa watu watatu, hali wamefungwa, katikati ya moto? Wakajibu, wakamwambia mfalme, Kweli, Ee mfalme. Akajibu, akasema, Tazama, mimi naona watu wanne, nao wamefunguliwa, wanatembea katikati ya moto hali hawana dhara; na sura yake yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu. Kisha Nebukadreza akaukaribia mdomo wa ile tanuru iliyokuwa inawaka moto. Akanena, akasema, Enyi Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watumishi wa Mungu Aliye juu, tokeni, mje huku. Ndipo Shadraka, na Meshaki, na Abednego, wakatoka katika ule moto. Na maamiri, na manaibu, na maliwali, na mawaziri, waliokuwa wamekusanyika pamoja, wakawaona watu hao, ya kuwa ule moto ulikuwa hauna nguvu juu ya miili yao, wala nywele za vichwa vyao hazikuteketea, wala suruali zao hazikubadilika, wala harufu ya moto haikuwapata hata kidogo. Nebukadreza akanena, akasema, Na ahimidiwe Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego; aliyemtuma malaika wake, akawaokoa watumishi wake waliomtumaini, wakaligeuza neno la mfalme, na kujitoa miili yao ili wasimtumikie mungu mwingine, wala kumwabudu, ila Mungu wao wenyewe. Basi mimi naweka amri ya kuwa kila kabila ya watu, na kila taifa, na kila lugha, watakaonena neno lo lote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, na Meshaki, na Abednego, watakatwa vipande vipande, na nyumba zao zitafanywa jaa; kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”



Hakikisha kuwa unafanya sehemu yako, unapambana, na Mungu atakusaidia, tambua ya kuwa una kitu cha ziada, na usisubiri mwanadamu akutetee, mtegemee Mungu mwangalie yeye, kumbuka ya kuwa una kitu cha ziada, usikubali kwa namna yoyote ile kupoteza ulichonacho kwa njia rahisi, Pambana kwa kumtegemea Mungu yeye aliyekuweka! Mshike Yesu tu yeye ndio msaada wetu mkubwa na anayeweza kutusaidia usiwategemee wanadamu.

Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye hekima!