Jumatano, 29 Oktoba 2014

Huduma Ya Kichungaji


UTANGULIZI

      Katika sehemu nyingi za ulimwengu leo, kanisa la Mungu linakua kwa kasi, Matokeo yake kumekuwa na kundi kubwa la wakristo wanaohitaji huduma ya kichungaji na uongozi wa kiroho. Maandiko yanawaita watu hao kondoo ambao wanahitaji mchungaji wa kuwaongoza, kuwatunza, kuwahudumia, kuwalisha, na kusimamia usalama wao. Kristo alitumia mfano huu wa kondoo na mchungaji kuonyesha ni huduma gani watu wanaihitaji, Kwa bahati mbaya Pamoja na kuwa na wachungaji wengi na maaskofu wengi na waangalizi bado kondoo wengi hawajaweza kufikiwa kwa huduma ya kichungaji huduma hii inahitajika sana.

     Wewe mwenyewe umekuwa ni shahidi jinsi ambavyo umekutana na Kondoo wengi nje ya kanisa lako au waliokimbilia katika kanisa lako wakitokea sehemu nyingine na huenda labda kwa mchungaji au askofu maarufu sana au kanisa maarufu sana na ukashangaa kuona kuwa alishindwa kupata huduma ya kichungaji, Hili likufumbue macho kuwa kama ulihudumia wa mwengine huenda na kondoo ambao Bwana amekuita kuwachunga wamewahi kutafuta huduma ya kichungaji kwa mtu mwingine wengine wakisikia hivyo wanaumia unaumia nini ? Jambo unalotakiwa kulifanya ni kudumisha na kuboresha huduma ya kichungaji Sikia huduma hii ni zaidi ya Kuhubiri kwa mbwembwe kupandisha sauti na kushusha au kufanya miujiza! Watu wanahitaji kufikiwa kwa karibu zaidi kamuulize Musa miujiza haikusaidia kupunguza manung’uniko waliyokuwa nayo watu na wala pamoja na upako aliokuwa nao hakuweza kuwafikia watu woote kihuduma hata hatimaye aliiona kazi hii kuwa ngumu “Musa akamwambia Bwana, Mbona umenitenda uovu mimi mtumishi wako?kwa nini sikupata neema machoni pako, hata ukanitwika mzigo wa watu hawa woote juu yangi?.... .MIMI SIWEZI KUWACHUKUA WATU HAWA WOTE PEKE YANGU, KWA KUWA NI MZIGO MZITO SANA WA KUNISHINDA… kama ukinitenda hivi nakuomba uniulie mbali..” unaona! Usifikiri basi kazi hii ya kichungaji na huduma hii ya kichungaji ni rahisi tu wengi imewashinda wengi wetu leo tungekuwa wahubiri wazuri na wakubwa sana lakini tuko hapa tuliko pia kama matokeo ya kushindwa kulelewa au kulelewa vizuri katika huduma nzuri za kichungaji yaani tumekosa malezi ya kichungaji. (Hesabu 11;11-12,14-15)

      Lengo na kusudi la somo hili si kuangalia wapi tumetoka na kutafuta kulaumu wengine hapana ni kujifunza kutokana na makosa na kuamua kutilia maanani kusudi kuu la somo hili ili kwamba tuweze kufanya vizuri zaidi ya kizazi kilichopita au kitakachopita katika huduma hii ya kichungaji kwa msingi huu basi tunapopitia somo hili na tuache kiburi tujinyenyenyekeze na kukubali kufundishika bila kujali kuwa tumechunga kwa miaka mingapi na taratibu moyoni omba sala hii 

Bwana yesu wewe ndiye mchungaji mwema mimi si mwema kukushinda wewe nisaidie najua kuwa umeniita katika huduma hii ya kichungaji lakini mimi siwezi kuchunga nataka wewe unifungue akili zangu na moyo wangu nipokee maelekezo nawe unipe zaidi ya maelekezo ili niwe faida katika mwili wako na kukuzalia matunda yaliyo bora nisamehe kwa woote niliowapoteza kwa kutokuwa na huduma bora ya kichungaji nisaidie tangu sasa kujifunza kutoka kwako asante Bwana Yesu kwa kuwa tangu sasa utanifanya kuwa mchungaji mwema kama ulivyo wewe amen”


     Naam baada ya sala hiyo moyoni naamini wote tutakuwa tayari kujifunza somo hili huduma za kichungaji kwa moyo wa unyenyekevu fuatana basi na muandaaji wa somo hili Mchungaji Innocent Mkombozi Kamote ambaye Mungu amemuandaa kutupa dira ya huduma ya kichungaji katika kozi hii Mungu na akubariki unapofuatana nami Amen.



MCHUNGAJI NA MAANDALIZI



 Huduma ya kichungaji ni huduma ya pekee na ya tofauti  Biblia inasema Naye ametoa wengine Waefeso 4;11 kwa msingi huu kazi ya kuwajenga watu wa Mungu wakue hata wafikie kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo ni kazi ambayo Mungu amewapa watu maalumu aliowaita kwa kusudi hilo kwa hivyo kazi hii inahitaji wito, Bila wito maalum mtu hawezi kuifanya kazi hii, haijalishi kuwa mtu amesoma jinsi gani au amepata mafunzo kiasi gani bila ya wito  mtu hawezi kukamilisha kazi hii ya huduma, Mungu anapomuita mtu humpa mtu huyo neema maalum ya kuweza kuikamilisha kazi hiyo.

      Kwa msingi huo kila mtu anapofikiri kuhusu Huduma ya kichungaji anapaswa kufahamu kuwa bila ya wito ni vigumu kutimiza kile ambacho Mungu anataka kifanyike kwa kondoo zake wito ni neema maalumu inayomwezesha mtu aliyeokoka kutimiza kwa kuwezeshwa na Roho Mtakatifu wajibu katika eneo ambalo Mungu anakusudia alitimize. Ni maombi yangu kuwa utatambua kwa upya kile ambacho Mungu amekujalia kwa kukuheshimu na kukupa wito huo maalum wa kuhudumia kondoo zake na hivyo utaomba na kuendeleza kile ambacho Mungu amekikusudia kwako kwa jina lake.



A: UFAHAMU KUHUSU WITO.


   Neno wito maana yake ni kumuita mtu au kumuhitaji kwa ajili ya shughuli Fulani maalumu, ofisini au kumuajiri au kumuamuru aje, au mkutane, au mkusanyike au kumpigia mtu mbiu kwa shughuli maalum nk. Hizi ni maana chache tu za neno wito zinaweza kuwako nyingi zaidi ya hizo Katika Biblia neno wito  lilitumika kama kuita kwa sauti Mwanzo 3;9,Yohana 10;3, au kuita kwa amri Daniel 4;14 na Matendo 4;18.Yesu alitumia neno wito kama mwaliko Mathayo 9;13 kuita pia kulikuwa na maana ya kumpa mtu jina 1Samuel 1;2,Mathayo 1;21,Na pia neno wito lilitumika kwa mtu aliyechaguliwa na Mungu kwa ajili ya huduma maalumu Waebrania 5;4.Neno wito pia lilihusisha maana ya kujitoa, kutumika bila kuwa na matumaini ya kupata faida, kujitoa katika kuhudumia wengine hii pia ni maana ya wito ijulikanayo sana kwa nchi ya Tanzania.



 AINA KUU TATU ZA WITO.


   Kibiblia wito umegawanyika katika maeneo makuu matatu hata ingawaje waalimu wengine hufundisha kuwa kuna aina kuu mbili za wito. Aina hizi za wito hutegemeana kwa kuwa huwezi kuwa na aina ile ya tatu ya wito bila kupitia hizi mbili za kwanza na huwezi kuwa na ule wa kwanza bila kutimiza huu wa pili kwa hivyo aina hizi za wito hutegemeana sana.



AINA YA KWANZA YA WITO NI WITO WA JUMLA KATIKA WOKOVU.


    Wito katika wokovu ni wa kwanza ni wito unaokuja na tangazo la kumtaka mtu aokoke, au akubali mpango wa wokovu, ni wito unaoambatana na kumtaka mtu atubu dhambi zake kwa kumaanisha kuziacha na kumwamini Yesu Kristo kama Bwana na mwokozi wito huu hutolewa kwa watu woote wala haubagui mtu maandiko yanasema ili kila aaminiye awe na uzima wa milele Yohana 3;16 wito huu unacho hitaji ni mwitikio wa mtu, haubagui mtu lakini watu hujibaguwa wenyewe kwa kuifanya mioyo yao kuwa migumu kupokea wokovu.



AINA YA PILI YA WITO NI WITO WA JUMLA KATIKA UTUMISHI.


    Aina hii ya wito ni wito unaokuja moja kwa moja baada ya kukubali wito wa kwanza kila mkristo aliyeokoka ameitwa kumtumikia Mungu, Mungu alipowaokoa wana wa Israel kutoka Misri alibainisha wazi kusudi la kuwaokoa kwake kuwa ni ili wapate kumtumikia Mungu angalia Kutoka 8; 1, 20, 9; 1, 13, 10; 7, 12; 31 Mungu anapokuwa ametuita kutoka dhambini makusudi yake makubwa ni ili tumtumikie hivyo basi kila mkristo ana wajibu wa kumtumikia Mungu

  • Woote tumeitwa kuwa mashahidi wake Matendo 1;8
  • Woote tunajumuishwa katika Agizo kuu linalobeba kuwaambia watu habari njema na kufundisha (Mathayo 28;19,Marko 16;15-16,Luka 24;47)
  • Nyakati za kanisa la kwanza wakristo woote waliifanya kazi ya Mungu na ishara zilifuatana nao Marko 16; 17.
  • Roho Mtakatifu alitolewa kwa waamini wote ili wote wawe na Nguvu za kushuhudia Matendo 1;8
  • Wengi walianzisha makanisa kokote walikotawanyika Matendo 8;1,4,11;19-22 hili lina maanisha kila mkristo yu aweza kufanya huduma au ameitwa kufanya huduma hizi
  • Mungu anataka kila mtu amtumikie na hivyo ametoa karama mbalimbali 1Koritho 12;7,11, na Biblia inaonyesha ya kuwa kila mtu amepewa karama Fulani ya neema 1Petro 4;10
  • Kristo anahitaji kila mkristo kujituma kulingana na neema aliyopewa ni kama mtu anapojenga Nyumba atahitaji mafundi waashi, Seremala, bomba wa Umeme Rangi n.k mtu mmoja tu hawezi kufanya kazi hizi zote Peke yake Kanisa linahitaji waalimu wa shule za jumapili, waalimu wa watoto, viongozi, mashemasi,wanaoshughulika na vijana n.k na ndio maana Mungu ametoa karama za kutenda kazi au masaidiano Warumi 12:1-8



AINA YA TATU YA WITO NI WITO MAALUMU KATIKA UTUMISHI.


    Aina hii ya wito inakuja miongoni mwa wakristo walioitwa katika wito wa wokovu na waliokuwemo katika wito wa utumishi lakini sasa wanatengwa maalumu wawe Karama kwa Mwili wa Kristo yaani kanisa kuuwezesha kukua kumwelekea Kristo (Waefeso 4;7-16) watu walioitwa katika wito maalum wa utumishi kwa ufupi tunaweza kusema kuwa wameitwa katika wito maalumu wa uongozi katika Kanisa hawa ni Mitume, Manabii, Wainjilisti, Wachungaji na Waalimu. Watu hawa hawajiiti wenyewe katika Eneo hili kwa ufupi ni kuwa wameitikia tu mpango wa Mungu katika maisha yao 1Timotheo 1; 12, Matendo 9; 15-16. Hivyo pamoja nakuwa kila Mkristo anayo huduma tunapaswa kutambua kuwa ziko huduma hizi ambazo Mungu ameziweka za kimaongozi na Hii ndiyo Huduma ya Kichungaji tuliyoitiwa.



MUNGU HUITA WATU NAMNA GANI? 


     Inapofikia hatua ya watu kujadili kuwa umeitwa namna gani na kila mtumishi kutoa ushuhuda wake jinsi walivyoitwa hapo ndipo wengine hingia mashaka wakidhani kuwa huenda labda hawajaitwa kwa vile wanavyojilinganisha na wengine Biblia inasema mtu anayejilinganisha na mwingine hana akili (2Wakoritho 10; 12) Kila mtu ni tofauti na mwingine  kwa sababu Mungu amekusudia uwe vile ulivyo, Mungu  huita watu kwa njia mbalimbali na kwasababu kila mtu ni wa pekee Mungu humuita  kila mtu kwa njia ya tofauti .

  • Musa aliitwa kutoka katika kichaka kilichokuwa kinawaka moto na hakiteketei Kutoka 3; kwa kusudi la kuwaokoa waisrael
  • Isaya aliona maono hekaluni na kusikia sauti ikimwambia nenda na uwaambie (Isaya 6;1-9
  • Paulo aliitwa kwa kupigwa nchini kwa mwanga mkali Matendo 9;1-20
  • Elisha kwa kutupiwa vazi na Eliya na kuambiwa amfuate 1Falme 19;19-20 kuwa mrithi wa Eliya
  • Yoshua kwa kuwekewa mikono na Musa Hesabu 27:18 Kuwaingiza watu katika Inchi ya kanaani
  • Timotheo kwa kuchaguliwa na Mchungaji wake Paulo na kuwekewa mikono Matendo 16;1-3  kwa kusudi la kuwa Mwinjilisti na Mchungaji
  • Samuel na Samsoni kwa kutolewa na wazazai wao kuokoa Taifa na kuwa kuhani Waamuzi 13,1Samuel1;11
  • Barnaba kupitia huduma yake Matendo 9;26,13:1-2 Kuwa Mishionari, Mchungaji, Mwalimu na mwinjilisti
  • Prisilla na Akila Kupitia huduma zao kuwa waalimu na wamishionari Matendo 18;18-26,Warumi 16;3
  • Gideoni kupitia malaika Waamuzi 6 ili kuwashinda maadui wa Israel, Mariam Malaika ili awe mama wa Masihi Luka 1; 26-38.
  • Kwa namna yoyote ile ambayo umeitwa wito unakuja kwa kupitia Roho wa Mungu 1Koritho 2;14,Yohana 10;27 na mtu husikia kwa masikio ya kiroho wala si kwa masikio ya asili, Mungu ndiye ambaye huita haijalishi ametumia njia gani kwani mtu huwa hajichagui mwenyewe Yohana 15;16, Mungu huwaongoza watu wake aliowaita hatua kwa hatua mpaka kufikia lengo alilolikusudia atumike Yohana 10;27, Zaburi 37;23 Matendo 13;2 na 16;6-10 Yeye Mwenyewe atakujaza hamu ya kuhubiri na kutaka kuwahudumia watu wake na kuwasimamia utajikuta unamtafuta na atathibitisha kwa namna nyingi kuwa yuko pamoja nawe atakupa vipawa ambavyo vina sauti yake na hutafurahia kufanya kazi nyingine yoyote.



MADHARA YA KUIFANYA KAZI YA MUNGU BILA WITO;


    Kuingia katika utumishi bila ya wito ni jambo la hatari sana 2Samuel 18; 19-33, Ezekiel 13; 36 na Walawi 10;1-2. Wako watu wengine leo huingia katika huduma kwa nia mbaya aidha wanataka Heshima au kuwa viongozi wakubwa katika watu au kuingia kwa sababu yoyote ile isiyompendeza Mungu



UMUHIMU WA WITO KUAMBATANA NA UPAKO.


     Kama mchungaji umeitwa katika huduma kwa maana kuwa umetumwa na Yesu kama yeye alivyotumwa na Baba yake, Yohana 17; 18 ni muhimu basi wito wako uandamane na upako Matendo 10; 38, Luka 4; 18 Kwa msingi huo basi kama Bwana amekutuma, Roho wa Mungu atakuwa juu yako bila ya kujali kuwa umeitwa namna gani na atakupaka mafuta maalumu kwa kusudi la kutimiza yale aliyoyakusudia.



Umuhimu wa upako


     Tendo la kupakwa mafuta lilikuwa la muhimu sana kwa jamii ya nyakati za Biblia na tamaduni za wakati ule Ruthu 3;3, Ruthu alijipaka mafuta ili ajiwakilishe kwa Boazi, hata hivyo wakati wa huzuni watu hawakujipaka mafuta Daniel 10;3, Mafuta pia yaliweza kutumiwa kama tiba Luka 10;34 na pia yalitumika wakati wa kumweka mtu wakfu (Kutoka 30;22-29 na 1Samuel 16;1 kutoka 29;29,30;26.kwa msingi huu wafalme, makuhani na manabii waliitwa wapakwa mafuta kwa sababu waliwekwa wakfu kwa kutiwa mafuta Lawi 4;3,4;16,6;20 na Zaburi 133;2 wakati mwingine waamuzi pia walikuwa na upako ingawa si kwa kuwekewa mafuta



Matokeo ya upako


     Upako unapokuwa juu ya mtu unampa Mungu nafasi ya kukamilisha wajibu fulani ndani ya mtu ambao kwa nguvu zake za kawaida asingeweza kuutimiza (Waamuzi 14;6,14;19,15;15-16,16;30 Mchungaji anapohudumu katika nguvu hizi huonekana shujaa.





Siri ya upako


      Siri ya kuwa na upako ni rahisi na ngumu, Yesu katika uanadamu wake alijiachia kwa Roho Mtakatifu kwa asilimia mia moja Hivyo Yesu alipokea Roho Mtakatifu bila kipimo (Yohana 3; 34) Hivyo basi kipimo cha upako wa mtu kinategemea jinsi gani anajiachia kwa Roho Mtakatifu na katika utii wa mapenzi ya Mungu, Kadiri mitume walivyojiachia kwa Roho Mtakatifu ndivyo na Roho alivyowatumia Luka 24; 49, Matendo 2; 37. Huduma ya kichungaji itakuwa na matokeo makubwa sana kama upako utakuwa juu yetu hivyo ni lazima tuuhitaji upako kwa gharama yoyote Zaburi 92; 10 


Tahadhari.


     Upako utafanya kazi juu ya mtu kulingana na wito ambao Mungu ameukusudia kwa mtu Matendo 9;15-16 Yohana 21;18-19 Paulo na Petro walikuwa na upako kulingana na huduma walizokuwa wameitiwa.Ni muhimu kujiachia kwa Mungu ili atuongoze kama atakavyo Matendo 19;15,10;6-8,16;9-12,18;9-11, Kama Mungu amekupaka anaweza kukutumia hata kama unatabia mbaya lakini hii ni hatari kwako kwani unaweza usiingie mbinguni, kumbuka pia kuwa upako ni gharama na hupatikana kwa maombi na si kwa kuambukizwa kirahisi tu, usiigize upako wa mtu mwingine,tumia upako kwa nidhamu kwani unaweza kufanya mambo makubwa sana lakini ni muhimu kuutumia kwa adabu, usiufungie mipaka, usiulazimishe wewe hubiri na kukaa katika neno 2Timotheo 4;2.



B: KUENDELEZA MAISHA YA KIROHO.


     Baada ya kuwa Mtumishi amethibitisha kuwa ameitwa  katika wito huu wa utumishi ulio maalumu hana budi kufahamu kuwa ana wajibu wa kuhakikisha anajiendeleza Kiroho ni hatari kuwahudumia wengine kisha tukajisahau kudumisha uhusiano wetu na Mungu na kosa hili limekuwa likifanywa na watumishi wengi wa Mungu na hatimaye hujikuta wakifilisika kiroho na kuharibika Wimbo uliobora 1;5-6.

  • Mtumishi awaye yote ni lazima awe amekutana na Mungu yeye mwenyewe kibinafsi, Mungu tunayejifunza habari zake ni Nafsi na hushughulika na mtu mmojammoja Binafsi Hivyo ni lazima ukutane naye Binafsi na abadilishe maisha yako kupitia wokovu. John Wesley Mwanzilishi wa Methodist alihubiri kwa muda kabla ya kuokoka si vizuri kwa mtu kuwa katika huduma huku akiwa hajakutana na Mungu Binafsi na kuzaliwa mara ya pili Kumbukumbu 18; 20.
  • Kuzaliwa mara ya pili pekee hakutoshi ni lazima mtumishi ahakikishe anakaa ndani ya Kristo Yohana 15;1-4 Matunda hayawezi kuzaliwa kama tawi litakuwa nje ya mzabibu, Aidha haiwezekani kabisa Mkristo mtumishi kufanya kazi hii bila kujazwa na Roho Mtakatifu  Matendo 2;38-39, Matendo 9;17.19;2 Efeso 5;18 ni jambo lisilofaa mtu kuwa mwalimu, muhubiri au mtumishi huku hajajazwa Roho Mtakatifu, Pamoja na mafundisho yoote mazuri na kukaa miguuni pa Yesu bado Aliwasisitiza wanafunzi wake kutokuhubiri kwanza mpaka wamevikwa uwezo huu utokao juu Roho Mtakatifu Luka 24;47-49 aidha ni muhimu ikumbukwe kuwa kujazwa Roho Mtakatifu sio sababu ya kukufanya kichwa kivimbe kwa kiburi  kusudi ni kutupa neema na nyenzo tunazozihitaji kwa ajili ya kazi Matendo 3;12 siku hizi hata watu wa dini wanajazwa Roho hivyo upentekoste sio issue ya kujivunia
  • Lazima uendelee kujifunza Biblia na kujisomea, Mtu hataishi kwa mkate tu bali kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu Mathayo 4; 4.Inasikitisha kuona kuwa watumishi wengi wa Mungu husoma neno la Mungu kwa sababu tu anajiandaa kwenda kufundisha wengine, hii sio halali lazima ulisome neno la Mungu kwa malengo na sio hovyo hovyo tu eti kwa kua unataka kufundisha hapana.
    1. Biblia lazima isomwe kwa kumaanisha ikiwa umeitwa na hii ndio huduma yako na unaishi kwa ajili ya Biblia basi huna budi kuisoma kwa kumaanisha Neno la Mungu kwako liwe swala la kufa na kupona Lazima ujifunze ujitoe kulisoma kuliishi na kulitegemea. Neno la Mungu ni upanga wa Roho ni silaha ya pekee katika kumshida shetani (Efeso 6;10-17,Ebrania 4;12) Sasa kama silaha hii utaipuuzia ni rahisi kushindwa vibaya vitani ndo maana haishangazi kuona watumishi wakishindwa leo.
    2. Lazima ulisome kwa moyo wa kutamani kujifunza na kwa kupondeka Zaburi 119;20 Moyo uliopondeka unaotamani kujifunza uliojaa shauku ya kumjua Mungu ni moyo ulio mwepesi kujua mapenzi na makusudi ya Mungu Filipi 3;8-11 Moyo wa aina hii utakusaidia kujifunza na kuona hata zaidi ya mipaka ya Dhehebu lako na theolojia yako. Roho wa Mungu atakufundisha zaidi ya uyajuayo. Ubishi wa kimadhehebu umewafunga watumishi wengi wa Mungu kumuwekea mipaka ya theolojia yao na misingi yao ya imani bila kufahamu kuwa Mungu hawezi kuwekwa katika kikombe Jifunze hata kwa wengine.
    3. Biblia isomwe kwa kusudi la kujijenga kiroho, Wahubiri wengi ukimuona anasoma neno ujue ana semina au anapaswa kuhubiri siku Fulani  huu ni ufisadi huko ni kuwaibia watu ndugu yangu soma kwa kusudi la kujijenga kiroho wewe mwenyewe kusoma kunakomaanishwa hapa si kwa ajili ya kutengeneza jumbe kwani kujitoa kwako katika kujisomea neno kutakusaidia  wewe kutengeneza jumbe pia hatuhitaji kutoatu tunahitaji pia kupokea
    4. Soma Biblia kwa Mpangilio maalum Biblia ina vitabu 66 unapaswa kuisoma kwa mpangilio maalumu hatuwezi kukupa yoote  lakini ni lazima ulenge kuisoma yenyewe kwanza licha ya kusoma vitabu vitakavyoihusu biblia kusoma kwako kusiwe kwenye mlengo mmoja tu soma kwa mpangilio utakaogusa agano la kale na jipya kwa namna mbalimbali si lazima iwe kitabu kwa kitabu tu.

  • Lazima ujitoe katika Kuomba. Wengi tumesikia ule usemi usemao unaposoma neno la Mungu Mungu huzungumza na wewe na unapoomba wewe unazungumza na Mungu ni lazima tuwe na Muda na Mungu wa kwetu Binafsi tunahitaji maombi yetu Binafsi, maombi na familia zetu, maombi na viongozi wa kanisa, maombi na waalimu wa shule za jumapili maombi na watu wenye mahitaji n.k Pamoja na yoote hapo maombi yako Binafsi ya sirini ni ya muhimu kwa shughuli zako za kiroho na maisha yako.
  • Lazima ujifunze Kutafakari. Kutafakari ni fani iliyopotea kwa wakristo wengi na watumishi pia hii ni kwa sababu ya uzembe, au uvivu au kutokupangilia au kutokujua umuhimu au kutokuwa na Muda wa kufanya hivyo na kutoa kipaumbele kwa mambo mengine. Lazima tuitafakari sheria ya Mungu (Zaburi 63; 6, 77; 12,143;5) Kutafakari sio swala la ndoto za mchana ni kuchukua muda wa kukaa kimya na kuzama ndani kufikiri kile ambacho bwana anafundisha katika neno lake, jinsi rehema zake zilivyo na kutaka kujua mengi kumuhusu.
  • Lazima uhakikishe unazaa matunda ya Roho Galatia 5; 22-23. Matunda ya roho ni muhimu sana kwa watumishi wa Mungu haya ndiyo yanayodhihirisha kuwa umekomaa kiroho matunda haya ni Upendo, Furaha, Amani, uvumilivu, utuwema, fadhili, Uaminifu, upole, na kiasi. Inawezekana yakawa yako mengi zaidi ya hayo lakini haya yanabeba mwelekeo mzima wa jinsi Mungu anavyotaka tuwe, Kwa bahati mbaya wengi tumeshuhudia watumishi wengi wa Mungu wakiwa na upungufu wa Matunda haya ya kiroho wengi sio waaminifu, wala hawana uvumilivu wamejaa kiburi, ugomvi na hukumu dhidi ya wengine kwa ufupi yale matendo ya mwili ndio hujidhihirisha kwao zaidi  kuliko haya ya roho haipaswi kuwa hivi ndugu zangu lazima Kristo aumbike ndani yetu Galatia 4;19, Watu ambao Kristo hajaumbika ndani yao utaona matendo ya mwili yakidhihirika au yakiwa ndani yao, ziko chuki, kuonea wivu huduma za wengine, uadui kugombana, choyo, uhasama, wizi wa sadaka za waamini, kutokulipa zaka kwa uaminifu, kupendelea watu ukabila kugombea ukubwa, taama za aina mbalimbali hasira kali, kukosa uvumilivu, kufurahia shida na taabu za wengine, kukomoa, kutoa adhabu kali kuliko kawaida na bila rehema kukosa uvumilivu, hakuna upendo, ulafi kukomoana, kuweko na makundimakundi faraka. tamaa za zinaa na uangaliaji wa picha za ngono, na mambo kadha wa kadhaa Hizi ni hali zinazoonekana wazi leo kwa watumishi, Huku wengi wakiwa wameridhika na pale walipo wakiwa hawana tena juhudi ya kujiendeleza Kiroho hivyo wengi wamedumaa huku wakiwataka washirika wakue Kiroho na kuwa kama Kristo huku wenyewe biashara imetushinda hali kama hizi zisipofanyiwa marekebisho Hatuwezi kuujenga Mwili wa Kristo leo Kipofu hawezi kumuongoza kipofu mwenzake.



C: Umuhimu wa Kujiendeleza Kielimu


   Kujiendeleza kielimu ni moja ya sehemu muhimu katika maandalizi kwa ajili ya huduma, ninaweza kusema kuwa elimu ni ya lazima katika kumtayarisha mtu kwa ajili ya huduma  hii inamaanisha kujizoeza kwa maarifa,nah ii inamaanisha kuwa lazima uende shule kila mtu anayetaka kumtumikia mungu lazima awe na elimu ya kutosha au apate ujuzi mwingi kadiri iwezekanavyo watu humdharau mtu asiye na elimu na humuheshimu mtu mwenye elimu “Elimu huleta ubaguzi wa halali” elimu itakusaidia katika kuilewa Biblia na kuwasilisha ujumbe unaoukusudia kwa lugha inayoweza kueleweka na kukubalika Biblia inaonyesha kuwa Mungu aliwatumia sana watu waliokuwa na elimu Musa Matendo 7;22,Daniel Daniel 1;4,17-20 na Paulo mtume 1Koritho 1;26-29.2;1-4,Wakolosi 1;9. Hta hivyo wenye elimu hawapaswi kujivunia elimu zao na kuwa na kiburi 1 Koritho 8;1-2, 1; 26-31 hata hivyo maarifa yaliyowekwa wakfu kwa ajili ya Mungu ni yenye faida kubwa kuliko ujinga.

§  Elimu ya kawaida pia ni ya muhimu kwa kazi ya Huduma John Wesley aliwaambia wahudumu vijana aliokuwa akiwafundisha kuwa wasome au waache huduma ukweli ni kuwa aliona umuhimu wa kuwa na elimu na uhusiano wa kufanya vizuri katika mambo ya kiroho Mchungaji asiyesoma anafananishwa na gari lisilo na mafuta hutafika mbali.

§  Soma kwa malengo ya kupanua ufahamu,Mchungaji unapaswa kufahamu mambo mengi ,wsoma kwa lengo la kuwa na ujuzi wa mambo meni,Soma kwa lengo la kuwa na ujuzi wa mambo yanayoendelea Information huwezi kuishi kama kisiwa tu maalbino wanauawa wewe hujui hata ni kwa nini wanauawa lazima upate taarifa kumbuka Elimu tunayoizungumzia hapa sio tu ya kukaa darasani lakini pia ya kujifunza wewe binafsi

§  Mchungaji anapaswa asome nini? Kuna mambo mengi na taarifa nyingi sana duniani ambazo huwezi kuzipitia zote kulingana na muda  hivyo kanuni inapaswa kuwa lazima uchague Be selective,Unahitaji kusoma na kusikiliza taarifa za habari na mambo yahusuyo ulimwengu  na mambo ya muhimu, Soma vitabu mbalimbali  vinavyohusu maisha ,Historia, Sayansi Jiografia nk. Sio lazima yale unayosoma ya we ya Kiroho tu hapana lakini soma mambo yatakayokufanya uwe na ujuzi fulanifulani kuhusu ulimwengu na shughulishughuli zinazoendelea

§  Mchungaji lazima uwe mtu unayefundishika msingi wa yote tunayoyazungumza hapo juu ni kuwa na moyo wa kufundishika kuna vyanzo vingi vinavyoweza kutusaidia kujifunza na unaweza kujifunza hata kutoka kwa mwendawazimu wako watu wengine kila wanacho kiona wanakikosoa tu ukiwa tayari kusikiliza hata kwa mwendawazimu unaweza kujifunza kitu Samsoni alitoa asali katika mzoga wa simba (Waamuzi 14;8-9). Nyuki wana tabia ya kuingia kila mahali kuokoteza hata chooni lakini baadaye hutengeneza kitu kitamu sana yaani asali wako watu wengine hawapendi kujifunza kutoka kwa wengine na matokeo yake hawafanikiwi katika huduma zao.



UMUHIMU WA MCHUNGAJI KUWA NA MAKTABA



    Mchungaji kuwa na vitabu ni jambo la muhimu usitegemee mafunuo tu mafunuo ya kweli na halisi huja pia kwa kujifunza kutoka kwa wengine Paulo mtume aliheshimu sana vitabu ingawa alikuwa ameketi chini ya waalimu maarufu walioheshimika sana wakati ule kama Gamaliel,Alikuwa na uzoefu katika huduma kwa miaka ipatayo 30 hivi na alikuwa na mafunuo makubwa hata kupelekwa katika mbingu ya tatu lakini bado alithamini vitabu angalia 2Timotheo 4;13 zaidi ya yote anamsihi Timotheo kuwa afanye bidii katika kusoma 1Timotheo 4;13 mwana falsafa mmoja alisema huyuni Edward Gibson “ ni afadhali niwe masikini lakini mwenye moyo wa kupenda kusoma vitabu kuliko kuwa mfalme asiye na moyo huo” kwa bahati mbaya sisi watu weusi hatuna tabia ya kupenda kujisomea hata wazungu wametugundua na wana usemi usemao ukitaka kumficha kitu mwafrika kiweke kitabuni. Muhubiri mashuhuri aliyeleta uamsho mkubwa Marekani Jonathan Edwards alikusanya maarifa yoote kuhusu Mungu ambayo yangeweza kumsaidia kupata maarifa kumhusu na kwa kweli kadiri alivyosoma ndivyo alivyoandika amekuwa mfano wa kuigwa wa wachungaji na wahubiri ambaye alikuwa na huduma kubwa kwa ajili ya upenzi wake wavitabu na kujisomea na kuwa na maktaba kubwa



MAKTABA YA MCHUNGAJI;


     Mchungaji lazima uwe na maktaba yenye vitabu vya aina mbalimbali hata hivyo kuna vitabu ambavyo tunavipa kipaumbele kama vitabu vya msingi amabvyo sitarajii vikosekane katika maktaba ya mchungaji Yeyote

  • Biblia. Biblia ni lazima ipewe kipaumbele cha kwanza kuwepo katika maktaba ya kichungaji hata hivyo haitoshi kuwa na biblia ya aina moja tu  lazima uwe na biblia za tafasiri tofautitofauti tangu King James Version ilipotafasiriwa mwaka 1611  hata leo kuna zaidi ya tafasiri 500 za kiingereza peke yake na ni vigumu kuelezea ipi ni nzuri hivyo ni muhimu kwa mchungaji kuwa na Biblia za matoleo tofauti tofauti hata ya wale wa imani potofu na pia Biblia zenye mafunzo Studies Bibles kwa bahati mbaya Nyingi ni za kiingereza.
  • Kamusi za biblia na kamusi za kawaida (Dictionaries) Ni muhimu kuwa nazo si utahitaji kujua maana ya baadhi ya maneno ya kawaida katika Lugha mbalimbali ikiwemo Kiswahili na kadhalika pia utahitaji kujua historia ya neno Fulani katika biblia na hata maana yaeke Bila kamusi za biblia utafahamuje hayo pia inasikitisha kuwa mpaka sasa hatuna kamusi za Biblia za Kiswahili zaidi ya zile za Don Fleming  hii ni aibu kwa wasomi wa Tanzania kushindwa hata kutafasiri zile za kiingereza katika Kiswahili zikasaidia watu watu wako na shughuli kasha unajiita Msomi mimi Bwana ameniagiza kuandika Commentary ya Kiswahili na shughuli ya kuitengeneza inaendelea.
  • Itifaki (Concordance) Hiki ni kitabu kinachosaidia katika utafutaji wa andiko Fulani badala ya kuchukua Muda mrefu kutafuta katika Biblia itifaki inasaidia kulipata andiko kwa wepesi katika kiswahili iko moja tu na inasemekana iliandikwa na walutheri wapentekoste mpaka leo tumelala. Za kiingereza ziko nyingi lakini iliyo nuri zaidi ni NIV Exhaustive Concordance of the Bible na Strongs hizo ni nzuri sana
  • Vitabu vya mchanganuo mbalimbali ya maandiko Commenteries Hizi nazo ziko za aina kuu mbili kitabu kimoja cha mchanganuo wa maandiko ambavyo mara nyingi ni nafuu lakini vinachanganua kifupi sana vingine vinavyochanganua kirefu vinakuwa ni mlolongo wa vitabu amabavyo kwakweli ni gharama kununua kimoja kimoja na kwa bahati mbaya katika Kiswahili tunayo moja tu ya bwana Don Fleming wa kanisa la biblia ambayo imetafasiriwa Commentaries nyingi ni za kiingereza inasikitisha kukosekana kwa Kiswahili niombee kwani Bwana amenipa mzigo wa kuandika katika kiwswahili hivyo Kumbuka Mchungaji Innocent kamote katika maombi yako ili nifanye hivyo kwa utukufu wake.
  • Vitabu vingine ambavyo sio vya Msingi bali vinapewa kipaumbele cha pili ni pamoja na vitabu vya kitheolojia, kuna vitabu vingi sana vya kitheolojia lakini vingi ni vya kiingereza, Vitabu vinavytoa maelezo kuhusu Biblia yaani Bible Introduction, vitabu vinavyohusu historia ya kanisa , Israel na vinginevyo
  • Vitabu vingine ni kama maarifa ya mchungaji, namna ya kuhubiri namna ya kutumia maandiko kwa halali, utunzi wa hutuba za kibiblia na mwisho vitabu vinginevyo vya kawaida.



MCHUNGAJI NA ELIMU YA CHUO CHA BIBLIA.


   Kadiri muda unavyokwenda ndivyo changamoto zinavyoongezeka zamani masomo ya wachungaji yaligusia tu maswala ya Biblia na huduma za kikanisa aidha na theolojia kidogo lakini kadiri siku zinavyokwenda umuhimu wa elimu nao umeongezeka yako makundi ya vijana yanayohitaji uangalizi maalumu, maswala ya muziki,maswala yanayohusiana na ushauri nasaha Counceling ambayo kwa kweli ni huduma kamili na inahitaji taaluma,maswala ya miradi,Vyombo vya habari na television, magazeti, redio maongozi ya kifedha usimamizi wa kitaaluma n.k haya yote yanahitaji kusoma na sio mafunuo tu.

   Hitaji la Elimu ya kichungaji limekaziwa katika maandiko Paulo anapoweka wazi kuwa kazi ya mchungaji na mwalimu ni kuwaandaa watu wa Mungu hata kazi ya huduma itendeke na mwili wa Kristo ujengwe ni lazima sisi wenyewe tuwe tumeandaliwa kwa kazi hiyo ya huduma  na elimu ndiyo  inayoweza kufanikisha jambo hilo

Inashangaza kuona jinsi watu wanavyoiponda elimu ya vyuo vya biblia lakini wenyewe wanataka kufundisha makanisani mwao unawezaje kufundisha huku wewe hujajifunza? 2Timotheo 2;2 ni msingi unaosisitiza umuhimu wa kujifunza kwa asili Vyuo vya biblia vilianzishwa wakati wa Nabii Samuel ambaye alikuwa na vyuo vya wana wa manabii 1Samuel 10;5-6, na baadaye tunaona Eliya akiwa anaendesha shule hii ya wana wa manabii 2Wafalme 2;3-7 hivyo manabii walikuwa  na shule zao maalumu zilizokuwa zikiwandaa kwa huduma za kinabii Itashangaza sana kuona watu wa leo wakipinga swala zima la watu kwenda vyuo vya biblia yako mambo mengi ambayo kadiri tutakavyojifunza utaona kuwa kunahitajika elimu au utaalamu katika hilo mfano namna ya kutafasiri maandiko lakini kwa kufupisha nataka kusisistiza tu umuhimu wa mchungaji kupitia vyuo vya Biblia na semina mbalimbali.


MCHUNGAJI NA MAHUSIANO



    Huduma ya kichungaji ni huduma ya wito lakini ina viwango ambavyo kwavyo Mungu ameviweka akikusudia kuwa tunapaswa kuwa navyo 1Timotheo 3; 2-5. Basi imempasa Askofu awe mtu asiyelaumika; Mume wa mke mmoja mwenye kiasi na Busara mtu wa utaratibu, Mkaribishaji ajuaye kufundisha, si mtu wa kuzoelea ulevi, si mpiga watubali awe mpole, si mtu wa kujadiliana wala asiwe mwenye kupenda fedha, mwenye kuisimamia nyumba yake vema ajuaye kutiisha watoto wake katika ustahivu (Yaani mtu asiyejua kuisimamia nyumba yake mwenyewe, atalitunzaje kanisa la Mungu?) Wala asiwe mtu aliyeongoka hivi karibuni asije akajivuna akaangukia katika hukumu ya ibilisi, Tena imempasa kushuhudiwa mema na watu woote walio nje ili asianguke katika lawama na mtego wa Ibilisi. Mistari hiyo hapo juu inaweka mpango wa kiwango ambacho Mungu anakikusudia kwetu kama watumishi kukifikia katika Eneo hili tutaangalia mahusiano ya mchungaji na familia yake ikiwa ni pamoja na ndoa na wajibu wa mama mchungaji hali kadhalika mchungaji kama  Mume, baba nyumbani na mtunzaji wa familia haya yana mchango mkubwa sana katika huduma ya kichungaji na maisha ya utumishi kwa ujumla viwango alivyoweka Mungu vinahitaji neema yake kuvifikia na penginepo Mungu ameviweka ili tuone mapungufu tuliyonayo ili tusiwe wenye kuhukumu wengine na badala yake tutambue mapungufu yetu tukijijua kuwa na sisi tunao wajibu wa kutimiza pamoja na kuwa tunalisimamia kanisa la Mungu.



A: UMUHIMU WA NDOA ILIYO BORA KATIKA UTUMISHI


  Kama kuna jambo lililo la muhimu sana katika utumishi ni ndoa na hasa ndoa iliyo bora, mahusiano ya ndoa kati ya mume na mke yanakwenda moja kwa moja katika muda wa wanandoa hao walipoanza mahusiano yao  walipo pendana na kuchaguana hili linapendeza sana Hata hivyo uchaguzi wa mke kwa Mchungaji ni swala la muhimu zaidi linalohitaji umakini zaidi kwa ufupi maongozi ya kimungu (Mithali 19;14,31;10-12) woote tunajua umuhimu wa ndoa na woote tunajua mpango wa Mungu kuhusu ndoa (Mwanzo 2;18, Mathayo 19;4-6) hatuwezi kujenga hoja katika namna watu wanavyopata wake zao kwa sabbabu ya tamaduni tofauti lakini Mungu alikusudia mwana ndoa awe Msaidizi mwenye kufaa, awe mwenzi wako na muwe na umoja  hii ni muhimu kwa kuwa ndoa hutoa uponyaji wa kisaikolojia na kimwili, Mchungaji yeyote anayeweza kuwa na ndoa iliyo bora ana nafasi ya kuwa kuwa mchungaji bora, ndoa yako na watoto wako wana mchango mkubwa katika huduma yako Lakini zaidi sana uhusiano wako wa kindoa na mumeo au mkeo  una uwezo wa kustawisha huduma na kuwa mfano wa kuigwa katika kanisa au huduma ambayo Bwana amekupa kusimamia kwa maana nyingine ndoa mbovu inaharibu huduma na inashusha heshima inayoonyesha una uwezo wa kusimamia familia nyingine na ndoa nyingine ambazo Mungu amekupa kuzisimamia

    Uchungaji wetu unaanzia katika ndoa zetu na familia zetu wako wahubiri wengine wana sura mbili sura aliyonayo nyumbani ni tofauti na sura aliyonayo kanisani wana familia lazima wamuone mchungaji kama baba wa kiroho zaidi ya jinsi kanisa litakavyomuona.



B; WAJIBU WA MAMA MCHUNGAJI.


  Mama mchungaji ana wajibu mkubwa sana katika maisha na huduma ya mumewe kule kukubali kuolewa na mchungaji lazima kuambatane na kukubali au kuheshimu kuwa mtu huyo ameitwa na Mungu kwa kufanya hivyo hata yeye ataishi maisha ya Furaha na amani kwa kuruhusu mapenzi ya Mungu katika maisha yao. Mama Mchungaji lazima awe na ujuzi binafsi kuhusu Mungu na awe na hekima itakayo muongoza yeye na mumewe pamoja na kazi ya Mungu

   Kuwa mama mchungaji si kazi rahisi kama tunavyofikiri wengi wameua huduma nzuri tu za waume zao na wengi wamekuwa si mfano mzuri wa kuigwa wakati mwingine wamechukiwa na washirika kwa kuwa vile walivyowategemea wawe sivyo wenyewe walivyo Mchungaji anaweza kumsaidia mkewe kwa kumruhusu kuhudhuria semina mbalimbali, kumnunulia baadhi ya vitabu au kumtafutia mwanamke mtumishi anayefanya vizuri na aliyekomaa kiroho anayeweza kumsaidia lakini lazima nao wawe wenye moyo uliopondeka wako mama wachungaji ambao hawafundishiki ni lazima wawe na ujuzi katika neno na mapambano kwa kweli wawe hodari katika vita vya utumishi wajue kuwa adui atapenda kuwatumia wao kama mlango wa kusambaratisha huduma za waume zao Biblia imejaa mifano ya wanawake walioruhusu kutumiwa na adui au kuwa kinyume na imani za waume zao hapa nitakupa mifano minne tu


  1. Hawa aliweza kutumika kama mlango wa kuingiza dhambi ulimwenguni Mwanzo 3;6.
  2. Mke wa Ayubu alitumiwa kuwa kinyume cha imani ya mumewe Ayubu Ayubu 2;9-10
  3. Mke wa Lutu inaonekana alipendezwa na maisha ya Sodoma na tabia zile kiasi cha kutothamini wokovu waliopewa na kuamuriwa  kutokuangalia nyuma Mwanzo 19;26
  4. Mke wa Manoa alikuwa na imani kwa Mungu akamtia moyo mumewe aliyekuwa na hofu kuwa Mungu angewaua na walibarikiwa kumpata mtoto Samson Waamuzi 13; 2, 23.

 Kwa msingi huu mke wa Mchungaji anaweza kuwa Baraka au kusababisha matatizo katika huduma ya mumewe, Mwanamke na atimize kila lililowajibu wake katika ndoa ikiwa ni pamoja na kumtosheleza mumewe katika Tendo la ndoa Mwanamke mpumbavu huibomoa nyumba yake kwa mikono yake mwenyewe Mithali 14;1 ni maombi yangu kuwa Mungu atawasaidia mama wachungaji kufahamu wajibu wao na kuhakikisha wanatunza zawadi zile ambazo Mungu amezitoa kwa kanisa lake watumishi  yaani hawa aliowatenga kwa ajili ya kazi yake katika kanisa.



WAJIBU WA MAMA MCHUNGAJI NYUMBANI


 Jukumu la kwanza la mke wa mchungaji ni Nyumbani kwake, Mchungaji na familia yake hata wasipopenda lakini jamii itajua tu kuwa ni wapi mchungaji anaishi na wataiangalia nyumba yake kama kielelezo kwa msingi huo watu wanatarajia nyumba ya mchungaji kuwa mfano wa kuigwa na familia yake pia inapaswa kuwa mfano wa kuigwa, na kama jamii haijawahi kuona familia ya Kikristo basi kwa mchungaji ndipo patakuwa mfano. Lazima nyumba hiyo iwe safi vitu vikae katika mpangilio, ukaribishaji uwe lugha nzuri ya mama na kujiamini wako wengine wanapoona wageni ndio huanza kuwauliza waume zao nini cha kufanya kwakuwaita pembeni mbele ya wageni hii sio tabia nzuri mama lazima ajiamini na kujifunza kumtegemea Mungu tabia ya choyo ni mbaya sana kwa wakristo lakini ni mbaya zaidi ikiwa kwa mama mchungaji majukumu ya kikanisa na kijamii yapewe nafasi ya pili ya kwanza ni nyumbani kwa mchungaji



WAJIBU WA MAMA MCHUNGAJI KANISANI.


     Mama mchungaji hapaswi kuwa na vyeo vingi sana kanisani kule kuwa mama mchungaji tu tayari ni wajibu mkubwa wa kutosha vinginevyo hataweza kukamilisha majukumu yote atakayopewa na itakuwa lawama anaweza kufanya hivyo pale huduma inapokuwa changa lakini majukumu yapungue kadiri wanavyopatikana watu wa kushika nafasi hizo

  • Mama mchungaji anaweza kukubali kwa hekima nafasi kadhaa kama kuhubiri na kufundisha n.k kwa kuonyesha mfano kwa wanawake wengine namna wanavyopaswa kutumika maana wengine usipotumika kabisa inakuwa kero mbona yeye hatuoni akifanya
  • Mama mchungaji anaweza kusaidia katika kazi za madhabahuni wakati wa maombezi na ushauri pia akumbuke kuwa ana nafasi kubwa katika kufundisha wanawake mabinti na vijana, wajane au hata shule za jumapili. n.k
  • Mama mchungaji lazima awe mtii kwa mumewe na mtetezi wa mumewe na mlinzi wa mumewe unapaswa kumsaidia katika kujua namna ya kuhubiri vizuri kwani una nafasi ya kumkosoa mumeo kwa upendo na kupokea watu wanasema nini hivyo hakikisha unafanya kwa ustaarabu.
  • Mama mchungaji hatakiwi kuwa mmbeya na mchonganishi wala hatakiwi kuwa na wivu mchungaji ni kiongozi wa jamii na watu watapenda kumsogelea hata wa jinsia tofauti hivyo homa ya wivu wa mama mchungaji haitakiwi kuwa juu muamini mumeo,Vumilia magumu na mapito pamoja na mumeo



 WAJIBU WA MAMA MCHUNGAJI KWA MUMEWE
 
     Kazi ya kichungaji ni kazi ngumu yenye migandamizo mingi mama mchungaji anapaswa kuwa mwenye kumtia moyo mumewe wakati wa kukata tamaa

     Mama mchungaji asaidie kutunza siri za washirika ambazo washirika watakuwa wakiwaeleza mambo ya ndani wanayokutana nayo bahati mbaya wako wanawake ambao ili waonekane wanajua mambo hupenda kuelezea vitu vya ndani vya washirika hii itaharibu watu kuwa wazi kwenu tunza siri anazokupa mumeo kwa faida ya kanisa kama amekueleza. Kwa kuwa mke mwema mama mchungaji ataweza kusababisha faida nyingi baadhi ni hizi zifuatazo;-

  1. Atasaidia watu wengine wanaojiandaa kuoa
  2. Atasaidia watu wanaokuja kupata ushauri wa matatizo ya ndoa na kuleta ufumbuzi wa matatizo yao
  3. Atawafanya watu waige mfano wa ndoa yake na kuizungumzia kama mfano
  4. Mungu atakutana na mahitaji yake kusudi aweze kuwa mchango mzuri kwa jamii ambayo Mungu amewaita kuitumikia kwa kweli Mungu atakubarikia.



C: Wajibu wa mchungaji kama mume baba na mtunzaji wa Familia


  1. Kama Mume

Huduma ya kichungaji kwa mtumishi tunaweza kusema kwa kiasi fulani kuwa imefanikiwa pale Mchungaji anapofanikiwa pia kuwa Baba mzuri na Mume mzuri, kama familia ya mchungaji imefanikiwa kuishi kwa viwango vinavyokusudiwa utaaminika zaidi katika kazi hii ya utumishi. Mchungaji anapaswa kuonyesha upendo wa dhati kwa familia yake ingawaje waafrika wakiona unampenda sana mkeo watasema unajidai Lakini Biblia imeagiza hivyo utaonyeshaje kuwa unampenda mkeo Biblia imetoa namna unavyoweza kuonyesha kujali na kumpenda mkeo

  • Ishi nae kwa akili onyesha kumuheshimu na kumuhesabu kama zawadi ya Mungu kwa ajili yako na kwa kufanya hivyo dua zenu au dua zako zitasikiwa 1Petro 3;7 ingawaje kila mwanamke anastahili kuheshimiwa kujaliwa na kupendwa sana kwa mke wa mchungaji inatakiwa izidi.
  • Uwe mwaminifu kwake ndoa ni uhusiano wa watu wawili wanaofanya muungano wa mwili mmoja mtu mke na mtu mume Mwanzo 2;24  kwa kuwa mchungaji ni mtu maarufu kwa cheo alicho nacho wanawake wengi huvutiwa na wachungaji na watajaribu kuvuta hisia zako kwao, wanawake wanamuona mchungaji kama mwanaume wa pekee sana kwao ambao wao hawana kwa hivyo kule tu kuwa mchungaji kunayafanya maisha yako yawe hatarini mchungaji atajilinda mwenyewe kwa kuruhusu watu wajue kuwa unampenda mkeo ufa wowote utakaogunduliwa na jamii kati yenu unaweza kuwa mwanya wa mapinduzi katika ndoa yako na utaharibu huduma Mungu aliyoweka ndani yako.
  • Mlee mkeo kiroho, Kuweni na muda wenu binafsi wa kujitoa pamoja kwa   Bwana katika maombi au kujisomea neno au ibada mambo haya ni muhimu kwa kila mshirika lakini ni muhimu sana kwa kila mchungaji, Wachungaji wengi wanaweza kuwa na maombi binafsi asubuhi na hata kujisomea neno huku wake zao wakiwa katika shughuli za kuandaa chai, kuandaa watoto kwenda shule au kufanya usafi hili linatufanya kutofautiana nao sana kiroho, kama unampenda mkeo lazima ujenge tabia ya kuwa na maombi ya pamoja na kutomuacha mbali kiroho wewe ni muhudumu mkuu wa mkeo kiroho pia

  1. Kama Baba

Watoto wanatolewa kama zawadi kwa wazazi  lakini pia Mungu ametuamini kwa kutupa watoto na hivyo tunawajibika kuwatolea hesabu, Kwa ujumla wao hawachagui kuzaliwa katika ulimwengu huu lakini wanazaliwa na wanatupa jukumu na wajibu wa maisha yao, na maadili na hata umilele wao kwa msingi huu basi kunachangamoto katika swala zima la malezi na jinsi mnavyojitawala

  • Kuwa mwangalifu unavyochukuliana na mkeo Hili ni jambo la msingi sana watoto wataanza kujifunza upendo na ukristo wa  kweli kulingana na namna unavyochukuliana na mkeo  hili lisipoangaliwa vema litapandikiza mbegu nzuri au isiyo nzuri kwa watoto hivyo ninyi wenyewe muwe kielelezo Mchungaji uko wakati utashughulika na mkeo katika maswala ya kutiana nidhamu sio ngumi lakini watoto wasijue kinachoendelea
  • Mchungaji ni kiongozi kuanzia nyumbani uko wakati ambapo itakubidi kutumia mamlaka kutiisha nidhamu kwa watoto na kuwaonyesha moyo wa kichungaji inahitajika neema ya Mungu kwani kushindwa kuwasimamia wanyumbani mwako ni kushindwa kulisimamia kanisa tutake tusitake.
  • Nidhamu ni lazima nyumbani wakati mwingine itakupasa kuchapa kama biblia isemavyo Mithali 13;24,19;18 na 23;13 huku ni kufundisha sawa na neno Displina la kilatini ambalo maana yake ni kufundisha Efeso 6;4
  • Malezi ya kiroho ni muhimu na kuwapa watoto elimu iliyo bora ni vizuri wakisoma shule nzuri na uwasimamie katika swala zima la kiroho na elimu. Pia tuhakikishe kuwa tunapatikana nyumbani na kuwa na muda na watoto baadhi ya watoto wa wachungaji walihojiwa na hivi ndivyo walivyosema

Ø  Ninamuona baba kwa nadra sana na wakati mwingine ni vigumu kumuona

Ø  Babaangu anakuwa safarini kila wakati alisema atabadilika lakini hajabadilika bado

Ø  Wazazi wangu wanaona huduma yao kuwa ni ya muhimu kuliko sisi  na kwa kweli ndivyo wanavyosema

Ø  Wanaamini huduma yao ni muhimu kuliko sisi

Ø  Wanafikiri kuwa maisha yao ni ya kutumika tu na kutokatoka

Ø  Hawana hata muda wa kukagua madaftari yetu


Hizo ni baadhi ya lawama zitokanazo na watoto wa wa wachungaji kwa sababu ya tabia zetu nyumbani zinazoathiriwa na huduma.


  1. Kama mtunzaji wa Familia.

Pamoja na majukumu yote ya kichungaji waliyonayo watumishi, bado mchungaji ana wajibu wa kuitunza familia yake, Familia ni ya muhimu sana. Wewe ni shahidi kuwa wako watumishi ambao wamelazimika kuacha huduma kwa sababu tu ya kutafuta kuzitunza familia zao na wako pia ambao wanalazimika kubaki katika huduma ambazo labda wangeziacha lakini kwa sababu ya maswala ya kifedha hawataki kutoka vyovyote iwavyo Mchungaji anapaswa kuitunza familia yake.

     Biblia hailaumu kuwa Fedha ni mbaya lakini ile tabia ya kupenda fedha zaidi ndio ovu 1Timotheo 6; 10. Kupenda fedha kwa namna hiyo ni kuabudu miungu Kolosai 3; 5, na Efeso 5;5 1Yohana 2;15, moja ya migogoro mikubwa kabisa katika nyumba nyingi ni maswala ya kifedha, Malalamiko ya mama mchungaji kuhusu maswala ya Fedha nyumbani yanaweza kupandikizia watoto tabia ya kuchukia huduma wakijua kuwa inachangia katika hali ya ukata waliyonayo, wanafamilia woote akiwemo mama wanapaswa kuridhika na kuishi maisha yaliyo sawa na kiwango cha mapato yao. Familia ya mchungaji iishi kwa bajeti inayolingana na mapato yao na ni lazima wawe na akiba au kutafuta namna ya kuwa na fedha za tahadhari badala ya kuishi kwa mikopo jambo linalopelekea wengine kukimbia huduma kwa aibu na wingi wa madeni, Wakati mwingine italazimu mama mchungaji afanye kazi zitakazoingiza kipato au hata mchungaji wakati anapoanza huduma anaweza aweza kufanya kazi za kumuingizia kipato ili kuitunza familia


UHUSIANO WA MCHUNGAJI NA JAMII



A; Uraia wa aina mbili.


    Ni ukweli unaokubalika kuwa injili sio tu inabadilisha tabia na kumuokoa mtu bali pia inabadilisha uhusiano wake yaani akiwa raia halali na mkazi wa ulimwengu hatawaliwi tu na sheria za ulimwengu huu, lakini ana uraia mpya na anaishi sawa na sheria za nchi mpya za utawala wa Bwana Yesu Kristo



Uhusiano na Mungu


     Mchungaji ni mtumwa katika uhusiano wake na Mungu Mathayo 24; 45. Mungu ametuita ili tuwe wafanyakazi pamoja na Yeye 1Koritho 3;9,2Wakoritho 5;17,Galatia 6;15,Efeso 4;24 na kolosai 3;10 watumishi ni mawakili wa siri za Mungu Efeso 3;8-9  mtumishi anapaswa kuendelea kudumisha uhusiano wake na Mungu Yeye ametuamini na ametupa injili 1Koritho 2;4 watumishi ni makuhani kwa ajili ya watu wa Mungu 1Petro 2;9 na ni walinzi Ezekiel 3;17;18.



Uhusiano na Bwana Yesu.


      Mchungaji anapaswa kuwa na uhusiano wa kudumu chini ya Yesu ambaye ni Mchungaji mkuu 1Petro 5;2-4,Matendo 20;28. Kondoo ni mali ya Yesu hivyo ni wajibu wa Mchungaji kuwalisha kuwatunza na kuhakikisha anazalisha Warumi 6;1-23, Kolosai 3;1-25. ni Lazima tufanye kazi hii kama Kristo atakavyo na kuiga mfano  wake tukitafuta kufanya mapenzi yake siku zote za huduma.



Uhusiano na kanisa lako


     Mchungaji ni mwangalizi wa mioyo ya wakristo Waebrania 13;17 hatuna budi kulipenda kanisa na kulilinda na mbwa mwitu na kuwasaidia woote wanaojikwaa na kuanguka Ezekiel 34;4, hakikisha kuwa unahusika vema na maisha na matatizo ya watu uliopewa kuwachunga fanyika msaada mkubwa kwao wafundishe, wahurumie, furahia maendeleo yao walinde ishi nao kama ndugu, Baba, kaka n.k  aidha mchungaji kanisani wewe ni kiongozi waongoze watu uwe na utawala bora watu hawawezi kufanya mambo bila kuongozwa mfano mwema ukiwa ni uongozi katika familia yako 1Timotheo 3;4-5 ongoza wewe ukiwa ndiye mfano mwema Wafilipi 3;17, 1Timotheo1;16 Ishi vizuri na wazee wako wa kanisa kwa upendo na urafiki.



B; Uhusiano wako na madhehebu mengine


     Katika hali isiyo ya kawaida udhehebu ni jambo linalochukua mioyo ya wengi hata kufikia hatua ya wengine kujifikiri kuwa huenda wao ndio bora zaidi kuliko wengine, Mapema sana katika huduma ya maisha ya Kristo mtu mwengine asiyeambatana na wanafunzi wa Yesu lakini huenda aliwahi kuhudhuria baadhi ya mikutano ya mafundisho ya Yesu alikuwa akifanyia kazi kile alichofundisha na kutoa pepo kwa jina la Yesu na wanafunzi wa Yesu walitaka mtu huyo azuiliwe Marko 9; 39-40. ni muhimu kufahamu kuwa yako madhehebu na vikundi ambavyo vyaweza kuwa tofauti na ulivyo vizoea lakini wako kazini na wanaifanya kazi ya Mungu vilevile.



Umuhimu wa kuheshimu utendaji katika mwili wa Kristo


     Moja ya baraka kubwa ya kuwa katika mwili wa Kristo ni kutambua kuwa utendaji wa Mwili wa Kristo ni mpana sana zaidi ya kanisa lako la mahali pamoja ni lazima ujue kuwa madhehebu na mashirika mbalimbali yanayohubiri injili ni mwili wa Kristo ni viungo vinavyofanya kazi mbalimbali katika mwili wa Kristo yaani kanisa (1Koritho 12;13) hivyo kuna umuhimu wa kutambua kuwa wengine wako pamoja nasi badala ya kugombana nao na kijifikiri kuwa ninyi ndo wenyewe au ndo bora kuliko wengine hii sio tabia ya Kristo. Yeye alituombea tuwe na umoja (Yohana 17;11,21-23.).



Mambo ya kuzingatia


     Pamoja na kuwa mwili wa Kristo ni mmoja tunapaswa kuwa na tahadhari dhidi ya imani potofu hivyo tunashirikiana bila kushiriki katika imani zilizo tofauti na tunavyoiamini Biblia kwa mfano

  • Chunguza kama kuna mafundisho yasiyoendana na biblia ili ujue wanaamini nini na wanapelekaje injili.
  • Chunguza namna wanavyotumia fedha au mapangilio wa mapato na matumizi ya fedha
  • Angalia mpango wao katika ushauri, maombi na namna wanavyofuatilia washirika au wanavyowapata.
  • Kama humjui kiongozi wa kundi hilo jaribu kutafuta taarifa kwa viongozi wako au wachungaji wengine siku zote watu wazuri huweka wazi mipango yao ya injili bila kificho
  • Unapogundua kuwa ziko tofauti na zinatokana na ufahamu tu kutoka katika maandiko au tamaduni zisizo na athari kubwa sana katika ukristo usisite kuwaheshimu wengine hatuhitaji sana kufanana katika kila kitu jambo la msingi si namna mtu anavyoabudu bali nani tunamwabudu, Mchungaji aliyekomaa hilo jaliwezi kumsumbua.



Kuibuka Kwa Madhehebu Kama Uyoga 


     Kuibuka kwa madhehebu ni jambo la kawaida ambalo watu watalishuhudia kaatika nyakati za leo, Madhehebu ni vikundi vya kidini  vilivyoungana au vinavyojenga kundi moja lenye uongozi,mapokeo,mafundisho,uzoefu na mikazo Fulani ingawa madhehebu hayo hayawezi kudai kuwa wao ni kanisa pekee la kweli  lakini wanaweza kufikiri kuwa wao pekee ndio wanawasiliswha ile kweli vizuri madhehebu mingine yana misimamo mikali na mengine misimamo ya wastani baadhi ya wakristo wanachukizwa na madhehebu titiri lakini wengine wako tayari kuyafia madhehebu yao, Nini sababu ya kuweko kwa utitiri huu wa madhehebu ziko sababu kadhaa

  • Madhehebu mengi yalitokea wakati mwingine kwa sababu ya Kulinda usafi wa kimafundisho hii hutokana na pale inapoonekana kuwa uchafu unaruhusiwa katika kanisa tofauti na msingi uliokusudiwa ndipo baadhi ya watu wanaotaka kulinda usafi wa mafundisho hutoka na kuanzisha dhehebu jipya hawa wako sawa na Yuda 1;3.
  • Sababu za kimaongozi  haya ni madhehebu yanayotokana na maongozi zaidi kuliko mafundisho Labda yuko kiongozi anayependwa na baadhi ya watu na inaonekana baadhi hawamkubali katika hitilafu Fulani wale wanaoonekana kuonewa huweza kuamua kutoka na kiongozi wampendaye kwa hiyo hawa hawatofautiani kimafundisho bali mfumo wa maongozi
  • Uonevu kutokana na shida za kimaonevu katika makanisa mengi wakati mwingine mtu anaweza kutoka na kuanzisha huduma yake huyu naye anaweza kuwa na mafundisho kama yaleyale ya awali. Tunaweza kushirikiana na wote wenye sababu kama hizi mbili za chini kwa vile utunzaji wa mafundisho wawezakuwa msingi wa kutoka kwao. 

 Unyenyekevu katika Dhehebu lako
 
     Hakuna dhehebu linaloweza kudai kuwa ndilo pekee linaloshikilia kweli yote pekee na kwamba ndilo dhehebu kamili lisilo na mapungufu kwa msingi huo basi unaweza kujinyenyekeza katika dhehebu lako kwa kuzingatia mambo ya msingi yafuatayo


  • Mshukuru Mungu aliyeruhusu uwepo hapo ulipo na kujifunza kumjua yeye kwa sehemu
  • Shughulika na programu zote zinazokusudiwa katika kanisa lako ikiwemo katiba.
  • Jilinde wewe mwenyewe na mafundisho yako wewe mwenyewe (1Timotheo 4;16) pia Linda wale ambao Mungu amekuweka uwachunge kwani utatoa hesabu kwaajili ya hao.



C; Maswala ya huduma


   Watumishi wengi wa mungu husongwa na mambo makuu mawili mahitaji ya shughuli za kukamilisha na muda wa kukamilisha shughuli zilizoko mbele yao matokeo yake wanajikuta wanchoka huku wakiwa hawajafanikisha wanayo yataka na inaonekana kama kwambo muda wao hautoshi.



Unahitaji kupumzika


   Watumishi wengi wanakuwa wanasongwa  na hatia hasa pale wanapojikuta wanahudumia sana watu  na kazi za kanisa na haimaye hujikuta wameshindwa kutimiza maswala yao binafsi na mahitaji ya familia yake hii ina maana kuwa wakati mwingine wanajisikia hatia kusema hapana kwa kazi ya Mungu na watu na kuwa nahitaji muda na familia yangu ,Neno hili wao huliona kuwa ni dhambi lakini kutokuwahudumia wa nyumbani mwako ni dhambi zaid Mchungaji unahitaji kupumzika na ili kutatua tatizo hili unahitaji ratiba isiyovunjika vunjika huko mbale tutajadili kuhusu ratiba lakini ni muhimu kuwa na wakati na familia yako na unahitaji mapumziko



Unahitaji kuwa mkarimu.


     1Timotheo 3;2 huduma ya ukaribishaji wageni (ukarimu) na kuwahudumia kimsingi linawahusu wachungaji bahati mbaya katika siku za leo wachungaji wanafikiri kuwa wao ndio hupaswa kuhudumiwa badala ya kyhudumia watu Biblia moja ya kiingereza inafafanua hivi “He must enjoy having guests in his home”  inawezekana ikawa ngumu kwa sababu ya kipato ulichonacho lakini si lazima iwe chakula cha gharama unaweza kuwakaribisha hata kwa chai tu, na unapokuwa ni wakati unahitaji mapumziko ni lazima watu wajue kuwa unapumzika ili wasifikiri unapatikana.


MAADILI YA KICHUNGAJI



A; Maisha binafsi ya kichungaji. Afya.


     Tumeona kuwa watumishi wa Mungu wanakosa hata muda wa kupumzika ni watu wenye shughuli nyingi sana ,wachungaji ambao saa zote wako na shughuli nyingi kiasi hiki  wanahitaji kuwa na Afya nzuri kwani afya yako ya mwili inauhusiano na Afya yako ya kiakili na kiroho kwa msingi huu kumbuka kuwa mwili wako ni hekalu la Roho Mtakatifu (1Koritho 6;15-20) kwa msingi huo lazima ukumbuke kuwa Mwili wako si wako mwenyewe na mwili huu ni zawadi kutoka kwa Mungu kwa msingi huo kama mchungaji hatakuwa na Afya nzuri atawezaje kubeba mzigo huu wa kazi kubwa ya mungu iliyoko mbeleni kwa msingi huo yako mambo ya msingi unayopaswa kuyazingatia ili uwe na afya nzuri kumbuka kuwa “A pastor should be phyisicaly fit”



Mchungaji lazima awe na Afya nzuri..


  • Uwe na muda wa kutosha kupumzika na kustarehe kila mchungaji ana kazi ngumu na majukumu mazito kwa msingi huo unapaswa kuwa na muda wa mapumziko Yesu alimaanisha kitu aliposema kuwa Sabato ilifanyika kwa ajili ya mwanadamu Marko 2;27 miili yetu imeumbwa katika namna ambayo inaweza kujijenga yenyewe ikipumzishwa vya kutosha. Kama Mungu mwenyewe alionyesha mfano wa kupumzika kwanini wewe usipumzike Kutoka 20;9-11. Yesu mwenyewe kwa kufahamu umuhimu wa kupumzika wakati Fulani aliwaambia wanafunzi wake wawe peke yao ili wapate kupumzika ( Marko 6;31)
  • Uwe na safari pamoja na familia yako mbali na nyumbani mpate Muda wa mapumziko huko  mapumziko yaweza kuchukua hata muda wa wiki moja au muwe na likizo wachungaji wengi hasa sisi wa Afrika hatuna likizo tunafanya kazi milele hii sio sifa bali ni kwa ujinga wako
  • Uwe na tabia ya kula vizuri kula vizuri hakuitaji wewe uwe tajiri  hiki ni chakula bora chenye makundi yoote muhimu ya chakula yanayojenga mwili na si kula sana kunakotakiwa bali kula kwa nidhamu wachungaji wengi huona kuwa kula ni kama kupoteza muda hivi hivyo hujali kazi zaidi.
  • Fanya mazoezi mazoezi sio dhambi kunawatu huokoka kupita kiasi hata wandhani kuwa kuchukua mazoezi ni dhambi hii sio sawa mchungaji chukua mazoezi cheza mpira ,kimbia n.k

Maisha binafsi ya kichungaji Kuvaa vizuri


     Mchungaji lazima utoke vizuri uwe na tabia ya kuvaa vizuri na kwa usafi smatness hili ni swala la msingi sana hakikisha kuwa unapiga mswaki vizuri,pakaa mafuta mazuri chana vizuri pafyumu nzuri,jitibu maralia na minyoo na funga kwa mpango maalum si kwa namna itakayoharibu afya


Maisha binafsi ya kichungaji Tabia yako 


     Mchungaji hushughulika na watu karibu muda woote na kwa kawaida kila jamii ina viwango vyake vya maadili tafadhali ishi sawa na viwango hivyo vinavyokusudiwa tabia yako njema itawavutia watu na kuleta ushuhuda mzuri katika jamii



B; MAISHA YA KICHUNGAJI KATIKA JAMII


Maisha binafsi ya kichungaji uhusiano wako na wachungaji wengine.


     Mchungaji unapaswa kuwa na uhusiano mzuri pia na wachungaji wengine au wachungaji wenzako, wakati mwingine Bwana ataruhusu mchungaji kuhama kutoka eneo moja kwenda eneo lingine na hivyo kuruhusu mchungaji mwingine kuchukua nafasi yake, hili linapotokea  nyakati nyingine limekuwa chanzo kikubwa cha kuweko mahusiano yasiyo mazuri,  kanisa ni mali ya Yesu Kristo kwa msingi huo unapolijenga lazima ulijenge katika msingi wa watu hao kuwa tayari kupokea watu wengine



Wajibu wako kama unahama


  • Mzungumzie vizuri mchungaji anayekuja nyuma yako
  • Kabidhi kanisa katika hali nzuri na moyo mweupe
  • Mshirikishe maono na mipango ya mbele ya kanisa husika
  • Tumia hekima na uangalifu unapoalikwa katika kanisa lako la zamani
  • Uwe makini unapotembelea au kuwasiliana na washirika wako wa zamani ili kuzuia kutokueleweka.
Wajibu wako kama unahamia
 
  • Tambua mchango mkubwa wa mchungaji aliyekutangulia wako watu wengine huponda kabisa mambo yaliyofanywa na wengine waliowatangulia kana kwamba hawajafanya kitu chochote kabisa
  • Tambua kuwa kila mtu ameumbwa kwa namna tofauti hivyo yule hawezi kuwa wewe wala wewe huwezi kuwa yule kumbuka kuwa kwa muda watu watakulinganisha na mchungaji wao wa kwanza usijali unachotakiwa ni kuongeza bidii katika maeneo yenye upungufu lakini usiigize kwani kila mtu ameumbwa tofauti
  • Fanya mabadiliko kwa hekima pale inapobidi kufanya mabadiliko fulani hakikisha unatumia hekima na kuwaelewesha watu kwanini unafanya hayo unayoyafanya  usifikiri kuwa kwakuwa yale yalifanywa na mtu mwengine basi ni mabaya 
Uchungaji kama taaluma yako.


     Uchungaji pia ni taaluma ukiacha ya kuwa kuna wito, kama taaluma ni lazima ujue kuwa wewe ni wakili wa Mungu unamwakilisha Mungu hivyo lazima uishi  sawa na viwango ambavyo Mungu anavikusudia ili kuwakilisha ufalme wake, Lazima uiheshimu kazi yako kama mtu mwenye taaluma ya kazi hiyo kwa bahati mbaya hakuna mtu atakayekusimamia nini cha kufanya katika kazi yako ya uchungaji hivyo ni wewe ndiye mwenye wajibu wa kujisimamia lazima ujisimamie na kujiuliza je mambo haya yanakwenda sawasawa

  • Jiulize je unakuwa na wakati wa kujisomea? Wengine huzurula mjini tu
  • Je unachukua muda wakutosha kujiandaa kwa jumbe mbalimbali?
  • Je nina ratiba maalumu ya kujiendeleza mwenyewe kiroho?
  • Je naweza kujifanyia tathimini mwenyewe kuwa sio muaminifu katika kazi hii?
  • Je naweza kujitathimini kwamba ninajitahidi kuendeleza huduma ambayo Mungu amenipa? Lazima mchungaji uonyeshe bidii katika maswala mbalimbali ya kihuduma ili ijulikane pia kuwa kazi hii pia ni taaluma yako na umeisomea na unaithamini.ili kujiwekea mipaka fanya pia mambo yafuatayo
    • Uwe na bidii katika kutimiza majukumu ya kazi zako.
    • Fika kwa wakati katika kila eneo unalopaswa kufanya hivyo

Mchungaji kama mwenyeji.


     Kuna wakati ambapo labda mtaalika mchungaji mgeni kwa kusudi la semina, mkutano au jambo lingine lolote hii ni muhimu kwa kuwa kanisa halijengwi na mtu mmoja tu hivyo si vibaya kualika wengine kwa ajili ya kujaziliza maeneo ambayo labda hujayafikia semina zisitumike kama gea ya wewe kupumzika kwa uvivu wa kuandaa masomo na kufundisha msingi wa kualika mgeni uwe ni baraka na mpango wa kufikia maeneo ambayo wengine wamepakwa mafuta kuyafikia kama Mungu anavyokusudia japokuwa unapomwalika mgeni ni muhimu kuzingatia yafuatayo

  • Mwelekeze namna ya kufika mahali ulipo na kanisa lilipo
  • Mpe eneo analopaswa kufikia na endapo atahitaji utulivu basi eneo hilo liwe hivyo
  • Mpe muda wa yeye kujua kuwa atapaswa kuoga,kujisomea na muda wa kula
  • Mwelezee muda wako wa ibada namna mnavyoendesha ibada zenu na kama kuna namna anavyotaka kuendesha ibada iliyo tofauti
  • Mweleze kuwa ibada inatakiwa iwe ndefu kiasi gani wengine huimba mpaka wanasahau muda wa mahubiri au kumbana muhubiri asiwe na mda wa kutosha
  • Unapokuwa mgeni nawe ni muhimu kuchukua tahadhari zenye kupunguza usumbufu viko vitu ambavyo kama utaviacha vinaweza kuleta usumbufu kwa mfano Taulo,mswaki n.k. na pia jihadhari na tabia ya kujichagulia vyakula na kupenda starehe au matazanio ya juu kifedha

HUDUMA YA KICHUNGAJI



A; Mchungaji na Mahubiri yake


     Kuhubiri ni moja ya majukumu ya msingi ya kichungaji na ni swala la lazima linalokamilisha huduma ya kichungaji (1Koritho 9;16) watu huokolewa kupitia mahubiri 1Koritho 1;21

     Kuhubiri maana yake ni nini kwa kilatini kuhubiri ni kutangaza hadharani lakini maandiko yanapo zungumzia kuhubiri humaanisha nini? Neno kutangaza limetajwa mara 61, na kutangaza habari njema limetajwa mara 50, na kufundisha limetajwa mara 90, kuhubiri kwa kibiblia ni kuzungumza habari zisizo za kwako, kwa asili habari zinazohubiriwa chanzo chake ni Mungu Biblia inaonya kuwa yeyote aliyesema kuwa Mungu amesema huku hakutumwa Mungu hakuwaheshimu watu hao Yeremia 14;14. hivyo mkazo katika Biblia unaohusu kuhubiri unahusu kile Mungu anachotaka kisemwe ndio maana Neno ”Asema Bwana lilikuwa maarufu ” hii ilikuwa inaonyesha ni kwa mamlaka gani mzungumzaji anazungumza si kwa sababu tu yeye ni mjumbe kwa hivyo tunaweza kusema kuhubiri kunahusisha ujumbe kutoka kwa Mungu.



Mjumbe.

      Ukweli kuwa kuhubiri kunahusisha ujumbe kutoka kwa Mungu ina maana kuwa mnenaji ni njia tu ya kupitisha ujumbe wa Mungu kwa watu wake vinginevyo ujumbe ungefikaje? Mungu ndiye lilikuwa somo kuu na manabii walikuwa ni wajumbe tu na hivyo si wao waliokuwa wakiupa ujumbe mamlaka bali Mungu hivyo watu walilipokea neno la manabii kama neno la Mungu 1Thesalonike 2;13. 

                                    

Kwa msingi huo ujumbe unahusiaha sehemu kuu tatu Mungu mtoaji wa somo,Mjumbe mpitishaji na watu wapokeaji wa somo husika  hivyo basi mahubiri huuhusisha maeneo makuu matatu na sio kujisemea tu.



Kwanini tuhubiri?


     Warumi 10;13-15 ni andiko ambalo linajibu wazi kwanini tuhubiri hii inaonyesha wazi kuwa mahubiri yana sababu  tangu mwanadamu amefarakana na Mungu kwa sababu ya dhambi anahitaji kupatanishwa na Mungu Injili ya Yesu Kristo  ni habari njema kutoka kwa Mungu kuwa mwanadamu anaweza kupatanishwa tena na Mungu kupitia kazi ya Kristo pale msalabani  na wakaokolewa (Rumi 1;16,10;14) Neno linapohubiriwa wenye dhambi husikia wanaamini wanaokolewa wanamkiri Yesu kuwa Bwana na mwokozi na kuokolewa hivyo mahubiri ni njia ya watu kuokolewa, Ni kuwawekea wazi kilichofichika,ni kuleta changamoto inayohitaji mwitikio,ni kuleta Habari maalumu sana.



Namna ya kuupeleka ujumbe


     Mungu anapokuwa amemuita mchungaji kama mtoa ujumbe ni muhimu kufahamu kuwa mtu huyo sasa anakuwa kati ya Mungu na wanadamu, Kwa msingi huo huwezi kusema unajiandaa bila kugusanishwa na pande zote mbili  na kwakuwa wewe umeitwa na Mungu unahitaji kumwangalia Yeye kwanza kwa ajili ya maandalizi.



Maandalizi ya ujumla


§  Tunza hali endelevu ya Kiroho na maisha yako kwa maana ya uhusiano wako na Yeye

§  Hakikisha kuwa unatunza jumbe zako au shamba lako la jumbe hii inamaanisha mambo unayojisomea n.k unayoyasikia kutoka katika jumbe za wengine ambayo baadaye yaweza kukufanya uweze kutengeneza jumbe zinapo hitajika Endeleza tabia ya kujaza mambo yawezayo kukusaidia katika kuapta jumbe.



Fanya maandalizi maalumu

                                                  

Ujumbe kutoka kwa Mungu




Maandalizi maalumu

         Tengeneza



        Wasilisha



     Kufanya maandalizi maalumu namna ya kupata ujumbe wa kuhubiri lazima Mchungaji aulize au aombe kutoka kwa Bwana, Mungu atatupa wazo kutoka katika neno lake kisha ingia katika maandalizi, fanya matengenezo ya jumbe kisha tumia ujumbe katika mazingira husika tunasikitika kuwa hatutaki kuingia ndani sana katika swala zima la somo la kutunga hutuba ambalo hushughulika na swala hilo hapa tunagusia kwa ufupi tu ili kukumbusha au kukupa mwanga.

  • Maaandalizi maalumu huanza na kupatikana kwa ujumbe.
  • Maandalizi maalumu hufuatiwa na kutafasiri biblia kwa usahihi hili hujumuisha
    1. Historia ya andiko
    2. Lugha iliyotumika
    3. Ushahidi kutoka katika maandiko mengine
    4. Maana ya kitheolojia ya andiko.

  • Baada ya hayo angalia uhalisi wa maisha ya watu husika
  • Tafuta taarifa zaidi katika shamba lako la jumbe au maktaba yako
  • Pangilia ujumbe wako kama kanuni za hotuba zinavyotaka. 
 Namna ya kuwasilisha ujumbe
 
  • Kusudi na kile kinachobebwa katika ujumbe kinawakilisha na kuamua ujumbe upelekwe vipi na hayo yatatambulisha kuwa Mungu anataka nini yaani kama ni ujumbe wa upendo sauti na muonekano wako utaashiria upendo siku hiyo
  • Angalia watu wako walivyo  na kiwango chao cha ufahamu na kiroho huku ukikumbuka kuwa wako wanaotaka kutambuliwa,wako waliovunjika moyo wako wenye majaribu ya aina mbalimbalio hivyo peleka ujumbe wako kwa hekima usiwaongezee watu matatizo bali utatue matatizo
  • Tumia sauti yako kwa makini yaani kulingana na kundi la watu usipaze sauti sana kama kuna watu 20 tu matumizi yako ya sauti ni lazima yaendane sawa na kundi lilioko
  • Hakikisha unavaa vizuri kwa namna ambayo itasaidia watu kupokea kile unachokikusudia
  • Unapotumia notes si vizuri kuzisoma unaweza kufanya hivyo mwanzoni lakini haitafurahisha kuendelea kuzisoma, kumbuka mwili wako nao uanzungumza.
  • Usiogope swala la hofu ni la kawaida na baada ya muda Roho wa Mungu atakusaidia 
Hitaji la Jumbe tofauti tofauti


   Watu wanahitaji jumbe tofauti tofauti kwa hivyo ni muhimu ukawasilisha jumbe si katika namna ileile ya siku zote jaribu kutumia jumbe tofautitofauti kuna aina nyingi sana za jumbe lakini zilizo kuu zinazojulikana sana ni tatu tu Ujumbe wa somo topical ujumbe wa andiko textual na ujumbe wa uchambuzi wa kifungu cha maandiko Expository.



Pangilia jumbe zako


   Kama mchungaji anahubiri mara tatu kwa wiki maana yake ni kuwa kwa mwaka utahubiri mara 156 hizi ni jumbe nyingi sana  na kama utahubiri kutoka katika eneo moja tu kwa mfano jumbe 156 za maswala ya unabii tu litakuwa swala gumu sana hivyo ni lazima uwe na mpangilio utakao ruhusu kutoa mlo kamili wa kibiblia kwa watu wako huku ukizingatia mahitaji yao lakini itakupasa kuhubiri kutoka katika nyanja  mbalimbali za kibiblia.ili kuwafikia watu  katika namna mbalimbali zingatia mambo yafuatayo

§  Angalia mahitaji ya watu wako

§  Tumia kalenda ya Kikristo

§  Tafuta namna ya kuwainua kiroho

§  Fundisha mafundisho ya biblia na watu maarufu katika Biblia biographical Sermons



B: Mchungaji na mafundisho yake

Mchungaji au muhubiri pia ni mwalimu ujumbe wa mahubiri unapohubiriwa pia unakuwa na mafundisho,Kristo alifanya kazi zote mbili alihubiri na kufundisha Mathayo 4;23 kuhubiri kunahusisha kushawishi, kuchochea, kutaka kutangaza, wakati kufundisha kunalenga kumpa mtu maarifa kuelimisha wataalaamu wanaamini kuwa kanisa linakuwa vizuri kiroho likiwa na mafundisho hata hivyo ni muhimu kufahamu pia kuwa wakati mwingine katika kufundisha kuna kuhubiri na katika kuhubiri kuna kufundisha vitu hivi huingiliana japo ni vitu viwili tofauti na kufundisha kunalenga

§  Kuleta matunda ya ufahamu

§  Kupandikiza tabia iliyo nzuri

§  Kupandisha juu viwango vya kikristo na utumishi alioitiwa kila mtu

Kufundisha kumeagizwa katika agizo kuu Mathayo 28;19-20 na kilichoagizwa kufundishwa ni neno la Mungu yoote niliyowaamuru, Kufundisha kuliagizwa kwa mataifa yoote, Mchungaji fundisha kwa mamlaka Yesu alifundisha kwa mamlaka Mathayo 4;24,5;1. Marko 1;22, Kufundisha ilikuwa ni sehemu muhimu ya lazima ya maisha yake na huduma Marko 10;1, kufundisha ilikuwa ni sehemu ya nyakati za kanisa la kwanza neno kufundisha  kwa kiyunani ni Didasko kufundisha ambayo ilikuwa ni sifa ya mtu aliyetakiwa kuwa kiongozi katika kanisa 1Timotheo 3;2. Lazima uwe na mbinu mbalimbali za ufundishaji somo la principal of teachings litashughulikia hilo, Fundisha ukiwa unachunguza nini kinaendelea, Fundisha kwa kufunua kweli zilizofichika Exposition na wakati mwingine ni vema ukitoa nakala za somo unalofundisha hii inasasidia kanisa kukua kwa haraka.



C: Mchungaji na huduma ya kichungaji

     Kazi ya mchungaji kwa lugha ya kiyunani ni Poimen ambalo neno hili kwa asili ni kulinda au kuchunga  neno hili kuchunga limetumika mara kumi na nane  katika Agano jipya tukielewa kazi zilizokuwa zikifanywa na wachungaji wa mifugo wa kawaida kama kondoo, ng’ombe n.k. tutaweza kuifahamu vizuri sana kazi ya kichgungaji



Mfano wa  Yesu Kristo kama mchungaji mwema

    Karibu mara saba katika injili waandishi wanatumia neno mchungaji kumhusu Yesu, na pia Kristo ametajwa kama mchungaji mkuu Waebrania 13;20 na Petro 2;25 na ingawaje injili  inavyomwelezea Yesu moja kwa moja kama mchungaji Mwema ni Yohana 10;11-14 Yesu anatoa mtazamo mzima wa kuwa yeye ni mchungaji mwema na hii ilikuwa ni kutimiza mtazamo mzima wa agano la kale kumhusu Yehova kama Mchungaji mwema Zaburi 23;1.Yeye anaonyesha mtazamo tofauti na viongozi wengine wachungaji ambao walikuwa waovu mioyoni mwao badala ya kuondoa uhai wa kondoo mchungaji mwema anautoa uhai wake kwa ajili ya kondoo hii inaonyesha jinsi kazi ya kichungaji inavyopaswa kuwa badala ya  kufaidika Mchungaji anajali na kujihusisha na kondoo kufikia viwango vya kujitoa uhai wake kwa maslahi ya kondoo hata ingawa walimkataa lakini  alikuja kwa ajili yao aliwahurumia aliugua kwa ajili yao na hasa pale alipoona wametawanyika kama kondoo wasio na mchungaji Luka 13;34, Mathayo 6;36. kuwahurumia katika lugha ya asili ni kuugua kwa huzuni kubwa kiasi cha kufikia hatua ya kuumwa Luka 15;4-6 inaonyesha zaidi jinsi mchungaji anavyoguswa hata na kondoo waliopotea ambapo mchungaji huyo hujihusisha sio tu na kuchunga lakini pia na kutafuta waliopotea na sio kutafuta tu hutafuta mpaka ampate ni watumishi wangapi leo wanafanya hiki ambacho Biblia inasema?



Mfano wa Paulo Mtume kama mchungaji

     Moja ya vifungu maarufu sana vinavyoizungumzia vema kazi ya kichungaji ni  Matendo 20;18-31 hapa tunaona mfano wa huduma ya kichungaji miaka mitatu Paulo mtume aliitumia pale Efeso kama mchungaji wa kondoo huku akitumika kama mtumwa mst 19, hata alipokuwa akiondoka alitilia maanani usalama wa kondoo kama mchungaji kiongozi wa kanisa akitamani uangalifu mkubwa wa kondoo kuendelezwa mst 28.Daudi aliwachunga kondoo wa baba yake na kuwa tayari kugharimika kupambana na dubu na simba mchungaji ana wajibu wa kuwalinda washirika kuhakikisha wanaukulia wokovu, kuwalinda na  mafundisho potofu na waalimu wa uongo, Mfano huu wa  Bwana Yesu na Paul unatufundisha jukumu kubwa la kichungaji kwa hivyo mafano wa wachungaji katika maandiko unaweka bayana  swala zima la shughuli za kichungaji kwamba kwa ujumla shughuli ya kichungaji ni kushughulika na mahitaji ya watu kuchunga kujali na kulinda bila ya upendeleo kwa gharama yoyote



Shughuli ya kichungaji hujumuisha ;-

*      Kuhubiri injili  1Koritho 1;21 Tito 1;3,Warumi 15;19,

*      Kufundisha Neno la Mungu 1Koritho 12; 28, Efeso 4; 8, 11.

*      Kusimamia Ibada kuhakikisha zinafanyika kwa Heshima na utaratibu 1Koritho 14;23,32,Efeso 5;18

*      Kulitunza kanisa kuhakikisha linajaa amani na upendo na umoja Yakobo 3;16 galatia 5;22.

*      Kuhakikisha wakristo wanakamilika Kiroho kufikia utakatifu Efeso 4;13,Kolosai 1;28 Mchungaji ni lazima uhakikishe watu hawapotei Yohana 17;12, hakikisha watu wanakua katika huduma na kutumia vipawa walivyopewa, Kukuza wale watakaosaidia katika shule za jumapili na maongozi  na kupandikiza moyo wa kupenda kuihubiri injili.

*      Mchungaji ni lazima ahakikishe kuwa anafanya maombezi kwa watu wenye shida mbalimbali, watu wana shida nyingi sana wanahitaji kuponywa Mathayo 9;35, Marko 16;17-18, Isaya 53;5

*      Hakikisha unakuwa na maono kwa ajili ya kanisa la Mungu Torati 2;3 kutoka 14;15 hakikisha unakua na hekima jinsi ya kutimiliza maono Epuka kuwatwika watu mizigo ya michango isiyo ya lazima hakikisha watu wanajitoa kwa hiyari kwa kadiri ya neema kama matokeo ya kujifunza na sio kulazimishwa Mungu huwabariki wanaotoa kwa moyo

*      Hakikisha unakua mvumilivu na unajifunza kumtegemea Mungu

*      Hakikisha kuwa unawatembelea washirika na wasio washirika katika mtaa wako au eneo uliuoko,hii ni njia ya kuwafikia kihuduma lakini hakikisha unakuwa na ratiba ya namna ya kufanya matembezi, gawa mji wako katika sehemu mbalimbali

*      Hakikisha unakua na huduma ya ukarimu katika nyumba yako kwa kukaribisha watu

*      Tembelea Hospitalini na magerezani lakini pia unaweza kuwashirikisha wengine katika huduma hii.



MCHUNGAJI NA HUDUMA YA USHAURI (COUNSELING)

     Tunaweza kusema kwa ukweli kuwa ushauri wa kichungaji ni huduma kamili kabisa ya kichungaji wakati mwingine tunaweza kusema kuwa huduma ya kichungaji haiwezi kuwa kamili bila ya kuweko kazi ya ushauri, Hata hivyo ushauri ni taaluma kamili na tunashauri mchungaji kujisomea zaidi kuhusu somo la ushauri wa kichungaji

      Ushauri kwa mtazamo wa Kikristo ni shughuli ya kukuza na kubadilisha mawazo wa muathirika kupitia ofisi ya mchungaji ambaye ndiye mshauri ambaye atatumia mbinu za kawaida na za kimungu kuhuisha kwa upya, kuponya, kukuza na kumfanya mtu kutua mzigo alionao na kuwa na uwezo wa kukabiliana na hali yoyote ngumu au iliyokuwa imeleta fadhaa uathirika hapo hau-husu tu maswala ya kimwili bali na kiroho pia

      Ziko aina nyingi za ushauri kama ushauri wa moja kwa moja na ushauri usio wa moja kwa moja ule wa moja kwa moja mchungaji na muathirika wataongea na kutafuta suluhu ya tatizo kwa siku moja au hata kwa siku kadhaa ule usio wa moja kwa moja Mchungaji huweza kutumia makundi katika kutatua tatizo la muhusika bila kundi hilo kuelewa kuwa wanatatua tatizo huku ukijumuisha mbinu nyingine zinazoweza kutumika.


 Viwango vya athari na maumivu wayapatayo watu LCU


Tukio
Kiwango LCU
Tukio
Kiwango LCU
Kufiwa & mpenzi
100%
MtotoShuleni
29%
Takaka
73%
Shida kisheria
29%
Watoto  wapweke
65%
Mke kuacha kazi
26%
Kufungwa
63%
Hali ya hewa tof
25%
Kufiwa na ndugu
63%
Kupitia tabia
24%
Kujiumiza
53%
Boss mkali
23%
Shughuli za ndoa
50%
Kubadili saa za k
20%
Kufokewa kazini
47%
Mabadiliko shule
20%
Ndoakupatanisha
45%
…”….kanisani
19%
Kujiuzulu
45%
…”…Kulala
19%
Afya mbaya
44%
…”…kula
15%
Mimba
40%
Likizo
15%
Ugumu ktk sex
39%
sikukuu
13%
Mtoto mpya
39%


Biashara mbaya
39%


kuchacha
38%


Kifo cha rafiki
37%


Kuhamishwa
36%









Mchungaji zingatia hayo hapo juu ni maumivu yanayowapata watu na viwango vya maumivu kwa asilimia zake hii ikupe changamoto namna ya kushughulika na watu wanaohitaji kuponywa majeraha hayo katika Kuwashauri waathirika wako

_____________    

Used by Permisiion of Holmes, T.H & Rahe, R.H.The Social readjustment rating Scale.Jounal of Psychosomatic Research II: 213-218, 1967.



Mchungaji kama kuhani au Mchungaji na huduma ya maombezi

        Karibu asilimia kubwa ya huduma ya kichungaji hufanyika hadharani.ingawaje inaweza kufanyika kwa ubora na kuleta matokeo yanayokusudiwa kama itafanyika sirini (Mathayo 6; 6) .hii haimaanishi kuwa huduma hiyo ya maombezi ni lazima ifanywe ndani tu lakini tunamaanisha swala la msingi inapofanyikia Luka 6;12. Mchungaji lazima awe muombezi kwa ajili ya watu katika eneo alioko



Mchungaji kama Kuhani

     Makuhani katika agano la kale walikuwa ni mawakili wa watu kwa Mungu na msemaji wa watu kwa Mungu na ilikuwa ni kupitia kuhani watu wangeweza kuwa karibu na Mungu au kupatanishwa na Mungu, Kupitia kifo cha Kristo kila mmoja leo anaweza kwenda moja kwa moja kwenye kiti cha rehema cha Mungu bila ya kuhitaji kuhani wa kibinadamu tangu pazia la hekalu lilipopasuka vipande viwili kutoka juu hata chini (Mathayo 27; 51) waamini wote wanaweza kukifikia kiti cha rehema cha Mungu kwa kuwa sasa wao ni makuhani na wafalme  (Ufunuo 1;6,1Petro 2;5,10).pamoja na hayo Biblia bado inatuagiza kuombeana sisi kwa sisi Yakobo 5; 16 na kuchukuliana mizigo Galatia 6;2.

      Kwa msingi huo basi mchungaji ana nafasi ya kipekee katika kuwafanyia watu maombi kwa kuwa anayajua mahitaji ya watu na yanawekwa wazi kwake kuliko kwa mtu mwingine awayeyote ni Mchungaji anayebeba waliojeruhiwa na mara nyingi ndiye anayebeba mzigo wa kanisa hususani pale linapoteseka Waebrania 4-5 imejaa mifano mizuri ya kazi za kikuhani jambo linalotoa picha ya kiazi ya kichungaji hivyo mchungaji kama kuhani anapaswa;-

§  Kuwa mwepesi kujua mahitaji ya watu

§  Kuwa na moyo wa huruma kwa ajili yao wanaorudi nyuma au kuanguka dhambini lazima uwajulishe kuwa kuna neema na rehama  wakati wa uhitaji Waebrania 4;16, wakati mtu anapoanguka sio wakati wa kuanza kumshutumu na kumlaumu na kutangaza madhabahuni kwani neno la Mungu linatosha kwa kwa kuonya na kufundisha  2Timotheo 3;16-17 hivyo litumike kwa upendo katika kutatua tatizo kwa huruma na rehema itakayo mwezesha muathirika kupokea msamaha

§  Onyesha kuhusika na maisha ya kila mtu,Hakuna ukuhani bila watu wala huwezi kumtenga kuhani na watu,Maandiko yanatuambia kuwa Yesu alijaribiwa katika mambo yote bila kufanya dhambi ,Kujua mambo ambayo watu wanapitia kunaweza kukusaidia wanapitia nini hivyo kuwafikia na kuwasaidia kwa kua unaelewa na unafahamu  hivyo maombi  na yawe silaha yako katika namna ya kuwahudumia.



Mchungaji na maswala ya kutia nidhamu

      Moja ya maswala magumu sana na yanayohitaji uangalifu mkubwa kwa mchungaji na viongozi wake wa kanisa ni  maswala ya kutia nidhamu.Hakuna mtu anayependa kutiwa nidhamu au anayekubali nidhamu na kwakweli wachungaji wengi hawapendi hata kuizungumzia nidhamu na kwa kweli biblia inapozungumzia nidhamu ina maana pana zaidi ya adhabu ambayo watumishi wengi hufikiria.



Nidhamu ni nini?

     Neno nidhamu linajumuisha maeneo makuu mawili Kufundisha na kusahihisha, Kufundisha ina maana ya kutoa mafunzo,kumkamilisha mtu, kitaaluma au kimaadili na kusahihisha maana yake ni kudhibiti au kurudisha katika utaratibu, siku zote kutia nidhamu au kusahihisha mtu lazima kuendane na kumpenda mtu yule unayempa nidhamu kama afanyavyo baba wa kawaida wa kidunia kwa wanawe.



Kusudi la kutia nidhamu

     Lengo kuu la kutia nidhamu ni kurejesha na sio adhabu au kukomoa.  (Waebrania 12; 10-11) Ni muhimu nidhamu itolewayo na kanisa iwe na lengo la kurejesha na sio kukomoa, ni kuhakikisha mtu anarudi katka uhusiano mzuri na Kristo na kanisa na sio kummbomoa mtu, ni kuhakikisha mtu anakuwa na tabia za kikristo na anaendelea katika kiasi, Watumishi wengi wa Mungu wamepoteza wengi katika eneo hili kwa kuwaharibu watu kabisa badala ya kuwaponya wametumia nafasi ya mtu kukosea kama sehemu ya kukomoa watu na kuhukumu kuliko hata Mungu alivyokusudia to hell! Hivi miili yetu inapougua si tunaitibu? Na hata kama kiungo kunachoumwa ni kimoja tunafanya hivyo kwa kuwa mwili woote unaugua si ndio? Na hata kama inahitaji operation kwa kweli mwili woote utaugua lakini kwa bahati mbaya wengi tumewapoteza kwa sababu za kipuuzi tu.

      Nidhamu inayohitaji operation ni zile zinzoonyesha kuwa Mtu huyo analeta mafundisho potofu Warumi 16;17;1Timotheo 6;3-5 au anaishi maisha ya uchafu Marko 7;20-22,1Koritho 5 na akitubu hurejezwa 2Koritho 2;5-11 na Mtu asiyetaka kutubu au mwenye kiburi Mathayo 18;17.



Kanuni za kumtia mtu nidhamu

  • Nidhamu lazima iendane na kanuni na sheria za kanisa husika wako wachungaji ambao hutoa adhabu kinyume hata na katiba au hata maongozi ya kanisa husika wakivunja hata katiba zao
  • Usimuhukumu mtu ndugu kaka au dada bila kumpa nafasi ya kujieleza na unapomtia nidhamu lazima ajue asili ya kosa lake na adhabu anayoistahili Mathayo 18;15-17
  • Adhabu lazima iwe ya kibiblia  ambayo mara nyingi lengo lake ni kumleta muathirika katika toba na sio vinginevyo
  • Inapokuwa hadharani ni kwa ajili ya kuonyesha toba aliyo nayo mtu kwa kanisa na kasha unamrejesha lakini wengine hufanya hivyo kwa kusudi la kudhalilisha na kumuaibisha mtu
  • Mtu aliyetubu lazima arejeshwe kwa ukamilifu katika ushirika (Yohana 21;15-19) Yesu hakumuuliza Petro ilikuwaje ukarudi nyuma bali alimuuliza swali kuhusi upendo wake kwake na kujikabidhi kwake  fahamu ya kuwa hesabu ya kila mshirika utaitoa siku ile endapo utakuwa umempoteza kwa uzembe.



C: Mchungaji na huduma maalum

     Huduma maalumu ni ibada za kichungaji za kidini ambazo huusihsa maswala ya ubatizo, Harusi, Mazishi na meza ya bwana, pia ziko ibada za uanachama, ibada za kuweka wakfu majengo na kuweka wakfu watoto n. Ibada hizi hutegemeana na kanisa husika namna na jinsi wanavyotakiwa kuziendesha hapa tutagusia kwa ufupi tu lakini ni jukumu la kila mtumishi kujifunza kuendesha ibada hizo kulingana na kanisa lake na tamaduni zao ingawa mara nyingi sana ibada hizi hufanana.



Ibada ya ndoa.

  • Zingatia matakwa yote ya serikali yahusuyo ndoa
  • Hakikisha kuwa wanandoa ni watu huru na sio waliolewa au kuoa mara ya kwanza na wenzi wao wako hai
  • Hakikisha kuwa ni wazima wa afya na wamekubaliana na kuaminiana
  • Endesha ibada sawa na kanuni za kanisa lako
  • Epuka kuwa na mahubiri marefu na yenye kuchoisha siku ya ndoa uwe na mafundisho ya kutosha na wanandoa kkabla ya siku ya harusi yao .



Ibada ya Mazishi.

  • Uwe na uzoefu wa mila na desturi za eneo husika
  • Tunia kanuni za kanisa lako katika mazishi,
  • Fika mapema na kutoa pole kwa wafiwa kisha kajiandae kwa ibada
  • Fika kwa wakati hubiri kwa ufupi na kuwakumbusha watu wajibu wao kwa Mungu



Ibada ya ubatizo wa maji.



  • Ibada ya ubatizo wa maji ni tangazo la kumpokea Yesu ni ishara ya nje ya ushahidi kuwa umeamua kuwa mkristo kwa hivyo ni muhimu kwa waamini wapya kubatizwa haraka iwezekanavyo na ni sehemu ya agizo kuu Mathayo 28;19.
  • Mafundisho ni muhimu yakitolewa kwa wahusika au muhusika  kama ilivyokua kwa towashi wa kushi na mkuu wa gereza katika Matendo 8 na 16
  • Hakikisha watu wamejiandaa vizuri,mavazi yavaliwe vizuri na kuweko nguo za kubatiziwa na kubadili,batiza wanaume kwanza kasha wanawake,hakikisha maji ni safi na ikiwezekana yawe yanayotembea



Ibada ya ushirika wa meza ya bwana.

  • Yesu aliagiza ushirika wa meza ya bwana kufanyika kwa ukumbusho wake (Luka 22; 19). Tendo hili ni kuutangaza mauti ya Kristo hata ajapo 1Koritho 11;26 hakuna muda au wakati maalumu uliowekwa kibiblia kushiriki meza ya bwana hivyo kila kanisa litafanya kulingana na nafasi yake na katiba zao
  • Andaa watu kuandaa meza ya bwana yaani mkate na vikombe hasa mashemasi na ni lazima wajue kuwa kila inapotangazwa wana wajibu wa kufanya maandalizi yanayo lingana.
  • Fundisha kuhusu mkate na juisi itumikayo vinawakilisha nini ili kuondoa dhana potofu kuhusu meza ya Bwana.
  • Andaa ibada na wale watakaokusaidia katika kushirikisha Nyimbo za ibada hii lazima zilenge kwenye kuendana na tukio husika,Lazima watu waongozwe katika kujichunguza kwa upya na kwa ndani zaidi kuhusu uhusiano wao na Mungu na kudhamiria kuwa na uhusiano imara zaidi au mpya zaidi

Ibada ya kuweka wakfu watoto

  • Fanya maandalizi kwa ajili ya ibada hii watangazie wazazi wawe tayari kwa ibada hii
  • Elezea maana na faida ya tendo hili kibiblia elezea tofauti yake na kwa nini hatubatizi watoto wadogo
  • Weka wakfu ibada toa vyeti.



MCHUNGAJI NA MAONGOZI



A; Maswala ya kuyapa kipaumbele.

     Tunaelekea katika kujadili madaya mwisho kabisa katika somo letu zuri za huduma ya kichungaji katika sehemu zote tumeona kuwa sehemu kuu za huduma ya kichungaji inatawaliwa na kuhubiri, kufundisha, kutoa ushauri wa kichungaji na huduma maalumu kwa ujumla huduma hizi zote tayari zinaweza kuwa mzigo wa kutosha kwa mchungaji na kumfanya kuzidiwa na shughuli hizi huku akihitajiwa kutimiza mambo yake na shughuli nyingine hivyo ni muhimu kwa mtumishi kujifunza namna ya kuchukuliana na majukumu aliyo nayo na kujua ni namna gani atayapa kipaumbele mchungaji anapofahamu majukumu yake ndipo anapoweza kujua kuwa ni kitu ngani nakipe kipaumbele Yesu alisema hazina ya mtu ilipo ndipo na moyo wake unapokuwepo Mathayo 6;21, hii maana yake ni kuwa pale tunapotoa kipaumbele ndipo panapoonyesha tumepapa umuhimu mkubwa! Kwa msingi huo wale walioitwa na Mungu hutoa kipaumbele katika kile Mungu alichowaitia.



  • Weka wazi majukumu yako.

     Usipojiwekea majukumu utamaliza siku ukiwa hujatimiza kitu “Aim at nothing and that is exactly what you will hit”Moja ya tatizo kubwa sana tulilonalo makanisani ni wachungaji pamoja na watu wao kutokujua kwa nini wapo na kwa msingi huo makanisa mengi yamepoteza mwelekeo huku watu wakiwa wenye shughuli nyingi sana lakini bila kuwa na kusudi maalumu tunakwenda lakini hatujui wapi tuendako, Lazima tujiulize kwa nini tuko duniani na kwa nini Mungu alistawisha kanisa hapa duniani?. Na ninini jukumu la kanisa hapa duniani haya maswali tukijiuliza yaweza kutupa kipaumbele cha kujua nini cha kufanya?



  • Jukumu la kanisa.

Majukumu aya kanisa tunaweza kuyagawa katika maeneo makuu matatu yafuatayo;-

  1. Jukumu kwa Mungu.

i)        Kumuabudu Mungu katika roho na kweli Yohana 4; 24.

ii)       Kutunza uhusiano usiovunjika na Mungu  1Yohana 1;7 na Efeso 4;15-16

iii)     Kushiriki katika huduma ya kuwaombea wengine Warumi 8;26

iv)     Kujiachia kwa Roho mtakatifu na kudhihirisha karama zake na matunda ya roho 1Korithians 12; 7; 14. Na Galatia 5;22-25.



  1. Jukumu kwa waamini

i)        Kufanya kazi ya kutimiza Agizo kuu.1 korithians 3;9.

ii)       Kulitumia neno la mungu kwa halali katika kanisa na kwa matumizi binafsi kolosai 3;16

iii)     Kutambua majira ya kinabii na wakati tulionao 1Thyesalonike 5;2

iv)     Kuweka uthamani kwa mambo ya milele 2korotho5;10-11.



  1. Jukumu kwa ilimwengu.

i)        Kuwahubiria injili kwani watu kimsingi wanahitaji wokovu Yohana 3;3

ii)       Kutoa uthamanio kwa nafsi za wanadamu amabo Yesu aliwafia 1Petro 1;18-19

iii)     Kutambua kuwa kuna hukumu ya milele na kuwa watapotea tusipowajibika

iv)     Kuhitaji nguvu za Roho mtakatifu ili kuwafikia na kuwaleta kwa Yesu Mdo 1;8.



Mchungaji na majukumu yake

      Majukumu katika mwili wa kristo ni mengi hivyi hakikisha kuwa unaweka mizani sahihi katika kuyatimiza yoote si vizuri kuelemea katika jukumu moja tu yako makanisa ambayo wao ni hodari kwa uinjilisti tu na sehemu nyingine wamelala,pia mchungaji hakikisha kuwa unatoa mlo kamili wa kiroho kwa washirika wako ili wakue kiroho Waebrania 5;11-14

      Mchungaji tekeleza majukumu yako kwa malengo hakikisha kanisa linatimiza wajibu wake wanaookolewa wafundishwe, wanaopotea wafuatiliwe, andaa viongozi na kuhakikisha kuwa kila mmoja anawajibika kufikia lengo la kumtumikia Mungu

     Tumia fedha vizuri na fanya tathimini ya malengo yako huku ukitoa kipaumbele kwa kazi uliyoitiwa.



B. Umuhimu wa matumizi mazuri ya Muda

     Kutokana na majukumu ya kichungaji tuliyo nayo mara nyingi utaona au tumeona Muda ukiwa kama haututoshi kwa kweli kutimiza majukumu tuliyo nayo, kunaendana pia na jinsi tunavyoutumia muda mbona wengine wanati miza majukumu yao pamoja na muda kuonekana kama usiotosheleza? Kila wiki una masaa 168,na kila siku masaa 24 kwa wastani unaweza kuyagawa masaa 24 katika maeneo makuu matatu

1)      Masaa nane ya kazi

2)      Masaa nane ya kulala

3)      Masaa nane ya shughuli nyingine kama kula, mazoezi, kusafiri, kutembea na kutafuta mahitaji mengine jihoji kuwa unayatumiaje masaa 24? Unawajibika kujipanga au kupanga ratiba kwa ujumla utaona kuwa wachungaji wana muda wa kutosha sana lakini hawajui kutumia muda ipasavyo na hivyo wengi hupoteza muda tu mtu mmoja alijaribu kufanya utafiti na kugundua kuwa kwa wastani wachungaji hutumia kipindi chao cha kuishi cha miaka 70 kwa mtindo huu ufuatao



    • Miaka mitatu ya elimu
    • Miaka nane ya mzaha
    • Miaka sita ya kula
    • Miaka mitano ya kusafiri
    • Miaka mine ya kuongea
    • Miaka kumi na nne ya kufanya kazi
    • Miaka mitatu kujisomea
    • Miaka ishirini na nne ya kulala
    • Miaka mitatu ya kupoteza muda

Unapofanya tathimini utagundua kuwa muda mwingi unapotea bure bila jambo la maana kufanyika kwa msingi huo basi ni muhimu kuhakikisha kuwa unatumia nyenzo ambazo zitaweza kurahisisha kazi kazi pia unaweza kujaribu kupunguza na kugundua vitu vinavyopoteza muda kama vifuatavyo

  • Punguza ndoto za mchana yaani kuwaza mambo ambayo unataka kuyatimiza kama kumaliza matatizo yako n.k
  • Punguza kutokuwa na malengo kujifanyia shughuli alimradi siku iende tu au shughuli za zimamoto
  • Punguza mazungumzo ya kijamii na utani yasiyo ya msingi sana
  • Hakikisha kuwa unakabidhi watu majukumu ambao wanauwezo wa kuyatimiza na kuwa hayatakugharimi wewe kushughulikia kila kitu
  • Kutokumalizia kazi fulanifulani si vema kwa mchungaji jiepushe sana na kuhairisha kazi za kufanya.



C; Umuhimu wa kupanga ratiba

     Ili kuepuka usumbufu usio na msingi ni muhimu kwa mchungaji kuwa mtuzaji wa muda kwa kujipangia ratiba uwe wakili mzuri wa muda 1Koritho 4;2

Uwe na malengo usijifanyie kazi hovyo hovyo

Ni muhimu kujipangia ratiba panga kuanzia na mambo ya msingi na yanayofuatia chagua mambo ya msuingi kila iitwapo leo amabyo ni muhimu kwako kuyatekeleza, jipangie malengo na muda wa kuyakamilisha malengo yako, ruhusu wakati mwingine kuingiliwa kwa ratiba yako hayo ni mambo ya kawaida, jifunze kusema hapana kuna mambo amabyo kama unaona haya kuyasemea hapana yanaweza kukugharimu muda, panga muda kwa familia yako, jiwekee ratiba itakayozingatia afya yako.

  

     D ; Kuwaandaa washirika kwa kazi ya huduma

      Mchungaji jukumu lako kubwa  ni kuwaandaa washirika kwa ajili ya utumishi Training jambo hili linawasumbua wachungaji wengi sana lazima utofautisha washirika wa mwaka huu na mwaka juzi kwa maana ya kuwa na madarasa ya wokovu yanayolingana na ukuaji na uzoefu katika utumishi wakipitia mafundisho ya maalumu ya kazi mbalimbali

    Kumbuka kuwa kanisa sio

1)      Kituo cha mafuta ya gari hapo si mahali ambapo watu wanakuja na mchungaji anawahudumia kasha wanakwenda zao ni lazima wafanye kitu

2)      Kliniki mahali ambapo watu wanazaliwa wanaangaliwa afya zao kasha wakikuwa wanaondoka

3)      Ukumbi wa sanaa watu wanakuja wanapata burudani kasha wanaondoka zao msanii mkuu ni mchungaji

4)      Kiwanja cha michezo ambapo watu huja kutazama michezo lakini wao si wachezaji kasha huenda zao

5)      Betrii inayochajiwa ambapo hutumika huko na kasha huja kuchajiwa tena washirika ni lazima wazalishe lazima watumike kanisa lolote ambalo limekufa washirika wake huwa hawana la ziada la kufanya zaidi ya kuwa watazamaji leo washirika wengi hata kushuhudia hawawezi

6)      Ondoa dhana potofu kuwa  ni mchungaji tu mwenye huduma au karama au kufikiri kuwa ni wachache tu wenye huduma au karama au waliojaaliwa kutumika

7)      Wakumbushe wajibu wa kibiblia wa kuhudumu ambapo biblia inaamini kuwa kila mtu ana karama Efeso 4;7 1Petro 4;10 na kuna tofauti za huduma 1Koritho 12;4 Warumi 12;6,na kuwa kila karama inahitajika Efeso 4;16 na kuwa kila mshirika ana jukumu la kuitumia karama aliyonayo 2Timotheo 1;6.1Timotheo 4;14.

8)      Washiriksa wakumbushwe kuhubiri na kufundisha kwa usahii, wafanye huduma na kupata uzoefu, watambue uwezo walionao, na wawe mfano wa kuigwa

9)      Tumia njia mbalimbali za kufundisha washirika zikiwemo semina, vitendo, kuwatambua, kuwatumia viongozi waliojifunza wape majukumu, weka wazi majukumu yao chagua watu kwa ajili ya majukumu husika

                                                                                 

Falsafa ya mwandishi wa somo;

“Uchungaji ni jukumu lililo zito sana wenye akili hulikimbia,Wajinga hulikimbilia,Wapumbavu huligombania Bali wanyenyekevu na wenye hekima  husema Tazama mimi ni mtumishi wa Bwana nisiye na faida  na iwe kwangu kama upendavyo”- Kamote.

Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima

Hakuna maoni: