Jumapili, 31 Januari 2016

AKADAI KUWA ATI ANAMUUGUZA KAKA YAKE!



Ni mwaka  1994 wakati nilipoingia kwenye kasheshe kubwa ambayo nusura iniingize jela, nikiwa ndio nina mwaka wa pili tangu nimeanza kazi nilimpachika binti mmoja mimba alikuwa ni binti wa shule akisoma darasa la sita wakati ule ,mwili wake ulikuwa mkubwa kiasi kwamba ukiambiwa kuwa yuko darasa la nne ungebisha lakini alikuwa bado mdogo ,baada ya kumpachika mimba mjomba wake  ambaye ndiye aliyekuwa akiishi naye alilifungia kibwebwe suala lile akitaka nipelekwe mahakamani, ndugu zangu na jamaa zangu walijitahidi kwa kadiri wawezavyo kuzuia jambo lile kufikishwa mahakamani, Mjomba wa binti alikubali lakini kwa sharti moja tu la mimi kumuoa mpwa wake mara moja 
                  Kumpa mwanamke mimba Ni neema au Karaha hasa inapokuwa sio mwanamke halali


Nilikubali kufanya hivyo haraka kwani nilishauona mlango wa ukonga ukiwa wazi mbele yangu, Nilimuoa binti Yule kwa ndoa ya mkeka wazazi wake hawakuweko kwani wanaishi vijijini mkoani Ruvuma, mwezi huo huo nililazimika kwenda mbeya kikazi , ambapo nilitakiwa kuishi kwa miezi mitatu kwa ajili ya kazi ya mkataba  ambayo kampuni yetu ilipata, Nilipokuwa Mbeya nilipata mwanamke ambaye alionekana kuwa ana adabu za kule kijijini kabisa , huyu nilimpata hospitalini nilipokuwa nimekwenda kutibiwa maralia , wiki ya tatu tangu kufika pale , Mbeya.

Sijui tulizoeana vipi Lakini alikuja kuwa rafiki yangu, alikuwa ni mwenyeji wa Ruvuma na pale Mbeya alukuwa amekuja kumuuguza kaka yake ambaye alilazwa katika hospitali ya rufaa pale mbeya nilimpenda kwa kweli hasa nidhamu yake na hekima  kiumri alikuwa amenizidi miaka mine, yaani mimi nilikuwa na miaka 29 na yeye 33, lakini kwa kutazama mimi ndiye nilionekana mkubwa, niliishi naye kama mke wangu hadi miezi mitatu ikaisha. Nilirudi Dar nikimuacha bado anauguza mgonjwa wake, wiki mbili baadaye alinijulisha kuwa Yule kaka yake amefariki na walikuwa wanakwenda kuzika Ruvuma , Bahati mbaya ni kwamba, siku hiyo hiyo , tuliletewa taarifa Baba wa mke wangu alikuwa amefariki, nilisahau maswala ya hawara yangu na nikaweka nguvu kwenye kifo cha baba mkwe.

Tuliamua kusafiri kwenda Ruvuma mke wangu wakati huo ana mimba ya miezi sita, tuliondoka mimi yeye na ndugu yangu mmoja, tulifika kijijini kwao jioni ambapo tulikuta mazishi yakiendelea , tulikwenda makaburini , tukimwacha mke wangu nyumbani kutokana na hali yake, tulipofika makaburini tulikuta ndiyo zamu ya kuweka mashada ya maua ikiwa inaendelea  ilikuwa kama ndoto Fulani kwani nilimuona Yule hawara yangu wa mbeya akiweka shada la maua huku akitajwa kama mke wa marehemu. Nilihisi kama nataka kupoteza fahamu Nilijikaza ingawa nilikuwa natoka jasho sana 

Baada ya mazishi tulirudi nyumbani ambapo ilibidi nitambulishwe kwa mzazi wa mke wangu na ndugu zake Nilitambulishwa kwanza kwa mama mkwe ambaye kumbe kule Mbeya alikuwa ni hawara yangu  kila mmoja kati yetu alijikaza ili isifahamike kinachoendele, lakini hiyo haikudumu kwa muda mrefu kwani mama mkwe wangu alilazimika kusema kwa wazazi wake ati akiogopa mkosi utokanao na jambo hilo, ilibidi siku ya nne baada ya msiba tufanyiwe tambiko la kiasili kuondoa laana, nataka nikuambie  katika maisha yangu huu ulikuwa mtihani mgumu, ninaye bado mke wangu na tumayasahau yaliyopita mama mkwe hajawahi kuja kwetu, ingawa sisi huwa tunaenda na kukaa siku chache kwake kila mwaka 
na Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote

Hakuna maoni: