Jumapili, 28 Februari 2016

Kushinda Vita kwa Mkate wa Shayiri! (Ngano)



Waamuzi 7:13 – 14

Moja ya waamuzi wanaotajwa kama mashujaa wa Imani katika agano jipya, Gideon ni mmoja wao, anatajwa kama moja ya watu waliotiwa nguvu na kufanywa kuwa Hodari na kukimbiza Majeshi ya wageni  Waebrania 11:32-35, Lakini tunaposoma Habari ya Gideoni na kuchunguza kwa kina tutagundua kuwa siri ya ushindi wa Gideoni ilitokana na imani yake ndogo kwa Mungu na utayari wa kuyatii maagizo ya Mungu, leo tutachukua Muda kuangalia kwa undani nini kilizunguka maisha ya Gideoni na ninini kilimpa Ushindi mkubwa?


 Gideon na watu 300 walitakiwa kupiga tarumbeta na kuangaza kwa mwenge wakati wa usiku na Mungu aliwapa ushindi

Tutajifunza somo hili kwa kuzingatia maswala kadhaa yafuatayo:-

1.      Hali mbaya ya wana wa Isarael wakati wa Gideoni
2.      Hali ya Gideoni na wito kutoka kwa Mungu
3.      Kushinda vita kwa mkate wa Shayiri

Hali mbaya ya wana wa Israel wakati wa Gideoni

Katika wakati wa Gideoni Israel walikuwa wanapitia moja ya aina ya ukoloni uliokuwa mbaya zaidi, wote tunakumbuka kuwa Israel waliwahi kuwa watumwa huko Misri, na kuwa Mungu aliwakomboa kutoka Utumwani kupitia Musa na kuwaleta Katika nchi ya Kanaani, wote tunafahamu kuwa utumwa wa kuelekea Misri ulitokana na wao kuishi miaka mingi huko, Lakini sasa Mungu alikuwa amewapa nchi yao na walikuwa Taifa huru, Hata hivyo Israel wanajikuta sasa wanatawaliwa na Wamidian, ukoloni wa kimidian ulikuwa ni wa tofauti, wao waliwatisha sana na kusababisha waishi chini ya mashimi na mahandaki, mapango na ngome za milimani, waliteka nyara kila kitu na kuharibu chakula hivyo hata kula yao ilikuwa ya shida, waliwapokonya mifugo na walikuja wakiwa wengi kama nzige kwa mujibu wa Biblia Waamuzi 6:1-6, hali iliyopelekea wana wa Israel kumlilia Bwana.

Africa na Asia na America wanafahamu sana hali ya ukoloni, Ukoloni ni hali ya taifa moja kuvuka mipaka yake na kwenda kulitawala lingine Kisiasa, kiuchumi,kijamii na kiutamaduni,

Pia uko ukoloni mamboleo, ambapo ukoloni huu ni taifa moja au zaidi au kikundi cha watu kuzitawala nchi nyingine kinyemela kwa kuziwekea vikwazo nchi nyingine au kuzifanya ziwe na Uchumi tegemezi, kwa faida ya mataifa yanayotegemewa

Zamani sana aina za ukoloni zilitofautiana Wakaldayo, waoa walikuwa waliwachukua watu na kuwahamishia katika nchi zao kama watumwa na kuwatumia kwa faida yao, Warumi au watu wa Ulaya walianzisha aina hii ya ukoloni wa inchi moja kubwa kwenda kutawala nchi nyingine kwa faida yao palepale walipo, Israel imepitia aina zote za utumwa, lakini utumwa uliombaya zaidi ni kumuonea mtu katika nchi yake mwenyewe palepale alipo, Hii ilikuwa inawaumiza sana wana wa Israel, na kwa wamidian sio walikuwa wakiwatawala lakini waliwapokonya Israel kila walichokuwa nacho, mpaka chakula na kuwafanya waishi kwa hofu kwenye mashimo hali hii ilimuuma sana Gideon Moyoni pia Waamuzi 6:11-13 Gideon alihesabu hali hii kama kutupwa na Mungu. Kwa vile wana wa Isarael walikuwa wamemlilia Mungu aliamua kumtumia Gideon ili kuwakomboa dhidi ya Jeshi lile kubwa.

Hali ya Gideoni na wito kutoka kwa Mungu

Mungu aliamua kumtumia Gideon kwa sababu kadhaa lakini ukweli Gideoni alikuwa tayari amezaliwa katika Mazingira ya hofu kubwa aliogopa kila kilichomzunguka na Mungu alifahamu hilo, lakini mtazamo wa Mungu kwa Gideoni ilikuwa Mungu anamuona Gideon kama shujaa Waamuzi 6:12, Malaika alimuita shujaa, Inagwa ukweli ilikuwa hakukuwa na mtu muoga aliyepata kutumiwa na Mungu kama Gideon, Mungu alimtazama akaona uko uwezo ndani ya Gideon na Mungu alitaka kumtia moyo Waamuzi 6:14 - 16, Gideoni alitiwa Moyo na alianza kwa kubomoa madhabahu ya miungu ya Baba yake na kuanza kumuabudu Mungu aliye hai, Gideoni alitaka uthibitisho kutoka kwa Mungu endapo Mungu atamtumia Waamuzi 6:33-40
Gideoni ni wazi kuwa alikuwa muoga hata hivyo, na Mungu aliifahamu hali yake, aliita jeshi kubwa la wanaume wapatao 32,000 lakini hawa wote walikuwa waoga sana na Mungu aliona hata wakishinda watajisifu kwa sababu ya wingi wao hivyo waoga walipunguzwa na 22,000, walirejea nyumbani na kumi elfu wakabaki na Gideon Bwana akasema hawa pia ni wengi na alimwambia Gideoni awachje kwa kuwaleta kunywa maji, waliokunywa kwa kiganja cha mkono ndio walioweza kupita nao walikuwa 300 tu Waamuzi 7:1-7, Hata hivyo Gideon bado alikuwa muoga hata hakuweza kutembea peke yake

Kushinda vita kwa mkate wa shayiri

Mungu alitafuta namna ya kumtia Nguvu Gideon Waamuzi 7:9-14 na kupitia ndoto hii ya mkate wa shayiri Gideoni alitiwa nguvu na waliwapiga vibaya wamidian na kuwaua wafalme wao wawili na kusambaratisha jeshi zima Waamuzi 7:15-25, Kwa nini Mungu alimpa ushindi Gideon
1.      Alichukizwa na hali ya mateso dhidi ya taifa lake
2.      Alikuwa mwenye kumuabudu Mungu, alivunja madhabau ya baba yake na kumuamini Mungu aliye hai
3.      Ingawa alikuwa muoga sana alitii kile Mungu alichokuwa akimuelekeza
4.      Alitiwa nguvu na ndoto ya mkate wa shayiri mkate huu ulianguka kutoka Mbinguni na kuipiga hema ya wamidian na kuisambaratisha vibaya, aliabudu.
5.      Gideon alihitaji kupandishwa imani na kuamini kuwa Mungu atamsaidia
6.      Gideon alikubali kwenda uwanja wa vita.


7.      Imani ndogo tuliyonayo katika Kristo ambaye ni mkate ushukao kutoka Mbinguni itakupa ushindi katika maisha yako, Yesu ndio Mkate wa ngano aliouona Gideon siri ya kushinda vita vya aina yoyote duniani inayotukumba watu wa Mungu, ni kumwamini Yesu ni kujitia nguvu kwa huyo yeye ndio kimbilio letu, aliye dhaifu na asemi mimi ni Hodari.
Ushundi wa Maisha yetu na mapambano ya aina mbalimbali utategemea na kiasi cha imani kitakachotutia nguvu kutoka mbinguni ni wazi kuwa Gideon alitiwa nguvu sana aliposikia tafasiri ya ndoto ya mkate wa shayiri, mkate huu ulioshuka kutoka mbinguni ulikuwa unamwakilisha Yesu Kristo kiasi chochote cha imani tulicho nacho katika Kristo hata kama ni kidogo kiasi gani kitatupa ushindi dhidi ya adui, hatihitaji silaha wala ujuzi wa vita tunahitaji utayari na kukubali kuelekezwa na Mungu na kisha kutiwa Nguvu Gideon alitiwa nguvu na Mungu kupitia ndoto ya mkate wa shayiri uliotoka Juu. Mungumape kila mmoja wetu ushindi kwa mkate wa Shayiri katika Jina la Yesu.

Hakuna maoni: