Alhamisi, 28 Januari 2016

UJUMBE: KUTAFUTA AMANI KWA BIDII


Waebrania 12:14 “Biblia inasema hivi, Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao”
Watu wengi sana duniani wanaishi maisha ya uchungu, na majuto na wakati mwingine kuzikosa Baraka za Mungu kwa sababu hawana ufahamu wa umuhimu wa kuwa na amani na watu wote, kukosa kuwa na amani na watu wote kunatukosesha Baraka nyingi sana ambazo Mungu amekusudia kwetu, leo tutazungumzia kwa undani sana umuhimu wa kuitafuta amani, tutajifunza somo hili kwa kuzingatia vipengele vitatu muhimu vya msingi vifuatavyo.


  • ·         Maana ya amani
  • ·         Maana ya neno bidii
  • ·         Kutafuta amani kwa bidii.



      Maana ya amani.
Neno amani linalotajwa katika Biblia ni tofauti sana na neno amani linavyotumika katika mazingira tuliyoyazoea, Kibiblia neno amani lina maana pana zaidi, Katika lugha ya Kiebrania neno amani maana yake ni SHALOM sawa na neno Salaam la kiarabu na Salama la Kiswahili, kwa kiyunani Irene neno hili linamaanisha ni kuwa na ustawi katika mazingira yote ya mwili nafsi na roho na kutokuwa na vita pande zote yaani vita vya kimwili na kiroho na nafsi ni kuwa na utulivu au SOLOMON kwa kiibrania yaani kuwa na amani pande zote au kutokuzungukwa na mazingira ya uadui au kuwa na maadui, wengi wetu tutakuwa tunafahamu kihistoria kuwa hata Mji wa “Dar es Salaam” una uhusiano na tafasiri ya kiarabu ya Amani ambapo Sultani Baraghash aliuona mji wa Mzizima kuwa ni bandari ya utulivu kuliko Zanzibar na kwa sababu alipewa ukanda wa Pwani ya Afrika mashariki kuutawala alihamishia makazi yake Mzizima na kupaita Dar es Salaam kwa kiarabu  ikiwa na maana ya Bandari ya salama, Jina Yerusalem kiibrania pia humaanisha mji wa Amani.
Msgingi mkubwa wa mafanikio ya mwanadamu awaye yote ni amani, ili Familia, Ndoa, taasisi, na hata taifa liweze kuwa na ustawi linahitaji amani, na shetani anajua wazi kabisa kuwa amani ikiwako kila kitu kitafanikiwa hivyo ili aweze kuvuruga Ndoa, Familia, taasisi au Taifa shetani atakachokifanya ni kuiiba amani kwanza kumbuka kuwa yeye anaitwa mwivi katika maandiko na kazi yake ni kuiba, kuchinja na kuua Yohana 10: 10 Biblia inasema hivi “Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele”. Shetani wakati wote atatafuta kuiiba amani ili kuharibu kila kitu yakiwamo mafanikio na baraka Mungu alizokusudia kwetu na amani inapotoweka kila kitu hupoteza maana na hata maisha huonekana kama hayana umuhimu tena.

Maana ya neno Bidii
Neno bidii au juhudi Katika kiingereza Biblia ya NIV inatumia neno “Make every Effort” na Biblia ya kiingereza iitwayo Amplified inatumia neno “Strive” ambalo maana yake ni  “try very hard to achieve” kwa maana nyingine Biblia inasema fanya kila juhudi, au jitihada au kila liwezekanalo, au kwa gharama yoyote au juu chini au hakikisha au pambana kwa namna yoyote ile kuhakikisha kuwa unakuwa na amani na watu wote, kama biblia inasisitiza hilo basi ni muhimu kuzingatia kuwa amani na watu wote ni jambo la muhimu sana sana

Kutafuta amani kwa Bidii 
Yakobo ni moja ya mfano muhimu sana wa kibiblia ya mtu aliyetatufa amani kwa bidii, wote tunafahamu historia yake na kaka yake pacha wake aliyeitwa Esau, wao walikuwa ndugu tena mapacha walikuwa pamoja kwa upendo na hawakuwahi kuwa na ugomvi wakati wowote mpaka tunaposoma kisa cha ajabu kuwa ndugu hao walifikia hatua ya kjuwa na uadui wa hali ya juu kiasi cha mmoja kutamani kumuua mwenzi wake kutokana na Yakobo kuuchukua Mbaraka wa Esau kwa hila, jambo hili lilivuruga kabisa mahusiano yao Mwanzo 27:41-45 Biblia inasema hivi
“Esau akamchukia Yakobo kwa ajili ya ule mbaraka babaye aliombarikia. Esau akasema moyoni mwake, Siku za kumlilia baba yangu zinakaribia, ndipo nitakapomwua ndugu yangu Yakobo.  Rebeka akaarifiwa maneno ya Esau, mwanawe mkubwa. Akapeleka mtu kumwita Yakobo, mwanawe mdogo, akamwambia, Tazama, katika habari zako Esau, ndugu yako, anajifariji moyo wake, maana anakusudia kukuua.  Na sasa, mwanangu, sikia sauti yangu, uondoke, ukimbilie kwa Labani, ndugu yangu huko Harani;  ukae kwake siku chache, hata ghadhabu ya ndugu yako igeuke;  hata ikuondokee ghadhabu ya ndugu yako, akasahau uliyomtenda. Ndipo nitakapopeleka watu kukuchukua kutoka huko. Kwa nini nifiwe nanyi nyote wawili siku moja?”
Unaona ndugu msomaji wangu uhusiano wa ndugu hao wa karibu inaweza kuwa picha yaw ewe na rafiki yako, au mpendwa mwenzako au mumeo au mkeo chuki inaingia kiasi cha kutaka kumalizana, hii ndio ilikuwa hali ya Esau na Yakobo waliachana vibaya na sio kwa amani, na kutokana na hiki alichokifanya Yakobo ukweli ni kuwa Yakobo alikabiliwa na maisha ya taabu na dhiki na matesoi mengi sana kuliko mtu yeyote katika Biblia aliteseka na kupata fadhaa nyingi sana kwa sababu aliuacha moyo wa kaka yake ukiwa hauna amani naye, hata ingawa alifanya kazi kupata mke na mali alizipata kwa shida nyingi yeye mwenyewe anakiri mbele ya Farao kuwa Maisha ya kusafiri kwake yamekuwa ya dhiki na mateso mengi kuliko ya kusafiri kwao baba zake unaweza kuona  Mwanzo 31:4-7 Biblia inaonyesha haya kuwa Yakobo hata huko Ujombani aliamua kutoroka kutokana na shida na taabu alizozipata
 Mwanzo 31:4-7 “Yakobo akatuma watu, akawaita Raheli na Lea waje nyikani kwenye wanyama wake. Akawaambia, Naona uso wa baba yenu, kwamba hanitazami vema kama jana na juzi. Lakini Mungu wa baba yangu amekuwa pamoja nami. Nanyi mmejua ya kwamba kwa nguvu zangu zote nimemtumikia baba yenu. Na baba yenu amenidanganya, akabadili mshahara wangu mara kumi; lakini Mungu hakumwacha kunidhuru.”
Mwanzo 31: 22-29, 39-42 “Miaka hii ishirini nimekaa kwako; kondoo zako wala mbuzi zako wake hawakuharibu mimba wala waume katika wanyama wako sikuwala. Kilichoraruliwa na hayawani sikukuletea, mimi mwenyewe nimetwaa hasara yake, wewe umekidai katika mkono wangu, ikiwa kilichukuliwa mchana, au ikiwa kilichukuliwa usiku. Hii ilikuwa hali yangu; mchana jua likanipata, na baridi usiku, usingizi ukanitoka machoni mwangu. Miaka hii ishirini nimekaa nyumbani mwako; nilikutumikia miaka kumi na minne kwa binti zako wawili, na miaka sita kwa wanyama wako, nawe umebadili mshahara wangu mara kumi. Kama Mungu wa baba yangu, Mungu wa Ibrahimu na Hofu ya Isaka, hangalikuwa pamoja nami, hakika sasa ungalinifukuza mikono mitupu. Mateso yangu na kazi za mikono yangu Mungu ameziona, akakukemea usiku huu”.
Unaweza kuona maisha ya Yakobo hayakuwa Rahisi licha ya Baraka alizokuwa amezipora alipitia shida mateso na maumivu mengi na sasa ni kama yuko Hatarini anaachana na mjomba wake katika mazingira magumu na sasa ni kama anakotoka kubaya na anakorudi kubaya ameteseka kwa takriban miaka 20 alipopoteza mnyama alilipishwa na sasa maisha yake yako hatarini alitambua kosa lake ni kwa sababu moyo wa kaka yake hauna amani na yeye
Mwanzo 32:3-8  Basi, Yakobo akapeleka wajumbe mbele yake kwenda kwa Esau nduguye mpaka nchi ya Seiri katika nyika ya Edomu.  Akawaagiza akisema, Mwambieni hivi bwana wangu, Esau, Hivi ndivyo asemavyo mtumwa wako, Yakobo; Nimekaa ugenini kwa Labani, na kukawia huko hata sasa, nami nina ng'ombe, na punda, na kondoo, na watumwa, na vijakazi; nami nimepeleka watu nimpashe bwana wangu habari, nipate neema machoni pako.  Wale wajumbe wakarudi kwa Yakobo wakisema, Tulifika kwa ndugu yako, Esau, naye anakuja kukulaki, na watu mia nne pamoja naye.  Ndipo Yakobo akaogopa sana, na kufadhaika sana, akawagawanya watu waliopo pamoja naye, na kondoo, na ng'ombe, na ngamia, wawe matuo mawili. Akasema, Akija Esau kwa kundi la kwanza, akalipiga, kundi litakalosalia litaokoka.”
Unaweza kupata picha katika mistari hii sasa Esau anapata habari kuwa Yakobo anakuja na anamkabili na askari wapatao mia nne ulikuwa wakati mgumu sana kwa Yakobo na hivyo aliamua kumuomba Mungu Mwanzo 32:9-12 biblia inasema wazi
 “Yakobo akasema, Ee Mungu wa baba yangu Ibrahimu, na Mungu wa baba yangu Isaka, BWANA, uliyeniambia, Rudi uende mpaka nchi yako, na kwa jamaa zako, nami nitakutendea mema;  mimi sistahili hata kidogo hizo rehema zote na kweli yote uliyomfanyia mtumwa wako; maana nalivuka mto huo wa Yordani na fimbo yangu tu, na sasa nimekuwa matuo mawili.  Uniokoe sasa na mkono wa ndugu yangu, mkono wa Esau, maana mimi namwogopa, asije akanipiga, na mama pamoja na wana. Nawe ulisema, Hakika nitakutendea mema, nami nitafanya uzao wako uwe kama mchanga wa bahari, usiohesabika kwa kuwa mwingi.”        
Pamoja na maombi ya kuonyesha kumuogopa Esau yak obo alitambua kuwa maombi pekee hayaytoshi na hivyo alilazimika kuandaa zawadi za kutosha ili aweze kupata suluhu na kuurejesha tena moyo wa kaka yake, wapendwa wengi hawafikiri kuwa unapoujeruhi moyo wa ndugu yako unahitaji kuutafuta tena kwa gharama yoyote, Ndugu yako akiwa na kinyongo nawe na uchungu nawe maisha yako yatakuwa ya taabu na mateso na uchungu mwingi na huwezinkufanikiwa sasa Yakobo alikuwa tayari amekwisha pata somo kuhususwala hili na alikuwa na uelewa kuwa Mungu sio wakwake pekee alitambua kuwa anapaswa kunyenyekea aliytambua kuwa Esau ni Bwana na Yeye ni mtumwa tu! Alikubali kujishusha nili kupata kibali kwa kaka yake
Wako wapendwa wengine wanaweza kukutukana na kukunenea maneno mabaya nay a kukubomoa na hata kufanya hila na uzushi ili uharibikiwe na kisha wakafikiri wako sahii mbele za Mungu, ni muhimu kufahamu kuwa Mungu katika upendo wake hafurahii udhalimu sasa Yakobo alibadilika na kuwa mtu mwingine akinyenyekea  angalia hatua alizochukua
Mwanzo 32:13-21 “Biblia inasema hivi Akakaa huko usiku ule. Kisha akatwaa baadhi ya vitu alivyokuwa navyo, kuwa zawadi kwa Esau, nduguye; mbuzi wake mia mbili, na mbuzi waume ishirini, kondoo wake mia mbili, na kondoo waume ishirini;  ngamia wanyonyeshao thelathini pamoja na wana wao, ng'ombe wake arobaini na mafahali kumi; punda wake ishirini na wana wao kumi.  Akawatia mkononi mwa watumwa wake, kila kundi peke yake. Naye akawaambia watumwa wake, Vukeni mbele yangu, mkaache nafasi kati ya kundi na kundi. Akamwagiza yule wa kwanza akasema, Esau, ndugu yangu, akikukuta, na kukuuliza, akisema, Wewe u wa nani? Unakwenda wapi? Tena ni wa nani hawa walio mbele yako?  Basi, useme, Ni wa mtumwa wako, Yakobo, ni zawadi, aliyompelekea bwana wangu, Esau. Na tazama, yeye mwenyewe yuko nyuma yetu. Akamwagiza tena wa pili, na wa tatu, wote waliofuata makundi, akisema, Hivi ndivyo mtakavyomwambia Esau, akiwakuta.  Tena semeni, Tazama, mtumwa wako, Yakobo, yuko nyuma yetu. Maana alisema, Nitamsuluhisha kwa zawadi inayonitangulia, baadaye nitamwona uso wake; huenda atanikubali uso wangu. Basi ile zawadi ikavuka mbele yake, naye mwenyewe akakaa usiku ule kambini”.
Yakobo alifanya jitihada kubwa sana katika kurejesha amani ni jambo la kushangaza kuona kuwa wako watu wanapoteza amani na ndugu zao jamaa zao na wanashindwa hata kutumia ujumbe wa shs 50 kwa simu kuomba radhi, kila mmoja anapokuwa na kiburi na kukataa kujishusha ni wazi kuwa amani haiwezi kupatikana Yakobo alijirudi kwa kweli alikuwa amebadilika si mwenye kupenda makuu tena
Mwanzo 33 :1-11 unaonyesha mafanikio ya jitihada ya kutuatuta amani kwa bidii bilia inasema hivi “Yakobo akainua macho yake, akaona, na tazama, Esau anakuja na watu mia nne pamoja naye. Akawagawanyia Lea, na Raheli, na wale vijakazi wawili, wana wao.  Akawaweka hao vijakazi na wana wao mbele, na Lea na wanawe nyuma yao, na Raheli na Yusufu mwisho.  Akapita mwenyewe mbele yao, akainama mpaka nchi mara saba, hata alipomkaribia ndugu yake. Esau akaja mbio kumlaki, akamkumbatia, na kumwangukia shingoni, akambusu; nao wakalia.  Akainua macho yake, akawaona wale wanawake na watoto, akauliza, Ni nani hawa walio pamoja nawe? Akasema, Ni watoto Mungu aliompa mtumwa wako kwa neema yake. Ndipo wale vijakazi, na wana wao, wakakaribia wakainama.  Lea naye, na wanawe, wakakaribia wakainama. Baadaye Yusufu na Raheli wakakaribia, wakainama.  Akasema, Kundi hili lote nililolikuta, maana yake ni nini? Akasema, Kunipatia kibali machoni pa bwana wangu. Esau akasema, Ninayo tele, ndugu yangu, uliyo nayo na yawe yako.  Yakobo akasema, Sivyo; kama nimekubalika machoni pako tafadhali upokee zawadi yangu mkononi mwangu, iwapo nimeona uso wako kama kuona uso wa Mungu, ukapendezwa nami. Pokea, tafadhali, mbaraka wangu, ulioletewa, kwa sababu Mungu amenineemesha, na kwa sababu ninavyo hivi vyote Akamshurutisha, naye akapokea”.

Biblia inaonyesha juhudi za Yakobo zilizaa matunda na hatimaye alipokelewa vema na Ndugu yake na wote wakalia machozi na kusameheana moyo wa Esau ukawa na amani na Yakobo!
Ni kupitia mfano huu wa Yakobo Biblia inasema tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote je unafanya jitihada gani kuhakikisha unakuwa na amani na watu wote, unawezaje kuendelea kusali na kuomba na kuabudu huku hauna amani na ndugu yako, mfanya kazi mwenzako,mkeo , mumeo nduguzo mwanasiasa mwenzako na kadhalika. Tukitafuta amani Mungu ataondoa huzuni zote na uadui na kutupa faraja na tutafurahia kila kinachotuzunguka

Mkuu wa wajenzi mwenye Hekima
Rev. Innocent Kamote.

Hakuna maoni: