Jumanne, 8 Novemba 2022

Kufa afavyo Mpumbavu!


2Samuel 3:33-34Ndipo mfalme akamwomboleza Abneri, akasema, Ilimpasaje Abneri kufa afavyo mpumbavu? Mikono yako haikufungwa, Wala miguu yako haikutiwa pingu; Aangukavyo mtu mbele ya wana wa uovu, ndivyo ulivyoanguka. Na watu wote wakaongeza kumlilia.” 



Utangulizi:

Abner alikuwa ni binamu na mkuu wa majeshi ya ulinzi wa Jeshi la Mfalme Sauli, Jina lake limejitokeza katika maandiko vilevile kama Abner mwana wa Ner jina lake maana yake baba yangu ni Ner  na neno Ner maana yake ni Mwanga au Nuru!, Mkuu huyu wa majeshi alitumika na Sauli na Jonathan na hata baada ya kifo chake alikuwa mwaminifu kwa Mtoto wa Sauli aliyeitwa Ishboshethi hivyo tunapata picha ya kuwa wakati wote wa vita vya Sauli na Daudi Abner ndiye aliyekuwa akiongoza mapambano hayo lakini kwa neema ya Mungu siku hadi siku Nyumba ya Sauli ilizidi kudhoofika dhidi ya Nyumba ya Daudi kama yanenavyo maandiko.

2Wafalme 3:1 “Basi kulikuwa na vita siku nyingi kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi; Daudi akaendelea akasitawi, lakini nyumba ya Sauli ikaendelea kudhoofika.”

Hata hivyo kutokana na kutambua mapenzi ya Mungu, Abner alitambua wazi kuwa Mungu alikuwa amekusudia Daudi awe mfalme tangu miaka mingi alipopakwa mafuta na Samuel Nabii, lakini kibishibishi upande wa Sauli walikuwa wanachelewesha au kushindana na makusudi ya Mungu, hatimaye Abner aliamua kuwa atasaidia kumkabidhi Daudi ufalme baada ya kugombea mwanamke kati yake na Ishboshethi mwana wa Sauli.

2Wafalme 3:6-9 “Ikawa, wakati vilipokuwapo vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi, Abneri akajipatia nguvu nyumbani kwa Sauli. Basi Sauli alikuwa na suria, jina lake akiitwa Rispa, binti Aya; Ishboshethi akamwuliza Abneri, Kwa nini umeingia kwa suria ya babangu? Basi Abneri akakasirika kwa maneno ya Ishboshethi, akasema, Je! Mimi ni kichwa cha mbwa, aliye wa Yuda? Hata leo hivi nawafanyia fadhili nyumba ya Sauli babako, na ndugu zake, na rafiki zake, nisikutie wewe mkononi mwa Daudi; nawe hata hivyo wanitia hatiani leo kwa mwanamke huyu. Mungu amfanyie Abneri vivyo, na kuzidi, nisipomtendea Daudi kama vile Bwana alivyomwapia;”

Kwa hiyo unaweza kupata picha kuwa kwa kiwango fulani kikubwa Abner alikuwa ni kikwazo kikubwa kwa mapenzi ya Mungu kwa Daudi kutimia akitetea upande wa Sauli na watoto wake na pia kumbe alijua mapenzi ya Mungu kuwa Mungu alimuapia Daudi Ufalme lakini kwa makusudi alikuwa akipingana na mapenzi ya Mungu na kuchelewesha kusudi la Mungu juu ya Daudi ashukuriwe Mungu kuwa makusudi yake hayawezi kuzuilika, Mungu aliutumia ugomvi wao na Ishbotheth kutimiza Mpango wake na Abner sasa alikuwa katika njia ya Mungu akijua wazi kuwa anatimiza mapenzi ya Mungu.

Abner na mapenzi ya Mungu.

Abner alifahamu kuwa kama amekosana na Ishbotheth mwana wa Sauli na kujipa nguvu yeye mwenyewe kwa vyovyote vile atakayepambana na Daudi angekuwa yeye, uso kwa uso, kwa ujumla Jemedari huyu alikuwa na tatizo la kiburi moyoni mwake maandiko yanaposema alijipatia nguvu katika nyumba ya Sauli maana yake alijiinua yeye mwenyewe

2Wafalme 3:6-7 “Ikawa, wakati vilipokuwapo vita kati ya nyumba ya Sauli na nyumba ya Daudi, Abneri akajipatia nguvu nyumbani kwa Sauli. Basi Sauli alikuwa na suria, jina lake akiitwa Rispa, binti Aya; Ishboshethi akamwuliza Abneri, Kwa nini umeingia kwa suria ya babangu?

Unaona akajipatia nguvu nyumbani mwa Sauli hii maana yake kibiblia alianza kujiinua alianza kuwa na kiburi, kuchukua mke au suria katika mila za kifalme kulikuwa hakuna tofauti na kujifanya mfalme au kutaka ufalme ona, 1Wafalme 2:13-23 “Ndipo Adonia mwana wa Hagithi akaja kwa Bath-sheba mamaye Sulemani. Naye akasema, Je! Umekuja kwa amani? Naye akajibu, Kwa amani. Tena akasema, Nina shauri ninalotaka kukuambia. Naye akamwambia, Sema. Basi akasema, Wajua ya kwamba ufalme ulikuwa wangu, na Israeli wote wakaniwekea nyuso zao ili nimiliki mimi; walakini sasa ufalme umegeuka kuwa wake ndugu yangu; kwa maana ulikuwa wake kutoka kwa Bwana. Basi sasa nina haja moja ninayokuomba, usinikataze hiyo. Naye akamwambia, Sema. Akasema, Nena, nakusihi, na Sulemani, mfalme, (kwa kuwa hawezi kukukataza neno), kwamba anioze Abishagi, Mshunami. Naye Bath-sheba akasema, Vema; nitasema na mfalme kwa ajili yako. Basi Bath-sheba akaingia kwa mfalme Sulemani, aseme naye kwa ajili ya Adonia. Naye mfalme akainuka kwenda kumlaki, akamwinamia, akaketi katika kiti chake cha enzi; kisha akaagiza awekewe kiti cha enzi mamaye mfalme; naye akaketi mkono wake wa kuume. Ndipo akasema, Haja moja ndogo nakuomba; usinikataze. Mfalme akamwambia, Omba, mama; kwa kuwa siwezi kukukataza neno. Naye akasema, Nataka Adonia, ndugu yako, aozwe Abishagi, Mshunami. Akajibu mfalme Sulemani akamwambia mamaye, Na mbona wamtakia Adonia Abishagi, Mshunami? Umtakie na ufalme pia; kwa kuwa yeye ni ndugu yangu mkubwa; naam, umtakie yeye, na Abiathari kuhani, na Yoabu mwana wa Seruya. Ndipo mfalme Sulemani akaapa kwa Bwana, akasema, Mungu anifanyie hivyo, na kuzidi, isipokuwa Adonia amenena neno hili juu ya uhai wake mwenyewe.” hivyo ili Daudi atawale ilikuwa lazima Abner ashughulikiwe, naye akijua yatakayompata baada ya kuasi nyumba ya Sauli sasa anakuja na mpango wa kukabidhi mamlaka ya kifalme kwa Daudi, lilikuwa wazo jema na mapenzi ya Mungu, lakini ni yeye ndiye aliyekuwa anachelewesha kusudi la Mungu, sasa anataka kurudisha mamlaka kwa Daudi.

2Wafalme 3:9-10 “Mungu amfanyie Abneri vivyo, na kuzidi, nisipomtendea Daudi kama vile Bwana alivyomwapia; kuupitisha ufalme toka nyumba ya Sauli, na kukisimamisha kiti cha Daudi juu ya Israeli, na juu ya Yuda, toka Dani mpaka Beer-sheba.”

Abner alikuwa mtu mwenye kujiamini kupita kawaida yeye alijifanya kuwa ni Mungu, pamoja na kuwa aliapa kwa Mungu lakini anapotumia neno KUUPITISHA UFALME TOKA NYUMBA YA SAULI NA KUKISIMAMISHA KITI CHA DAUDI JUU YA ISRAEL NA JUU YA YUDA hii ilikuwa ni kazi ambayo haifanyiki kibinadamu neno kupitisha Katika kiingereza linasomeka kama “To translate” ambalo katika kiebrania maana yake ni Abar likisomeka kama AW-BAR ambalo maana yake ni ni sawa na kutenga au kusababisha au kuweka wakfu au kuhamisha kimsingi hayo yanaweza kufanywa na Mungu tu ona Wakolosai 1:13 “Naye alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wa pendo lake;”  unaweza kuona Lugha hiyo pia katika Waebrania 11:5 “Kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha; maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu.” Kwa hiyo kumamisha au kupitisha ni kumtoa mtu katika hali moja na kumpeleka katika hali nyingine hii ni kazi ya Mungu na sio ya Mwanadamu. Ni wazi kuwa kamanda huyu alikuwa na kiburi.

Abner vilevile alikuwa ni mtu hatia ya damu ya shujaa anayeitwa Asahel, Huyu alikuwa moja ya watu mashujaa aliyekuwa na mbio za kufukuzia maadui kama mbio za kulungu, katika mashujaa watatu waliotoka kwa Seruya waliojulikana kama wana wa Seruya Asahel alikuwa ni hodari lakini zaidi sana aliyekuwa na uwezo wa kukimbiza adui, Asahel alikuwa akimkimbiza Abner na kwaajili ya kujihami Abneri alimshihi sana aache kumfuatilia lakini Asahel alikaza na kwa sababu hiyo yeye alimuua ona

2Samuel 18-28 Na wana watatu wa Seruya walikuwako huko, Yoabu, na Abishai, na Asaheli; na Asaheli alikuwa mwepesi wa miguu kama kulungu. Naye Asaheli akamfuatia Abneri; na katika kwenda kwake hakugeuka kwenda mkono wa kuume wala mkono wa kushoto katika kumfuatia Abneri. Basi Abneri akatazama nyuma yake, akasema, Ni wewe, Asaheli? Akajibu, Ni mimi. Basi Abneri akamwambia, Geuka mkono wa kuume au mkono wa kushoto, ukamshike mmoja wa vijana, ukazitwae silaha zake. Lakini Asaheli hakukubali kugeuka na kuacha kumfuata. Abneri akamwambia Asaheli mara ya pili, Geuka, acha kunifuatia mimi; kwa nini nikupige hata chini? Hapo ningewezaje kuinua uso wangu mbele ya Yoabu, ndugu yako? Lakini akakataa kugeuka; kwa hiyo Abneri akampiga tumboni kwa ncha ya nyuma ya mkuki wake, ule mkuki ukamtoka kwa nyuma; naye akaanguka hapo, akafa papo hapo; ikawa, watu wote waliofika hapo, alipoanguka Asaheli na kufa, wakasimama. Ila Yoabu na Abishai wakamfuatia Abneri; na jua likachwa hapo walipoufikilia mlima wa Ama, uelekeao Gia, katika njia ya nyika ya Gibeoni. Nao wana wa Benyamini wakakusanyika pamoja nyuma ya Abneri, wakawa kikosi kimoja, wakasimama juu ya mlima. Ndipo huyo Abneri akamwita Yoabu, akasema, Je! Upanga uwale watu sikuzote? Je! Hujui ya kwamba utakuwa uchungu mwisho wake? Basi itakuwa hata lini usijewaamuru watu warudi na kuacha kuwafuatia ndugu zao? Naye Yoabu akasema, Aishivyo Mungu, usingalinena, basi asubuhi wangalikwenda zao, wasiwafuatie kila mtu ndugu yake. Basi Yoabu akapiga tarumbeta, na watu wote wakasimama, wasiwafuatie Israeli tena, wala hawakupigana tena.” Mtu aliyeua mtu mwingine alipaswa kusalimisha maisha yake katika mojawapo ya miji sita ya makimbilio ili mwenye kujilipiza kisasi kwaajili ya nduguye aije akamuua, Hata hivyo Abneri hakuweza kujali maelekezo hayo ya torati kwa vile alikuwa akijiamini kutokana na umahiri wake katika vita

Agano la Abner na Daudi.

Pamoja na madhaifu makubwa aliyokuwa nayo Abner, huyu pia alikuwa ni jemadari wa vita, alikuwa ni mzoefu wa vita shujaa na kamanda mwenye nguvu sana lakini pia alikuwa mpenda amani na mwangalifu mno, katika uwezo wa kujihami,  ulifika wakati akaona pia kuwa sasa Israel wanahitaji amani.

2Samuel 3:12-16 “Basi Abneri akatuma wajumbe kwa Daudi mahali alipokuwapo, akisema, Nchi hii ni ya nani? Fanya agano nami, na tazama, mkono wangu utakuwa pamoja nawe, ili kuwaleta Israeli wote kwako. Daudi akasema, Vema, nitafanya agano nawe, lakini nina sharti moja nitakalo kwako, nalo ni hili; Hutaniona uso wangu, isipokuwa uniletee Mikali, binti Sauli, hapo ujapo kuniona uso wangu. Basi Daudi akatuma wajumbe kwa Ishboshethi, mwana wa Sauli, kusema, Nipe mke wangu Mikali, niliyemposa kwa govi mia za Wafilisti. Basi Ishboshethi akatuma watu, akamnyang'anya Paltieli, mwana wa Laishi, mumewe, mwanamke huyo. Huyo mumewe akafuatana naye, akiendelea na kulia, akamfuata mpaka Bahurimu. Ndipo Abneri akamwambia, Haya, rudi. Naye akarudi.”

Kwa kuwa ilikuwa ni desturi ya Israel mtu anapofanya agano lazima wawekeana masharti Daudi aliitumia nafasi hiyo kumdai Abner ili aweze kumona uso wake amletee mke wa ujana wake aliyemuoa kwa gharama ya givi za wafilisti 100 lakini yeye aliua 200 ambaye alikuwa ni mikali Binti wa Sauli jambo ambalo Abner alilitii,  hii ilikuwa picha halisi ya kuwa Abner kweli alikuwa anataka amani Jambo hili lilimpendeza Daudi, hata hivyo Daudi hakuwa anahitaji sana Nguvu ya Abner kwani vijana wa Daudi walikuwa wameshaonyesha uwezo mkubwa sana kivita kumzidi yeye ona

2Samuel2:14-17 “Abneri akamwambia Yoabu, Tafadhali vijana hawa na waondoke na kucheza mbele yetu. Yoabu akasema, Haya! Na waondoke. Basi wakaondoka, wakaenda upande wa pili kwa hesabu yao watu kumi na wawili wa Benyamini, na wa Ishboshethi, mwana wa Sauli na watu kumi na wawili wa watumishi wa Daudi. Wakakamatana, kila mtu akimshika mwenziwe kichwa chake, na kutia upanga wake katika ubavu wa mwenzake; wakaanguka pamoja; hata mahali pale pakaitwa Helkath-hasurimu, napo ni katika Gibeoni. Vita vile vilikuwa vikali sana siku ile; naye Abneri akashindwa, na watu wa Israeli, mbele ya watumishi wa Daudi.”

Hata hivyo swala la kuwa na amani ya pamoja lilikuwa ni wazo zuri na mapenzi ya Mungu hivyo Daudi alilikubali na alimkubali Abneri kama mtu mwenye akili na mwema na aliyekubali kushindwa na kukubali mpango wa Mungu.    

Kufa afavyo Mpumbavu!

Abneri alikuja Hebron ili aweze kuonana na Daudi na kufanya patano naye 2 Samuel 3:20-23 “Basi Abneri akamwendea Daudi huko Hebroni, na watu ishirini pamoja naye. Daudi akamfanyia karamu Abneri, na watu wote waliokuwa pamoja naye. Kisha Abneri akamwambia Daudi, Nitaondoka, niende zangu; nami nitamkusanyia bwana wangu mfalme Israeli wote, ili wafanye agano nawe, ukamiliki juu ya wote inaowatamani roho yako. Basi Daudi akamruhusu Abneri; naye akaenda zake kwa amani. Na tazama, watumishi wa Daudi pamoja na Yoabu walitoka jeshini, wakaleta mateka mengi pamoja nao; lakini Abneri hakuwako Hebroni kwa Daudi; maana alikuwa amemruhusu, naye amekwisha kwenda zake kwa amani. Hata Yoabu, na jeshi lote waliokuwa pamoja naye, walipofika, watu wakamwambia Yoabu, wakisema, Abneri, mwana wa Neri, alikuja kwa mfalme, naye amemruhusu, naye amekwenda zake kwa amani.”

Daudi aliamini kuwa yalikuwa ni mapatano ya kweli na kuwa Abneri sasa anakwenda kuwakusanya watu kwaajili ya Daudi ili wafanye patano naye na kumfanya mfalme kwa njia ya amani, Hata hivyo Kamanda mkuu wa majeshi ya Daudi alikuwa hayuko wakati hilo likifanyika na kwa medani za kivita Yoabu hakuamini kuwa Abneri alikuwa na nia ya dhati ya kufanya hivyo yeye alikumbuka kuwa huyu ndiye alikuwa mpinzani mkubwa wa kuzuia kusudi la Mungu na iweje leo aweze kuwa mwema aidha Yoabu alikuwa na ufahamu kuwa Abneri pia alikuwa na kisasi cha damu ya kumuua Asaheli Ndugu yake, Yoabu alisikitika kuwa ni kwanini Abneri amekuja na Daudi anamuachia aende zake kwa amani inawezekanaje mtu mwenye nia ovu kesho akawa na nia njema? Hivyo Yoabu aliagiza kuwa Abneri arudi akidhani ya kuwa ameitwa tena na Daudi kumbe Yoabu alitaka kujilipizia kisasi kwaajili ya Ndugu yake ona

2Samuel 3:24-27 “Basi Yoabu akamwendea mfalme, akasema, Umefanyaje? Tazama, Abneri amekuja kwako; mbona umemruhusu, naye amekwisha kwenda zake?  Wewe wamjua Abneri, mwana wa Neri, ya kuwa alikuja ili kukudanganya, apate kujua kutoka kwako, na kuingia kwako, akajue yote uyatendayo. Naye Yoabu alipotoka kwa Daudi, akapeleka wajumbe kumfuata Abneri, wakamrudisha kutoka kisima cha Sira; lakini Daudi alikuwa hana habari. Basi Abneri alipokuwa amerudi Hebroni, Yoabu akamchukua kando hata katikati ya lango, ili aseme naye kwa faragha; akampiga mkuki wa tumbo huko, hata akafa; kwa ajili ya damu ya Asaheli, ndugu yake.”

Tukio hili lilimsikitisha sana Daudi, kwani lingeweza kuhesabika ya kuwa amechukua ufalme kwa upanga, hata hivyo Daudi alifahamu kuwa Abneri hakuwa na nia ya uovu, hivyo alilaani vikali tukio la Yoabu. Na kumlaani Yoabu pamona na nyumba yake kwa kumuua mtu ambaye alikuwa anataka amani, Daudi aliitisha mbiu ya maombolezo lilikuwa ni tukio la kusikitisha sana Hata hivyo katika maombolezo hayo Daudi hakumlaumu yeyote bali alimlaumu Abneri mwenyewe kwa kufa kipumbavu ona

2Samuel 3:28-34 “Hata baadaye Daudi aliposikia, akasema, Mimi na ufalme wangu hatuna hatia milele mbele za Bwana, kwa sababu ya damu ya Abneri, mwana wa Neri; na imwangukie Yoabu kichwani pake, na nyumba yote ya babaye, tena hiyo nyumba ya Yoabu isikose kuwa na mtu mwenye kutoka damu, au aliye na ukoma, au mwenye kutegemea fimbo, au mwenye kuanguka kwa upanga au mwenye kuhitaji chakula. Basi Yoabu, na Abishai nduguye, walimwua Abneri, kwa sababu yeye alimwua ndugu yao Asaheli katika vita huko Gibeoni. Kisha Daudi alimwambia Yoabu, na watu wote waliokuwa pamoja naye, Rarueni nguo zenu, mkajivike nguo za magunia, mkamlilie Abneri. Naye mfalme Daudi akaifuata jeneza. Wakamzika Abneri katika Hebroni; naye mfalme akapaza sauti yake, akalia kaburini kwa Abneri, nao watu wote wakalia. Ndipo mfalme akamwomboleza Abneri, akasema, Ilimpasaje Abneri kufa afavyo mpumbavu? Mikono yako haikufungwa, Wala miguu yako haikutiwa pingu; Aangukavyo mtu mbele ya wana wa uovu, ndivyo ulivyoanguka. Na watu wote wakaongeza kumlilia.”

Kwa nini Daudi amsikitikie Abneri kuwa amekufa kipumbavu?  Hii ni kwa sababu Abneri aliuawa pembeni kidogo tu ya lango la mji wa Hebroni, Mji wa  Hebroni ulikuwa ni mji wa makimbilio, miji ya makimbilio ilikuwa ni miji maalumu iliyotengwa kwaajili ya kutunza uhai wa mtu aliyeua kwa bahati mbaya, Abneri alikuwa amemuua Asaheli hivyo ilikuwa rahisi kwa mtu mwenye kutaka kisasi cha damu ya ndugu yake kumuua na mahali sahihi na salama ni kwenye moja ya miji ya makimbilio na Hebron ulikuwa ni mojawapo ya miji hiyo, hii ni miji ambayo muuaji angekimbilia humo angekula angevaa na kuishi salama miji hii iliwekwa na Mungu kwa sababu hiyo!

Hesabu 35:9-16 “Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia, Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Mtakapovuka mto wa Yordani na kuingia nchi ya Kanaani, Ndipo mtajiwekea miji iwe miji ya makimbilio kwa ajili yenu; ili kwamba mwenye kumwua mtu, pasipo kukusudia kumwua, apate kukimbilia huko. Na hiyo miji itakuwa kwenu kuwa makimbilio, kumkimbia mwenye kutwaa kisasi, ili asiuawe mwenye kumwua mtu, hata atakaposimama mbele ya mkutano ahukumiwe. Na hiyo miji mtakayowapa itakuwa kwenu ni miji sita ya makimbilio. Mtawapa miji mitatu ng'ambo ya pili ya Yordani, na miji mitatu mtawapa katika nchi ya Kanaani; miji hiyo itakuwa ni miji ya makimbilio. Miji hiyo sita itakuwa miji ya makimbilio kwa ajili ya wana wa Israeli, na kwa ajili ya mgeni, na kwa ajili ya huyo aketiye kati yao hali ya ugeni; ili kila amwuaye mtu, naye hakukusudia kumwua, apate kukimbilia huko. Lakini kama alimpiga kwa chombo cha chuma, akafa, ni mwuaji huyo; mwuaji hakika yake atauawa.”

·         Ni miji iliyowekwa na Mungu kwaajili ya usalama wa kila mtu.

·         Ni miji iliyowekwa na Mungu kwaajili ya kupate neema ya kutokuuawa

·         Ni miji iliyowekwa na Mungu ikiwa na mamlaka ya kuokoa

·         Ni miji iliyowekwa na Mungu kwa makusudi ya kutunza uhai

·         Ni miji Iliyokuwa maarufu na iliyojulikana sana na kila mtu aliijua

·         Ni miji iliyowekwa na Mungu kutoa mahitaji ya kutosha kwa kila anayekimbilia

·         Ni miji iliyokuwa imeandaliwa kwa maelekezo ya Mungu

·         Ni miji ambayo njia zake hazikufungwa

·         Miji hii ilikuwa sita tu katika nchi nzima ya Israel

 

1.       Kadesh – maana yake Haki

2.       Shekemu – mabega maana yake nguvu za Mungu

3.       Hebron -  maana yake Ushirika

4.       Bezeri – maana yake Ngome

5.       Ramoth – maana yake juu

6.       Na Golan – Maana yake Furaha

Kwa hiyo ilihitajika hatua moja tu kujikinga ndani ya mji wa Hebron, kwa mtu aliyekuwa shujaa, aliyepigana vita vingi sana, jemadari, anakujaje kufa wakati wa amani tena hatua chache tu kutoka lango la mji unaoweza kuokoa, tena akiwa na silaha zake, tena akiwa hajatiwa pingu, tena akiwa hajafungwa miguu wala mikono, tena akiwa hajachukua tahadhari ya aina yoyote,  Komandoo anawezaje kufa kirahisi namna ile, kimsingi yako mambo ambayo yako katika uwezo wetu ambayo tulitakiwa kuchukua hatua moja tu na hiyo ingetuweka mahali salama, Mungu ametupa Mwokozi, ametupa Yesu Kristo aliye haki yetu, aliye na nguvu za kiungu za kutusaidia ambaye anahitaji ushirika na kila mtu, ambaye ni ngome imara, ambaye yuko mkono wa kuume wa Mungu mbinguni ambaye ni furaha yetu, yuko tayari kutoa neema kwa kila mtu, yuko tayari kuokoa, yuko tayari kutuhifadhi na kutunza uhai wetu, anatoa kila kitu ni msaada ulio karibu, yuko tayari kumsaidia kila mtu hata bila kujali umefanya dhambi kiasi gani yuko tayari kusamehe na kukuhifadhi ni kifo cha kujitakia kufa bila kumpokea Yesu, ni aibu kukaa karibu na injili na kushindwa kuchukua hatua moja tu itakayostawisha usalama wako milele, ndani ya mji yuko mfalme ambaye anataka amani na wewe anakuamini hata kama watu hawakuamini, iweje leo ushindwe kuchukua hatua, ndugu yangu ni aibu ni kufa kipumbavu kama tutashindwa kumtumia Yesu aliyetupa kila kitu katika maisha yetu, ni hatua moja tu ya maombi, ni hatua moja tu ya kufunga, ni hatua moja tu ya kukumbuka kuwa liko lango la Hebron ni kuingia tu hakuna wa kukuzuia hupaswi kufa kipumbavu!  Na huwezi kuwa salama nje ya mji wa makimbilio! Kamanda mwenye akili na mwenye kujua mapenzi ya Mungu na mtu ambaye aklikuwa na nguvu na mzoezu wa vita ilikuwaje akafa kipumbavu, leo hii yako magonjwa mengine kama yakituua ni kwa sababu tumejitakia, maandiko yanasema kila atakayeliitia jina la Bwana ataokoka, tena yanasema nimekukimbilia wewe bwana nisiabike milele, mtu mweye akili na hekima kama wewe huwezi kuangamia ilihali unajua ya kuwa Yesu ni kimbilio na msaada wetu, heri leo kama utayatoa maisha yako kwake na kukubali msaada mkubwa utokao kwake !

Na Rev. Innocent Samuel Kamote

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: