Jumanne, 25 Oktoba 2016

Kuuona wema wa Bwana katika nchi ya walio hai!


 
Adniko la Msingi: Zaburi 27:13. “Naamini ya kuwa nitauona wema wa BWANA Katika nchi ya walio hai


Utangulizi:

Zaburi ya 27 ni wazi kabisa kuwa ni zaburi ya Daudi, Zaburi hii ina mambo mengi sana ya kutafakari, Muda hauwezi kutosha kutafakari mambo yote, lakini leo nataka tutafakari tumaini kuu la ajabu alilokuwa nalo Daudi, kuhusu ndoto yake na ahadi za Mungu kwake, Haikuwa wazi kabisa kuwa Daudi hapa alikuwa anapigana vita ya aina gani, au bwana alikuwa amempa ushindi wa namna gani ama bado adui walikuwa wakimtishia na ulifikia wakati akaogopa  lakini bado alisalia na tumaini moja tu kwamba yeye anaamini kuwa atauona wema wa Bwana katika nchi ya walio hai! Ni kitu gani kinampa Daudi moyo wa imani hii

1.       Mstari  1-3 Alikuwa na ujuzi kuwa Bwana ni Nuru yake. Kwamba hakuna giza mbele kama unamtumainia Mungu, hofu yote inaondoka na unaweza kuiona future ( kuwa na Maisha mazuri na ya furaha) hata kama kuna kila aina ya hila, wazushi, waongo, watenda mabaya, watesi, adui, majeshi ya maadui, hivi vyote haviwezi kumtisha Daudi kwa sababu Bwana ni Nuru yake, mtu asiye na Mungu yumo gizani, ataishi maisha ya hofu kuu sana kwa sababu.

·         Watenda mabaya, wenye dhambi, waovu, wicked or evil doer
·         Watesi, waonezi, wasengenyaji, wanyanyasaji
·         Adui, foes, enemies, wapinzani, wasiotaka ufanikiwe
·         Jeshi, wanaopigana nao kimwili na kiroho, kisaikolojia, kiakili na vyovyote vile

Daudi alisema hawaogopi hao kabisa kwa sababu Bwana ni ngome ya uzima wake, Huu ulikuwa ni uthibitisho ulio dhahiri kuwa Daudi alidumisha uhusiano wake na Mungu, mtu yeyote yule atakayedumisha uhusiano wake na Mungu hawezi kutembea gizani, hawawezi kupoteza tumaini hata kama wataogopa watajitia moyo, na Mungu kwa hakika atawapigania na kuwalinda hakuna adui anaweza kufanikiwa kwako kama ilivyokuwa kwa Daudi ndivyo itakavyokuwa kwa kila anayemtanguliza Mungu mbele

2.       Mstari 4-5 Daudi anaeleza sababu kubwa ya kumtegemea Mungu ni kwamba pia akipewa uhai na kulindwa na Mungu atautumia uhai huo kukaa nyumbani mwa Bwana, ana kiu na shauku ya kutaka kuendelea kumuabudu Mungu, ni kama anaweka Nadhiri kwa Mungu mradi Bwana atanisitiri siku ya Mabaya na kuniinua, basi katika maisha yangu nitamuabudu, nitamtafakari, hekaluni mwake nitamuimbia, Daudi aliongeza aina nyingine ya Mapito na maombi aliyotaka mungu amtendee lakini kubwa zaidi anahitimisha kwa imani kuwa

3.       Anaamini kuwa atauona wema wa Bwana katika nchi ya walio hai, katika eneo hili Daudi alimuomba Mungu Mstari 12, asimtie katika nia ya adui zake, nia ya adui zake ni kumuangusha ni kuona kuwa hafanikiwi, ni kutoa ushahidi wa uongo na maneno ya Jeuri sana, Lakini Daudi anaamini atauona wema wa Bwana katika inchi ya walio hai

Mstari 13 jambo gani kubwa tunajifunza, hapa Daudi alielewa wazi kuwa kuna maisha baada ya kufa, alijua kuna kuishi milele, alijua kuna kwenda Mbinguni, lakini hakufurahia kuishi kwa shida Duniani, hapa alimuamini Mungu kuwa hatamuacha afe bila kumuonyesha mema katika nchi ya walio hai yaani hapa Duniani,

Kuingia mbinguni sawa kupo, kula vizuri mbinguni sawa kupo, magari ya farasi mbinguni sawa yapo, maisha ya matanuzi huko mbinguni sawa yapo lakini Daudi aliomba auone wema wa Mungu hapa Duniani kwenye nchi ya walio hai, kuna nchi ya wafu sawa, lakini kabla ya kwenda huko je nisionje mema ? kuna kufaulu kule mbinguni sawa, lakini ndo nifeli na Duniani, kuna majumba mbiguni sawa lakini ndo niishi katika kijinyumba cha nyasi Duniani? Kuna magari ya farasi za moto mbinguni sawa lakini je hapa duniani nisiendeshe hata toyo?, kuna hali ya hewa nzuri Mbinguni sawa lakini ndio nisipigwe hata na kiyoyozi duniani Daudi alimuomba Mungu kwamba ni lazima ufikie wakati vita vimalizike, mapambano yaishe, awe na wakati wa starehe, afanye kazi ya kuabudu

ndugu ulivyopambana duniani inatosha sasa mwambie Mungu akufurahishe akuonyeshe wema wake sasa, lazima ufikie ndoto zako na kuepushwa na kila aina ya mabaya ya dunia hii na Mungu atakupa kustarehe Hatimaye daudi alistarehe

2Samuel 7:1-2 “1. Ikawa, mfalme alipokuwa akikaa katika nyumba yake, hapo Bwana alipomstarehesha, asiudhiwe na adui zake waliomzunguka pande zote, 2. mfalme akamwambia Nathani, nabii, Angalia sasa, mimi ninakaa katika nyumba ya mierezi, bali sanduku la Mungu linakaa ndani ya mapazia.

Uko wakati wa Mapambano lakini pia uko wakati wa kustarehe Mungu na akufanikishe katika vita vyako na pia akujaalie wakati wa Kustarehe kama ilivyokuwa kwa Daudi


Naamini ya kuwa nitauona wema wa BWANA Katika nchi ya walio hai
Rev. Innocent Kamote
Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima!

Hakuna maoni: