Jumatatu, 29 Februari 2016

Ukawa ni ugeni wa kupiga deki !



Nilitoka huko kwetu liwetwe Songea mara baada ya kumaliza elimu ya msingi, shangazi yangu alimuomba kaka yake ambaye ni baba yangu anichukue huku Dar es Salaam ili nimsaidie shughuli zake za mama nitilie, tulipanda basi la shabiby hadi hapa Dar safari yetu haikuwa nzuri nilisikia kizunguzungu na kutapikaa nia nzima, ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kusafiri na kupanda basi kutoka kijiji chetu. 

 Mara yangu ya kwanza kupanda basi kutoka Songea kuja Dar es Salaam

Kijana niliyekuwa naye jirani alionekana kunihurumia sana kutokana na ile hali, Tulipofika ubungo kijana Yule alionesha wema kwangu kwani alitusaidia kushusha mizigo, tulipanda basi la ubungo mwenge – mbagala ili tufike keko shangazi alikokuwa anaishi.

Nilipenda sana mazingira ya keko kwani watu wa nyumbani walikuwa wengi hivyo sikuchelewa kuwa mwenyeji Shangazi alinichukua kwenye shughuli zake kutokana na ucheshi niliokuwa na adabu ya watu wa Songea hasa kitendo cha kuamkia watu, kuwapa chakula wateja na kuwakaribisha , kushukuru nikiwa nimepiga hatua  nikiwa nimepiga magoti kiliwafurahisha wateja . kati ya wateja waliokuwa wanajaza wateja wanajaza mgahawa wetu  ni pamoja na kijana niliyekaa naye siti moja wakati wa safari ya kutoka songea kuna vitu ambavyo  hutokea kwa njia ya ajabu  sana, tuilizidi kumpenda na kumuona ni ndugu yetu hasa, hatimaye kijana Yule aliutumia mwanya huo kumweleza shangazi nia yake ya kutaka tuwe wawili ili tuijaze dunia, sijui ni kwa nini  shangazi aliniruhusu kuhamia kwa Yule kijana kwani tulianza kuunganisha mwili na kuwatafuta hao watoto hata kabla ya ridhaa ya viongozi wa dini au wa mila  yetu na wazazi pia au alifanya hivyo ili kutoa muda kwetu wa kupimana tabia na mengineyo.

Siku ya nne baada ya kuhamia kwa huyo mshirika wangu, wifi yangu alikuja kunisalimia , aliniletea zawadi  ya unga mweupe wa muhogo  unaorowekwa kwenye maji, kule Songea tunaita kindowole na dagaa wa ziwa nyasa Niliushambulia ugali huo kama vile sina akili nzuri vile. Yaani niliula kwa pupa sana , Mshirika wangu siku ile alienda kazini  usikui ili arudi asubuhi. Hivyo ilipotimu majira ya saa sita hivi usiku nilisikia tumbo linauma kwa mtindo unaoashiria kuwa vyakula vyote vilivyomo tumboni vitoke nje Nilitoka chumbani kuelekea mlango wa kutoka nje  Mlango ulinishinda kufungua  na Uharo usiokuwa wa kawaida wala adabu ulinitoka, na kinyesi kilitapakaa pale mlangoni, kumbe inzi wa huku Dar hawalali waliamshana usiku ule na kushangilia neema ile iliyokuwa imewazukia. Wapangaji wenzangu  waliamshana na kusimama  kwenye milango ya vyumba vyao  huku wakiwa wameshangaa wazi na kunidharau, labda kwa kuniona mshamba . Kazi ya kupiga deki  ilianza usiku  huo huo Mpenzi wangu aliporudi kutoka kazini nilimsimulia yote yaliyotokea  na nilimuomba tuhame ila Mpenzi wangu hakuwa tayari kuhama  kwa wakati ule, kwa hiyo asubuhi ya silku ile  na siku zilizofuata zilikuwa ni za fedheha kwangu, Hatimaye hata hivyo tulihama, Hadi leo nikiona unga wa muhogo au ugali wa muhogo tumbo linafanya  fujo ya ghafla, kama vile kunipa tahadhari lakini huwa ninaula unapokuja kwenye anga zangu.  

Hakuna maoni: