Alhamisi, 4 Februari 2016

Hakika ya Wokovu !


Mstari wa Msingi;(Zaburi 103;12)’Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi Ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi”

        Utangulizi;
        Moja ya mbinu kubwa anayoitumia shetani na kufanikiwa kuwarudisha watu nyuma Katika uchanga wao ni kuwafanya wautilie mashaka wokovu, Atawatia mashaka kujihoji kama kweli wamesamehewa dhambi zao, njia hii ataitumia pia kwako atakufanya ujiulize maswali kuwa wewe nawe umneokoka? Au unajidanganya mwenyewe? Atakuuliza mbona hakuna badiliko lolote? Mbona uko vile, au mbona umekasirika leo asubuhi na waliookoka hawapaswi kuwa na hasira? Hii yote ni gea ya kukutia mashaka ili uhisi kuwa hujaokoka na hatimaye kurudi nyuma.


 Kurudi Nyumbani

       Ni muhimu kufahamu kuwa tunapokea wokovu kwa Imani na si kwa kuona au kwa hisia au kujisikia kuwa sasa nimeokoka, tunapookoka miili yetu itakuwa vilevile na hakutakuwa na badiliko isipokuwa katika roho kunatokea mabadiliko makubwa, Mambo ya kiroho yanatambulika kwa kungalia neno la Mungu linasema nini tangu ulipoamua kukata shauri na kutubu dhambi zako kwa kumaanisha kuziacha ukiamini kazi aliyoifanya Yesu pale msalabani haya ndiyo yanayotokea katika ulimwengu wa kiroho;-

  • Dhambi zako Zimesamehewa na Mungu hazikumbuki tena ;
Mtu anapoamua kutubu dhambi zake kwa kumaanisha kuziacha Mungu humsamehe mtu huyo na hakumbuki tena dhambi hizo (Zaburi 103;12).”Kama mashariki ilivyo mbali na magharibi ndivyo alivyoweka dhambi zetu mbali nasi” Isaya 1;18.

  • Mungu  huyafuta makosa Yetu kwa ajili yake Mwenyewe;
(Isaya 43; 25) Biblia inasema “Mimi naam mimi ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; wala sitazikumbuka dhambi zako” Ni mpango wa Mungu mwenyewe kabisa kutusamehe na kutuketisha katika pendo la mwana wake Tangu tulipookolewa tunao ukombozi yaani msamaha wa dhambi (Kolosai 1;13-14,21-22)

  • Dhambi zetu zilizokuwa nyekundu kama Bendera zinafutwa kuwa nyeupe kama Theluji.
    Hii ni ahadi ya Mungu mwenyewe kuwa anapotuita kwake na tukakubali hutupa thawabu ya msamaha na kutuhesabu kama viumbe vipya huku akituhakikishia msamaha wa dhambi (Isaya 1;18).

  • Sasa Unao uhakika wa uzima wa milele.
 Kabla ya kutubu dhambi zetu kwa kumaanisha kuziacha na kumwamini Yesu mwana wa Mungu aliyekufa kwa ajili  ya dhambi zetu.Tulikuwa katika ghadhabu ya Mungu na hivyo uzima wa milele ulikuwa Mbali nasi,Tulikua chini ya hukumu Lakini sasa tu warithi wa pamoja na Kristo (Yohana 3;18,36,Warumi 8;14-17,1Yohana 5;11-13).

  • Hutapotea kamwe ukiwa mikononi mwa Yesu
Kuanzia ulipokata shauri kuokoka  wewe sasa uko mikononi mwa YesuKristo nay eye nia yake  na mapenzi yake kabisa ni  kwamba uendee mbinguni  huko aliko na kufurahi pamoja naye milele na milele  ni mapenzi ya Baba yake pia  na kwa kua ana nguvu kuliko Shetani  atahakikisha ya kuwa yeyote atakaye kukupokea kutoka katika mikono yake  ili urudi katika ghadhabu ya milele hatafanikiwa Yohana 10;27-29 hiyo ndiyo ahadi yake kwako Hata hivyo ni muhimu kufahamu kuwa hata wewe una sehemu ya kufanya ili haya yaweze kutimia kwako  mambo yafuatayo ni muhimu sasa kwako kuyafanyia kazi 

a.       Jifunze kuisikia sauti ya Bwana Yesu
Sauti ya Bwana Yesu ni Neno la Mungu inakupasa kila uatakalojifunza katika Neno la Mungu yaani Biblia ulisikie na kuliweka Moyoni, Ni lazima upende kusikia Neno la Mungu na upende pia kulisoma na kulijifunza neno la Mungu

b.      Jifunze kumfuata Yesu
Yesu alikuwa mtii kwa Baba yake sisi nasi kama kondoo wake inatupasa kuwa watii pia, Neno la Mungu linapotutaka kubadilika ni muhimu tuwe watii na kujifunza kumfuata bwana Yesu kila jambo analolitaka tulifanye basi lifanyike mara moja  huko ndiko kumfuata bwana Yesu si vema kujiongoza wenyewe katika kila jambo  lakini na tuyafuatae maongozi ya Bwana Yesu  Yeye ndiye mwokozi wetu  na Bwana wetu Warumi 10;9 Jina Bwana humaanisha mtawala hivyo kumkubali Yesu kuwa ni Bwana maana yake ni kukubali atutawale, Hapo mwanzo tulifanya kila tuliloliona jema machoni petu lakini sasa inatupasa kukubali maongozi ya Mungu wetu  sisi sio waasi tena Mungu alituokoa kutoka katika maasi 1Yohana 3;4  kwa msingi huo hatupaswi kumuasi tena Mungu  ukiyafanya haya hutapotea kamwe na hakuna atakaye kutoa katika mikono ya Mungu na uzima wa milele ni wako  na makao yako sasa ni mbinguni Yohana 10;27-29 

Madhara ya kufanya dhambi baada ya kuokoka
Dhambi ni jambo la kuchukiza sana machoni pa Mungu Mungu anawapenda sana watu lakini Mungu anachukia dhambi, kuna uwezekano kwa mtu aliyeokoka kufanya dhambi lakini mara anapogundua kuwa amefanya dhambi anapaswa  kutubu dhambi hiyo mara moja na Bwana atatusamehe 1Yohana 2;1 “Watoto wangu wadogo nawaandikia ili kwamba msitende dhambi na kama mtu akitenda dhambi tunaye mwombezi kwa baba  Yesu Kristo mwenye haki naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu wala si kwa dhambi zetu tu bali na kwa dhambi za ulimwengu wote” 1Yohana 1;9 “Tukiziungama dhambi zetu Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi  zetu na kutusafisha  na udhalimu wote” Kwa msingi huo basi ni vema kuungama dhambi hiyo kwa toba na kutokukusudia kuirudia tena hapo utakuwa salama  na wokovu wako utakuweko palepale.

Lakini ni muhimu kufahamu kuwa mtu aliyeokoka hafanyi dhambi kwa kukusudia wala hapaswi kuishi maisha ya dhambi 1Yohana 5;18 mtu aliyeokoka anachukia dhambi na anapokuwa ameifanya anahuzunika sana  na kutubu  maana tumeitwa kuwa watakatifu, katika hatua za mwanzoni mwa wokovu ni rahisi kukosea katika maeneo mbali mbali  lakini inakupasa kutubu na kuacha  Waefeso 1;4-5 Tumeitwa katika utakatifu 

 Kwa msingi huo sasa jitambue kama mtoto halali wa Mungu na kuwa umeokoka uzima wa milele ni wako na kuamini ya kuwa yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwetu ataikamilisha Wafilipi 1;6

Hakuna maoni: