Alhamisi, 4 Februari 2016

Jinsi ya Kuukulia Wokovu !



Mstari wa msingi 1Petro 2;2 “ Kama watoto waliozaliwa sasa yatamanini maziwa ya akili yasiyoghoshiwa ili kwa hayo mpate kuukulia wokovu”

Ni muhimu kufahamu kuwa tangu ulipoamua kuokoka wewe sasa umekuwa mtoto wa Mungu Biblia inasema katika Yohana 3;6 “ Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili na kilichozaliwa kwa Roho ni roho wewe umezaliwa kwa roho ndiyo maana inatajwa pia kuwa umezaliwa mara ya pili , hapo mwanzo ulizaliwa katika mwili na kilichozaliwa kwa mwili ni mwili  na kamwe hakiwezi kuishinda dhambi, lakini sasa umezaliwa mara ya pili na ufalme wa Mungu ni wako, kwa msingi huo sasa tungependa kutafakari jambo moja la msingi sana 

 wokovu ni hatua

Mtoto mchanga wa kimwili anapozaliwa  yaani katika hali ya kawaida ya kibinadamu  ili aendelee kuishi anapaswa au analazimika kupewa maziwa ili aweze kuishi jambo kama hili ni sawa kwa mtoto wa kiroho pia vinginevyo anaweza kufa au kudumaa na hatimaye kuwa dhaifu na kufa, kufa kiroho ni kurudi nyuma na kumtumikia shetani sasa ili mtu aliyezaliwa mara ya pili aweze kuendelea katika wokovu ni lazima anywe maziwa ya Kiroho 1Wakoritho 3;1-2 na Waebrania 5;13 “Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki kwa kuwa ni mtoto mchanga” Hivyo mara baada ya kuzaliwa kiroho au kuokoka tunakuwa bado hatujui sana neno la haki tunahitaji maziwa ili tuweze kukua katika wokovu.

Maana ya maziwa
Maziwa haya ni kinywaji cha kiroho Kutoka kwa Yesu Kristo ni neno la Mungu au neno la Kristo soma 1Wakoritho 10;4 wote wakanywa kinywaji kile cha roho kwa maana waliunywea mwamba wa roho uliowafuatia na mwamba ule ulikuwa ni Kristo” Mtu awaye yote aliyeokoka kama hatapata mafundisho ya neno la Mungu  atadumaa nakujiweka katika hali ya kufa kiroho na kurudi tena katika utumwa wa dhambi, hakuna uwezekano  wowote wakuendelea na wokovu bila mafundisho ya neno la Mungu  Neno la Mungu lina sehemu kubwa sana katika maisha ya kiroho ya mtu.

1.       Ni chakula cha kiroho.
Biblia inasema mtu hataishi kwa mkate tu bali kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu, kwa msingi huo kusudi la kuishi kwetu halitegemei kula chakula cha kawaida tu bali na chakula cha kiroho ambalo ni neno la Mungu Yeremia 15;16 “maneno yako yalionekana nami nikayala…” Neno la Mungu ni chakula halisi Yesu alisema amlaye yeye ataishi kwanini kwa sababu Yesu ni neno la Mungu Yohana 1;1 Ufunuo 1913 Yohana 6;48-58 Tukiacha kulila Neno la Mungu  baada ya kuzaliwa mara ya pili  hatutaweza kuishi milele ili kuishi milele ni lazima tumle Yesu Kristo Yohana 6;48-49,57-58, Yeye ndiye chakula cha uzima  Mathayo 4;4 Yesu alisema mtu hataishi kwa mkate tu…” Kumbukumbu la torati 8;3 Mungu aliwafundisha Israel kuwa hawawezi kuishi kwa mkate tu bali kwa kila litokalo katika kinywa cha Mungu ni kwa ujuzi huu watatakatifu waliotutangulia walifahamu umuhimu wa kulishika Neno kama chakula Ayubu 23;12, wao waliiona sheria ya Mungu yaani neno kuwa la thamani kuliko maelfu ya dhahabu na fedha”

2.       Ni taa na mwanga wa njia yetu ya Mbinguni
Njia ya mbinguni ni nyembamba sana  kwa maana nyingine imesonga  na mlango ni mwembamba sana Mathayo 7;14 ili wakati wote tuweze kutembea  bila kuanguka au kuteleza  na kuingia katika njia iendayo upotevuni  inatupasa kuwa na mwanga Mathayo 7;13, tusipolizingatia Neno la Mungu tunaweza kupotea  katika wokovu Zaburi 119;105 Neno lako ni taa ya miguu yangu, Mithali 6;21-23 sheria ya Mungu ni nuru…”

3.       Ni silaha ya ushindi dhidi ya dhambi.
      Ni vigumu kabisa kuishinda dhambi bila kujaa neno la Mungu Yesu Kristo alimshinda shetani katika mathayo sura ya 4 kwa kutumia neno la Mungu aliposema imeandikwa, kumbe kumshinda adui na kuishinda dhambi kunahitaji uwe na ujuzi pia wa neno la Mungu  Huwezi kuishinda dhambi na adui shetani kama hupendi kuhudhuria mafundisho na ibada ambako tunajifunza Neno la Mungu, Zaburi ya 119;11 Biblia inasema Moyoni mwako nimeliweka Neno lako nisije nikakutenda dhambi kumbe kujifunza neno la Mungu na kulifanyia kazi yaani kulitii kunatusafishia njia ya kwenda mbinguni Zaburi ya 119;9 Jinsi gani kijana aisafishe njia yake ni kwa kutii Neno la Mungu na kulifuata daima, Neno la Mungu pia hufanya maisha yetu kuwa safi Yohana 15;3,Yohana 17;17, kuacha kujifunza neno la Mungu kunaweza kutufanya pia kufanya dhambi bila kujua Mambo ya walawi 5;17

4.       Ni Afya ya miili yetu na nyundo ya kuyavunja matatizo tuliyo nayo
Ikiwa tuliponywa kwa Neno la Mungu katika mikutano ya injili au katika maombezi yoyote ni neno la Mungu linalotuhakikishia uzima wakati wowote, mara nyingi shetani anapotuona kuwa tunaujuzi wa Neno la Mungu hawezi kurudi kutufuata fuata tena Luka 11;24-26, hata kama hatujapokea uponyaji wa miili yetu bado ni muhimu kufahamu kuwa Neno la Mungu ndio ufunguo wa uponyaji wetu Mithali 4;20-22 Yohana 6;63. Yatafute maneno ya Mungu na kuyaweka moyoni.
 Unapokuwa umebanwa na matatizo ya aina yoyote  dawa siyo kuacha kutafuta mafundisho ya Neno la Mungu  tumia kila inavyowezekana kulitafuta Neno na kulitumia lenyewe ni kama nyundo ya kuvunja vunja kila aina ya matatizo matatizo yote yanayoonekana kama mawe magumu Neno linauwezo wa kuyavunja Yeremia 23;29 Je Neno langu si kama moto? Asema Bwana na kama nyundo ivunjayo mawe vipande vipande?

Vizuizi vya kukuzuia kupata mafundisho au chakula cha kiroho yaani Neno la Mungu.
Tumeona jinsi ambavyo neno la Mungu lina faida nyingi sana katika maisha yetu ikiwa ni pamoja na kutufanya tuishi milele na milele kwa msingi huo basi ni muhimu kufahamu kuwa shetani hatapedezwa na sisi kulipata Neno la Mungu kwa msingi huo kutakuwa na vizuizi vya kila aina kutoka kwake ili tusiwezi kulielewa na kulijifunza Yeye anajuwa wazi kabisa kuwa hawezi kumshinda mtu aliyejaa neno kama ilivyokuwa kwa Bwana Yesu Mathayo 4;1-11 kwa msingi huo atahakikisha kuwa kwa gharama yoyote ile anatuzuia kulipata Neno  na ndio maana hukusudia kutuua kiroho mapema katika uchanga wetu ili tusifikie ngazi ya kulijua Neno ambalo kwalo anajua kuwa hataweza kutushinda tena alikusudia kumuua Yesu mapema  Mathayo 2;13,16, sisi nasi tunapookolewa ni muhimu kufahamu kuwa tunakuwa tumezaliwa kwa Roho na hivyo ibilisi atahakikisha kuwa anatuua mapema kabla hatujalijua sana neno kwa kuwa tunazifahamu fikra zake ni muhimu kujifunza mbinu zake mapema kabla hajaanza kuzitumia na kutupata 2Wakorotho 2;11 tukizifahamu mbinu anazozitumia basi hatutampa nafasi ya kukuua mpinge naye atakukimbia Waefeso 4;27.Yakobo 4;7.

Njia Tano anazozitumia shetani Kumzuia mtoto mchanga kupata Neno la Mungu ili kumuua.
·         Kumfanya ajione anajua na akatae kufundishwa
Biblia inasema mtu akidhani kuwa anajua neno  hajui bado kama impasavyo kujua  1Koritho 8;2 Mtu awaye yote akikosa ladha ya chakula na kukataa kula akisema kuwa anajisikia kuwa ameshiba  maisha ya mtu huyo yako hatarini hiki ndicho shetani anachokifanya kwa watu wengi waliookoka   huwafanya wajione kuwa wanajua na hawahitaji kujifunza tena  na kutokukubali kujifunza neno la Mungu na hatimaye hujikuta wanakufa kiroho mtu akitaka kujifunza siku zote ni lazima ujifanye kuwa mjinga Zaburi 73;22,24 na ni lazima ukubali kufundishwa na Mungu siku hadi siku Zaburi 143 ;10 Tunapokuwa katika hali ya kukubali kufundishwa ndipo tunapata nafasi ya kumpendeza Mungu Zaburi 25;4-5,Yohana 6;45 Isaya 54;13 Kuangamizwa kwetu kunatokana na kukosa maarifa Hosea 4;6 kwa msingi huo ni lazima tukubali kufanya sehemu yetu na kukubali kujifunza Neno la Mungu na kamwe tusikubali kulizoea Neno kila siku kubali kujifunza kana kwamba ndio unaanza sasa ukifanya hivyo ushindi utakuwa ni wako.

·         Kumfanya asongwe na shughuli za dunia na udanganyifu wa mali.
Mathayo 13;22 tunajifunza mfano wa mbegu zilizoangukia kwenye miiba kuwa ni watu wanaoshindwa kukua kiroho kwa sababu ya kushindwa kudumu katika neno na kusongwa na shughuli za dunia na udanganyifu wa mali, kwa msingi huo ni lazima uwe mwerevu katika mema fahamu kuwa lolote lile linalokuzuia kujifunza Neno la Mungu wakati mwingine ni kifungo cha kukufanya usikue kiroho na huyo ni adui 3Yohana 1;2 Mungu anapenda tufanikiwe katika mambo yote  lakini msingi wa mafanikio ya kweli huanzia rohoni na ndio maana Yesu alisema tutafute kwanza ufalme wa Mungu na haki yake na mengine yote tutazidishiwa  Mathayo 6;33 kumbuka kuwa haitakufaidia kitu kama utaupata ulimwengu mzima na kupoteza nafsi yako ? Marko 8;36 ni muhimu kufanya kazi na kujishughulisha kwani Biblia inasema asiye fanya kazi kula na asile lakini ni muhimu kutokutawaliwa na utafutaji wa mali na kujikosesha mambo ambayo ndio msingi wa baraka za mwili pia kwa kila jambo kuna majira yake Muda wa ibada uwe ibada na Muda wa kazi na biashara na uwe muda wa kazi na biashara Muhubiri 3;1 kwa msingi huo wakati wa kipindi cha neno acha shughuli zako nyingine maana neno la Mungu ndio uhai wa maisha yetu hivyo ni muhimu likapewa kipaumbele.
·         Kuwafanya watu wawe wanatoa udhuru wakati wote wanapohitajika kwenda kwenye neno
Una weza kushangaa kuwa siku za ibada ya kujifunza maneno ya Mungu ndio kunatokea sababu kadhaa wa kadhaa ili mradi tu kukufanya usione umuhimu wa kuja kujifunza neno la Mungu inapotokea hali hiyo fahamu kuwa ni hila za adui  Luka 14;16-20 Yesu alitoa mfano wa watu walioalikwa harusini lakini kila mmoja alionekana ana sababu za msingi za kumfanya asihudhuria sherehe ile  hali iliyomuudhi mwenye harusi Luka 14;33 Yesu alihitimisha kwa kuonya kuwa “basi kadhalika kila mmoja wenu asiyeacha vyote  alivyo navyo hawezi kuwa mwanafunzi wangu” 

·         Kumletea mtu dhiki au udhia kwa ajili ya wokovu.
Mathayo 13;20-21 ni mfano wa Yule aliyepandwa kwenye miamba kwa kukosa mizizi  inapotukia dhiki huchukizwa , hiii ni mbinu nyingine ya adui ili kwamba aweze kuwakatisha watu tamaa ya kujifunza neno la Mungu kisha wafe kiroho inakupasa kuvumilia yanapotokea magumu  na wala uusiliache neno la Mungu  heri ni wale wanaostahimili Mathayo 5;11-12,1Petro 4;12-16 Yakobo 5;10

·         Kukufanya utafute mafundisho yaliyo karibu na nyumbani
Katika hali isiyokuwa ya kawaida wakati mwingine shetani anaweza kuleta ushawishi unaoonekana kama wenye busara kwa kukushawishi kufuata mafundiho yanayopatikana karibu na nyumbani  ili kukupeperusha  kwa kupenda njia ya mkato Mungu alipandisha Israel kutoka Misri aliwapitisha katika njia iliyo ndefu na ya mbali kwenda kanaani Kutoka 13;17-18 si vibaya kusali karibu na nyumbani kwako kama wana mafundisho mazuri lakini ni vema kukaa na wale waliokuzaa kiroho kwani hao ndio wana uchungu na wewe na pia endapo mafundisho ya mahali hapo ni dhaifu basi ni afadhali kwenda mbali kwa faida ya roho yako  hekima ya Mungu wakati mwingine hutafutwa kwa gharama Mathayo 12;42 ukitaka ukue kiroho wakati mwingine uwe kama malikia wa sheba.

Umuhimu wa kunywa maziwa Yasiyoghoshiwa Incorrupt Gospel 1Petro 2;2
Maziwa yasiyoghoshiwa ni neno la Mungu halisi lisilochanganywa na chochote, neno la Mungu ambalo limechanganywa na mapokeo ya wanadamu halifai katika malezi ya kiroho, baada ya kuokolewa kama utakuweko mahali ambapo neno la Mungu linachanganywa na mapokeo ya wanadamu mahali hapo panaandaa mauti yako ya Kiroho, ni muhimu kwako kukaa mahali ambapo unajifunza Neno la Mungu safi lisilochanganywa na mapokeo ya kidini kwani hayo ni sumu ya kuua watu wa kirohon kaa mahali penye mafundisho ambayo ni neno la Mungu halisi.

Uchungu wa mwana aujuaye ni mzazi wagalatia 4;19-20
Neno la Mungu linatufundisha kuwa Mzazi wa kiroho kama ilivyo kwa mzazi wa kimwili anakuwa na uchungu wa mtoto wake kuliko Yule asiyekuzaa ili uweze kupata huduma nzuri kaa na wale waliokuzaa kiroho wao wana uchungu wa kweli kwaajili yako, hudhuria ibada hapo njoo na kalamu na daftari andika mafundisho yote unayojifunza ukijua ya kuwa nawe utakuwa kiroho na kuwa mwalimu wa wengine huo ndio mpango wa Mungu kwaa jili yako Ubarikiwe.

Maoni 3 :

Bila jina alisema ...

Barikiwa sana mafundisho no mazuri, nmeyapenda

Bila jina alisema ...

Ubarikiwe sana nimebarikiwa sana!

Bila jina alisema ...

Somo zuri